Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Samoa
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • MAENDELEO NCHINI SAMOA YA MAREKANI

      Kabla ya muda wa akina Sellars kukaa nchini Samoa kumalizika katika mwaka wa 1954, Ron aliamua kutuma maombi yao ya kuwa wakazi nchini Samoa ya Marekani badala ya kurudi Australia. Ron anaandika: “Nilipozungumza na mwanasheria mkuu wa Samoa ya Marekani na kumweleza kwamba serikali ya Samoa ilikuwa imekataa maombi yetu kwa sababu za kidini, aliniambia, ‘Bwana Sellars, tuna uhuru wa kidini nchini Samoa ya Marekani, nitafanya juu chini mpaka mpate vibali hivyo.’”

      Ron na Dolly waliwasili mji wa Pago Pago, nchini Samoa ya Marekani mnamo Januari 5, 1954. Mwanasheria huyo aliwapa vibali vya kuingia kwa sharti moja, kwamba Ron awe akiripoti ofisini kwake mara kwa mara na kumweleza mengi zaidi kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Hivyo, wakawa na mazungumzo mengi mazuri ya Biblia.

      Baadaye mwezi huo, mwanasheria huyo aliwaalika Ron na Dolly nyumbani kwake kwa ajili ya chakula. Kwa kuwa padri wa Katoliki na padri wa London Missionary Society walikuwa wamealikwa pia, kukawa na mazungumzo ya Biblia yenye kusisimua. Ron anakumbuka: “Tulipokaribia kuondoka, mwanasheria huyo alitushukuru sote kwa kufika na kusema, ‘Nafikiri Bwana na Bibi Sellars ndio washindi katika mazungumzo yetu leo.’ Muda si muda, tukapata vibali vyetu vya kuwa wakazi wa kudumu. Mwanasheria mkuu aliponijulisha baadaye kwamba serikali ingekubali maombi zaidi ya wamishonari Mashahidi nchini, niliijulisha ofisi ya tawi ya Australia bila kukawia.”

      Ualesi (Wallace) Pedro, Mtokelau mwenye umri wa miaka 19, ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza nchini Samoa ya Marekani kujiweka wakfu kwa Yehova. Lydia Pedro, mtu wao wa ukoo aliyekuwa painia wa pekee huko Fiji, alikuwa amemwachia ndugu ya Wallace kitabu “Let God Be True,” alipowatembelea mwaka wa 1952. Wallace alikipata kitabu hicho nyumbani kwa ndugu yake na kukisoma kwa makini.

      Baada ya kukutana na familia ya Pedro mwaka wa 1954, Ron na Dolly walijifunza na dada na ndugu mkubwa wa Wallace. Wallace alimwamini Yehova Mungu, lakini kwa sababu ya kushuku dini, mwanzoni aliogopa kujiunga na wengine katika funzo. Muda si muda, alisadiki kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli, naye akaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida Fagatogo. Alifanya maendeleo ya haraka ya kiroho na mnamo Aprili 30, 1955, Wallace akabatizwa katika Bandari ya Pago Pago.

      Kufikia Januari 1955, mwaka mmoja tu baada ya Ron na Dolly kufika, watu saba walikuwa wakihudhuria mikutano katika nyumba ndogo ya painia katika kijiji cha Fagatogo. Kwa sababu ya uhaba wa viti, watu waliketi sakafuni. Muda si muda, watatu kati yao walianza kuandamana na Ron na Dolly katika huduma ya shambani. Ijapokuwa ilikuwa siku ya mambo madogo, kulikuwa na mengi akibani.

      WAMISHONARI WA GILEADI WAWASILI

      Mnamo Februari 4, 1955, wamishonari Paul na Frances Evans, na pia Gordon na Patricia Scott kutoka Marekani, walifika Samoa ya Marekani. Waliishi katika makao ya wamishonari ya Fagatogo. Kutoka katika makao hayo, mtu angeweza kuona watu na pilikapilika zao za kila siku kijijini. Leonard (Len) Helberg, mwangalizi wa mzunguko aliyetembelea Pago Pago mwaka huo asimulia mambo aliyojionea:

      “Wamishonari walikuwa wakikaa katika nyumba kubwa iliyokuwa juu ya duka kubwa la zamani. Upande mmoja, ng’ambo ya kijito, kulikuwa na baa, nao mabaharia walipenda kujiburudisha humo wakati wa jioni. Walipolewa na kuanza kusababisha vurugu barabarani, polisi wa kijiji hicho, ambaye alikuwa mfupi lakini ngangari, angejipenyeza katikati ya umati huo akiwa na sigara yake mdomoni huku akivurumisha makonde huku na huku ili kutenganisha pande mbili zinazozozana. Upande wa nyuma wa nyumba hiyo, kutoka katika kanisa lililokuwa likipakana na nyumba yetu kulikuwa na kelele za mahubiri ya kuwatisha watu kuhusu moto wa mateso. Tukiwa kwenye varanda upande wa mbele, tulikuwa tukiona umati wa watu ukikusanyika karibu na benki mara moja kwa mwezi siku ya mshahara. Wamishonari kutoka katika makanisa, walikuja kutoka pande zote za kisiwa hicho ili kukusanya fungu la kumi kutoka kwa waumini wao kabla hawajatumia mishahara yao.”

      Katika mazingira hayo yenye vituko, watu wengi walipendezwa na mambo ya kiroho. Len anaeleza: “Mmishonari mmoja alikuwa akianza mahubiri saa 12 asubuhi kwa kuongoza funzo la Biblia katika kibanda cha kunyolea kilichokuwa karibu na nyumba yao, kabla kinyozi huyo kufungua kazi. Baada ya hapo, angejifunza na mwokaji mikate, kabla ya kununua mkate ambao angerudi nao nyumbani kwa ajili ya kiamsha-kinywa. Baadaye siku hiyo, ndugu huyohuyo alijifunza na kikundi cha wafungwa katika jela iliyokuwa katika kijiji hicho.” Kufikia mwisho wa mwaka huo, wamishonari hao walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 60 hivi yaliyokuwa yakihudhuriwa na watu zaidi ya 200.

      “SINEMA YA BURE LEO”

      Mojawapo ya sababu zilizochochea watu wengi kupendezwa na kweli ni ile filamu The New World Society in Action.e Filamu hiyo ya kwanza kutayarishwa na tengenezo miaka 40 baada ya ile filamu ya “Photo-Drama of Creation,” ilionyesha kazi ulimwenguni pote ya kuhubiri na kuchapisha, hali kadhalika utendaji wa tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Katika ziara yake ya majuma manne nchini Samoa ya Marekani mwaka wa 1955, Len alionyesha jumla ya watu 3,227 filamu hiyo katika maonyesho 15 tofauti-tofauti, wastani wa watu 215 hivi kwa kila onyesho.

      Len akumbuka: “Kabla ya kila onyesho, tulizunguka kwa gari kijiji kizima tukitawanya vikaratasi vilivyokuwa na matangazo kuhusu filamu hiyo. Wakati huohuo tulipaaza sauti, ‘Kuna sinema ya bure leo,’ na kutaja mahali ambapo sinema hiyo itaonyeshwa.”

      Filamu hiyo iliwavutia watu wengi. Baada ya kila onyesho, watazamaji walitaka kujua mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova na mafundisho yao. Watu waliopendezwa hawakungoja watembelewe nyumbani na Mashahidi, badala yake walijileta wenyewe katika makao ya wamishonari, ambapo wamishonari waliongoza mafunzo kadhaa sehemu tofauti-tofauti katika makao hayo wakati uleule. Kikundi kimoja kilipoondoka kingine kiliingia. “Miaka kadhaa baadaye,” Ron Sellars anasema, “bado watu walikuwa wakihusianisha mambo waliyoona katika filamu ile na Mashahidi wa Yehova.”

      BIDII KATIKA KAZI YA KUHUBIRI YAGUSA MIOYO

      Miezi miwili baada ya ziara ya Len Helberg, kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova nchini Samoa ya Marekani lilianzishwa katika kijiji cha Fagatogo. Katika kipindi cha mwaka mmoja tu idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 14 mpaka 22. Karibu wakati huohuo mapainia wa pekee wawili, Fred na Shirley Wegener, kutoka Australia walikuja kulisaidia kutaniko hilo. Sasa Fred ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Samoa.

      Wahubiri, mapainia, na wamishonari hao walikuwa ‘wakiwaka roho.’ (Rom. 12:11) Len anasema: “Kwa sababu ya bidii yao na kwa kuwa watu wengi katika eneo hilo walipendezwa na Biblia, kufikia katikati ya miaka ya 1960, katika karibu kila nyumba kijijini Fagatogo kulikuwa mtu anayejifunza Biblia. Pia, katika kipindi hicho, kila nyumba katika kisiwa hicho ilihubiriwa angalau mara moja kila mwezi.”

      Kampeni hiyo kubwa ya kuhubiri iliwachochea watu wa eneo hilo kupatanisha maoni yao na mafundisho ya Biblia. Len asema: “Kila mtu akapata kujua kwamba watu wataishi milele duniani, hakuna moto wa mateso, na kwamba wafu hawajui lolote. Watu walijifunza mambo hayo ya msingi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova bali si kutoka katika makanisa yao. Sababu ni kwamba tulizungumza nao kibinafsi na kujadiliana nao kwa kutumia Biblia zao wenyewe.”

      Hata hivyo, dini na uhusiano wa kifamilia uliwafanya wengi wasichukue hatua. Baadhi yao waliendelea kuishi maisha mapotovu yaliyoendekezwa na makanisa badala ya maadili mazuri ya Wakristo wa kweli. Lakini kuna wengine waliokuwa wanyoofu kama yule mfanyabiashara katika mfano wa Yesu, ambao waliiona kweli kuwa lulu yenye thamani kubwa. Watu wengi wanyoofu kama hao walisimama imara upande wa kweli.—Mt. 13:45, 46.

      UTAMADUNI WA KISAMOA

      Caroline Pedro, painia kutoka Kanada ambaye aliolewa na Wallace Pedro mwaka wa 1960, anasema: “Tulifurahia sana kuhubiri zamani hizo. Karibu katika kila nyumba kulikuwa na mtu aliyependezwa na ujumbe wa Biblia. Ilikuwa rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia, na mara nyingi familia nzima-nzima ziliketi kusikiliza.

      “Hatuwezi kusahau jinsi ilivyokuwa tulipokuwa tukihubiri vijijini. Kwa kawaida watoto wadogo walikuwa wakitufuata kutoka nyumba moja hadi nyingine wakisikiliza kwa makini mahubiri yetu. Kisha wangekimbia hadi nyumba iliyofuata na kuwaambia kwamba tunakuja. Hata waliwaeleza wenye nyumba ujumbe wetu na maandiko tuliyokuwa tukitumia! Ili kuwaweza watoto hao, tulitayarisha aina mbalimbali za utangulizi.”

      Walipokuwa wakihubiri, akina ndugu walijitahidi kuheshimu utamaduni wa eneo hilo. (1 Kor. 9:20-23) Charles Pritchard, aliyekuwa mmishonari na ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya New Zealand, anasema: “Kwa sababu ya joto, nyumba za vijijini hazina kuta, hivyo tungeweza kuona kwa urahisi ikiwa kuna mtu au la. Kulingana na utamaduni wa Samoa, kuzungumza na mwenye nyumba ukiwa tumesimama au kabla ya kukaribishwa, ni kukosa adabu. Hivyo, tulipoikaribia nyumba, tulisubiri mwenye nyumba atukaribishe. Kisha, angetandika mkeka safi sakafuni ndani ya nyumba. Hiyo ilikuwa ishara tuvue viatu, tuingie na kuketi kwenye mkeka huo tukiwa tumepishanisha miguu yetu.” Haikuwa rahisi kwa wamishonari wengi kuketi hivyo sakafuni kwa muda mrefu. Hata hivyo, waliruhusiwa kunyoosha miguu na kuifunika kwa mkeka. Kwa kufanya hivyo, waliepuka kumwelekezea mwenye nyumba miguu jambo ambalo Wasamoa huliona kuwa ukosefu mkubwa wa adabu.

      John Rhodes, ambaye kwa miaka 20 alikuwa mmishonari nchini Samoa na Samoa ya Marekani anasema: “Wenye nyumba walitukaribisha na kusema kwamba tumewaonyesha heshima kubwa kwa kuwapelekea ujumbe wa Biblia katika nyumba zao duni. Kisha wangetusalimu kwa kutuuliza maswali kama vile: Mmetoka wapi? Mna watoto? Kwenu ni wapi?”

      Helen, mke wa John, anasema: “Sikuzote tulizungumza na wenye nyumba tukitumia maneno ya heshima ambayo kwa kawaida yalitumiwa wakati wa pindi rasmi. Kufanya hivyo kulionyesha kwamba tunamheshimu mwenye nyumba na kuufanya ujumbe wetu wa Biblia uheshimiwe.”

      Caroline Pedro anasema: “Salamu hizo zilitusaidia kufahamiana na watu mbalimbali na familia zao. Hivyo tungeweza kuwasaidia vizuri zaidi kiroho.”

      Baada ya salamu, wahubiri wangeweza kutoa ujumbe wa Ufalme. Robert Boies ambaye aliwahi kuwa mmishonari anakumbuka hivi: “Kwa kawaida wenye nyumba walitusikiliza kwa makini haidhuru mazungumzo hayo yalichukua muda gani. Kisha, wangerudia mambo mbalimbali tuliyozungumzia ili kuonyesha kwamba wanauona ujumbe wetu kuwa muhimu.”

      Ilikuwa kawaida kuwa na mazungumzo marefu ya Biblia kwa sababu watu wengi walikuwa wameisoma Biblia. Caroline Pedro anasema: “Mazungumzo hayo yalinisaidia kuelewa vizuri zaidi habari mbalimbali za Biblia.” Wenye nyumba wengi walikubali vitabu na magazeti yetu. Baada ya muda, wahubiri wangeweza kutofautisha kati ya wadadisi tu na wale wanaopendezwa kikweli na mambo ya kiroho.

      Wapya wengi waliopendezwa ambao walianza kuhudhuria mikutano, walitamani sana kuhubiri. John Rhodes anasema: “Kiasili, Wasamoa huzungumza kwa ufasaha, na wapya wengi wangeweza kuzungumza na wengine kuhusu imani yao kwa usadikisho hata pasipo mazoezi mengi. Hata hivyo, tuliwatia moyo watumie mapendekezo yaliyochapishwa na kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko badala ya kutegemea tu uwezo wao wa kiasili wa kusema.” Mazoezi hayo mazuri hatimaye yaliwasaidia wengi kuwa wahubiri stadi.

  • Samoa
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 87]

      “Nilifurahi Kila Siku”

      RONALD SELLARS

      ALIZALIWA 1922

      ALIBATIZWA 1940

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na mke wake, Olive (Dolly), walifika Samoa wakiwa mapainia wa pekee mwaka wa 1953. Alihitimu shule ya wamishonari ya Gileadi mwaka wa 1961. Ron bado anatumikia akiwa painia wa pekee huko Samoa ya Marekani.

      SERIKALI ya Samoa ilipokataa kuongeza muda wetu wa kukaa, mimi na Dolly tulihamia Samoa ya Marekani. Tulishushwa na meli kwenye gati la mji wa Pago Pago saa tisa alfajiri, wakati ambapo hakukuwa na watu. Hakukuwa na wahubiri wengine katika nchi hiyo nasi tulikuwa na dola 12 tu mfukoni. Baadaye asubuhi hiyo, baba ya mtu ambaye awali alikuwa akijifunza Biblia alitupa mahali pa kukaa. Alikuwa na chumba kimoja, nasi tulikuwa tukilala kwenye kona, iliyotengwa kwa pazia. Ingawa tulitaka kutafuta nyumba ya kukaa, tulianza kuhubiri nyumba ya jirani yake.

      Majuma kadhaa baadaye, tulikodisha nyumba kubwa iliyokuwa juu ya duka la jumla katika kijiji cha Fagatogo. Ukiwa katika nyumba hiyo, ungeweza kuona vizuri Bandari ya Pago Pago hata hivyo ilikuwa tupu. Ndugu Knorr alikuwa ametuambia: “Mtakapoenda kwenye visiwa vya Pasifiki, huenda maisha yakawa magumu. Huenda mkalazimika kutandaza makatoni ya vitabu sakafuni na kuyatumia kama kitanda.” Hivyo ndivyo tulivyofanya! Miezi mingi ilipita kabla hatujapata pesa za kutosha kutengeneza kitanda, meza, na viti vinavyofaa. Hata hivyo, tulifurahi kuwa na nyumba yetu wenyewe.

      Ingawa mke wangu mpendwa alikufa mwaka wa 1985, bado mimi huenda katika utumishi wa shambani siku nyingi. Ninapofikiria miaka zaidi ya 50 ambayo nimetumia katika utumishi wa upainia na umishonari, kwa kweli ninaweza kusema kwamba nilifurahi kila siku!

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 88]

      “Walinichochea Kumpenda Yehova”

      WALLACE PEDRO

      ALIZALIWA 1935

      ALIBATIZWA 1955

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mtu wa kwanza kubatizwa nchini Samoa ya Marekani. Yeye na mke wake, Caroline, walifanya upainia, baadaye wakawa na familia. Sasa wanatumikia Seattle, Washington, Marekani.

      NILIPOANZA kujifunza Biblia na kuanza kuhubiri, nilifukuzwa nyumbani nikiwa tu na nguo nilizokuwa nimevaa! Usiku huo nililala ufuoni. Nilimwomba Yehova anipe ujasiri wa kumtumikia hata iweje.

      Siku iliyofuata, nilikuwa katika maktaba ya shule wakati ambapo Ndugu Paul Evans aliingia bila mimi kumtarajia. Alipoona kwamba kuna jambo linalonisumbua, aliniambia, “Twende kwenye makao ya wamishonari, tukazungumze.” Wamishonari walinikaribisha kwa fadhili, na mwaka huohuo nikabatizwa.

      Baada ya kumaliza masomo yangu ya sekondari, nilianza kufanya upainia pamoja na wamishonari. Baadaye nikamwoa Caroline Hinsche, painia mwenye bidii kutoka Kanada aliyekuwa akitumikia nchini Fiji, nasi tukawa mapainia wa pekee nchini Samoa ya Marekani.

      Hatua kwa hatua mtazamo wa wazazi wangu ulianza kubadilika. Baba yangu alijifunza Biblia kabla hajafa, na mama yangu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 72. Ninathamini sana kielelezo cha wamishonari hao wa kwanza-kwanza. Walinichochea kumpenda Yehova, jambo ambalo limenitegemeza hadi leo hii!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki