Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yule Mwanamke Tasa Ashangilia
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • [Picha katika ukurasa wa 220]

      Baada ya ubatizo wake, Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu, na andiko la Isaya 54:1 likaanza kupata utimizo wake ulio wa maana zaidi

  • Yule Mwanamke Tasa Ashangilia
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Yule “Mwanamke” Atambuliwa

      3. Kwa nini “mwanamke” huyo tasa atakuwa na sababu ya kushangilia?

      3 Sura ya 54 inaanza kwa hali ya furaha: “Imba, wewe [“mwanamke,” “NW”] uliye tasa, wewe usiyezaa; paza sauti yako kwa kuimba, piga kelele, wewe usiyekuwa na utungu; maana watoto [“wana,” “NW”] wake aliyeachwa ni wengi kuliko watoto wake yeye aliyeolewa, asema BWANA.” (Isaya 54:1) Isaya anasisimuka kama nini kusema maneno hayo! Na utimizo wake utawaletea faraja iliyoje Wayahudi walioko uhamishoni Babiloni! Wakati huo Yerusalemu bado atakuwa ukiwa. Kwa maoni ya kibinadamu, itaonekana ni kama hakuna kamwe tumaini la jiji hilo kukaliwa na watu tena, sawa na vile isivyo kawaida mwanamke tasa kutumainia kuzaa watoto siku za uzeeni. Lakini “mwanamke” huyu ana baraka kubwa wakati wake ujao—atapata nguvu za uzazi. Yerusalemu atachachawa kwa shangwe ya ajabu. Atamiminikwa tena na “wana,” au wakaaji.

      4. (a) Mtume Paulo anatusaidiaje kuona kwamba bila shaka Isaya sura ya 54 ina utimizo mkubwa kuliko ule wa mwaka wa 537 K.W.K.? (b) “Yerusalemu la juu” ni nini?

      4 Huenda ikawa Isaya hajui jambo hili, lakini unabii wake utakuwa na utimizo zaidi ya mmoja. Mtume Paulo ananukuu kutoka Isaya sura ya 54 na kueleza kwamba “mwanamke” huyo anamaanisha kitu muhimu sana kuliko jiji la kidunia la Yerusalemu. Anaandika hivi: “Yerusalemu la juu ni huru, nalo ni mama yetu.” (Wagalatia 4:26) Hilo “Yerusalemu la juu” ni nini? Kwa wazi si lile jiji la Yerusalemu lililo katika Nchi ya Ahadi. Jiji hilo ni la kidunia, wala haliko “juu” katika makao ya kimbingu. “Yerusalemu la juu” ni “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu, tengenezo lake la viumbe-roho walio hodari.

      5. Katika drama ya mfano iliyoonyeshwa kwenye Wagalatia 4:22-31, ni nani wanaofananishwa na (a) Abrahamu? (b) Sara? (c) Isaka? (d) Hagari? (e) Ishmaeli?

      5 Ingawa hivyo, Yehova anawezaje kuwa na wanawake wawili wa mfano—mmoja wa kimbingu na yule mwingine wa kidunia? Je, hali hii inakosa upatano? Hata kidogo. Mtume Paulo anaonyesha kwamba jibu limo katika mfano wa kiunabii uliowekwa na familia ya Abrahamu. (Wagalatia 4:22-31; ona “Familia ya Abrahamu—Mfano wa Kiunabii,” katika ukurasa wa 218.) Sara, yule “mwanamke huru” aliyekuwa mke wa Abrahamu, anafananisha tengenezo la Yehova la viumbe-roho lililo kama mke. Naye Hagari, mjakazi aliyekuwa mke wa pili, au suria, wa Abrahamu anafananisha Yerusalemu la kidunia.

      6. Tengenezo la Mungu la kimbingu lilipitia kipindi kirefu cha utasa katika maana gani?

      6 Tukiwa na habari hizo za msingi, tunaanza kuona maana yenye kina kirefu ya Isaya 54:1. Baada ya miongo ya utasa, Sara alimzaa Isaka akiwa na umri wa miaka 90. Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kimbingu lilipitia kipindi kirefu cha utasa. Kule nyuma katika Edeni, Yehova aliahidi kwamba “mwanamke” wake angetokeza ile “mbegu.” (Mwanzo 3:15, NW) Miaka zaidi ya 2,000 baadaye, Yehova alifanya agano lake pamoja na Abrahamu kuhusu ile Mbegu ya ahadi. Lakini “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu alilazimika kungoja karne nyingi sana kabla ya kutokeza Mbegu hiyo. Hata hivyo, wakati ulifika watoto wa huyo aliyekuwa ‘mwanamke tasa’ wakawa wengi sana kuliko wale wa Israeli wa asili. Mfano unaohusu huyo mwanamke tasa unatusaidia kuona ni kwa nini malaika walikuwa na hamu nyingi sana ya kushuhudia ile Mbegu iliyotabiriwa ikiwasili. (1 Petro 1:12) Hilo lilitukia lini hatimaye?

      7. “Yerusalemu la juu” lilipata pindi ya kushangilia wakati gani, kama vile ilivyotabiriwa kwenye Isaya 54:1, na kwa nini unajibu hivyo?

      7 Kuzaliwa kwa Yesu akiwa mtoto wa kibinadamu hakika kulikuwa pindi ya kushangilia miongoni mwa malaika. (Luka 2:9-14) Lakini hilo silo tukio lililotabiriwa kwenye Isaya 54:1. Yesu alipozaliwa kwa roho takatifu mwaka wa 29 W.K., hapo ndipo alipopata kuwa mwana wa kiroho wa “Yerusalemu la juu,” akikubaliwa na Mungu mwenyewe peupe kuwa yeye ni ‘Mwana wake, mpendwa.’ (Marko 1:10, 11; Waebrania 1:5; 5:4, 5) Hapo ndipo yule “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu alipopata sababu ya kushangilia, kwa kutimiza Isaya 54:1. Sasa hatimaye mwanamke huyo akawa ametokeza ile Mbegu iliyoahidiwa, yule Mesiya! Karne zake za utasa zikawa zimekwisha. Hata hivyo, huo haukuwa mwisho wa kushangilia kwake.

      Huyo Mwanamke Tasa Apata Wana Wengi Sana

      8. Kwa nini “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu alikuwa na sababu ya kushangilia baada ya kutokeza ile Mbegu iliyoahidiwa?

      8 Baada ya Yesu kufa na kufufuliwa baadaye, “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu alishangilia kupokea Mwana huyo mwenye upendeleo akiwa “mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu.” (Wakolosai 1:18) Kisha mwanamke huyo akaanza kutokeza wana zaidi wa kiroho. Kwenye Pentekoste ya 33 W.K., karibu wafuasi 120 wa Yesu walitiwa mafuta kwa roho takatifu, na kwa njia hiyo wakafanywa kuwa warithi-washirika pamoja na Kristo. Baadaye siku hiyo, wengine 3,000 waliongezwa. (Yohana 1:12; Matendo 1:13-15; 2:1-4, 41; Waroma 8:14-16) Jamii hiyo ya wana iliendelea kukua. Wakati wa karne za mapema za uasi-imani wa Jumuiya ya Wakristo, ukuzi huo ulipungua ukawa haba sana. Lakini, mambo yangebadilika katika karne ya 20.

      9, 10. Maagizo ‘kupanua mahali pa hema’ yangemaanisha nini kwa mwanamke aliyeishi hemani nyakati za kale, na kwa nini huo ni wakati wa shangwe kwa mwanamke huyo?

      9 Isaya anaendelea kutoa unabii juu ya kipindi fulani cha ukuzi wa kustaajabisha: “Panua mahali pa hema yako, na wayatandaze mapazia ya maskani yako; usiwakataze; ongeza urefu wa kamba zako; vikaze vigingi vya hema yako. Kwa maana utaenea upande wa kuume na upande wa kushoto; na wazao wako watawamiliki mataifa; wataifanya miji iliyokuwa ukiwa kukaliwa na watu. Usiogope; maana hutatahayarika; wala usifadhaike; maana hutaaibishwa; kwa kuwa utaisahau aibu ya ujana wako, pia mashutumu ya ujane wako hutayakumbuka tena.”—Isaya 54:2-4.

      10 Hapa Yerusalemu anaambiwa mambo kana kwamba ni mke na mama anayekaa katika mahema, sawa na Sara. Anapobarikiwa kwa kupata familia inayoongezeka, umefika wakati wa mama huyo kuhakikisha kwamba nyumba yake inapanuliwa. Anahitaji kuongeza urefu wa mapazia yake na kamba zake na kuvipigilia imara vigingi vya hema mahali pake papya. Hiyo ni kazi inayomfurahisha, na kwa kuwa huo ni wakati wa shughuli nyingi, anaweza kusahau kwa urahisi miaka mingi aliyoitumia akihangaika bila kujua kama siku moja angezaa watoto wa kuendeleza ukoo wa familia.

      11. (a) “Mwanamke” wa kimbingu wa Mungu alibarikiwaje mwaka wa 1914? (Ona kielezi-chini.) (b) Kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea, watiwa-mafuta walio duniani wamepata baraka gani?

      11 Yerusalemu la kidunia lilibarikiwa kwa kupata wakati wa kujengwa upya jinsi hiyo baada ya ule uhamisho wa Kibabiloni. “Yerusalemu la juu” limebarikiwa hata zaidi.a Hasa tangu mwaka wa 1919, “wazao” wake watiwa-mafuta wamechanuka katika hali yao ya kiroho iliyorudishwa. (Isaya 61:4; 66:8) ‘Waliwamiliki mataifa’ katika maana ya kwamba walienea wakaingia nchi nyingi kuwatafuta wale ambao wangetaka kujiunga na familia yao ya kiroho. Matokeo ni kwamba, ukuzi mkubwa ulivuvumka kwa kukusanya wale wana watiwa-mafuta. Idadi yao ya mwisho ya 144,000 ilionekana kuwa imejazwa wakati fulani katikati ya ile miaka ya 1930. (Ufunuo 14:3) Wakati huo, kukusanywa kwa watiwa-mafuta kuliacha kuwa lengo kuu la kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, mpanuko haukukoma eti kwa sababu mkusanyo wa watiwa-mafuta ulikoma.

      12. Ni nani zaidi ya watiwa-mafuta ambao wamekusanywa wakaingizwa katika kutaniko la Kikristo tangu miaka ya 1930?

      12 Yesu mwenyewe alitabiri kwamba licha ya yeye kuwa na “kundi dogo” la ndugu watiwa-mafuta, angekuwa pia na “kondoo wengine” ambao ni lazima waletwe ndani ya zizi la kondoo la Wakristo wa kweli. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Ingawa waandamani hao waaminifu wa watiwa-mafuta hawamo miongoni mwa wana watiwa-mafuta wa “Yerusalemu la juu,” wanatimiza sehemu muhimu iliyotajwa na unabii zamani. (Zekaria 8:23) Kuanzia miaka ya 1930 hadi leo, “umati mkubwa” wa waandamani hao umekusanywa, matokeo yakawa ni mpanuko usio na kifani wa kutaniko la Kikristo. (Ufunuo 7:9, 10) Leo huo umati mkubwa una mamilioni ya watu. Mpanuko wote huo umetokeza uharaka wa kuongeza Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na ofisi za tawi. Maneno ya Isaya yanaonekana yamezidi kufaa sana. Ni pendeleo kama nini kuwa sehemu ya mpanuko huo uliotabiriwa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki