-
Je, Biblia Ni Kitabu cha Kawaida Tu?Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Je, Biblia Ni Kitabu cha Kawaida Tu?
“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida . . . , ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 TIMOTHEO 3:16, 17.
SI KILA mtu anayekubaliana na maneno kama hayo. Wewe una maoni gani kuhusu Biblia?
• Je, ni kitabu cha fasihi kilichoandikwa kwa ustadi?
• Ni mojawapo ya vitabu vitakatifu vinavyokubaliwa?
• Ni kitabu cha hadithi za kale zenye mafundisho mazuri?
• Au ni Neno la Mungu
Swali ambalo unapaswa kujiuliza ni, Je, ni muhimu kuchunguza unaloamini? Fikiria yale ambayo Biblia yenyewe inasema: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Hivyo, Biblia inataja kwamba kusudi lake ni kutufundisha na kutupatia faraja na tumaini.
Hata hivyo, ikiwa Biblia ingekuwa tu kitabu cha fasihi au mojawapo ya vitabu vitakatifu, je, ungetazamia ikufundishe na iongoze familia yako, hasa ikiwa ujumbe wake ungekuwa tofauti na yale unayofikiria kuwa sawa? Ikiwa Biblia ingekuwa kitabu cha hadithi za kale, je, ungeweza kupata faraja na tumaini kutokana na ahadi zake?
Kwa upande mwingine, watu wengi ambao wamejifunza Biblia wameamini kwamba ni Neno la Mungu na ni kitabu cha kipekee. Kwa nini? Ni nini kinachoifanya Biblia iwe tofauti na vitabu vingine? Tunakutia moyo uchunguze mambo matano yanayotajwa katika makala zifuatazo yanayoifanya Biblia kuwa kitabu cha kipekee.
-
-
Historia Sahihi, Wala Si HadithiMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Historia Sahihi, Wala Si Hadithi
“Nimefuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.”—LUKA 1:3.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Hadithi na hekaya hueleza mambo yenye kuvutia lakini hazitaji mahali, tarehe, na majina hususa ya watu. Kinyume cha hilo, Biblia ina habari nyingi za kihistoria ambazo zinawahakikishia wasomaji kwamba ina “maneno ya kweli kabisa.”—Zaburi 119:160, The Psalms for Today, iliyotafsiriwa na R. K. Harrison.
MFANO: Biblia inasema kwamba “Nebukadneza mfalme wa Babiloni . . . [aka]mpeleka Yehoyakini [Mfalme wa Yuda] uhamishoni Babiloni.” Baadaye, “Evil-merodaki mfalme wa Babiloni, katika mwaka wa kuwa kwake mfalme, akakiinua kichwa cha Yehoyakini mfalme wa Yuda kutoka katika nyumba ya kifungo.” Zaidi ya hayo, “[Yehoyakini] alipewa posho daima kutoka kwa mfalme, kila siku kama inavyostahili, siku zote za maisha yake.”—2 Wafalme 24:11, 15; 25:27-30.
MAMBO AMBAYO WATAALAMU WA VITU VYA KALE WAMEGUNDUA: Katika magofu ya Babiloni la kale, wataalamu wa vitu vya kale waligundua hati za usimamizi zilizokuwa na tarehe ya wakati wa utawala wa Nebukadneza wa Pili. Hati hizo zina orodha ya kiwango cha chakula ambacho wafungwa na watu wengine waliotegemea nyumba ya kifalme walipewa. Orodha hiyo inatia ndani “Yaukini [Yehoyakini],” ambaye alikuwa “mfalme wa nchi ya Yahud (Yuda),” pamoja na familia yake. Vipi kuhusu kuwapo kwa Evil-merodaki, mfalme aliyetawala baada ya Nebukadneza? Chombo fulani kilichopatikana karibu na jiji la Susa kilikuwa na maandishi haya: “Jumba la kifalme la Amili-Marduki [Evil-merodaki], Mfalme wa Babiloni, mwana wa Nebukadneza, Mfalme wa Babiloni.”
UNA MAONI GANI? Je, kuna kitabu kingine chochote kitakatifu na cha kale ambacho kina habari hususa na sahihi za kihistoria? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
[Blabu katika ukurasa wa 5]
“Habari za mfuatano wa matukio na za kijiografia zilizo katika Biblia ni sahihi kabisa na ni zenye kutegemeka kuliko zile zinazotolewa na hati nyingine zozote za kale.”—KITABU A SCIENTIFIC INVESTIGATION OF THE OLD TESTAMENT, CHA ROBERT D. WILSON
[Picha katika ukurasa wa 5]
Hati yA Babiloni inayomtaja Mfalme Yehoyakini wa Yuda
[Picha Hisani katika ukurasa wa 5]
© bpk, Berlin/Vorderasiatisches Museum, SMB/Olaf M. Tessmer/Art Resource, NY
-
-
Sahihi KisayansiMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Sahihi Kisayansi
“Je, kufikia sasa sikukuandikia mashauri na ujuzi, nikuonyeshe ukweli wa maneno ya kweli, ili urudishe maneno yaliyo kweli.”—METHALI 22:20, 21.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Vitabu vya kale vina habari zisizotegemeka na mawazo hatari ambayo sayansi ya kisasa imethibitisha kuwa ni ya uwongo. Hata leo, waandishi wengi wanalazimika kubadili habari zilizo katika vitabu vyao ili zipatane na uvumbuzi wa kisasa. Lakini Biblia inadai kwamba ilitungwa na Muumba na Neno lake “linadumu milele.”—1 Petro 1:25.
MFANO: Sheria ya Musa iliwaamuru Waisraeli wachimbe na kufunika mavi yao “nje ya kambi.” (Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Ikiwa wangegusa mnyama au mwanadamu aliyekufa, Waisraeli walipaswa kujisafisha kwa maji. (Mambo ya Walawi 11:27, 28; Hesabu 19:14-16) Watu waliokuwa na ugonjwa wa ukoma walitengwa hadi uchunguzi wa kitiba ulipothibitisha kwamba hawangewaambukiza watu wengine.—Mambo ya Walawi 13:1-8.
MAMBO AMBAYO TIBA YA KISASA IMETHIBITISHA: Kuondoa kinyesi kwa njia inayofaa, kunawa mikono, na kutenga wagonjwa bado ndiyo njia bora ya kupambana na magonjwa. Ikiwa hakuna vyoo karibu au mfumo wa kuondoa maji machafu na takataka, Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani (CDC) vinatoa ushauri huu: “Funika mavi angalau mita 30 hivi kutoka mahali penye maji.” Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, watu wanapohakikisha kwamba wanaondoa kinyesi kwa njia inayofaa, wanapunguza magonjwa ya kuharisha kwa asilimia 36. Miaka isiyozidi 200 iliyopita, madaktari waligundua kwamba waliwaambukiza wagonjwa wengi wakati walipowagusa kabla ya kunawa mikono baada ya kugusa maiti. CDC inasema kwamba kunawa mikono ndiyo “njia pekee iliyo na matokeo zaidi katika kuzuia kusambaa kwa magonjwa.” Vipi kuhusu kuwatenga watu walio na ukoma au magonjwa mengine? Hivi karibuni, jarida linaloitwa Saudi Medical Journal lilisema hivi: “Janga la ugonjwa wa kuambukiza linapokumba eneo fulani, mbinu pekee ya kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo ni kuwatenga watu ambao tayari wameambukizwa.”
UNA MAONI GANI? Je, ungetazamia kitabu kingine chochote kitakatifu na cha kale kiwe na habari zinazopatana na sayansi ya kisasa? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
“Ni jambo lenye kuvutia kusoma mambo yanayohusu usafi yaliyofuatwa wakati wa Sheria ya Musa.”—KITABU MANUAL OF TROPICAL MEDICINE, CHA DAKT. ALDO CASTELLANI NA DAKT. ALBERT J. CHALMERS
-
-
Kitabu Chenye UpatanoMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Kitabu Chenye Upatano
“Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 PETRO 1:21.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Mara nyingi, hati za kale hazipatani hata iwe ziliandikwa wakati uleule.Vitabu ambavyo vimeandikwa na watu mbalimbali, wakiwa mahali tofauti, na wakati tofauti-tofauti huwa havipatani katika sehemu zote. Hata hivyo, Biblia inadai kwamba vitabu vyake vyote 66 vilitungwa na Mtu mmoja, hivyo vina ujumbe unaopatana.—2 Timotheo 3:16.
MFANO: Musa, mchungaji aliyeishi katika karne ya 16 K.W.K., aliandika katika kitabu cha kwanza cha Biblia kwamba kuna “uzao” ambao ungekuja kuokoa wanadamu. Baadaye, kitabu hicho kilitabiri kwamba uzao huo ungetokana na ukoo wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. (Mwanzo 3:15; 22:17, 18; 26:24; 28:14) Miaka 500 hivi baadaye, nabii Nathani alifunua kuwa uzao huo ungetokea katika ukoo wa kifalme wa Daudi. (2 Samweli 7:12) Miaka elfu moja baadaye, mtume Paulo alieleza kwamba uzao huo ungetia ndani Yesu na kikundi cha wafuasi wake waliochaguliwa. (Waroma 1:1-4; Wagalatia 3:16, 29) Hatimaye, kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., kitabu cha mwisho katika orodha ya Biblia kilitabiri kwamba washiriki wa ule uzao wangetoa ushahidi kumhusu Yesu duniani, wainuliwe hadi mbinguni, na kutawala pamoja naye kwa miaka 1,000. Uzao huo utamharibu Ibilisi na kuokoa wanadamu.—Ufunuo 12:17; 20:6-10.
MAONI YA WACHAMBUZI WA BIBLIA: Baada ya kuchunguza kwa kina vitabu vyote 66 vya Biblia, Louis Gaussen aliandika kwamba alishangazwa na “upatano wa ajabu wa vitabu hivyo, ambavyo viliandikwa katika kipindi cha miaka 1,500 na waandikaji wengi, . . . ambao walijaribu kutimiza lengo moja, na wakaendelea kufunua mambo kwa utaratibu fulani, ingawa wao wenyewe hawakuelewa kwa ukamili, yaani, historia ya ukombozi wa ulimwengu kupitia Mwana wa Mungu.”—Theopneusty—The Plenary Inspiration of the Holy Scriptures.
UNA MAONI GANI? Je, Ungetazamia kitabu kilichoandikwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 1,500 na waandikaji tofauti-tofauti wapatao 40 kiwe na upatano kamili? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
“Maandishi haya yanapounganishwa, yanafanyiza kitabu kimoja . . . Hakuna kitabu kingine chochote ulimwenguni kinachoweza kulinganishwa nacho.”—KITABU THE PROBLEM OF THE OLD TESTAMENT, CHA JAMES ORR
-
-
Biblia Ina Manufaa Hata LeoMnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
Biblia Ina Manufaa Hata Leo
“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.”—ZABURI 119:105.
BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Vitabu vingine vinaweza kuonekana kwamba vimeandikwa kwa ustadi, lakini havifai kutoa mwongozo maishani. Pia, vitabu vya kisasa vya kutoa maelekezo vinahitaji kufanyiwa marekebisho mara kwa mara. Kwa upande mwingine, Biblia inadai kwamba “mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi.”—Waroma 15:4.
MFANO: Ingawa haikuandikwa kwa kusudi la kutoa mwongozo wa kitiba, Biblia ina mapendekezo yanayofaa kuhusu jinsi ya kuwa na afya nzuri na hisia zinazofaa. Kwa mfano, inasema kwamba “moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Methali 14:30) Biblia pia inaonya hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Vilevile, inasema kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
MAMBO AMBAYO UTAFITI UMEFUNUA: Utulivu, urafiki mzuri, na ukarimu unaweza kuboresha afya yako. Gazeti The Journal of the American Medical Association linasema hivi: “Wanaume wanaopandwa na hasira haraka wako katika hatari mara mbili zaidi ya kupatwa na ugonjwa wa kupooza kuliko wanaume wanaoweza kudhibiti hasira yao.” Utafiti uliofanywa kwa miaka kumi nchini Australia ulionyesha kwamba wazee ambao “wana marafiki wa karibu na pia watu wanaowaeleza mambo yao ya siri,” wanaweza kuishi kwa muda mrefu zaidi. Na katika mwaka wa 2008, watafiti nchini Kanada na Marekani waligundua kwamba “kutumia pesa kuwasaidia wengine hufanya mtu awe na furaha zaidi kuliko kutumia pesa kujinufaisha mwenyewe.”
UNA MAONI GANI? Je, unaweza kutumaini ushauri wa kitiba kutoka katika kitabu kilichoandikwa karibu miaka 2,000 iliyopita? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?
[Blabu katika ukurasa wa 8
“Ninavutiwa sana na Biblia . . . kwa sababu ina ushauri mzuri wa kitiba.”—HOWARD KELLY, M.D., MMOJA WA WAANZILISHI WA KITENGO CHA KITIBA KATIKA CHUO KIKUU CHA THE JOHNS HOPKINS
-
-
“Uzima wa Milele Ndio Huu”Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
-
-
“Uzima wa Milele Ndio Huu”
“Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—YOHANA 17:3.
UJUZI unaweza kuokoa uhai. Nouhou mwenye umri wa miezi kumi alipougua, mama yake, ambaye ni mhudumu wa afya nchini Niger, alijua hatua aliyopaswa kuchukua. Alimtayarishia mwana wake kinywaji kwa kuchanganya maji safi, sukari, na chumvi. Kulingana na Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa (UNICEF), kwa sababu ya “hatua hiyo ya haraka aliyochukua, mtoto wake alipona mara moja.”
Pia, ujuzi wa Biblia unaweza kuokoa uhai wa watu. Musa, mwandikaji wa kwanza wa Biblia, alisema hivi: “Si neno lisilo na thamani kwenu, bali linamaanisha uhai wenu, na kwa neno hili mnaweza kurefusha siku zenu.” (Kumbukumbu la Torati 32:47) Je, kweli Biblia inaweza kurefusha siku zetu? Inawezaje kumaanisha uhai kwetu?
Makala tano zilizotangulia katika mfululizo huu zimeonyesha kwamba Biblia ni kitabu ambacho hakiwezi kufananishwa na kitabu kingine chochote kwa sababu ya unabii wenye kutegemeka, usahihi wa kihistoria na kisayansi, upatano wa vitabu vyake, na mwongozo unaofaa. Mambo hayo yanathibitisha kwamba Biblia ni kitabu cha kipekee. Hivyo basi, Biblia inapotaja kwamba inaweza kukuelekeza katika njia ya kupata maisha marefu, yaani, uzima wa milele, je, hupaswi kuichunguza kwa makini?
Tunakutia moyo ujifunze jinsi ujuzi sahihi wa Biblia unavyoweza kufanya uwe na amani ya akili sasa na furaha ya kudumu wakati ujao. Mashahidi wa Yehova watafurahia kukuonyesha jinsi unavyoweza kupata ujuzi huo sahihi.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Biblia ni kitabu cha kipekee kwa sababu hakuna kitabu kingine kinachotoa majibu yenye kuridhisha kwa maswali muhimu tunayojiuliza kama vile:
• Ni nini kusudi la maisha?
• Kwa nini wanadamu wanateseka sana?
• Je, kuna tumaini kwa wapendwa wangu waliokufa?
Unaweza kupata majibu yanayotegemea Biblia katika kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-