-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Historia ya Kisasa ya Bosnia na Herzegovina
“Mei 16, 1992 (16/5/1992), tukiwa watu 13, tulikusanyika pamoja katika nyumba fulani wakati makombora yaliporushwa huko Sarajevo. Makombora mawili yaligonga jengo ambamo tulikuwa tumekusanyikia. Ingawa wengine wetu walikuwa Wakroatia, Waserbia, na Wabosnia—makabila yaleyale matatu ambayo yalikuwa yakiuana kule nje—tuliunganishwa na ibada safi. Kufikia asubuhi, kulipokuwa na utulivu kidogo, tuliondoka kwenye nyumba hiyo na kutafuta mahali salama. Kama tulivyokuwa tumefanya usiku uliotangulia, tulimlilia Yehova kwa sauti katika sala, naye akatusikia.”—Halim Curi.
Sarajevo, ambalo lilikuwa na wakaaji zaidi ya 400,000, lilikabili mazingiwa ya muda mrefu zaidi na yenye kuogopesha zaidi katika historia ya leo. Ndugu na dada zetu wangeweza kukabiliana jinsi gani na mizozo yote ya kikabila na ya kidini iliyokuwa ikiigawanya nchi? Kabla hatujasimulia mambo yaliyowapata, acheni kwanza tupate habari zaidi kuhusu Bosnia na Herzegovina.
Nchi inayoitwa Bosnia na Herzegovina iko katikati ya nchi iliyoitwa Yugoslavia, nayo imezungukwa na Kroatia, Serbia, na Montenegro. Wakaaji wana uhusiano wa karibu wa kifamilia na wa kitamaduni, nao wanakazia sana ukarimu. Wanapenda kunywa kahawa fulani ya pekee na kwenda kwenye mikahawa inayoitwa kafići. Ingawa wakaaji wa Bosnia wanafanana sana, kuna Wabosnia, Waserbia, na Wakroatia. Wengi wao hawadai kuwa watu wanaofuata dini sana, hata hivyo, dini ndiyo imesababisha mgawanyiko. Wabosnia wengi ni Waislamu, Waserbia wengi ni wa Kanisa Othodoksi la Serbia, na Wakroatia wengi ni washiriki wa Kanisa Katoliki.
Chuki ya kidini na ya kikabila iliyoongezeka sana mapema katika miaka ya 1990 ilitokeza sera yenye kusikitisha ya kusafisha makabila. Majeshi yaliwafukuza raia—katika vijiji na majiji makubwa—ili kutenga maeneo yenye makabila fulani tu kwa ajili ya vikundi vyao vya kidini. Msimamo wa ndugu na dada zetu wa kutounga mkono upande wowote ulijaribiwa. Huko Bosnia, kama ilivyo katika nchi nyingine zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia, watu wengi wanafuata dini ya wazazi wao, na kwa kawaida jina la familia linaonyesha dini inayofuatwa na familia. Watu wenye moyo mzuri wanapokuwa watumishi wa Yehova, huenda wakaonwa kuwa wameisaliti familia yao na utamaduni wao. Hata hivyo, ndugu zetu wamejifunza kwamba ushikamanifu kwa Yehova ni ulinzi.
JIJI LAZINGIRWA
Kama tulivyoona, ndugu wa Yugoslavia waliguswa moyo sana na upendo na umoja uliokuwepo katika kusanyiko la mwaka wa 1991 la “Wapendao Uhuru wa Kimungu” huko Zagreb, Kroatia. Kusanyiko hilo lisiloweza kusahaulika liliwatia nguvu kukabiliana na matatizo ambayo yangetokea baadaye. Wakati fulani, Wabosnia, Waserbia, na Wakroatia walikuwa wakiishi pamoja kwa amani huko Sarajevo. Kisha, jeshi likazingira jiji hilo na kila mtu akanaswa ndani—kutia ndani ndugu zetu. Ingawa kulikuwa na msukosuko wa kisiasa, hakuna aliyejua hali hiyo ingeendelea kwa muda gani.
Halim Curi, mzee wa kutaniko huko Sarajevo, alisema hivi: “Watu wanakufa njaa. Kila mwezi wanapewa kilo chache tu za unga, gramu 100 za sukari, na nusu lita ya mafuta. Wakipata kipande chochote kidogo cha ardhi jijini, wanakitumia kupandia mboga. Watu wanakata miti ya Sarajevo ili wapate kuni. Miti inapokwisha, wanabomoa sakafu za mbao za nyumba zao ili wazitumie kupikia na kupasha joto nyumba zao. Wanatumia chochote kinachoweza kuteketea, hata viatu vilivyochakaa.”
Jiji la Sarajevo lilipozingirwa, Ljiljana Ninković na mume wake Nenad walinaswa jijini na kutenganishwa na binti zao wawili. Ljiljana anasema: “Tulikuwa familia ya kawaida yenye watoto wawili, nasi tulikuwa na nyumba na gari. Halafu kwa ghafula, mambo yakabadilika kabisa.”
Lakini mara nyingi waliona mkono wa Yehova ukiwalinda. Ljiljana anaendelea kusimulia: “Nyumba yetu ililipuliwa kwa bomu mara mbili baada tu ya sisi kuondoka. Ingawa tulipata matatizo, tulifurahia mambo madogo-madogo. Kwa mfano, tulifurahia kwenda kwenye bustani kuchuna majani fulani (ya dandelion) ili kutengeneza saladi, hivyo hatukula wali mkavu. Tulijifunza kutosheka na vitu tulivyokuwa navyo na kutochezea kitu chochote.”
KUPATA MAANDALIZI YA KIMWILI NA YA KIROHO
Tatizo moja kubwa lilikuwa kupata maji. Nyumba hazikuwa na maji ya bomba. Iliwabidi watu watembee kilomita tano kupitia maeneo yenye wavamizi ili kupata maji. Na walipofika mahali pa kuteka maji, walipanga foleni kwa saa nyingi wakisubiri kujaza mitungi yao, halafu iliwabidi kuanza safari ndefu ya kurudi nyumbani wakiwa wamejitwika mitungi hiyo.
Halim anasema: “Imani yetu ilijaribiwa tuliposikia kwamba maji yangepatikana nyumbani kwa muda mfupi. Wakati huo kila mtu alioga, alifua nguo, na kuteka na kuhifadhi maji katika mitungi mingi iwezekanavyo. Lakini namna gani ikiwa maji yangepatikana wakati wa mkutano wa kutaniko? Ilitubidi tuamue—ama kwenda kwenye mkutano au kubaki nyumbani kuteka maji.”
Ingawa maandalizi ya kimwili yalihitajiwa sana, akina ndugu walithamini sana maandalizi ya kiroho. Kwenye mikutano, ndugu walipata chakula cha kiroho na pia habari kuhusu wale waliofungwa gerezani, wale walioumizwa, au hata wale waliouawa. Milutin Pajić, ambaye ni mzee wa kutaniko, anasema: “Tulikuwa kama familia. Tulipohudhuria mikutano, hatukutaka kuondoka. Baada ya mikutano mingi, tulibaki kwa saa nyingi tukizungumza kuhusu kweli.”
Maisha hayakuwa rahisi, na mara nyingi akina ndugu walihofia maisha yao. Lakini walitanguliza mambo ya kiroho. Ingawa vita vilizidi kuigawanya nchi, watu wa Yehova walifurahia uhusiano wa karibu hata zaidi kati yao na pamoja na Baba yao wa mbinguni. Watoto waliona ushikamanifu wa wazazi wao, na ukawachochea kuwa washikamanifu kabisa kwa Yehova.
Mji wa Bihać, ulio karibu na mpaka wa Kroatia, ulizingirwa kwa karibu miaka minne. Wakaaji hawangeweza kutoka nje, na misaada haingeweza kuingizwa ndani. Osman Šaćirbegović, ndugu pekee aliye katika mji huo, anasimulia: “Mwanzoni mwa vita, hali ilikuwa mbaya sana, si hasa kwa sababu ya hali ngumu lakini kwa sababu tulikuwa tukikabili jambo geni, jambo ambalo hatukuwa tumekabili awali. Inashangaza kwamba makombora yalipoanza kurushwa, wasiwasi ulipungua kwa sababu tulitambua kwamba si makombora yote yanayosababisha kifo. Makombora mengine hata hayalipuki.”
Kwa kuwa hakuna aliyejua mapigano hayo yangedumu kwa muda gani, Betheli za Zagreb, Kroatia, na Vienna, Austria zilishirikiana kuhifadhi misaada katika Majumba ya Ufalme na nyumba za Mashahidi huko Sarajevo, Zenica, Tuzla, Mostar, Travnik, na Bihać. Mapigano yalipoendelea, majiji yalizingirwa kwa ghafula na kutenganishwa. Kwa kuwa misaada haingeweza kusafirishwa, muda si muda maandalizi yalikwisha. Hata hivyo, ingawa miji mbalimbali ya Bosnia ilitenganishwa na maeneo mengine ya ulimwengu, umoja wa kindugu wa Mashahidi wa Yehova haukudhoofika kamwe. Hali hiyo ilikuwa tofauti kabisa na ile chuki ya kikabila na ya kidini iliyokuwa ikienea kama moto kotekote nchini.
WENYE BIDII LAKINI WAANGALIFU
Zaidi ya matatizo ya kupata vitu vya msingi vya kila siku, kulikuwa pia na hatari ya kushambuliwa na wavamizi waliokuwa kotekote Sarajevo, ambao walikuwa wakiwapiga risasi raia wowote wale. Pia, makombora yaliendelea kurushwa angani na kuwaua watu. Nyakati nyingine, ilikuwa hatari kutembea katika miji iliyozingirwa. Watu waliishi kwa woga. Lakini ndugu zetu walitumia hekima na ujasiri kwa usawaziko na kuendelea kuwahubiria habari njema ya Ufalme watu waliohitaji sana faraja.
Mzee mmoja anasema hivi: “Wakati wa mashambulizi makali zaidi huko Sarajevo, maelfu ya makombora yalilipuka kwa siku moja tu. Jumamosi hiyo asubuhi, akina ndugu waliwapigia simu wazee na kuwauliza, ‘Mkutano wa utumishi wa shambani utakuwa wapi?’”
Dada mmoja alisema hivi: “Niliona kwamba watu wanahitaji sana kweli. Hilo hasa ndilo jambo lililonisaidia kuvumilia na kupata shangwe wakati wa hali ngumu.”
Wakaaji wengi walitambua kwamba walihitaji tumaini la Biblia. Ndugu mmoja alisema hivi: “Watu wanatutafuta ili wapate msaada wa kiroho, badala ya sisi kuwatafuta. Wanakuja kwenye Jumba la Ufalme na kuomba funzo.”
Mafanikio mengi katika kazi ya kuhubiri wakati wa vita yalichangiwa na umoja ulio katika undugu wetu wa Kikristo, ambao watu waliuona waziwazi. Nada Bešker, dada ambaye amekuwa akitumika akiwa painia wa pekee kwa miaka mingi, anasimulia hivi: “Ulikuwa ushahidi mkubwa. Watu wengi waliona ndugu Wabosnia na Waserbia wakihubiri pamoja. Na walipomwona dada Mkroatia pamoja na dada ambaye zamani alikuwa Mwislamu wakijifunza pamoja na Mserbia, walitambua waziwazi kwamba sisi ni tofauti.”
Matokeo ya bidii ya akina ndugu yanaweza kuonekana mpaka leo hii kwa sababu wengi ambao wanamtumikia Yehova sasa walikubali kweli wakati wa vita. Kwa mfano, kutaniko la huko Banja Luka liliongezeka mara mbili, hata ingawa wahubiri 100 walihamia makutaniko mengine.
FAMILIA YENYE UAMINIFU
Ndugu zetu walikuwa waangalifu sana nyakati zote. Hata hivyo, wengine walipatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa” kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa. (Mhu. 9:11) Božo Ðorem, ambaye ni Mserbia, alibatizwa kwenye kusanyiko la kimataifa huko Zagreb mwaka wa 1991. Baada ya kurudi Sarajevo, alifungwa gerezani mara kadhaa, na akiwa huko alitendewa vibaya sana kwa sababu ya msimamo wake wa kutounga mkono upande wowote. Mwaka wa 1994, alifungwa gerezani kwa miezi 14. Tatizo kubwa ni kwamba hangeweza kuwa pamoja na mke wake, Hena, na binti yao mwenye umri wa miaka mitano, Magdalena.
Muda mfupi baada ya Božo kuwekwa huru kutoka gerezani, msiba ulitokea. Alasiri moja yenye utulivu, wote watatu walienda kuongoza funzo la Biblia karibu na nyumba yao. Walipokuwa njiani, utulivu ulivurugwa na mlipuko wa kombora. Hena na Magdalena walikufa papo hapo, na Božo alikufa baadaye hospitalini.
MSIMAMO WA KIKRISTO WA KUTOUNGA MKONO UPANDE WOWOTE
Kwa kuwa ubaguzi ulikuwa ukienea sana, watu walilazimishwa kuunga mkono upande fulani. Huko Banja Luka, kutaniko lilikuwa na ndugu wengi vijana ambao wanajeshi walitaka kuwatumia katika vita. Kwa sababu hawakuunga mkono upande wowote, walipigwa viboko.
Osman Šaćirbegović anakumbuka hili: “Polisi walituhoji mara nyingi na kutuita waoga kwa kuwa hatukupigana ili kulinda familia zetu.”
Osman alikuwa akiwaambia polisi hivi: “Bunduki zenu zinawalinda, sivyo?”
Kisha polisi wangejibu, “Bila shaka.”
“Je, mnaweza kukubali kubadilisha bunduki zenu kwa mizinga ili mwe salama zaidi?”
“Ndiyo.”
“Je, mnaweza kukubali kubadilisha mizinga kwa vifaru?”
“Bila shaka.”
Kisha Osman aliwaambia: “Mngefanya yote hayo ili mwe salama zaidi. Mimi ninalindwa na Yehova, Mungu mweza-yote, Muumba wa ulimwengu wote. Je, kuna ulinzi bora zaidi kuliko huo?” Jibu lilikuwa wazi, na baada ya hapo polisi wangemwacha.
MISAADA YAFIKA
Ingawa ndugu katika nchi za karibu walijua kwamba Mashahidi Wabosnia walikuwa wakiteseka, kwa muda fulani ilikuwa vigumu kuwapelekea misaada ndugu zetu wenye uhitaji. Kisha, mnamo Oktoba 1993, wenye mamlaka walisema kwamba misaada hiyo inaweza kusafirishwa. Ijapokuwa kulikuwa na hatari, ndugu zetu waliamua kutumia nafasi hiyo vizuri. Mnamo Oktoba 26, malori matano yalianza safari ya kwenda Bosnia kutoka Vienna, Austria, yakiwa na tani 16 za chakula na kuni. Msafara huo ungepita jinsi gani katika maeneo mengi yaliyokuwa bado na mapigano makali?c
Nyakati fulani katika safari hiyo akina ndugu walikabili hatari kubwa. Dereva mmoja anakumbuka hivi: “Nilianza safari nikiwa nimechelewa asubuhi hiyo, nami nikajipata nyuma ya malori mengine yaliyokuwa yakipeleka misaada. Nilipokaribia kituo kimoja cha ukaguzi, malori yote yalisimama ili maofisa wakague vibali. Kwa ghafula, nikasikia mlio wa risasi za mvamizi, kisha tukaona dereva ambaye si Shahidi akiwa amepigwa risasi.”
Ni madereva tu walioruhusiwa kuingia Sarajevo wakiwa na malori yao, hivyo iliwabidi ndugu wengine waliosafiri pamoja nao wasubiri nje ya jiji. Lakini kwa kuwa walitaka sana kuwatia moyo ndugu zao wenyeji, walitafuta simu, wakawapigia simu wahubiri huko Sarajevo, na kuwatolea hotuba ya watu wote yenye kutia moyo. Mara nyingi wakati wa vita, waangalizi wanaosafiri, Wanabetheli, na washiriki wa Halmashauri ya Nchi walihatarisha maisha yao ili kuwasaidia ndugu zao kupata vitu vya kimwili na kuendelea kuwa imara kiroho.
Kwa karibu miaka minne, bidhaa hazingeweza kuwafikia ndugu zetu huko Bihać. Ingawa chakula cha kimwili hakikuruhusiwa kuvuka vizuizi vilivyotenganisha mji, ndugu zetu waliweza kupata chakula cha kiroho. Jinsi gani? Walipata laini ya simu na mashini ya faksi, ambayo iliwawezesha kupata mara kwa mara Huduma Yetu ya Ufalme na nakala za Mnara wa Mlinzi. Walichapa tena vichapo hivyo na kugawia kila familia nakala moja. Vita vilipoanza, kulikuwa na kikundi kidogo tu cha wahubiri watatu waliobatizwa. Pia, kulikuwa na wahubiri wengine 12 ambao walisubiri kwa miaka miwili pindi inayofaa ili wabatizwe katika maji ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova.
Haikuwa rahisi kutenganishwa kwa miaka mingi hivyo. Osman anasema: “Wanafunzi wangu wa Biblia hawakuwa wamewahi kuhudhuria kusanyiko wala mikutano wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Tulizungumza mara nyingi kuhusu wakati ambapo tutaweza kufurahia undugu wetu.”
Hebu wazia jinsi akina ndugu walivyofurahi Agosti 11, 1995, wakati magari mawili yaliyoandikwa “Misaada ya Mashahidi wa Yehova” yalipoingia Bihać. Yalikuwa magari ya kwanza ya kibinafsi kufaulu kuleta misaada tangu jiji lilipozingirwa! Nayo yalifika wakati tu akina ndugu walipoanza kuhisi kwamba wamedhoofika sana, kimwili na kiakili.
Majirani huko Bihać waliona jinsi akina ndugu walivyotunzana, kama vile kwa kurekebisha madirisha yaliyovunjika. Osman anasema: “Jambo hilo liliwavutia majirani wangu, kwa kuwa walijua hatuna pesa. Ulikuwa ushahidi mkubwa sana, na bado wanauzungumzia.” Sasa kuna kutaniko lenye bidii lenye wahubiri 34 na mapainia 5 katika mji wa Bihać.
SAFARI ISIYOSAHAULIKA!
Akina ndugu zetu walihatarisha maisha yao mara nyingi ili kupeleka chakula na vitabu katika miji yenye vita huko Bosnia. Lakini safari ya Juni 7, 1994 ilikuwa tofauti. Msafara wa malori matatu yaliyobeba washiriki wa Halmashauri ya Nchi na wafanyakazi wengine yaliondoka Zagreb, Kroatia, mapema asubuhi hiyo. Walikusudia kufikisha misaada na kufanya kusanyiko la pekee lililofupishwa, la kwanza katika muda wa miaka mitatu!
Jiji la Tuzla ni moja ya maeneo yaliyokuwa yamechaguliwa kwa ajili ya programu hiyo ya pekee. Mwanzoni mwa vita, kulikuwa na wahubiri 20 hivi tu waliobatizwa katika kutaniko. Ilishangaza kama nini kuona watu zaidi ya 200 wakiwa wamekusanyika kusikiliza programu ya kusanyiko! Watu 30 walibatizwa. Leo, jiji la Tuzla lina makutaniko matatu na wahubiri zaidi ya 300.
Huko Zenica, akina ndugu walipata mahali pazuri pa kukutania, lakini walishindwa kupata kidimbwi cha ubatizo. Mwishowe, baada ya jitihada nyingi, walipata pipa ambalo lingeweza kutumiwa. Lakini tatizo ni kwamba pipa hilo lilikuwa linanuka, kwa kuwa zamani lilitumiwa kuwekea samaki! Hata hivyo, waliotaka kubatizwa ambao walikuwa wameukubali mwaliko wa Yesu wa kuwa “wavuvi wa watu,” hawakuogopa. (Mt. 4:19) Herbert Frenzel, ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Kroatia, alikuwepo ili kutoa hotuba ya ubatizo. Anaripoti hivi: “Wale waliotaka kubatizwa walikuwa wamesubiri kwa muda mrefu sana ili wabatizwe hivi kwamba hakuna jambo ambalo lingewazuia! Baada ya kubatizwa walihisi ni kana kwamba wamepata ushindi!” Leo, kuna kutaniko lenye bidii lenye wahubiri 68 huko Zenica.
Huko Sarajevo, programu ingeweza kufanyiwa tu kwenye makutano ya barabara ambapo wavamizi walikuwa wakiwashambulia watu kwa risasi. Akina ndugu walipofika salama kwenye kusanyiko, walikabili tatizo la kupata mahali pa ubatizo na njia ya kuhifadhi maji, ambayo yalipatikana kwa shida. Ili kuhakikisha kwamba kuna maji ya kutosha kwa ajili ya ubatizo, wale wanaotaka kubatizwa waliambiwa wapange foleni kulingana na ukubwa wao, nao wakabatizwa kuanzia yule mdogo zaidi mpaka yule mkubwa zaidi!
Ilikuwa siku yenye furaha kama nini kwa ndugu na dada zetu! Hawakuruhusu matukio yoyote yenye kuogopesha yawanyang’anye shangwe yao kubwa ya kuabudu pamoja. Leo, kuna makutaniko matatu imara katika jiji la Sarajevo.
BAADA YA VITA
Njia za kuingiza bidhaa zilipofunguliwa, maisha yakawa rahisi zaidi kwa ndugu na dada zetu. Hata hivyo, sera ya kusafisha makabila iliendelea, na watu wakaendelea kufukuzwa makwao. Ivica Arabadžić, mzee anayetumika Kroatia, anakumbuka akitimuliwa kwenye nyumba ya familia yao huko Banja Luka. “Mtu mmoja alikuja na bunduki na kutuambia tuondoke, akisema kwamba sasa hiyo ni nyumba yake. Alikuwa amefukuzwa kwenye nyumba yake huko Šibenik, Kroatia, kwa sababu alikuwa Mserbia. Sasa alitaka tuondoke. Polisi mmoja wa jeshi niliyejifunza naye aliingilia kati kutusaidia. Ingawa hatungeweza kuendelea kumiliki nyumba yetu, tulikubaliana na Mserbia huyo tubadilishane nyumba—yeye akachukua yetu nasi tukachukua yake. Haikuwa rahisi kwetu kuhama nyumba yetu na kutaniko lililotusaidia kujifunza kweli, lakini hatukuwa na lingine la kufanya. Tulichukua vitu vichache na kuhamia nyumba yetu ‘mpya’ huko Kroatia. Lakini tulipofika Šibenik, mtu mwingine alikuwa tayari ameingia katika nyumba hiyo yetu. Sasa tungefanya nini? Ndugu zetu walitukaribisha mara moja, na mzee fulani akaturuhusu tuishi katika nyumba yake kwa mwaka mmoja mpaka tuliposuluhisha tatizo hilo la nyumba.”
Bado kuna msukosuko wa kisiasa hata leo, lakini kweli inaendelea kusitawi huko Bosnia na Herzegovina, ambako karibu asilimia 40 ya watu wanadai kuwa Waislamu. Tangu vita vilipokwisha, ndugu zetu wamejenga Majumba ya Ufalme mapya. Jumba moja hasa, huko Banja Luka, ni zaidi ya mahali pa kukutania. Jumba hilo linawakilisha ushindi wa kisheria. Kwa miaka mingi, ndugu zetu walijaribu kupata ruhusa ya kujenga Jumba la Ufalme katika eneo hilo ambako Kanisa la Othodoksi la Serbia lina uvutano mkubwa. Baada ya vita, ingawa ndugu zetu huko Bosnia walitambuliwa kisheria, walinyimwa ruhusa ya kujenga Jumba la Ufalme huko Banja Luka. Mwishowe, baada ya kusali sana na kujitahidi sana, akina ndugu walipewa ruhusa ya kujenga. Ushindi huo umeweka msingi wa kisheria unaoweza kutumiwa kupata ruhusa ya kujenga Majumba mengine ya Ufalme katika eneo hilo la Bosnia na Herzegovina.
Uhuru huo wa ibada umewawezesha mapainia wa pekee 32, wengi wao wakiwa wametoka nchi nyingine, wasaidie kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa. Bidii yao katika huduma na ushikamanifu wao kwa miongozo ya kitheokrasi ni baraka kubwa.
Sasa makusanyiko yanafanywa kwa amani katika jiji la Sarajevo, ambako ndugu zetu walishambuliwa mara nyingi na wavamizi wenye kufyatua risasi miaka 10 tu iliyopita. Makusanyiko hayo yanahudhuriwa na wajumbe kutoka nchi zote zilizokuwa sehemu ya Yugoslavia. Ingawa vita vya karne iliyopita vimeharibu nchi hiyo maridadi yenye milima, watu wa Yehova wamezidi kuwa na uhusiano wa karibu wakiwa wameunganishwa na “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Leo, makutaniko 16 yenye wahubiri 1,163 huko Bosnia na Herzegovina yanamsifu kwa umoja Mungu wa kweli, Yehova.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 195, 196]
Tuliahidi Kurudi
HALIM CURI
ALIZALIWA 1968
ALIBATIZWA 1988
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alisaidia kupanga na kusambaza misaada huko Sarajevo. Sasa anatumika akiwa mzee, mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali, na wakili wa Mashahidi wa Yehova huko Bosnia na Herzegovina.
MWAKA wa 1992, jiji la Sarajevo lilizingirwa na wanajeshi. Tulipokosa kupata magazeti mapya, tulijifunza magazeti ya zamani. Akina ndugu walitumia taipureta nzee kunakili makala za funzo zilizopatikana. Ingawa kulikuwa na wahubiri 52 tu, watu zaidi ya 200 walihudhuria mikutano yetu, nasi tuliongoza mafunzo ya Biblia 240 hivi.
Mnamo Novemba 1993, wakati vita vilipokuwa vimepamba moto, binti yetu, Arijana, alizaliwa. Haikuwa rahisi hata kidogo kumlea mtoto wakati huo. Nyakati nyingine, hatukuwa na maji ya bomba wala umeme kwa majuma mengi. Tulipata kuni kwa kupasua vyombo vya nyumbani vya mbao, nasi tulipitia maeneo hatari ili kufika kwenye mikutano. Wavamizi walifyatua risasi kiholela, hivyo ilitubidi tukimbie ili kuvuka barabara fulani na vizuizi.
Siku moja yenye utulivu, tulipokuwa tukirudi nyumbani kutoka kwenye mkutano pamoja na mke wangu na mtoto wetu na Ndugu Dražen Radišić, risasi zilianza kufyatuliwa ghafula. Tulilala chini barabarani, lakini nilipigwa risasi tumboni. Nilikuwa na maumivu makali sana. Watu wengi waliona kilichotukia kupitia madirisha ya nyumba zao, na vijana fulani wenye ujasiri walitoka nje ya nyumba haraka na kutupeleka mahali salama. Nilikimbizwa hospitalini, ambako walitaka kunitia damu mishipani haraka. Nilimweleza daktari kwamba dhamiri yangu haiwezi kuniruhusu nitiwe damu mishipani. Walinishinikiza nifikirie tena jambo hilo; lakini niliazimia kusimama imara na nilikuwa tayari kwa matokeo yoyote yale. Nilifanyiwa upasuaji kwa muda wa saa mbili na nusu, na nilipata nafuu bila kutiwa damu mishipani.
Baada ya upasuaji, nilihitaji kupumzika, lakini ilikuwa vigumu kufanya hivyo kwa sababu ya vita. Tuliamua kutembelea familia yetu huko Austria. Hata hivyo, njia pekee ya kutoka Sarajevo ilipitia chini ya uwanja wa ndege. Njia hiyo ilikuwa na urefu wa mita 900 na kimo cha sentimita 120 hivi. Mke wangu alimbeba mtoto, nami nikajaribu kubeba mizigo. Lakini kwa sababu ya upasuaji, ilibidi mke wangu anisaidie.
Tulifurahia sana kukaa Austria. Tulipokuwa tukiondoka Sarajevo, tuliwaahidi ndugu zetu na Muumba wetu kwamba tutarudi. Haikuwa rahisi hata kidogo kuiacha familia yetu huko Austria, hasa mama yangu. Lakini tuliwaeleza kwamba tulikuwa tumemwahidi Mungu tutarudi Sarajevo ikiwa angetusaidia kutoka huko na kupumzika kidogo. Sasa je, kweli tungeweza kumwambia Mungu: “Asante kwa kutusaidia kufika huku. Tunafurahia sana kuwa huku, na sasa tungependa kukaa huku”? Pia, akina ndugu wa Sarajevo walituhitaji. Mke wangu, Amra, alinitegemeza sana katika mambo yote hayo.
Hivyo, Desemba 1994, tulifika kwenye ile njia ya chini ya ardhi huko Sarajevo. Wakati huu tulikuwa tukiingia Sarajevo kutoka nje. Watu walipotuona tukirudi kupitia mfereji huo, walituuliza: “Mnafanya nini? Kila mtu anataka kuondoka, lakini ninyi mnarudi katika jiji lililozingirwa?” Siwezi kueleza kikamili shangwe tuliyokuwa nayo tulipokutana tena na ndugu zetu kwenye Jumba la Ufalme la Sarajevo. Hatujawahi kamwe kujuta kwamba tulirudi.
-