-
Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na WanadamuMnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 15
-
-
Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na Wanadamu
“Kulikuwa na karamu ya ndoa katika Kana . . . Yesu na wanafunzi wake walialikwa pia kwenye karamu hiyo ya ndoa.”—YOHANA 2:1, 2.
1. Simulizi kumhusu Yesu akiwa Kana linaonyesha nini?
YESU, mama yake, na baadhi ya wanafunzi wake walijua kwamba arusi yenye kuheshimika miongoni mwa watu wa Mungu huleta shangwe. Kristo hata alifanya arusi moja iwe ya pekee sana alipofanya huko muujiza wake wa kwanza kuandikwa katika Biblia, na hivyo akafanya tukio hilo liwe lenye shangwe zaidi. (Yohana 2:1-11) Huenda umehudhuria na kufurahia arusi za Wakristo wanaotaka kumtumikia Yehova kwa furaha wakiwa wamefunga ndoa. Au huenda unatazamia kufanya arusi kama hiyo au kumsaidia rafiki yako afaulu katika arusi yake. Ni nini kinachoweza kufanywa ili arusi ifanikiwe?
2. Biblia inasema nini kuhusu arusi?
2 Wakristo wametambua kwamba shauri la Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho husaidia sana mwanamume na mwanamke wanapopanga kufunga ndoa. (2 Timotheo 3:16, 17) Ni kweli kwamba Biblia haionyeshi utaratibu hususa wa kufuatwa katika arusi za Kikristo. Hilo linaeleweka kwa sababu desturi na hata matakwa ya kisheria yanatofautiana ikitegemea mahali na wakati. Kwa mfano, katika Israeli la kale hakukuwa na utaratibu rasmi wa arusi. Siku ya arusi, bwana-arusi alimleta bibi-arusi nyumbani kwake mwenyewe au kwa baba yake. (Mwanzo 24:67; Isaya 61:10; Mathayo 1:24) Hatua hiyo ya hadharani iliwakilisha arusi ambayo haikuwa na utaratibu rasmi kama ilivyo katika arusi nyingi leo.
3. Yesu alichangia shangwe kwenye tukio gani huko Kana?
3 Waisraeli waliiona hatua hiyo kuwa arusi au kufunga ndoa. Baadaye, huenda walifanya karamu kama ile inayotajwa kwenye Yohana 2:1. Tafsiri nyingi za Biblia zinatafsiri mstari huo hivi: “Palikuwa na arusi huko Kana.” Lakini kwa kufaa neno la awali linatafsiriwa “karamu ya ndoa.”a (Mathayo 22:2-10; 25:10; Luka 14:8) Simulizi hilo linaonyesha wazi kwamba Yesu alikuwapo naye akachangia shangwe kwenye karamu hiyo iliyohusiana na arusi ya Kiyahudi. Hata hivyo, jambo kuu ni kwamba arusi za wakati huo zinatofautiana na za leo.
4. Wakristo fulani huamua kufanya arusi ya aina gani, na kwa nini?
4 Katika nchi nyingi leo, ni lazima Wakristo wanaotaka kufunga ndoa watimize matakwa fulani ya kisheria. Baada ya kuyatimiza, wanaweza kufanya arusi kwa njia yoyote inayokubalika kisheria. Wanaweza kufuata utaratibu usiohusisha mambo mengi, wakisimamiwa na hakimu, meya, au mhudumu aliyepewa mamlaka na Serikali. Watu fulani huamua kufanya arusi kwa njia hiyo, labda kwa kuwaalika watu wachache wa ukoo au marafiki Wakristo ili wawe mashahidi wa kisheria au washiriki shangwe ya tukio hilo muhimu. (Yeremia 33:11; Yohana 3:29) Vivyo hivyo, huenda Wakristo wengine wakaamua kutofanya karamu kubwa ya arusi ambayo inahusisha mipango mingi na gharama kubwa. Badala yake, huenda wakaamua kula chakula pamoja na baadhi ya marafiki wa karibu. Haidhuru tuna mapendezi gani ya kibinafsi kuhusu jambo hilo, tunapaswa kutambua kwamba Wakristo wengine wakomavu wanaweza kuwa na maoni tofauti na yetu.—Waroma 14:3, 4.
5. Kwa nini Wakristo wengi hutaka hotuba ya arusi itolewe wanapofunga ndoa, nayo huzungumzia mambo gani?
5 Wakristo wengi wanaopanga kufunga ndoa huamua hotuba inayotegemea Biblia itolewe kwenye arusi yao.b Wanatambua kwamba Yehova alianzisha ndoa na kupitia Neno lake yeye huandaa mashauri yenye hekima yanayoonyesha jinsi ya kufanikiwa na kuwa na furaha katika ndoa. (Mwanzo 2:22-24; Marko 10:6-9; Waefeso 5:22-33) Watu wengi wanaopanga kufunga ndoa hutaka marafiki Wakristo na watu wa ukoo washiriki tukio hilo lenye furaha. Hata hivyo, tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu matakwa mbalimbali ya kisheria, utaratibu, na hata desturi za kwetu? Makala hii itazungumzia hali za maeneo mbalimbali. Huenda baadhi ya hali hizo zikatofautiana sana na hali za kwenu. Vyovyote vile, unaweza kupata kanuni za jumla au mambo ambayo ni muhimu kwa watumishi wa Mungu.
Ndoa Inayoheshimika Ni Ndoa Halali Kisheria
6, 7. Kwa nini tunapaswa kutilia maanani matakwa ya kisheria kuhusu kufunga ndoa, nasi tunaweza kuonyeshaje kwamba tunafanya hivyo?
6 Ingawa Yehova alianzisha ndoa, serikali za wanadamu zimeweka sheria fulani kwa wale wanaofunga ndoa. Na hilo ni jambo linalofaa. Yesu alisema: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Vivyo hivyo, mtume Paulo alitoa mwongozo huu: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.”—Waroma 13:1; Tito 3:1.
7 Katika nchi nyingi, Kaisari, au serikali, huamua ni nani anayestahili kufunga ndoa. Kwa hiyo, Wakristo wawili ambao wako huru Kimaandiko wanapoamua kufunga ndoa, wanajitahidi kufuata sheria za nchi yao kuhusu ndoa. Huenda sheria hizo zikatia ndani kupata cheti cha ndoa, kutumia ofisa aliyewekwa rasmi na serikali, na labda kuiandikisha ndoa. Kaisari Agusto alipoagiza watu wakafanye “uandikisho,” Maria na Yosefu walitii agizo hilo, nao wakaenda Bethlehemu ‘ili wapate kuandikishwa.’—Luka 2:1-5.
8. Mashahidi wa Yehova hawafanyi nini, na kwa nini?
8 Wakristo wawili wanapofunga ndoa kupatana na matakwa ya kisheria yanayokubalika, wanakuwa na wajibu machoni pa Mungu. Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawaandikishi ndoa mara ya pili kwa kurudia utaratibu wa kisheria, wala hawarudii nadhiri za ndoa, kama vile wakati wenzi wanapoadhimisha mwaka wa 25 au 50 wa arusi yao. (Mathayo 5:37) (Makanisa fulani hupuuza utaratibu wa ndoa ya kiserikali, yakidai kwamba si ndoa halali kwa sababu kasisi au kiongozi wa dini hakufanya sherehe au kuwatangaza kuwa mume na mke.) Katika nchi nyingi, serikali humpa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova mamlaka ya kuandikisha ndoa. Ikiwa ndivyo ilivyo, yaelekea kwamba atafanya hivyo katika Jumba la Ufalme ambapo hotuba ya arusi itatolewa. Jumba la Ufalme ni mahali pa ibada ya kweli na panafaa kwa ajili ya hotuba inayohusu mpango huo ambao ulianzishwa na Yehova Mungu.
9. (a) Wakristo wanaotaka kufunga ndoa ya kiserikali, wanaweza kuamua kufanya nini? (b) Wazee wanaweza kuhusikaje katika mipango ya arusi?
9 Kulingana na sheria za nchi nyingine, watu wanahitajiwa kufunga ndoa katika ofisi za serikali, kama vile makao makuu ya halmashauri ya jiji, au mbele ya ofisa aliyewekwa rasmi na serikali. Mara nyingi, baada ya kuchukua hatua hiyo ya kisheria, Wakristo huamua kuwa na hotuba ya arusi kwenye Jumba la Ufalme siku hiyohiyo au siku inayofuata. (Haingefaa siku nyingi zipite kati ya kufanya utaratibu wa kisheria na kutolewa kwa hotuba ya Biblia, kwa kuwa wameoana machoni pa Mungu na wanadamu, kutia ndani kutaniko la Kikristo.) Wale wanaotaka kufunga ndoa ya kiserikali na baada ya hapo wawe na hotuba ya arusi kwenye Jumba la Ufalme, wanapaswa kuomba ruhusa ya wazee wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko. Mbali na kuhakikisha kwamba watu hao wana sifa nzuri, waangalizi hao watahakikisha kwamba arusi haivurugi saa za mikutano ya kawaida na mipango mingine kwenye jumba. (1 Wakorintho 14:33, 40) Pia, watachunguza matayarisho yoyote ambayo huenda wenzi hao wakaomba yafanywe kwenye jumba na kuamua ikiwa tangazo litatolewa kuhusu matumizi ya jumba.
10. Ikiwa ndoa ilifungwa kiserikali, hotuba ya arusi itatolewaje?
10 Mzee anayetoa hotuba ya arusi atajitahidi kuitoa kwa uchangamfu, kwa njia yenye kujenga kiroho, na kwa heshima. Ikiwa wenzi hao walifunga ndoa ya kiserikali, mzee huyo ataeleza wazi kwamba wenzi hao wamefunga ndoa kulingana na sheria ya Kaisari. Ikiwa hawakufanya nadhiri za ndoa walipofunga ndoa ya kiserikali, wenzi hao wanaweza kufanya hivyo wakati wa hotuba.c Ikiwa utaratibu waliofuata wa ndoa ya kiserikali ulitia ndani nadhiri, lakini wenzi hao wapya wangependa kuweka nadhiri mbele za Yehova na kutaniko, watasema nadhiri hizo kwa kutumia wakati uliopita, wakionyesha kwamba tayari walikuwa ‘wameunganishwa.’—Mathayo 19:6; 22:21.
11. Katika nchi fulani, mwanamume na mwanamke hufungaje ndoa, na ni mambo gani yatakayotajwa katika hotuba ya arusi?
11 Katika nchi fulani, huenda sheria isiruhusu mwanamume na mwanamke wafunge ndoa kwa kufuata utaratibu fulani rasmi, hata mbele ya ofisa wa serikali. Arusi hutukia wakati wanapompa ofisa cheti cha ndoa kilichotiwa sahihi. Mara tu baada ya hapo, cheti hicho cha ndoa huandikishwa. Katika njia hiyo, mwanamume na mwanamke huonwa kuwa mume na mke, na siku hiyo kuwa tarehe ya ndoa yao. Kama ilivyotajwa mwanzoni, huenda wenzi hao waliofunga ndoa wakaamua kwamba hotuba inayotegemea Biblia itolewe kwenye Jumba la Ufalme. Ndugu mkomavu kiroho ambaye ameombwa atoe hotuba atawajulisha wote wanaohudhuria kwamba wenzi hao wamefunga ndoa kwa sababu ndoa yao imetoka tu kuandikishwa. Nadhiri yoyote itatolewa kulingana na maagizo yaliyo kwenye fungu la 10 na maelezo ya chini ya fungu hilo. Wale wanaohudhuria sherehe hiyo kwenye Jumba la Ufalme watashangilia pamoja na wenzi hao na kufaidika na mashauri kutoka katika Neno la Mungu.—Wimbo wa Sulemani 3:11.
Ndoa ya Kimila na ya Kiserikali
12. Ndoa ya kimila ni ndoa ya aina gani, na wale walio katika ndoa hiyo wanapaswa kufanya nini?
12 Katika nchi fulani, huenda wale wanaotaka kufunga ndoa wakaamua kufanya ndoa ya kimila. Hilo halirejelei watu wawili wanaoishi tu pamoja, wala halirejelei wale wanaoishi pamoja kama mume na mke kwa njia isiyo halali. Huenda zoea hilo likakubaliwa katika maeneo mengine ingawa si ndoa halali kabisa.d Tunazungumzia ndoa ambayo inafuata desturi zinazotambuliwa na wengi katika kabila au eneo fulani. Huenda hilo likatia ndani kulipa kabisa na kukubaliwa kwa mahari, na hivyo wenzi hao wanakuwa wamefunga ndoa halali kisheria na Kimaandiko. Serikali huona ndoa hiyo ya kimila kuwa halali kisheria na isiyoweza kuvunjwa. Kwa kawaida, ndoa hiyo ya kimila inaweza baadaye kuandikishwa na wenzi kupewa cheti rasmi. Kuandikisha ndoa kunaweza kuwa ulinzi kwa wenzi hao au kwa mke ikiwa atakuwa mjane na kwa watoto wowote ambao huenda wakazaliwa baadaye. Kutaniko linapaswa kumhimiza yeyote ambaye amefanya ndoa ya kimila aiandikishe haraka iwezekanavyo. Inaonekana kwamba chini ya Sheria ya Musa, ndoa na kuzaliwa kwa watoto kuliandikishwa kirasmi.—Mathayo 1:1-16.
13. Baada ya kufunga ndoa ya kimila, hotuba ya arusi inafaa ishughulikiweje?
13 Wenzi waliounganishwa kwa njia halali katika ndoa ya kimila wanakuwa mume na mke wanapofunga ndoa hiyo. Kama ilivyotajwa mwanzoni, huenda Wakristo wanaoingia katika ndoa hiyo iliyo halali kisheria wakataka hotuba ya arusi itolewe, kisha waweke nadhiri kwenye Jumba la Ufalme. Wakifanya hivyo, msemaji atatangaza kwamba wenzi hao walikuwa tayari wamefunga ndoa kulingana na sheria za Kaisari. Kutakuwa tu na hotuba moja ya ndoa. Kuna ndoa moja, yaani, ndoa ya kimila iliyo halali kisheria, na hotuba moja ya Kimaandiko. Mambo hayo mawili, yaani, kufunga ndoa ya kimila na hotuba ya Kimaandiko, yanapaswa kufanywa kwa muda unaokaribiana, na ikiwezekana siku hiyohiyo, ili ndoa ya Kikristo iheshimiwe katika jamii.
14. Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa ndoa za kimila na kiserikali zinakubalika?
14 Katika nchi fulani ambako ndoa za kimila zinaonwa kuwa ndoa halali, kuna pia ndoa za kiserikali (au kisheria). Kwa kawaida, ndoa za kiserikali hufungwa mbele ya ofisa wa serikali, na huenda zikahusisha kuweka nadhiri ya ndoa na kutia sahihi cheti. Wakristo fulani wanapendelea ndoa za kiserikali badala ya ndoa za kimila. Si takwa la kisheria kufuata taratibu zote mbili; kila moja ya ndoa hizo ni halali kisheria. Yale yanayosemwa katika fungu la 9 na la 10 kuhusu hotuba ya arusi na nadhiri yanahusu pia ndoa za kiserikali. Jambo muhimu ni kwamba wenzi hao wamefunga ndoa kwa njia inayoheshimika machoni pa Mungu na wanadamu.—Luka 20:25; 1 Petro 2:13, 14.
Kudumisha Heshima Katika Ndoa
15, 16. Heshima inapaswa kuonyeshwaje katika ndoa?
15 Tatizo lilipotokea katika ndoa ya mfalme Mwajemi, mshauri mkuu aliyeitwa Memukani alitoa shauri lifuatalo ambalo lingekuwa lenye manufaa: ‘Wake wote wawape waume zao heshima.’ (Esta 1:20) Katika ndoa za Kikristo, shauri hilo halihitaji kutolewa na mfalme yeyote wa kibinadamu kwa sababu wake huwaheshimu waume zao kwa kupenda. Vivyo hivyo, waume Wakristo huwapa wake zao heshima na kuwasifu. (Methali 31:11, 30; 1 Petro 3:7) Si lazima miaka mingi ipite ili mtu aanze kuiheshimu ndoa yake. Anapaswa kuanza kuiheshimu tangu mwanzo, yaani, tangu siku ya arusi.
16 Heshima hiyo haipaswi kuonyeshwa tu na mwanamume na mwanamke, au mume na mke siku ya arusi. Ikiwa mzee Mkristo atatoa hotuba ya arusi, anapaswa kuitoa kwa njia yenye heshima. Hotuba hiyo inapaswa kuelekezwa kwa wale wanaofunga ndoa. Msemaji atawaheshimu wenzi hao kwa kuepuka mizaha au hadithi za kitamaduni. Hapaswi kutia ndani mambo aliyojionea ambayo yanaweza kuwaaibisha wenzi hao na wasikilizaji. Badala yake, atajitahidi kuwa mchangamfu na mwenye kujenga, huku akikazia Mwanzilishi wa ndoa na mashauri Yake bora. Naam, mzee akitoa hotuba ya arusi kwa njia yenye heshima atasaidia kuifanya ndoa hiyo imletee Yehova Mungu heshima.
17. Kwa nini arusi za Kikristo huhusisha matakwa ya kisheria?
17 Yaelekea kwamba umeona makala hii ina mambo mengi ya kisheria kuhusu ndoa. Huenda baadhi ya mambo hayo yasihusu eneo lenu moja kwa moja. Hata hivyo, sote tunapaswa kutambua kwamba ni muhimu mipango ya arusi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ipatane na sheria za nchi na matakwa ya Kaisari. (Luka 20:25) Paulo alituhimiza hivi: “Wapeni wote haki zao, yeye anayetaka kodi, kodi; yeye anayetaka ushuru, ushuru; yeye anayetaka . . . heshima, heshima hiyo.” (Waroma 13:7) Naam, inafaa Wakristo, tangu siku ya arusi, waheshimu mpango wa Mungu uliopo sasa wa ndoa.
18. Arusi inaweza kutia ndani jambo gani linalohitaji kutiliwa maanani, na ni wapi tunapoweza kupata habari kuhusu jambo hilo?
18 Arusi nyingi za Kikristo hutia ndani tafrija na karamu. Kumbuka kwamba Yesu alihudhuria karamu ya arusi. Ikiwa arusi itakuwa na tafrija kama hiyo, mashauri ya Biblia yanaweza kutusaidiaje kufanya tafrija hiyo kwa njia ambayo itamheshimu Mungu na kuwaletea sifa wenzi hao wapya na kutaniko la Kikristo? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.e
-
-
Thibitisha Imani Yako Kupitia Maisha YakoMnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 15
-
-
Thibitisha Imani Yako Kupitia Maisha Yako
“Imani, ikiwa haina matendo, imekufa yenyewe.”—YAKOBO 2:17.
1. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walitilia maanani imani na matendo?
KWA ujumla, Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha imani yao kupitia maisha yao. Mwanafunzi Yakobo aliwahimiza hivi Wakristo wote: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.” Naye akaongeza hivi: “Kama vile ambavyo mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo pia imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 1:22; 2:26) Miaka 35 hivi baada ya kuandika maneno hayo, bado Wakristo wengi walikuwa wakithibitisha imani yao kwa matendo yanayofaa. Lakini inasikitisha kwamba wengine hawakuwa wakifanya hivyo. Yesu alilipongeza kutaniko la Smirna; lakini aliwaambia hivi washiriki wengi wa kutaniko la Sardi: “Mimi nayajua matendo yako, kwamba una jina kuwa uko hai, lakini umekufa.”—Ufunuo 2:8-11; 3:1.
2. Wakristo wanapaswa kujiuliza maswali gani kuhusu imani yao?
2 Hivyo, Yesu aliwahimiza Wakristo huko Sardi na wengine ambao baadaye wangesoma maneno yake wathibitishe upendo wao wa kwanza kuelekea kweli ya Kikristo na kuwa macho kiroho. (Ufunuo 3:2, 3) Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Matendo yangu yakoje? Je, matendo yangu yanaonyesha waziwazi kwamba ninafanya yote niwezayo kuthibitisha imani yangu katika shughuli zangu zote, hata katika mambo yasiyohusiana moja kwa moja na kazi ya kuhubiri au mikutano ya kutaniko?’ (Luka 16:10) Kuna mambo mengi maishani yanayohusika, lakini acheni tuzungumzie jambo moja tu: tafrija, kutia ndani zile zinazofanywa katika arusi za Kikristo.
Tafrija Ndogo
3. Biblia inasema nini kuhusu kushiriki katika tafrija?
3 Wengi wetu hufurahia kualikwa kwenye tafrija ya Wakristo wenye furaha. Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” ambaye hutaka watumishi wake wawe wenye furaha. (1 Timotheo 1:11) Mungu alimwongoza Sulemani kuandika jambo hili la hakika katika Biblia: “Nikapongeza kushangilia, kwa sababu wanadamu hawana jambo bora chini ya jua kuliko kula na kunywa na kushangilia, na kwamba hilo liambatane nao katika kazi yao ngumu muda wa siku za maisha yao.” (Mhubiri 3:1, 4, 13; 8:15) Shangwe hiyo inaweza kuonekana familia inapokula pamoja au katika tafrija nyingine ndogo ya waabudu wa kweli.—Ayubu 1:4, 5, 18; Luka 10:38-42; 14:12-14.
4. Mtu anayepanga tafrija anapaswa kufikiria nini?
4 Ikiwa unapanga na kusimamia tafrija kama hiyo, unapaswa kufikiria kwa uangalifu mambo yatakayohusika, hata ikiwa unawaalika waamini wachache tu kwa ajili ya chakula na mazungumzo ya kirafiki. (Waroma 12:13) Ni vizuri uhakikishe kwamba ‘mambo yote yanatendeka kwa adabu,’ yakiongozwa na “hekima inayotoka juu.” (1 Wakorintho 14:40; Yakobo 3:17) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu. Epukeni kuwa vikwazo.” (1 Wakorintho 10:31, 32) Ni baadhi ya mambo gani yanayohitaji kufikiriwa kwa uangalifu sana? Kufikiria mambo hayo mapema kunaweza kukusaidia kuhakikisha kwamba mambo ambayo wewe na wageni wako mtafanya yataonyesha imani yenu kupitia matendo.—Waroma 12:2.
Mtafanya Tafrija ya Aina Gani?
5. Kwa nini yule anayepanga tafrija anapaswa kufikiria kwa uangalifu ikiwa ataandaa vileo na kuwa na muziki?
5 Watu wengi wanaopanga tafrija huhitaji kuamua iwapo wataandaa vileo. Si lazima kuwe na vileo ili tafrija iwe yenye kujenga. Kumbuka kwamba Yesu aliandaa chakula kwa ajili ya kundi kubwa la watu waliomjia. Aliwaandalia mikate na samaki wengi. Simulizi hilo halisemi kwamba aliandaa divai kimuujiza ingawa tunajua kwamba angeweza kufanya hivyo. (Mathayo 14:14-21) Ukiamua kuandaa vileo kwenye tafrija, uwe mwenye kiasi na uhakikishe kwamba kuna vinywaji vingine kwa ajili ya wale wasiokunywa vileo. (1 Timotheo 3:2, 3, 8; 5:23; 1 Petro 4:3) Usimlazimishe kamwe mtu yeyote anywe kinywaji ambacho kinaweza kumuuma “kama nyoka.” (Methali 23:29-32) Namna gani muziki au kuimba? Ikiwa tafrija yenu itakuwa na muziki, bila shaka utachagua muziki huo kwa uangalifu ukifikiria mdundo na maneno ya nyimbo. (Wakolosai 3:8; Yakobo 1:21) Wakristo wengi wameona kwamba kucheza nyimbo za Ufalme (Kingdom Melodies au Mélodies du Royaume) au hata kuimba nyimbo hizo pamoja hufanya tafrija iwe yenye furaha. (Waefeso 5:19, 20) Na nyakati zote hakikisha kwamba muziki hauchezwi kwa sauti ya juu hivi kwamba unavuruga mazungumzo mazuri au kuwasumbua majirani.—Mathayo 7:12.
6. Mwenye kupanga tafrija anaweza kuonyeshaje kwamba ana imani iliyo hai katika mazungumzo au shughuli nyinginezo?
6 Kwenye tafrija, Wakristo wanaweza kuzungumzia mambo mbalimbali, kusoma habari fulani kwa sauti, au kusimulia mambo yaliyoonwa yenye kupendeza. Ikiwa mazungumzo yanaenda kombo, yule mwenye kupanga tafrija anaweza kuyanyoosha kwa busara. Pia, anapaswa kuwa mwangalifu ili yeyote asitawale mazungumzo. Ikiwa mtu fulani anatawala mazungumzo, mwenye kupanga tafrija anaweza kuingilia mazungumzo kwa busara na kuwahusisha wengine, labda kwa kuwaomba wachanga wajieleze au kwa kuzungumzia jambo tofauti litakalowachochea wengine watoe maoni yao. Vijana kwa wazee watafurahia jambo hilo katika tafrija. Ikiwa wewe unayesimamia utaelekeza mambo kwa hekima na busara, ‘usawaziko wako utajulikana’ kwa wahudhuriaji wote. (Wafilipi 4:5) Wataona wazi kwamba una imani iliyo hai, na unaionyesha katika sehemu zote za maisha yako.
Arusi na Karamu za Arusi
7. Kwa nini kupanga arusi na tafrija za arusi kunahitaji uangalifu wa pekee?
7 Arusi ya Kikristo ni mojawapo ya matukio yenye kuleta shangwe. Watumishi wa kale wa Mungu, kutia ndani Yesu na wanafunzi wake, walikubali kushiriki katika matukio hayo yenye furaha, kutia ndani karamu. (Mwanzo 29:21, 22; Yohana 2:1, 2) Hata hivyo, hivi karibuni, imeonekana wazi kwamba kupanga tafrija za arusi kunahitaji jitihada za pekee ili tafrija hizo ziendeshwe kwa busara na usawaziko wa Kikristo. Lakini, tafrija ni mambo ya kawaida katika maisha yanayompa Mkristo nafasi ya kuonyesha imani yake.
8, 9. Desturi za arusi nyingi zinapatanaje na maneno tunayosoma kwenye 1 Yohana 2:16, 17?
8 Watu wengi ambao hawajui wala hawajali kanuni za Kimungu, huona arusi kuwa nafasi ya kufanya mambo kupita kiasi, au mahali ambapo mtu ana uhuru wa kufanya lolote atakalo. Mwanamke mmoja aliyeolewa hivi karibuni aliliambia hivi gazeti moja la Ulaya kuhusu arusi yake ya “kifalme”: ‘Tulibebwa katika msafara wenye magari manne yenye kukokotwa na farasi na kufuatwa na magari mengine 12 yenye kukokotwa na farasi, na gari lingine lenye bendi inayopiga muziki. Kisha, kukawa na chakula kitamu sana na muziki motomoto; ilikuwa sherehe kubwa. Siku hiyo nilikuwa malkia kama nilivyotamani.’
9 Huenda desturi zikatofautiana katika sehemu mbalimbali, lakini maneno hayo yanapatana kabisa na yale ambayo mtume Yohana aliandika: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” Je, unaweza kuwazia Wakristo wakomavu wakitaka kufanya arusi ya “kifalme” yenye karamu kubwa? Badala ya kufanya hivyo, mtazamo wao unapaswa kuonyesha kwamba wanatambua kuwa “yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:16, 17.
10. (a) Ili kuwa na arusi yenye usawaziko, kwa nini ni muhimu kufanya mipango? (b) Maamuzi kuhusu wageni watakaoalikwa yanapaswa kufanywaje?
10 Wenzi Wakristo wanahitaji kuona mambo kihalisi na kuwa na usawaziko, na Biblia inaweza kuwasaidia. Ingawa siku ya arusi ni muhimu, wanajua kwamba ni mwanzo tu wa ndoa ya Wakristo wawili ambao wanatazamia kuishi milele. Hawahitaji kufanya karamu kubwa ya arusi. Wakiamua kufanya tafrija, wanapaswa kuhesabu gharama yake na kufikiria jinsi itakavyokuwa. (Luka 14:28) Wakiwa pamoja kama Wakristo, mume ndiye kichwa kulingana na Maandiko. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:22, 23) Hivyo, bwana-arusi ndiye aliye na daraka la kusimamia karamu ya arusi. Bila shaka, atawasiliana na bibi-arusi kuhusu mambo kama vile wageni watakaoalikwa au idadi ya wageni watakaohudhuria karamu ya arusi. Huenda isiwezekane au isifae kuwaalika marafiki na watu wote wa ukoo. Kwa hiyo, huenda watahitaji kufanya maamuzi fulani kwa usawaziko. Wenzi hao wanapaswa kuwa na uhakika kwamba hata wasipowaalika baadhi ya Wakristo wenzao, Wakristo hao wataelewa na hawataudhika.—Mhubiri 7:9.
“Msimamizi wa Karamu”
11. “Msimamizi wa karamu” anaweza kutimiza nini katika arusi?
11 Wenzi wakiamua kufanya karamu ya arusi, wanaweza kuhakikishaje kwamba karamu hiyo ni yenye heshima? Kwa miaka mingi sasa, Mashahidi wa Yehova wametambua hekima ya kutilia maanani jambo fulani linalotajwa kuhusiana na kikusanyiko ambacho Yesu alihudhuria huko Kana. Kulikuwa na “msimamizi wa karamu,” ambaye bila shaka alikuwa mwamini mkomavu. (Yohana 2:9, 10) Vivyo hivyo, bwana-arusi mwenye hekima atachagua ndugu Mkristo aliye mkomavu kiroho atimize daraka hilo muhimu. Baada ya kujua mapendezi ya bwana-arusi, msimamizi wa karamu anaweza kutekeleza mapendezi hayo kabla na wakati wa karamu.
12. Bwana-arusi anapaswa kufikiria nini kuhusu matumizi ya vileo?
12 Kupatana na yale tuliyozungumzia kwenye fungu la 5, wenzi fulani huamua kutoandaa vileo katika karamu ili visitumiwe vibaya na hivyo kufanya karamu hiyo isiwe yenye furaha na isifanikiwe. (Waroma 13:13; 1 Wakorintho 5:11) Hata hivyo, ikiwa vileo vitaandaliwa, bwana-arusi anapaswa kuhakikisha kwamba vinaandaliwa kwa kiasi. Kulikuwa na divai kwenye arusi ambayo Yesu alihudhuria huko Kana, naye aliandaa divai nzuri. Inapendeza kwamba msimamizi huyo wa karamu alieleza hivi: “Wengine wote hutoa divai nzuri kwanza, na ile hafifu wakati ambapo watu wameingiwa na kileo. Wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.” (Yohana 2:10) Hapana shaka kwamba Yesu hakuwatia moyo watu walewe, kwa kuwa alichukia zoea hilo. (Luka 12:45, 46) Akistaajabia uzuri wa divai hiyo, msimamizi huyo alionyesha wazi kwamba aliwahi kuwaona watu fulani wakilewa katika karamu ya arusi. (Matendo 2:15; 1 Wathesalonike 5:7) Kwa hiyo, bwana-arusi na Mkristo mwenye kutegemeka ambaye amemweka kuwa msimamizi wa karamu wanapaswa kuhakikisha kwamba wahudhuriaji wote wanafuata mwongozo huu ulio wazi: “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake.”—Waefeso 5:18; Methali 20:1; Hosea 4:11.
13. Wenzi wanapaswa kufikiria nini wakiamua kuwa na muziki kwenye karamu yao ya arusi, na kwa nini?
13 Kama ilivyo kwenye tafrija nyinginezo, ikiwa kutakuwa na muziki, kiasi cha sauti kinapaswa kutiliwa maanani ili kuwawezesha watu wazungumze bila shida. Mzee mmoja Mkristo alisema hivi: “Kadiri usiku unavyoingia, wakati mazungumzo yanapopamba moto au watu wanapoanza kucheza dansi, ndivyo nyakati nyingine sauti ya muziki inavyoongezeka. Muziki uliokuwa ukichezwa kwa sauti ya chini unaweza kuwa wenye kelele na kuvuruga mazungumzo. Karamu ya arusi ni pindi ya kuwa na ushirika mzuri. Ingesikitisha kama nini ikiwa muziki ungechezwa kwa sauti ya juu na hivyo kuvuruga pindi hiyo!” Katika jambo hilo, bwana-arusi na msimamizi wa karamu wanahitaji kuchukua hatua ya kuamua aina ya na kiasi cha sauti ya muziki, bila kuacha daraka hilo mikononi mwa wanaoshughulikia muziki, iwe wamekodiwa au hapana. Paulo aliandika hivi: “Lolote lile mnalofanya kwa neno au kwa tendo, fanyeni kila jambo katika jina la Bwana Yesu.” (Wakolosai 3:17) Wageni wanaporudi nyumbani baada ya karamu ya arusi, je, watakumbuka kuwa muziki ulionyesha kwamba wenzi hao walifanya kila jambo kwa jina la Yesu? Inapaswa kuwa hivyo.
14. Wakristo wanapaswa kukumbuka nini kwa shangwe kuhusiana na arusi?
14 Naam, arusi iliyopangwa vizuri inaweza kukumbukwa kwa shangwe. Adam na Edyta, ambao walifunga ndoa miaka 30 iliyopita, walisema hivi kuhusu arusi moja: “Ungeweza kwa kweli kuona roho ya Kikristo. Kulikuwa na nyimbo za kumsifu Yehova na vilevile burudani nyingine nzuri. Kucheza dansi na muziki hayakuwa mambo muhimu. Ilikuwa sherehe yenye kupendeza na yenye kujenga, na kila kitu kilifanywa kupatana na kanuni za Biblia.” Ni wazi kwamba kuna mambo mengi ambayo bwana na bibi-arusi wanaweza kufanya ili kuthibitisha imani yao kwa matendo.
Zawadi za Arusi
15. Ni mashauri gani ya Biblia yanayoweza kufuatwa kuhusu zawadi za arusi?
15 Katika nchi nyingi ni jambo la kawaida kwa marafiki na watu wa ukoo kuwapa zawadi wale wanaofanya arusi. Ni vizuri kukumbuka nini ukiamua kutoa zawadi? Kumbuka maneno haya ya mtume Yohana: “Mtu kujionyesha mali yake maishani.” Yohana hakuhusianisha jambo hilo na Wakristo ambao wanaonyesha imani yao kwa matendo, lakini alilihusianisha na ‘ulimwengu ambao unapitilia mbali.’ (1 Yohana 2:16, 17) Tukifikiria maneno ya Yohana yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, je, wenzi hao wapya wanapaswa kutangaza majina ya wale ambao wametoa zawadi? Wakristo wa Makedonia na Akaya walitoa michango kwa ajili ya akina ndugu huko Yerusalemu, lakini hakuna jambo linaloonyesha kwamba majina yao yalitangazwa. (Waroma 15:26) Wakristo wengi wanaotoa zawadi za arusi wasingetaka wajulikane ili wasijiletee sifa. Kuhusu jambo hilo, fikiria shauri la Yesu kwenye Mathayo 6:1-4.
16. Kuhusiana na zawadi za arusi, wenzi wapya wanaweza kuepukaje kuumiza hisia za wengine?
16 Kutangaza majina ya waliotoa zawadi kunaweza “kuchochea mashindano” kuhusu ni zawadi gani iliyo bora au ghali zaidi. Hivyo, wenzi wapya Wakristo huepuka kutangaza majina ya wenye kutoa zawadi. Kutangaza majina ya watu wanaotoa zawadi kwaweza kuwaaibisha wengine ambao labda hawakuweza kutoa zawadi. (Wagalatia 5:26; 6:10) Kwa kweli si vibaya kwa bwana na bibi-arusi kujua ni nani aliyetoa zawadi fulani. Labda wanaweza kuona jina la yule aliyetoa zawadi kwenye kadi iliyoambatanishwa na zawadi hiyo ingawa haitasomwa mbele ya watu wote. Tunaponunua, kutoa, au kupokea zawadi za arusi, sote tuna nafasi ya kuthibitisha kwamba hata katika jambo la kibinafsi kama hilo, imani yetu inaonyeshwa kwa matendo yetu.a
17. Wakristo wanapaswa kuwa na lengo gani kuhusiana na imani na matendo yao?
17 Kuthibitisha imani yetu kunahusisha mengi zaidi ya kuishi maisha ya adili, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Acheni kila mmoja wetu awe na imani iliyo hai ambayo inamwongoza katika kila jambo analofanya. Naam, tunaweza kuonyesha imani yetu kwa matendo ambayo ‘yanafanywa kwa ukamili,’ kutia ndani yale ambayo tumezungumzia.—Ufunuo 3:2.
18. Maneno ya Yohana 13:17 yanaweza kuthibitikaje kuwa ya kweli kuhusiana na arusi za Kikristo na tafrija?
18 Baada ya Yesu kuwawekea mitume wake waaminifu kielelezo kizuri kwa kujishusha na kuwaosha miguu, alisema hivi: “Ikiwa mnajua mambo haya, wenye furaha ni ninyi ikiwa mnayatenda.” (Yohana 13:4-17) Katika maeneo tunamoishi leo, huenda isiwe lazima au jambo la kawaida kuosha miguu ya mtu mwingine, kama vile mgeni anayetutembelea. Hata hivyo, kama tulivyoona katika makala hii, tunaweza kuonyesha imani yetu kwa kuwatendea wengine kwa upendo na ufikirio katika mambo mengine maishani, kutia ndani yale yanayohusu tafrija na arusi za Kikristo. Tunaweza kufanya hivyo iwe tunafanya arusi au tumealikwa kwenye arusi au tafrija ya arusi ya Wakristo wenye furaha ambao wanataka kuonyesha imani yao kwa matendo.
[Maelezo ya Chini]
a Mambo mengine kuhusu arusi na karamu za arusi yanazungumziwa katika makala inayofuata yenye kichwa, “Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi.”
Ungejibuje?
Unaweza kuthibitishaje imani yako
• unapopanga tafrija?
• unapopanga arusi au karamu ya arusi?
• unapotoa au kupokea zawadi za arusi?
[Picha katika ukurasa wa 24]
Hata unapowaalika watu wachache tu, ongozwa na “hekima inayotoka juu”
-
-
Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya ArusiMnara wa Mlinzi—2006 | Oktoba 15
-
-
Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi
“SIKU yangu ya arusi ilikuwa mojawapo ya siku muhimu zaidi na yenye shangwe maishani mwangu,” akasema Gordon, ambaye amekuwa katika ndoa kwa karibu miaka 60. Ni nini kinachofanya siku ya arusi iwe muhimu kwa Wakristo wa kweli? Hiyo ni siku ambayo wanafanya nadhiri takatifu kwa wale ambao wanawapenda sana, yaani, mwenzi wao na Yehova Mungu. (Mathayo 22:37; Waefeso 5:22-29) Naam, watu wanaopanga kufunga ndoa wangependa kufurahia siku yao ya arusi, lakini pia wanataka kumheshimu Mwanzilishi wa ndoa.—Mwanzo 2:18-24; Mathayo 19:5, 6.
Bwana-arusi anaweza kuongezaje heshima ya pindi hiyo yenye furaha? Bibi-arusi anaweza kuonyeshaje heshima kwa mume wake na kwa Yehova? Wengine wanaohudhuria wanaweza kuongezaje shangwe ya siku ya arusi? Kuchunguza kanuni kadhaa za Biblia kutatusaidia kujibu maswali hayo, na kufuata kanuni hizo kutapunguza matatizo ambayo yanaweza kuvuruga pindi hiyo ya pekee.
Ni Nani Mwenye Daraka?
Katika nchi nyingi huenda mhudumu aliye Shahidi wa Yehova akafunganisha ndoa kisheria. Hata katika nchi ambako ni lazima ndoa ifunganishwe kisheria na ofisa wa serikali, huenda wenzi fulani wakataka hotuba inayotegemea Biblia itolewe kwa ajili yao. Kwa kawaida, hotuba hiyo humhimiza bwana-arusi afikirie wajibu aliopewa na Mungu akiwa kichwa cha familia. (1 Wakorintho 11:3) Kwa hiyo, bwana-arusi ndiye aliye na daraka kuu kuhusiana na mambo yanayotukia katika arusi. Bila shaka, kwa kawaida mipango ya arusi na tafrija ambayo huenda ikafuata hufanywa mapema. Kwa nini huenda ikawa vigumu kufanya mipango hiyo?
Sababu moja ni kwamba watu wa ukoo wanaweza kujaribu kuongoza mipango ya arusi. Rodolfo, ambaye amefunganisha ndoa nyingi, anasema: “Nyakati nyingine, bwana-arusi hubanwa sana na watu wa ukoo, hasa ikiwa wanasaidia kulipia gharama za karamu ya arusi. Huenda wakawa na kauli zenye nguvu kuhusu mambo yatakayofanywa katika arusi na kwenye karamu ya arusi. Hilo linaweza kumnyang’anya bwana-arusi daraka lake la Kimaandiko la kusimamia tukio hilo.”
Max, ambaye amekuwa akifunganisha ndoa kwa miaka zaidi ya 35, anasema hivi: “Nimeona kuna mwelekeo wa bibi-arusi kuongoza katika kuamua mambo yatakayotukia katika arusi na kwenye karamu ya arusi, huku bwana-arusi akinyimwa nafasi ya kutoa maoni yake.” David, ambaye pia amefunganisha ndoa nyingi anaeleza hivi: “Huenda mabwana-arusi hawajazoea kuongoza na kwa kawaida hawajihusishi sana katika matayarisho ya arusi.” Bwana-arusi anaweza kutimizaje ifaavyo daraka lake?
Mawasiliano Huongeza Shangwe
Ili bwana-arusi afaulu kutimiza kwa mafanikio daraka lake kuhusiana na matayarisho ya arusi, anapaswa kuwasiliana vizuri. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) Hata hivyo, ili mipango isivunjike, bwana-arusi anaweza kuzungumzia matayarisho ya arusi pamoja na bibi-arusi, watu wa familia, na wengine ambao wanaweza kutoa mashauri mazuri yanayotegemea Biblia.
Naam, ni muhimu wale wanaotarajia kufunga ndoa wazungumze kwanza pamoja kuhusu mipango na mambo yanayoweza kufanywa. Kwa nini? Kwa mfano, ona alichosema Ivan na mke wake, Delwyn, wanaotoka katika malezi tofauti lakini ambao wamefurahia maisha ya ndoa kwa miaka mingi. Akikumbuka mipango ya arusi yao, Ivan anasema hivi: “Nilikuwa na mawazo hususa kuhusu yale niliyotaka yafanywe katika arusi yangu, kutia ndani karamu pamoja na marafiki wangu wote, keki ya arusi, na bibi-arusi aliyevalia nguo nyeupe. Kwa upande mwingine, Delwyn, alitaka tuwe na arusi ndogo, na isiyo na mambo mengi wala keki ya arusi. Hata alifikiria kuvaa nguo ya kawaida badala ya nguo ya arusi.”
Wenzi hao walitatuaje tofauti hizo? Waliwasiliana kwa fadhili na unyoofu. (Methali 12:18) Ivan anaongeza hivi: “Tulijifunza makala zinazotegemea Biblia kuhusu arusi, kama zile zilizochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la Septemba 15, 1984, au Kiingereza, Aprili 15, 1984, au Kifaransa, Julai 15, 1984.a Makala hizo zilitusaidia kuwa na maoni ya kiroho kuhusu arusi. Kwa sababu ya malezi yetu tofauti, tulihitaji kukubaliana katika mambo kadhaa ya kibinafsi. Sote tulibadili mtazamo wetu.”
Aret na Penny walifanya vivyo hivyo. Aret anasema hivi kuhusu siku yao ya arusi: “Mimi na Penny tulizungumzia mapendezi yetu kuhusiana na arusi, na tuliweza kukubaliana. Tulisali ili Yehova abariki siku hiyo. Pia, nilitafuta mashauri ya wazazi wetu na baadhi ya wenzi walio wakomavu kutanikoni. Mapendekezo yao yalitusaidia sana. Kwa sababu hiyo, arusi yetu ilikuwa nzuri sana.”
Kudumisha Heshima Katika Mavazi na Mapambo
Ni jambo linaloeleweka kwa bibi na bwana-arusi kutaka kuvalia kwa njia iliyo nzuri siku yao ya arusi. (Zaburi 45:8-15) Huenda wakatumia wakati, jitihada, na pesa kununua mavazi yanayofaa. Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kuwasaidia kuchagua mavazi yenye heshima na yanayovutia?
Fikiria mavazi ambayo bibi-arusi anavaa siku hiyo. Mashauri ya Biblia yanafaa kila mahali, licha ya kwamba kila mtu ana mapendezi yake na kila nchi ina mitindo yake ya mavazi. Wanawake wanapaswa ‘kujipamba kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.’ Shauri hilo linawafaa wanawake Wakristo nyakati zote, na bila shaka linahusu pia siku ya arusi. Ukweli ni kwamba si lazima kuwa na “mavazi yaliyo ghali sana” ili arusi iwe yenye shangwe. (1 Timotheo 2:9; 1 Petro 3:3, 4) Inaridhisha kama nini kufuata shauri hilo!
David, aliyetajwa mwanzoni, anaeleza hivi: “Wenzi wengi hujitahidi kufuata kanuni za Biblia, na wanastahili kupongezwa. Hata hivyo, nyakati nyingine, mabibi-arusi na waandamani wao huvaa nguo zisizo na kiasi ambazo hazifichi sehemu kubwa ya kifua au nguo nyepesi zinazoonyesha mwili.” Mzee fulani ambaye ni Mkristo mkomavu anapozungumza na bibi na bwana-arusi kabla ya arusi, huwasaidia kuwa na mtazamo wa kiroho. Jinsi gani? Kwa kuwauliza ikiwa nguo watakazovaa zitakuwa zenye kiasi hivi kwamba zinaweza kuvaliwa kwenye mikutano ya Kikristo. Ni kweli kwamba mtindo wa nguo za arusi unaweza kuwa tofauti na ule wa nguo zinazovaliwa kwenye mikutano ya kawaida na nguo hizo zinaweza kupatana na desturi za mahali, lakini zinapaswa kuwa zenye kiasi kulingana na viwango vya Kikristo vyenye heshima. Hata ikiwa watu fulani ulimwenguni wanaona viwango vya maadili vya Biblia kuwa vyenye kubana mno, Wakristo wa kweli huwa tayari kupinga jitihada za ulimwengu za kuwafinyanga wafanane nao.—Waroma 12:2; 1 Petro 4:4.
Penny anasema: “Badala ya kuona mavazi au karamu ya arusi kuwa ndiyo mambo muhimu zaidi, mimi na Aret tulikazia fikira sehemu ya kiroho ya tukio hilo. Hiyo ndiyo iliyokuwa sehemu muhimu zaidi ya siku hiyo. Mambo ya pekee ninayokumbuka si, nguo nilizovaa au chakula nilichokula, bali ni watu nilioshirikiana nao siku hiyo na furaha niliyopata kwa sababu ya kuolewa na mwanamume ninayempenda.” Ni vizuri wenzi Wakristo wakumbuke mambo hayo wanapopanga arusi yao.
Jumba la Ufalme—Mahali Panapoheshimiwa
Inapowezekana, wenzi wengi Wakristo hupendelea arusi yao ifanyiwe katika Jumba la Ufalme. Kwa nini wao hupendelea Jumba la Ufalme? Wenzi fulani walieleza sababu yao: “Tulitambua kwamba ndoa ni mpango mtakatifu wa Yehova. Kufunga ndoa katika Jumba la Ufalme, mahali petu pa ibada, kulikazia akilini mwetu tangu mwanzo kwamba Yehova anapaswa kuwa sehemu ya ndoa yetu. Faida nyingine ya kufanyia arusi katika Jumba la Ufalme badala ya mahali pengine ni kwamba watu wetu wa ukoo wasio waamini ambao walihudhuria waliona jinsi tunavyothamini sana ibada ya Yehova.”
Wazee wa kutaniko wanaohusika wakikubali Jumba la Ufalme litumiwe kwa ajili ya arusi, wenzi hao wanapaswa kuwajulisha mapema kuhusu matayarisho yatakayofanywa. Njia moja ambayo bibi na bwana-arusi wanaweza kuonyesha kwamba wanawaheshimu wale walioalikwa kwenye arusi ni kuazimia kabisa kufika kwa wakati. Na bila shaka, wanapaswa kuhakikisha kwamba mambo yote yanafanywa kwa njia ya heshima.b (1 Wakorintho 14:40) Hivyo, wataepuka vituko vinavyofanywa katika arusi nyingi za kilimwengu.—1 Yohana 2:15, 16.
Pia, wale wanaohudhuria arusi wanaweza kuonyesha kwamba wana maoni ya Yehova kuhusu ndoa. Kwa mfano, hawapaswi kutarajia arusi hiyo iwe bora kuliko arusi nyingine za Kikristo, kana kwamba kuna mashindano ya arusi iliyokuwa kubwa. Wakristo wakomavu wanatambua pia kwamba kuwa katika Jumba la Ufalme kwa ajili ya hotuba inayotegemea Biblia ni jambo muhimu na lenye faida zaidi kuliko kuhudhuria karamu ya arusi au tafrija ambayo huenda ikafuata. Ikiwa wakati au hali zinamruhusu Mkristo kuhudhuria tukio moja tu kati ya matukio hayo mawili, bila shaka itafaa kuwa katika Jumba la Ufalme. Mzee anayeitwa William anasema hivi: “Ikiwa wageni wanakosa kwenda katika Jumba la Ufalme bila sababu lakini wanaenda kwenye karamu ya arusi baadaye, hilo linaonyesha kwamba hawathamini utakatifu wa tukio hilo. Hata ikiwa hatukualikwa kwenye karamu, tunaweza kuonyesha kwamba tunawaunga mkono bibi na bwana-arusi na kutoa ushahidi mzuri kwa watu wa ukoo wasio waamini kwa kuhudhuria arusi katika Jumba la Ufalme.”
Shangwe Inayodumu Hata Baada ya Siku ya Arusi
Wafanya-biashara hujipatia faida kubwa kutokana na sherehe za arusi. Ripoti moja ya hivi karibuni inasema kwamba arusi ya kawaida nchini Marekani “hugharimu dola 22,000 za Marekani, au nusu ya mshahara wa wastani wa [mwaka nzima] katika familia ya Kimarekani.” Wenzi wengi wapya na familia zao hushawishiwa na matangazo ya biashara na hivyo kujiingiza katika deni kubwa kwa ajili ya siku hiyo moja, deni ambalo wanalipa kwa miaka mingi. Je, hiyo ni njia ya busara ya kuanzisha ndoa? Huenda wale wasiojua au wasiojali kanuni za Biblia wakaamua kutumia pesa nyingi hivyo, lakini Wakristo wa kweli wako tofauti kama nini!
Wenzi wengi Wakristo wamefanya arusi ndogo zenye usawaziko na gharama ndogo huku wakikazia sehemu ya kiroho ya tukio hilo. Hivyo, wameweza kutumia wakati na mali zao kulingana na wakfu wao kwa Mungu. (Mathayo 6:33) Fikiria mfano wa Lloyd na Alexandra, ambao wamekuwa katika huduma ya wakati wote kwa miaka 17 tangu wafunge ndoa. Lloyd anasema hivi: “Huenda watu fulani waliona arusi yetu kuwa tukio ndogo, lakini mimi na Alexandra tuliifurahia sana. Tulihisi kwamba arusi yetu haipaswi kutulemea kifedha, bali inapaswa kuwa siku ya kusherehekea mpango wa Yehova wa kuwaletea watu wawili furaha kubwa.”
Alexandra anaongezea hivi: “Kabla ya kufunga ndoa nilikuwa painia, na sikutaka kuacha pendeleo hilo ili nifanye arusi kubwa. Arusi yetu ilikuwa ya pekee sana. Hata hivyo, ilikuwa siku ya kwanza tu ya sisi kuishi pamoja. Tulifuata mashauri ya kuepuka kukazia sana sherehe ya kufunga ndoa na tumetafuta mwongozo wa Yehova katika maisha yetu ya ndoa. Bila shaka, hilo limetuletea baraka za Yehova.”c
Naam, siku yenu ya arusi ni pindi ya pekee. Mitazamo na matendo yanayofanywa katika siku ya arusi yanaweza kuwa na uvutano katika maisha yenu ya ndoa miaka ijayo. Kwa hiyo, mtegemee Yehova ili akuongoze. (Methali 3:5, 6) Kazia akilini umuhimu wa kiroho wa tukio hilo. Mtegemezane katika kutimiza madaraka yenu mliyopewa na Mungu. Mkifanya hivyo, mtaiwekea ndoa yenu msingi imara, na mkiwa na baraka za Yehova, mtakuwa na shangwe itakayodumu kwa muda mrefu hata baada ya siku ya arusi.—Methali 18:22.
-