Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kuandaa Fasihi kwa Ajili ya Wanafunzi wa Biblia wa Ramaniema

      Mojawapo makala za kwanza kuandikwa na C. T. Russell ilitangazwa katika 1876, katika Bible Examiner, kilichohaririwa na George Storrs wa Brooklyn, New York. Baada ya Ndugu Russell kushirikiana na N. H. Barbour wa Rochester, New York, Russell aliandaa fedha kwa ajili ya kuchapwa kwa kitabu Three Worlds na gazeti lililoitwa Herald of the Morning. Yeye alitumikia akiwa mhariri-msaidizi wa gazeti hilo na, katika 1877, alitumia vifaa vya Herald ili kuchapa kijitabu The Object and Manner of Our Lord’s Return. Ndugu Russell alithamini sana mambo ya kiroho na pia ya kibiashara, lakini ni Barbour aliyekuwa na ujuzi wa kupanga chapa na kutunga.

      Hata hivyo, Barbour alipokataa thamani ya kulipia dhambi ya dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, Ndugu Russell alikatiza uhusiano naye. Kwa hiyo, katika 1879 wakati Russell alipoanza kuchapa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, alilazimika kutegemea wachapaji wa kibiashara.

      Mwaka uliofuata, trakti za kwanza kati ya mfululizo mwingi wa trakti zilizobuniwa ili kuwavutia watu na kweli za Biblia zilitayarishwa ili zichapwe. Upesi kazi hiyo ikawa ya kadiri kubwa. Ili kuishughulikia, Zion’s Watch Tower Tract Society ilifanyizwa mnamo Februari 16, 1881, W. H. Conley akiwa msimamizi na C. T. Russell akiwa katibu na mweka-hazina. Mipango ilifanywa ili mashirika ya kibiashara yaweze kuchapa katika majiji mbalimbali ya Pennsylvania, New York, na Ohio, kutia na Uingereza. Katika 1884, Zion’s Watch Tower Tract Societya ilianzishwa kihalali, C. T. Russell akiwa msimamizi, na mkataba wayo ulionyesha kwamba ilikuwa sosaiti ambayo ingefanya zaidi ya kuelekeza uchapaji. Kusudi layo halisi lilikuwa la kidini; lilianzishwa “ili kueneza Kweli za Biblia katika lugha mbalimbali.”

      Kusudi hilo lilifuatiliwa kwa bidii iliyoje, Katika 1881, katika muda wa miezi minne, trakti 1,200,000 zenye jumla ya kurasa 200,000,000 zilichapwa. (“Trakti” nyingi zilikuwa hasa kwa namna ya vitabu vidogo.) Baadaye, kutokezwa kwa trakti za Biblia kwa ajili ya kugawanywa bure kuliongezeka kufikia makumi ya mamilioni mwaka baada ya mwaka. Trakti hizo zilichapwa katika lugha 30 na kugawanywa si katika Amerika tu, bali pia katika Ulaya, Afrika Kusini, Australia, na nchi nyinginezo.

      Jambo jingine la kazi hiyo lilianza katika 1886, wakati Ndugu Russell alipomaliza kuandika kitabu The Divine Plan of the Ages, buku la kwanza kati ya mfululizo wa mabuku sita ambayo yeye binafsi aliandika. Kuhusiana na kutangazwa kwa mabuku ya kwanza manne katika mfululizo huo (1886-1897), pamoja na trakti na Watch Tower kuanzia 1887 hadi 1898, alitumia Tower Publishing Company.b Baadaye, kupanga chapa na kutunga kulifanywa na akina ndugu kwenye Bible House katika Pittsburgh. Ili kupunguza gharama, walinunua karatasi ya kuchapa pia. Mara nyingi Ndugu Russell alipeleka maagizo kwa mashirika zaidi ya moja ili hasa yachape na kujalidi. Alipanga kwa uangalifu, akiagiza kimbele vitabu vingi vya kutosha ili avipate kwa bei ya chini. Kuanzia wakati wa kuchapwa kwa kitabu cha kwanza kilichoandikwa na C. T. Russell kufikia 1916, mabuku sita yaliyojumlika kuwa 9,384,000 yalitokezwa na kugawanywa.

      Kuchapa fasihi za Biblia hakukukoma baada ya kifo cha Ndugu Russell. Mwaka uliofuata, buku la saba la Studies in the Scriptures lilichapwa. Lilitolewa kwa familia ya Betheli mnamo Julai 17, 1917. Uhitaji wacho ulikuwa mwingi sana hivi kwamba kufikia mwisho wa mwaka huo, Sosaiti ilikuwa imetoa maagizo ya nakala 850,000 katika Kiingereza na wachapaji na wajalidi wa kibiashara. Chapa katika lugha nyinginezo zilikuwa zikitolewa katika Ulaya. Kwa kuongezea, mwaka huo trakti karibu milioni 38 zilichapwa.

      Lakini, wakati wa kipindi cha mnyanyaso mwingi katika 1918, huku maofisa wa Sosaiti wakiwa wamefungwa isivyo haki, makao yao makuu (yaliyoko Brooklyn, New York) yalibomolewa. Mabamba ya kuchapia yaliharibiwa. Wafanyakazi waliopungua sana walihamisha ofisi kurudi Pittsburgh kwenye orofa ya tatu ya jengo moja katika 119 Federal Street. Je, hilo lingewazuia kutokeza fasihi za Biblia?

      Je, Wapaswa Wafanye Uchapaji Wao Wenyewe?

      Baada ya kuachiliwa kwa msimamizi wa Sosaiti, J. F. Rutherford, na washiriki wake kutoka gerezani, Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika Cedar Point, Ohio, katika 1919. Walifikiria yale ambayo Mungu alikuwa ameruhusu yatukie wakati wa mwaka uliotangulia na yale ambayo Neno lake lilionyesha kwamba wanapaswa kuwa wakifanya wakati wa siku zilizokuwa mbele. Tangazo lilitolewa kwamba gazeti jipya, The Golden Age, lingechapwa likiwa chombo cha kutumia katika kuelekeza watu kwa Ufalme wa Mungu ukiwa tumaini pekee la wanadamu.

      Kama ilivyokuwa imefanya zamani, Sosaiti ilipanga ili mashirika ya kibiashara yachape. Lakini nyakati zilikuwa zimebadilika. Kulikuwa na matatizo ya wafanyakazi katika shughuli ya uchapaji na matatizo katika soko la karatasi. Mpango wenye kutegemeka zaidi ulihitajiwa. Ndugu walisali juu ya jambo hilo na wakawa macho kuona maelekezo ya Bwana.

      Kwanza, wangepaswa waweke wapi ofisi za Sosaiti? Je, wangepaswa kuhamisha makao makuu kurudi Brooklyn? Baraza la waelekezi la Sosaiti ilifikiria juu ya jambo hilo, na halmashauri iliteuliwa ili ichunguze hali hiyo.

      Ndugu Rutherford aliagiza C. A. Wise, makamu wa msimamizi wa Sosaiti, aende Brooklyn aone kama Betheli ingefunguliwa tena na kukodisha mahali ambapo Sosaiti ingeanza shughuli za uchapaji. Akiwa na tamaa ya kujua ni mwendo upi Mungu angebariki, Ndugu Rutherford alisema: “Nenda ukaone ikiwa ni mapenzi ya Bwana turudi Brooklyn.”

      “Nitajuaje ikiwa ni mapenzi ya Bwana tuweze kurudi au la?” akauliza Ndugu Wise.

      “Kushindwa kupata makaa-mawe katika 1918 ndiko kulikotulazimisha tuhame kutoka Brooklyn turudi Pittsburgh,”c Ndugu Rutherford akajibu. “Acha tufanye makaa-mawe yawe ndiyo jaribio. Wewe nenda ukaagize makaa-mawe.”

      “Unafikiri ninapaswa kuagiza tani ngapi ili kufanya jaribio hilo?”

      “Lifanye liwe jaribio linalofaa,” Ndugu Rutherford akapendekeza. “Agiza tani 500.”

      Hivyo ndivyo Ndugu Wise alivyofanya barabara. Na tokeo lilikuwa nini? Alipopeleka maombi kwa wenye mamlaka, alipewa hati ya kupata makaa-mawe tani 500—ya kutosha kutimiza mahitaji yao kwa miaka kadhaa! Lakini wangeiweka wapi? Sehemu kubwa za orofa ya chini ya Kao la Betheli ziligeuzwa kuwa maghala ya makaa-mawe.

      Matokeo ya jaribio hilo yalichukuliwa kuwa ishara ya mapenzi ya Mungu. Kufikia mwanzo wa Oktoba 1919, kwa mara nyingine tena walikuwa wakianza kuendeleza utendaji wao wakiwa Brooklyn.

      Sasa, je, wanapaswa wafanye uchapaji wao wenyewe? Walijitahidi kununua matbaa-mabamba-mviringo ya kuchapa magazeti lakini waliambiwa kwamba kulikuwa na chache tu katika Marekani na kwamba kulikuwa hakuna uwezekano wa kupata moja kwa miezi mingi. Hata hivyo, walikuwa na uhakika kwamba ikiwa yalikuwa mapenzi ya Bwana, angeweza kufungua njia. Na alifanya hivyo!

      Miezi michache tu baada ya wao kurudi Brooklyn, waliweza kununua matbaa-mabamba-mviringo. Walikodisha orofa tatu katika jengo moja lililokuwa umbali wa majengo manane kutoka Kao la Betheli, kwenye 35 Myrtle Avenue. Kufikia mapema 1920 Sosaiti ilikuwa na kiwanda chayo cha kuchapisha—kidogo, lakini chenye vifaa vingi. Ndugu waliokuwa na ujuzi wa kutosha kuendesha vifaa hivyo walijitoa wenyewe ili kusaidia katika kazi hiyo.

      Toleo la Februari 1 la The Watch Tower mwaka huo lilichapwa kwa matbaa ya Sosaiti. Kufikia Aprili, The Golden Age pia lilikuwa likitolewa kwa matbaa yao wenyewe. Kufikia mwisho wa mwaka huo, ilikuwa furaha kwa The Watch Tower kuripoti: “Wakati wa sehemu kubwa ya mwaka kazi yote ya THE WATCH TOWER, THE GOLDEN AGE, na vijitabu vingi, ilikuwa imefanywa na mikono iliyojitakasa, lakini kusudi moja ndilo lililoelekeza vitendo vyao, na kusudi hilo ni kumpenda Bwana na kusudi lake la uadilifu. . . . Majarida mengine na vichapo yalipotakiwa kukoma kwa sababu ya upungufu wa karatasi au matatizo ya wafanyakazi, vichapo vyetu viliendelea kutokezwa bila tatizo.”

      Nafasi kwenye kiwanda ilikuwa ndogo sana, lakini kiasi cha kazi kilichofanywa kilistaajabisha. Kiasi cha The Watch Tower kilichochapwa kilikuwa nakala 60,000 kwa kila toleo. Lakini The Golden Age lilichapwa huko pia, na katika mwaka wa kwanza, toleo la Septemba 29 lilikuwa la pekee. Lilikuwa na habari nyingi juu ya kufunuliwa kwa wachochezi wa mnyanyaso dhidi ya Wanafunzi wa Biblia kuanzia 1917 hadi 1920. Nakala milioni nne zilichapwa! Mmojawapo wafanyakazi wa matbaa ya kiwanda alisema hivi baadaye: ‘Kila mtu isipokuwa mpishi alitumikia ili kutokeza toleo hilo.’

      Katika mwaka wao wa kwanza wa kutumia matbaa-mabamba-mviringo ya kuchapa magazeti, Ndugu Rutherford aliomba akina ndugu ikiwa wangeweza pia kuchapa vijitabu kwa matbaa hiyo. Mwanzoni, haikuonekana kuwa yawezekana. Wafanyakazi wa matbaa hiyo walisema kwamba haingewezekana. Lakini akina ndugu walijaribu na wakapata matokeo mazuri. Pia walifanyiza mashine yao wenyewe ya kukunja na hivyo wakapunguza uhitaji wa wafanyakazi katika sehemu hiyo ya kazi kutoka 12 hadi 2. Ni nini kilichowafanikisha? “Ujuzi na baraka ya Bwana” ndivyo msimamizi wa kiwanda alivyokata kauli.

      Hata hivyo, haikuwa katika Brooklyn pekee kwamba Sosaiti ilikuwa ikianzisha shughuli za uchapaji. Baadhi za shughuli za uchapaji katika lugha za kigeni zilisimamiwa na ofisi katika Michigan. Ili kushughulikia mahitaji yaliyohusiana na kazi hiyo, Sosaiti ilipeleka mashine ya Linotaipu, matbaa za kuchapa, na vifaa vingine vilivyohitajika katika Detroit, Michigan katika 1921. Huko fasihi zilichapwa katika Kipoland, Kirusi, Kiukrainia, na lugha nyinginezo.

      Katika mwaka uo huo, Sosaiti ilitoa kitabu The Harp of God, kilichoandikwa kwa njia inayofaa wale wanaoanza kujifunza Biblia. Kufikia 1921 Sosaiti haikuwa imejaribu kuchapa na kujalidi vitabu vyayo yenyewe. Je, wangepaswa kujitahidi kuanza kazi hiyo pia? Kwa mara nyingine, walitafuta mwelekezo wa Bwana.

      Ndugu Waliojitoa Wachapa na Kujalidi Vitabu

      Katika 1920, The Watch Tower lilikuwa limeripoti kwamba makolpota wengi walikuwa wamelazimika kuacha utumishi huo kwa sababu wachapaji na wajalidi wa vitabu walishindwa kufanyiza vitabu vilivyoagizwa na Sosaiti. Akina ndugu kwenye makao makuu walitoa sababu kwamba ikiwa hawangewategemea watengenezaji wa kibiashara wenye matatizo mengi ya kazi, wangetimiza ushahidi mwingi zaidi kuhusu makusudi ya Mungu kwa wanadamu. Ikiwa wangechapa na kujalidi vitabu vyao wenyewe, ingekuwa pia vigumu zaidi kwa wapinzani kuingilia kazi hiyo. Na baadaye walitumaini wangeweza kupunguza gharama ya kuchapa mabuku na hivyo waweze kuyafanya yapatikane kwa urahisi zaidi kwa umma.

      Lakini hilo lingetaka nafasi na vifaa vingi zaidi, na wangelazimika kujifunza stadi mpya. Je, wangeweza kufanya hivyo? Robert J. Martin, mwangalizi wa kiwanda, alikumbuka kwamba katika siku za Musa, Yehova alikuwa ‘amewajaza Bezaleli na Oholiabu hekima ya moyoni ili waifanye kazi yote’ iliyohitajiwa katika kujenga tabenakulo takatifu. (Kut. 35:30-35) Akiwa na simulizi hilo la Biblia akilini, Ndugu Martin alikuwa na uhakika kwamba Yehova angeweza pia kufanya chochote kilichohitajiwa ili kwamba watumishi wake waweze kuchapa fasihi ili wautangaze Ufalme.

      Baada ya kutafakari kwingi na sala nyingi, mipango hususa ilianza kutokea. Akitazama nyuma kwa yale yaliyotokea, Ndugu Martin alimwandikia Ndugu Rutherford baadaye hivi: “Siku iliyo kuu kupita zote ilikuwa ile siku ulipotaka kujua ikiwa kulikuwa na sababu yoyote nzuri kwa nini sisi hatupaswi kuchapa na kujalidi vitabu vyetu vyote. Lilikuwa wazo la kusisimua, kwa sababu lilimaanisha kufunguliwa kwa kiwanda kamili cha kupanga chapa, kupakaza kwa umeme, kuchapa na kujalidi, ikihitaji kuendesha mashine nyingi tusizofahamu, sanasana mashine ambazo hatukujua zilikuwako, na uhitaji wa kujifunza stadi nyingi. Lakini hiyo ilionekana kuwa ndiyo njia bora zaidi ya kupunguza gharama ya vitabu baada ya ile vita.

      “Ulikodisha jengo la orofa sita kwenye barabara ya 18 Concord Street (kukiwa na wakazi katika orofa mbili); na mnamo Machi 1, 1922, tukahamia humo. Ulitununulia mashine kamili za kupanga chapa, kupakaza kwa umeme, kuchapa na kujalidi, nyingi zazo zikiwa mpya, baadhi yazo zikiwa zimetumiwa; na tukaanza kazi.

      “Mojawapo kiwanda kikubwa cha uchapaji kilichokuwa kimekuwa kikifanya sehemu kubwa ya kazi yetu kilisikia yale tuliyokuwa tukifanya na msimamizi wa kiwanda hicho akaja, ili kutuzuru. Aliona vifaa vipya na akasema hivi kwa uzito, ‘Hapa mna kiwanda cha uchapaji kilicho bora zaidi, na hakuna yeyote katika kiwanda anayejua jinsi ya kukiendesha. Katika miezi sita kiwanda chote cha uchapaji kitakuwa takataka; na mtagundua kwamba watu wanaostahili kuwachapia ni wale ambao sikuzote wamekuwa wakiwachapia, wakiifanya iwe shughuli yao.’

      “Hilo lilisikika kuwa jambo la akili vya kutosha, lakini lilisahau Bwana; na sikuzote amekuwa pamoja nasi. Ujalidi ulipoanza alimtuma ndugu ambaye ametumia maisha yake yote katika shughuli ya ujalidi. Alikuwa msaada mkubwa wakati alipohitajiwa zaidi. Kwa msaada wake, na roho ya Bwana ikitenda kazi miongoni mwa ndugu waliokuwa wakijaribu kujifunza, upesi tulianza kufanyiza vitabu.”

      Kwa kuwa kiwanda kwenye barabara ya Concord Street kilikuwa na nafasi kubwa, shughuli za uchapaji kutoka Detroit ziliunganishwa na zile za Brooklyn. Kufikia mwaka wa pili katika sehemu hiyo, ndugu walikuwa wakifanyiza asilimia 70 ya vitabu na vijitabu vilivyohitajiwa, kutia na magazeti, trakti, na vikaratasi vya ukaribishaji. Mwaka uliofuata, walilazimika kutumia orofa mbili zilizobaki za kiwanda kwa sababu ya ukuzi wa kazi.

      Je, wangeweza kuongeza mwendo wa kutokeza vitabu? Matbaa ya kuchapia ilitengenezwa katika Ujerumani, ikasafirishwa kwa meli hadi Amerika, na kuanza kufanya kazi katika 1926 hasa kwa kusudi hilo. Kwa kadiri walivyojua, matbaa hiyo ya kuchapa ndiyo iliyokuwa ya aina yake ya kwanza kutumiwa katika Amerika ili kuchapa vitabu.

      Hata hivyo, shughuli zote za uchapaji za Wanafunzi wa Biblia hazikuwa katika Amerika pekee.

      Shughuli za Uchapaji za Ramaniema Katika Nchi Nyinginezo

      Akitumia mashirika ya kibiashara, Ndugu Russell alikuwa amefanya uchapaji katika Uingereza mapema kama 1881. Hilo lilikuwa likifanywa katika Ujerumani kufikia 1903, Ugiriki kufikia 1906, Finland kufikia 1910, na hata Japani kufikia 1913. Wakati wa miaka iliyofuata vita ya ulimwengu ya kwanza, kiasi kikubwa cha uchapaji huo—wa vitabu, vijitabu, magazeti, na trakti—kilifanywa katika Uingereza, nchi za Skandinavia, Ujerumani, na Poland, na mwingine ulifanywa katika Brazili na India.

      Kisha, katika 1920, mwaka uleule ambao Sosaiti ilianza kufanya uchapaji wayo yenyewe wa magazeti katika Brooklyn, mipango ilifanywa ili ndugu zetu pia katika Ulaya wafanye kiasi cha kazi hiyo. Kikundi kimoja katika Uswisi kilianzisha kiwanda cha uchapaji katika Bern. Hilo lilikuwa shirika lao wenyewe la biashara. Lakini wote walikuwa Wanafunzi wa Biblia, na walitokeza fasihi za Sosaiti katika lugha za Ulaya kwa gharama ya chini sana. Baadaye, Sosaiti ilipata umiliki wa kiwanda hicho cha uchapaji na ikakipanua. Ili kujazia uhitaji wa haraka katika nchi za Ulaya zilizodhoofika kiuchumi wakati huo, kiasi kikubwa sana cha fasihi za bure kilitokezwa huko. Wakati wa miaka ya mwisho ya 1920, vichapo katika lugha nyingi vilisafirishwa kutoka kwa kiwanda hicho.

      Wakati uleule, kupendezwa kwingi katika ujumbe wa Ufalme kulikuwa kukionyeshwa katika Rumania. Kujapokuwa na upinzani mwingi kwa kazi yetu huko, Sosaiti ilianzisha kiwanda cha kuchapa katika Cluj, ili kupunguza gharama za fasihi na kuifanya ipatikane kwa urahisi zaidi kwa watu wenye njaa ya kweli katika Rumania na nchi zilizo karibu. Katika 1924 kiwanda hicho kiliweza kutokeza vitabu vilivyojalidiwa karibu robo milioni, kwa kuongezea magazeti na vijitabu, katika Kirumania na Kihungaria. Lakini yule aliyesimamia kazi huko alithibitika kuwa asiye mwaminifu kwa amana yake na akafanya vitendo vilivyotokeza kupotea kwa mali na vifaa vya Sosaiti. Kujapokuwa hayo, ndugu waaminifu katika Rumania waliendelea kufanya yote waliyoweza ili kushiriki kweli za Biblia na wengine.

      Katika Ujerumani kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, idadi kubwa ya watu walikuwa wakimiminika kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Lakini Wajerumani walikuwa wakipata taabu kubwa ya kiuchumi. Ili kupunguza gharama ya fasihi za Biblia kwa manufaa yao, Sosaiti ilisitawisha kazi ya uchapaji yayo yenyewe huko pia. Katika Barmen, mwaka 1922, uchapaji ulifanywa kwa kutumia matbaa-tambarare kwenye sehemu ya ngazi katika Kao la Betheli na kwenye nyingine katika kibanda cha mbao. Mwaka uliofuata akina ndugu walihamia Magdeburg kwenye vifaa bora zaidi. Walikuwa na majengo mazuri huko, mengine yaliongezwa, na vifaa vya kuchapa na kujalidi vitabu vikawekwa. Kufikia mwisho wa 1925, iliripotiwa kwamba uwezo wa kutokeza vitabu wa kiwanda hicho ungekuwa mkubwa angalau kama ule uliotumiwa kwenye makao makuu katika Brooklyn.

      Uchapaji mwingi uliofanywa hasa na akina ndugu ulianza kwa kiwango kidogo. Ilikuwa hivyo katika Korea, ambako katika 1922 Sosaiti ilianzisha kiwanda kidogo cha kuchapa chenye vifaa vya kutokeza fasihi katika Kikorea na pia Kijapani na Kichina. Baada ya miaka michache, vifaa hivyo vilihamishiwa Japani.

      Kufikia 1924 kuchapwa kwa vitu vidogo kulifanywa pia katika Kanada na katika Afrika Kusini. Katika 1925 matbaa ndogo ilianzishwa katika Australia na nyingine katika Brazili. Upesi ndugu katika Brazili walikuwa wakitumia vifaa vyao kuchapa The Watch Tower kwa Kireno. Tawi la Sosaiti katika Uingereza lilipata kifaa chayo cha kwanza cha kuchapia katika 1926. Katika 1929 njaa ya kiroho ya watu wanyenyekevu katika Hispania ilikuwa ikitoshelezwa kwa kuchapwa kwa The Watch Tower katika matbaa ndogo huko. Miaka miwili baadaye matbaa ilianza kuendeshwa katika orofa ya chini ya ofisi ya tawi katika Finland.

      Wakati uo huo, upanuzi ulikuwa ukiendelea kwenye makao makuu ya ulimwenguni.

      Kiwanda Chao Wenyewe Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu

      Tangu 1920 Sosaiti ilikuwa ikikodiwa nafasi ya kiwanda katika Brooklyn. Hata jengo lililotumiwa kuanzia 1922 na kuendelea halikuwa katika hali nzuri; jengo zima lingetikisika sana wakati matbaa-mabamba-mviringo ilipokuwa ikiendeshwa katika orofa ya chini. Isitoshe, nafasi zaidi ilihitajiwa ili kushughulikia kazi iliyokuwa ikikua. Ndugu walitoa sababu kwamba fedha zilizopatikana zingeweza kutumiwa vyema zaidi ikiwa wangekuwa na kiwanda chao wenyewe.

      Eneo fulani lililokuwa karibu na Kao la Betheli lilionekana kuwa sehemu inayofaa sana, kwa hiyo wakashindania bei yalo. Matokeo yakawa, Shirika la Madawa la Squibb liliwashinda kwa kutoa fedha nyingi zaidi; lakini walipojenga kwenye eneo hilo, walilazimika kushindilia mabamba 1,167 ya saruji ili kuwa na msingi imara. (Miaka mingi baadaye, Watch Tower Society ilinunua majengo hayo kutoka kwa Squibb, yakiwa tayari na ule msingi mzuri!) Hata hivyo, sehemu ambayo Sosaiti ilinunua katika 1926 ilikuwa na udongo unaoweza kustahimili uzito uliofaa kujengea.

      Katika Februari 1927 walihamia kwenye jengo lao jipya kabisa kwenye barabara ya 117 Adams Street katika Brooklyn. Liliwaandalia karibu nafasi mara mbili zaidi ya ile waliyokuwa wakitumia kufikia wakati huo. Lilijengwa vizuri, kazi ikianzia kutoka orofa za juu kuelekea chini kwenye idara mbalimbali hadi ilipofika Idara ya Usafirishaji kwenye orofa ya chini.

      Hata hivyo, ukuzi haukuwa umekamilika. Katika muda wa miaka kumi ilibidi kiwanda hicho kipanuliwe; na upanuzi zaidi ungefuata baadaye. Zaidi ya kuchapa mamilioni ya nakala za magazeti na vijitabu kila mwaka, kiwanda kilikuwa kikitokeza vitabu vilivyojalidiwa vipatavyo 10,000 kila siku. Biblia zilizokamilishwa zilipotiwa miongoni mwa vitabu hivyo katika 1942, Watch Tower Society ilikuwa mbele katika uwanja mpya wa shughuli ya uchapaji. Ndugu walijaribujaribu hadi walipoweza kuchapa karatasi nyepesi ya Biblia kwenye matbaa-mabamba-mviringo—jambo ambalo wachapaji wengine hawakujaribu hadi miaka mingi baadaye.

      Wakati ambapo kutokeza vitabu vingi kulikuwa kukiendelea, vikundi vyenye mahitaji ya pekee havikukosa kushughulikiwa. Mapema kama 1910, Mwanafunzi wa Biblia katika Boston, Massachusetts, na mwingine katika Kanada walikuwa wakishirikiana ili kutokeza tena fasihi za Sosaiti katika Braille (chapa kwa ajili ya vipofu). Kufikia 1924, kutoka kwa ofisi katika Logansport, Indiana, Sosaiti ilikuwa ikitokeza vichapo ili kunufaisha vipofu. Hata hivyo, kwa sababu ya itikio dogo sana wakati huo, kazi ya Braille ilikomeshwa katika 1936, na mkazo ukatiwa kwenye kuwasaidia vipofu kwa njia ya rekodi za vinanda pamoja na uangalifu wa kibinafsi. Baadaye, katika 1960, fasihi za Braille zilianza tena kutokezwa—wakati huu katika unamnanamna mwingi zaidi, na kwa itikio bora zaidi hatua kwa hatua.

  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 585]

      ‘Uthibitisho wa Roho ya Yehova’

      “Kuchapwa kwa vitabu na Biblia kwa mafanikio kwenye matbaa-mabamba-mviringo na watu wasio na ujuzi [na katika wakati ambao wengine hawakuwa ­wakichapa bado] ni uthibitisho wa usimamizi wa Yehova na uelekezo wa roho yake,” akasema Charles Fekel. Ndugu Fekel alijua vema yale yaliyohusika, kwa kuwa alikuwa ameshiriki katika usitawishaji wa shughuli za kuchapa kwenye makao makuu ya Sosaiti kwa zaidi ya nusu karne. Katika miaka yake ya baadaye, alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

      [Picha]

      Charles Fekel

  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 581]

      Kupanga Chapa

      Mwanzoni yote yalifanywa kwa mkono, herufi mojamoja

      Afrika Kusini

      Kuanzia 1920 hadi miaka ya 1980, mashine za Linotaipu zilitumiwa

      Marekani

  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 582]

      Kutengeneza Mabamba

      Kuanzia miaka ya 1920 hadi ya 1980, mabamba ya chuma cha risasi yalitengenezwa kwa ajili ya kuchapa kwa matbaa ya maandishi yaliyoinuliwa

      [Picha]

      1. Mistari ya maandishi ya kurasa za habari iliyochapwa ilitiwa katika fremu za chuma ziitwazo viunzi

      2. Chini ya kani-eneo, alama ya maandishi ilifanywa kwenye chombo ambacho kingeweza kutumiwa kuwa mfinyango

      3. Chuma moto cha risasi kilimwagwa kwenye mfinyango ili kufanyiza mabamba ya chuma ya kuchapa

      4. Chuma kisichotakiwa kiliondolewa kwenye bamba

      5. Mabamba yalitiwa nikeli ili yaweze kudumu

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki