Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Biblia Yashambuliwa
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • Biblia Yashambuliwa

      MAANDISHI yote yanayojulikana kama Biblia, au Maandiko Matakatifu, yaliandikwa katika kipindi cha zaidi ya miaka 1,600. Sehemu ya zamani zaidi ya maandishi hayo iliandikwa na Musa; sehemu ya mwisho iliandikwa na mwanafunzi wa Yesu Kristo aliyekuwa na umri wa karibu miaka 100.

      Jitihada za kuwazuia watu wasisome Maandiko zimefanywa kwa muda mrefu sana hata kabla ya Wakati wetu wa Kawaida, katika Enzi za Kati, au hata katika nyakati za kisasa. Rekodi moja ya kale inayoonyesha majaribio hayo ni ile iliyoandikwa na nabii wa Mungu Yeremia, aliyeishi zaidi ya miaka 600 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo.

      Ujumbe Usiopendwa na Wengi Washambuliwa

      Nabii Yeremia aliongozwa na Mungu kuandika katika kitabu cha kukunjwa ujumbe ulioshutumu wakaaji wa Yuda la kale waliotenda dhambi na kuwaonya kwamba mji wao mkuu, Yerusalemu, ungeharibiwa ikiwa hawangebadili njia zao. Mwandishi wa Yeremia, Baruku, alisoma ujumbe huo kwa sauti, hadharani katika hekalu la Yerusalemu. Aliusoma mara ya pili mbele ya wakuu wa Yuda, nao wakampelekea Mfalme Yehoyakimu kitabu hicho cha kukunjwa. Mfalme alipoyasikia maneno ya Mungu, alikasirika sana. Kwa hiyo, akakikata kile kitabu cha kukunjwa vipande-vipande na kukiteketeza.—Yeremia 36:1-23.

      Kisha Mungu akamwamuru Yeremia: “Chukua tena kitabu cha kukunjwa, kingine, nawe uandike juu yake yale maneno yote ya kwanza yaliyokuwa juu ya kile kitabu cha kwanza, ambacho Yehoyakimu mfalme wa Yuda aliteketeza.” (Yeremia 36:28) Miaka 17 hivi baadaye, kama tu Mungu alivyokuwa ametabiri kupitia Yeremia, Yerusalemu liliharibiwa, watawala wake wengi wakauawa, na wakaaji wake wakapelekwa uhamishoni huko Babiloni. Ujumbe uliokuwa ndani ya kitabu hicho cha kukunjwa—pamoja na habari kuhusu kushambuliwa kwa kitabu chenyewe—umeokoka hadi leo katika kitabu cha Biblia cha Yeremia.

      Biblia Yaendelea Kuteketezwa

      Si Yehoyakimu peke yake aliyejaribu kuliteketeza Neno la Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo. Baada ya kuvunjika kwa Milki ya Ugiriki, Israeli ikawa chini ya utawala wa ukoo wa Seleuko. Antioko Epifane, aliyekuwa Mfalme wa Ukoo wa Seleuko, ambaye alitawala kuanzia 175 hadi 164 K.W.K., alitaka kuunganisha milki yake kwa kutumia utamaduni wa Kigiriki. Ili afanye hivyo, alijaribu kuwalazimisha Wayahudi wakubali maisha, desturi, na dini ya Kigiriki.

      Mnamo 168 K.W.K., Antioko alivamia hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Juu ya madhabahu iliyokuwapo, alijenga madhabahu nyingine ili kumtukuza mungu Zeu wa Wagiriki. Pia Antioko aliwakataza Wayahudi wasishike Sabato na akawaamuru wasiwatahiri wana wao. Adhabu ya kutotii ilikuwa kifo.

      Njia moja ambayo Antioko alitumia ili kuwafanya Wayahudi wabadili dini ilikuwa kuharibu vitabu vyote vya kukunjwa vilivyokuwa na Sheria. Ingawa Antioko alijaribu kufanya mabadiliko hayo katika Israeli yote, alishindwa kuharibu nakala zote za Maandiko ya Kiebrania. Vitabu fulani vya kukunjwa vilivyofichwa vizuri na Wayahudi waliokuwa Israeli havikuteketezwa, na nakala nyingine za Maandiko Matakatifu zilihifadhiwa na Wayahudi waliokuwa wakiishi katika maeneo mengine.

      Amri ya Diokletiani

      Mtawala mwingine maarufu aliyejaribu kuharibu Maandiko alikuwa Maliki Mroma Diokletiani. Mnamo 303 W.K., Diokletiani alitoa amri kadhaa zilizosema kwamba Wakristo wateswe vikali. Hilo lilitokeza kile ambacho wanahistoria fulani wamekiita “Yale Mateso Makubwa.” Amri yake ya kwanza iliagiza kwamba nakala zote za Maandiko ziteketezwe na mahali ambapo Wakristo walikutania pabomolewe. Harry Y. Gamble, profesa wa masomo ya dini katika Chuo Kikuu cha Virginia, aliandika hivi: “Diokletiani alijiambia kwamba Wakristo wote, popote walipo, lazima wawe na vitabu kadhaa na alijua kwamba vitabu hivyo ni muhimu ili Wakristo waendelee kuwapo kama jamii.” Mwanahistoria Eusebio wa Kaisaria, huko Palestina, aliyeishi katika kipindi hicho, alisema hivi: “Tulijionea kwa macho yetu wenyewe nyumba za sala zikibomolewa kabisa, na Maandiko yaliyopuliziwa na matakatifu yakiteketezwa sokoni.”

      Inasemekana kwamba miezi mitatu baada ya Diokletiani kutoa amri yake, meya wa jiji la Cirta, lililokuwa Afrika Kaskazini na ambalo sasa linaitwa Constantine, aliwaamuru Wakristo wamkabidhi ‘maandishi yao yote ya sheria’ na “nakala za maandiko.” Masimulizi ya kipindi hicho yanaonyesha kwamba kulikuwa na Wakristo walioona ni afadhali kuteswa na kuuawa badala ya kutoa nakala zao za Biblia ziharibiwe.

      Kusudi la Mashambulio Hayo

      Yehoyakimu, Antioko, na Diokletiani walikuwa na kusudi moja: kuliangamiza Neno la Mungu. Hata hivyo, Biblia iliokoka majaribio yote ya kuliangamiza. Watawala wa Roma baada ya Diokletiani walianza kudai kwamba wao ni Wakristo. Lakini bado mashambulizi dhidi ya Biblia yaliendelea. Kwa nini?

      Watawala hao pamoja na viongozi wa kanisa walidai kwamba kusudi la kuiteketeza Biblia halikuwa kuiangamiza. Badala yake wanaume hao walikuwa tu wakijaribu kuwazuia watu wa kawaida wasiipate Biblia. Lakini kwa nini viongozi wa kidini walifanya hivyo? Na kanisa lilifanya jitihada zipi ili kujaribu kuwazuia watu wasiisome Biblia? Acheni tuone.

  • Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • Walijaribu Kuwazuia Watu Wasilipate Neno la Mungu

      KADIRI wakati ulivyopita, jitihada zilifanywa ili kuitafsiri Biblia katika lugha ambazo watu walizungumza kwa ukawaida. Ni wachache tu ambao wangeweza kusoma Biblia katika lugha zake za awali za Kiebrania au Kigiriki. Ingekuwa vigumu kwa wengi wetu kuelewa Neno la Mungu ikiwa leo lingepatikana katika lugha hizo za kale tu.

      Karibu miaka 300 kabla ya Yesu kuishi duniani, kazi ilianza ya kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki. Tafsiri hiyo inajulikana kama Septuajinti ya Kigiriki. Miaka 700 hivi baadaye, Jerome alitokeza tafsiri maarufu inayojulikana kama Vulgate. Hiyo ilikuwa tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania na Kigiriki katika Kilatini, lugha iliyokuwa ikitumiwa kwa ukawaida katika Milki ya Roma wakati huo.

      Baadaye, Kilatini kiliacha kuwa lugha ya kawaida. Ni watu wenye elimu tu walioendelea kutumia Kilatini, na Kanisa Katoliki lilipinga mbinu za kutafsiri Biblia katika lugha nyingine. Viongozi wa kidini walisisitiza kwamba Biblia ilifaa tu kuwa katika lugha ya Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini.a

      Migawanyiko Katika Kanisa na Kutafsiriwa kwa Biblia

      Katika karne ya tisa W.K., Methodius na Cyril, wamishonari Wathesalonike waliokuwa wametumwa na Kanisa la Mashariki huko Byzantium, walipendekeza kwamba Kislavonia kitumiwe katika kanisa. Kusudi lao lilikuwa kuwawezesha watu wa Slavonia wa Ulaya Mashariki kujifunza kumhusu Mungu katika lugha yao wenyewe kwa kuwa hawakuelewa Kigiriki au Kilatini.

      Hata hivyo, wamishonari hao walikabili upinzani mkali kutoka kwa makasisi Wajerumani, ambao walijaribu kulazimisha kwamba Kilatini kitumiwe ili kuzuia Ukristo wa Byzantium usienee. Kwa wazi, siasa zilikuwa muhimu kwao kuliko watu kupata elimu ya kidini. Mizozo kati ya sehemu ya Magharibi na ya Mashariki ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ulifanya Kanisa Katoliki na Kanisa la Othodoksi la Mashariki zigawanyike katika mwaka wa 1054.

      Kuzuia Biblia Isitafsiriwe

      Mwishowe, Kanisa Katoliki likaanza kuona Kilatini kuwa lugha takatifu. Kwa sababu hiyo, katika mwaka wa 1079 Vratislaus, dyuki wa Bohemia, alipoandika barua akiomba ruhusa ya kutumia Kislavonia katika ibada kanisani, Papa Gregory wa Saba alimjibu hivi: “Hatuwezi kwa njia yoyote kukubali ombi hili.” Kwa nini?

      “Kwa wale wanaochunguza jambo hili kwa uangalifu,” akasema Gregory, “ni wazi kwamba ilimpendeza Mungu kufanya sehemu fulani ya Maandiko Matakatifu isieleweke kabisa kwa sababu, ikiwa kila mtu angeelewa kila kitu, basi [Maandiko] yangefanywa kuwa ya kawaida tu na kuvunjiwa heshima au watu wasio na akili nyingi wangeyaelewa vibaya na hivyo waasi.”

      Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, na ilipaswa kuwa hivyo. Msimamo huo uliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu ya watu wa kawaida. Hawakutaka watu wa kawaida wachunguze mambo ambayo waliona kuwa ni ya makasisi tu.

      Mnamo 1199, Papa Innocent wa Tatu aliandika kuhusu watu walioonwa kuwa wazushi ambao walitafsiri Biblia katika Kifaransa na wakaamua kuwa na mazungumzo kati yao kuihusu. Innocent alitumia maneno haya ya Yesu kuwahusu: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” (Mathayo 7:6) Kwa nini alikuwa na maoni hayo? “Ili mtu wa kawaida na ambaye hana elimu asiwe na kimbelembele cha kujifunza Maandiko matakatifu yaliyotukuka, au kuwahubiria watu kuyahusu.” Mara nyingi, wale waliopinga amri ya papa walipelekwa kwa watesaji ambao waliwalazimisha waungame kwamba wao ni wazushi. Wale waliokataa kukana msimamo wao waliteketezwa wakiwa hai.

      Wakati wa kile kipindi kirefu cha kuwazuia watu wasiipate na kuisoma Biblia, barua ya Papa Innocent ilitumiwa mara nyingi ili kutetea wazo la kwamba Biblia haipaswi kutumiwa wala kutafsiriwa katika lugha nyingine. Punde tu baada ya amri yake kutolewa, Biblia katika lugha nyingine zikaanza kuteketezwa, na pia watu fulani waliomiliki Biblia waliteketezwa. Katika karne zilizofuata, maaskofu na watawala wa nchi za Ulaya zilizokuwa chini ya udhibiti wa Kanisa Katoliki walitumia njia yoyote waliyoweza ili kuhakikisha kwamba marufuku yaliyowekwa na Papa Innocent wa Tatu yalifuatwa.

      Viongozi wa Kanisa Katoliki walijua kwamba mafundisho mengi ya dini hiyo hayakutegemea Biblia bali yalitegemea mapokeo ya kanisa. Bila shaka, hiyo ilikuwa sababu moja iliyowafanya wawazuie waumini wao wasiipate Biblia. Iwapo wangeisoma basi wangetambua kwamba mafundisho ya kanisa yalipingana na Maandiko.

      Matokeo ya Yale Mabadiliko Makubwa ya Kidini

      Uprotestanti ulibadili hali ya kidini barani Ulaya. Majaribio ya Martin Luther ya kuleta mabadiliko katika Kanisa Katoliki na kujitenga kwake katika mwaka wa 1521 kulitegemea hasa uelewaji wake wa Maandiko. Kwa hiyo, utengano huo ulipokamilika, Luther, aliyekuwa mtafsiri mwenye kipawa, alijitahidi kuifanya Biblia ipatikane kwa watu wote.

      Tafsiri ya Luther ya Kijerumani na usambazaji wake ulivuta fikira za Kanisa Katoliki, ambalo liliona kwamba umaarufu wa Biblia ya Luther ulipaswa kufunikwa kwa kutokeza Biblia nyingine iliyokubaliwa na kanisa. Tafsiri mbili za aina hiyo katika Kijerumani zilitokezwa upesi baada ya hapo. Lakini, mnamo 1546, baada ya miaka isiyozidi 25, Baraza la Trent la Kanisa Katoliki, liliamua kwamba kuchapishwa kwa vichapo vyovyote, kutia ndani tafsiri za Biblia, hakupaswi kufanywa bila idhini ya kanisa.

      Baraza la Trent liliagiza kwamba “kuanzia sasa Maandiko matakatifu . . . yatachapishwa kwa njia sahihi iwezekanayo; na kwamba itakuwa kinyume cha sheria kwa yeyote kuchapisha, au kumlipa mtu achapishe, vitabu vyovyote kuhusu mambo matakatifu bila jina la mwandishi kuonyeshwa; au kuviuza wakati ujao, au kuvimiliki, isipokuwa kwanza viwe vimechunguzwa na kuidhinishwa [na askofu wa eneo hilo].”

      Mnamo 1559, Papa Paul wa Nne alichapisha orodha ya kwanza ya vitabu vilivyopigwa marufuku na Kanisa Katoliki. Orodha hiyo ilikataza mtu kuwa na tafsiri za Biblia za Kifaransa, Kihispania, Kiholanzi, Kiingereza, Kiitaliano, na Kijerumani, kutia ndani tafsiri fulani za Kilatini. Watu wowote waliotaka kusoma Biblia waliambiwa wapate idhini iliyoandikwa kutoka kwa maaskofu au watesaji—jambo ambalo hakuna mtu angetaka kufanya kwani angeshukiwa kuwa mzushi.

      Watu waliojaribu kumiliki au kugawa Biblia katika lugha za kawaida katika eneo lao walilazimika kukabiliana na hasira ya Kanisa Katoliki. Wengi walikamatwa, wakateketezwa kwenye mti ulio wima au juu ya mti uliolazwa, wakahukumiwa kifungo cha maisha, au wakapelekwa kwenye meli wakafanye kazi ngumu ya kupiga makasia. Biblia zilizokusanywa ziliteketezwa. Makasisi Wakatoliki waliendelea kukusanya na kuteketeza Biblia hadi kufikia karne ya 20.

      Hilo halimaanishi kwamba Waprotestanti wamekuwa na mtazamo tofauti au wameitetea Biblia. Katika karne ya 18 na 19, baadhi ya wanatheolojia Waprotestanti walianza kutumia mbinu ya kujifunza Biblia ambayo baadaye ilikuja kuitwa uchambuzi wa Biblia. Kadiri muda ulivyopita, watu wengi walikubali nadharia za Darwin kwamba uhai haukuumbwa bali ulijitokeza wenyewe kwa njia fulani na kupitia mageuzi ukawa bora bila msaada wa Muumba.

      Wanatheolojia, na hata makasisi wengi, walifundisha kwamba Biblia ilitegemea hasa hekaya. Kwa sababu hiyo, si ajabu leo kuwasikia makasisi Waprotestanti, kutia ndani wengi wa wafuasi wao, wakisema kwamba Biblia si sahihi kihistoria.

      Huenda umesikia watu wakisema kwamba Biblia si sahihi, na huenda umeshangazwa na majaribio yaliyofanywa ili kuiangamiza katika karne zilizopita. Hata hivyo, majaribio hayo yalishindwa. Biblia iliokoka!

      Kwa Nini Imeokoka?

      Ni kweli kwamba watu wengi wameonyesha kuwa wanaipenda Biblia na wamekuwa tayari kufa ili kuitetea. Hata hivyo, kuokoka kwake kunategemea nguvu kubwa zaidi kuliko upendo wa wanadamu. Biblia imeokoka kwa sababu wote ambao waliandika Biblia waliongozwa na roho ya Mungu.—Isaya 40:8; 1 Petro 1:25.

      Kusoma na kufuata kile ambacho Biblia inasema kutatusaidia kuboresha maisha, afya, na familia zetu. Mungu anataka Biblia iokoke na itafsiriwe katika lugha nyingi kadiri inavyowezekana ili wote wapate nafasi ya kujifunza jinsi wanavyoweza kumpenda, kumtumikia, na hatimaye kufurahia baraka zake za milele. Bila shaka, sisi sote tunatamani mambo hayo!

      Yesu alisema hivi katika sala kwa Baba yake wa mbinguni: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Biblia—yale Maandiko ambayo Yesu alisoma na kufundisha—ndiyo njia ya Mungu ya kujibu maswali ambayo watu wanyoofu huuliza.

      Unatiwa moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu ujumbe wa Mungu kwa wanadamu unaopatikana katika Biblia. Mashahidi wa Yehova, wanaotokeza gazeti hili, watafurahi kukusaidia kufanya hivyo.b

      [Maelezo ya Chini]

      a Inaonekana kwamba wazo hilo lilitokana na maandishi ya askofu Mhispania, Isidore wa Seville (560-636 W.K.), aliyesema hivi: “Kuna lugha tatu takatifu, Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini, na hizo ndizo lugha kuu ulimwenguni pote. Sababu ni kwamba shtaka dhidi ya Bwana lililoandikwa juu ya msalaba na Pilato lilikuwa katika lugha hizo tatu.” Bila shaka, uamuzi wa kuandika shtaka hilo katika lugha hizo tatu ulifanywa na Waroma wapagani. Uamuzi huo haukutoka kwa Mungu.

      b Unaweza kuwasiliana nao bila masharti, kwa kutumia anwani moja kati ya zile zilizoonyeshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili au kupitia Tovuti ya www.watchtower.org.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Watu wa kawaida hawangeweza kupata Biblia kwa urahisi, jambo ambalo liliwafanya makasisi waendelee kuwa na mamlaka juu yao

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      Watu waliojaribu kumiliki au kugawa Biblia walipokamatwa, waliteketezwa kwenye mti au wakahukumiwa kifungo cha maisha

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      MAJIBU YA BIBLIA

      Muumba anataka tupate majibu ya maswali haya ya msingi:

      ● Kwa nini tuko hapa?

      ● Kwa nini watu wanateseka sana?

      ● Wafu wako wapi?

      ● Wanadamu wanaelekea wapi?

      Biblia inajibu maswali haya na kutoa mashauri ya jinsi tunavyoweza kupata furaha ya kweli.

      [Chati/Picha katika ukurasa wa 6]

      PINDI AMBAPO BIBLIA ILISHAMBULIWA

      m. 636 W.K.

      Isidore wa Seville anadai kwamba Kiebrania, Kigiriki, na Kilatini ni lugha “takatifu” kwa hiyo ndizo lugha ambazo Biblia Takatifu inapaswa kutafsiriwa

      1079

      Papa Gregory wa Saba anakataa katakata ombi la Vratislaus la kutumia Kislavonia kanisani, akisema kwamba watu “wasio na akili nyingi” hawapaswi kuwa na Maandiko

      1199

      Papa Innocent wa Tatu anasema kwamba wote wanaojaribu kutafsiri au kuwa na mazungumzo kuhusu Biblia ni wazushi. Wale wanaopinga amri ya papa wanateswa na kuuawa

      1546

      Kwa amri ya Baraza la Trent, uchapishaji wowote wa tafsiri za Biblia unapaswa kwanza kuidhinishwa na Kanisa Katoliki

      1559

      Papa Paul wa Nne anawazuia watu wasiwe na Biblia katika lugha za kawaida. Tafsiri za lugha za kienyeji zinakusanywa na kuteketezwa, na mara nyingi watu waliteketezwa pamoja na Biblia walizomiliki

      [Hisani ya Picha]

      Pope Gregory VII: © Scala/White Images/Art Resource, NY; Pope Innocent III: © Scala/Art Resource, NY; Council of Trent: © Scala/White Images/Art Resource, NY; Pope Paul IV: © The Print Collector, Great Britain/HIP/Art Resource, NY

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

      From Foxe’s Book of Martyrs

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki