-
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”
“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.”—MATHAYO 28:18, 19.
1, 2. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo gani? (b) Ni maswali gani kuhusu amri za Yesu tutakayozungumzia?
ILIKUWA siku ya masika huko Israeli mwaka wa 33 W.K., nao wanafunzi wa Yesu walikuwa wamekusanyika kwenye mlima fulani huko Galilaya. Bwana wao aliyefufuliwa alikuwa karibu kupanda mbinguni, lakini kwanza alihitaji kuwaambia jambo fulani muhimu. Yesu alitaka kuwapa mgawo fulani. Mgawo gani huo? Wanafunzi wake waliitikiaje? Na mgawo huo unatuhusuje leo?
2 Yale ambayo Yesu alisema yameandikwa kwenye Mathayo 28:18-20: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Yesu alitaja “mamlaka yote,” “mataifa yote,” “mambo yote,” na “siku zote.” Amri zake kuhusu taarifa hizo nne hutokeza maswali manne mafupi ambayo ni muhimu. Maswali hayo ni, kwa nini? wapi? nini? na lini? Na tuzungumzie maswali hayo moja baada ya lingine.a
“Nimepewa Mamlaka Yote”
3. Kwa nini tunapaswa kutii amri ya kufanya wanafunzi?
3 Kwanza, kwa nini tunapaswa kutii amri ya kufanya wanafunzi? Yesu alisema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Maneno “kwa hiyo” huonyesha sababu kuu kwa nini tunapaswa kutii amri hiyo. Hiyo ni kwa sababu Yesu, aliyetoa amri hiyo, ana “mamlaka yote.” Mamlaka yake ni kuu kadiri gani?
4. (a) Yesu ana mamlaka kuu kadiri gani? (b) Kufahamu mamlaka ya Yesu kunapaswa kuathirije maoni yetu kuhusu amri ya kufanya wanafunzi?
4 Yesu ana mamlaka juu ya kutaniko lake, na tangu mwaka wa 1914 amekuwa na mamlaka juu ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa hivi karibuni. (Wakolosai 1:13; Ufunuo 11:15) Yeye ni malaika mkuu na hivyo ana mamlaka juu ya jeshi la mbinguni la mamia ya mamilioni ya malaika. (1 Wathesalonike 4:16; 1 Petro 3:22; Ufunuo 19:14-16) Amepewa mamlaka na Babake ili kuangamiza ‘serikali zote na mamlaka yote na nguvu zote’ zinazopinga kanuni za uadilifu. (1 Wakorintho 15:24-26; Waefeso 1:20-23) Mamlaka ya Yesu si juu ya wale walio hai tu. Yeye pia ni “mwamuzi wa walio hai na wafu,” naye ana nguvu alizopewa na Mungu za kuwafufua wale waliolala katika kifo. (Matendo 10:42; Yohana 5:26-28) Bila shaka, amri inayotolewa na Mtu aliyepewa mamlaka kuu kama hiyo inapaswa kuonwa kuwa muhimu sana. Kwa hiyo, sisi hutii kwa heshima na kwa hiari amri ya Kristo ya ‘kwenda na kufanya wanafunzi.’
5. (a) Petro alitiije maneno ya Yesu? (b) Petro alibarikiwaje kwa kutii maagizo ya Yesu?
5 Mapema katika huduma yake duniani, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwa njia yenye kutokeza kwamba kutambua mamlaka yake na kutii amri zake kungewaletea baraka. Pindi moja alimwambia hivi Petro ambaye alikuwa mvuvi: “Vuta mpaka mahali penye kilindi, nanyi mshushe nyavu zenu, mvue.” Petro alikuwa na hakika kwamba hakukuwa na samaki, hivyo akamwambia Yesu: “Mwalimu, tulitaabika usiku wote na hatukupata chochote.” Hata hivyo, Petro aliongeza kusema hivi kwa unyenyekevu: “Lakini nitazishusha nyavu kwa amri yako.” Baada ya kutii amri ya Kristo, Petro alivua “samaki wengi sana.” Akiwa amelemewa na hisia, Petro ‘alianguka magotini pa Yesu, akisema: “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana.”’ Lakini Yesu akamjibu: “Acha kuogopa. Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:1-10; Mathayo 4:18) Tunajifunza nini kutokana na masimulizi hayo?
6. (a) Masimulizi kuhusu samaki waliovuliwa kimuujiza yanaonyesha nini kuhusiana na utii ambao Yesu hutaka? (b) Tunaweza kumwigaje Yesu?
6 Yesu aliwapa Petro, Andrea, na mitume wengine mgawo wa “kuwa wavuvi wa watu,” si kabla, bali baada ya kuvua samaki wengi sana isivyo kawaida. (Marko 1:16, 17) Ni wazi kwamba Yesu hakutaka wamtii bila kufikiri. Aliwapa sababu yenye kusadikisha ya kumtii. Kama vile kutii amri ya Yesu ya kutupa nyavu kulivyowawezesha kuvua samaki wengi isivyo kawaida, ndivyo kutii amri ya Yesu ya ‘kuvua watu’ kungetokeza baraka nyingi. Mitume walitii wakiwa na imani kamili. Masimulizi hayo yanamalizia: “Wakazirudisha mashua kwenye nchi kavu, wakaacha kila kitu, wakamfuata.” (Luka 5:11) Leo, tunapowatia wengine moyo washiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, tunamwiga Yesu. Hatutaki tu watu wafanye yale tunayowaambia, bali sisi huwapa sababu zenye kusadikisha za kutii amri ya Kristo.
Sababu Zenye Kusadikisha na Nia Ifaayo
7, 8. (a) Tuna sababu gani za Kimaandiko za kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi? (b) Ni andiko gani ambalo hasa hukuchochea kuendelea na kazi ya kuhubiri? (Ona pia maelezo ya chini.)
7 Kwa kuwa tunakubali mamlaka ya Kristo, tunashiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Tuna sababu gani nyingine za Kimaandiko za kufanya kazi hiyo ambazo tunaweza kuwaeleza wale tunaotaka kuwachochea watende mema? Fikiria mambo yafuatayo yaliyosemwa na Mashahidi kadhaa waaminifu kutoka nchi mbalimbali, kisha ona jinsi maandiko yaliyotajwa yanavyounga mkono maelezo yao.
8 Roy, aliyebatizwa mwaka wa 1951: “Nilipojiweka wakfu kwa Yehova, niliahidi kumtumikia sikuzote. Ninataka kutimiza ahadi yangu.” (Zaburi 50:14; Mathayo 5:37) Heather, aliyebatizwa mwaka wa 1962: “Ninapofikiria yote ambayo Yehova amenifanyia, nataka kumshukuru kwa kumtumikia kwa uaminifu.” (Zaburi 9:1, 9-11; Wakolosai 3:15) Hannelore, aliyebatizwa mwaka wa 1954: “Kila mara tunapokuwa katika huduma tunasaidiwa na malaika, hilo ni pendeleo lililoje!” (Matendo 10:30-33; Ufunuo 14:6, 7) Honor, aliyebatizwa mwaka wa 1969: “Wakati wa hukumu ya Yehova ufikapo, singependa yeyote katika ujirani wangu amlaumu Yehova na Mashahidi wake kwamba hawakujali na kusema, ‘Sikuonywa!’” (Ezekieli 2:5; 3:17-19; Waroma 10:16, 18) Claudio, aliyebatizwa mwaka wa 1974: “Tunapohubiri, tunakuwa ‘machoni pa Mungu’ na ‘kushirikiana na Kristo.’ Ebu wazia, tunapokuwa katika huduma, tunashirikiana na Marafiki wetu walio bora zaidi!”—2 Wakorintho 2:17.b
9. (a) Masimulizi kuhusu jinsi Petro na mitume wengine walivyovua samaki huonyesha nini kuhusu nia inayofaa ya kumtii Kristo? (b) Ni nini iliyo nia inayofaa ya kumtii Mungu na Kristo leo, na kwa nini?
9 Masimulizi kuhusu kuvuliwa kwa samaki wengi isivyo kawaida yanaonyesha pia umuhimu wa kuwa na nia inayofaa ya kumtii Kristo, yaani, upendo. Petro aliposema, “Ondoka kwangu, kwa sababu mimi ni mtu mwenye dhambi,” Yesu hakuondoka, wala hakumshutumu Petro kwa dhambi yoyote. (Luka 5:8) Yesu hata hakumkemea Petro kwa kumwomba aondoke, bali alimjibu hivi kwa fadhili: “Acha kuogopa.” Ingekuwa nia mbaya kumtii Kristo kwa sababu ya woga usiofaa. Badala yake, Yesu alimwambia Petro kwamba yeye na wenzake wangetumiwa kuwa wavuvi wa watu. Vivyo hivyo, leo hatuogopeshi watu au kuwafanya waone aibu au wahisi wana hatia, ili kuwalazimisha wamtii Kristo. Utii wa nafsi yote unaotegemea upendo kwa Mungu na Kristo ndio tu hufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Mathayo 22:37.
‘Fanyeni Wanafunzi Kutoka kwa Watu wa Mataifa Yote’
10. (a) Ni jambo gani kuhusu amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi lililotokeza tatizo gumu kwa wanafunzi wake? (b) Wanafunzi waliitikiaje amri ya Yesu?
10 Swali la pili tunaloweza kuuliza kuhusiana na amri ya Kristo ni, kazi hiyo ya kufanya wanafunzi inapaswa kufanywa Wapi? Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ Kabla Yesu hajaanza huduma yake, watu wa mataifa walikaribishwa ikiwa walikuja Israeli kumtumikia Yehova. (1 Wafalme 8:41-43) Yesu aliwahubiria hasa Wayahudi wa asili, lakini sasa aliwaambia wafuasi wake waende kwa watu wa mataifa yote. Kwa kweli, eneo la uvuvi, au eneo la kuhubiri, la wanafunzi wake lilikuwa kama “kidimbwi” kidogo, yaani, walivua katika eneo la Wayahudi wa asili, lakini baada ya muda mfupi wangevua katika “bahari” nzima ya wanadamu. Ingawa badiliko hilo lilitokeza tatizo gumu kwa wanafunzi, walitii kwa utayari maagizo ya Yesu. Miaka inayopungua 30 baada ya Yesu kufa, mtume Paulo aliweza kuandika kwamba habari njema zilikuwa zimehubiriwa si kwa Wayahudi tu bali kwa “uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.
11. Kumekuwa na mpanuko gani wa ‘maeneo ya uvuvi’ tangu mapema karne ya 20?
11 Vivyo hivyo, hivi karibuni eneo la kuhubiri limepanuka. Mwanzoni mwa karne ya 20, ‘maeneo ya uvuvi’ yalikuwa tu katika nchi chache. Hata hivyo, wafuasi wa Kristo wakati huo waliiga kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza, nao walipanua kwa bidii eneo walilohubiri. (Waroma 15:20) Mapema miaka ya 1930, walikuwa wakifanya wanafunzi katika nchi mia moja hivi. Leo ‘maeneo yetu ya uvuvi’ yanapatikana katika nchi 235.—Marko 13:10.
“Kutoka Katika Lugha Zote”
12. Unabii kwenye Zekaria 8:23 unakazia jambo gani gumu?
12 Kufanya wanafunzi katika mataifa yote ni jambo gumu si kwa sababu tu ya ukubwa wa eneo bali pia kwa sababu ya lugha nyingi zinazotumiwa. Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Zekaria: “Na itakuwa katika siku hizo kwamba watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: ‘Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zekaria 8:23) Katika utimizo mkubwa zaidi wa unabii huo, “mtu aliye Myahudi” huwakilisha mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta, nao “watu kumi” huwakilisha “umati mkubwa.”c (Ufunuo 7:9, 10; Wagalatia 6:16) Umati huo mkubwa wa wanafunzi wa Kristo ungepatikana katika mataifa mengi, na kama vile Zekaria alivyosema, wangezungumza lugha mbalimbali. Je, leo watu wa Mungu wanatoka katika mataifa mengi, nao huzungumza lugha mbalimbali? Ndiyo.
13. (a) Kumekuwa na badiliko gani kuhusu lugha kati ya watu wa Mungu leo? (b) Jamii ya mtumwa mwaminifu imefanya nini kuhusu uhitaji unaoongezeka wa chakula cha kiroho katika lugha mbalimbali? (Tia ndani sanduku “Vichapo kwa Ajili ya Wasioweza Kuona.”)
13 Katika mwaka wa 1950 lugha ya asili ya Mashahidi wa Yehova 3 kati ya 5 ulimwenguni ilikuwa Kiingereza. Kufikia mwaka wa 1980 uwiano huo ulibadilika ukawa Mashahidi 2 kati ya 5, na leo ni Shahidi 1 tu kati ya 5 ambaye lugha yake ya asili ni Kiingereza. Jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara imefanya nini kuhusiana na badiliko hilo? Jamii hiyo imeandaa chakula cha kiroho katika lugha nyingi zaidi. (Mathayo 24:45) Kwa mfano, mwaka wa 1950 vichapo vyetu vilichapishwa katika lugha 90, lakini leo vichapo vyetu vinachapishwa katika lugha 400 hivi. Je, hatua hiyo ya kuwafikiria watu wanaozungumza lugha mbalimbali imekuwa na matokeo? Ndiyo! Wastani wa watu 5,000 hivi ‘kutoka lugha zote’ huwa wanafunzi wa Kristo kila juma! (Ufunuo 7:9) Na ongezeko hilo linaendelea. Katika nchi fulani “nyavu” zinanasa samaki wengi sana!—Luka 5:6; Yohana 21:6.
Je, Unaweza Kushiriki Katika Huduma Yenye Kuthawabisha?
14. Tunawezaje kuwasaidia watu katika eneo letu wanaozungumza lugha tofauti na yetu? (Tia ndani sanduku “Lugha ya Ishara na Kufanya Wanafunzi.”)
14 Kwa sababu ya kuwepo kwa wahamiaji katika nchi nyingi za Magharibi, imewabidi Mashahidi wafanye wanafunzi kutoka ‘kila lugha’ katika nchi zao. (Ufunuo 14:6) Tunawezaje kuwasaidia wale walio katika eneo letu ambao wanazungumza lugha tofauti na yetu? (1 Timotheo 2:4) Tunaweza kutumia vifaa vifaavyo katika uvuaji wa mfano. Wape watu hao vichapo katika lugha yao. Ikiwezekana, panga Shahidi anayezungumza lugha yao awatembelee. (Matendo 22:2) Sasa ni rahisi zaidi kufanya mipango hiyo, kwa kuwa Mashahidi wengi wamejifunza kuzungumza lugha nyingine mbali na lugha yao ya asili ili kuwasaidia wageni wawe wanafunzi wa Kristo. Ripoti zinaonyesha kwamba inathawabisha kusaidia kwa njia hiyo.
15, 16. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba inathawabisha kuwasaidia wale wanaozungumza lugha ya kigeni? (b) Huenda tukafikiria maswali gani kuhusu utumishi katika eneo la lugha ya kigeni?
15 Fikiria mifano miwili kutoka Uholanzi ambako kazi iliyopangwa ya kuhubiri Ufalme inafanywa katika lugha 34. Mashahidi wawili ambao ni mume na mke walijitolea kwenda kufanya wanafunzi kati ya wahamiaji wanaozungumza Kipolandi. Jitihada zao zilikuwa na matokeo makubwa sana hivi kwamba ilimbidi mume kupunguza wakati anaotumia kazini ili awe na siku moja zaidi kila juma ya kujifunza Biblia pamoja na wale wanaopendezwa. Muda si muda, wenzi hao walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 20 kila juma. Walisema: “Huduma yetu hutufurahisha sana.” Wale wanaofanya wanafunzi hufurahi hasa wakati wale wanaosikia kweli za Biblia katika lugha yao wanapotoa shukrani. Kwa mfano, wakati mkutano fulani ulifanywa katika lugha ya Vietnam, mtu mmoja mzee alisimama na kuomba aruhusiwe kuzungumza. Huku akilengwa-lengwa na machozi, aliwaambia Mashahidi hivi: “Asanteni kwa jitihada zenu za kujifunza lugha yangu ngumu. Ninashukuru sana kujifunza mambo mengi mazuri kutoka katika Biblia nikiwa mzee.”
16 Kwa hiyo, haishangazi kwamba wale wanaotumika katika makutaniko yanayozungumza lugha za kigeni wanathawabishwa sana. Mume na mke kutoka Uingereza walisema: “Tumefurahia zaidi huduma katika maeneo ya lugha za kigeni katika miaka 40 ambayo tumekuwa tukihubiri juu ya Ufalme.” Je, unaweza kurekebisha hali zako ili ushiriki katika huduma hiyo yenye kufurahisha? Ikiwa bado uko shule, je, unaweza kujifunza lugha ya kigeni ili kujitayarisha kwa ajili ya huduma hiyo? Huenda kwa kufanya hivyo ukawa na maisha yenye kuridhisha, yaliyojaa baraka. (Methali 10:22) Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazazi wako?
Kubadili Njia Zetu za Kuhubiri
17. Tunawezaje kuwafikia watu wengi zaidi katika eneo letu la kutaniko?
17 Inaeleweka kwamba hali haziruhusu wengi wetu kutupa “nyavu” katika maeneo ya lugha za kigeni. Hata hivyo, tunaweza kuwafikia watu wengi zaidi kuliko tunavyofanya sasa katika eneo letu la kutaniko. Jinsi gani? Kwa kubadili njia zetu za kuhubiri, bali si ujumbe wetu. Katika maeneo mengi, watu wanaoishi katika nyumba zenye ulinzi mkali wanazidi kuongezeka. Wengine wengi hawapatikani nyumbani tunapowatembelea katika huduma yetu ya nyumba kwa nyumba. Kwa hiyo, huenda tukahitaji kutupa “nyavu” zetu wakati tofauti na sehemu tofauti. Kwa njia hiyo, tunamwiga Yesu. Alijitahidi sana kuzungumza na watu katika hali mbalimbali.—Mathayo 9:9; Luka 19:1-10; Yohana 4:6-15.
18. Kutoa ushahidi katika hali tofauti-tofauti kumekuwaje na matokeo? (Tia ndani sanduku “Kufanya Wanafunzi Katika Maeneo ya Wafanyabiashara.”)
18 Katika maeneo fulani duniani, kuhubiri popote watu wanapoweza kupatikana ni njia muhimu ya kufanya wanafunzi. Wafanya-wanafunzi wenye uzoefu wamekuwa wakizingatia zaidi kutoa ushahidi katika maeneo tofauti-tofauti. Zaidi ya kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, sasa wahubiri wanatoa ushahidi kwenye viwanja vya ndege, ofisini, madukani, kwenye maegesho ya magari, vituo vya basi, barabarani, bustanini, kwenye fuo, na kwingineko. Wengi wa Mashahidi waliobatizwa majuzi huko Hawaii walihubiriwa mara ya kwanza kwenye sehemu hizo. Kubadili njia zetu za kuhubiri hutusaidia kutimiza kikamili amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi.—1 Wakorintho 9:22, 23.
19. Ni sehemu gani za mgawo ambao Yesu alitupatia ambazo zitazungumziwa katika makala inayofuata?
19 Mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi haukutia ndani tu habari kuhusu kwa nini na ni wapi tunakopaswa kufanya kazi hiyo, bali pia habari kuhusu ni nini tunachopaswa kuhubiri na tunapaswa kuendelea kufanya hivyo hadi lini. Sehemu hizo mbili za mgawo ambao Yesu alitupatia zitazungumziwa katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Katika makala hii, tutazungumzia maswali mawili ya kwanza. Nayo maswali mawili ya mwisho yatazungumziwa katika makala inayofuata.
b Tunapata sababu zaidi za kuhubiri kwenye Methali 10:5; Amosi 3:8; Mathayo 24:42; Marko 12:17; Waroma 1:14, 15.
c Ili upate habari zaidi kuhusu utimizo mbalimbali wa unabii huo, ona gazeti Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 2001, ukurasa wa 12, na kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Pili, ukurasa wa 408, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’
“Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—MATHAYO 28:19, 20.
1. Ni mazungumzo gani yaliyotokea kati ya mwanafunzi Filipo na mtu fulani kutoka Ethiopia?
MTU fulani kutoka Ethiopia alikuwa amesafiri hadi Yerusalemu. Huko alimwabudu Yehova, Mungu aliyempenda. Yaonekana pia alipenda Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. Alipokuwa akirudi nyumbani katika gari lake la kukokotwa, alikuwa akisoma nakala ya maandishi ya nabii Isaya, wakati alipokutana na Filipo, mwanafunzi wa Kristo. Filipo alimuuliza Mwethiopia huyo hivi: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Mtu huyo akajibu: “Ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Filipo alimsaidia mwanafunzi huyo mnyoofu wa Biblia kuwa mwanafunzi wa Kristo.—Matendo 8:26-39.
2. (a) Ni katika njia gani jibu lililotolewa na Mwethiopia lilikuwa muhimu sana? (b) Tutazungumzia maswali gani kuhusu mgawo ambao Kristo alitoa wa kufanya wanafunzi?
2 Jibu la Mwethiopia huyo ni muhimu sana. Alisema: ‘Ninawezaje, mtu fulani asiponiongoza.’ Naam, alihitaji mtu wa kumwongoza. Maneno hayo yanaonyesha umuhimu wa maagizo hususa ambayo Yesu alitia ndani katika mgawo aliotoa wa kufanya wanafunzi. Ni maagizo gani? Ili kupata jibu, na tuendelee na mazungumzo yetu kuhusu maneno ya Yesu katika Mathayo sura ya 28. Makala iliyotangulia ilikazia maswali—kwa nini? na wapi? Sasa tutazungumzia maswali mengine mawili kuhusu amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi—nini? na lini?
“Kuwafundisha Kushika Mambo Yote”
3. (a) Mtu anakuwaje mwanafunzi wa Yesu Kristo? (b) Kufanya wanafunzi hutia ndani kufundisha nini?
3 Tunapaswa kufundisha nini ili kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Kristo? Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo ni lazima tufundishe mambo ambayo Kristo aliamuru.a Lakini ni nini kinachoweza kufanywa ili kuhakikisha kwamba mtu anayefundishwa amri za Yesu hatakuwa tu mwanafunzi bali ataendelea kuwa mwanafunzi? Jambo moja muhimu tunaloona ni kwamba Yesu alichagua maneno yake kwa makini. Ona kwamba hakusema tu: ‘Wafundisheni kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ Bali alisema: ‘Wafundisheni kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.’ (Mathayo 19:17) Hiyo inamaanisha nini?
4. (a) Inamaanisha nini kutii amri fulani? (b) Onyesha jinsi ambavyo sisi humfundisha mtu kushika amri za Kristo?
4 Kushika amri humaanisha “kutenda kupatana” na amri iliyotolewa, yaani, kuitii, au kuifuata. Basi, tunawezaje kumfundisha mtu kushika, au kutii, mambo ambayo Kristo aliamuru? Fikiria jinsi mtu anayewafundisha watu kuendesha gari anavyowaonyesha wanafunzi wake kushika sheria za barabarani. Mwalimu huyo anaweza kuwafundisha wanafunzi wake sheria za barabarani wanapokuwa darasani. Hata hivyo, ili kuwafundisha wanafunzi hao jinsi ya kutii sheria hizo, anapaswa kuwaongoza wanapoendesha gari katika barabara yenye magari na wanapojitahidi kutumia mambo ambayo wamejifunza. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia pamoja na watu, sisi huwafundisha amri za Kristo. Hata hivyo, tunahitaji pia kuwaongoza wanafunzi wanapojitahidi kufuata maagizo ya Kristo maishani na katika huduma. (Yohana 14:15; 1 Yohana 2:3) Hivyo, ili kufuata kikamili amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi tunahitaji kuwafundisha na kuwaongoza watu. Kwa njia hiyo, tunaiga kielelezo kilichowekwa na Yesu na Yehova mwenyewe.—Zaburi 48:14; Ufunuo 7:17.
5. Kwa nini huenda mtu tunayejifunza Biblia naye akasita kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi?
5 Kuwafundisha wengine kushika amri za Yesu hutia ndani kuwasaidia watii amri ya kufanya wanafunzi. Huenda hilo likawa jambo gumu kwa baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia. Hata kama hapo awali walikuwa washiriki wenye bidii wa kanisa fulani la dini zinazojiita za Kikristo, haielekei kwamba wale waliokuwa walimu wao wa kidini waliwafundisha kwenda na kufanya wanafunzi. Viongozi fulani wa dini wanakiri waziwazi kwamba dini zinazojiita za Kikristo zimeshindwa kabisa kuwafundisha waumini wao kueneza injili. John R. W. Stott, msomi wa Biblia alisema hivi kuhusu amri ya Yesu ya kwenda ulimwenguni na kuwasaidia watu wa namna zote wawe wanafunzi: “Leo udhaifu ulio mkubwa zaidi wa Wakristo waeneza-injili ni kule kushindwa kwetu kutii kile kinachomaanishwa na amri hiyo.” Aliongeza kusema: “Tuna mwelekeo wa kutangaza ujumbe wetu kutoka mbali. Wakati mwingine sisi huonekana kama watu ambao wanawashauri watu wanaozama maji huku tukiwa mahali salama ufuoni. Hatuingii majini kuwaokoa. Tunaogopa kulowa maji.”
6. (a) Tunawezaje kuiga kielelezo cha Filipo tunapomsaidia mwanafunzi wa Biblia? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba tunajali wakati mwanafunzi wa Biblia anapoanza kuhubiri?
6 Ikiwa mtu tunayejifunza Biblia naye alikuwa mshiriki wa dini ambayo waumini wake ‘huogopa kulowa maji,’ huenda ikawa vigumu kwake kuacha kuogopa maji ya mfano, na kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Atahitaji msaada. Hivyo, tunahitaji kuwa wenye subira tunapotoa maagizo na mwongozo ambao humsaidia kuwa na uelewaji wenye kina na kumchochea kutenda, kama vile mafundisho ya Filipo yalivyomsaidia yule Mwethiopia kuelewa mambo na kumchochea kubatizwa. (Yohana 16:13; Matendo 8:35-38) Pia, tamaa yetu ya kuwafundisha wanafunzi wa Biblia kushika amri ya kufanya wanafunzi hutuchochea kuwasaidia na kuwaongoza wanapochukua hatua za kwanza katika kuhubiri Ufalme.—Mhubiri 4:9, 10; Luka 6:40.
“Mambo Yote”
7. Kuwafundisha wengine ‘washike mambo yote’ hutia ndani kuwafundisha amri zipi?
7 Hatuwafundishi tu wanafunzi wetu wapya kufanya wanafunzi. Yesu alituagiza tuwafundishe wengine ‘washike mambo yote’ aliyoamuru. Bila shaka, hilo linatia ndani amri mbili zilizo kuu—kumpenda Mungu na kumpenda jirani. (Mathayo 22:37-39) Mwanafunzi mpya anawezaje kufundishwa ashike amri hizo?
8. Onyesha jinsi mwanafunzi mpya anavyoweza kufundishwa amri ya kuonyesha upendo.
8 Fikiria tena mfano wa mtu anayefundishwa kuendesha gari. Mwanafunzi huyo anapoendesha gari katika barabara yenye magari akiwa pamoja na mwalimu wake, yeye hujifunza kwa kumsikiliza mwalimu wake na pia kwa kuwatazama madereva wengine. Kwa mfano, huenda mwalimu huyo akamwonyesha dereva ambaye kwa fadhili anamruhusu mwingine apite mbele yake; au dereva ambaye kwa heshima anapunguza mwangaza wa taa zake za mbele ili asifanye madereva kutoka upande ule mwingine wasione vizuri; au dereva anayejitolea kumsaidia rafiki ambaye gari lake limeharibika. Mifano hiyo humfundisha mwanafunzi mambo muhimu anayoweza kutumia anapoendesha gari. Vivyo hivyo, mwanafunzi mpya anayesafiri kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima hujifunza kutoka kwa mwalimu wake na pia kutokana na vielelezo vizuri anavyoona kwenye kutaniko.—Mathayo 7:13, 14.
9. Mwanafunzi mpya hujifunzaje maana ya kushika amri ya kuonyesha upendo?
9 Kwa mfano, huenda mwanafunzi wa Biblia akamwona mzazi asiye na mwenzi wa ndoa ambaye hujitahidi sana kuja kwenye Jumba la Ufalme akiandamana na watoto wake wadogo. Huenda akamwona mtu aliyeshuka moyo ambaye huhudhuria mikutano kwa uaminifu ingawa anapambana na mshuko-moyo, mjane mzee anayewapeleka wazee wengine kwenye kila mkutano wa kutaniko kwa gari lake, au kijana anayesaidia kusafisha Jumba la Ufalme. Huenda mwanafunzi huyo wa Biblia akamwona mzee wa kutaniko ambaye kwa uaminifu huwa mstari wa mbele katika utumishi wa shambani licha ya kuwa na madaraka mengi kutanikoni. Huenda akakutana na Shahidi ambaye ni mlemavu na asiyeweza kutoka nyumbani lakini ambaye huwatia moyo wote kiroho wanaomtembelea. Huenda mwanafunzi huyo akaona mume na mke ambao wanajitahidi sana kufanya marekebisho maishani mwao ili kuwatunza wazazi wao waliozeeka. Kwa kuwatazama Wakristo hao wenye fadhili, wenye kusaidia, na wanaotegemeka, mwanafunzi huyo mpya hujifunza kupitia kielelezo chao maana ya kutii amri ya Kristo ya kumpenda Mungu na jirani, na hasa waamini wenzetu. (Methali 24:32; Yohana 13:35; Wagalatia 6:10; 1 Timotheo 5:4, 8; 1 Petro 5:2, 3) Kwa njia hiyo, kila mshiriki wa kutaniko la Kikristo anaweza—na anapaswa—kufundisha na kuongoza.—Mathayo 5:16.
“Mpaka Umalizio wa Mfumo wa Mambo”
10. (a) Tutaendelea kufanya wanafunzi mpaka lini? (b) Yesu aliweka kielelezo gani kuhusu kutimiza migawo?
10 Tunapaswa kuendelea kufanya wanafunzi mpaka lini? Mpaka umalizio wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 28:20) Je, tutaweza kutimiza sehemu hii ya mgawo wa Yesu? Tunaazimia kufanya hivyo tukiwa kutaniko la duniani pote. Katika miaka iliyopita tumefurahia kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kuwatafuta wale ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Matendo 13:48) Leo, Mashahidi wa Yehova hutumia wastani wa saa zaidi ya milioni tatu kila siku katika mwaka kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ulimwenguni pote. Sisi hufanya hivyo kwa kuwa tunafuata kielelezo cha Yesu. Alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Hiyo pia ndiyo tamaa yetu ya kutoka moyoni. (Yohana 20:21) Hatutaki tu kuanza kazi tuliyokabidhiwa, bali tunataka kuimaliza.—Mathayo 24:13; Yohana 17:4.
11. Ni nini kimewapata baadhi ya ndugu na dada zetu Wakristo, nasi tunapaswa kujiuliza nini?
11 Hata hivyo, tunasikitika kuona kwamba baadhi ya waamini wenzetu wamekuwa dhaifu kiroho, na hivyo wamepunguza mwendo au wameacha kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Je, kuna njia ya kuwasaidia waanze kushirikiana tena na kutaniko na kurudia kazi yao ya kufanya wanafunzi? (Waroma 15:1; Waebrania 12:12) Jinsi ambavyo Yesu aliwasaidia mitume wake walipopatwa na udhaifu wa muda huonyesha jinsi tunavyoweza kufanya leo.
Onyesha Kwamba Unajali
12. (a) Punde kabla ya Yesu kufa, mitume wake walifanya nini? (b) Yesu alishughulikaje na mitume wake licha ya wao kuonyesha udhaifu mkubwa?
12 Kifo cha Yesu kilipokaribia mwishoni mwa huduma yake duniani, mitume ‘walimwacha na kukimbia.’ Kama Yesu alivyokuwa ametabiri, ‘walitawanyika na kwenda kila mmoja kwenye nyumba yake.’ (Marko 14:50; Yohana 16:32) Yesu alishughulikaje na rafiki zake waliokuwa wamedhoofika kiroho? Punde baada ya Yesu kufufuka, aliwaambia hivi baadhi ya wafuasi wake: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu, ili wapate kwenda zao Galilaya; na huko wataniona.” (Mathayo 28:10) Ingawa mitume walionyesha udhaifu mkubwa, bado Yesu aliwaita “ndugu zangu.” (Mathayo 12:49) Hakuwa amekata tamaa kuwaelekea. Kwa njia hiyo, Yesu akawa mwenye rehema na mwenye kusamehe, kama vile Yehova alivyo mwenye rehema na mwenye kusamehe. (2 Wafalme 13:23) Tunawezaje kumwiga Yesu?
13. Tunapaswa kuwaonaje wale ambao wamekuwa dhaifu kiroho?
13 Tunapaswa kuwajali sana wale waliopunguza mwendo au walioacha kushiriki katika huduma. Tungali tunakumbuka kazi za upendo ambazo waamini hao wenzetu walifanya zamani— wengine labda kwa miaka mingi. (Waebrania 6:10) Kwa kweli tunakosa ushirika wao. (Luka 15:4-7; 1 Wathesalonike 2:17) Lakini tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali?
14. Kwa kumwiga Yesu, tunawezaje kumsaidia mtu aliye dhaifu?
14 Yesu aliwaambia mitume waliovunjika moyo kwamba wanapaswa kwenda Galilaya na kwamba wangemwona huko. Kwa kweli, Yesu aliwaalika wahudhurie mkutano fulani wa kipekee. (Mathayo 28:10) Vivyo hivyo leo, tunawatia moyo wale walio dhaifu kiroho wahudhurie mikutano ya kutaniko la Kikristo, na huenda tukahitaji kuwatia moyo mara nyingi ili wafanye hivyo. Kuhusu mitume, mwaliko wa Yesu ulikuwa na matokeo, kwa kuwa ‘wale wanafunzi kumi na mmoja waliingia Galilaya mpaka kwenye mlima ambako Yesu alikuwa amewafanyia mpango.’ (Mathayo 28:16) Tunafurahi kama nini wakati wale walio dhaifu wanapoitikia mwaliko wetu wa uchangamfu, na kuanza tena kuhudhuria mikutano ya Kikristo!—Luka 15:6.
15. Tunawezaje kufuata kielelezo cha Yesu katika kuwakaribisha watu dhaifu wanaokuja mahali petu pa mikutano?
15 Tutafanyaje Mkristo aliye dhaifu anapofika kwenye Jumba la Ufalme? Yesu, alifanya nini alipoona mitume wake ambao imani yao ilikuwa imedhoofika kwa muda, wakiwa mahali walipopanga kukutana? ‘Yesu alikaribia na kuzungumza nao.’ (Mathayo 28:18) Hakuwatazama tu kutoka mbali, bali alienda walipokuwa. Wazia jinsi mitume walivyofurahi wakati Yesu alipochukua hatua hiyo! Sisi pia na tuchukue hatua ya kwanza na kuwakaribisha kwa uchangamfu wale walio dhaifu kiroho ambao wanajitahidi kurudi katika kutaniko la Kikristo.
16. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi ambavyo Yesu alishughulika na wafuasi wake? (b) Tunawezaje kuonyesha maoni kama ya Yesu kuelekea walio dhaifu? (Ona maelezo ya chini.)
16 Yesu alifanya jambo gani lingine? Kwanza, alitoa tangazo fulani: “Nimepewa mamlaka yote.” Pili, akatoa mgawo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Tatu, akatoa ahadi: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote.” Lakini je, umeona jambo ambalo Yesu hakufanya? Hakuwakemea wanafunzi kwa udhaifu na shaka zao. (Mathayo 28:17) Je, njia yake ilikuwa na matokeo? Ndiyo, kwa kuwa muda si muda mitume walikuwa wameanza tena “kufundisha na kutangaza habari njema.” (Matendo 5:42) Kwa kuiga kielelezo cha Yesu kuhusu jinsi tunavyowaona na tunavyowatendea walio dhaifu, tunaweza kutarajia kupata matokeo kama hayo yenye kuchangamsha moyo katika kutaniko letu.b—Matendo 20:35.
“Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”
17, 18. Maneno ya Yesu “mimi nipo pamoja nanyi siku zote” yana matokeo gani yenye kuimarisha?
17 Maneno haya ya mwisho kuhusu mgawo ambao Yesu alitoa, “Nipo pamoja nanyi siku zote,” yana matokeo yenye kuimarisha kwa wote wanaojitahidi kutimiza amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi. Hata tukabili upinzani wa aina gani kutoka kwa maadui dhidi ya kazi yetu ya kuhubiri Ufalme, na hata watuchongee kwa njia gani, hatupaswi kuogopa. Kwa nini? Kwa kuwa Yesu, Kiongozi wetu, ambaye ana ‘mamlaka yote mbinguni na duniani,’ yuko pamoja nasi ili kutusaidia!
18 Ahadi ya Yesu “mimi nipo pamoja nanyi siku zote” hutufariji sana pia. Tunapojitahidi kutii amri ya Kristo ya kufanya wanafunzi, sisi hupata furaha na pia huzuni wakati mwingine. (2 Mambo ya Nyakati 6:29) Baadhi yetu hupatwa na huzuni tunapoomboleza kifo cha mpendwa. (Mwanzo 23:2; Yohana 11:33-36) Wengine wanapambana na uzee, wakati afya na nguvu zinapoendelea kuzorota. (Mhubiri 12:1-6) Hata wengine hukabili vipindi ambapo wanalemewa na hali ya kuvunjika moyo. (1 Wathesalonike 5:14) Na hesabu inayoongezeka kati yetu hupambana na hali ngumu za kiuchumi. Hata hivyo, licha ya magumu hayo, sisi hufanikiwa katika huduma yetu kwa sababu Yesu yuko pamoja nasi “siku zote,” hata zile siku ngumu zaidi maishani mwetu.—Mathayo 11:28-30.
19. (a) Kuna maagizo gani katika mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi? (b) Ni nini hutusaidia kutimiza mgawo ambao Kristo alitoa?
19 Kama ambavyo tumeona katika makala hii na ile iliyotangulia, mgawo ambao Yesu alitoa wa kufanya wanafunzi unahusu sehemu zote nne. Yesu alituambia ni kwa nini na ni wapi tunapopaswa kutekeleza amri yake. Pia alituambia ni nini tunachopaswa kufundisha na tunapaswa kufanya hivyo mpaka lini. Kweli, ni jambo gumu kutimiza mgawo huo. Lakini kwa kuwa Kristo aliye na mamlaka anatuunga mkono na yupo pamoja nasi, tunaweza kuutimiza! Je, hukubali?
[Maelezo ya Chini]
a Kitabu kimoja cha marejeo kinaonyesha kwamba Yesu alisema, “kuwabatiza . . . kuwafundisha,” bali si ‘kuwabatiza na kuwafundisha.’ Hivyo, katika amri ya kubatiza na kufundisha ‘si lazima mambo hayo mawili yafuatane.’ Bali, “kufundisha ni tendo linaloendelea, ambalo kwa kadiri fulani hutangulia na kufuata ubatizo.”
b Habari zaidi kuhusu jinsi unavyopaswa kuwaona na kuwasaidia walio dhaifu inapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 2003, ukurasa wa 15-18.
-
-
‘Wafundisheni Kushika Mambo Yote Ambayo Nimewaamuru Ninyi’Mnara wa Mlinzi—2004 | Julai 1
-
-
a Kitabu kimoja cha marejeo kinaonyesha kwamba Yesu alisema, “kuwabatiza . . . kuwafundisha,” bali si ‘kuwabatiza na kuwafundisha.’ Hivyo, katika amri ya kubatiza na kufundisha ‘si lazima mambo hayo mawili yafuatane.’ Bali, “kufundisha ni tendo linaloendelea, ambalo kwa kadiri fulani hutangulia na kufuata ubatizo.”
-