Usijiwekee Vizuizi—Kushinda Hisia za Kujiona Hustahili
1. Kwa nini wengine husita kuanzisha funzo la Biblia?
1 Je, unasita kuanzisha funzo la Biblia kwa sababu unahisi huna uwezo wa kuongoza funzo kwa mafanikio? Nyakati nyingine watumishi waaminifu wa kale, kama Musa na Yeremia, walihisi hawakustahili kupata migawo waliyokuwa nayo. (Kut. 3:10, 11; 4:10; Yer. 1:4-6) Kwa hiyo, watu wengi huwa na hisia kama hizo. Tunawezaje kushinda hisia hizo?
2. Kwa nini tusitosheke tu kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuacha kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ifanywe na wengine?
2 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hatazamii tufanye jambo linalopita uwezo wetu. (Zab. 103:14) Hivyo basi, mgawo wetu wa “kufanya wanafunzi,” yaani “kuwafundisha,” ni kazi ambayo tunaweza kutimiza. (Mt. 28:19, 20) Si pendeleo ambalo Yehova amewapa tu wale wenye uzoefu mwingi au vipawa vya pekee miongoni mwetu. (1 Kor. 1:26, 27) Kwa hiyo, tusitosheke tu kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuacha kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ifanywe na wengine.
3. Yehova ametusaidiaje tustahili kufanya kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia?
3 Yehova Hutusaidia Tustahili: Yehova ndiye hutusaidia tustahili kufanya wanafunzi. (2 Kor. 3:5) Kupitia tengenezo lake ametufundisha kweli za Biblia ambazo hata watu wenye elimu nyingi sana katika ulimwengu huu hawazijui. (1 Kor. 2:7, 8) Amehifadhi rekodi ya njia ambazo Mwalimu Mkuu, Yesu, alitumia kufundisha ili tuweze kuzifuata, naye huendelea kutoa mazoezi kupitia kutaniko. Kwa kuongezea, Yehova ametuandalia msaada wa kufundisha Biblia. Ameandaa vifaa kama vile kitabu Biblia Inafundisha, ambacho hufundisha kweli kwa njia yenye mpangilio mzuri na inayoeleweka kwa urahisi. Huenda kuongoza funzo la Biblia kukawa rahisi kuliko tunavyofikiri.
4. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia?
4 Musa na Yeremia waliweza kutimiza migawo yao kwa msaada wa Yehova. (Kut. 4:11, 12; Yer. 1:7, 8) Sisi pia, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie. Isitoshe, tunapoongoza funzo la Biblia, tunamfundisha mtu fulani ukweli kumhusu Yehova, na jambo hilo linapendeza machoni pa Mungu. (1 Yoh. 3:22) Kwa hiyo, uwe na lengo la kushiriki katika kazi yenye kufurahisha na yenye kuthawabisha zaidi ya kuongoza mafunzo ya Biblia.