-
Ukristo wa Mapema na SerikaliMnara wa Mlinzi—1996 | Mei 1
-
-
Kumlipa Kaisari “Haki” Zake
Yesu aliandaa kanuni ambayo ingeongoza mwenendo wa Mkristo kuelekea Serikali ya Roma au kuelekea serikali yoyote ile alipotangaza hivi: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” (Mathayo 22:21) Shauri hili kwa wafuasi wa Yesu lilitofautiana kabisa na mtazamo wa Wayahudi wenye kufuatia utukuzo wa taifa ambao walichukia kutawalwa na Roma na kubisha juu ya uhalali wa kulipa kodi kwa mamlaka ya kigeni.
Baadaye, Paulo aliwaambia hivi Wakristo walioishi Roma: “Kwa hiyo kuna sababu yenye kushurutisha nyinyi watu kuwa katika ujitiisho, si kwa sababu ya hasira hiyo ya kisasi tu, bali pia kwa sababu ya dhamiri yenu. Kwa maana hiyo ndiyo sababu mnalipa kodi pia; kwa maana wao [“mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali] ni watumishi wa Mungu wa watu wote wakitumikia daima kwa kusudi hilihili. Walipeni wote haki zao, kwa yeye atakaye kodi, kodi; kwa yeye atakaye ushuru, ushuru.” (Waroma 13:5-7, NW) Ingawa Wakristo hawakuwa sehemu ya ulimwengu, walikuwa na wajibu wa kuwa wakazi wenye kufuatia haki na wenye kulipa kodi, wakilipa Serikali kwa ajili ya utumishi mbalimbali uliotolewa.—Yohana 17:16.
Lakini je, maneno ya Yesu yanahusu kulipa kodi pekee? Kwa kuwa Yesu hakufafanua kihususa yaliyo ya Kaisari na yaliyo ya Mungu, kuna mambo yasiyo wazi sana ambayo ni lazima yaamuliwe kulingana na hali zilizopo au kulingana na uelewevu wetu wa Biblia nzima. Kwa maneno mengine, kuamua ni mambo yapi Mkristo awezayo kulipa Kaisari nyakati nyingine yaweza kuhusisha dhamiri ya Mkristo iliyoelimishwa na kanuni za Biblia.
Usawaziko Wenye Uangalifu Kati ya Wadai Wawili Wenye Kushindana
Watu wengi huelekea kusahau kwamba baada ya kutaja kwamba Kaisari alipwe yaliyo yake, Yesu aliongezea hivi: “Na [lipeni] Mungu yaliyo ya Mungu.” Mtume Petro alionyesha mambo ya kutangulizwa na Wakristo. Mara tu baada ya kushauri juu ya unyenyekeo kwa “mfalme,” au maliki, na “magavana” wake, Petro aliandika: “Iweni kama watu huru, na bado mkishika uhuru wenu, si kama kisitiri cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu. Heshimuni watu wa namna zote, iweni na upendo kwa ushirika wote wa akina ndugu, iweni katika hofu ya Mungu, iweni na heshima kwa mfalme.” (1 Petro 2:16, 17, NW) Mtume alionyesha kwamba Wakristo ni watumwa wa Mungu, si wa mtawala wa kibinadamu. Ingawa wanapaswa kuonyesha heshima na staha ifaayo kwa wawakilishi wa Serikali, wao wanapaswa kufanya hivyo katika kumhofu Mungu, ambaye sheria zake ni kuu kuliko zote.
Miaka mingi mapema Petro alielewesha wazi ukuu wa sheria ya Mungu juu ya sheria ya mwanadamu. Sanhedrini ya Kiyahudi ilikuwa baraza la utekelezaji wa mambo ambalo Waroma walilipatia mamlaka ya kiserikali na mambo ya kidini. Lilipoamuru wafuasi wa Yesu wakome kufundisha katika jina la Kristo, Petro pamoja na mitume wengine walijibu hivi kwa staha lakini kwa uthabiti: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kwa wazi, iliwapasa Wakristo wa mapema wadumishe usawaziko wenye uangalifu kati ya utii kwa Mungu na unyenyekeo ufaao kwa mamlaka za kibinadamu. Tertullian alisema hivi mapema katika karne ya tatu W.K.: “Ikiwa zote ni za Kaisari, Mungu atabakiziwa nini?”
-
-
Mungu na KaisariMnara wa Mlinzi—1996 | Mei 1
-
-
Mungu na Kaisari
“Basi, vya Kaisari mpeni Kaisari, na vya Mungu mpeni Mungu.”—LUKA 20:25.
1. (a) Ni nini cheo cha Yehova kilichokwezwa? (b) Tunawiwa nini na Yehova ambacho hatuwezi kumpa Kaisari?
YESU KRISTO alipotoa agizo hilo, hakuwa na shaka lolote kwamba matakwa ya Mungu kwa watumishi Wake hutangulia chochote ambacho Kaisari, au Serikali, huenda akataka wafanye. Yesu alijua zaidi ya mtu yeyote ukweli wa sala ya mtunga-zaburi kwa Yehova: “Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, na mamlaka [enzi kuu]a yako ni ya vizazi vyote.” (Zaburi 145:13) Ibilisi alipomtolea Yesu mamlaka juu ya falme zote za dunia ikaliwayo, Yesu alijibu hivi: “Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Luka 4:5-8) Ibada haingepewa kamwe “Kaisari,” iwe Kaisari ni maliki wa Roma, mtawala mwingine wa kibinadamu, au Serikali yenyewe.
2. (a) Cheo cha Shetani ni nini kuhusiana na ulimwengu huu? (b) Shetani ana cheo chake kwa ruhusa ya nani?
2 Yesu hakukana kwamba falme za ulimwengu zilikuwa za Shetani. Baadaye, alimwita Shetani “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 16:11) Kuelekea mwisho wa karne ya kwanza W.K., mtume Yohana aliandika: “Twajua ya kuwa sisi tu wa Mungu; na dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Hili halimaanishi kwamba Yehova ameacha enzi kuu yake juu ya dunia. Kumbuka kwamba Shetani alisema hivi alipokuwa akimtolea Yesu utawala juu ya falme za kisiasa: “Nitakupa uwezo juu ya tawala zote hizi, . . . kwa maana nimepewa hivi vyote.” (Luka 4:6, Habari Njema kwa Watu Wote) Shetani hutawala falme za ulimwengu kwa ruhusa ya Mungu tu.
3. (a) Serikali za mataifa zina cheo gani mbele ya Yehova? (b) Tunaweza kusemaje kwamba utii kwa serikali za ulimwengu huu haumaanishi kujitiisha kwa Shetani, mungu wa ulimwengu huu?
3 Vivyo hivyo, Serikali hutawala kwa sababu tu Mungu akiwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu airuhusu ifanye hivyo. (Yohana 19:11) Hivyo, “mamlaka zilizopo” zaweza kusemwa kuwa “zimewekwa na Mungu katika mahali pa vyeo vyazo vyenye kuhusiana.” Kwa kuilinganisha na mamlaka kuu kuliko zote ya enzi kuu ya Yehova, mamlaka yao ni kidogo sana. Hata hivyo, hizo ni “mhudumu wa Mungu,” “watumishi wa Mungu wa watu wote,” kwa sababu hizo huandaa utumishi unaohitajika, hudumisha amani na utengamano, na kuadhibu watenda maovu. (Waroma 13:1, 4, 6, NW) Basi Wakristo wahitaji kuelewa kwamba hata ikiwa Shetani ndiye mtawala asiyeonekana wa ulimwengu huu, au mfumo huu, wao hawamtii Shetani wanapotambua utii wao unaohusu Serikali. Wao wanamtii Mungu. Katika mwaka huu wa 1996, Serikali ya kisiasa ingali sehemu ya “mpango wa Mungu,” mpango wa muda ambao Mungu aruhusu uwepo, na watumishi wa Yehova wa kidunia wanapaswa kutambua hivyo.—Warumi 13:2.
Watumishi wa Kale wa Yehova na Serikali
4. Kwa nini Yehova aliruhusu Yosefu kuwa mashuhuri katika serikali ya Misri?
4 Katika nyakati za kabla ya Ukristo, Yehova aliwaruhusu baadhi ya watumishi wake wawe na vyeo mashuhuri katika Serikali za mataifa. Kwa kielelezo, katika karne ya 18 K.W.K., Yosefu akawa waziri mkuu wa Misri, akiwa wa pili tu kwa Farao mwenye kutawala. (Mwanzo 41:39-43) Matukio yaliyofuata yalidhihirisha kwamba Yehova alipanga mambo hivyo ili Yosefu atumikie akiwa chombo cha kuhifadhi ‘mbegu ya Abrahamu,’ wazao wake, kwa ajili ya kutimizwa kwa makusudi Yake. Bila shaka yapasa kukumbukwa kwamba Yosefu aliuzwa utumwani Misri, naye aliishi katika kipindi ambacho watumishi wa Mungu hawakuwa na Sheria ya Kimusa wala “sheria ya Kristo.”—Mwanzo 15:5-7, NW; 50:19-21; Wagalatia 6:2.
5. Kwa nini Wayahudi waliokuwa uhamishoni waliamriwa ‘wautakie amani’ Babiloni?
5 Karne nyingi baadaye nabii mwaminifu Yeremia alipuliziwa na Yehova awaambie Wayahudi waliokuwa uhamishoni wanyenyekee watawala walipokuwa uhamishoni Babiloni na hata kuliombea amani jiji hilo. Katika barua yake kwao, yeye aliandika: “BWANA wa majeshi, Mungu wa Israeli, awaambia hivi watu wote waliochukuliwa mateka, . . . Kautakieni amani mji ule, ambao nimewafanya mchukuliwe mateka, mkauombee kwa BWANA; kwa maana katika amani yake mji huo ninyi mtapata amani.” (Yeremia 29:4, 7) Sikuzote watu wa Yehova wana sababu ya ‘kutafuta amani’ kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya taifa wanaloishi, ili wawe na uhuru wa kuabudu Yehova.—1 Petro 3:11.
6. Ingawa walipewa vyeo vya juu vya kiserikali, ni kwa njia zipi Danieli na waandamani wake watatu walikataa kuridhiana kuhusu Sheria ya Yehova?
6 Wakati walipokuwa uhamishoni katika Babiloni, Danieli na Wayahudi wengine waaminifu watatu ambao walikuwa mateka katika utumwa Babiloni walinyenyekea mazoezi ya Serikali nao wakawa watumishi wa serikali wenye vyeo vya juu katika Babilonia. (Danieli 1:3-7; 2:48, 49) Hata hivyo, hata wakati walipokuwa wakizoezwa, wao walichukua msimamo thabiti juu ya masuala ya ulaji ambayo yangeweza kuwafanya wavunje Sheria ambayo Mungu wao, Yehova, alikuwa ameandaa kupitia Musa. Wao walibarikiwa kwa kufanya hivyo. (Danieli 1:8-17) Mfalme Nebukadneza alipoisimamisha sanamu ya Serikali, waandamani watatu wa Danieli Waebrania yaonekana walishurutishwa kuhudhuria sherehe hizo wakiwa pamoja na wakuu wenzao wa Serikali. Hata hivyo, wao walikataa ‘kuanguka na kuiabudu’ hiyo sanamu ya Serikali. Tena, Yehova akabariki uaminifu-maadili wao. (Danieli 3:1-6, 13-28) Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova hustahi bendera ya taifa wanamoishi, lakini hawataifanyia tendo la ibada.—Kutoka 20:4, 5; 1 Yohana 5:21.
7. (a) Danieli alichukua msimamo gani mzuri, ijapokuwa alikuwa na cheo cha juu katika mfumo wa kiserikali wa Babiloni? (b) Ni mabadiliko yapi yaliyokuja katika nyakati za Kikristo?
7 Baada ya kuanguka kwa utawala mpya wa Babiloni, Danieli alipewa cheo kikubwa katika utawala mpya wa Umedi na Uajemi ambao ulichukua mahali pa Babiloni. (Danieli 5:30, 31; 6:1-3) Lakini hakuacha cheo chake cha juu kimfanye aridhiane uaminifu-maadili wake. Sheria ya Serikali ilipotaka amwabudu Mfalme Dario badala ya Yehova, yeye alikataa. Kwa sababu hiyo, alitupwa kwa simba, lakini Yehova alimwokoa. (Danieli 6:4-24) Bila shaka, hilo lilitukia katika nyakati za kabla ya Ukristo. Mara kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, watumishi wa Mungu wakaja kuwa ‘chini ya sheria mbele za Kristo.’ Mambo mengi ambayo yaliruhusiwa chini ya mfumo wa Kiyahudi yalipaswa kuonwa kwa njia tofauti, kwa kutegemea njia ambayo sasa Yehova alikuwa akishughulikia watu wake.—1 Wakorintho 9:21; Mathayo 5:31, 32; 19:3-9.
Mtazamo wa Yesu Kuelekea Serikali
8. Ni tukio gani lionyeshalo kwamba Yesu aliazimia kuepuka kujihusisha kisiasa?
8 Yesu Kristo alipokuwa duniani, yeye aliweka viwango vya juu zaidi kwa ajili ya wafuasi wake, naye alikataa kujiingiza kabisa katika mambo ya kisiasa au kijeshi. Baada ya Yesu kulisha kimuujiza maelfu kadhaa ya watu kwa vipande vichache vya mkate na samaki wadogo wawili, Wayahudi walitaka kumkamata na kumfanya kuwa mfalme wa kisiasa. Lakini Yesu akawaepa na kuenda milimani upesi. (Yohana 6:5-15) Kuhusu tukio hili, The New International Commentary on the New Testament chasema: “Kulikuwa na tamaa kubwa sana ya utaifa miongoni mwa Wayahudi wa wakati huo, na bila shaka wengi wa wale waliouona huo muujiza walihisi kwamba hapa palikuwa na kiongozi wa kimungu, ambaye alifaa kabisa kuwaongoza dhidi ya Waroma. Basi wakaazimia kumfanya mfalme.” Hicho chaongezea kwamba Yesu “alikataa kwa dhati” toleo hili la uongozi wa kisiasa. Kristo hakuunga mkono maasi yoyote ya Kiyahudi dhidi ya utawala wa Kiroma. Kwa kweli alitabiri matokeo ya uasi ambao ungetokea baada ya kifo chake—ole mbaya sana kwa wakazi wa Yerusalemu na uharibifu wa jiji hilo.—Luka 21:20-24.
9. (a) Yesu alifafanuaje uhusiano baina ya Ufalme wake na ulimwengu? (b) Ni mwongozo gani ambao Yesu aliwapa wafuasi wake kwa habari ya shughuli zao na serikali za ulimwengu?
9 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alimwambia hivi mwakilishi wa kipekee wa maliki wa Roma katika Yudea: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa.” (Yohana 18:36) Mpaka Ufalme wake ukomeshe utawala wa serikali za kisiasa, wanafunzi wa Kristo hufuata kielelezo chake. Wao hujitiisha kwa mamlaka zilizowekwa lakini hawajiingizi katika miradi yazo ya kisiasa. (Danieli 2:44; Mathayo 4:8-10) Yesu aliwaandalia wanafunzi wake miongozo, akisema: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” (Mathayo 22:21) Mapema, katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alikuwa amesema: ‘Mtu akikulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye maili mbili.’ (Mathayo 5:41) Katika muktadha wa mahubiri haya, Yesu alikuwa akitoa kielezi juu ya kanuni ya kuwa tayari kunyenyekea matakwa halali, iwe ni katika mahusiano ya kibinadamu au katika matakwa ya kiserikali ambayo yanapatana na sheria ya Mungu.—Luka 6:27-31; Yohana 17:14, 15.
Wakristo na Kaisari
10. Kulingana na mwanahistoria mmoja, Wakristo wa mapema walichukua msimamo gani wa kidhamiri kuhusu Kaisari?
10 Miongozo hii michache ilipasa kuongoza uhusiano kati ya Wakristo na Serikali. Katika kitabu chake The Rise of Christianity, mwanahistoria E. W. Barnes aliandika: “Wakati wowote, katika karne nyingi zijazo, ikiwa Mkristo angekuwa na shaka juu ya wajibu wake kwa Serikali, yeye angeendea mafundisho yenye mamlaka ya Kristo. Angelipa kodi: fedha za kutozwa huenda zilikuwa nyingi—hizo zilikuwa zisizoweza kuvumilika kabla ya kuanguka kwa Milki ya Magharibi—lakini Mkristo angezivumilia. Vilevile angekubali wajibu mwingine wote wa Serikali, maadamu hakutakikana kumpa Kaisari yaliyo ya Mungu.”
11. Paulo aliwashaurije Wakristo jinsi ya kushughulika na watawala wa kilimwengu?
11 Ilikuwa kupatana na hiyo kanuni kwamba, muda uzidio kidogo miaka 20 baada ya kifo cha Kristo, mtume Paulo aliwaambia Wakristo katika Roma: “Kila nafsi na iwe katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa.” (Waroma 13:1, NW) Karibu miaka kumi baadaye, muda mfupi kabla ya kufungwa kwake kwa mara ya pili na kuuawa katika Roma, Paulo alimwandikia Tito hivi: “Uwakumbushe watu [Wakristo wa Krete] kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema; wasimtukane mtu ye yote, wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote.”—Tito 3:1, 2.
Uelewevu Wenye Kuendelea Juu ya “Mamlaka Zilizo Kubwa”
12. (a) Charles Taze Russell alikuwa na maoni gani juu ya msimamo ufaao wa Mkristo kuhusu mamlaka za kiserikali? (b) Kuhusu kutumikia katika jeshi, ni maoni gani yaliyotofautiana ambayo Wakristo watiwa-mafuta walikuwa nayo wakati wa Vita ya Ulimwengu 1?
12 Mapema kama 1886, Charles Taze Russell aliandika katika kitabu The Plan of the Ages: “Wala Yesu wala Mitume hawakuingilia watawala wa kidunia kwa njia yoyote. . . . Walifundisha Kanisa kutii sheria, na kustahi wale walio mamlakani kwa sababu ya cheo chao, . . . walipe kodi zao zilizowekwa, na ila tu zilipopingana na sheria za Mungu (Mdo. 4:19; 5:29) hawakuwa wapinge sheria yoyote iliyowekwa. (Rum. 13:1-7; Mt. 22:21) Yesu na Mitume na kanisa la mapema wote walikuwa watii-sheria, ingawa wao walikuwa tofauti na serikali za ulimwengu huu nao hawakushiriki katika hizo.” Kitabu hiki kilitambulisha kwa usahihi “mamlaka za juu,” au “mamlaka zilizo kubwa,” zinazotajwa na mtume Paulo, kuwa mamlaka za kiserikali za kibinadamu. (Warumi 13:1, King James Version) Katika 1904 kitabu The New Creation kilisema kwamba Wakristo wa kweli “wapaswa kuwa miongoni mwa watu wenye kutii sheria zaidi wa wakati huu—si wachochezi, si wagomvi, si watafuta-makosa.” Jambo hilo lilieleweka kwa wengine kumaanisha unyenyekeo kamili kwa mamlaka, hata kufikia hatua ya kukubali utumishi katika jeshi wakati wa Vita ya Ulimwengu 1. Hata hivyo wengine waliona utumishi wa jeshi kuwa kinyume cha taarifa hii ya Yesu: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Bila shaka, uelewevu wazi zaidi wa unyenyekeo wa Kikristo kwa mamlaka zilizo kubwa ulihitajika.
13. Ni badiliko gani katika uelewevu wa utambulisho wa mamlaka za juu lililotolewa katika 1929, na hilo lilithibitikaje kuwa lenye manufaa?
13 Katika 1929, wakati sheria za serikali mbalimbali zilipoanza kukataza mambo aliyoyaamuru Mungu au kudai mambo ambayo sheria ya Mungu ilikataza, ilihisiwa kwamba mamlaka za juu lazima zilikuwa ni Yehova Mungu na Yesu Kristo.b Huo ulikuwa ndio uelewevu wa watumishi wa Yehova katika kipindi chenye umaana cha kabla ya na wakati wa Vita ya Ulimwengu 2 na kuendelea hadi ile Vita Baridi, iliyokuwa yenye kuogofywa pia na yenye utayari kijeshi. Kwa kutazama nyuma, ni wazi kwamba maoni hayo, ambayo yalitukuza ukuu kupita wote wa Yehova na Kristo wake, yalisaidia watu wa Mungu kudumisha msimamo usioridhiana kamwe katika kipindi hicho chote kigumu.
Unyenyekeo Husianifu
14. Nuru iliyoongezeka iliangazwaje kwenye Warumi 13:1, 2 na maandiko yanayohusiana nalo katika 1962?
14 Katika 1961 New World Translation of the Holy Scriptures ilikamilishwa. Utayarishaji wayo ulihitaji uchunguzi wa kina sana wa lugha ya Maandiko. Tafsiri sahihi kabisa ya maneno ambayo hayakutumiwa katika Warumi sura ya 13 pekee bali yaliyotumiwa pia katika mafungu kama Tito 3:1, 2 na 1 Petro 2:13, 17 yalidhihirisha kwamba usemi “mamlaka zilizo kubwa” haukurejezea Mamlaka Kuu Kupita Zote, Yehova, na Mwanaye, Yesu, bali ulirejezea mamlaka za kiserikali za kibinadamu. Mwishoni-mwishoni mwa 1962, makala zilichapishwa katika Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) zilizotoa maelezo sahihi ya Warumi sura ya 13 na pia kuandaa mwono wa wazi kuliko ule wa wakati wa C. T. Russell. Makala hizi zilisema kwamba utii wa Kikristo kwa mamlaka hauwezi kuwa kamili. Ni lazima uwe husianifu, ili usifanye watumishi wa Mungu wapingane na sheria za Mungu. Makala zaidi za Mnara wa Mlinzi zimekazia jambo hili muhimu.c
15, 16. (a) Uelewevu mpya wa Warumi sura ya 13 ulitokeza maoni gani yenye usawaziko mzuri zaidi? (b) Ni maswali gani yanayobaki kujibiwa?
15 Ufunguo huu wa uelewevu sahihi wa Warumi sura ya 13 umewezesha watu wa Yehova kusawazisha staha inayostahili mamlaka za kisiasa na msimamo usioridhiana juu ya kanuni za Kimaandiko zilizo muhimu. (Zaburi 97:11; Yeremia 3:15) Umewawezesha wawe na maoni yafaayo juu ya uhusiano wao na Mungu na shughuli zao na Serikali. Umehakikisha kwamba huku wakimpa Kaisari yaliyo ya Kaisari, hawapuuzi kumpa Mungu yaliyo ya Mungu.
16 Lakini, mambo ya Kaisari ni yapi hasa? Serikali yaweza kudai Mkristo nini kihalali? Maswali haya yatazungumzwa katika makala ifuatayo.
-
-
Kumpa Kaisari Yaliyo ya KaisariMnara wa Mlinzi—1996 | Mei 1
-
-
Kumpa Kaisari Yaliyo ya Kaisari
“Wapeni wote haki zao.”—WARUMI 13:7.
1, 2. (a) Kulingana na Yesu, Wakristo wanapaswa kusawazishaje wajibu wao kwa Mungu na kwa Kaisari? (b) Ni nini lililo hangaikio la kwanza la Mashahidi wa Yehova?
KULINGANA na Yesu, kuna mambo tunayowiwa na Mungu na mambo tunayowiwa na Kaisari, au Serikali. Yesu alisema: “Mpeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu mpeni Mungu.” Kwa maneno hayo machache, yeye alitatanisha maadui na kujumlisha kwa ufupi mtazamo wenye usawaziko ambao ni lazima tuwe nao katika uhusiano wetu na Mungu na katika shughuli zetu na Serikali. Si ajabu kwamba wasikilizaji wake “wakamstaajabia sana”!—Marko 12:17.
2 Bila shaka, hangaikio la kwanza la watumishi wa Yehova ni kumpa Mungu yaliyo ya Mungu. (Zaburi 116:12-14) Hata hivyo, kwa kufanya hivyo wao hawasahau kwamba Yesu alisema ni lazima wampe Kaisari mambo fulani. Dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia zataka kwamba wao wafikirie kwa sala ni kwa kadiri gani wanaweza kumpa Kaisari yale atakayo. (Warumi 13:7) Katika nyakati za kisasa, wanasheria wengi wametambua kwamba mamlaka ya serikali ina mipaka na kwamba watu na serikali kila mahali wako chini ya sheria ya asili.
3, 4. Ni maelezo yapi ya kupendeza ambayo yamesemwa kuhusu sheria ya asili, sheria iliyofunuliwa, na sheria ya kibinadamu?
3 Mtume Paulo alirejezea sheria hii ya asili alipoandika hivi kuhusu watu wa ulimwengu: “Mambo ya Mungu yanayojulikana yamekuwa dhahiri ndani yao, kwa maana Mungu aliwadhihirishia. Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru.” Ikiwa wataiitikia, sheria ya asili hata itazisukuma dhamiri za hawa wasioamini. Hivyo, Paulo aliongezea: “Watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao [“kwa asili,” NW] yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia.”—Warumi 1:19, 20; 2:14, 15.
4 Katika karne ya 18, mwanasheria maarufu Mwingereza William Blackstone aliandika: “Sheria hii ya asili, ikiwa na [umri uleule] na binadamu na kuamriwa na Mungu mwenyewe, bila shaka ni yenye kuwajibisha zaidi kuliko [sheria] yoyote ile. Hiyo ni ya lazima katika dunia nzima, katika nchi zote, na katika nyakati zote: hakuna sheria za kibinadamu zilizo halali, ikiwa zinapingana na hii.” Blackstone aliendelea kusema juu ya “sheria iliyofunuliwa,” kama ipatikanavyo katika Biblia, akasema hivi: “Juu ya misingi hiyo miwili, hutegemea sheria ya asili na sheria iliyofunuliwa, sheria zote za kibinadamu; yaani, hakuna sheria za kibinadamu zinazopaswa kupingana na hizi.” Hayo yapatana na aliyosema Yesu kuhusu Mungu na Kaisari, kama ilivyorekodiwa kwenye Marko 12:17. Kwa wazi, kuna maeneo ambapo Mungu huwekea mipaka yale ambayo Kaisari aweza kutaka kwa Mkristo. Sanhedrini hasa ilivuka mipaka kama hiyo ilipoamuru mitume wakome kuhubiri kuhusu Yesu. Hivyo, mitume walijibu hivi kwa usahihi: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29.
“Yaliyo ya Mungu”
5, 6. (a) Kwa sababu ya kuzaliwa kwa Ufalme katika 1914, Wakristo wapaswa kuweka nini karibu zaidi akilini? (b) Mkristo hutoaje uthibitisho wa kwamba yeye ni mhudumu?
5 Wakristo walipaswa kuwa na hakika wasimpe Kaisari yaliyo ya Mungu hasa tangu 1914, Yehova Mungu aliye Mweza-Yote alipoanza kutawala akiwa mfalme kupitia Ufalme wa Kimesiya wa Kristo. (Ufunuo 11:15, 17) Zaidi ya wakati mwingine wowote, sheria ya Mungu sasa yataka Wakristo wasiwe “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, NW) Wakiwa wamejiweka wakfu kwa Mungu, Mpaji-Uhai wao, ni lazima wadhihirishe wazi kwamba wao hawawi tena mali ya nafsi zao wenyewe. (Zaburi 100:2, 3) Kama Paulo alivyoandika, sisi “tu mali ya Bwana.” (Warumi 14:8) Na zaidi, wakati wa ubatizo wa Mkristo, yeye huwekwa rasmi kuwa mhudumu wa Mungu, ili aweze kusema aliyosema Paulo: “Mungu . . . ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu.”—2 Wakorintho 3:5, 6, NW.
6 Mtume Paulo aliandika hivi pia: “Naitukuza huduma iliyo yangu.” (Warumi 11:13) Hakika twapaswa kufanya vivyo hivyo. Tuwe tunashiriki katika huduma wakati wote au nusu-wakati, twakumbuka kwamba Yehova mwenyewe alitupa mgawo wa huduma yetu. (2 Wakorintho 2:17) Kwa kuwa wengine huenda wakatilia shaka hadhi yetu, ni lazima kila Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa atoe uthibitisho dhahiri na wa kweli kwamba yeye kwa kweli ni mhudumu wa habari njema. (1 Petro 3:15) Huduma yake yapaswa ionekane katika mwenendo wake. Akiwa mhudumu wa Mungu, Mkristo apaswa kupendekeza na kuzoea maadili safi, ategemeze muungano wa familia, kuwa mfuatiaji-haki, na kustahi sheria na utengamano. (Warumi 12:17, 18; 1 Wathesalonike 5:15) Uhusiano wa Mkristo na Mungu na huduma yake aliyopewa kimungu ndiyo mambo ya maana zaidi katika maisha yake. Hawezi kuacha mambo hayo kwa amri ya Kaisari. Kwa wazi, hayo ni mambo ya kuhesabiwa miongoni mwa “yaliyo ya Mungu.”
“Yaliyo ya Kaisari”
7. Mashahidi wa Yehova wana sifa gani kuhusu kulipa kodi?
7 Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba wana wajibu wa ‘kuwa katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa,’ watawala wa kiserikali. (Waroma 13:1, NW) Hivyo, Kaisari, Serikali, anapodai mambo halali, dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia huwaruhusu kulipa madai hayo. Kwa kielelezo, Wakristo wa kweli wamo miongoni mwa watu wenye mifano bora zaidi wa kulipa kodi duniani. Katika Ujerumani gazeti la habari Münchner Merkur lilisema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Wao ndio wafuatiaji-haki zaidi na walipaji wa kodi wasiochelewa kamwe kuliko wote katika Jamhuri ya Muungano.” Katika Italia gazeti la habari La Stampa lilionelea hivi: “Wao [Mashahidi wa Yehova] ndio raia walio waaminifu-washikamanifu zaidi ambao yeyote angetamani: wao hawaepi kodi wala kutafuta kuchenga sheria zisizowafaa kwa ajili ya faida yao wenyewe.” Watumishi wa Yehova hufanya hivyo “kwa sababu ya dhamiri” zao.—Warumi 13:5, 6.
8. Je, twawiwa na Kaisari kodi za kifedha tu?
8 Je, “yaliyo ya Kaisari” ni kulipa kodi tu? La. Paulo aliorodhesha mambo mengine, kama vile hofu na heshima. Katika kitabu chake Critical and Exegetical Hand-Book to the Gospel of Matthew, msomi Mjerumani Heinrich Meyer aliandika: “Kwa [yaliyo ya Kaisari] . . . hatupaswi kuelewa kuwa yanahusu kodi ya serikali tu, bali kila kitu ambacho ni haki ya Kaisari kwa sababu ya utawala wake halali.” Mwanahistoria E. W. Barnes, katika kitabu chake The Rise of Christianity, alionelea kwamba Mkristo angelipa kodi ikiwa aliwiwa nazo na “vilevile kukubali matakwa mengine yote ya Serikali, mradi tu hangeombwa ampe Kaisari yaliyo ya Mungu.”
9, 10. Huenda Mkristo akasita kivipi kuhusu kumpa Kaisari haki yake, lakini ni mambo gani ya hakika yanayopaswa kukumbukwa?
9 Ni mambo yapi ambayo huenda Serikali ikataka bila kuingilia mambo ambayo kwa halali ni ya Mungu? Wengine wamehisi kwamba wao waweza kihalali kumpa Kaisari fedha kwa njia ya kulipa kodi bila jambo jingine la ziada. Hakika, wao hawangehisi vizuri kumpa Kaisari kitu chochote ambacho huenda kikachukua wakati ambao ungeweza kutumiwa katika utendaji mbalimbali wa kitheokrasi. Hata hivyo, ingawa ni kweli kwamba tunapaswa ‘kumpenda Yehova Mungu wetu kwa moyo wetu wote, na kwa nafsi yetu yote, na kwa akili zetu zote, na kwa nguvu zetu zote,’ Yehova hututarajia kutumia wakati katika kufanya mambo mengine zaidi ya utumishi wetu mtakatifu. (Marko 12:30; Wafilipi 3:3) Kwa kielelezo, Mkristo aliyefunga ndoa hushauriwa atumie wakati katika kumpendeza mwenzi wake wa ndoa. Utendaji huo si mbaya, lakini mtume Paulo asema kwamba hizo ni “mambo ya dunia” na si “mambo ya Bwana.”—1 Wakorintho 7:32-34; linganisha 1 Timotheo 5:8.
10 Zaidi, Kristo aliwaamuru wafuasi wake ‘kutoa’ kodi, na kwa hakika hiyo yahusisha kutumia wakati uliowekwa wakfu kwa Yehova—kwa kuwa maisha zetu zote zimewekwa wakfu kwake. Ikiwa wastani wa kodi katika nchi ni asilimia 33 ya mapato (ni juu zaidi katika nchi nyinginezo), hiyo yamaanisha kwamba kila mwaka mfanyakazi wa kawaida hulipa Hazina ya Serikali fedha zinazolingana na mapato yake ya miezi minne. Kwa maneno mengine, mwishoni mwa maisha yake ya kufanya kazi, mfanyakazi wa kawaida atakuwa ametumia karibu miaka 15 akichuma fedha za kodi ambazo “Kaisari” anataka. Fikiria vilevile suala la shule. Katika nchi zilizo nyingi sheria hutaka kwamba wazazi wapeleke watoto wao shuleni kwa muda wa miaka kadhaa. Miaka ya kwenda shuleni hutofautiana nchi kwa nchi. Katika sehemu zilizo nyingi takwa ni kusoma muda mrefu. Ni kweli kwamba kwenda shuleni kwa kawaida kunanufaisha, lakini ni Kaisari anayeamua ni sehemu gani ya maisha ya mtoto ambayo ni lazima itumiwe hivyo, na wazazi Wakristo hukubaliana na uamuzi wa Kaisari.
Utumishi wa Kijeshi wa Lazima
11, 12. (a) Kaisari hudai nini katika nchi nyingi? (b) Wakristo wa mapema walionaje utumishi wa kijeshi?
11 Dai jingine la Kaisari katika nchi fulani ni utumishi wa kijeshi wa lazima. Katika karne ya 20, mpango huu umeanzishwa na mataifa yaliyo mengi katika nyakati za vita na mataifa mengine katika nyakati za amani vilevile. Katika Ufaransa, wajibu huu uliitwa kwa miaka mingi kodi ya damu, ikimaanisha kwamba kila mwanamume kijana alipaswa kuwa tayari kudhabihu uhai wake kwa ajili ya Serikali. Je, hili ni jambo ambalo wale ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova waweza kufanya kwa kudhamiria? Wakristo wa karne ya kwanza walionaje jambo hili?
12 Ingawa Wakristo wa mapema zaidi walijaribu kuwa raia wema, imani yao iliwazuia wasiue mwingine au kutoa uhai wao wenyewe ukiwa dhabihu kwa ajili ya Serikali. The Encyclopedia of Religion yasema: “Mababa wa mapema wa kanisa, kutia ndani Tertullian na Origen, walithibitisha kwamba Wakristo walizuiwa kutoa uhai wa binadamu, kanuni iliyowazuia wasishiriki katika jeshi la Roma.” Katika kitabu chake The Early Church and the World, Profesa C. J. Cadoux aandika: “Angalau kufikia wakati wa utawala wa Marcus Aurelius [161-180 W.K.], hakuna Mkristo ambaye angekuwa mwanajeshi baada ya kubatizwa.”
13. Kwa nini walio wengi katika Jumuiya ya Wakristo hawaoni utumishi wa kijeshi kama Wakristo wa mapema walivyouona?
13 Kwa nini washiriki wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo hawaoni mambo kwa njia hiyo leo? Kwa sababu ya badiliko kubwa lililotukia katika karne ya nne. Kichapo cha Katoliki A History of the Christian Councils chaeleza: “Wakristo wengi, . . . chini ya maliki wapagani, walikataa kwa sababu za kidini utumishi wa kijeshi, na walikataa katakata kuwa wanajeshi, au walitoroka jeshi. Sinodi [ya Arles, iliyofanywa katika 314 W.K.], ikifikiria mabadiliko yaliyofanywa na Konstantino, iliweka wajibu wa kwamba ni lazima Wakristo watumikie katika vita, . . . kwa sababu Kanisa lina amani (in pace) [na serikali] chini ya mkuu aliye rafiki ya Wakristo.” Kwa sababu ya kuacha mafundisho ya Yesu, tangu wakati huo mpaka sasa, makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wametia moyo makundi yao kutumikia katika majeshi ya mataifa, ingawa watu fulani mmoja-mmoja wamechukua msimamo wakiwa wakataaji-kidhamira.
14, 15. (a) Ni kwa misingi gani Wakristo katika sehemu fulani hudai achilio la kutofanya utumishi wa kijeshi? (b) Mahali ambapo hakuna achilio la kutofanya utumishi wa kijeshi, ni kanuni zipi za Kimaandiko zitakazosaidia Mkristo afanye maamuzi yaliyo sahihi kwa habari ya utumishi wa kijeshi?
14 Je, Wakristo leo wana wajibu wa kufuata umati katika jambo hili? La. Ikiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa anaishi katika nchi ambako wahudumu wa dini huachiliwa wasifanye utumishi wa kijeshi, yeye anaweza kutumia uandalizi huo, kwa kuwa kwa hakika yeye ni mhudumu. (2 Timotheo 4:5) Nchi kadhaa, kutia ndani Marekani na Australia, zimetoa achilio hilo hata wakati wa vita. Na wakati wa amani, katika nchi nyingi zinazodumu kulazimisha utumishi wa kijeshi, Mashahidi wa Yehova, wakiwa wahudumu wa dini, huachiliwa wasifanye utumishi wa kijeshi. Kwa njia hiyo, wao waweza kuendelea kusaidia watu kwa utumishi wao wa umma.
15 Lakini, vipi ikiwa Mkristo aishi katika nchi ambayo achilio halitolewi kwa wahudumu wa dini la kutofanya utumishi wa kijeshi? Basi atapaswa kufanya uamuzi wa kibinafsi kulingana na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. (Wagalatia 6:5) Huku akifikiria mamlaka ya Kaisari, yeye atapima kwa uangalifu anachowiwa na Yehova. (Zaburi 36:9; 116:12-14; Matendo 17:28) Mkristo atakumbuka kwamba ishara ya Mkristo wa kweli ni upendo kwa waamini wote wenzake, hata wale wanaoishi katika nchi nyinginezo au wa makabila mengine. (Yohana 13:34, 35; 1 Petro 2:17) Na zaidi, yeye hatasahau kanuni za Kimaandiko zinazopatikana katika maandiko kama vile Isaya 2:2-4; Mathayo 26:52; Warumi 12:18; 14:19; 2 Wakorintho 10:4; na Waebrania 12:14.
Utumishi wa Kiraia
16. Katika nchi nyinginezo, ni utumishi gani usio wa kijeshi ambao Kaisari hudai wale wanaokataa utumishi wa kijeshi wafanye?
16 Hata hivyo kuna nchi ambazo ingawa Serikali haiachilii wahudumu wa dini wasifanye utumishi wa kijeshi, hata hivyo yatambua kwamba kuna watu mmoja-mmoja ambao huenda wakakataa utumishi wa kijeshi. Nyingi za nchi hizo hufanya uandalizi kwa wakataaji hao wa kidhamira ili wasilazimishwe kufanya utumishi wa kijeshi. Katika sehemu fulani utumishi wa kiraia utakikanao, kama vile kazi yenye kufaidi jumuiya, huonwa kuwa utumishi wa kitaifa usio wa kijeshi. Je, Mkristo aliyejiweka wakfu aweza kufanya utumishi kama huo? Hapa tena, ni lazima Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa afanye uamuzi wake mwenyewe kulingana na msingi wa dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.
17. Je, kuna kielelezo cha Kibiblia cha utumishi wa kiraia usio wa kijeshi?
17 Yaonekana kwamba utumishi wa lazima ulifanywa katika nyakati za Biblia. Kitabu kimoja cha historia chasema: “Kwa kuongezea kodi na ushuru zilizotozwa kwa raia wa Yudea, kulikuwa pia na kazi ngumu ya lazima [kazi ambayo mamlaka za umma hulazimisha mtu kufanya bila malipo]. Hilo lilikuwa zoea la kale katika Mashariki, ambalo mamlaka za Kigiriki na Kiroma ziliendelea kudumisha. . . . Agano Jipya, pia, lataja vielelezo vya kazi ngumu ya lazima katika Yudea, jambo linaloonyesha jinsi zoea hilo lilivyokuwa limeenea. Kwa kupatana na desturi hiyo, wanajeshi walimlazimisha Simoni Mkirene abebe msalaba [mti wa mateso] wa Yesu (Mathayo 5:41; 27:32; Marko 15:21; Luka 23:26).”
18. Ni aina zipi za utumishi wa kijumuiya usio wa kijeshi wala usio wa kidini ambazo Mashahidi wa Yehova mara nyingi hushiriki kufanya?
18 Vivyo hivyo, raia katika nchi fulani leo hutakiwa na Serikali au mamlaka za mitaa kushiriki katika aina mbalimbali za utumishi wa jumuiya. Nyakati nyingine hiyo ni kufanya kazi fulani hususa, kama vile kuchimba visima au kujenga barabara; nyakati nyingine hiyo hufanywa kwa ukawaida, kama vile kushiriki kila juma katika kufagia barabara, kusafisha shule au hospitali. Mahali ambapo utumishi kama huo wa kiraia ni kwa manufaa ya jumuiya nao hauhusiki na dini isiyo ya kweli au kwa njia nyingine haupingi dhamiri za Mashahidi wa Yehova, mara nyingi wamekubali. (1 Petro 2:13-15) Mara nyingi hili limetokeza ushahidi bora na nyakati nyingine kunyamazisha wale ambao hushtaki Mashahidi isivyo kweli kuwa wapinga-serikali.—Linganisha Mathayo 10:18.
19. Mkristo anapaswa kushughulikiaje jambo Kaisari akimwambia afanye kazi ya utumishi wa kitaifa usio wa kijeshi kwa kipindi cha wakati fulani?
19 Lakini, namna gani ikiwa Serikali inataka Mkristo afanye kwa kipindi fulani utumishi wa kiraia ambao ni sehemu ya utumishi wa kitaifa ulio chini ya usimamizi wa serikali? Hapa tena ni lazima Wakristo wafanye uamuzi wao wenyewe kwa kutegemea dhamiri iliyoarifiwa. “Sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.” (Warumi 14:10) Wakristo wanaokabiliwa na takwa la Kaisari wanapaswa kulichunguza hilo kwa sala na kulitafakari.a Inaweza kuwa jambo la hekima pia kulizungumza hilo jambo pamoja na Wakristo wakomavu kutanikoni. Baada ya kufanya hivyo ni lazima uamuzi wa kibinafsi ufanywe.—Mithali 2:1-5; Wafilipi 4:5.
20. Ni maswali gani na kanuni zipi za Kimaandiko ambazo husaidia Mkristo kusababu juu ya suala la utumishi wa kiraia wa kitaifa usio wa kijeshi?
20 Wanapofanya utafiti huo, Wakristo wangetaka kufikiria kanuni kadhaa za Biblia. Paulo alisema kwamba ni lazima ‘tunyenyekee kwa wenye uwezo na mamlaka na kuwa tayari kwa kila kazi njema, tuwe wema, tukionyesha upole wote kwa watu wote.’ (Tito 3:1, 2) Wakati uo huo, Wakristo wangefanya vyema kuchunguza kazi ya kiraia wanayotakiwa kufanya. Wakikubali kuifanya, je, wataweza kudumisha kutokuwamo kwao kwa Kikristo? (Mika 4:3, 5; Yohana 17:16) Je, hiyo ingewahusisha na dini fulani isiyo ya kweli? (Ufunuo 18:4, 20, 21) Je, kufanya kazi hiyo kungewazuia au kuwawekea mipaka isivyofaa kwa kutimiza madaraka yao ya Kikristo? (Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25) Kwa upande mwingine, je, wataendelea kufanya maendeleo ya kiroho, labda hata kushiriki katika huduma ya wakati wote huku wakifanya utumishi wanaotakiwa kufanya?—Waebrania 6:11, 12.
21. Uwe ni uamuzi gani anaofanya Mkristo, kutaniko lapaswa kumwonaje ndugu anayefanya utumishi wa kiraia wa kitaifa usio wa kijeshi?
21 Namna gani ikiwa majibu yenye haki ya Mkristo kwa maswali hayo yamfanya aamue kwamba utumishi wa kiraia wa kitaifa ni “kazi njema” anayoweza kufanya kwa kutii mamlaka? Huo ni uamuzi wake mbele ya Yehova. Wazee waliowekwa rasmi na wengine wanapaswa kustahi kabisa dhamiri ya huyo ndugu na kuendelea kumwona kuwa Mkristo mwenye msimamo mzuri. Hata hivyo, Mkristo akihisi kwamba hawezi kufanya utumishi huu wa kiraia, msimamo wake vilevile wapaswa kustahiwa. Yeye pia ataendelea kuwa na msimamo mzuri naye anapaswa kupokea utegemezo wenye upendo.—1 Wakorintho 10:29; 2 Wakorintho 1:24; 1 Petro 3:16.
22. Hata tukabiliwe na hali gani, tutaendelea kufanya nini?
22 Tukiwa Wakristo hatutakoma kumtolea “atakaye heshima, heshima hiyo.” (Waroma 13:7, NW) Tutastahi utaratibu mzuri na kutaka kuwa raia wenye amani, wanaotii sheria. (Zaburi 34:14) Hata tunaweza kuombea “wafalme na wote wenye mamlaka” watu hawa wanapohitaji kufanya maamuzi yanayoathiri maisha na kazi yetu ya Kikristo. Kwa sababu ya kumpa Kaisari yaliyo ya Kaisari, twatumaini kwamba ‘tutaishi maisha ya utulivu na amani.’ (1 Timotheo 2:1, 2) Zaidi ya yote, tutaendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme ukiwa ndio tumaini pekee la wanadamu, kwa kudhamiria tukimpa Mungu yaliyo ya Mungu.
-