Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Sosaiti Yenye Kuchapa Biblia

      Ilikuwa katika 1896 kwamba rejezeo la moja kwa moja kwenye Biblia lilitiwa rasmi katika jina la shirika halali lililokuwa likitumiwa wakati huo na Wanafunzi wa Biblia katika kazi yao ya kuchapa. Wakati huo Zion’s Watch Tower Tract Society ilikuja kuitwa kihalali Watch Tower Bible and Tract Society.a Sosaiti haikuwa mchapaji na mjalidi wa Biblia mara hiyo, lakini ilikuwa mtangazaji wazo mwenye bidii, ikipanga mambo mengi hususa, ikiandaa mambo ya ziada yenye thamani, na kisha kupanga na mashirika ya kibiashara ili yazichape na kuzijalidi.

      Hata kabla ya 1896, Sosaiti ilikuwa ikifanya mengi ikiwa mgawanyaji wa Biblia. Ilivuta fikira kwenye tafsiri mbalimbali za Biblia zilizopatikana, ikazinunua kwa wingi ili iweze kuzipata kwa bei nafuu, na kisha ikaziuza kwa bei ambayo nyakati nyingine ilikuwa asilimia 35 tu ya ile bei ya kawaida, si ili ipate faida ya kibiashara bali ili itoe utumishi kwa wasomaji wayo. Miongoni mwa Biblia hizo kulikuwa na chapa nyingi za King James Version zilizokuwa rahisi kubeba na kutumia, pia ‘Biblia za Walimu’ (King James Version ikiwa na misaada kama konkodansi, ramani, na marejezo ya pambizoni) zilizokuwa kubwa zaidi, The Emphatic Diaglott ikiwa na fasili ya mstari kati ya mstari wa Kigiriki na Kiingereza, tafsiri ya Leeser iliyotia maandiko ya Kiingereza kando ya yale ya Kiebrania, tafsiri ya Murdock kutoka Siria ya kale, The Newberry Bible yenye marejezo ya pambizoni yaliyoelekeza fikira kwenye sehemu ambazo jina la kimungu lilitokea katika lugha ya awali pamoja na mambo mengi yenye thamani yaliyoonyeshwa katika maandiko ya Kiebrania na Kigiriki, New Testament ya Tischendorf yenye marejezo ya vielezi-chini yaliyoonyesha maelezo tofauti-tofauti katika hati tatu kati ya zile za Biblia ya Kigiriki ya kale zilizo kamili zaidi (Sinaitic, Vatican, na Alexandrine), Biblia ya Variorum yenye vielezi-chini vilivyoonyesha si maandishi tofauti ya hati za kale tu bali pia tafsiri mbalimbali za sehemu za maandiko za wanachuo mashuhuri, na tafsiri halisi ya Young. Sosaiti pia ilitoa misaada kama vile Cruden’s Concordance na Analytical Concordance ya Young yenye maelezo juu ya maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki. Katika miaka iliyofuata, mara nyingi Mashahidi wa Yehova duniani pote walipata maelfu mengi ya Biblia kutoka kwa sosaiti za Biblia katika lugha zozote zilizopatikana na wakazigawanya.

      Mapema kama 1890, kulingana na ithibati inayopatikana, Sosaiti ilipanga kuwa na uchapaji wa pekee, wenye jina layo, wa Chapa ya Pili ya The New Testament Newly Translated and Critically Emphasised, kama ilivyotayarishwa na mtafsiri wa Biblia Mwingereza Joseph B. Rotherham. Kwa nini tafsiri hiyo? Kwa sababu ya uhalisi wayo na jitihada yayo ya kunufaika kikamili na utafiti uliokuwa umefanywa ili kuwa na maandiko ya Kigiriki yaliyo sahihi zaidi na kwa sababu msomaji alisaidiwa na alama zilizotumiwa na mtafsiri ili kutambulisha ni maneno au semi gani zilizokaziwa kipekee katika maandiko ya Kigiriki.

      Katika 1902 uchapaji wa pekee wa Chapa ya Mistari Sambamba ya Biblia ya Holman ulifanywa kwa mpango wa Watch Tower Society. Ilikuwa na pambizo zilizo pana ambazo ndani yazo kulichapwa marejezo ya mahali katika vichapo vya Watch Tower ambapo mistari mbalimbali ilielezwa, na pia ilikuwa na faharisi ikiorodhesha vichwa vingi vya habari pamoja na mitajo ya Maandiko na marejezo yenye msaada kwenye vichapo vya Sosaiti. Biblia hiyo ilikuwa na maneno ya tafsiri mbili—tafsiri ya King James ikiwa juu ya ile ya Revised Version mahali palipokuwa na tofauti yoyote. Pia ilitia ndani konkodansi yenye kutia mambo mengi iliyofahamisha mtumizi maana mbalimbali za maneno ya lugha ya awali.

      Mwaka uo huo, Watch Tower Society ilimiliki mabamba ya kuchapia ya The Emphatic Diaglott, yanayotia ndani maandiko ya Kigiriki ya J. J. Griesbach ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (chapa ya 1796-1806) pamoja na tafsiri ya Kiingereza ya mistari kati ya mistari. Pamoja na hiyo kulikuwa na fasili ya maandiko ya Benjamin Wilson mzaliwa wa Uingereza, aliyekuwa akiishi Geneva, Illinois, Marekani. Mabamba hayo na haki ya kuwa wachapaji pekee yalikuwa yamenunuliwa na kisha Sosaiti ikapewa kuwa zawadi. Baada ya nakala ambazo tayari zilikuwa katika akiba kuweza kupelekewa watu, mipango ilifanywa na Sosaiti ili nakala zaidi zitokezwe, na hizo zilipatikana katika 1903.

      Miaka minne baadaye, katika 1907, Chapa ya Wanafunzi wa Biblia ya King James Version ilichapwa. “Kitabu cha Walimu wa Biblia Waberoya” kilijalidiwa pamoja nayo ikiwa nyongeza. Hiyo ilitia ndani maelezo hususa ya mistari kutoka sehemu zote za Biblia, pamoja na marejezo kwenye vichapo vya Watch Tower kwa ajili ya maelezo kamili zaidi. Chapa yenye nyongeza iliyopanuliwa zaidi ilichapwa mwaka mmoja hivi baadaye.

      Biblia hizo ziliagizwa kutoka kwa wachapaji na wajalidi katika vifungu vya kati ya 5,000 na 10,000 wakati mmoja, ili gharama isiwe kubwa. Sosaiti ilitamani kufanya tafsiri mbalimbali za Biblia na vifaa vya utafiti vinavyohusiana vipatikane kwa urahisi kwa watu wengi kadiri iwezekanavyo.

      Kisha katika 1926 Watch Tower Society ilichukua hatua kubwa kwenda mbele katika kuhusika kwayo katika kuchapa Biblia.

      Kuchapa Biblia Kwenye Matbaa Yetu Wenyewe

      Ilikuwa miaka 36 baada ya Watch Tower Bible and Tract Society kuanza kutangaza Biblia kwa mara ya kwanza, kwamba iliweza kuchapa na kujalidi Biblia katika kiwanda chayo yenyewe. Biblia ya kwanza kutokezwa hivyo ilikuwa The Emphatic Diaglott, ambayo mabamba yayo yalikuwa mali ya Sosaiti kwa miaka 24. Katika Desemba 1926 Biblia hiyo ilichapwa kwenye matbaa-tambarare katika kiwanda cha Sosaiti cha Concord Street katika Brooklyn. Kufikia sasa, 427,924 yazo zimetokezwa.

  • Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 604]

      Tafsiri Chache Kati ya Zile Zilizotumiwa na Wanafunzi wa Biblia wa Ramaniema

      Tafsiri halisi ya Young

      Tafsiri ya Leeser (Kiebrania kando ya Kiingereza)

      “New Testament” ya Tischendorf (yenye fasili tofauti-tofauti kutoka hati za Kigiriki MSS)

      Tafsiri ya Murdock (kutoka Kisiria)

      “The Emphatic Diaglott” (Kigiriki hadi Kiingereza)

      Variorum Bible (yenye fasili mbalimbali za Kiingereza)

      “The Newberry Bible” (yenye maandishi ya thamani pambizoni)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki