-
Usijiwekee Vizuizi—Kushinda Hisia za Kujiona HustahiliHuduma ya Ufalme—2012 | Novemba
-
-
Usijiwekee Vizuizi—Kushinda Hisia za Kujiona Hustahili
1. Kwa nini wengine husita kuanzisha funzo la Biblia?
1 Je, unasita kuanzisha funzo la Biblia kwa sababu unahisi huna uwezo wa kuongoza funzo kwa mafanikio? Nyakati nyingine watumishi waaminifu wa kale, kama Musa na Yeremia, walihisi hawakustahili kupata migawo waliyokuwa nayo. (Kut. 3:10, 11; 4:10; Yer. 1:4-6) Kwa hiyo, watu wengi huwa na hisia kama hizo. Tunawezaje kushinda hisia hizo?
2. Kwa nini tusitosheke tu kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuacha kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ifanywe na wengine?
2 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hatazamii tufanye jambo linalopita uwezo wetu. (Zab. 103:14) Hivyo basi, mgawo wetu wa “kufanya wanafunzi,” yaani “kuwafundisha,” ni kazi ambayo tunaweza kutimiza. (Mt. 28:19, 20) Si pendeleo ambalo Yehova amewapa tu wale wenye uzoefu mwingi au vipawa vya pekee miongoni mwetu. (1 Kor. 1:26, 27) Kwa hiyo, tusitosheke tu kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuacha kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ifanywe na wengine.
3. Yehova ametusaidiaje tustahili kufanya kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia?
3 Yehova Hutusaidia Tustahili: Yehova ndiye hutusaidia tustahili kufanya wanafunzi. (2 Kor. 3:5) Kupitia tengenezo lake ametufundisha kweli za Biblia ambazo hata watu wenye elimu nyingi sana katika ulimwengu huu hawazijui. (1 Kor. 2:7, 8) Amehifadhi rekodi ya njia ambazo Mwalimu Mkuu, Yesu, alitumia kufundisha ili tuweze kuzifuata, naye huendelea kutoa mazoezi kupitia kutaniko. Kwa kuongezea, Yehova ametuandalia msaada wa kufundisha Biblia. Ameandaa vifaa kama vile kitabu Biblia Inafundisha, ambacho hufundisha kweli kwa njia yenye mpangilio mzuri na inayoeleweka kwa urahisi. Huenda kuongoza funzo la Biblia kukawa rahisi kuliko tunavyofikiri.
4. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia?
4 Musa na Yeremia waliweza kutimiza migawo yao kwa msaada wa Yehova. (Kut. 4:11, 12; Yer. 1:7, 8) Sisi pia, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie. Isitoshe, tunapoongoza funzo la Biblia, tunamfundisha mtu fulani ukweli kumhusu Yehova, na jambo hilo linapendeza machoni pa Mungu. (1 Yoh. 3:22) Kwa hiyo, uwe na lengo la kushiriki katika kazi yenye kufurahisha na yenye kuthawabisha zaidi ya kuongoza mafunzo ya Biblia.
-
-
Usijiwekee Vizuizi—Kushughulika na Ratiba Yenye Mambo MengiHuduma ya Ufalme—2012 | Novemba
-
-
Usijiwekee Vizuizi—Kushughulika na Ratiba Yenye Mambo Mengi
1. Kwa nini wengine husita kuanzisha funzo la Biblia?
1 Wahubiri fulani husita kuanzisha funzo la Biblia kwa sababu wana ratiba yenye mambo mengi. Kushughulikia mahitaji ya mwanafunzi wa Biblia kunachukua wakati. Wakati unahitajika ili kujitayarisha kwa ajili ya funzo, kuliongoza, na kumsaidia mwanafunzi ashinde vizuizi anavyopata. Mtume Paulo alisema kwamba aliitoa nafsi yake ili awasaidie Wathesalonike kumjua Yehova. (1 The. 2:7, 8) Tunaweza kuongozaje funzo la Biblia hata tukiwa na ratiba yenye mambo mengi?
2. Upendo wetu kwa Yehova unaathirije jinsi tunavyotumia wakati wetu?
2 Wakati Unahitajika Ili Kumtumikia Yehova: Ukweli wa mambo ni kwamba wakati unahitajika ili kumtumikia Yehova. Kwa mfano, kwa kawaida sisi hutumia wakati kuhudhuria mikutano, kushiriki katika huduma, kusoma Biblia, na kusali. Kwa kupenda, mtu aliyefunga ndoa na mwenye mambo mengi hupanga kutumia wakati pamoja na mwenzi wake wa ndoa. Je, hatupaswi kufurahia zaidi ‘kununua wakati’ kumtumikia Yehova kwa sababu tunampenda? (Efe. 5:15-17; 1 Yoh. 5:3) Kulingana na Yesu, sehemu muhimu ya ibada yetu ni kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kutafakari jambo hilo kutatusaidia tusisite kukubali jukumu la kuongoza funzo la Biblia.
3. Tunaweza kufanya nini ili kuongoza funzo la Biblia hata wakati ambapo hali zinavuruga ratiba yetu ya utumishi wa shambani?
3 Lakini namna gani ikiwa ratiba yetu inavurugwa na kazi ya kuajiriwa, matatizo ya afya yasiyo na tiba, au migawo ya kitheokrasi? Wahubiri wengine ambao mara kwa mara hulazimika kuwa mbali na nyumbani huongoza funzo la Biblia kupitia simu au kupitia kompyuta zilizounganishwa pamoja. Wale ambao ratiba yao huvurugika kwa sababu ya matatizo ya afya yasiyo na tiba wamepanga ili mwanafunzi awatembelee nyumbani. Wengine wamefanya mipango ili mhubiri mwenye kutegemeka ajifunze na mwanafunzi wao wa Biblia wakati ambapo hawapatikani.
4. Ni baraka gani tunazopata tunaposhiriki katika kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia?
4 Paulo alipata shangwe nyingi kwa sababu alitumia wakati wake na nguvu zake kuwasaidia wengine kujifunza kweli. (Mdo. 20:35) Alipotafakari kuhusu wale wote ambao alikuwa amefanikiwa kuwasaidia huko Thesalonike, alichochewa kumshukuru Yehova. (1 The. 1:2) Tunaweza kuridhika na kuongeza shangwe yetu katika huduma iwapo hatutaruhusu ratiba yenye mambo mengi ituzuie kushiriki katika kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia.
-