Mradi Wako Maishani Ni Nini?
SIKU baada ya siku Kenichi alikuwa na wazo moja tu: ‘Kupata dhahabu iliyokuwa mahali fulani katika vilima hivi.’ Kwa miaka 35 alikuwa ameitafuta bila kuacha katika vilima hivyo nje ya mji wa kwao wa Kijapani. “Sina wakati kwa ajili ya mke wala marafiki,” ndivyo alivyokuwa akisema. Akawa mtu mpweke, mwenye kuchochewa na utafutaji wa dhahabu isiyopatikana kwa urahisi.
Halafu akiwa mwenye umri wa miaka 65 Kenichi alikipata kitu kile alichokuwa akikitafuta. Sasa alikuwa ameipata mali yake! Itikio lake lilikuwa nini baada ya kuufikia mradi wa maisha yake yote? Alisema hivi: “Hapo kwanza nilitaka tu kuwa tajiri. Lakini sasa dhahabu hii si ya maana sana.”
Pengine unafahamu ni kwa sababu gani Kenichi aliona hivyo. Ni kweli kwamba yeye alikuwa tajiri. Lakini katika kuutafuta utajiri huo alikuwa ametumia miaka 35 iliyo bora zaidi maishani mwake—miaka ambayo hangeiona tena. Mwanamume huyo asiye na rafiki aligundua kwamba kuufikia mradi wake halikuwa jambo linalostahili. Je! kumekuwa miradi maishani mwako ambayo ulijitahidi mno kuifikia, ndipo ukakuta tu hairidhishi? Baada ya kuchunguza maisha ya wengine “ambao wamepata utimizo wa tamaa zao,” msaikolojia Daniel Levinson aliripoti kwamba mara nyingi wao “wanaanza kuuliza, ‘Je! ni haya tu? Yalistahili yote niliyojilazimisha kuacha nilipokuwa nikijitahidi?’”
Kwa upande mwingine, huenda ukawa mmoja wa wale ambao wameona upumbavu wa kufuatia miradi ya mambo ya kimwili na kwa hiyo, unasita-sita kuhusu miradi yako mwenyewe. Kukosa mradi fulani hasa maishani kwaweza kuleta umizo sawa na kufuatia mradi wa kipumbavu. Dakt. Bennett Leventhal, daktari wa maradhi yanayohusu akili za watoto, anasadiki kwamba matatizo ya kitabia ya vijana wengi wenye wazazi matajiri yanatokea kwa sababu wazazi wao hawawezi kuwapa “miradi mingine licha ya fanaka ya mambo ya kimwili.” Viunga vya Chicago, ambapo Dakt. Leventhal anafanya kazi yake, vina mojayapo ya hesabu za juu zaidi za kujiua katika Marekani—hasa kati ya vijana. Kulingana na makala moja ya mhariri katika gazeti la Ujeremani linaloheshimiwa Franktfurter Allgemeine (Septemba 12, 1981), kisababishaji kikuu cha ongezeko kubwa mno la matumizi mabaya ya dawa za kulevya, kutokutii, kushuka moyo na uhalifu wa kipumbavu kati ya vijana ni “ongezeko la maoni ya kujiona bila kusudi.” Ndiyo, hawana mradi wo wote unaofaa maishani.
Mradi Unaofaa Ni Nini?
Kupata riziki yao ya kila siku peke yake ndio mradi wa wengi. Uchunguzi wa karibuni juu ya vijana 1,000 Wamarekani kutoka jamii za rangi mbalimbali na hali mbalimbali za kiuchumi uligundua kwamba “kupata kazi ya kuajiriwa ninayofurahia” ndio uliokuwa mradi wao mkuu. Lakini, kama ambavyo pengine unajua, mara nyingi mradi huo waweza kuwa wenye kukatisha tamaa na usioridhisha. Bado, tamaa nyingi mno ya kupata chakula, mavazi na makao ndio mradi pekee halisi wa walio wengi.
Mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuwa duniani alielekeza kwenye mradi tofauti. Yeye alisema: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele.” Aliwasihi watu watazame mambo ya maana zaidi na kujitahidi kufikia mipango inayoweza kuleta uzima wa milele. Ni watu wa namna gani ambao wangepewa zawadi hiyo? Kulingana na Yesu, ni wale ambao juu yao Mungu ‘ametia muhuri’ ya kibali yake. (Yohana 6:27) Kwa hiyo kujitahidi kupata kibali ya Mungu na hivyo kupokea uzima wa milele katika furaha ndio mradi ambao Yesu aliweka mbele ya wanafunzi wake.—2 Petro 3:13.
Tofauti Inayoletwa na Kuwa na Mradi
Wafuasi wa Yesu walifanya mabadiliko makubwa sana katika namna yao ya kuishi kwa sababu mioyo yao ilikazwa juu ya mradi huo wa maana kupita yote. Mmoja wao, mtume Paulo, bila shaka alikuwa amezaliwa na wazazi wenye utajiri katika mji wenye kuheshimiwa sana wa upande wa Mashariki ya Kati. Alikuwa amepata elimu ya juu kutoka kwa mwalimu na hakimu Myahudi mwenye heshima nyingi naye alikuwa akifanya maendeleo makubwa zaidi ya wengi wa umri wake katika kazi ya cheo kikubwa. Hata hivyo, kwa sababu yeye alikuwa ‘akikaza mwendo, aufikilie [mradi wa] thawabu ya mwito [wa juu] wa Mungu,’ aliyaona mambo hayo kuwa ni “mavi” na akatoa maisha yake ili kufanya mambo yenye kukubaliwa na Mungu. Sawa na walivyokuwa wale Wakristo wengine, kujitoa kwa Paulo na kusudi lake moja yalikuwa mambo yaliyokuwa wazi kwa watazamaji.—Matendo 22:1-3; Wagalatia 1:14; Wafilipi 3:5-8, 14.
Juhudi na kusudi moja lilo hilo ni mambo yanayoonekana leo kwa Wakristo wa kweli. Baada ya kuchunguza kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, mwandishi mmoja wa gazeti la Kanada aliripoti kwamba sababu kuu ya ongezeko lao ni “kadiri kubwa mno ya kujiona na wajibu na kujitoa kunakoonyeshwa na Mashahidi.” Wengi wao wamepata furaha ya kweli kwa kufuatia mradi wa uzima badala ya kufuatia mambo mengine.
Kwa mfano, Marko mwenye umri wa miaka 19 alikuwa amefikia mradi wake wa kuwa mmoja wa washindanaji bora zaidi wa pikipiki katika California (Marekani). “Nilikuwa nimefikia kiwango cha kushinda mbio nyingi. Nilijulikana sana, nilikuwa na fedha zote nilizotaka na kupendwa na msichana ye yote mjini,” akasema Marko. “Walakini baada ya kushinda mbio fulani mashuhuri nilijiuliza mwenyewe, ‘Je! ni haya tu? Sasa nimefikia sehemu bora zaidi ya maisha yangu walakini mbona sijajiona nimetimiza jambo?’ “Wengine walikuwa wakichunguza kazi yake ya kupiga mbio yenye kutokeza mno na walikuwa wakitaka kufanya mwendo wake wa maisha uwe mradi wao. “Walikuwa wanajaribu kupata jambo lile nililokuwa nimelipata, lakini hayo yote yalikuwa ni upumbavu. Mimi sikuwa na kitu na bado wao walikuwa wanakitaka!” Muda si muda Marko alijifunza Biblia kwa uzito pamoja na Mashahidi wa Yehova akaona thamani ya kufuatia mradi unaofaa. Baada ya kuwa mmoja wa Mashahidi, aliyatoa maisha yake ili kupata kibali ya Mungu na kuwasaidia wengine katika njia ya kiroho. Alipotafakari juu ya maisha yake tangu wakati huo, Marko, ambaye sasa ni mwenye umri wa miaka 27, alisema hivi: “Sasa nilipata marafiki wa kweli na furaha ya kuwasaidia wengine kwa njia ya kiroho. Hatimaye nikawa naona maisha yangu yanatimiza jambo lenye kuwaletea watu ubora wa kudumu.”
Lakini kufuatia mradi kunahusu maisha ya Mkristo kwa kadiri gani? Ni jitihada ya kadiri gani inayohitajiwa na Mkristo ili kufikia mradi huo? Na ni katika njia gani kufuatia mradi unaofaa kunaleta uradhi? Ni miradi gani ya kwanza anayopaswa mtu kujitahidi kufikia anapojikaza sana kufikia mradi wa mwisho wa uzima wa milele? Maulizo hayo yatazungumzwa katika makala inayofuata.