-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ofisi ya Tawi Yajengwa
Katika mwaka wa 1914, ofisi ya kwanza ya tawi nchini Guyana ilifunguliwa nyumbani kwa Phillips, na haikuhamishwa hadi mwaka 1946. Mwaka huo kulikuwa na wahubiri 91 nchini humo. Mwaka wa 1959, wahubiri walikuwa wameongezeka na kufikia 685, na kazi ikaendelea kupanuka. Kwa hiyo, mnamo Juni 1960, ndugu walinunua kiwanja kwenye barabara ya Brickdam namba 50, Georgetown. Nyumba zilizokuwa kwenye kiwanja hicho zilifanyiwa marekebisho madogo na kutumiwa kama ofisi ya tawi na makao ya wamishonari. Lakini kufikia mwaka wa 1986, majengo hayo yakawa hayatoshi. Kwa hiyo, baada ya kupata kibali cha Baraza Linaloongoza, ofisi mpya ilijengwa kwenye kiwanja hicho. Watumishi wa kimataifa, wakisaidiwa na ndugu wenyeji, walimaliza ujenzi huo mwaka wa 1987.
Kama vile binti za Shalumu, ambao walimsaidia baba yao kujenga upya sehemu fulani ya kuta za Yerusalemu, dada walisaidia sana katika ujenzi huo. (Neh. 3:12) Kwa mfano, dada 120 waliokuwa katika vikundi kumi hivi, walitengeneza matofali 12,000 ya saruji ambayo yalihitajiwa katika ujenzi huo. Walitumia visanduku 16 vya kutengenezea matofali, nao wakamaliza kazi hiyo kwa siku 55. Hiyo haikuwa kazi rahisi hata kidogo! Walihitaji kutumia vipimo sahihi walipochanganya saruji na mchanga ili mchanganyiko ushikamane vizuri na pia usiwe na maji mengi, la sivyo matofali yangebomoka yalipoinuliwa kutoka kwenye visanduku.
Ndugu wenyeji ndio waliokuwa walinzi usiku na mara nyingi walikuja moja kwa moja kutoka kazini. Wengine walifanya kazi pamoja na watumishi wa kimataifa ambao waliwafundisha mbinu mbalimbali za ujenzi. Harrinarine (Indaal) Persaud, mmoja wa ndugu hao, anasema: “Nilipewa kazi ya kuweka mapambo fulani kwenye vizingiti vya dirisha, nami sikuwa nimewahi kufanya kazi hiyo. Nilijitahidi na hatimaye nikafaulu kuyaweka vizuri. Baada ya kuchunguza kazi yangu na kupendezwa nayo, ndugu aliyesimamia ujenzi alisema: ‘Sasa utafanya vivyo hivyo kwenye madirisha yote.’” Leo, ndugu huyo kijana huwafundisha wengine ustadi huo wanapojenga Majumba ya Ufalme.
Kwa kuwa iliwabidi ndugu kuagiza vitu fulani kutoka nje ya nchi, walihitaji msaada wa wakuu wa serikali. Kwa sababu hiyo, maofisa wengi walikuja mahali tulipokuwa tukijenga, kutia ndani Rais Forbes L. Burnham na msafara wake. Wote, akiwemo seremala fulani mwenyeji, walivutiwa na jinsi jengo hilo lilivyojengwa kwa ustadi. Seremala huyo alisema: “Ninyi mnajenga majengo ya hali ya juu sana.” Mnamo Januari 14, 1988, Don Adams, mwakilishi wa Brooklyn ambaye wakati huo alikuwa mwangalizi wa eneo la dunia, alitoa hotuba ya kuweka jengo hilo wakfu.
Mnamo Februari 12, 2001, ujenzi mwingine ulianza, lakini katika eneo lingine. Kwa mara nyingine, kazi hiyo ilifanywa na watumishi wa kimataifa wakisaidiwa na ndugu wenyeji. Ofisi hiyo mpya ya tawi iliwekwa wakfu mnamo Jumamosi, Februari 15, 2003. Hotuba ya kuweka jengo hilo wakfu, ambayo ilitolewa na Richard Kelsey kutoka ofisi ya tawi ya Ujerumani, ilisikilizwa na watu 332.
Wamishonari wengi waliotumikia nchini Guyana zamani walirudi kwa ajili ya tukio hilo, baadhi yao kwa mara ya kwanza tangu waondoke miaka mingi iliyopita! Watu 4,752 kutoka nchi 12, ambao ni zaidi ya mara mbili ya idadi ya wahubiri wa Guyana, walihudhuria mkutano wa pekee Jumapili.
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 197]
Ofisi ya tawi ya zamani kwenye barabara ya Brickdam namba 50, Georgetown, iliyojengwa mwaka wa 1987
-