Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Mafundisho ya Kipagani Yapenyeza Ndani

      Mafundisho safi ya Kristo yamo katika maandishi—yamehifadhiwa katika Maandiko Matakatifu. Kwa kielelezo, Yesu alifundisha wazi kwamba Yehova ndiye “Mungu pekee wa kweli” na kwamba nafsi ya kibinadamu yaweza kufa. (Yn. 17:3; Mt. 10:28, NW) Hata hivyo, mitume walipokufa na muundo wa kitengenezo ukadhoofika, mafundisho hayo yaliyo wazi yalifisidiwa kwa kadiri mafundisho ya kipagani yalivyopenyeza ndani ya Ukristo. Jambo kama hilo lingeweza kutokeaje?

      Sababu moja kuu ilikuwa ule uvutano wenye hila wa falsafa ya Kigiriki. Chaeleza hivi The New Encyclopædia Britannica: “Kuanzia katikati ya karne ya 2 WK Wakristo waliokuwa na mazoezi fulani katika falsafa ya Kigiriki walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kulingana na mitajo ya falsafa hiyo, ili kutosheleza akili zao wenyewe na pia ili kuongoa wapagani walioelimishwa.” Mara watu wenye mawazo ya kufuata falsafa walipokuja kuwa Wakristo, haikuchukua muda mrefu kabla ya falsafa ya Kigiriki na ule uitwao eti “Ukristo” kuungana kwa njia isiyotenganika.

      Tokeo la muungano huo ni kwamba, mafundisho ya kipagani kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi yalipenyeza polepole yakaingia katika Ukristo uliochafuliwa. Hata hivyo, mafundisho hayo yarudi nyuma mbali sana kupita wanafalsafa Wagiriki. Kwa kweli Wagiriki waliyapata kutokana na tamaduni za zamani zaidi, kwa maana kuna uthibitisho wa kwamba mafundisho hayo yalikuwa katika dini za kale za Kimisri na Kibabiloni.

      Kwa kadiri mafundisho ya kipagani yalivyoendelea kupenyeza ndani ya Ukristo, mafundisho mengine ya Kimaandiko yalipotoshwa pia au yakaachiliwa mbali.

      Tumaini la Ufalme Lafifia

      Wanafunzi wa Yesu walijua sana kwamba ilikuwa lazima wakae macho wakitazamia “kuwapo” kwa Yesu kulikoahidiwa na kuja kwa Ufalme wake. Baada ya muda ilifahamiwa kwamba Ufalme huo utatawala juu ya dunia kwa miaka elfu na kuigeuza iwe paradiso. (Mt. 24:3; 2 Tim. 4:18; Ufu. 20:4, 6, NW) Waandikaji wa Biblia Wakristo waliwasihi mashahidi wa karne ya kwanza waendelee kuwa macho kiroho na kuendelea kujitenga na ulimwengu. (Yak. 1:27; 4:4; 5:7, 8; 1 Pet. 4:7) Lakini mara mitume walipokufa, taraja la Kikristo la kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wake lilififia. Kwa nini?

      Sababu moja ilikuwa kuchafuliwa kiroho kulikosababishwa na fundisho la Kigiriki la kutokufa kwa nafsi. Kwa kadiri lilivyotia mizizi miongoni mwa Wakristo, tumaini la mileani liliachiliwa hatua kwa hatua. Kwa nini? The New International Dictionary of New Testament Theology chaeleza hivi: “Fundisho la kutokufa kwa nafsi liliingia kuchukua mahali pa eskatolojia [fundisho juu ya “Mambo ya Mwisho”] ya AJ [Agano Jipya] pamoja na tumaini layo la ufufuo wa wafu na uumbaji upya (Ufu. 21 mistari inayofuata), hivi kwamba nafsi hupokea hukumu baada ya kifo na hufikia paradiso ambayo sasa hufikiriwa kuwa ya ulimwengu mwingine.” Yaani, Wakristo waasi-imani walifikiri kwamba nafsi iliendelea kuwa hai baada ya mwili kufa na kwamba kwa hiyo baraka za Utawala wa Mileani wa Kristo lazima ziwe zahusiana na makao ya roho. Hivyo walihamisha Paradiso kutoka duniani hadi mbinguni, ambako, wao waliamini, ndiko nafsi iliyookolewa huenda wakati wa kufa. Basi, hakukuwa na uhitaji wa kuwa macho kutazamia kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wake, kwa kuwa wakati wa kufa wote walitumaini kujiunga na Kristo mbinguni.g

  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 36]

      Plato na “Ukristo”

      Mwanafalsafa Mgiriki Plato (aliyezaliwa kama 428 K.W.K.) hakuwa na njia ya kujua kwamba hatimaye mafundisho yake yangepata njia ya kuingia ndani ya Ukristo ulioasi imani. Mambo makuu ambayo Plato aliuchangia “Ukristo” yalihusu mafundisho ya Utatu na kutokufa kwa nafsi.

      Mawazo ya Plato juu ya Mungu na asili yalikuwa na uvutano juu ya fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo. Chaeleza hivi “Nouveau Dictionnaire Universel”: “Utatu wa Kiplato, wenyewe ukiwa ni mpango mpya tu wa utatu-utatu mwingi wa kale zaidi wenye kurudi nyuma kwenye watu wa mapema kabisa, huonekana kuwa ni utatu wa maelezo ya akili ya kifalsafa ya sifa zilizozaa nyutu tatu au watu wa kimungu wanaofundishwa na makanisa ya Kikristo. . . . Wazo hili la mwanafalsafa Mgiriki la utatu wa kimungu . . . laweza kupatikana katika dini zote za kale [za kipagani].”—Buku la 2, ukurasa 1467.

      Kuhusu fundisho la nafsi isiyoweza kufa, “New Catholic Encyclopedia” yasema: “Dhana ya Kikristo ya nafsi ya kiroho iliyoumbwa na Mungu na kutiwa katika mwili wakati wa mtungo wa mimba ili kufanyiza mwanadamu kuwa kitu kizima kilicho hai ni tunda la usitawi wa muda mrefu wa falsafa ya Kikristo. Ni kupitia Origen tu [aliyekufa kama 254 W.K.] katika Mashariki na Mt. Augustine [aliyekufa 430 W.K.] katika Magharibi kwamba nafsi ikathibitishwa kuwa namna ya kiroho na dhana ya kifalsafa iliyofanyizwa kutoka asili yayo. . . . Fundisho lake [la Augustine] . . . lilikuwa na mambo mengi (kutia na makosa fulanifulani) kutokana na mawazo mapya ya Plato.”—Buku la 13, kurasa 452, 454.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki