Uwe na Mradi wa Kuongoza Funzo la Biblia
1 “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) Maneno hayo yaliyosemwa na Yesu Kristo bila shaka yanahusu hali ambazo wahudumu Wakristo wanaziona leo.
2 Watu wenye mioyo myeupe ambao wanapenda kujifunza njia za Yehova wanaendelea kupatikana. Jambo hilo linaonekana kutokana na idadi ya wanafunzi wanaobatizwa kila mwaka. Ikiwa kwa kweli ungependa kuongoza funzo la Biblia, unaweza kufanya nini?
3 Jiwekee Mradi: Jambo la kwanza, unapaswa kuweka mradi wa kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia. Mradi huo unapaswa kuwa akilini unaposhiriki katika huduma ya shambani. Kwa kuwa kufundisha na kuhubiri ni moja ya majukumu tuliyokabidhiwa tukiwa Wakristo, tunahitaji kufanya kila kitu tunachoweza kuongeza utendaji wetu katika kazi hii ya kuongoza mafunzo ya Biblia.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
4 Mambo Mengine ya Kukumbukwa: Lazima wahubiri wa Ufalme watoe sala ya kutoka moyoni. Nyakati fulani tumekutana na watu ambao wamesali ili wapate msaada wa kiroho. Jinsi lilivyo pendeleo kutumiwa na Yehova kukutana na watu hao na kuwafundisha!—Hag. 2:7; Mdo. 10:1, 2.
5 Dada mmoja alisali ili apate funzo la Biblia na akatandaza trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? mahali anapofanyia kazi. Mwanamke mmoja alichukua trakti moja, akaisoma yote. Alipoanza kujaza kuponi, dada yetu alizungumza naye na akafanikiwa kuanzisha funzo la Biblia.
6 Wahubiri wenzako ambao wamepata matokeo mazuri katika kuongoza mafunzo ya Biblia wanaweza kukusaidia ufikie mradi wako wa kuongoza funzo la Biblia. Sali upate funzo la Biblia na utumie maandalizi yote yanayopatikana ili ufikie mradi huo. Huenda hivi karibuni utapata shangwe ya kuongoza funzo la Biblia.