-
Ukurasa wa Kichwa/Ukurasa wa WachapishajiJe, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Ukurasa wa Kichwa/Ukurasa wa Wachapishaji
Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
Chapa ya 2012
Broshua hii haiuzwi. Ni sehemu ya kazi ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote inayotegemezwa kwa michango ya hiari.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko ya Kiebrania ni kutoka katika Union Version ya Kiswahili chapa ya 1994, manukuu ya Maandiko ya Kigiriki ni kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mahali ambapo herufi NW zinafuata nukuu, zaonyesha kwamba tafsiri inatoka New World Translation of the Holy Scriptures-With References ya Kiingereza.
-
-
YaliyomoJe, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Yaliyomo
4 1 Je, Dini Zote Hufundisha Kweli?
5 2 Unawezaje Kujifunza Kweli Kumhusu Mungu?
8 3 Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?
12 4 Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?
15 5 Ukweli Kuhusu Uchawi na Ulozi
19 6 Je, Mungu Huzikubali Cini Zote?
22 7 Ni Nani Wanaofuata Dini ya Kweli?
-
-
Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
MUNGU MWEZA YOTE ndiye Bwana wa ulimwengu wote. Uhai wetu wa sasa na wa wakati ujao unamtegemea. Ana uwezo wa kuthawabisha na uwezo wa kuadhibu. Ana uwezo wa kutupatia uhai na uwezo wa kuuondoa uhai. Tukipata kibali chake, tutafaidika; lakini tukikosa kibali chake, tutapatwa na mabaya. Basi, ni muhimu kama nini kwamba ibada yetu ikubalike kwake!
Watu huabudu katika njia mbalimbali. Ikiwa dini ni kama barabara, je, barabara zote za kidini zinakubaliwa na Mungu? La, sivyo. Yesu, nabii wa Mungu, alionyesha kwamba kuna barabara mbili tu. Alisema: “Ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.
Kuna dini aina mbili tu: moja inayoongoza watu kwenye uhai na nyingine inayowaongoza kwenye uharibifu. Kusudi la broshua hii ni kukusaidia uitambue barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele.
-
-
Je, Dini Zote Hufundisha Kweli?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 1
Je, Dini Zote Hufundisha Kweli?
1. Ni zipi baadhi ya dini zinazofuatwa barani Afrika?
KARIBU kila mtu barani Afrika anakubali kwamba ni muhimu kumwabudu Mungu. Lakini watu hawakubaliani juu ya jinsi ya kumwabudu. Baadhi yao huabudu misikitini, huku wengine wakiabudu kwenye sehemu za kuabudia za kiasili. Wengine huenda kanisani. Lakini ni makosa kufikiri kwamba kuna dini tatu tu barani Afrika. Waislamu wana sheria na imani zinazotofautiana. Dini za kiasili hutofautiana sana katika sehemu mbalimbali. Kuna migawanyiko mikubwa hata zaidi kati ya makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo. Kotekote barani Afrika, kuna makanisa mengi madogo-madogo ambayo yamejitenga na yale makanisa makubwa.
Dini Yetu Inapaswa Kutegemea Kweli
2. (a) Kwa kawaida ni nini kinachoamua dini ya mtu? (b) Ni mambo gani ambayo hayathibitishi kwamba dini yetu inampendeza Mungu?
2 Ni nini kinachoamua jinsi watu watakavyoabudu? Watu wengi hukubali dini ya wazazi wao. Matukio ya kale pia huamua dini ambayo watu wanafuata leo. Kitabu The Africans—A Triple Heritage chasema: “Uislamu ulienea kaskazini mwa Sahara kupitia uvamizi, . . . nao Ukristo ukaenea kusini mwa Sahara kwa njia hiyohiyo. Uislamu ulienezwa kaskazini mwa Sahara kwa upanga, nao Ukristo ukaenezwa kusini mwa Sahara kwa bunduki.” Hata hivyo, wengi wetu huamini kwamba dini yetu inampendeza Mungu. Lakini dini haiwezi kuwa ya kweli kwa sababu tu wazazi wetu wanaifuata au kwa sababu wazazi wetu wa kale walilazimishwa na taifa fulani la kigeni waifuate.
3-5. Ni mfano gani unaotusaidia kuona kwamba si dini zote zinazofundisha kweli?
3 Ingawa dini zote hudai kwamba zina mwongozo wenye kutegemeka kuhusu kumtumikia Mungu, mafundisho ya dini hizo hutofautiana. Dini hufundisha mambo mengi yanayotofautiana kumhusu Mungu na mambo anayotaka tufanye. Hebu fikiria mfano huu: Tuseme umepata kazi katika kampuni fulani kubwa. Unapoenda kazini siku ya kwanza, unaelezwa kwamba mkubwa wa kampuni ameenda likizo. Hivyo unawauliza wafanyakazi watatu unachopaswa kufanya. Mfanyakazi wa kwanza anakuambia kwamba mkubwa anataka ufagie sakafu. Wa pili anakuambia kwamba unapaswa kupaka jengo rangi. Naye watatu anakuambia uwapelekee watu barua.
4 Kisha unawauliza wafanyakazi hao kuhusu mkubwa wa kampuni hiyo. Wa kwanza anakuambia kwamba mkubwa huyo ni kijana mrefu na mkali. Wa pili anakuambia kwamba yeye ni mzee mfupi na mwenye fadhili. Watatu anakuambia kwamba mkubwa huyo si mwanamume bali ni mwanamke. Yaelekea utaamua kwamba wafanyakazi wote watatu hawasemi kweli. Ikiwa unataka kuendelea kufanya kazi katika kampuni hiyo, yaelekea utafanya uchunguzi fulani ili kumjua vizuri mkubwa huyo na yale anayotaka ufanye.
5 Dini ziko hivyo. Kwa kuwa kuna mafundisho mengi sana kumhusu Mungu na mambo anayotaka tufanye, tunapaswa kuhakikisha kwamba ibada yetu inapatana na kweli. Lakini tunawezaje kujifunza kweli kumhusu Mungu?
-
-
Unawezaje Kujifunza Kweli Kumhusu Mungu?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 2
Unawezaje Kujifunza Kweli Kumhusu Mungu?
1, 2. Ni mfano gani unaoonyesha uhitaji wa kuwa na njia fulani ya kuamua mambo ya kidini?
TUNAWEZA kumjuaje Mungu? Je, ni lazima tuchunguze mafundisho yote ya dini mbalimbali? Hiyo haiwezekani. Na hata kama inawezekana, tungejuaje mafundisho ya kweli?
2 Bila shaka, kwa kuwa kuna mafundisho mbalimbali kumhusu Mungu, tunahitaji njia ya kujua ukweli wa mambo, njia ambayo itakubaliwa na kila mtu. Kwa mfano: Tuseme kuna ubishi sokoni kuhusu urefu wa kitambaa fulani. Muuzaji anasema kwamba kitambaa hicho kina urefu wa meta tatu, lakini mnunuzi anasema kwamba kitambaa hicho hakifiki meta tatu. Ubishi huo unaweza kutatuliwaje? Kwa kupima urefu wa kitambaa hicho kwa utepe wa kupimia.
3. Kwa nini Biblia iliandikwa?
3 Je, kuna utepe wa kupimia, yaani, njia fulani tunayoweza kutumia kuamua mambo ya kidini? Ndiyo, tunaweza kutumia Biblia. Mungu aliagiza Biblia iandikwe ili watu kila mahali wajifunze kweli kumhusu yeye. Biblia imechapwa kwa wingi sana. Nayo imetafsiriwa, kwa sehemu au yote nzima, katika lugha zaidi ya 2,100. Karibu kila mtu anaweza kusoma kweli kumhusu Mungu katika lugha yake mwenyewe.
4. Biblia ina habari gani?
4 Biblia ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Inaeleza mambo ambayo hatungeweza kuyajua kutokana na chanzo kingine. Inaeleza juu ya viumbe wanaoishi katika makao ya roho. Inafunua mawazo ya Mungu, utu wake, na kusudi lake. Inaeleza kuhusu jinsi alivyoshughulika na watu kwa maelfu ya miaka. Inataja mambo yatakayotukia wakati ujao. Nayo inaonyesha jinsi ambavyo tunaweza kupata barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele.
Kwa Nini Uiamini Biblia?
5. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Biblia inapatana na sayansi?
5 Kuna sababu nyingi zinazoweza kutufanya tuamini kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu. Sababu moja ni kwamba Biblia inapatana na sayansi. Zamani za kale, watu ulimwenguni pote walifikiri kwamba dunia ilikuwa imeshikiliwa na kitu fulani. Kwa mfano, zamani watu huko Afrika Magharibi waliamini kwamba dunia imeshikiliwa na nyoka aliyejikunja, akiwa amejikunja mara 3,500 juu ya dunia na mara 3,500 chini ya dunia. Hata hivyo, kupatana na sayansi, mwandishi mmoja wa Biblia aliandika zaidi ya miaka 3,500 iliyopita kwamba Mungu ‘anautundika ulimwengu pasipo kitu.’—Ayubu 26:7.
6. Ni uthibitisho gani mkubwa zaidi unaoonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha Mungu?
6 Uthibitisho mkubwa zaidi unaoonyesha kwamba kwa kweli Biblia ni kitabu cha Mungu ni kutimizwa kikamili kwa utabiri wake kuhusu wakati ujao. Tofauti na watu wanaofanya uaguzi, kwa kweli Mungu anajua wakati ujao. Kila jambo analosema hutimia.
7. Ni unabii gani wa Biblia ambao ulitimizwa wakati uliopita?
7 Unabii mwingi sana wa Biblia ulitimizwa zamani. Kwa mfano, miaka 700 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, Biblia ilisema kwa usahihi kwamba yeye angezaliwa katika mji wa Bethlehemu, na ikawa hivyo. (Mika 5:2; Mathayo 2:3-9) Mbali na unabii mwingine mwingi kumhusu Yesu, Biblia pia ilitabiri kwamba angezaliwa na bikira na mwishowe angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha. Unabii huo pia ulitimia. Bila shaka, hakuna mwanadamu ambaye angeweza kutabiri mambo hayo!—Isaya 7:14; Zekaria 11:12, 13; Mathayo 1:22, 23; 27:3-5.
8. Ni unabii gani wa Biblia unaotimizwa leo, nao unathibitisha nini?
8 Unabii mwingi wa Biblia unatimizwa leo. Hebu ona mifano michache:
● “Taifa litainuka dhidi ya taifa [katika vita], na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya dunia, na katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza na upungufu wa chakula.”—Luka 21:10, 11.
● Kutakuwa na ‘ongezeko la uasi-sheria.’—Mathayo 24:12.
● “Katika siku za mwisho . . . watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, . . . wasiotii wazazi, . . . wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, . . . wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.”—2 Timotheo 3:1-5.
Je, hukubali kwamba mambo haya yanatukia leo? Ukweli na usahihi wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba Biblia ni kitabu cha pekee, Neno la Mungu lililopuliziwa!—2 Timotheo 3:16.
Je, Biblia Imebadilishwa?
9, 10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu hakuwaruhusu watu waibadili Biblia?
9 Tuseme una kiwanda na kwamba umeandika sheria ambazo wafanyakazi wako wanapaswa kufuata. Ikiwa adui fulani angebadili sheria hizo, ungefanya nini? Je, hungerekebisha sheria zilizobadilishwa? Vivyo hivyo, Mungu hawaruhusu watu wabadili kweli ya Neno lake, Biblia.
10 Wale ambao wamejaribu kubadili mafundisho ya Neno la Mungu hawakufaulu. Tunapolinganisha Biblia tuliyo nayo sasa na nakala za Biblia za zamani, tunaona kwamba zinafanana. Jambo hilo linaonyesha kwamba katika miaka mingi ambayo imepita, Biblia haikubadilishwa.
Mapokeo ya Kusimuliwa—Je, Yanategemeka?
Dini za kiasili za Waafrika hazina vitabu vitakatifu vya zamani. Mapokeo, desturi, na imani kumhusu Mungu husimuliwa kutoka kizazi hadi kingine. Kitabu West African Traditional Religion kinasema: “Huenda habari zinazosimuliwa zisiwe sahihi. Mara nyingi, mambo fulani huongezwa au kuondolewa katika habari hizo, nazo hubadilishwa au kupotoshwa, hutiwa chumvi au zinakuwa zenye kutatanisha hivi kwamba mara nyingi ni vigumu kutofautisha kweli na habari za kubuniwa.”
Sanduku: Kitabu kimoja kinasema nini kuhusu kutegemeka kwa mapokeo?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]
Mother and starving child: © Giacomo Pirozzi/Panos Pictures
-
-
Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 3
Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?
1. Dini ya kiasili imelinganishwaje na mlima?
IMANI za kiasili za Waafrika zimelinganishwa na mlima. Juu kabisa kuna Mungu, ambaye ana nguvu nyingi zaidi za kiroho. Chini kidogo kuna miungu au roho wengine wadogo, ambao ni watumishi wa Mungu. Chini yao kuna wazazi wa kale waliokufa, ambao huzikumbuka familia zao duniani na kuzisaidia. Chini kabisa kuna roho wenye nguvu kidogo: wachawi, waaguzi, na walozi.
2. Msemo mmoja wa Kiafrika unaonyeshaje kwamba imani za kiasili huathiri dini?
2 Imani hizo za kiasili zimeathiri sana dini nyingine barani Afrika. Msemo mmoja wa Kiafrika unasema: “Kufuata Dini (ya Kikristo au Kiislamu) hakutuzuii kuabudu miungu yetu.”
3. Ni wapi tunapoweza kujifunza kweli kuhusu viumbe wanaoishi katika makao ya roho?
3 Je, imani za kiasili za Kiafrika zina ukweli gani? Biblia hutuambia kweli kuhusu viumbe wanaoishi katika makao ya roho.
Yehova, Mungu wa Kweli
4. Dini zilizo kubwa barani Afrika zinakubali nini?
4 Dini tatu kubwa barani Afrika hukubali kwamba kuna Mungu na kwamba yeye ndiye mkuu kuliko wote. Biblia husema kuwa yeye ndiye “Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu [“mwenye uwezo,” NW], mwenye kuogofya.” (Kumbukumbu la Torati 10:17) Waislamu pia wanaamini kuna Mungu mmoja aliye mkuu kuliko wote. Kuhusu dini za kiasili za Afrika, Profesa Geoffrey Parrinder anasema: “Waafrika wengi wamekuwa wakiamini kwamba kuna Mungu mkuu kuliko wote, baba wa miungu na wanadamu, muumba wa ulimwengu wote.”
5. Ni baadhi ya majina gani yanayotumiwa kumwita Mungu?
5 Hata hivyo, ingawa kila mahali watu wanamwamini Mungu, watu wengi hawamjui vizuri. Hatua ya kwanza ya kumjua mtu ni kulijua jina lake. Katika dini mbalimbali, watu hawaelewani kuhusu jina la Mungu. Kwa kawaida, Jumuiya ya Wakristo humwita Mungu, jina la cheo linalomaanisha “Mwenye Uwezo.” Waislamu wanamwita Allah. Majina ambayo wafuasi wa dini za kiasili humwita Aliye Mkuu Kuliko Wote hutofautiana kulingana na lugha zao. Katika kitabu chake, Concepts of God in Africa, John S. Mbiti anaorodhesha majina zaidi ya 500 ya Kiafrika ambayo yamepewa Mungu. Kwa mfano, katika Kiyoruba (Nigeria), Mungu anaitwa Olodumare; Wakikuyu (Kenya) humwita Ngai; nao Wazulu (Afrika Kusini) humwita Unkulunkulu.
6, 7. Jina la Mungu ni nani, na tunajuaje hivyo?
6 Mungu mwenyewe anasema jina lake ni nani? Mungu alipomwagiza Musa awaongoze Waisraeli kutoka Misri, Musa aliuliza: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?”—Kutoka 3:13.
7 Mungu alimwambia: “Mimi ni YEHOVA; nami nilimtokea Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao.” (Kutoka 6:2, 3) Jina hilo linapatikana zaidi ya mara 7,000 katika Biblia, ingawa tafsiri fulani za Biblia zimeliondoa na badala yake zimetumia majina ya cheo kama “Mungu” au “Bwana.”
8. Yehova ni Mungu wa aina gani, nasi lazima tufanye nini iwapo tunataka kibali chake?
8 Yehova ni Mungu wa aina gani? Yeye ni roho, mweza yote, na mtukufu. Yeye ni mkuu kuliko wote, hakuna anayelingana naye wala aliye sawa na yeye. (Kumbukumbu la Torati 6:4; Isaya 44:6) Yehova alimwambia Musa hivi: “Mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [“anayesisitiza ujitoaji usiohusisha wengine,” NW].” Yaani, ili kupata kibali cha Yehova, ni lazima tumwabudu yeye peke yake. Hataki tuabudu kitu kingine chochote au mtu mwingine yeyote.—Kutoka 20:3-5.
Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu
9. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yesu si sawa na Yehova?
9 Leo watu wengi hawamjui Yesu vizuri. Wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanaamini kwamba Yesu ni sehemu ya Utatu “Mtakatifu.” Lakini Biblia haifundishi kwamba Mungu ni watu watatu katika mmoja. Wala haifundishi kwamba Yesu ni sawa na Yehova. Yesu mwenyewe alisema: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.”—Yohana 14:28.
10. Yesu alikuwa wapi kabla ya kuja duniani?
10 Biblia hufundisha kwamba kabla ya kuishi duniani akiwa mwanadamu, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo. Yehova aliumba Adamu na Hawa duniani na pia akaumba viumbe wa roho mbinguni. Yesu ndiye kiumbe wa roho wa kwanza kuumbwa na Yehova.—Yohana 17:5; Wakolosai 1:15.
11. Yesu alizaliwa akiwa mwanadamu jinsi gani?
11 Miaka ipatayo 2,000 iliyopita, Yehova alihamisha uhai wa kiumbe huyu wa roho hadi katika tumbo la uzazi la bikira aitwaye Maria. Malaika Gabrieli alimwambia: “Utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu. Naye atatawala akiwa mfalme . . . , na hakutakuwa na mwisho wa ufalme wake.”—Luka 1:31, 33.a
12. Sababu moja iliyofanya Yesu aje duniani ni nini?
12 Hivyo Yesu alizaliwa, akakua akawa mtu mzima, na kuwafundisha watu mapenzi na kusudi la Yehova. Alimwambia hivi gavana mmoja Mroma: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Kwa kufikiria yale aliyofundisha Yesu, tunaweza kujifunza kweli kuhusu mapenzi na kusudi la Mungu. Tunaweza kujifunza jinsi ya kupata kibali cha Mungu.
13. Ni nini sababu ya pili iliyofanya Yesu aje duniani?
13 Sababu ya pili iliyofanya Yesu aje duniani ni kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mathayo 20:28) Alifanya hivyo ili tuwekwe huru na dhambi tuliyorithi kutoka kwa babu yetu Adamu. Jambo hilo nalo linatuwezesha kuishi milele. Mtume Yohana aliandika: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.
14. (a) Ni jambo gani lililompata Yesu baada ya kufa akiwa mwanadamu? (b) Sasa Yesu ana cheo gani mbinguni?
14 Baada ya kifo chake akiwa mwanadamu, Yesu alifufuliwa na kwenda mbinguni, ambako alianza tena kuishi akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu. (Matendo 2:32, 33) Baadaye, Yehova alimpa “mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:13, 14) Yesu amefanywa kuwa Mfalme mwenye uwezo; yeye ni Mfalme wa serikali ya mbinguni ya Yehova. Hivi karibuni ataonyesha uwezo wake katika dunia yote.
Malaika, Wahudumu wa Mungu
15. Malaika waliumbwa wakati gani na wapi?
15 Mbali na Yehova na Yesu, kuna viumbe wengine wanaoishi katika makao ya roho. Yehova aliumba viumbe wengine wa roho wanaoitwa malaika. Gabrieli aliyezungumza na Maria ni mmoja wao. Malaika hawakuanza maisha yao wakiwa wanadamu duniani. Waliumbwa huko mbinguni muda mrefu kabla ya wanadamu kuumbwa duniani. (Ayubu 38:4-7) Kuna mamilioni ya malaika.—Danieli 7:10.
16. Kwa nini wanadamu hawapaswi kuabudu malaika?
16 Malaika waaminifu hawataki tuwaabudu. Mtume Yohana alijaribu mara mbili kuabudu malaika, lakini wakamkemea, wakisema: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! . . . Abudu Mungu.”—Ufunuo 19:10; 22:8, 9.
17. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba malaika wanaweza kuwalinda watumishi wa Mungu, na kwa nini jambo hilo linafariji?
17 Malaika hawawatokei tena watu wa Mungu duniani, kama walivyofanya walipowakomboa mitume wa Yesu kutoka gerezani. (Matendo 5:18, 19) Hata hivyo, tukimwabudu Yehova kupatana na Neno lake, Biblia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tutalindwa na malaika zake wenye nguvu na wasioonekana. Biblia inasema: “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.” (Zaburi 34:7; 91:11) Kwa nini jambo hilo litufariji? Kwa sababu kuna maadui hatari katika ulimwengu wa roho wanaotaka kutuangamiza!
Shetani, Adui wa Mungu
18. (a) Kwa nini malaika mmoja alimwasi Mungu? (b) Malaika huyo mwasi alipewa majina gani?
18 Malaika wengine wa Mungu walikosa kuwa waaminifu kwake. Malaika hao walimwasi Mungu, wakawa maadui wake na wa watu wake duniani. Jambo hilo lilitokeaje? Malaika wote ambao Yehova aliumba walikuwa waadilifu na wema. Hata hivyo, mmoja wa wana hao wakamilifu wa roho alitaka watu wamwabudu naye akatenda kupatana na tamaa hiyo mbaya. Roho huyo mwovu alipewa jina Shetani, linalomaanisha “Mpinzani [wa Mungu].” Anaitwa pia Ibilisi, jina linalomaanisha “Mchongezi,” kwa kuwa yeye husema uwongo mbaya sana kumhusu Yehova.
19. Kwa nini Shetani alimtesa Yobu, naye alifanyaje hivyo?
19 Shetani huwakaza watu wajiunge naye katika kumwasi Mungu. Ona yale aliyomfanyia Yobu mtumishi mwaminifu wa Mungu. Yobu alikuwa tajiri sana. Alikuwa na kondoo 7,000, ngamia 3,000, ng’ombe-jike na ng’ombe-dume 1,000, na punda-jike 500. Alikuwa pia na watoto kumi na watumishi wengi. Kwanza, Shetani aliua mifugo ya Yobu na watumishi wake. Kisha akatokeza “upepo wenye nguvu” ulioharibu nyumba na kusababisha vifo vya watoto wote wa Yobu. Baadaye, Shetani alimtesa Yobu kwa “majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.”—Ayubu 1:3-19; 2:7.
20. (a) Yobu alithawabishwaje kwa uaminifu wake? (b) Ingawa Yobu alikuwa mwaminifu kwa Mungu, Shetani amewafanyaje watu wengine wengi?
20 Licha ya jaribu hilo kali, Yobu aliendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu. Kwa hiyo Yehova alimponya na ‘kumpa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza.’ (Ayubu 42:10) Shetani alishindwa kuvunja uaminifu wa Yobu, lakini amefaulu kuwafanya watu wengine wengi wamwache Mungu. Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.”—1 Yohana 5:19.
21. (a) Shetani alionyeshaje tamaa yake ya kutaka kuabudiwa? (b) Kwa nini Yesu alikataa kumwabudu Shetani?
21 Shetani hutaka sisi tumwabudu. Alionyesha jambo hilo waziwazi wakati alipomjaribu Yesu miaka 2,000 hivi iliyopita. Biblia inasimulia: “Ibilisi akamchukua [Yesu] kwenda pamoja naye kwenye mlima ulioinuka juu isivyo kawaida, na kumwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo, naye akamwambia: ‘Hakika nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.’” Yesu alikataa na kusema: “Enda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.’” (Mathayo 4:8-10) Yesu alijua sheria ya Yehova vizuri, naye alikataa kumwabudu Shetani.
Roho Waovu
22. Roho waovu wamewatendea wanadamu nini?
22 Malaika wengine walijiunga na Shetani katika kumwasi Mungu. Malaika hao waovu ni maadui wa watu duniani. Ni wakatili sana. Zamani walifanya watu fulani kuwa bubu na vipofu. (Mathayo 9:32, 33; 12:22) Waliwafanya wengine kuwa wagonjwa au watende kana kwamba wamerukwa na akili. (Mathayo 17:15, 18; Marko 5:2-5) Hata waliwatesa watoto.—Luka 9:42.
23. (a) Roho waovu wanataka wanadamu wafanye nini? (b) Shetani na roho waovu wamedanganya watu wafanye nini?
23 Kama Shetani, roho hao waovu pia hutaka kuabudiwa. Badala ya kukataa kuabudiwa na wanadamu na hivyo kuonyesha wanatambua kwamba Mungu pekee ndiye anayestahili kuabudiwa, wao wanatamani sana ibada hiyo, wanaitafuta, na kuiendeleza. Shetani na roho waovu hutumia udanganyifu, uwongo, na hofu ili kuwafanya watu wawaabudu. Bila shaka, si watu wengi wanaojua kwamba wanamwabudu Shetani na roho wake waovu. Watu wengi wangeshangaa sana kujua kwamba dini yao humtukuza Shetani. Na hata Biblia inaonya: “Vitu ambavyo mataifa huvidhabihu huwa wavidhabihu kwa roho waovu, na si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20.
24. Ni mbinu gani ambayo Shetani hutumia kuwadanganya watu?
24 Njia moja ambayo Shetani na roho wake waovu hutumia kufanya watu wawaabudu ni kueneza imani zisizo za kweli kuhusu wafu. Na tuone Biblia hufundisha nini kuhusu wafu.
[Maelezo ya Chini]
a Qurani inataja kuzaliwa kwa Yesu kimuujiza kwenye Sura ya 19 (Mariamu). Inasema: “Tukampelekea [Mariamu] Muhuisha Sharia yetu (Jibrili)—akajimithilisha kwake (kwa sura ya) binadamu aliye kamili. (Mariamu) akasema: ‘Hakika mimi najikinga kwa (Mwenyezi Mungu) Mwingi wa rehema (Aniepushe) nawe. Ikiwa unamuogopa Mungu (basi ondoka nenda zako).’ (Malaika) akasema: ‘Hakika mimi ni Mjumbe wa Mola wako: ili nikupe mwana mtakatifu.’ Akasema: ‘Nitawezaje kupata mtoto, hali hajanigusa mwanamume (yoyote kwa njia halali) wala mimi si (mwanamke) mwenye kuzini.’ (Malaika) akasema: ‘Ni kama hivyo (unavyosema; lakini) Mola wako amesema: “Haya ni sahali Kwangu, na ili Tumfanye Muujiza kwa wanaadamu na rehema itokayo kwetu (ndiyo tumefanya hivi);” na hili ni jambo lililokwisha hukumiwa.’”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Malaika waaminifu hukataa kuabudiwa
-
-
Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 4
Wazazi Wetu wa Kale Wako Wapi?
1, 2. Watu wengi wanaamini nini kuhusu wazazi waliokufa?
WATU wengi sana barani Afrika wanaamini kwamba kifo si mwisho wa maisha bali ni badiliko tu linalomwezesha mtu kuendelea na maisha mahali pengine. Wengi wanafikiri kwamba wazazi wao wa kale walihama ulimwengu wenye kuonekana na kwenda ulimwengu usioonekana, yaani walihama ulimwengu wa wanadamu na kwenda ulimwengu wa roho.
2 Inaaminika kwamba wazazi hao wa kale, au roho zao, huhakikisha kwamba familia zao duniani wanaendelea kuishi na wana ufanisi. Kulingana na maoni hayo, roho za wazazi wa kale ni marafiki wao wenye nguvu nyingi, wanaoweza kuleta mavuno mazuri, kuleta hali njema, na kuwakinga wasipatwe na mabaya. Wazazi hao wa kale wakipuuzwa au kukasirishwa, inasemekana kwamba wanaweza kusababisha misiba kama vile ugonjwa, umaskini, na maafa.
3. Watu fulani huabudu wazazi wa kale jinsi gani?
3 Watu walio hai hufuata mila na desturi fulani ili kuwaheshimu na kudumisha uhusiano mzuri na roho za wazazi wa kale. Mambo hayo huonekana mara nyingi kwenye desturi za mazishi, kama vile kesha na sherehe zinazofanywa baada ya mazishi. Wazazi wa kale huabudiwa kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, kabla ya kunywa pombe, watu fulani humwaga kiasi kidogo chini kwa ajili ya wazazi wao wa kale. Pia, baada ya mlo kupikwa, chakula fulani huachwa katika nyungu ili wazazi hao waliokufa wakija wapate chakula.
4. Watu wengi huamini nini kuhusu nafsi?
4 Watu wengine huamini kwamba watu walio hai wana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Inasemekana kwamba mtu akiwa mzuri, nafsi yake huenda mbinguni au peponi, lakini mtu akiwa mbaya, inasemekana kwamba nafsi yake huhukumiwa kwenda motoni. Mara nyingi watu huchanganya fundisho hilo na mapokeo. Kwa mfano, nyakati nyingine matangazo ya vifo katika magazeti husema kwamba mtu “ameaga dunia” au “ameitwa.” Imani hizo zinatokana na lile fundisho kwamba nafsi, au roho, huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Biblia husema nini kuhusu jambo hilo?
Nafsi na Roho
5, 6. Nafsi ni nini kulingana na Biblia?
5 Biblia inaonyesha kwamba nafsi si kitu kilicho ndani ya mtu; nafsi ni mtu mwenyewe. Kwa mfano, Mungu alipomwumba Adamu, “mtu [huyo] akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Adamu hakupewa nafsi; yeye alikuwa nafsi, mtu kamili.
6 Hiyo ndiyo sababu Biblia fulani hutumia maneno “mwanadamu,” “kiumbe,” au “mtu” badala ya neno “nafsi,” ambalo lilitumiwa kutafsiri neno la lugha ya awali. Tunasoma kwamba nafsi zinaweza kuzaliwa. (Mwanzo 46:18) Watu wanaweza kula. (Mambo ya Walawi 7:20) Nafsi zinaweza kufunga. (Zaburi 35:13) Nafsi zinaweza kuzimika au kukamatwa. (Yona 2:7, Zaire Swahili Bible; Zaburi 7:5) Watu wanaweza kuibwa. (Kumbukumbu la Torati 24:7). Maneno “nafsi” na “mtu” yanamaanisha kitu kimoja.
7. Ni maandiko gani ya Biblia yanayoonyesha kwamba nafsi inaweza kufa?
7 Kwa kuwa nafsi ni mtu mwenyewe, mtu anapokufa, nafsi hufa pia. Andiko la Ezekieli 18:4 (ZSB) linasema: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” Pia, andiko la Matendo 3:23 linasema: “Kwa kweli, nafsi yoyote [au, mtu] isiyomsikiliza Nabii huyo itaangamizwa kabisa kutoka miongoni mwa watu.” Kwa hiyo nafsi si kitu kinachoendelea kuishi baada ya mwili kufa.
8. Roho iliyo ndani ya wanadamu ni nini?
8 Roho si sawa na nafsi. Roho ni nguvu ya uhai iliyo ndani ya wanadamu ambayo huwawezesha kutimiza shughuli za maisha. Roho ni kama umeme. Nguvu za umeme zinaweza kuzungusha upepeo au kufanya friji iwe baridi lakini umeme peke yake hauwezi kuzungusha hewa au kufanya vitu viwe baridi. Kwa njia hiyohiyo, roho yetu hutuwezesha kuona, kusikia, na kufikiri. Lakini roho peke yake haiwezi kufanya mambo hayo bila macho, masikio, au ubongo. Hiyo ndiyo sababu Biblia husema hivi kuhusu mwanadamu: “Pumzi [“roho,” NW] yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.
9. Ni nini ambacho nafsi na roho hazifanyi?
9 Kwa hiyo, kulingana na Biblia, nafsi na roho hazitoki mwilini mtu anapokufa na kuendelea kuishi katika makao ya roho.
Hali ya Wafu
10. Biblia inasema nini kuhusu hali ya wafu?
10 Hivyo, basi, wafu wako katika hali gani? Kwa kuwa Yehova ndiye aliyewaumba wanadamu, yeye pia anajua kile ambacho hutupata tunapokufa. Neno lake hufundisha kwamba wafu hawana uhai, hawawezi kusikia, kuona, kuongea, wala kufikiria chochote. Biblia inasema:
● “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5.
● “Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja.”—Mhubiri 9:6.
● “Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko [kaburini] uendako wewe.”—Mhubiri 9:10.
11. Baada ya Adamu kufanya dhambi, Yehova alimwambia nini?
11 Fikiria yale ambayo Biblia inasema kuhusu mzazi wetu wa kwanza, Adamu. Yehova alimwumba Adamu “kwa mavumbi ya ardhi.” (Mwanzo 2:7) Kama Adamu angalitii sheria ya Yehova, angaliishi milele kwa furaha duniani. Hata hivyo, Adamu alivunja sheria ya Yehova, na adhabu ikawa kifo. Adamu alienda wapi alipokufa? Mungu alimwambia: ‘Utairudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’—Mwanzo 3:19.
12. Ni nini kilichompata Adamu alipokufa?
12 Adamu alikuwa wapi kabla Yehova hajamwumba kutoka mavumbini? Hakuwapo. Kwa hiyo Yehova aliposema kwamba Adamu ‘angeirudia ardhi,’ Alimaanisha kwamba Adamu angerudi katika hali ya kukosa uhai kama vile mavumbi. Adamu hakuendelea kuishi katika ulimwengu wa roho. ‘Hakuiaga dunia’ kwenda katika makao ya roho ya wazazi wa kale. Hakuenda mbinguni wala motoni. Alirudi katika ile hali ya kutokuwa na uhai; hali ya kutokuwapo.
13. Ni nini huwapata wanadamu na wanyama wanapokufa?
13 Je, jambo hilo huwapata wanadamu kwa ujumla? Ndiyo. Biblia inaeleza: “[Wanadamu na wanyama] huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhubiri 3:19, 20.
14. Kuna tumaini gani kwa wafu?
14 Biblia inaahidi kwamba Mungu atawaamsha wafu waishi katika dunia paradiso. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Lakini jambo hilo litatukia wakati ujao. Wakati huu wafu wamelala usingizi wa kifo. (Yohana 11:11-14) Hatupaswi kuwaogopa wala kuwaabudu, kwa kuwa hawawezi kutusaidia wala kutudhuru.
15, 16. Shetani hujaribuje kufanya watu waamini kwamba wafu hawajakufa?
15 Fundisho kwamba hatufi ni uwongo ambao huenezwa na Shetani Ibilisi. Ili kuwafanya watu waamini uwongo huo, yeye na roho wake waovu hujaribu kuwadanganya watu waamini kwamba ugonjwa na matatizo mengine husababishwa na roho za wafu. Ni kweli kwamba matatizo fulani husababishwa na roho waovu. Pia ni kweli kwamba matatizo mengine hayasababishwi na roho waovu. Hata hivyo, si kweli kwamba wale wanaolala usingizi wa kifo wanaweza kutudhuru.
16 Kuna njia nyingine ambayo roho waovu hutumia kujaribu kuwadanganya watu wafikiri kwamba yale ambayo Biblia husema kuhusu kifo si kweli. Wao hudanganya watu wafikiri kwamba wameona wafu au kuongea nao. Roho waovu hufanya hivyo kupitia maono, ndoto, watu wanaowasiliana na roho, au njia nyinginezo. Hata hivyo, watu hawawasiliani na wafu, bali huwasiliana na roho waovu wanaojifanya kuwa watu waliokufa. Hiyo ndiyo sababu Yehova huwashutumu vikali watu ambao huwasiliana na roho na wale ambao hutafuta habari kutoka kwa wafu.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Zekaria 10:2.
Wafu Hawawezi Kutusaidia
Chifu mmoja maarufu wa Afrika Magharibi alikufa mwaka wa 1990. Alikuwa na wake watano na watoto wengi. Alikuwa anapata pesa nyingi sana kutokana na biashara zake mbili.
Chifu huyo alipokufa, watu wa familia yake walifuata mila za mazishi kwa makini, wakiamini kwamba kwa kufanya hivyo wanaiheshimu roho yake. Wake zake walivaa nguo nyeusi, wakaachilia nywele zao bila kuzichana, wakawa wanakula chakula kidogo, na hawakuoga. Walilia na kuomboleza kwa siku saba baada ya mazishi. Kisha, kupatana na desturi za huko, familia nzima ikakusanyika pamoja na watu wa ukoo katika sherehe ya kula, kunywa, na kucheza dansi ili kumalizia desturi za mazishi.
Kwa kweli, kama chifu huyo aliyekufa angekuwa na uwezo, angeilinda familia yake yenye upendo na kuibariki sana! Lakini hakufanya hivyo. Biashara zake zilifilisika. Watu wa familia yake waligombania mali aliyoacha na baadaye wakatengana. Sasa kumebaki watu wachache sana katika makao makubwa ya chifu huyo ambayo wakati mmoja yalijaa watu.
Wafu Hawawezi Kutudhuru
Katika kijiji fulani nchini Nigeria, mtu mmoja alikufa na kuzikwa. Baadaye, mke wake aliota kwamba mume wake alitaka saa yake. Aliamini ndoto hiyo, hivyo akachukua saa hiyo na kuifukia kando ya mwili wa mume wake.
Mwanamume kijana aitwaye Dunikan aliifukua saa hiyo kisiri na kuitumia miaka mingi hadi ikachakaa. Hakupatwa na jambo lolote baya. Kama mtu huyo aliyekufa angekuwa na uwezo juu ya watu walio hai, bila shaka angemwadhibu mwizi huyo aliyeiba saa yake kutoka kaburini!
Sanduku: Ni mambo gani yaliyoonwa ambayo yanayoonyesha kwamba wafu hawawezi kutusaidia wala kututendea mabaya?
-
-
Ukweli Kuhusu Uchawi na UloziJe, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 5
Ukweli Kuhusu Uchawi na Ulozi
1. Imani kwamba kuna uchawi na ulozi imeenea kadiri gani?
“BARANI Afrika, haina haja kuuliza kama kuna wachawi,” chasema kitabu African Traditional Religion, na kuendelea kusema kwamba “Waafrika wa hali zote huamini sana uchawi.” Watu wasio na elimu na hata wenye elimu ya juu huamini kwamba kuna uchawi na ulozi. Viongozi wa dini ya Kiislamu na wa Jumuiya ya Wakristo pia huamini kuna uchawi na ulozi.
2. Watu wengi wanaamini nguvu za uchawi hutoka wapi?
2 Watu wengi barani Afrika wanaamini kwamba kuna nguvu fulani ya kiroho yenye uwezo sana. Wanaamini kwamba Mungu anaidhibiti nguvu hiyo. Viumbe wa roho na wazazi wa kale wanaweza kuitumia. Na watu fulani pia wanajua jinsi ya kupata sehemu ya nguvu hiyo na kuitumia katika uchawi unaotoa ulinzi au uchawi unaodhuru.
3. Uchawi unaodhuru ni nini, na watu huamini unaweza kufanya nini?
3 Uchawi unaodhuru, hutumiwa kwa maadui. Inaaminika kwamba wale wanaoutumia wana nguvu za kutuma popo, ndege, nzi, na wanyama wengine wakashambulie watu. Watu wengi huamini kwamba uchawi husababisha mapigano, utasa, magonjwa, na hata kifo.
4. Watu wengi wanaamini nini kuhusu wachawi, nao wanatoa sababu gani ya kuamini hivyo?
4 Katika sehemu nyingi za Afrika, watu wengi wanaamini kwamba binadamu anaweza kubadilika au kubadilishwa na kuwa mnyama. Wengi wanaamini kuwa wachawi wana uwezo wa kubadilika kuwa chui au nyoka. Hali kadhalika, watu wengi huhofu kwamba mchawi anaweza kuwabadili watu wengine kuwa wanyama. Katika Afrika magharibi, inaaminiwa kwamba wachawi wanaweza kutuma roho za wanadamu kupitia ndege au wanyama wengine ili kuwadhuru watu wengine. Waafrika wengi huhisi kwamba mabadiliko hayo ya mtu kuwa mnyama yamethibitishwa na watu fulani waliojionea kwa macho. Wao hudai kwamba zile hadithi nyingi zinazosimuliwa na watu wenye akili timamu haziwezi kuwa mambo ya kukisia tu.
5. Uchawi unaoaminiwa kuleta ulinzi ni nini, nao hutumiwaje?
5 Uchawi unaoaminiwa kutoa ulinzi unasemekana kwamba hukinga mtu na mabaya. Wale wanaotumia uchawi huo huvaa pete au bangili za uchawi. Wao hunywa dawa fulani ya uchawi au kuipaka mwilini ili kujikinga. Nyumbani kwao au chini ya ardhi, wao huficha vitu ambavyo wanaamini vina nguvu za kuwalinda. Wanatumainia hirizi zenye maandiko ya Qurani au ya Biblia.
Uwongo na Udanganyifu
6. Shetani na roho wake waovu walifanya nini zamani, nasi tunapaswa kuzionaje nguvu zao?
6 Ni kweli kwamba Shetani na roho wake waovu ni maadui hatari wa wanadamu. Wana nguvu za kudhibiti akili na maisha ya watu, na zamani hata waliwapagaa wanadamu na wanyama. (Mathayo 12:43-45) Ingawa hatupaswi kupuuza nguvu zao, hatupaswi pia kuziona kuwa kubwa mno.
7. Shetani anataka tuamini nini, na ni mfano gani unaoonyesha jambo hilo?
7 Shetani ni mdanganyifu stadi. Yeye huwapumbaza watu wafikiri kwamba ana nguvu nyingi kuliko ilivyo kwa kweli. Kwa mfano: Wakati wa vita vya hivi karibuni katika nchi moja ya Afrika, askari-jeshi walitumia vikuza sauti ili kuwaogopesha maadui wao. Kabla ya kushambulia, askari hao walikuwa wakivumisha mlio mkubwa wa mizinga na bunduki uliokuwa umerekodiwa. Walitaka maadui wao wafikiri kwamba wanashambuliwa na jeshi lenye silaha nzito-nzito. Kwa njia hiyohiyo, Shetani hutaka watu waamini kwamba ana nguvu kubwa mno. Kusudi lake ni kuogopesha watu wasifanye mapenzi ya Yehova bali wafanye mapenzi yake. Na tuone aina tatu za uwongo ambao Shetani hutaka watu waamini.
8. Ni uwongo gani ambao Shetani huendeleza?
8 Uwongo mmoja ambao Shetani huendeleza ni huu: Hakuna jambo lolote baya linalotukia tu; kila jambo baya husababishwa na mtu fulani au na nguvu zisizo za kawaida. Kwa mfano, tuseme mtoto amekufa kwa ugonjwa wa malaria. Huenda mama yake anajua kwamba malaria ni ugonjwa ambao huenezwa na mbu. Lakini huenda pia akaamini kwamba mtu fulani alitumia uchawi kutuma mbu aje kumwuma mtoto wake.
9. Biblia inaonyeshaje kwamba Shetani hasababishi kila tatizo?
9 Ingawa Shetani ana nguvu za kusababisha matatizo fulani, ni kosa kuamini kwamba ana nguvu za kusababisha kila tatizo. Biblia inasema: “Si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Mkimbiaji mmoja anaweza kukimbia kwa kasi kushinda wengine, lakini asishinde. ‘Tukio fulani lisilotazamiwa’ linaweza kumfanya asishinde. Labda anajikwaa na kuanguka au anapatwa na tatizo la misuli. Mambo hayo yanaweza kumpata yeyote. Si lazima yawe yanasababishwa na Shetani au uchawi; yanatukia tu.
10. Ni nini ambacho husemwa kuwahusu wachawi, na tunajuaje kwamba huo ni uwongo?
10 Uwongo wa pili ambao Shetani huendeleza ni huu: Wachawi wanaweza kubadilika au kubadilishwa kuwa wanyama ili kuwadhuru wengine. Hebu jiulize: ‘Ikiwa wachawi wanaweza kufanya hivyo, ni nini hasa hutoka katika mwili na kuingia ndani ya mwili wa mnyama?’ Kama tulivyoona, roho si kitu kinachoweza kuuacha mwili wa mtu. Roho ni nguvu ya uhai ambayo huutia mwili nguvu lakini haiwezi kufanya chochote bila mwili. Kubadilika na kuwa mnyama ni kinyume cha sheria za maumbile zilizoanzishwa na Yehova Mungu. Bila shaka, Mungu hangepuuza sheria zake kwa kuwapa wanadamu uwezo wa kujibadili na kuwa wanyama wasio na akili.
11. Tunajuaje kwamba wachawi hawawezi kuiacha miili yao au kujibadili kuwa wanyama, na je, wewe unaamini hilo?
11 Roho haiwezi kuuacha mwili na kwenda kufanya jambo lolote baya au zuri. Hivyo, wachawi hawawezi kuiacha miili yao au kujibadili kuwa wanyama. Kwa kweli hawafanyi mambo wanayodai au wanayofikiri wamefanya.
12. Ni kwa njia gani Shetani huwafanya watu waamini kwamba wamefanya mambo ambayo hawakufanya?
12 Tunaweza kuelezaje mambo ambayo wale waliokuwa wachawi wanakiri kwamba walifanya? Shetani anaweza kufanya watu waamini kwamba wameona mambo ambayo hawakuona. Kupitia maono, Shetani anaweza kufanya watu wafikiri kwamba wameona, kusikia, au kufanya mambo ambayo hawakufanya. Kwa njia hiyo, Shetani anatarajia kugeuza watu wamwache Yehova na kuwafanya wafikiri kwamba Biblia si ya kweli.
13. (a) Je, uchawi unaoaminiwa kuleta ulinzi unafaa? (b) Biblia inasema nini kuhusu uchawi?
13 Uwongo wa tatu ni huu: Uchawi unaoaminiwa kutoa ulinzi unafaa kwa kuwa inaaminika kwamba unaweza kuumaliza nguvu ule uchawi unaodhuru. Biblia haitofautishi kati ya uchawi unaotoa ulinzi na uchawi unaodhuru. Inashutumu uchawi wa aina zote. Ona sheria ambazo Yehova alipatia taifa la Israeli kuhusu uchawi na wale wanaoutumia:
● ‘Msifanye uchawi.’—Mambo ya Walawi 19:26, Biblia Habari Njema.
● “Mtu mume au mtu mke aliye na pepo, au aliye mchawi, hakika atauawa.”—Mambo ya Walawi 20:27.
● “Asionekane kwako . . . mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-14.
14. Kwa nini Yehova alitunga sheria za kupinga uchawi?
14 Sheria hizo zinaonyesha wazi kwamba Mungu hakutaka watu wake wawe wachawi. Yehova aliwapa watu wake sheria hizo kwa sababu aliwapenda na hakutaka wawe watumwa wa woga na ushirikina. Hakutaka wakandamizwe na roho waovu.
15. Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova ana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani?
15 Ingawa Biblia haizungumzii kwa undani mambo ambayo roho waovu wanaweza kufanya na wasiyoweza kufanya, inaonyesha kwamba Yehova Mungu ana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani na roho wake waovu. Yehova alimfanya Shetani atupwe kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:9) Ona pia kwamba Shetani aliomba ruhusa ya kumjaribu Yobu naye alitii amri ya Mungu ya kutomwua Yobu.—Ayubu 2:4-6.
16. Tunapaswa kumtegemea nani atulinde?
16 Andiko la Mithali 18:10 linasema: “Jina la BWANA ni ngome imara; mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Hivyo tunapaswa kumtegemea Yehova atulinde. Watumishi wa Mungu hawategemei hirizi au dawa za uchawi ziwalinde dhidi ya matendo maovu ya Shetani na roho wake waovu, wala hawaogopi walozi. Watumishi wa Mungu huamini yale ambayo Biblia inasema: “Macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
17. Andiko la Yakobo 4:7 linatuhakikishia nini, lakini tunapaswa kufanya nini?
17 Wewe pia unaweza kuwa na uhakika huo ikiwa unamtumikia Yehova. Andiko la Yakobo 4:7 linasema: “Jitiisheni wenyewe kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia.” Ikiwa unamtumikia Mungu wa kweli na kujitiisha kwake, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakulinda.
Je, Wachawi Wanaweza Kudhibiti Radi?
Mapema mwaka wa 1977, wachawi 14 waliuawa kwa kuchomwa moto karibu na Pietersburg, Afrika Kusini. Gazeti la Drum la Afrika Kusini lilisema hivi kuhusu tukio hilo: “Wanaume na wanawake wameshikwa na woga. Wanaogopa kulogwa na kupigwa kwa radi . . .
“Ni lazima hatua fulani ichukuliwe . . . Kwa sababu hiyo, gazeti DRUM linawatolea wachawi wote mwito huu: Kuna pesa kiasi cha Randi 5 000 [sawa na dola 5,750 (za Marekani) wakati huo] kwenye ofisi zetu zitakazopewa yeyote ambaye katika mwezi wa Machi 1977, ataweza kumpiga na kumwua Stanley Motjuwadi kwa radi. Ikiwa hamwezi kufanya hivyo, basi acheni kila mtu ajue kwamba kule kujifanya kwamba mnaweza kudhibiti radi ni upumbavu na upuuzi mtupu.
“Kwa hiyo, enyi wachawi waongo, anzeni kujitayarisha. Mpigeni na kumwua Stanley Motjuwadi kwa radi ikiwa mnaweza.”
Je, wachawi hao waliweza kumpiga Stanley Motjuwadi kwa radi? Hapana, hawakuweza. Bw. Motjuwadi, mmoja wa waandishi wa Drum, hakufa bali alifanikiwa sana katika kazi yake na mwishowe akawa mhariri wa gazeti hilo.
Sanduku: Mwandishi mmoja nchini Afrika Kusini aliwatolea wachawi mwito gani, na matokeo yakawaje?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Wachawi hawawezi kujibadili kuwa wanyama
[Picha katika ukurasa wa 17]
Mara kwa mara, mambo mabaya hutokea tu
-
-
Je, Mungu Huzikubali Dini Zote?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 6
Je, Mungu Huzikubali Dini Zote?
1. Neno la Mungu linaonyesha kuna aina zipi mbili za dini?
YESU alisema, “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Neno la Mungu linaonyesha kwamba kuna aina mbili tu za dini: moja ya kweli, na nyingine isiyo ya kweli; moja inayofaa, na nyingine isiyofaa; moja inayoongoza kwenye uhai, na nyingine inayoongoza kwenye uharibifu.
2. Maandiko yanaonyeshaje kwamba Mungu hapendezwi na dini zote?
2 Watu wengine hufikiri kwamba Mungu hupendezwa na dini zote. Maandiko yafuatayo ya Biblia yanaonyesha kwamba hilo si kweli:
● “Wana wa Israeli walifanya tena yaliyo maovu mbele za macho ya BWANA, wakawatumikia Mabaali, na Maashtorethi, na miungu ya Shamu, na miungu ya Sidoni, na miungu ya Moabu, na miungu ya wana wa Amoni, na miungu ya Wafilisti; nao wakamwacha BWANA, wala hawakumtumikia yeye. Hasira za BWANA ziliwaka juu ya Israeli.” (Waamuzi 10:6, 7) Tukiabudu sanamu au miungu mingine yoyote isipokuwa Mungu wa kweli, hatutapata kibali cha Yehova.
● “Watu hawa huniheshimu mimi [Mungu] kwa midomo yao, bali mioyo yao imeondolewa mbali nami. Ni bure kwamba wao hufuliza kuniabudu, kwa sababu wao hufundisha amri za watu kuwa mafundisho.” (Marko 7:6, 7) Ikiwa watu wanaodai kumwabudu Mungu wanafundisha mawazo yao wenyewe badala ya kufundisha yaliyo katika Biblia, ibada yao ni ya bure. Haikubaliwi na Mungu.
● “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ni lazima ibada yetu ipatane na ukweli wa Neno la Mungu.
Matunda ya Dini Zisizo za Kweli
3. Unaweza kutumia njia gani moja kutofautisha dini ya kweli na isiyo ya kweli?
3 Tunaweza kujuaje kama dini inampendeza Mungu? Yesu alisema: “Kila mti mwema hutokeza matunda bora, lakini kila mti uliooza hutokeza matunda yasiyofaa kitu . . . Basi, kwa kweli kwa matunda yao mtawatambua watu hao.” Yaani, ikiwa dini imetokana na Mungu itazaa matunda mema; lakini ikiwa imetokana na Shetani, itazaa matunda mabaya. —Mathayo 7:15-20.
4. Waabudu wa Yehova huonyesha sifa gani?
4 Dini ya kweli hutokeza watu wanaopendana na wanaowapenda wengine. Hiyo ni kwa sababu Yehova mwenyewe ni Mungu mwenye upendo. Yesu alisema: “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” Je, dini zinatimiza takwa hilo la ibada ya kweli?—Yohana 13:35; Luka 10:27; 1 Yohana 4:8.
5. Ensaiklopedia moja inaelezaje biashara ya watumwa Waafrika?
5 Hebu fikiria biashara ya watumwa Waafrika. Kichapo The New Encyclopædia Britannica kinasema: “Kati ya mwaka wa 650 na 1905, Waafrika wapatao 18,000,000 walisafirishwa kupitia eneo la Waislamu la Sahara na Bahari ya Hindi kwenda kuuzwa kuwa watumwa. Kuanzia katikati ya karne ya 15 Wazungu kutoka Ulaya walianza kufanya biashara ya watumwa katika pwani ya Afrika magharibi, na kufikia mwaka wa 1867 Waafrika kati ya 7,000,000 na 10,000,000 walisafirishwa wakiwa watumwa kupelekwa Amerika Kaskazini na Kusini na visiwa vya Karibea.”
6. Dini ilihusikaje katika biashara ya watumwa?
6 Dini ilichukua msimamo gani wakati huo wa msukosuko barani Afrika ambapo wanaume, wanawake, na watoto walitenganishwa na familia zao, wakafungwa minyororo, wakatiwa alama kwa chuma chenye moto, na kununuliwa au kuuzwa kama ng’ombe? Bethwell Ogot anaandika hivi katika gazeti la Daily Nation la Nairobi, Kenya: “Wakristo na Waislamu wanafundisha kwamba wanadamu wanapaswa kuwa na umoja, lakini dini hizo mbili zilitokeza watu wenye ubaguzi wa rangi walioweka watumwa. Waislamu wa Mashariki ya Kati na vilevile Wakristo wa Magharibi wanapaswa kukiri kwamba wana hatia kwa sababu walishindwa kushutumu biashara ya watumwa na ubaguzi wa kijamii uliosababisha mateso makubwa kwa Waafrika kwa karne nyingi.”
Dini na Vita
7. Viongozi wa kidini wamehusikaje katika vita?
7 Dini isiyo ya kweli imeonyesha matunda yake yaliooza katika njia nyinginezo. Kwa mfano, ingawa Biblia husema, ‘mpende jirani yako,’ viongozi wa kidini kote ulimwenguni wameunga mkono vita na kuichochea kwa bidii.—Mathayo 22:39.
8. (a) Viongozi wa kidini walichocheaje mauaji katika vita barani Afrika? (b) Pasta mmoja alisema nini kuhusu viongozi wa kidini wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria?
8 Inajulikana vizuri kwamba katika mwaka wa 1994, watawa kadhaa wa kike na pia makasisi walishiriki kuua katika mauaji makubwa ya watu yaliyotokea Rwanda. Dini pia imehusika sana katika vita vingine barani Afrika. Kwa mfano, wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha umwagikaji mwingi wa damu nchini Nigeria, dini za pande zote mbili ziliwachochea watu wapigane. Vita hivyo vilipokuwa vikiendelea, pasta mmoja alisema kwamba viongozi wa makanisa “wameacha kazi ambayo Mungu aliwapa.” Pia alisema: “Sisi tunaojiita makasisi wa Mungu tumekuwa makasisi wa Shetani.”
9. Biblia inasema nini kuhusu wahudumu wa Shetani?
9 Biblia inasema vivyo hivyo: “Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru. Kwa hiyo si jambo kubwa ikiwa wahudumu wake pia wafuliza kujigeuza umbo wenyewe kuwa wahudumu wa uadilifu.” (2 Wakorintho 11:14, 15) Kama vile watu wengi waovu hujifanya kuwa watu wazuri, Shetani naye huwadanganya watu kupitia wahudumu wake ambao kazi zao ni mbovu na matunda yao yameoza ingawa wao huonekana kuwa waadilifu.
10. Viongozi wa kidini wamemkana Mungu jinsi gani?
10 Ulimwenguni pote, viongozi wa kidini wamehubiri upendo, amani, na wema, lakini wana chuki, wameshiriki katika vita, na hawamwogopi Mungu. Biblia huwafafanua vizuri inaposema: “Wao hutangaza hadharani wamjua Mungu, lakini wao humkana yeye kwa kazi zao.”—Tito 1:16.
Tokeni Katika “Babiloni Mkubwa”
11. Biblia inafafanuaje dini isiyo ya kweli?
11 Tunaweza kupata maoni ya Yehova kuhusu dini zisizo za kweli kwa kusoma kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Katika kitabu hicho, dini isiyo ya kweli inafafanuliwa kuwa mwanamke wa mfano ambaye anaitwa “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:5) Ona jinsi Mungu anavyomfafanua:
● “Kahaba mkubwa . . . ambaye wafalme wa dunia walifanya uasherati naye.” (Ufunuo 17:1, 2) Badala ya kuonyesha uaminifu kwa Mungu, dini isiyo ya kweli imejiingiza katika siasa na mara nyingi huambia serikali yale ambayo serikali hizo zinapaswa kufanya.
● “Katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Dini isiyo ya kweli imenyanyasa na kuua watumishi waaminifu wa Mungu na imesababisha vifo vya watu wengi sana vitani.
● “Alijitukuza mwenyewe na kuishi katika anasa isiyo na aibu.” (Ufunuo 18:7) Dini isiyo ya kweli ina mali nyingi sana ambazo viongozi wake hutumia kuishi maisha ya anasa.
● “Kwa zoea [lake] la kuwasiliana na roho mataifa yote yaliongozwa vibaya.” (Ufunuo 18:23) Kupitia fundisho lake lisilo la kweli kwamba nafsi haifi, dini isiyo ya kweli imewafanya watu wajiingize katika kila aina ya uwasiliani-roho na ulozi na imewafanya waogope wafu na kuabudu wazazi wa kale.
12. Biblia inatoa onyo gani kuhusu dini isiyo ya kweli?
12 Biblia inawaonya watu vikali wajitenge na dini isiyo ya kweli ikisema: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake.”—Ufunuo 18:4, 5.
13. Ni nini kitakachoipata dini isiyo ya kweli na wale wanaoifuata?
13 Hivi karibuni, Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, ataharibiwa kabisa. Biblia inasema: “Katika siku moja tauni zake zitakuja, kifo na kuomboleza na njaa kali, naye atachomwa kabisa kwa moto, kwa sababu Yehova Mungu, aliyemhukumu, ni mwenye nguvu.” (Ufunuo 18:8) Ili kuepuka “kupokea sehemu ya tauni zake,” tunapaswa kuvunja kabisa uhusiano wowote na dini isiyo ya kweli, na kuepuka kabisa mazoea, sherehe na mafundisho ambayo humchukiza Mungu. Tunapaswa kufanya hivyo haraka. Maisha yetu yamo hatarini!—2 Wakorintho 6:14-18.
[Picha katika ukurasa wa 20, 21]
Dini isiyo ya kweli imehusika katika vita na biashara ya watumwa
[Hisani]
Kuwabariki askari: Daily Times of Nigeria; mashua ya kubebea watumwa: Schomburg Center for Research in Black Culture/The New York Public Library/Astor, Lenox and Tilden Foundations
-
-
Ni Nani Wanaofuata Dini ya Kweli?Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 7
Ni Nani Wanaofuata Dini ya Kweli?
1. Ni lazima tufanye nini ili kumpendeza Mungu?
NI LAZIMA tuepuke kabisa dini isiyo ya kweli ili tuwe na uhusiano mzuri na wenye upendo pamoja Mungu. Ni lazima tufuate dini ya kweli. Leo mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanafanya hivyo.
2. Mashahidi wa Yehova wanaweza kupatikana wapi, na wanafanya kazi gani?
2 Kama Biblia ilivyotabiri, waabudu wa kweli wanafanyiza “umati mkubwa” ambao umetoka “katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:9) Katika nchi 235, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanawasaidia wengine wajifunze njia za upendo za Yehova na matakwa yake.
Kutambua Waabudu wa Kweli
3. Mashahidi wa Yehova humwabudu nani, nao huepuka ibada za aina gani?
3 Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba Yehova peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa. Wao hukataa kuinamia sanamu au picha za kidini. (1 Yohana 5:21) Hawaabudu wafu kwa kushiriki kesha au sherehe nyingine zinazoendeleza imani za dini isiyo ya kweli na “mafundisho ya roho waovu.” (1 Timotheo 4:1) Hata hivyo, wao huwafariji waliofiwa kwa kuwaeleza ahadi ya Mungu kwamba wafu watafufuliwa katika dunia paradiso.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.
4. Watu wa Mungu huuonaje uchawi?
4 Mashahidi wa Yehova huepuka uchawi na ulozi, kwa kuwa wanajua mambo hayo yanatokana na Ibilisi. Hawatumaini uchawi uwalinde bali wao humtumaini Yehova.—Mithali 18:10.
5. Ni katika njia gani Mashahidi wa Yehova “si sehemu ya ulimwengu”?
5 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16) Yesu mwenyewe alikataa kujihusisha na siasa katika siku zake. (Yohana 6:15) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa, utukuzo wa taifa, au kung’ang’ania vyeo katika ulimwengu huu. Hata hivyo, wao hulipa kodi na kutii sheria za nchi wanamoishi.—Yohana 15:19; Waroma 13:1, 7.
6. Watumishi wa Mungu hufuata maagizo gani kuhusu ndoa na talaka?
6 Kwa sababu Mashahidi wa Yehova hutii agizo la serikali, wao huhakikisha kwamba ndoa zao zimeandikishwa kisheria. (Tito 3:1) Wao hutii agizo la Mungu na hivyo hawaoi wake wengi. (1 Timotheo 3:2) Na zaidi, kwa sababu wanafuata kanuni za Mungu, inakuwa vigumu kutalikiana au ndoa zao kuvunjika.
7. Mashahidi huonyeshanaje upendo?
7 Mashahidi wa Yehova wanapendana. Upendo huo, pamoja na upendo wao kwa Mungu, huwaunganisha kuwa udugu wa kweli, ingawa wametoka katika makabila na mataifa mbalimbali. Kunapotokea msiba au uhitaji fulani, Mashahidi wa Yehova huchukua hatua mara moja na kusaidiana. Mashahidi huonyesha upendo kwa jinsi wanavyoishi.—Yohana 13:35.
8. Watu wa Mungu huepuka mazoea gani mabaya?
8 Watu wa Yehova hujitahidi sana kuishi kwa unyofu na kwa uaminifu. Wao huepuka wizi, uongo, ukosefu wa maadili, ulevi, na udanganyifu katika biashara. Waume hawawapigi wake zao. Kabla ya kuwa Mashahidi wa Yehova, baadhi yao walifanya mambo hayo, lakini kwa msaada wa Yehova wakaacha. ‘Walioshwa wakawa safi’ mbele za Mungu.—1 Wakorintho 6:9-11.
Watu Wanaofanya Mapenzi ya Mungu
9. Kitabu kimoja kilisema nini kuhusu dini za Kikristo zinazofuata tamaduni za Kiafrika?
9 Bila shaka, dini nyingi hudai kuwa za kweli. Huenda dini hizo zikataja kazi zenye nguvu ili kuthibitisha madai yao. Kwa mfano, kuhusiana na dini za Kikristo zinazofuata tamaduni za Kiafrika, kitabu fulani kinasema: “Kwa sehemu kubwa kazi ya wachawi imechukuliwa na [makundi mapya ya Kikristo]. . . . Wao hudai kwamba wanatabiri na kufanya miujiza. Manabii wao huona maono na kutafsiri ndoto. Wao hutumia maji matakatifu, mafuta matakatifu, majivu, mishumaa na uvumba ili kuponya na kuzuia magonjwa.”
10, 11. Kwa nini ile inayoitwa eti miujiza leo haionyeshi kwamba dini imekubaliwa na Mungu?
10 Wafuasi wa dini hizi hudai kwamba miujiza huthibitisha kwamba dini yao imekubaliwa na Mungu. Lakini hiyo inayoitwa eti miujiza haithibitishi kwamba dini imekubaliwa na Yehova. Shetani huwapa waabudu fulani wasio wa kweli nguvu za kufanya ‘kazi zenye nguvu.’ (2 Wathesalonike 2:9) Na zaidi ya hayo, Biblia ilitabiri kwamba zawadi za kimuujiza kutoka kwa Mungu, kama vile kutoa unabii, kuzungumza kwa lugha, na ujuzi wa kipekee, ‘zingeondolewa mbali.’—1 Wakorintho 13:8.
11 Yesu alionya: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbingu, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye katika mbingu ataingia. Wengi wataniambia katika siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya kazi nyingi zenye nguvu katika jina lako?’ Na bado ndipo hakika nitaungama kwao: Sikuwajua nyinyi kamwe! Ondokeni kwangu, nyinyi wafanyakazi wa uasi-sheria.”—Mathayo 7:21-23.
12. Ni nani watakaoingia katika Ufalme wa mbinguni?
12 Hivyo basi, ni nani watakaoingia katika Ufalme wa mbinguni? Ni wale wanaofanya mapenzi ya Yehova.
Wahubiri wa Ufalme wa Mungu
13. Mungu amewaagiza watu wake wafanye kazi gani leo, na ni nani wanaoifanya?
13 Mungu anataka watu wake wafanye nini leo? Yesu alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Hii ndiyo kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wanafanya kwa bidii.
14. Ufalme wa Mungu ni nini, na ni nani watakaotawala katika Ufalme huo?
14 Katika “dunia yote inayokaliwa,” Mashahidi wa Yehova hutangaza Ufalme wa Mungu kuwa serikali ya mbinguni ambayo itatawala dunia nzima kwa uadilifu. Wao hufundisha kwamba Yehova amemweka rasmi Kristo Yesu kuwa Mfalme wa Ufalme huo, pamoja na watawala wenzake 144,000 ambao wamechaguliwa kutoka kwa wanadamu.—Danieli 7:14, 18; Ufunuo 14:1, 4.
15. Ufalme huo utaharibu nini?
15 Mashahidi hutumia Biblia kuonyesha watu kwamba Ufalme wa Mungu utaharibu ulimwengu wote wa Shetani. Dini isiyo ya kweli pamoja na mafundisho yake yanayomvunjia Mungu heshima na kumtukuza Ibilisi itaondolewa kabisa! (Ufunuo 18:8) Serikali za kibinadamu ambazo humpinga Mungu zitaondolewa pia! —Danieli 2:44.
16. Ni nani watakaokuwa raia wa Kristo Yesu, nao wataishi wapi?
16 Na zaidi ya hayo, Mashahidi wa Yehova hujulisha watu kwamba Yesu Kristo atawaletea faida nyingi wale wanaofanya yale ambayo Mungu anataka. Watakuwa raia zake duniani. Biblia inaahidi: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.
17. Ni nani peke yao wanaotangaza Ufalme wa Mungu?
17 Hakuna kundi lingine la watu linalofanya mapenzi ya Mungu kwa kuhubiri habari njema za Ufalme. Mashahidi wa Yehova peke yao ndio hujulisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu duniani pote.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mashahidi wa Yehova wameungana kuwa udugu wa ulimwenguni pote
-
-
Kataa Dini Isiyo ya Kweli; Fuata Dini ya KweliJe, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 8
Kataa Dini Isiyo ya Kweli; Fuata Dini ya Kweli
1. Watu wapaswa kufanya uchaguzi gani leo kuhusu ibada?
YESU alisema: “Yeye asiyekuwa upande wangu yuko dhidi yangu.” (Mathayo 12:30) Tunakuwa ama upande wa Yehova ama upande wa Shetani. Watu wengi hufikiri kwamba wanamtumikia Mungu kwa njia inayokubalika, lakini Biblia inasema kwamba Shetani ‘anaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Mamilioni ya watu wanaamini kwamba wanamwabudu Mungu, lakini ukweli ni kwamba wanamtumikia Shetani Ibilisi! Leo ni lazima watu wachague kama watamtumikia Yehova, “Mungu wa kweli,” au Shetani, “baba ya uwongo.”—Zaburi 31:5; Yohana 8:44.
Toka Katika Dini Isiyo ya Kweli
2. Shetani hutumia njia gani kujaribu kuwazuia watu wasimwabudu Yehova?
2 Ni jambo la hekima kuchagua kumtumikia Yehova kwa sababu kufanya hivyo hufanya mtu akubaliwe naye. Lakini Shetani hampendi mtu yeyote anayemtumikia Mungu; yeye huwanyanyasa wale wanaomtumikia Mungu. Njia moja anayotumia ni dhihaka au upinzani kutoka kwa wengine, hata kutoka kwa marafiki na watu wa familia. Yesu alionya hivi: “Kwa kweli, maadui wa mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake mwenyewe.”—Mathayo 10:36.
3. Watu wa familia yenu au marafiki wakikupinga usimwabudu Mungu, utafanya nini?
3 Utafanya nini iwapo utapatwa na mambo hayo? Watu wengi husita kuacha dini yao hata ingawa wanajua si ya kweli. Wanaona kwamba kufanya hivyo ni kukosa uaminifu kwa familia zao. Je, kweli hayo ni maoni mazuri? Kama ungegundua kwamba wengine katika familia yenu wanatumia dawa za kulevya, je, hungewaonya kwamba dawa hizo zitawadhuru? Je, hungekataa kujiunga nao kutumia dawa hizo?
4. Yoshua aliwaambia nini Waisraeli kuhusu ibada katika siku zake?
4 Yoshua aliwatia moyo Waisraeli waache matendo na mapokeo ya kidini ya mababu zao ambayo hayakufaa. Alisema: “Sasa mcheni BWANA, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng’ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye BWANA.” (Yoshua 24:14) Yehova alimbariki Yoshua kwa sababu alikuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake. Yehova atatubariki pia ikiwa tutakuwa waaminifu kwake.—2 Samweli 22:26.
Haribu Vitu Vinavyotumiwa Katika Ibada Isiyo ya Kweli
5. Kwa nini tunapaswa kuharibu vitu vya uchawi?
5 Kutoka katika dini isiyo ya kweli pia kunatia ndani kuharibu vitu vyovyote vya uchawi ambavyo huenda tukawa navyo, kama vile hirizi, pete za uchawi, bangili za uchawi, na kadhalika. Jambo hilo ni muhimu kwa sababu linaonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kabisa.
6. Wakristo wa mapema walifanya nini na vitabu vyao vya uchawi?
6 Ona jinsi Wakristo fulani wa mapema walivyofanya walipoamua kufuata dini ya kweli. Biblia inasema: “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa kimzungu wakaleta pamoja vitabu vyao wakavichoma kabisa mbele ya kila mtu.”—Matendo 19:19.
7. Tunaweza kufanya nini roho waovu wakitusumbua?
7 Huenda watu fulani wanaoanza kumtumikia Yehova na ambao walihusika na ulozi au uchawi wakasumbuliwa na roho waovu. Roho hao wakikusumbua, sali kwa Yehova ukitaja jina lake kwa sauti kubwa. Atakusaidia.—Mithali 18:10; Yakobo 4:7.
8. Wakristo huzionaje sanamu, mifano, na picha zinazotumiwa katika ibada isiyo ya kweli?
8 Wale wanaotaka kumtumikia Yehova hawapaswi kuweka au kutumia sanamu, mfano, au picha yoyote inayohusiana na ibada isiyo ya kweli. Wakristo wa kweli ‘wanatembea kwa imani, si kwa kuona.’ (2 Wakorintho 5:7) Wanaheshimu sheria ya Mungu inayokataza kutumia mfano wowote katika ibada.—Kutoka 20:4, 5.
Shirikiana na Watu wa Yehova
9. Biblia inatoa ushauri gani kuhusu kupata hekima?
9 Biblia inasema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima.” (Mithali 13:20) Tukitaka kuwa na hekima, tunahitaji kutembea, au kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hao ndio watu wanaotembea katika barabara inayoongoza kwenye uhai.—Mathayo 7:14.
10. Mashahidi wa Yehova wanaweza kukusaidiaje umtumikie Mungu?
10 Mashahidi wa Yehova hujali watu kikweli. Kazi yao ni kusaidia watu wenye mioyo minyofu waelewe kweli za Biblia zinazoongoza kwenye uhai wa milele. Wanaweza kukusaidia ujifunze Biblia bila malipo. Watajibu maswali yako na kukuonyesha jinsi ya kutumia ujuzi wa Biblia maishani mwako.—Yohana 17:3.
11. Mikutano ya Kikristo itakusaidiaje?
11 Kwenye mikutano yao, ambayo kwa ukawaida hufanywa kwenye Majumba ya Ufalme, utajifunza mengi kuhusu njia za Yehova. Tamaa yako ya kufuata dini ya kweli itachochewa. Utazoezwa pia jinsi ya kuwasaidia wengine wajifunze kweli za Biblia.—Waebrania 10:24, 25.
12. Sala inaweza kukusaidiaje umtumikie Mungu?
12 Unapoendelea kujifunza mengi juu ya mapenzi na kusudi la Mungu, inaelekea utathamini zaidi njia zake zenye upendo. Unapaswa pia kuzidisha tamaa yako ya kufanya mambo yanayompendeza na kuepuka yale yasiyompendeza. Kumbuka kwamba unaweza kusali kwa Yehova na kumwomba akusaidie kufanya mambo yanayofaa na kuepuka yale yasiyofaa.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wafilipi 4:6.
13. Unaweza kufurahishaje moyo wa Yehova?
13 Unapoendelea kukua kiroho, inaelekea utaona uhitaji wa kujiweka wakfu, na kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Utaufurahisha moyo wa Yehova kwa kujiunga na watu wake. (Mithali 27:11) Utakuwa kati ya watu wenye furaha ambao Mungu anasema hivi kuwahusu: “Mimi nitakaa miongoni mwao na kutembea miongoni mwao, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”—2 Wakorintho 6:16.
Mafundisho ya Kidini—Ya Kweli na Yasiyo ya Kweli
● Utatu: Dini nyingi hufundisha kwamba Mungu ni Utatu. Zinasema kwamba “Baba ni Mungu, Mwana [Yesu] ni Mungu, na Roho Takatifu ni Mungu, na hata hivyo, hawa si Miungu watatu bali ni Mungu mmoja.”
Biblia hata haitaji neno “Utatu,” wala haifundishi kwamba Yehova ni watu watatu katika mmoja. Yehova peke yake ndiye Mungu. Andiko la 1 Wakorintho 8:6 lasema: “Kwa kweli kwetu kuna Mungu mmoja Baba.” Yehova ndiye Mkuu Kuliko Wote. Yesu si Mungu, bali yeye ni “Mwana wa Mungu.” (1 Yohana 4:15) Vivyo hivyo, roho takatifu si Mungu wala hata si mtu. Hiyo ni nguvu ya Mungu ya utendaji.—Matendo 1:8; Waefeso 5:18.
● Nafsi: Dini nyingi hufundisha kwamba nafsi ni kitu fulani ndani ya mtu ambacho hakiwezi kufa. Biblia hufundisha kwamba nafsi ni mtu na hapana shaka mtu anaweza kufa.—Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4, ZSB.
● Moto wa Mateso: Dini zisizo za kweli hufundisha kwamba nafsi za waovu huteswa milele katika moto. Biblia husema kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Biblia pia hufundisha kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Yehova, Mungu mwenye upendo, hawezi kutesa watu kwa moto.
[Swali ya Funzo]
Sanduku: Biblia hufundisha nini kuhusu Utatu, nafsi, na moto wa mateso?
Niliacha Kushirikiana na Roho Waovu
Usiku mmoja nilipokuwa nimelala usingizi pamoja na mume wangu, nilisikia sauti ikiniita kwa jina mara tatu. Kisha nikaona dari likipasuka, na kitu kama mpira unaowaka moto, kikaniangukia tumboni. Mume wangu hata hakuona mambo hayo. Kwa miezi kadhaa, nilihisi joto kali.
Miezi sita baadaye, ile sauti iliniita tena. Mara, nyumba nzima ikaonekana kana kwamba imo ndani ya maji mengi. Nyoka mkubwa alitoka katika yale maji na kujiviringisha kwenye mkono wangu. Nilijaribu bila mafanikio kumwondoa nyoka huyo kwa kutikisa mkono. Niliogopa sana. Kisha yale maji na yule nyoka akatoweka, nami nikaangushwa chini kwa kishindo. Nilipoteza fahamu kwa muda wa saa kadhaa. Kisha ile sauti ikaniambia nirudi kwenye hekalu moja kijijini la watu waliokuwa wakiponya kwa kuwasiliana na roho. Nilipomwuliza roho huyo anaitwaje, alinipa jina lililomaanisha “utakuwa tajiri lakini hutapata mtoto.” Aliahidi kunitajirisha kwa kunipa nguvu za kuponya.
Wagonjwa kutoka mbali na karibu walikuja kwangu. Kabla hawajafika nyumbani kwangu, ningewaona katika kioo changu cha pekee. Kisha mtu alipofika, ningepiga mkono wake kwa mkono wangu nami ningefunuliwa mara moja tatizo au ugonjwa wake pamoja na tiba yake. Roho huyo pia aliniambia kiasi cha pesa ambacho watu wangepaswa kulipa.
Nilipata pesa na zawadi nyingi sana kutoka kwa watu nilioponya. Nikawa “tajiri,” lakini pia nikajua maana ya maneno “hutapata mtoto.” Kila wakati nilipozaa mtoto, yule aliyemtangulia alikufa. Jambo hili lilinihuzunisha sana. Katika miaka 12 niliyotumikia roho huyo, sita kati ya watoto wangu walikufa.
Nilianza kusali kwa bidii ili Mungu anisaidie. Siku moja Mashahidi wa Yehova walinitembelea na ingawa kwa kawaida nilikuwa nikiwafukuza, siku hiyo niliamua kuwasikiliza. Tulipokuwa tunazungumza, niligundua kwamba nilikuwa nikimtumikia roho mwovu! Niliamua kuacha kuwasiliana na roho.
Nilipomwambia roho huyo uamuzi wangu, alinionya nisifanye uamuzi huo. Hata hivyo, nilimwambia, “Uhusiano wangu na wewe umekwisha.”
Nilichoma vitu vyote nilivyotumia katika uaguzi. Nikajifunza Biblia na wale Mashahidi, nikawa mtumishi wa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1973. Sasa nina watoto watano wenye afya. Mume wangu pia alibatizwa na kuwa Shahidi.”—Imesimuliwa na Josephine Ikezu.
Sanduku: Mwanamke mmoja aliachaje kushirikiana na roho waovu?
[Picha katika ukurasa wa 26]
Unaweza kufuataje dini ya kweli?
-
-
Dini ya Kweli Inaweza Kukufaidi Milele!Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
-
-
Sehemu ya 9
Dini ya Kweli Inaweza Kukufaidi Milele!
1. Itakuwaje ‘tukimkaribia Mungu’?
YEHOVA anawapenda wale wanaomtumikia, nawe ukimwabudu, yeye atakubariki sasa na wakati ujao. Biblia inasema: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.”—Yakobo 4:8.
2. Tunaweza kumkaribiaje Mungu, na jambo hilo litakuwa na matokeo gani kwa sala zetu?
2 Ili kumkaribia Mungu ni lazima ujifunze na kutumia Neno lake. Yehova atasikiliza sala zako na kuzijibu ukisali kupatana na mapenzi yake. Mtume Mkristo Yohana aliandika: “Huu ndio uhakika ambao tunao kumwelekea yeye [Mungu], kwamba, hata iwe ni nini ambacho twaomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia. Zaidi, ikiwa twajua yeye hutusikia kwa habari ya chochote kile tunachoomba, twajua tutakuwa na mambo yaliyoombwa kwa kuwa tumeyaomba kwake.”—1 Yohana 5:14, 15.
3-7. Tunaweza kupataje hekima ya Mungu, nayo inaweza kutusaidiaje?
3 Zaidi ya hayo, unapomkaribia Mungu, atakupatia hekima ya kushughulika na mambo yanayotokea kila siku maishani. Biblia inasema: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, acheni afulize kumwomba Mungu.”—Yakobo 1:5.
4 Hekima ya Mungu inaweza kukusaidiaje? Kwanza, inaweza kukusaidia kujua mambo yasiyompendeza Yehova. Unaweza pia kujua ni kwa nini mambo hayo ni mabaya na utafanya nini ili kuyaepuka. Ujuzi huo unaweza kukulinda usipatwe na matatizo mengi yanayowasumbua watu kwa jumla. Kwa mfano, kutii ushauri wa Mungu wa kuwa safi kiadili huwasaidia watu wake wasipate mimba haramu, magonjwa yanayoambukizwa kingono, na kuepuka kuvunjika kwa ndoa au ndoa zisizo na furaha.
5 Hekima ya Mungu inaweza kukusaidia katika njia gani nyingine? Hekima hiyo inaweza kukusaidia kupata faida kamili maishani. Inaweza kukusaidia ufanye maamuzi ya busara kuhusu mambo fulani, kama vile kutumia vizuri pesa zako. Utaweza kufuatia miradi inayofaa na kuacha ile isiyo na faida ya kudumu.
6 Hekima ya Mungu pia inaweza kukusaidia katika mahusiano yako na wengine. Maisha yako ya familia yanaweza kuwa yenye furaha zaidi. Unaweza kuwa na urafiki wa kweli na wenye kudumu pamoja na wengine na hata kuheshimiwa na wale wasiomtumikia Mungu.
7 Na zaidi ya hayo, kuwa na hekima ya Mungu kutaboresha maoni yako kuhusu maisha. Itakusaidia kukabiliana na matatizo na mambo yanayovunja moyo maishani. Pia, utakuwa na maoni yanayofaa na yenye usawaziko kuhusu wakati ujao. Maoni yanayofaa yatakusaidia uwe na afya njema kiakili na kimwili.—Mithali 14:30; Isaya 48:17.
8. Ukimtumikia Mungu, ni mambo gani ambayo hutaogopa?
8 Ukimtumikia Mungu wa kweli, hutakuwa na woga ambao huwasumbua wale wasiomtumikia. Hutawaogopa wafu kwa sababu unajua kwamba waliokufa wako makaburini na hawawezi kufanya lolote. Hutaogopa kufa kwa kuwa una uhakika na ahadi ya Mungu ya kuwafufua wafu. Na kwa kuwa unajua kwamba Mungu ni mwenye nguvu zote, hutaogopa uchawi au ulozi.—Yohana 8:32.
Wenye Haki Watairithi Dunia
9-11. Ni nani watakaoishi katika Paradiso, na ni nani ambao hawataishi humo?
9 Ukimkaribia Mungu, hutaogopa wakati ujao. Kama tulivyoona, Biblia ilitabiri mengi ya matatizo tunayoona duniani leo. Yehova anatuambia kwamba mambo hayo ni ya muda tu; hivi karibuni Ufalme wa Mungu utafanya dunia hii kuwa paradiso.—Luka 21:10, 11, 31; 23:43.
10 Wale wanaomkaribia Yehova na kumtumikia ndio tu watakaoishi katika Paradiso. Biblia inasema: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo. Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
11 Wale wanaokataa kwa ukaidi kutii sheria za uadilifu za Mungu wataangamia milele. (2 Wathesalonike 1:8, 9) Hawatakuwapo tena. Wataangamia pamoja na Shetani na roho wake waovu katika kifo cha milele. (Ufunuo 20:10, 14) Lakini wale wanaojifunza kumhusu Yehova na kumtumikia watafurahia kuishi katika Paradiso duniani.
Wakati Ujao Mzuri Sana!
12. Biblia inasema nini kuhusu wakati ujao?
12 Yehova atawafanyia mambo mazuri sana wale wanaompenda! Hebu ona yale ambayo Neno lake linasema kuhusu maisha katika dunia Paradiso:
● Chakula kingi: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.
● Nyumba nzuri: “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake.”—Isaya 65:21.
● Kazi yenye kufurahisha: “Wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:22, 23.
● Hakuna magonjwa: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
● Hakuna ulemavu: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
● Hakuna maumivu, maombolezo, kifo: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.
● Hakuna vita: “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:9.
● Uhai wa milele: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.
13. Ni nani peke yake anayeweza kufanya dunia hii kuwa paradiso, na kwa nini?
13 Wanadamu hawawezi kutimiza mambo hayo, lakini Yehova ana uwezo wa kufanya lolote analosema. Hakuna kinachoweza kumzuia asifanye kile anachotaka kufanya. Biblia inasema: “Kwa Mungu hakuna tangazo lolote litakalokuwa lisilowezekana.”—Luka 1:37.
14. Unaweza kutembeaje katika barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele?
14 Kupitia Mashahidi wake, Yehova anawatolea watu kila mahali nafasi ya ‘kuingia kupitia lango jembamba’ na kutembea katika barabara inayoongoza kwenye uhai wa milele. Na uwe kati ya watu wenye furaha wanaokubali mwaliko huo. Na ufuate dini ya kweli na kufurahia baraka za Yehova milele!—Mathayo 7:13, 14.
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 31]
-