Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • 1 Kwa Nini Tusali?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      1 Kwa Nini Tusali?

      SALA. Kuna mambo machache katika Biblia yanayopendwa na ambayo husababisha udadisi mwingi kama vile sala. Fikiria maswali saba ambayo yanaulizwa kwa ukawaida kuhusu sala, na kisha ujiunge nasi ili kuchunguza majibu yanayopatikana katika Biblia. Makala hizi zimeandaliwa ili kukusaidia uanze kusali au uboreshe sala zako.

      ULIMWENGUNI pote, watu wa kila utamaduni na dini husali. Wanasali wakiwa peke yao au wakiwa kikundi. Wanasali wakiwa katika makanisa, mahekalu, masinagogi, misikiti, au mahali penginepo pa ibada. Wanatumia mikeka ya kusalia, rozari, magurudumu ya sala, sanamu, vitabu vya sala, au sala ambazo zimeandikwa katika vibao vidogo ambavyo huning’inizwa ukutani.

      Sala inawafanya wanadamu wawe tofauti na viumbe vingine vyote duniani. Ni kweli kwamba kwa kadiri fulani tunafanana na wanyama. Kama tu wanyama, tunahitaji chakula, hewa, na maji. Pia tunazaliwa, tunaishi, na kisha tunakufa. (Mhubiri 3:19) Lakini wanadamu pekee ndio wanaosali. Kwa nini?

      Labda jibu rahisi ni kwamba tuna uhitaji wa kusali. Kwa ujumla sala huonwa kuwa njia ya wanadamu ya kuwasiliana na ulimwengu wa roho, kuwasiliana na chochote ambacho watu hukiona kuwa kitakatifu na chenye kudumu. Biblia inaonyesha kwamba tuliumbwa tukiwa na tamaa ya mambo hayo. (Mhubiri 3:11) Wakati fulani Yesu Kristo alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

      Ni jambo linalopatana na akili kwamba ‘uhitaji wa kiroho’ ndio unaofanya watu wawe na majengo makubwa na vifaa vya ibada vya kale, na kutumia saa nyingi katika sala. Bila shaka, watu fulani hujitegemea au kuwategemea wanadamu wenzao ili kutosheleza mahitaji yao ya kiroho. Je, huoni kwamba wanadamu hawana uwezo wa kutosheleza uhitaji huo kikamili? Sisi ni dhaifu sana, maisha yetu ni mafupi, na hatuna uwezo wa kujua wakati ujao. Mtu anayeweza kutimiza uhitaji huo, lazima awe mwenye hekima, mwenye nguvu zaidi, na anayedumu kwa muda mrefu zaidi kuliko sisi. Ni mahitaji gani hayo ya kiroho ambayo yanatusukuma tusali?

      Fikiria hili: Je, umewahi kutamani kupata mwongozo, hekima, au majibu ya maswali yanayoonekana kuwa hayawezi kujibiwa na mwanadamu? Je, umewahi kuhisi kwamba unahitaji faraja baada ya kupata msiba mkubwa, au unahitaji kupata mwongozo wa kufanya uamuzi mzito, au kusamehewa baada ya kulemewa na hisia za hatia?

      Kulingana na Biblia, hizo zote ni sababu nzuri zinazoweza kumfanya mtu asali. Biblia ndicho kitabu kinachotegemeka zaidi kuhusiana na suala hili, na kina sala za wanaume na wanawake wengi waaminifu. Walisali ili wapate faraja, mwongozo, msamaha, na majibu ya maswali magumu.—Zaburi 23:3; 71:21; Danieli 9:4, 5, 19; Habakuki 1:3.

      Hata ingawa sala hizo zilitofautiana, zilikuwa na jambo fulani linalofanana. Wote waliotoa sala walitambua jambo fulani muhimu ambalo lilifanya sala zao zijibiwe, na ambalo linapuuzwa na watu leo. Walijua walipaswa kusali kwa nani.

  • 2 Tusali Kwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      2 Tusali Kwa Nani?

      JE, MUNGU anasikiliza sala zote bila kujali zinaelekezwa kwa nani? Leo, watu wengi wanafikiria hivyo. Wazo hilo linaungwa mkono na watu wanaopendelea kuchanganya ibada na wanaotaka dini zote zikubalike, ijapokuwa kuna tofauti kati ya dini hizo. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba wazo hilo si la kweli?

      Biblia inafundisha kwamba mara nyingi watu hawaelekezi sala zao kwa Mungu wa kweli. Zamani Biblia ilipokuwa ikiandikwa, lilikuwa jambo la kawaida kwa watu kuelekeza sala zao kwa sanamu za kuchongwa. Hata hivyo, Mungu alionya tena na tena kuhusu zoea hilo. Kwa mfano, andiko la Zaburi 115:4-6 linasema hivi kuhusu sanamu: “Zina masikio, lakini haziwezi kusikia.” Wazo hilo liko wazi. Kwa nini usali kwa mungu ambaye hawezi kukusikia?

      Simulizi fulani la Biblia linaeleza zaidi kuhusu jambo hilo. Nabii wa kweli Eliya aliwaambia manabii wa Baali wasali kwa mungu wao, kisha yeye asali kwa Mungu wake. Eliya alisema kwamba Mungu wa kweli angejibu sala lakini yule wa uwongo hangejibu. Manabii hao wa Baali walikubali kufanya hivyo, nao wakasali kwa bidii kwa muda mrefu, huku wakilia kwa sauti kubwa—lakini hawakufanikiwa! Simulizi hilo linasema: “Hapakuwa na yeyote aliyejibu, wala aliyewasikiliza.” (1 Wafalme 18:29) Lakini ni nini kilichotokea Eliya aliposali?

      Baada ya Eliya kusali, Mungu wake alijibu mara moja kwa kutuma moto kutoka mbinguni ili kuteketeza dhabihu ambayo Eliya alitayarisha. Kwa nini sala hiyo ilijibiwa? Kuna jambo moja muhimu katika sala ya Eliya ambayo inapatikana katika 1 Wafalme 18:36, 37. Sala yake ilikuwa fupi sana. Katika Kiebrania cha awali, sala hiyo ina maneno 30 hivi. Hata hivyo, katika maneno hayo machache, Eliya alitumia mara tatu jina la Mungu la kibinafsi, Yehova.

      Baali, ambaye jina lake linamaanisha “mmiliki” au “bwana,” alikuwa mungu wa Wakanaani, na kila eneo lilikuwa na sanamu yake ya Baali. Hata hivyo, Yehova ni jina la kipekee, linalomrejelea Mungu mmoja tu katika ulimwengu wote. Mungu huyu aliwaambia watu wake hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isaya 42:8.

      Je, sala ya Eliya na zile za manabii wa Baali zilienda kwa yule Mungu wa kweli? Ibada ya Baali iliwashushia watu heshima kwa kuwataka wafanye ukahaba na hata kutoa watu dhabihu. Kinyume cha hilo, ibada ya Yehova iliwakweza watu wake, Israeli, kwa kuwaepusha na matendo hayo mapotovu. Hebu fikiria hili: Ikiwa unamwandikia barua rafiki unayemheshimu sana, je, unaweza kutarajia barua hiyo ipelekwe kwa mtu mwenye jina tofauti na ambaye ana sifa tofauti na zile za rafiki yako? Bila shaka, hapana!

      Ikiwa unasali kwa Yehova, unasali kwa Muumba, ambaye ni Baba ya wanadamu wote.a Nabii Isaya alisali hivi: “Wewe, Ee Yehova, ni Baba yetu.” (Isaya 63:16) Huyo ndiye ambaye Yesu Kristo alimrejelea alipowaambia wafuasi wake: “Mimi ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.” (Yohana 20:17) Yehova ndiye Baba ya Yesu. Huyo ndiye Mungu ambaye Yesu alisali kwake na kuwafundisha wafuasi wake wafanye vivyo hivyo.—Mathayo 6:9.

      Je, Biblia inatuagiza tusali kwa Yesu, kwa Maria, kwa watakatifu, au kwa malaika? Hapana—tunapaswa kusali kwa Yehova tu. Acheni tuchunguze sababu mbili za kufanya hivyo. Kwanza, sala ni ibada, na Biblia inasema kwamba ni Yehova pekee anayepaswa kuabudiwa. (Kutoka 20:5) Pili, Biblia inafunua kwamba Yehova pekee ndiye mwenye jina la cheo “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Hata ingawa Yehova amewapa wengine majukumu mengi, hajampa mtu yeyote jukumu la kusikiliza sala. Ameahidi kusikiliza sala zetu yeye mwenyewe.

      Hivyo, ikiwa unataka Mungu asikilize sala zako, kumbuka himizo hili linalopatikana katika Maandiko: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Matendo 2:21) Hata hivyo, je, Yehova anasikiliza sala zote bila masharti yoyote? Au kuna jambo lingine tunalohitaji kujua ikiwa tunataka Yehova asikilize sala zetu?

      [Maelezo ya Chini]

      a Mapokeo fulani ya kidini yanasema kwamba ni kosa kutaja jina la kibinafsi la Mungu, hata katika sala. Hata hivyo, jina hilo linapatikana karibu mara 7,000 katika lugha za awali za Biblia, hasa katika sala na zaburi za watumishi waaminifu wa Yehova.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Jambo ambalo Eliya aliwaambia manabii wa Baali wafanye linathibitisha kwamba sala zote hazielekezwi kwa Mungu wa kweli

  • 3 Tusali Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      3 Tusali Jinsi Gani?

      KUHUSIANA na sala, mapokeo mengi ya kidini yanakazia mambo kama vile jinsi ya kukaa unaposali, maneno yanayotumiwa, na taratibu fulani za kidini. Hata hivyo, Biblia inatusaidia kutokazia fikira mambo hayo na badala yake kufikiria kwa uzito swali hili, “Tunapaswa kusali jinsi gani?”

      Biblia inasema kwamba watumishi waaminifu wa Mungu walisali wakiwa mahali tofauti-tofauti na katika mkao tofauti. Walisali kimyakimya au kwa sauti ikitegemea hali. Walisali wakiangalia juu mbinguni au wakiwa wamesujudu. Badala ya kutumia sanamu, rozari, au vitabu vya sala, walisali kutoka moyoni kwa maneno yao wenyewe. Ni nini kilichofanya sala zao zisikilizwe na Mungu?

      Kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, walielekeza sala zao kwa Mungu mmoja tu, Yehova. Kuna jambo lingine muhimu. Tunasoma hivi katika 1 Yohana 5:14: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” Sala zetu zinapaswa kupatana na mapenzi ya Mungu. Hilo linamaanisha nini?

      Ili kusali kulingana na mapenzi ya Mungu, tunahitaji kujua mapenzi yake ni nini. Kwa hiyo, kujifunza Biblia ni muhimu ili kuboresha sala zetu. Je, hilo linamaanisha kwamba ili Mungu asikilize sala zetu ni lazima tuwe wasomi wa Biblia? Hapana. Lakini Mungu anatazamia tujifunze mapenzi yake na tujitahidi kuyaelewa, na kuishi kupatana na yale tunayojifunza. (Mathayo 7:21-23) Tunahitaji kusali kulingana na yale tunayojifunza.

      Kadiri tunavyojifunza kumhusu Yehova na mapenzi yake, ndivyo imani yetu inavyozidi kukomaa. Hilo ni jambo lingine muhimu linaloweza kutusaidia kuboresha sala zetu. Yesu alisema: “Mambo yote mnayoomba katika sala, mkiwa na imani, mtapokea.” (Mathayo 21:22) Kuwa na imani hakumaanishi kuamini lolote bila kufikiri. Badala yake, kunamaanisha kuamini jambo fulani ambalo hata ingawa halionekani, kuna uthibitisho ulio wazi unaounga mkono jambo hilo. (Waebrania 11:1) Biblia ina uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Yehova ambaye hatuwezi kumwona ni halisi, anategemeka, na yuko tayari kujibu sala za wale wanaomwamini. Zaidi ya hayo, nyakati zote tunaweza kuomba tuongezewe imani, na Yehova anapenda kutupa kile tunachohitaji.—Luka 17:5; Yakobo 1:17.

      Ona pendekezo lingine muhimu kuhusu jinsi ya kusali. Yesu alisema: “Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Kwa hiyo, Yesu ndiye njia ambayo tunaweza kuitumia kumfikia Baba, Yehova. Hivyo, Yesu aliwaambia wafuasi wake wasali katika jina lake. (Yohana 14:13; 15:16) Hilo halimaanishi kuwa tunapaswa kusali kwa Yesu. Badala yake, tunasali katika jina la Yesu, tukikumbuka kwamba tunaweza tu kumfikia Baba yetu mkamilifu na mtakatifu kwa sababu ya Yesu.

      Wafuasi wa karibu wa Yesu walimsihi hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Bila shaka, kama ambavyo tumeona, hawakuwa wakiomba wafundishwe mambo ya msingi tu. Badala yake walitaka kujua mengi—kwa maneno mengine walikuwa wakiuliza, ‘Tunapaswa kusali kuhusu nini?’

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Sala ambazo Mungu anasikiliza ni zile zinazopatana na mapenzi yake, zinazotolewa kwa imani, na katika jina la Yesu

  • 4 Tusali Kuhusu Nini?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      4 Tusali Kuhusu Nini?

      IMETAJWA kuwa sala inayorudiwa-rudiwa sana kati ya sala zote za Wakristo. Iwe hilo ni kweli au si kweli, sala ya kielelezo ya Yesu, ambayo nyakati nyingine inaitwa Sala ya Bwana au ya Baba Yetu, ndiyo sala ambayo wengi hawaielewi. Watu wengi huirudia-rudia kila siku. Lakini Yesu hakukusudia sala hiyo itumiwe kwa njia hiyo. Kwa nini tunasema hivyo?

      Muda mfupi tu kabla ya kufundisha sala hiyo, Yesu alisema: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.” (Mathayo 6:7) Je, Yesu alikuwa akipinga maneno yake mwenyewe kwa kufundisha sala ambayo ingekaririwa na kurudiwa-rudiwa? Bila shaka, hapana! Badala yake, Yesu alikuwa akitufundisha mambo tunayopaswa kutaja na kuyatanguliza tunaposali. Acheni tuchunguze kwa makini yale aliyosema katika sala hiyo iliyoandikwa katika Mathayo 6:9-13.

      “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”

      Hivyo, Yesu alikuwa akiwakumbusha wafuasi wake kuwa sala zote zinapaswa kuelekezwa kwa Baba yake, Yehova. Lakini unajua ni kwa nini jina la Mungu ni la maana sana na kwa nini linapaswa kutakaswa, au kufanywa takatifu?

      Tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu, mambo mengi ya uwongo yamesemwa kuhusu jina takatifu la Mungu. Adui ya Mungu, Shetani, alimwita Yehova Mtawala mwongo na mwenye ubinafsi ambaye hana haki ya kuutawala uumbaji Wake. (Mwanzo 3:1-6) Wengi wameunga mkono madai ya Shetani, wakifundisha kwamba Mungu hana upendo na hana huruma. Pia wanakana kwamba kuna Muumba. Wengine wamelishambulia jina la Mungu, Yehova, kwa kuliondoa katika tafsiri fulani za Biblia na kuwakataza watu wasilitumie.

      Biblia inaonyesha kwamba Mungu atarekebisha ukosefu huo wote wa haki. (Ezekieli 39:7) Kwa kufanya hivyo, atatimiza mahitaji yako yote na kutatua matatizo yako. Atafanya hivyo jinsi gani? Maneno yanayofuata katika sala ya Yesu yanatoa jibu.

      “Ufalme wako na uje.”

      Leo, viongozi wa kidini wamechanganyikiwa sana kuhusiana na Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, kama wasikilizaji wa Yesu walivyojua, manabii wa Mungu walikuwa wametabiri tangu zamani kwamba Masihi, Mkombozi aliyechaguliwa na Mungu, angetawala katika Ufalme ambao ungeubadili ulimwengu. (Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44) Ufalme huo utatakasa jina la Mungu kwa kufunua uwongo wa Shetani na kisha kumwondoa Shetani na kazi zake zote. Utaondoa vita, magonjwa, njaa, na hata kifo. (Zaburi 46:9; 72:12-16; Isaya 25:8; 33:24) Unaposali Ufalme wa Mungu uje, unasali kwamba ahadi hizo zote zitimie.

      “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”

      Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba mapenzi ya Mungu yatatimizwa hapa duniani kama yanavyotimizwa mbinguni, makao ya Mungu. Imethibitika kwamba mapenzi ya Mungu hayawezi kuzuiwa yasitimizwe mbinguni; huko, Mwana wa Mungu alipigana vita na Shetani na malaika zake, na kuwatupa hapa duniani. (Ufunuo 12:9-12) Ombi hili la tatu, kama tu yale maombi mawili ya kwanza katika sala ya kielelezo, linatusaidia kukazia uangalifu wetu jambo lililo muhimu hata zaidi, yaani, mapenzi ya Mungu, bali si mapenzi yetu. Ni kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu tu ndiko kunakoweza kuwaletea viumbe wake wote mambo mema. Hivyo, hata mwanadamu mkamilifu Yesu alimwambia Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.

      “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.”

      Pia, Yesu alionyesha kwamba tunaweza kusali kuhusu mahitaji yetu. Hakuna ubaya wowote kusali kwa Mungu kuhusu mahitaji yetu ya kila siku. Kwa kweli, kufanya hivyo kunatukumbusha kwamba Yehova ndiye “huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Biblia inafunua kwamba yeye ni mzazi mwenye upendo ambaye hufurahia kuwapa watoto wake kile wanachohitaji. Hata hivyo, kama mzazi mwenye upendo, Mungu hawezi kuwapa watu wake vitu ambavyo havitawaletea faida yoyote.

      “Utusamehe madeni yetu.”

      Je, kweli kuna deni lolote ambalo Mungu anakudai? Je, kweli unahitaji akusamehe deni hilo? Watu wengi leo hawaelewi dhambi ni nini wala hawaelewi uzito wake. Lakini Biblia inafundisha kwamba dhambi ndiyo chanzo cha matatizo yetu, kwa sababu ndiyo inayosababisha kifo cha wanadamu. Kwa kuwa tumezaliwa katika dhambi, mara kwa mara sote tunatenda dhambi, na tunategemea msamaha wa Mungu ili tuweze kuishi milele wakati ujao. (Waroma 3:23; 5:12; 6:23) Inatuliza kujua maneno haya ya Biblia: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.

      “Utukomboe kutokana na yule mwovu.”

      Je, unajua ni kwa nini unahitaji sana ulinzi wa Mungu? Wengi hawataki kuamini kwamba Shetani, “yule mwovu,” yupo. Lakini Yesu alifundisha kwamba Shetani ni kiumbe halisi, hata akamwita “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 16:11) Shetani ameupotosha ulimwengu huu anaoutawala, na anatamani sana kukupotosha ili usiweze kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Baba yako, Yehova. (1 Petro 5:8) Hata hivyo, Yehova ana nguvu zaidi kuliko Shetani na anafurahia kuwalinda wale wanaompenda.

      Bila shaka, mambo ambayo tumezungumzia katika sala ya kielelezo ya Yesu, hayatii ndani kila jambo linalopaswa kutajwa katika sala. Kumbuka andiko la 1 Yohana 5:14 linatuambia hivi kumhusu Mungu: “Hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” Hivyo, usifikiri kwamba mahangaiko yako ni madogo sana hivi kwamba hupaswi kumweleza Mungu katika sala.—1 Petro 5:7.

      Hata hivyo, namna gani kuhusu mahali na wakati wa kusali? Je, ni muhimu kufikiria mambo hayo?

  • 5 Tusali Wakati Gani na Mahali Gani?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      5 Tusali Wakati Gani na Mahali Gani?

      BILA shaka, umeona kwamba dini nyingi kubwa zinakazia kuwa na majengo ya sala yenye madoido na zinapanga wakati hususa wa kusali. Je, Biblia inasema ni lazima tuwe na mahali hususa na wakati hususa wa kusali?

      Biblia inaonyesha kwamba kuna nyakati zinazofaa za kusali. Kwa mfano, kabla ya kula na wafuasi wake, Yesu alitoa sala ya kumshukuru Mungu. (Luka 22:17) Na wanafunzi wake walipokutana ili kuabudu, walisali pamoja. Hivyo, waliendeleza desturi iliyokuwa ikifuatwa tangu zamani katika masinagogi ya Wayahudi na katika hekalu huko Yerusalemu. Mungu alikusudia hekalu liwe “nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote.”—Marko 11:17.

      Watumishi wa Mungu wanapokusanyika na kusali pamoja, maombi yao yanaweza kuwa na matokeo mazuri. Mungu hufurahi ikiwa wanakusanyika wakiwa na nia moja na sala inayotolewa kwa ajili yao inapatana na kanuni za Maandiko. Sala hiyo hata inaweza kumchochea Mungu afanye jambo ambalo huenda hangefanya. (Waebrania 13:18, 19) Mashahidi wa Yehova husali kwa ukawaida katika mikutano yao. Unakaribishwa kwa uchangamfu uende kwenye Jumba la Ufalme ambalo liko karibu nawe ili usikie sala hizo.

      Hata hivyo, Biblia haisemi ni lazima tuwe na mahali hususa na wakati hususa wa kusali. Katika Biblia, tunasoma kuhusu watumishi wa Mungu waliosali wakati na mahali tofauti-tofauti. Yesu alisema: “Unaposali, ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.”—Mathayo 6:6.

      Bila shaka, huo ni mwaliko wenye kupendeza, sivyo? Unaweza kusali kwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote wakati wowote, hata ukiwa faraghani, na kuwa na hakika kwamba atakusikiliza. Si ajabu kwamba mara nyingi Yesu alihitaji kuwa peke yake ili asali! Wakati fulani alisali kwa Mungu usiku kucha, bila shaka, akitafuta mwongozo wa kufanya uamuzi fulani mzito.—Luka 6:12, 13.

      Wanaume na wanawake wengine katika Biblia walisali walipotaka kufanya maamuzi mazito au walipopatwa na hali fulani ngumu. Nyakati fulani walisali kwa sauti na nyakati nyingine wakasali kimyakimya; walisali walipokuwa katika kikundi na hata walipokuwa peke yao. Jambo muhimu ni kwamba walisali. Hata Mungu huwaambia watumishi wake hivi: “Salini bila kuacha.” (1 Wathesalonike 5:17) Yuko tayari kuwasikiliza bila kuchoka wale wanaofanya mapenzi yake. Je, huo si mwaliko wenye upendo?

      Bila shaka, katika ulimwengu huu wenye shaka, wengi wanataka kujua ikiwa sala inaweza kuwasaidia. Huenda ukauliza, ‘Je, kweli sala inaweza kunisaidia?’

      [Blabu katika ukurasa wa 9]

      Tunaweza kusali wakati wowote, mahali popote

  • 6 Je, Inaweza Kutusaidia?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      6 Je, Inaweza Kutusaidia?

      JE, SALA inaweza kutusaidia? Jibu ni ndiyo, kwa kuwa Biblia inaonyesha kwamba sala za watumishi waaminifu wa Mungu zinawanufaisha. (Luka 22:40; Yakobo 5:13) Kwa kweli, sala inaweza kutusaidia sana kiroho, kihisia, au hata kimwili. Jinsi gani?

      Tuseme kwamba mtoto wako amepokea zawadi. Je, ungemfundisha kwamba inatosha tu kuhisi shukrani moyoni? Au ungemfundisha kusema asante? Tunapoeleza hisia zetu muhimu, tunafanya ziwe wazi na hata ziwe na uzito zaidi. Je, inaweza kuwa hivyo tunapozungumza na Mungu? Bila shaka! Fikiria mifano fulani.

      Sala za shukrani. Tunapomshukuru Baba yetu kwa mambo mazuri anayotufanyia, tunaonyesha kwamba tunathamini baraka hizo. Kwa hiyo, tunaweza kujihisi wenye shukrani zaidi, wenye furaha zaidi, na wenye mtazamo mzuri hata zaidi.—Wafilipi 4:6.

      Mfano: Yesu alimshukuru Baba yake kwa jinsi alivyosikiliza na kujibu sala zake.—Yohana 11:41.

      Sala za kuomba msamaha. Tunapomwomba Mungu msamaha tunafanya dhamiri yetu iwe yenye nguvu, toba yetu iwe ya kutoka moyoni, na tunaelewa zaidi uzito wa dhambi. Pia, tunapata kitulizo kutokana na hali yenye kulemea ya kujisikia kuwa wenye hatia.

      Mfano: Daudi alisali ili kuonyesha toba na huzuni yake.—Zaburi 51.

      Sala za kuomba mwongozo na hekima. Tunapomwomba Yehova atuongoze au atupe hekima ili tufanye maamuzi yanayofaa, jambo hilo linaweza kutusaidia kuwa wanyenyekevu. Pia, linaweza kutukumbusha kwamba tumepungukiwa na vilevile kutusaidia kuimarisha imani kwa Baba yetu wa mbinguni.—Methali 3:5, 6.

      Mfano: Kwa unyenyekevu Sulemani aliomba mwongozo na hekima ili aweze kutawala Israeli.—1 Wafalme 3:5-12.

      Sala wakati wa taabu. Tunapomweleza Yehova yaliyo moyoni mwetu wakati ambapo tumevurugika kihisia, mioyo yetu inaburudika na tunajifunza kumtegemea badala ya kujitegemea wenyewe.—Zaburi 62:8.

      Mfano: Mfalme Asa alisali alipokabili adui hatari.—2 Mambo ya Nyakati 14:11.

      Sala za kuwatakia hali njema wenye uhitaji. Sala kama hizo hutuwezesha kushinda ubinafsi na kuwa wenye rehema na huruma.

      Mfano: Yesu alisali kwa ajili ya wafuasi wake.—Yohana 17:9-17.

      Sala za sifa. Tunapomtukuza Yehova kwa ajili ya kazi na sifa zake za ajabu, heshima na uthamini wetu kwake unaongezeka. Sala kama hizo zinaweza kutusaidia kumkaribia Mungu ambaye pia ni Baba yetu.

      Mfano: Daudi alimsifu Mungu kwa uchangamfu kwa sababu ya kazi zake za uumbaji.—Zaburi 8.

      Baraka nyingine inayohusianishwa na sala ni “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Wafilipi 4:7) Si rahisi kupata utulivu katika ulimwengu huu wenye msukosuko. Lakini kuwa na utulivu kunatusaidia kuwa na afya nzuri. (Methali 14:30) Hata hivyo, je, utulivu huo unatokana tu na jitihada zetu wenyewe? Au kuna jambo lingine muhimu linalohusika?

      [Blabu katika ukurasa wa 10]

      Sala ina manufaa mengi—kimwili, kihisia, na hata kiroho

  • 7 Je, Mungu Atasikiliza na Kujibu Sala Zetu?
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Oktoba 1
    • Sala

      7 Je, Mungu Atasikiliza na Kujibu Sala Zetu?

      SWALI hilo linafanya watu wasisimuke na kuwa na hamu ya kupata jibu. Biblia inaonyesha kwamba Yehova husikiliza sala leo. Iwe atasikiliza sala za mtu au hatazisikiliza, hilo hasa litategemea mtu mwenyewe.

      Yesu aliwalaumu viongozi wa kidini wa nyakati zake ambao walisali kwa unafiki, wakihangaikia tu kuonekana kuwa waadilifu. Alisema kuwa watu hao wangepata “thawabu yao kwa ukamili,” akimaanisha kwamba wangepata tu kile walichotaka sana, yaani, kuonekana na watu, bali si kile walichohitaji, yaani, kusikilizwa na Mungu. (Mathayo 6:5) Vivyo hivyo leo, wengi husali kulingana na mapenzi yao bali si ya Mungu. Kwa kuwa wanapuuza kanuni za Biblia ambazo tumezungumzia, Mungu hasikilizi sala zao.

      Namna gani wewe? Je, Mungu atasikiliza na kujibu sala zako? Jibu halitegemei wewe ni wa jamii, taifa, au cheo gani katika jamii. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Je, wewe unafanya hivyo? Ikiwa unamwogopa Mungu, inamaanisha kwamba unamheshimu sana, na hutaki kumchukiza. Unapotenda uadilifu, unajitahidi kufanya yale ambayo Mungu anasema ni sawa badala ya kufanya mapenzi yako au ya wanadamu wenzako. Je, kweli unataka Mungu asikilize sala zako? Biblia inaonyesha jinsi unavyoweza kusali ili Mungu asikilize sala zako.a

      Bila shaka, wengi wanataka Mungu ajibu sala zao kwa kufanya muujiza. Lakini hata katika nyakati za Biblia, si mara nyingi Mungu alijibu sala kwa kufanya miujiza. Baada ya muujiza mmoja kufanywa, miaka mingi ilipita kabla ya mwingine kufanywa. Zaidi ya hilo, Biblia inaonyesha kwamba kipindi cha kufanya miujiza kiliisha baada ya siku za mitume. (1 Wakorintho 13:8-10) Je, hilo linamaanisha kwamba leo Mungu hajibu sala? Hapana! Ona baadhi ya sala ambazo anajibu.

      Mungu anatupa hekima. Yehova ndiye Chanzo pekee cha hekima yote ya kweli. Yeye huitoa kwa ukarimu, akiwapa wale wanaotaka mwongozo wake na wanaojitahidi kuishi kulingana na mwongozo huo.—Yakobo 1:5.

      Mungu hutupa roho yake takatifu na faida zote zinazotokana nayo. Roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu. Hakuna nguvu inayozidi hiyo. Inaweza kutusaidia kuvumilia majaribu. Inaweza kutupa amani tunapokabili hali ngumu. Inaweza kutusaidia kusitawisha sifa nyingine nzuri na zinazopendeza. (Wagalatia 5:22, 23) Yesu aliwahakikishia wafuasi wake kwamba Mungu hutoa zawadi hiyo kwa ukarimu.—Luka 11:13.

      Mungu huwapa ujuzi wale wanaomtafuta kwa bidii. (Matendo 17:26, 27) Ulimwenguni pote, kuna watu ambao wanatafuta kweli kwa unyofu. Wanataka kujua kumhusu Mungu—jina lake ni nani, kusudi lake la kuumba dunia na wanadamu, na jinsi wanavyoweza kumkaribia. (Yakobo 4:8) Mara nyingi, Mashahidi wa Yehova wanakutana na watu kama hao, nao hufurahi kujibu maswali hayo kwa kutumia Biblia.

      Je, hiyo ndiyo sababu ulichukua gazeti hili? Je, unamtafuta Mungu? Labda hii ndiyo njia anayotumia kujibu sala yako.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kusali na kusikilizwa na Mungu, ona sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki