-
“Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu Alimaanisha Nini Aliposema Maneno Hayo?‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 1
“Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu Alimaanisha Nini Aliposema Maneno Hayo?
“Nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”
1, 2. Ni mwaliko gani wa maana zaidi ambao mwanadamu anaweza kupata, nasi tunapaswa kujiuliza swali gani?
NI MWALIKO gani wa maana zaidi ambao umewahi kupata? Huenda ni wakati ulipoalikwa kuhudhuria tukio la pekee, kama vile arusi ya watu unaowapenda sana. Au huenda ni siku ulipoitiwa kazi ya maana. Ikiwa umewahi kupata mialiko kama hiyo, bila shaka ulisisimuka na kuona kwamba umependelewa sana. Hata hivyo, ukweli ni kwamba umepata mwaliko wa maana hata zaidi. Kila mmoja wetu amepata mwaliko huo. Na maisha yetu hutegemea sana iwapo tunaukubali au kuukataa mwaliko huo. Huo ndio uamuzi wa maana zaidi maishani.
2 Huo ni mwaliko gani? Ni mwaliko wa Yesu Kristo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mweza-Yote, Yehova, nao unapatikana katika Biblia. Yesu alisema hivi katika Marko 10:21: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ Huo ni mwaliko wa Yesu kwa kila mmoja wetu. Tunapaswa kujiuliza, ‘Je, nitaukubali mwaliko huo?’ Huenda jibu likaonekana kuwa rahisi. Ni nani anayeweza kuukataa mwaliko wa maana kama huo? Ajabu ni kwamba wengi wanaukataa. Kwa nini?
3, 4. (a) Mtu aliyemwendea Yesu kuuliza kuhusu uzima wa milele alikuwa na mambo gani ambayo watu wangeweza kuyaonea wivu? (b) Huenda Yesu aliona sifa gani nzuri za kijana huyo tajiri mwenye mamlaka?
3 Kwa mfano, mfikirie mwanamume mmoja aliyepata mwaliko huo moja kwa moja miaka 2,000 hivi iliyopita. Aliheshimiwa sana. Alikuwa na angalau mambo matatu ambayo wanadamu huyatamani, au hata kuwaonea wivu watu wenye mambo hayo, yaani, ujana, mali, na mamlaka. Biblia inamtaja kuwa “kijana,” aliyekuwa “tajiri sana,” na “mtawala.” (Mathayo 19:20; Luka 18:18, 23) Hata hivyo, kijana huyo alikuwa na sifa nyingine ya maana. Alikuwa amesikia kumhusu Mwalimu Mkuu, Yesu, naye alipenda mambo aliyoyasikia.
4 Watawala wengi wa siku hizo hawakumpa Yesu heshima aliyostahili. (Yohana 7:48; 12:42) Lakini mtawala huyo alitenda tofauti. Biblia inatuambia hivi: “[Yesu] alipokuwa akitoka aende, mtu fulani akamkimbilia akapiga magoti mbele yake na kumuuliza: ‘Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?’” (Marko 10:17) Ona jinsi kijana huyo alivyotamani sana kuzungumza na Yesu, hata akamkimbilia Yesu hadharani, kama vile maskini na watu wa hali ya chini wangefanya. Isitoshe, alipiga magoti kwa heshima mbele ya Kristo. Hivyo, kwa kiasi fulani alikuwa mnyenyekevu na alitambua uhitaji wake wa kiroho. Yesu alithamini sifa hizo njema. (Mathayo 5:3; 18:4) Basi, haishangazi kwamba ‘Yesu alimtazama na kumpenda.’ (Marko 10:21) Yesu alimjibu kijana huyo jinsi gani?
Mwaliko wa Pekee
5. Yesu alimjibu kijana huyo tajiri jinsi gani, na kwa nini “jambo moja” alilokosa si umaskini? (Ona pia maelezo ya chini.)
5 Yesu alionyesha kwamba tayari Baba yake alikuwa ametoa habari juu ya swali hilo la maana kuhusu kupata uzima wa milele. Alirejelea Maandiko, naye kijana huyo akasisitiza kwamba alikuwa akitii Sheria ya Musa kwa uaminifu. Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa na ufahamu wa pekee, Yesu angeweza kuona mambo yaliyokuwa katika moyo wa kijana huyo. (Yohana 2:25) Alitambua kwamba mtawala huyo ana tatizo la kiroho, tatizo zito sana. Hivyo, Yesu akamwambia: “Umekosa jambo moja.” “Jambo” gani? Yesu alimwambia: “Nenda, ukauze vitu ulivyo navyo uwape maskini.” (Marko 10:21) Je, Yesu alimaanisha kwamba ni lazima mtu awe maskini ili amtumikie Mungu? Hapana.a Alikuwa akifunua jambo fulani la maana sana.
6. Yesu alitoa mwaliko gani, na kukataa kwa kijana huyo tajiri kulifunua jambo gani lililokuwa katika moyo wake?
6 Ili kuonyesha waziwazi jambo ambalo kijana huyo alikosa, Yesu alimpa mwaliko huu wa pekee: ‘Njoo uwe mfuasi wangu.’ Hebu wazia, Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi alimwalika kijana huyo uso kwa uso, amfuate! Pia, Yesu alimwahidi thawabu isiyo na kifani. Alimwambia: “Utakuwa na hazina mbinguni.” Je, aliukubali mwaliko huo wa pekee? Masimulizi hayo yanasema: “Akasikitishwa na neno hilo na kwenda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.” (Marko 10:21, 22) Hivyo basi, maneno hayo ya Yesu yasiyotazamiwa yalifunua tatizo lililokuwa katika moyo wa kijana huyo. Alipenda sana mali zake, na hapana shaka kwamba alipenda sana pia mamlaka na umaarufu aliopata. Inasikitisha kuwa alipenda sana vitu hivyo kuliko alivyompenda Kristo. Basi, “jambo moja” ambalo kijana huyo alikosa ni kumpenda Yesu na Yehova kwa moyo wote na kwa kujidhabihu. Kwa kuwa kijana huyo hakuwa na upendo huo, aliukataa mwaliko huo wa pekee! Hata hivyo, mwaliko huo unakuhusu wewe namna gani?
7. Je, mwaliko wa Yesu unatuhusu sisi leo? Eleza.
7 Yesu hakumwalika kijana huyo tu wala watu wachache tu. Yesu alisema: ‘Mtu yeyote akitaka kunifuata, na anifuate sikuzote.’ (Luka 9:23) Ona kwamba “mtu yeyote” anaweza kuwa mfuasi wa Kristo ikiwa kwa kweli ‘anataka.’ Mungu anawavuta watu wa aina hiyo, wenye moyo mnyoofu, kwa Mwana wake. (Yohana 6:44) Si matajiri tu, si maskini tu, si watu wa jamii au taifa fulani tu, wala si wale wanaoishi katika kipindi fulani cha wakati tu, bali wote wanapewa nafasi ya kukubali mwaliko wa Yesu. Kwa hiyo, maneno haya ya Yesu, ‘Njoo uwe mfuasi wangu,’ kwa kweli yanakuhusu wewe pia.
-
-
“Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu Alimaanisha Nini Aliposema Maneno Hayo?‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
a Yesu hakumwambia kila mtu aliyemfuata aache mali zake zote. Na ingawa alisema ingekuwa vigumu sana kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu, aliongeza hivi: “Mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:23, 27) Kwa kweli, baadhi ya wafuasi wa Kristo walikuwa matajiri. Walipata mashauri hususa katika kutaniko la Kikristo, lakini hawakuagizwa wawape maskini mali zao zote.—1 Timotheo 6:17.
-