Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uhai Ulianzaje?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • Watafiti wamegundua kwamba ili chembe iendelee kuwa hai, angalau aina tatu tofauti za molekuli tata lazima zifanye kazi pamoja—DNA au deoksiribonyukilia asidi, RNA (ribonucleic acid), na protini. Leo, ni wanasayansi wachache wanaoweza kudai kwamba chembe kamili iliyo hai ilijitokeza yenyewe kutokana na mchanganyiko wa kemikali zisizo hai. Hata hivyo, kuna uwezekano gani kwamba RNA au protini zinaweza kujitokeza zenyewe?a

      Wanasayansi wengi huhisi kwamba huenda uhai ulijitokeza wenyewe kwa sababu ya jaribio fulani lililofanywa kwa mara ya kwanza mwaka wa 1953. Mwaka huo, Stanley L. Miller aliweza kutengeneza asidi-amino, kemikali za msingi zinazofanyiza protini, kwa kupitisha nguvu za umeme ndani ya mchanganyiko wa gesi zilizodhaniwa kuwa zingewakilisha anga la dunia. Tangu wakati huo, asidi-amino zimepatikana pia katika vimondo. Ugunduzi huo unamaanisha kwamba kemikali za msingi za uhai zinaweza kujitokeza tu zenyewe?

      Robert Shapiro, aliyekuwa profesa wa kemia katika Chuo Kikuu cha New York, asema: “Baadhi ya waandikaji wameamini kwamba kemikali zote za msingi za uhai zinaweza kutengenezwa kwa urahisi kwa kutumia majaribio kama yale ya Miller na kwamba zinapatikana katika vimondo. Hata hivyo sivyo ilivyo.”2b

      Fikiria molekuli ya RNA. Imefanyizwa na molekuli ndogo zinazoitwa nukliotidi. Nukliotidi ni aina tofauti ya molekuli na ni tata zaidi kidogo kuliko asidi-amino. Shapiro anasema kwamba “hakuna nukliotidi za aina yoyote zinazoripotiwa kuwa zilitokana na majaribio yanayohusisha umeme wala katika uchunguzi wa vimondo.”3 Pia anasema kwamba uwezekano wa molekuli kujifanyiza bila mpangilio maalum na kujikusanya kutoka kwa kemikali nyingi za msingi “ni mdogo sana hivi kwamba hata kama ungetokea mahali popote katika ulimwengu unaoonekana, lingeonwa bahati njema.”4

      Namna gani molekuli za protini? Zinaweza kufanyizwa kutokana na asidi-amino 50 hivi au maelfu kadhaa ya amino-asidi zilizokusanywa pamoja katika mpangilio hususa wa hali ya juu. Protini ya wastani katika chembe yoyote ina amino-asidi 200. Hata katika chembe hizo kuna maelfu ya aina tofauti-tofauti za protini. Uwezekano wa kwamba protini moja tu iliyo na amino-asidi 100 pekee ingeweza kujifanyiza kwa njia isiyo na mpangilio maalum duniani, umekadiriwa kuwa mara moja tu hivi baada ya kufanya majaribio hayo mara milioni bilioni.

      Mtafiti Hubert P. Yockey, anayeunga mkono fundisho la mageuzi ana maelezo zaidi. Anasema: “Haiwezekani kwamba chanzo cha uhai ni ‘protini tu.’”5 RNA inahitajika kutengeneza protini, hata hivyo, protini zinahusika katika utengenezaji wa RNA. Namna gani ikiwa, licha ya uwezekano huo mdogo sana, protini na molekuli ya RNA zingetokea mahali pamoja wakati uleule? Kuna uwezekano wowote kwamba zinaweza kufanyiza uhai unaoweza kutokeza chembe ambazo zinaweza kuzaana na kuendeleza uhai? “Yaelekea uwezekano wa jambo hilo kujitokeza lenyewe (kukiwa na mchanganyiko usio na mpangilio maalum wa protini na RNA) ni mdogo sana,” asema Dkt. Carol Clelandc, mshiriki wa NASA (National Aeronautics and Space Administration’s Astrobiology Institute). “Hata hivyo,” aendelea, “yaelekea watafiti wengi wanafikiri kwamba ikiwa wataelewa jinsi protini na RNA zinavyojifanyiza kupitia njia za asili, basi kwa njia fulani haitakuwa vigumu kuelewa jinsi kemikali hizo zinavyoshirikiana.” Kuhusu nadharia za leo zinazoeleza jinsi huenda kemikali hizo za msingi zilivyojitokeza zenyewe, anasema: “Hakuna yoyote kati ya nadharia hizo inayoeleza kwa usahihi jinsi jambo hilo lilivyotukia.”6

      Kwa nini ukweli huu ni muhimu? Wazia changamoto inayowakabili watafiti ambao huamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe. Wamepata amino-asidi fulani ambazo zinapatikana pia katika chembe zilizo hai. Kupitia majaribio yaliyofanywa kwa ustadi mkubwa, wametengeneza molekuli tata zaidi katika maabara zao. Hatimaye, wanatarajia kutengeneza sehemu zote zinazohitajiwa ili kuunda chembe “sahili.” Hali yao inaweza kulinganishwa na ya mwanasayansi anayechukua vitu vya asili na kuvigeuza kuwa chuma, plastiki, silikoni, na waya; kisha anatengeneza roboti. Halafu anairatibu roboti hiyo ili iweze kutengeneza roboti nyingine zinazofanana nayo. Kwa kufanya hivyo, anathibitisha nini? Kwamba mtu mwenye akili anaweza kutengeneza mashini yenye kuvutia.

      Vivyo hivyo, ikiwa wanasayansi watawahi kutengeneza chembe, watakuwa wametimiza jambo lenye kustaajabisha kwelikweli—hata hivyo, je, watakuwa wakithibitisha kwamba chembe hiyo inaweza kujitokeza yenyewe bila mwelekezo wowote? Kinyume cha hilo, watakuwa wanathibitisha jambo lililo tofauti kabisa, sivyo?

      Una maoni gani? Uthibitisho wote wa kisayansi kufikia sasa unaonyesha kwamba uhai unaweza kutokezwa tu na uhai ambao tayari upo. Kuamini kwamba hata chembe “sahili” iliyo hai ilijitokeza yenyewe kutokana na kemikali zisizo na uhai, kunahitaji imani kubwa isiyo na msingi.

  • Je, Kweli Kuna Aina Yoyote ya Uhai Inayoweza Kuitwa Duni?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • Wanasayansi wengi husema nini? Chembe zote zilizo hai ziko katika vikundi viwili—zenye kiini na zisizo na kiini. Chembe za wanadamu, wanyama, na mimea zina kiini. Chembe za bakteria hazina kiini. Chembe zenye kiini huitwa eukaryotic. Chembe zisizo na kiini huitwa prokaryotic. Kwa kuwa chembe zisizo na kiini si tata sana kama zile zenye kiini, watu wengi huamini kwamba chembe za wanyama na mimea zilitokana na chembe za bakteria.

      Wengi hufundisha kwamba kwa mamilioni ya miaka, baadhi ya chembe “sahili” zisizo na kiini zilimeza chembe nyingine lakini hazikuzimeng’enya. Badala yake, kulingana na nadharia hiyo, tukio fulani la “asili” lisilotegemea akili, lilifanyiza mabadiliko muhimu kuhusiana na utendaji-kazi wa chembe zilizomezwa na pia kuendelea kuzihifadhi chembe hizo ndani ya chembe “kimelewa” (iliyozimeza) ilipokuwa ikijigawanya.9a

  • Je, Kweli Kuna Aina Yoyote ya Uhai Inayoweza Kuitwa Duni?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • Uthibitisho unafunua nini? Maendeleo katika elimu ya mikrobiolojia yamewawezesha wanasayansi kuchunguza sehemu yenye kustaajabisha ya ndani ya chembe hai sahili za prokaryotic zinazojulikana. Wanasayansi wanaounga mkono mageuzi wanakisia kwamba chembe za kwanza zilizo hai zilifanana na chembe hizo.10

      Ikiwa nadharia ya mageuzi ni ya kweli, basi inapaswa kueleza kinagaubaga jinsi chembe “sahili” ya kwanza ilivyojitokeza yenyewe. Kwa upande mwingine, ikiwa uhai ulitokana na Muumba, kunapaswa kuwa na uthibitisho wa ubunifu wa hali ya juu hata katika viumbe vidogo sana. Kwa nini usitembelee chembe ya prokaryotic? Unapoichunguza, jiulize ikiwa chembe hiyo inaweza kujitokeza yenyewe.

      UKUTA UNAOILINDA CHEMBE

      Ili uingie ndani na kuchunguza chembe ya prokaryotic, utahitaji kusinyaa na kuwa mdogo zaidi ya nukta iliyo mwishoni mwa sentensi hii. Chembe hiyo inalindwa na utando wenye kunyumbulika unaotenda kama ukuta wa matofali unaokizunguka kiwanda. Utando huo ni mwembamba sana hivi kwamba matabaka 10,000 ya utando huo yanalingana na unene wa karatasi moja. Hata hivyo, utando wa chembe ni tata sana kuliko ukuta wa matofali. Jinsi gani?

      Kama ukuta unaolinda kiwanda, utando wa chembe hulinda vitu vilivyo ndani dhidi ya hatari inayoweza kutokea. Hata hivyo, utando huo si mgumu; unaruhusu chembe “kupumua” na hivyo kuwezesha molekuli ndogo, kama oksijeni, kuingia au kutoka. Lakini utando huo huzuia molekuli zilizo tata zaidi zinazoweza kusababisha madhara zisiingie bila chembe kuziruhusu. Utando huo pia huzuia molekuli zenye manufaa zisitoke nje ya chembe. Utando huo hufanya hivyo jinsi gani?

      Kifikirie tena kiwanda. Huenda kina walinzi wanaochunguza bidhaa zinazoingia na kutoka kiwandani kupitia milango iliyo kwenye ukuta. Vivyo hivyo, utando wa chembe una protini za molekuli maalum zinazotenda kama milango na walinzi.

      Baadhi ya protini hizo (1) zina tundu katikati linaloruhusu aina fulani tu ya molekuli kuingia ndani na kutoka nje ya chembe. Protini nyingine ziko wazi upande mmoja wa utando wa chembe (2) na upande mwingine umefungwa. Zina maeneo ya kutia nanga (3) yenye maumbo yanayotoshea dutu fulani hususa. Dutu hiyo inapotia nanga, upande ule mwingine wa protini hufunguka na kuiachilia dutu hiyo kupitia utando (4). Mambo yote hayo hufanyika katika sehemu ya nje ya hata chembe sahili zaidi.

      NDANI YA KIWANDA

      Tuseme “walinzi” wamekuruhusu kuingia na sasa uko ndani ya chembe. Ndani ya chembe ya prokaryotic kumejaa umajimaji ambao una virutubisho vingi, chumvi, na dutu nyingine. Chembe hutumia viambato hivyo vya msingi kutengeneza bidhaa inazohitaji. Hata hivyo, mambo hayo hayatendeki kiholela. Kama kiwanda kinachoendeshwa vizuri, chembe hupanga utendaji mbalimbali wa maelfu ya kemikali ili ufanyike kwa utaratibu hususa na kulingana na wakati ulioratibiwa.

      Chembe hutumia muda mwingi kutengeneza protini. Inafanya hivyo jinsi gani? Kwanza, utaona chembe ikitengeneza kemikali za msingi 20 hivi zinazoitwa asidi-amino. Kemikali hizo za msingi hupelekwa hadi kwenye ribosomu (5), zinazoweza kulinganishwa na mashine zinazojiendesha zenyewe ambazo zinaunganisha asidi-amino katika utaratibu fulani ili kutengeneza protini hususa. Kama vile ambavyo huenda utendaji wote wa kiwanda ukaongozwa na programu ya kompyuta, utendaji mwingi wa chembe unaongozwa na “programu ya kompyuta” au molekuli ya DNA (6). Ribosomu hupokea kutoka kwa DNA nakala yenye maagizo kamili inayoiambia ni protini gani itakayotengeneza na jinsi ya kuitengeneza (7).

      Kinachotokea protini inapotengenezwa ni chenye kustaajabisha! Kila moja hujikunja na kufanyiza umbo la kipekee lenye nyuso tatu (8). Umbo hilo ndilo linaloamua kazi hususa ambayo protini hiyo itafanya.b Wazia sehemu za injini zikiunganishwa pamoja. Kila sehemu inapaswa kutengenezwa kwa usahihi kabisa ili injini hiyo ifanye kazi. Vivyo hivyo, ikiwa protini haijatengenezwa kwa usahihi kamili na kukunjwa katika umbo hususa, haitaweza kufanya kazi yake vizuri na huenda hata ikaharibu chembe.

      Protini inajuaje njia kutoka mahali ilipotengenezewa mpaka mahali inapohitajika? Kila protini inayotengenezwa na chembe inakuwa na “anwani” ili kuhakikisha kwamba protini hiyo itafika mahali inapohitajika. Ingawa maelfu ya protini hutengenezwa na kutumwa kila dakika, kila moja hufika mahali inapohitajika.

      Kwa nini ukweli huu ni muhimu? Molekuli tata zilizo ndani ya vitu sahili vilivyo hai haziwezi kujizalisha. Zikiwa nje ya chembe, molekuli hizo hujigawanya. Zikiwa ndani ya chembe, haziwezi kujizalisha bila msaada wa molekuli nyingine tata. Kwa mfano, vimeng’enya vinahitajiwa ili kutengeneza molekuli ya pekee ya nishati inayoitwa adenosine triphosphate (ATP), hata hivyo, nishati kutoka kwa ATP inahitajika ili kutengeneza vimeng’enya. Vivyo hivyo, DNA (sehemu ya 3 inazungumzia molekuli hiyo) inahitajika ili kutengeneza vimeng’enya, hata hivyo, vimeng’enya vinahitajika ili kutengeneza DNA. Pia, protini nyingine zinaweza tu kutengenezwa na chembe, hata hivyo, chembe inafanyizwa kwa protini.c

      Mwanasayansi Radu Popa hakubaliani na masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji. Hata hivyo, katika mwaka wa 2004 aliuliza: “Mambo ya asili yanawezaje kutokeza uhai ikiwa baada ya kufanya majaribio yote hayo kwa makini sana tumeshindwa?”13 Pia alisema: “Mifumo tata inayohitajika kwa ajili ya utendaji wa chembe iliyo hai ni ya hali ya juu sana hivi kwamba haingeweza kujitokeza yenyewe kwa wakati uleule.”14

      Una maoni gani? Watu wanaoamini nadharia ya mageuzi husema kwamba Mungu hakuhitaji kuingilia kati ili kutokeza uhai duniani. Hata hivyo, kadiri wanasayansi wanavyozidi kuelewa mambo fulani kuhusu uhai, ndivyo wanavyotambua kwamba haiwezekani kuwa ulijitokeza wenyewe. Ili kuepuka utata huo, wanasayansi fulani wanaoamini mageuzi, wangependa kutenganisha nadharia ya mageuzi na suala la chanzo cha uhai. Lakini kwa maoni yako, hilo linapatana na akili?

      Nadharia ya mageuzi inategemea dhana ya kwamba mfuatano wa matukio mengi yasiyoelekezwa yalianzisha uhai. Kisha nadharia hiyo inadokeza kwamba mfuatano mwingine wa matukio ya kiholela ulitokeza aina mbalimbali zenye kustaajabisha na tata za vitu vyote vilivyo hai. Hata hivyo, ikiwa nadharia hiyo haina msingi, namna gani zile nadharia nyingine zinazoitegemea? Kama vile ghorofa lililojengwa bila msingi litakavyoporomoka, ndivyo nadharia ya mageuzi ambayo haiwezi kueleza chanzo cha uhai itakavyoporomoka.

  • Maagizo Yalitoka Wapi?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • Wanasayansi wengi husema nini? Wanabiolojia wengi na wanasayansi fulani hufikiri kwamba DNA pamoja na maagizo yake yaliyopangwa vilitokana na matukio yaliyojitokeza yenyewe ambayo yalifanyika kwa kipindi cha mamilioni ya miaka. Wanasema kwamba hakuna uthibitisho wa ubuni katika maumbile ya molekuli hiyo wala katika habari inayobeba na kuituma wala jinsi inavyofanya kazi.17

  • Maagizo Yalitoka Wapi?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • Uthibitisho unafunua nini? Ikiwa fundisho la mageuzi ni la kweli, basi inapaswa angalau kuonekana kwamba huenda DNA ilijitokeza yenyewe kupitia mfuatano wa matukio.

  • Maagizo Yalitoka Wapi?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • UMBO LA MOLEKULI YENYE KUSTAAJABISHA

      Acheni tuifananishe sehemu hii ya kromosomu ya mfano na kamba. Ina unene wa sentimita 2.6 hivi. Imefungwa kwa mkazo sana kuzunguka vibiringo (4), ambavyo husaidia kutengeneza koili ndani ya koili. Koili hizo zimeunganishwa kwa kitu kama nguzo ambayo huzishikilia. Maelezo kwenye ubao yanaonyesha kwamba kamba hiyo imepangwa vizuri. Ikiwa ungeivuta kamba hiyo kutoka kwenye kila kromosomu hizo za mfano na kuinyoosha yote kutoka mwisho mmoja hadi mwingine, urefu wake unaweza kufika karibu nusu ya dunia!a

      Kitabu kimoja cha sayansi kinauita mfumo huo wa kupanga “mafanikio makubwa ya uhandisi.”18 Je, maoni ya kwamba hakuna mhandisi aliyehusika katika mafanikio hayo yanakusadikisha? Ikiwa jumba hilo la maonyesho lingekuwa na bohari kubwa yenye mamilioni ya bidhaa za kuuza ambazo zimepangwa vizuri sana hivi kwamba ungeweza kupata chochote unachohitaji kwa urahisi, ungesema kwamba hakuna mtu aliyepanga bohari hiyo? Bila shaka hapana! Hata hivyo, utaratibu huo ni wa hali ya chini ukilinganishwa na ule tunaozungumzia.

      Kwenye ubao wa maelezo katika jumba la makumbusho, unaalikwa kuchukua kiasi fulani cha kamba hiyo na kuitazama kwa ukaribu (5). Unapoipitisha kwenye vidole vyako, unatambua kwamba hiyo si kamba ya kawaida. Imefanyizwa kwa nyuzi mbili zilizosokotwa pamoja. Nyuzi hizo zimeunganishwa kwa fito ndogo-ndogo zinazoachana kwa nafasi ileile. Kamba hiyo inafanana ngazi iliyosokotwa mpaka ikafanana na ngazi ya mzunguko (6). Kisha unatambua: Mkononi mwako una molekuli ya DNA ya mfano—mojawapo ya maajabu makubwa ya uhai!

      Molekuli moja ya DNA iliyopangwa kwa utaratibu pamoja na vibiringo na nguzo zake, hufanyiza kromosomu moja. Vipago vya ngazi huitwa pea za msingi (7). Hivyo hufanya kazi gani? Vyote hivyo ni vya nini? Unapata maelezo rahisi kwenye ubao wa maelezo.

      MFUMO WA PEKEE WA KUHIFADHI HABARI

      Kulingana na ubao wa maelezo, ili kuelewa DNA, lazima mtu aelewe kwanza vile vipago, yaani, fito zinazounganisha sehemu mbili za ngazi. Wazia ngazi ikiwa imekatwa mara mbili. Kila kipande kina vipago vinavyotokeza. Vipago hivyo ni vya aina nne tu. Wanasayansi huviita A, T, G, na C. Wanasayansi walishangaa kugundua kwamba mpangilio wa herufi hizo hutuma habari kwa njia fulani iliyofupishwa.

      Huenda unajua kwamba mawasiliano ya Morse yalianzishwa katika karne ya 19 ili watu waweze kuwasiliana kwa njia ya telegrafu. Mfumo huo ulitumia “herufi” mbili tu—nukta na kistari. Hata hivyo, “herufi” hizo zingeweza kutumiwa kuwakilisha maneno au sentensi nyingi. Mfumo wa DNA una herufi nne. Mpangilio wa herufi hizo—A, T, G, na C—hufanyiza “maneno” yanayoitwa codons. Codons zimepangwa katika “maghorofa” yanayoitwa chembe za urithi. Kwa wastani, kila chembe ya urithi ina herufi 27,000. Chembe hizo pamoja na mitanuko iliyo kati yake huungana na kufanyiza vitu kama sura za kitabu—kromosomu mojamoja. Kromosomu 23 zinahitajika ili kutengeneza “kitabu” kizima—habari zote kuhusu chembe za urithi za kiumbe kilicho hai.b

      Chembe za urithi zingekuwa kitabu kikubwa. Kingekuwa na habari nyingi kadiri gani? Kwa ujumla, chembe za urithi za mwanadamu hufanyizwa kwa pea za msingi au vipago bilioni tatu hivi kwenye ngazi ya DNA.19 Wazia ensaiklopedia kadhaa ambazo kila moja ina zaidi ya kurasa 1,000. Chembe za urithi zinaweza kujaza mabuku 428 ya aina hiyo. Ukiongeza nakala ya pili iliyo katika kila chembe utapata jumla ya mabuku 856. Ikiwa ungechapa mabuku hayo ya chembe hizo za urithi wewe mwenyewe, ingekuwa kazi ya kudumu—bila likizo—ambayo ingekuchukua miaka 80 hivi!

      Bila shaka, kazi ya aina hiyo ingekuwa yenye kuchosha tu. Ungeweza jinsi gani kujaza mamia ya mabuku makubwa kwenye kila moja ya chembe zako ndogo sana trilioni 100? Kushindilia habari nyingi kadiri hiyo na kwa njia bora hivyo ni jambo linalopita uwezo wetu.

      Profesa fulani wa sayansi ya molekuli na kompyuta alisema: “Gramu moja ya DNA, ambayo ikikaushwa inaweza kuchukua ujazo wa sentimita moja ya mchemraba, ina habari nyingi kama zile zinazoweza kutoshea katika diski trilioni moja hivi.”20 Hilo linamaanisha nini? Kumbuka kwamba DNA ina chembe za urithi, maagizo yanayofanyiza mwili wenye kustaajabisha wa mwanadamu. Kila chembe ina maagizo kamili. DNA ina habari nyingi sana hivi kwamba chembe zinazotoshea kwenye kijiko cha chai zinaweza kubeba maagizo yanayotosha kufanyiza idadi ya wanadamu wote walio hai leo, mara 350! DNA inayohitajika kufanyiza watu bilioni saba wanaoishi duniani leo haiwezi hata kufanyiza utando mwembamba kwenye kijiko hicho.21

      KITABU KISICHO NA MWANDIKAJI?

      Licha ya maendeleo katika kupunguza ukubwa wa vitu, hakuna kifaa chochote cha kuhifadhi habari kilichotengenezwa na mwanadamu kinachoweza kukaribia uwezo wa DNA. Hata hivyo, tunaweza kuilinganisha na diski. Fikiria hili: Huenda diski ikatushangaza kwa sababu ya muundo wake mzuri, sehemu yake ya juu inayong’aa, mpangilio wake mzuri. Tunaona uthibitisho ulio wazi kwamba watu wenye akili waliitengeneza. Namna gani ikitiwa habari—si habari yoyote tu bali habari yenye kueleweka, maagizo kamili ya kujenga, kudumisha, na kufanyia marekebisho mitambo tata? Habari hiyo haibadilishi uzito au ukubwa wa diski hiyo. Hata hivyo, habari hiyo ndiyo sehemu muhimu zaidi ya diski hiyo. Je, maagizo hayo yaliyoandikwa hayakusadikishi kwamba kuna mtu mwenye akili anayehusika? Je, maandishi hayahitaji mwandikaji?

      Tunaweza kuilinganisha DNA na diski au kitabu. Kitabu kimoja kinachozungumzia chembe za urithi kinasema: “Kusema kweli, kulinganisha chembe za urithi na kitabu hata si usemi wa kitamathali. Ni kweli kabisa. Habari za kielektroniki hufanyiza kitabu . . . Na ndivyo na chembe za urithi.” Mwandikaji huyo aongezea: “Chembe za urithi ni kitabu chenye ujuzi mwingi kwa sababu katika hali nzuri kinaweza kujinakili na kujisoma chenyewe.”22 Hilo linatokeza sehemu nyingine muhimu ya DNA.

      MASHINI ZILIZO MWENDONI

      Ukiwa umesimama kwa utulivu, unashangaa ikiwa kwa kweli kiini cha chembe kimesimama tuli kama jumba la makumbusho. Kisha unaona ubao mwingine wa maelezo. Juu ya chombo cha glasi kuna DNA ya mfano yenye maandishi yanayosema: “Bonyeza Kitufe Upate Ufafanuzi.” Unabonyeza kitufe, naye msimuliaji anasema: “DNA inatimiza angalau kazi mbili muhimu. Kwanza inatokeza nakala yake. Lazima DNA inakiliwe ili kila chembe mpya iwe na nakala kamili ya habari zilezile za chembe za urithi. Tafadhali tazama onyesho hili.”

      Mashini inayoonekana kuwa tata inaingia kupitia mlango ulio upande mmoja wa ubao wa maelezo. Ni roboti nyingi zilizounganishwa pamoja. Mashini hiyo inaenda kwa DNA, inajipachika, na kuanza kusonga pamoja na DNA kama vile gari-moshi linavyofuata reli. Inasonga kwa kasi hivi kwamba huwezi kuona kwa urahisi kinachoendelea, lakini unaweza kuona kwamba nyuma yake sasa kuna kamba mbili zilizokamilika za DNA badala ya moja.

      Msimuliaji anaeleza: “Hii ni njia rahisi sana ya kuonyesha kinachoendelea DNA inapojinakili. Kikundi cha molekuli zinazoitwa vimeng’enya husafiri pamoja na DNA, kwanza zinajigawanya katika sehemu mbili, kisha zinatumia kila uzi kama kigezo cha kutengeneza uzi mwingine mpya unaofanana nao. Hatuwezi kukuonyesha sehemu zote zinazohusika—kama vile kifaa ambacho hutangulia mashini ya kunakili na kukata upande mmoja wa DNA ili iweze kujizungusha kwa urahisi bila kujifunga. Wala hatuwezi kukuonyesha jinsi DNA ‘inavyosahihishwa’ mara kadhaa. Makosa yanagunduliwa na kusahihishwa kwa usahihi wa hali ya juu sana.”—Ona picha katika ukurasa wa 16 na 17.

      Msimuliaji anaendelea: “Kile tunachoweza kukuonyesha waziwazi ni mwendo. Uliona roboti hii ikisonga kwa mwendo wa kasi sana, sivyo? Kimeng’enya husonga kwenye ‘njia’ ya DNA kwa kiwango cha vipago au pea za msingi 100 hivi kwa kila sekunde.23 Ikiwa ‘njia’ hiyo ingekuwa na ukubwa wa reli, ‘injini’ hiyo ingekuwa ikikimbia kwa mwendo wa zaidi ya kilomita 80 kwa saa. Katika bakteria, mashini za kunakili zinaweza kusonga kwa kasi mara kumi zaidi ya mwendo huo! Katika chembe ya mwanadamu, mamia ya mashini hizo za kunakili hufanya kazi katika sehemu tofauti-tofauti kando ya ‘njia’ ya DNA. Mashini hizo hunakili chembe zote za uhai kwa saa nane tu.”24 (Ona sanduku “Molekuli Inayoweza Kusomwa na Kunakiliwa,” katika ukurasa wa 20.)

      “KUSOMA” DNA

      Roboti za kunakili DNA zinabingirika na kuondoka jukwaani. Mashini nyingine inatokea. Hiyo pia inasonga katika mtanuko wa DNA, lakini polepole. Unaona kamba ya DNA ikiingia upande mmoja wa ile mashini na kutokea upande mwingine—bila kubadilika. Lakini uzi mmoja mpya unatokea kwenye tundu tofauti la mashini hiyo kama mkia unaoota. Ni nini kinachoendelea?

      Tena msimuliaji anafafanua: “Kazi ya pili ya DNA ni kurekodi. DNA haiondoki ndani ya kiini. Hivyo basi, chembe zake za urithi—viambato vya protini vinavyofanyiza mwili wako—zinaweza kusomwa na kutumiwa jinsi gani? Mashini hiyo ya vimeng’enya inapata mahali kando ya DNA ambapo chembe ya urithi ilikuwa imewashwa na kemikali zinazoingia kutoka nje ya kiini cha chembe. Kisha mashini hiyo inatumia molekuli inayoitwa RNA (ribonucleic acid) kutengeneza nakala ya chembe hiyo ya urithi. Molekuli ya RNA inafanana sana na uzi mmoja wa DNA, lakini zinatofautiana. Kazi yake ni kuchukua habari zilizo ndani ya chembe za urithi. Molekuli ya RNA inapokea habari hiyo ikiwa ndani ya mashini ya kimeng’enya, kisha inaondoka kwenye kiini na kwenda kwa mojawapo ya ribosomu ambapo habari hiyo itatumiwa kutengeneza protini.”

      Unapoendelea kutazama onyesho hilo, unajawa na mshangao. Unavutiwa sana na jumba hilo la makumbusho na ujuzi wa waliochora ramani yake na kujenga mitambo yake. Lakini namna gani ikiwa jumba hilo lote pamoja na vifaa vyote vilivyomo vingeanza kutenda, vikionyesha kazi nyingi mbalimbali zinazofanyika ndani ya chembe ya mwanadamu wakati uleule mmoja? Hilo lingekuwa onyesho lenye kustaajabisha kama nini!

      Hata hivyo, unagundua kwamba mambo hayo yote yanayofanywa na mashini ndogo lakini tata sana yanaendelea sasa hivi ndani ya chembe zako trilioni 100! DNA yako inasomwa, ikitoa maagizo ya kutengeneza mamia ya maelfu ya protini tofauti-tofauti zinazofanyiza mwili wako—vimeng’enya vyake, tishu, viungo, na kadhalika. Sasa hivi DNA yako inanakiliwa na kusahihishwa ili kupata maagizo mengine mapya yatakayosomwa katika kila chembe mpya.

      KWA NINI UKWELI HUU NI MUHIMU?

      Acheni tujiulize tena, ‘Maagizo yote hayo yalitoka wapi?’ Biblia inasema kwamba “kitabu” hiki pamoja na maandishi yake yanatokana na Mwandikaji anayepita uwezo wa mwanadamu. Je, kauli hiyo imepitwa na wakati au haipatani na sayansi?

      Fikiria hili: Wanadamu wanaweza hata kujenga jumba hilo ambalo tumezungumzia? Ikiwa wangejaribu, wangekumbana na matatizo mengi. Mambo mengi kuhusu chembe za urithi za mwanadamu na jinsi zinavyofanya kazi hayajaeleweka bado. Wanasayansi bado wanajaribu kuelewa mahali chembe zote za urithi zinapatikana na kazi zake. Nazo chembe za urithi zina sehemu ndogo tu ya uzi wa DNA. Namna gani ile mitanuko mingine isiyo na chembe za urithi? Wanasayansi wameiita mitanuko hiyo, DNA zisizohitajiwa, hata hivyo, hivi karibuni wamekuwa wakirekebisha maoni hayo. Huenda mitanuko hiyo ikadhibiti jinsi na kwa kadiri gani chembe za urithi zinavyotumika. Hata kama wanasayansi wangetengeneza mfano kamili wa DNA na mashini za kunakili na kusahihisha, je, wangeweza kuufanya ufanye kazi kama DNA halisi?

      Mwanasayansi mashuhuri Richard Feynman aliacha ujumbe huu ubaoni muda mfupi kabla ya kifo chake: “Kile ambacho siwezi kutengeneza, sikielewi.”25 Unyenyekevu wake unavutia na maneno yake ni ya kweli kabisa kuhusiana na DNA. Wanasayansi hawawezi kutengeneza DNA pamoja na uwezo wake wa kujinakili na kujirekodi; wala hawawezi kuielewa kikamili. Hata hivyo, wengine hudai kwamba wanajua ilijitokeza yenyewe bila kuelekezwa. Je, kweli uthibitisho ambao umechunguza unaunga mkono kauli hiyo?

      Wasomi fulani wameamua kwamba uthibitisho huo una maana tofauti. Kwa mfano, Francis Crick, mwanasayansi aliyegundua kwamba DNA inafanana na ngazi ya mzunguko, aliamua kwamba molekuli hiyo imepangwa kwa utaratibu sana hivi kwamba haiwezi kuwa ilijitokeza yenyewe bila kufuata mpangilio maalum. Alipendekeza kwamba huenda viumbe fulani wenye akili kutoka nje ya dunia vilituma DNA duniani ili kuanzisha uhai.26

      Hivi karibuni zaidi, mwanafalsafa mashuhuri Antony Flew, aliyeunga mkono fundisho la kwamba hakuna Mungu kwa miaka 50, alibadili maoni yake. Akiwa na umri wa miaka 81 alikiri kwamba mtu fulani mwenye akili aliumba uhai. Kwa nini alibadili maoni yake? Baada ya kuichunguza DNA. Alipoambiwa kwamba huenda maoni yake mapya yasikubaliwe na wanasayansi, inasemekana Flew alijibu: “Inasikitisha. Maishani mwangu nimeongozwa na kanuni . . . fuata uthibitisho, popote utakapokuelekeza.”27

      Una maoni gani? Uthibitisho unaelekeza wapi? Wazia kwamba umepata chumba cha kompyuta katikati mwa kiwanda. Kompyuta hiyo inaendesha programu tata inayoelekeza kazi zote kiwandani. Isitoshe, programu hiyo daima inatuma maagizo kuhusu jinsi ya kuunda na kudumisha kila mashini, nayo inajinakili na kujisahihisha. Uthibitisho huo utakusaidia ufikie mkataa gani? Kwamba kompyuta hiyo na programu yake vilijitengeneza vyenyewe, au kwamba vilitengenezwa na watu wenye utaratibu na akili? Uthibitisho uko wazi.

  • Maagizo Yalitoka Wapi?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
    • [Sanduku katika ukurasa wa 21]

      UKWELI WA MAMBO NA MASWALI

      ◼ Ukweli wa mambo: Molekuli ya DNA imetiwa ndani ya kromosomu kwa njia yenye utaratibu sana hivi kwamba imeitwa “mafanikio ya kihandisi.”

      Swali: Utaratibu wa aina hiyo ungeweza kujitokezaje wenyewe bila kuelekezwa?

      ◼ Ukweli wa mambo: Hakuna kompyuta yoyote leo iliyo na uwezo mkubwa wa kuhifadhi habari kama DNA.

      Swali: Ikiwa mafundisanifu wa kompyuta hawawezi kuwa na matokeo kama hayo, kitu kisicho na akili kingeweza kufanya hivyo jinsi gani bila kuongozwa?

      ◼ Ukweli wa mambo: DNA ina maagizo yote yanayohitajika kutokeza mwili usio na kifani wa mwanadamu na kuudumisha katika maisha yake yote.

      Swali: Maandishi hayo yangetokeaje bila mwandikaji, programu hiyo ingetokeaje bila mtengenezaji wa programu?

      ◼ Ukweli wa mambo: Ili DNA ifanye kazi, lazima inakiliwe, isomwe, na kusahihishwa na kikundi cha molekuli tata zinazoitwa vimeng’enya, ambavyo lazima vishirikiane kwa utaratibu wa hali ya juu na upesi sana.

      Swali: Je, unaamini kwamba mitambo ya hali ya juu sana na yenye kutegemeka inaweza kujitokeza yenyewe? Bila uthibitisho kamili, je, hiyo haingekuwa sawa na kuwa na imani bila msingi?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki