Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mashini Yenye Uwezo Mkubwa Zaidi Ulimwenguni”
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • “Mashini Yenye Uwezo Mkubwa Zaidi Ulimwenguni”

      UBONGO wa mtoto mchanga umesemwa kuwa ndiyo “mashini yenye uwezo mkubwa zaidi ulimwenguni,” na kwa sababu nzuri. Mtoto anazaliwa akiwa tayari kufyonza kila kitu anachoona, kusikia, na kugusa.

      Zaidi ya yote, mtoto huvutiwa na wanadamu wengine, yaani, anavutiwa watu wanapomgusa, anavutiwa na nyuso na sauti zao. Kitabu Babyhood, kilichoandikwa na Penelope Leach, kinasema hivi: “Uchunguzi mwingi umefanywa kuhusu mambo yanayovutia zaidi macho ya mtoto, sauti zinazovuta fikira zake, na vitu anavyopenda kugusa mara nyingi. Yote hayo hutimizwa kwa urahisi na mtu mzima anayemtunza.” Haishangazi kwamba wazazi wanatimiza fungu muhimu katika ukuzi wa mtoto!

      ‘Nilisema Kama Kitoto’

      Wazazi na vilevile madaktari wa watoto wanashangazwa sana na uwezo wa mtoto wa kujifunza lugha kwa kuisikia tu. Watafiti wamegundua kwamba siku chache tu baada ya kuzaliwa, mtoto anajua sauti ya mama yake na anaipenda kuliko sauti ya mtu asiyemfahamu; majuma machache tu baadaye, anaweza kutofautisha kati ya sauti za lugha ya wazazi wake na za lugha nyingine; na miezi michache baadaye, anajua tofauti kati ya maneno na hivyo anaweza kutofautisha usemi wa kawaida na sauti zisizoweza kueleweka.

      Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Nilipokuwa mtoto mchanga nilisema kitoto.” (1 Wakorintho 13:11, Biblia Habari Njema) Mtoto mchanga husema kwa njia gani? Kwa kawaida anabubujika kwa mambo yasiyoeleweka. Je, hizo ni kelele tu zisizo na maana? La! Katika kitabu chake What’s Going On in There?—How the Brain and Mind Develop in the First Five Years of Life, Dakt. Lise Eliot anatukumbusha kwamba kusema kunahusisha “ustadi wa ajabu wa ubongo wa kutendesha misuli inayodhibiti midomo, ulimi, kaakaa, na zoloto na kuifanyisha kazi kwa haraka na upatano.” Anaongezea hivi: “Ingawa huenda ikaonekana kwamba kusudi la sauti zisizoeleweka za watoto wachanga ni kuvuta fikira za watu tu, sauti hizo hutimiza jambo muhimu katika kuzoeza misuli kusonga kwa upatano wakati atakapoanza kuongea.”

      Wazazi wanapoongea kwa msisimuko mwingi pamoja na mtoto wao mchanga anapopiga kelele zisizoeleweka, hilo hutimiza kusudi fulani. Msisimuko huo humchochea mtoto aendelee kutokeza sauti hizo. Mazungumzo hayo kati ya mtoto na wazazi humfundisha mtoto mchanga mambo yanayohusika katika mazungumzo—ustadi ambao atautumia katika maisha yake yote.

      Majukumu Yanabadilika

      Wazazi wa mtoto mchanga huwa na shughuli nyingi za kumtimizia mtoto wao mahitaji yake ya kila siku. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumlisha. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumbadilisha nepi. Mtoto anapolia, lazima kuwe na mtu wa kumbeba. Utunzaji huo unafaa na unahitajika. Hiyo ndiyo njia kuu ambayo wazazi wanatimiza jukumu lao wakiwa watunzaji.—1 Wathesalonike 2:7.

      Ukizingatia mambo yaliyozungumziwa hapa juu, ni jambo la asili kwa mtoto kuhisi kwamba yeye ndiye mtu muhimu zaidi na kwamba watu wazima, hasa wazazi wake, wapo ili tu kumtimizia mahitaji yake yote. Maoni hayo yana kasoro lakini inaeleweka ni kwa nini anahisi hivyo. Kumbuka kwamba kwa zaidi ya mwaka mmoja, hivyo ndivyo mtoto amezoea kutendewa. Kwa maoni yake, yeye ni mfalme wa milki fulani iliyo na watu wakubwa ambao wamewekwa hapo ili tu wamtumikie. John Rosemond, mshauri wa mambo ya familia anaandika hivi: “Kwa muda usiozidi miaka miwili, mtoto amefundishwa kuwa na maoni hayo; inachukua miaka kumi na sita hivi kuyarekebisha! Na jambo la kushangaza ni kwamba wazazi ndio walio na jukumu la kufanya hivyo: wao ndio humfanya mtoto awe na maoni hayo, kisha kwa upole wanamfundisha kwamba maoni hayo hayafai.”

      Anapofikia umri wa miaka miwili hivi, mtoto anaanza kutambua kwamba maoni yake hayafai mzazi anapoacha kuwa mtunzaji na kuanza kuwa mfundishaji. Sasa mtoto anatambua kwamba wazazi wake hawatii amri yake; badala yake yeye ndiye anayetarajiwa kutii amri yao. Serikali yake imepinduliwa, na huenda asifurahie mabadiliko hayo. Akiwa amekasirika, anajaribu kushikilia mamlaka yake juu ya wazazi. Jinsi gani?

      Kukabiliana na Milipuko ya Hasira

      Wanapofikia umri wa miaka miwili hivi, tabia za watoto wengi hubadilika sana, hilo likitia ndani kuwa na milipuko ya hasira. Hicho huwa kipindi kigumu sana kwa wazazi. Kwa ghafula, mtoto wako anatumia sana maneno “Hapana!” au “Sitaki!” Huenda akawa na hasira kujielekea au kuwaelekea wazazi wake huku akipambana na hisia zake zinazobadilika-badilika. Anataka kukaa mbali nawe, na wakati huohuo, anataka kuwa karibu nawe. Wazazi waliochanganyikiwa hawajui la kufanya, hawana suluhisho. Tatizo ni nini?

      Hebu fikiria mabadiliko makubwa ambayo yametukia katika maisha ya mtoto. Hadi hivi karibuni, alihitaji tu kutoa kilio, na watu wazima walimtimizia mahitaji yake mara moja. Sasa anaanza kutambua kwamba “utawala” wake ulikuwa wa muda tu na sasa itabidi ajifanyie mambo fulani. Pole kwa pole, anaanza kutambua kwamba anapaswa kujitiisha kama Biblia inavyosema: “Watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo.”—Wakolosai 3:20.

      Wakati wa kipindi hicho kigumu, wazazi wanapaswa kushikilia mamlaka yao. Wakifanya hivyo kwa uthabiti lakini kwa upendo, mtoto atazoea jukumu lake jipya. Na mambo atakayojifunza yatamsaidia kadiri anavyokua.

      Kusitawisha Utu Wake

      Wanyama, na hata mashini, zinaweza kutambua maneno na kuiga usemi. Lakini ni mwanadamu peke yake anayeweza kutua na kujichunguza. Kwa hiyo, mtoto anapokuwa na umri wa miaka miwili au mitatu hivi, anakuwa na hisia za kujitutumua, kuaibika, kuhisi hatia, na kadhalika. Hizo ni hatua za kwanza za kuwa mtu mzima mwenye sifa za kiadili—mtu anayeweza kusimama imara na kutetea lililo sawa, hata wengine wanapofanya jambo baya.

      Kufikia hatua hiyo, wazazi wanafurahia jambo lingine. Mtoto wao anaanza kujali hisia za wengine. Alipokuwa na umri wa miaka miwili, alikuwa akicheza kando ya wenzake, lakini sasa anacheza pamoja nao. Pia anatambua wakati ambapo wazazi wake wanafurahia jambo fulani, na huenda akataka kuwafurahisha. Kwa hiyo, inaelekea kwamba ataweza kufundishwa kwa urahisi.

      Mtoto anapotimia umri wa miaka mitatu anaanza kujifunza yaliyo sawa na yasiyo sawa, mema na mabaya. Ni wazi kwamba huo ndio wakati wa wazazi kuwafundisha watoto wao kuwa watu wazima wanaotegemeka.

      [Blabu katika ukurasa wa 5]

      Siku chache tu baada ya kuzaliwa, mtoto anajua sauti ya mama yake na anaipenda kuliko sauti ya mtu asiyemfahamu

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Mtoto anapotimia umri wa miaka mitatu anaanza kujifunza yaliyo sawa na yasiyo sawa, mema na mabaya

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      SABABU INAYOMFANYA MTOTO AENDELEE KULIPUKA KWA HASIRA

      “Wazazi fulani hudhani kwamba mtoto analipuka kwa hasira kwa sababu hawakumtimizia mahitaji yake,” anaandika John Rosemond, katika kitabu New Parent Power. “Kwa hiyo, wazazi hudhani kwamba ikiwa wao ndio wamesababisha mtoto alipuke kwa hasira, basi lazima warekebishe kosa hilo haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, ikiwa walikuwa wamekataa jambo fulani wanabadili nia mara moja na kulikubali. Au baada ya kumchapa mtoto, wanampa zaidi ya alichotaka, ili wasihisi hatia. Mbinu hiyo hufanikiwa. Mtoto huacha kulipuka kwa hasira, mzazi anatulia, na mtoto anajua kwamba akilipuka kwa hasira atapewa anachotaka, kwa hiyo anatumia mbinu hiyo tena na tena.”

  • Maoni ya Wazazi
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Maoni ya Wazazi

      Ikiwa wewe ni mzazi wa mtoto ambaye hajaanza kwenda shule, huenda ukawa na kibarua kigumu. Kwa mfano, utakabiliana jinsi gani na milipuko ya hasira ya mtoto? Unaweza kutumia njia gani kumfundisha mtoto wako ajue jema na baya na umrekebishe kwa njia yenye usawaziko? Ona jinsi wazazi fulani walivyokabiliana na changamoto hizo.

      MILIPUKO YA HASIRA

      “Katika miaka miwili ya kwanza, mtoto hutarajia apewe anachotaka. Mtoto wetu alikuwa na tatizo hilo. Kama asingepewa alichotaka, angerusha vitu. Kwa kuwa alikuwa mtoto wetu wa kwanza, hatukujua jinsi ya kushughulika na milipuko ya hasira. Hata wazazi wenzetu walipotuambia kwamba jambo hilo ni la kawaida kwa watoto walio na umri huo, hatukufarijika kwa njia yoyote.” —Susan, Kenya.

      “Alipokuwa na umri wa miaka miwili, binti yetu angelala kwenye sakafu, apige kelele, alie, na kurusharusha miguu yake hewani . . . Jambo hilo lilikuwa linaudhi kama nini! Ilikuwa kazi ya bure kujaribu kuongea naye wakati kama huo. Kwa hiyo, mimi na mume wangu tungempeleka chumbani mwake na kumwambia kwa upole kwamba atakapoacha kulia, anaweza kutoka, kisha tuzungumze kuhusu jambo hilo. Alipotulia, mmoja wetu angeingia chumbani mwake na kumsaidia atambue kwamba tabia yake si nzuri. Mbinu hiyo ilifanikiwa. Hata wakati mmoja tulimsikia akimwomba Yehova msamaha. Kadiri wakati ulivyopita, milipuko yake ilipungua na hatimaye ikaisha kabisa.”—Yolanda, Hispania.

      “Watoto wachanga hujaribu sana kupima ikiwa wanaweza kufanya mambo fulani bila kuadhibiwa. Mtoto huchanganyikiwa anapoachwa tu afanye jambo alilokatazwa. Tuligundua kwamba tulipokuwa imara, bila kubadili sheria, watoto wetu walijifunza hatua kwa hatua kwamba kupiga kelele hakungewasaidia kupata wanachotaka.”—Neil, Uingereza.

      NIDHAMU

      “Mtoto anapokuwa chini ya umri wa miaka mitano, ni vigumu sana kujua ikiwa anakusikiliza. Ni jambo la maana sana kurudia-rudia mambo unayomwambia. Yarudie mara nyingi kadiri unavyoweza, ukitumia ishara na sauti thabiti.”—Serge, Ufaransa.

      “Hata ingawa tuliwalea katika mazingira yaleyale, kila mmoja wa watoto wetu wanne alikuwa tofauti kabisa. Binti mmoja angelia mara tu alipotambua ametuudhi; mwingine angejaribu kutupima aone ikiwa tungemwacha afanye mambo fulani bila kumwadhibu. Nyakati nyingine, ingetosha tu kumtazama mtoto kwa ukali au kumkemea, ilhali nyakati nyingine ingebidi kutoa adhabu hususa.”—Nathan, Kanada.

      “Ni muhimu sana kwamba usilegeze msimamo wako. Lakini wakati huohuo, mzazi hapaswi kushikilia sana maoni yake au kuwa mkali. Nyakati nyingine, mtoto anapoonyesha kwa kweli anasikitikia kosa alilofanya, tunahisi kwamba ni vyema kuwa na usawaziko na kupunguza adhabu tutakayompa.”—Matthieu, Ufaransa.

      “Mimi hujitahidi sana nisiweke sheria nyingi mno, lakini zile chache ambazo tayari zipo hazibadiliki. Mwanangu mwenye umri wa miaka mitatu anajua matokeo ya kutotii, na hilo humsaidia ajiendeshe kwa njia inayofaa. Ninapokuwa nimechoka, ni rahisi sana kupuuza makosa anayofanya. Lakini ili asione kwamba sheria zinaweza kubadilika, mimi hujilazimisha kuchukua hatua. Kuhakikisha kwamba sheria hazibadiliki-badiliki ni muhimu sana!”—Natalie, Kanada.

      KUTOBADILI SHERIA

      “Watoto wadogo wana kumbukumbu nzuri sana, kwa hiyo wanakumbuka vizuri sana mzazi anapobadili sheria.”—Milton, Bolivia.

      “Wakati mwingine, mwana wangu anauliza jambo moja akitumia njia tofauti ili aone kama tutatoa jibu lilelile. Nikisema jambo moja na mama yake aseme jambo tofauti, anatambua haraka tofauti hiyo na kujaribu kupata anachotaka.”—Ángel, Hispania.

      “Nikiwa na furaha mimi hupuuza tabia mbaya ya mwana wangu, lakini nikiwa nimekasirika mimi humwadhibu kwa hasira. Niligundua kwamba jambo hilo lilifanya azidi kuwa na tabia mbaya.”—Gyeong-ok, Korea.

      “Ni muhimu watoto wadogo waelewe kwamba ikiwa tabia fulani ni mbaya leo, daima itabaki kuwa hivyo.”—Antonio, Brazili.

      “Wazazi wakibadili-badili sheria, mtoto atajiambia kwamba Baba na Mama hawana msimamo, na kwamba wao hufanya maamuzi kwa kutegemea hisia zao. Lakini wazazi wakiwa na msimamo, watoto watajua jambo baya haliwezi kugeuka kuwa zuri. Hiyo ni njia moja ambayo wazazi wanaweza kuwalinda na kuwaonyesha watoto wao upendo.”—Gilmar, Brazili.

      “Watoto wanaweza kutumia vibaya nafasi ambazo mzazi hawezi kuepuka kufanya jambo aliloombwa na mtoto wake—kama vile kunapokuwa na watu wengine. Kama jibu langu ni hapana, mimi husema hivyo tangu mwanzo, nami humwambia mwana wangu wazi kwamba sitamsikiliza hata akiendelea kunibembeleza.”—Chang-seok, Korea.

      “Lazima wazazi wakubaliane. Ikiwa mimi na mke wangu hatukubaliani kuhusu jambo fulani, tunalizungumzia faraghani. Watoto wanaweza kujua ikiwa maoni ya wazazi yanatofautiana, na watatumia vibaya nafasi hiyo.”—Jesús, Hispania.

      “Mtoto akijua kwamba wazazi wana umoja na hawawezi kubadili msimamo hata wanapobembelezwa, anajihisi akiwa salama. Anajua anachotarajia kutoka kwa wazazi, iwapo atatii au la.”—Damaris, Ujerumani.

      “Mimi na mke wangu huamini kwamba tunapomwahidi binti yetu kwamba tutampa kitu fulani kizuri hatupaswi kubadili ahadi yetu. Hivyo anajifunza kutumainia ahadi zetu.” —Hendrick, Ujerumani.

      “Iwapo kila wakati mwajiri wangu angebadili mambo anayotazamia nifanye kazini, ningeudhika. Ndivyo ilivyo pia kwa watoto. Wanajihisi salama wanapojua sheria na wanapojua kwamba sheria hizo hazitabadilika. Wanapaswa pia kuelewa vizuri adhabu ya kuvunja sheria hizo, na kwamba adhabu yenyewe haibadiliki.”—Glenn, Kanada.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      “Acheni Ndiyo yenu imaanishe Ndiyo, na Siyo yenu, Siyo.”—Yakobo 5:12

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      MASIMULIZI YA FAMILIA

      Mimba Ambayo Haikutarajiwa​—Jinsi Tulivyobadili Maisha Yetu

      Limesimuliwa na Tom na Yoonhee Han

      Tom: Tulikuwa tumeoana kwa miezi sita tu wakati ambapo mke wangu, Yoonhee, aligundua kwamba yeye ni mja-mzito. Kwa nje, nilijifanya kuwa mtulivu ili nimhakikishie Yoonhee kwamba anaweza kunitegemea ili apate faraja na utegemezo. Lakini kwa kweli nilikuwa na hofu moyoni!

      Yoonhee: Nililemewa na hisia—na nilijawa na woga! Nililia tena na tena; sikujihisi nikiwa tayari kuwa mama.

      Tom: Hata mimi sikujihisi nikiwa tayari kuwa baba! Lakini baada ya kuongea na wazazi wengine, tulitambua kwamba watu wengi hupata mimba bila kutarajia. Tulifaidika pia kusikia kuhusu shangwe ambazo wazazi wengine hupata. Pole kwa pole, wasiwasi wangu ulibadilika na nikaanza kutazamia kuwa na mtoto.

      Yoonhee: Amanda alipozaliwa, tulianza kukabili changamoto za aina nyingine. Alilia bila kukoma, nami sikuweza kulala kwa majuma kadhaa. Nilikosa hamu ya kula, na nilijihisi mchovu kupita kiasi. Mwanzoni, nilijaribu kujitenga na watu. Lakini nikatambua kwamba kujitenga kwa kukaa nyumbani hakutanisaidia. Kwa hiyo, nikaanza kuchangamana na akina mama wengine. Kufanya hivyo kulinisaidia kubadilishana mawazo nao, na nikatambua kwamba si mimi peke yangu niliyekuwa na matatizo hayo.

      Tom: Nilijitahidi kudumisha ratiba nzuri katika familia. Kwa mfano, tukiwa Mashahidi wa Yehova, mimi na Yoohnee tuliazimia kuwa wa kawaida katika kazi ya kuhubiri na mikutanoni. Pia, mtu hupata gharama nyingine kwa sababu ya kuwa na mtoto mchanga, na nyingine huja bila kutarajiwa. Tulijitahidi kuishi kulingana na mapato yetu ili tusijiingize katika madeni, ambayo yangetuletea mfadhaiko zaidi.

      Yoonhee: Mwanzoni, nilifikiri kwamba hatuwezi kwenda kuhubiri, kwa kuwa watoto wanaweza kuwa wasumbufu sana. Lakini ukweli ni kwamba watu wengi hupenda sana watoto wachanga. Kutambua jambo hilo kulinisaidia kuendelea kuhubiri na kuwa na maoni yanayofaa kumhusu mtoto wangu.

      Tom: Biblia inasema kwamba watoto “ni urithi kutoka kwa Yehova” na “ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Maneno hayo yananionyesha kwamba mtoto ni zawadi yenye thamani sana. Kama ilivyo na urithi mwingine wowote ule, unaweza kuamua utautumia kwa njia gani: Ama uuhifadhi vizuri ama uupoteze. Ninajifunza kwamba kila hatua katika ukuzi wa mtoto ni ya pekee, na ninahitaji kujionea kila hatua katika maisha ya binti yangu kwa sababu inapopita, haiwezi kurudiwa.

      Yoonhee: Nyakati nyingine, mambo tusiyoyatarajia hutukia katika maisha yetu, na kupata mtoto bila kutazamia si jambo baya. Sasa Amanda ana umri wa miaka sita, na sioni kama ninaweza kuishi bila yeye.

      [Picha]

      Tom na Yoonhee wakiwa na binti yao, Amanda

  • Kulea Watoto Wachanga Hadi Wanapobalehe
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Kulea Watoto Wachanga Hadi Wanapobalehe

      “Kabla ya watoto wako kufikia umri wa miaka mitano, wao huwa katika mazingira mazuri ya nyumbani na ni rahisi kuwafundisha sifa nzuri. Lakini mara tu wanapoanza kwenda shuleni, wanakumbana na njia tofauti za kufanya mambo na za kuzungumza.”—Valter, Italia.

      WATOTO wanapozidi kukua, wao hujaribu kuelewa ulimwengu wao unaozidi kupanuka. Wao huchangamana na watu wengi zaidi—watoto wanaocheza nao, wanafunzi wenzao, na watu wa ukoo. Kama Valter aliyenukuliwa hapo juu anavyosema, si wewe tu uliye na uvutano juu ya mtoto wako tena, kama ulivyofanya alipokuwa mchanga. Hiyo ndiyo sababu unapaswa kutumia kipindi kati ya utoto na kubalehe kumfundisha mtoto wako umuhimu wa kutii na kuwa na adabu. Pia ni muhimu kumpa mwongozo kuhusu mambo yaliyo sawa na yaliyo makosa.

      Si rahisi kumfundisha mambo hayo wala haichukui muda mfupi. Huenda ukahitaji ‘kumkaripia, kumkemea, kumhimiza, kwa ustahimilivu wote na ufundi wa kufundisha.’ (2 Timotheo 4:2) Wazazi Waisraeli waliamriwa hivi kuhusu sheria za Mungu: ‘Uzikazie kwa mwana wako na kuzisema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kama andiko hilo linavyoonyesha, ni muhimu sana kuwafundisha kwa kuendelea.

      Kuna magumu fulani yanayohusika katika kutimiza daraka la kuwalea watoto. Acheni tufikirie baadhi yake.

      Wakati wa Kusikiliza

      Biblia inasema kwamba ingawa kuna “wakati wa kusema,” pia kuna wakati wa kusikiliza. (Mhubiri 3:7) Ni katika njia gani unaweza kumfundisha mtoto wako kusikiliza wakati wengine wanapozungumza—kutia ndani wewe unapozungumza? Njia moja ni kumwekea mfano. Je, wewe huwasikiliza wengine kwa makini, kutia ndani watoto wako?

      Watoto wanaweza kukengeushwa kwa urahisi, na bila shaka ni rahisi kukosa subira unapojaribu kuwasiliana nao. Kila mtoto ni tofauti, kwa hiyo chunguza na utambue njia bora za kuwasiliana na mtoto wako. Kwa mfano, David, baba mmoja nchini Uingereza, anasema hivi: “Mimi humwomba binti yetu arudie jambo nililomwambia kwa kutumia maneno yake mwenyewe. Hilo linamsaidia ajifunze kusikiliza kadiri anavyokua.”

      Yesu alipokuwa akiwafundisha wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:18) Ikiwa watu wazima wanapaswa kufanya hivyo, basi ni muhimu hata zaidi kwa watoto kuwasikiliza wengine kwa makini!

      “Kusameheana kwa Hiari”

      Biblia inasema: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Wakolosai 3:13) Watoto wanaweza kuzoezwa kusitawisha uwezo wa kusamehe. Jinsi gani?

      Kama vile ambavyo tumetaja kuhusu ustadi wa kusikiliza vizuri, unahitaji kuweka mfano. Acha watoto wako wakuone ukisitawisha roho ya kusamehe unaposhughulika na wengine. Marina, mama mmoja nchini Urusi, hujitahidi kufanya hivyo. Anasema: “Tunajaribu kuwawekea watoto wetu mfano mzuri wa kuwasamehe wengine, kuachilia mambo tunapokosewa, na kutoudhika,” na anaongezea hivi: “Ninapowakosea watoto wangu, mimi huwaomba msamaha. Ninataka wajifunze kufanya vivyo hivyo wanaposhughulika na wengine.”

      Uwezo wa kutatua ugomvi na kusamehe utakuwa muhimu wanapokuwa watu wazima. Wazoeze watoto wako sasa kuwafikiria wengine na kukubali makosa yao. Kwa kuwafundisha mambo hayo, utakuwa ukiwapa zawadi bora itakayowasaidia sana wanapokua.

      “Mjionyeshe Kuwa Wenye Shukrani”

      Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ watu wengi ‘wanajipenda wenyewe.’ (2 Timotheo 3:1, 2) Sasa, wakati ambapo watoto ni wachanga, ndio wakati wa kuwafundisha kuwa wenye shukrani. “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani,” akaandika mtume Paulo.—Wakolosai 3:15.

      Hata watoto wanapokuwa wachanga, wanaweza kujifunza kuwa na adabu na kuwafikiria wengine. Jinsi gani? “Njia bora unayoweza kuwafundisha watoto kuwa na mtazamo wenye shukrani ni kuonyesha mtazamo huo kila wakati unapokuwa nyumbani,” ndivyo Dakt. Kyle Pruett alivyowaeleza waandishi wa gazeti Parents. Anaongezea hivi: “Hilo linamaanisha kwamba unapaswa kusema kwa ukawaida jinsi unavyothamini sana msaada unaopata na mambo mengine wanayofanya yanayoonyesha ufikirio . . . Unahitaji kufanya hivyo mara nyingi.”

      Baba mmoja nchini Uingereza anayeitwa Richard, anajitahidi kufanya hivyo: “Mimi na mke wangu huwashukuru wale ambao wametuonyesha fadhili, kama vile walimu au babu na nyanya,” anasema. “Familia fulani inapotualika kwa ajili ya mlo, sisi huandika kadi ya kuwashukuru, na watoto wote hutia sahihi au wanachora picha fulani juu ya kadi hiyo.” Kuwatendea wengine fadhili na kuwa mwenye shukrani kutamsaidia mtoto wako kusitawisha urafiki wa kudumu na wa karibu baadaye maishani.

      “Usimnyime Nidhamu”

      Watoto wako wanapozidi kukua, ni muhimu wajifunze kwamba mambo wanayofanya yana madhara. Hata wanapokuwa wachanga, lazima watoto wajitiishe chini ya mamlaka, si nyumbani tu bali pia shuleni na katika jamii. Unaweza kuwasaidia watoto wako kujifunza kanuni inayosema kwamba utavuna unachopanda. (Wagalatia 6:7) Jinsi gani?

      Biblia inasema: “Usimnyime . . . nidhamu.” (Methali 23:13) Ikiwa umesema wazi kwamba utamwadhibu mtoto kwa sababu ya tendo fulani baya, usiogope kufanya kama ulivyosema na kumtia nidhamu. “Ni muhimu kutobadili-badili msimamo,” anasema Norma, mama mmoja nchini Argentina. “Kubadili-badili msimamo humtia moyo mtoto kufanya anavyotaka.”

      Wazazi wanaweza kuepuka ubishi mwingi baada ya mtoto kufanya jambo baya kwa kuhakikisha kwamba mtoto anaelewa mapema matokeo ya kutotii. Watoto watakubali nidhamu kwa urahisi iwapo wanajua sheria na wanajua kitakachotukia wakivunja sheria hizo na ikiwa wana sababu ya kuamini kwamba adhabu haiwezi kubadilishwa.

      Bila shaka, ili nidhamu iwe na matokeo, inapaswa kutolewa bila hasira. Biblia inasema: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Nidhamu haipaswi kutolewa kwa ukatili na haipaswi kuwa yenye kudhuru—kimwili au kihisia.

      Lakini unaweza kuzuia hasira yako jinsi gani mtoto wako anapokukasirisha kabisa? “Si rahisi kufanya hivyo nyakati zote,” anasema Peter, baba mmoja nchini New Zealand, “lakini watoto wanahitaji kujifunza kwamba nidhamu hutolewa kwa sababu ya tendo walilofanya na si kwa sababu mzazi ameshindwa kujizuia.”

      Peter na mke wake hujaribu kuwasaidia watoto wao waone faida ya muda mrefu ya nidhamu wanayopewa. “Hata watoto wanapofanya jambo lenye kuchukiza sana,” anasema, “sisi hujaribu kuwaonyesha tungependa wawe watu wa aina gani badala ya kukazia kosa walilofanya.”

      “Usawaziko Wenu na Ujulikane”

      Mungu alisema hivi kuhusu nidhamu ambayo angewapa watu wake: “Nitakutia adabu kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 46:28) Utafanikiwa zaidi ukitoa nidhamu kwa haki na inayolingana na makosa yaliyofanywa. Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane.”—Wafilipi 4:5.

      Sehemu moja ya kuwa na usawaziko ni kutoa nidhamu kwa njia ambayo haitawavunjia watoto wako heshima. Santi, baba mmoja nchini Italia, anasema: “Sijawahi kumshushia heshima mwanangu au binti yangu. Badala yake mimi hujaribu kutambua sababu iliyomfanya atende jambo fulani na kushughulikia jambo hilo. Ikiwezekana, siwatii nidhamu watoto wangu mbele ya watu wengine, au hata mbele ya wenzao. Nami sifanyi ucheshi kuhusu udhaifu wao iwe ni mbele ya watu au faraghani.”

      Richard, aliyenukuliwa awali, anatambua hekima ya kuwa na usawaziko. “Hupaswi kukusanya makosa kadhaa kisha kutoa nidhamu kwa makosa hayo yote mara moja,” anasema. “Baada ya kutoa nidhamu, ni muhimu kwamba usiendelee kuzungumza kuhusu jambo hilo na kumkumbusha mtoto kuhusu makosa yake.”

      Kulea watoto ni kazi ngumu inayohitaji mtu ajidhabihu lakini inaleta thawabu nyingi. Hivyo ndivyo Yelena, mama mmoja nchini Urusi alivyogundua. Anasema: “Nimeamua kufanya kazi kwa saa chache kila juma ili niwe na wakati mwingi wa kuwa pamoja na mwana wangu. Hilo linahitaji jitihada na nimepata hasara ya kifedha, lakini ninapomwona mwanangu akiwa na shangwe nyingi na uhusiano wetu ukiimarika, ninatambua kwamba nilijidhabihu kwa njia inayofaa.”

      [Picha katika ukurasa wa 11]

      Watoto wanaweza kujifunza kuwafikiria wengine

      [Picha katika ukurasa wa 12]

      Watie watoto wako nidhamu kwa njia ambayo haitawavunjia heshima

  • Maoni ya Wazazi
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Maoni ya Wazazi

      Unaweza kuwasaidia watoto wako jinsi gani waone thamani ya kuwa watiifu kadiri wanavyokua? Unaweza kutumia njia gani kuwafundisha stadi zenye thamani kadiri wanavyoendelea kuwa watu wazima? Ona mambo ambayo wazazi fulani kutoka sehemu zote ulimwenguni wamesema.

      KAZI ZA NYUMBANI NA KUSHIRIKIANA NA WENGINE

      “Tunapokula pamoja na kuzungumzia mambo yaliyotukia siku nzima, kila mtoto anajifunza kuwa msikivu. Wanapotuona tukisikiliza kwa makini, hilo linawasaidia kuheshimiana na kujiheshimu wenyewe.”—Richard, Uingereza.

      “Inavutia kama nini kuwatazama watoto wetu wakitendeana kwa heshima na kuona wakijaribu kusuluhisha mizozo kati yao wenyewe bila ya kutuhusisha. Pia, wao huwasiliana kwa uhuru na watu wazima.”—John, Afrika Kusini.

      “Mimi si mkamilifu, na wakati mwingine ninawaumiza hisia watoto wangu bila kukusudia. Ninapofanya hivyo, ni muhimu sana niwaombe msamaha kwa kosa nililofanya.”—Janelle, Australia.

      “Tunawazoeza watoto wetu kufanya kazi za nyumbani. Kuwafundisha kufanya mambo yanayowafaidi wengine husaidia familia iishi vizuri na kwa amani na hufanya watoto wetu wahisi wametimiza jambo fulani muhimu.”—Clive, Australia.

      “Si rahisi, lakini ni muhimu kuwafundisha kuwaelewa wengine, kuwaheshimu, na kusamehe.”—Yuko, Japani.

      USAFI NA AFYA

      “Watoto wetu walipokuwa wadogo, tuliwafundisha kuoga na tulifanya wafurahie jambo hilo kwa kutumia sabuni zilizokuwa na maumbo mbalimbali, sabuni ya maji iliyo kwenye chupa yenye picha za katuni fulani, na sifongo zenye maumbo ya wanyama wadogo.”—Edgar, Mexico.

      “Tulipokuwa tukiishi mahali ambapo hakukuwa na maji ya bomba, nilihakikisha kwamba kuna sabuni na mtungi wa maji mahali ambapo kila mmoja wetu angeweza kuosha mikono kabla ya kuingia nyumbani.”—Endurance, Nigeria.

      “Tunawapa watoto vyakula vyenye lishe nzuri kila siku, na kuwaeleza kwa nini mlo kama huo ni muhimu. Watoto hutaka sana kujua vyakula mbalimbali vinatayarishwa kwa njia gani, kwa hiyo mimi huwaomba wanisaidie kutayarisha mlo. Wakati tunaotumia pamoja kupika husaidia tupate nafasi zaidi za kuwasiliana.”—Sandra, Uingereza.

      “Mazoezi ni muhimu sana, na tukiwa wazazi, tunajitahidi kuweka mfano mzuri. Watoto wetu hufurahi tunapokimbia, tunapoogelea, tunapocheza mpira pamoja au kuendesha baiskeli pamoja tukiwa familia. Mbali na kujifunza kwamba mazoezi ni muhimu, wameona pia yanafurahisha.”—Keren, Australia.

      “Jambo ambalo watoto wanahitaji hasa ni kutumia wakati pamoja na wazazi wao. Hakuna jambo linaloweza kuchukua mahali pake—si pesa, zawadi, wala kutalii. Mimi hufanya kazi saa za asubuhi tu wakati ambapo watoto wako shuleni. Halafu alasiri mimi hutenga wakati wa kuwa pamoja nao.”—Romina, Italia.

      NIDHAMU

      “Tumegundua kwamba kuna njia nyingi zinazofaa za kutoa nidhamu; inategemea hali. Nyakati nyingine, nidhamu inaweza kutia ndani kuzungumzia mambo kwa uzito na mtoto, na wakati mwingine huenda ukahitaji kumzuia asifanye mambo fulani anayopenda.”—Ogbiti, Nigeria.

      “Sisi huwaomba watoto wetu warudie maagizo tuliyowapa ili kuhakikisha wameyaelewa vizuri. Halafu tunahakikisha kwamba tumefanya kama tulivyosema. Ikiwa tunataka watoto wetu watii maagizo tunayowapa, ni lazima tuhakikishe kwamba tunatoa nidhamu tuliyosema tutawapa wanapokosa kutii.”—Clive, Australia.

      “Mimi huinama ninapowarekebisha watoto wangu ili niwe sawa na kimo chao, na mbinu hiyo ina mafanikio. Kufanya hivyo kunawafanya wanisikilize kwa makini kabisa. Pia kunawasaidia waone ishara zangu za uso zinazokazia maneno ninayowaambia.”—Jennifer, Australia.

      “Sisi huepuka kuwaambia watoto wetu, ‘Hakuna wakati wewe unatusikiliza,’ hata kama huo ndio ukweli wa mambo. Pia, hatukemei mtoto mbele ya wenzake. Tunawanong’onezea au tunawapeleka kando na kuongea nao wakiwa peke yao.”—Rudi, Msumbiji.

      “Ni rahisi kuwaongoza watoto, na wanapenda kuwaiga wengine. Kwa sababu hiyo, ni lazima tuwalinde wasiathiriwe na watoto wenzao shuleni, vyombo vya habari, na watu wengine katika jamii na tuwasaidie wakuze tabia nzuri zinazotegemea kanuni zinazofaa. Kanuni bora za mwenendo huwasaidia wakatae kitu chochote chenye madhara.”—Grégoire, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

      “Ni lazima nidhamu itolewe kwa uthabiti, kwa haki, na bila kubadilika-badilika. Ni lazima watoto waelewe matokeo mabaya ya kuvunja sheria na wajue kwamba unamaanisha kile unachosema.”—Owen, Uingereza.

      [Blabu katika ukurasa wa 14]

      “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

      MASIMULIZI YA FAMILIA

      Kufanikiwa Ukiwa Mzazi Asiye na Mwenzi

      Mahojiano na Lucinda Forster

      Ni hali gani ngumu zaidi unayokabili ukiwa mzazi asiye na mwenzi?

      Kuwa mzazi si jambo rahisi, lakini nikiwa mzazi asiye na mwenzi ni vigumu sana kwangu kupangia jinsi nitakavyotumia wakati na nguvu zangu. Inachukua muda kuwafundisha kanuni na sheria na bado nipate nafasi ya kupumzika na kucheka nao. Mara nyingi ninalazimika kudhabihu wakati wangu wa kupumzika ili nifanye kazi za nyumbani.

      Wewe hudumisha mawasiliano mazuri na binti zako jinsi gani?

      Wazazi wanapotalikiana, watoto wanaweza kuanza kuhisi kwamba hawana usalama na kuwa na hasira. Matatizo yanapotokea, ninaona kwamba ni muhimu kuwatazama usoni na kuongea nao kwa utulivu. Mimi husubiri hadi kila mtu anapotulia, kisha ninajaribu kuwaeleza jambo linalonihangaisha bila kulifanya lionekane kama jambo kubwa sana. Mimi huwaomba maoni, kisha ninawasikiliza kwa makini, na kuwaonyesha kwamba ninajali sana hisia zao. Ninawaonyesha ninapendezwa na mambo yao ya shule na kuwapongeza kwa wanayotimiza. Sikuzote sisi hula pamoja mezani katika mazingira yaliyotulia tukiwa tumestarehe kabisa. Pia kila mara ninawaambia jinsi ninavyowapenda sana.

      Wewe hutoa nidhamu jinsi gani?

      Watoto wanahitaji mipaka iliyo wazi, na ni muhimu kuhakikisha kwamba haibadiliki-badiliki. Ninajaribu kuwa mwenye fadhili lakini thabiti. Ni lazima nizungumze na watoto wangu na niwaeleze kwa nini tabia fulani ni mbaya. Ninajaribu pia kuwauliza maswali ili nijue maoni yao kuhusu jambo walilofanya kabla ya kuwaadhibu. Ikiwa nimewakosea—kwa mfano, ikiwa niliwaelewa vibaya—ninawaomba msamaha.

      Unatumia njia gani kuwafundisha watoto wako kuwaheshimu watu wengine?

      Mimi huwakumbusha jambo ambalo Yesu alifundisha—watendee wengine kama vile unavyotaka utendewe. (Luka 6:31) Ninawatia moyo wasuluhishe matatizo yao wenyewe kwa wenyewe kadiri wanavyoweza, na ninawafundisha umuhimu wa kujibu kwa upole na kwa fadhili wanapokasirishwa.

      Ninyi hufanya nini wakati wa mapumziko?

      Si kila mara tunaweza kugharimia kwenda likizo mbali, kwa hiyo tunatafuta katika magazeti mambo tunayoweza kufanya ambayo hayatatugharimu sana. Tunapanga tafrija au tunatembelea maeneo yanayokuzwa mimea michanga. Tunapanda mboga kwenye bustani yetu na kufurahia kuzichuma kwa ajili ya kupika. Tafrija ni muhimu, hata kama tutatembelea tu bustani iliyo karibu na nyumbani.

      Mmepata shangwe na thawabu gani?

      Limekuwa jambo gumu kwetu kuishi katika familia yenye mzazi mmoja, lakini tuna uhusiano mzuri, na tumejifunza kuthamini baraka tulizo nazo. Ninafurahi ninapoona jinsi kila mtoto anavyokua na kusitawisha utu wa kipekee. Wanataka kuwa karibu nami, na ninathamini ushirika wao. Wanatambua haraka kama nimefurahi au nimehuzunika, na mara nyingine wananikumbatia ili kunihakikishia kwamba wananipenda. Mimi hufurahi sana wanaponionyesha upendo. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba tumejionea upendo wa Muumba anayetujali ambaye ametutegemeza katika hali nyingi ngumu. Biblia imeniimarisha niendelee kujitahidi kuwa mzazi bora.—Isaya 41:13.

      [Picha]

      Lucinda pamoja na binti zake, Brie na Shae

  • Kubalehe—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Kubalehe​—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima

      HEBU wazia kwamba umesafiri kutoka kwenye eneo lenye joto hadi kwenye eneo lenye baridi kali. Baada tu ya kushuka ndege, unatambua kwamba hilo ni eneo lenye theluji nyingi. Je, unaweza kuzoea hali hizo? Ndiyo, lakini itakubidi ufanye mabadiliko fulani.

      Unapatwa na hali kama hiyo watoto wako wanapobalehe. Huenda ikaonekana kwamba watoto wako wanabadilika mara moja. Yule mvulana ambaye aliambatana nawe kokote ulikoenda, sasa anataka kuchangamana tu na vijana wenzake. Yule msichana ambaye alitamani sana kukueleza jinsi siku yake ilivyokuwa, sasa anakujibu kwa maneno machache tu.

      “Habari ya shule?” unamwuliza.

      “Nzuri,” anajibu.

      Halafu kimya.

      “Unafikiria nini?” unamwuliza.

      “Hakuna,” anajibu.

      Halafu kimya tena.

      Kwani ni nini kimetukia? Muda mfupi uliopita, “inaonekana ni kana kwamba ulikuwa na ruhusa ya kujua mambo ya siri katika maisha ya watoto wako,” kinasema kitabu Breaking the Code. Kinaendelea kusema kwamba ni kana kwamba hakuambii mambo mengi na huenda hata akawaambia wengine mambo ambayo hawezi kukuambia. Huenda ukahisi ni kana kwamba unamtazama kijana wako akikua na huwezi kumsaidia.

      Je, hilo linamaanisha kwamba haiwezekani kuwa na uhusiano wa karibu na watoto wako wanapobalehe? La hasha! Unaweza kuwa karibu na watoto wako wanapobalehe. Hata hivyo, kwanza, unahitaji kuelewa ni nini hasa kinachoendelea katika kipindi hicho cha ukuzi chenye kusisimua na vilevile kilicho na matatizo.

      Wanaacha Kuwa Watoto na Kuwa Watu Wazima

      Wakati fulani uliopita, watafiti walifikiri kwamba ubongo wa mtoto huwa umekomaa kabisa kufikia wakati anapokuwa na umri wa miaka mitano. Sasa wanaamini kwamba ingawa ukubwa wa ubongo hubadilika kidogo sana baada ya umri huo, hilo ni tofauti kabisa kuhusu kazi unaofanya. Vijana wanapoanza kubalehe, homoni zilizo ndani ya miili yao huanza kubadili jinsi wanavyofikiri. Kwa mfano, watoto wadogo hawachanganui mambo, wanayaona jinsi yalivyo tu, lakini vijana wanaobalehe huchanganua mambo kwa undani zaidi. (1 Wakorintho 13:11) Wao huanza kuwa na msimamo wao na hawaoni haya kujieleza.

      Paolo, anayeishi nchini Italia aliona kwamba kijana wake alikuwa akipitia mabadiliko hayo. “Ninapomtazama mwanangu,” anasema, “ninahisi kana kwamba yeye ni mwanamume mdogo na si mvulana tena. Si kwa sababu ya mabadiliko ya mwili wake. Kile kinachonishangaza zaidi ni jinsi anavyofikiri. Haogopi kueleza maoni yake na kuyatetea!”

      Je, umeona mabadiliko hayo katika kijana wako anayebalehe? Huenda alipokuwa mtoto, alifuata tu maagizo aliyopewa. Alihitaji tu kuambiwa, “Kwa sababu nimesema hivyo.” Sasa, kwa kuwa anabalehe, anataka kujua sababu za kufanya mambo, na hata wakati mwingine angependa kujua kwa nini kuna sheria fulani nyumbani. Huenda nyakati nyingine ikaonekana kwamba anaasi kwa sababu ya jinsi anavyotoa maoni yake.

      Hata hivyo, usikate kauli kwamba kijana wako anataka kukiuka sheria ulizoweka. Huenda akawa anajitahidi kuishi kulingana na viwango ulivyomwekea, anajaribu tu kuona jinsi vitakavyofaa katika maisha yake. Hebu wazia unahamia nyumba nyingine pamoja na vitu vyako. Je, itakuwa rahisi kupata nafasi ya kuweka kila kitu katika nyumba yako mpya? Huenda isiwe rahisi. Hata hivyo, ukweli ni kwamba hutatupa kitu chochote unachoona kuwa ni cha thamani.

      Kijana wako yuko katika hali kama hiyo anapojitayarishia wakati ambapo “atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ni kweli, huenda wakati huo uko mbali sana; kijana wako bado si mtu mzima. Lakini sasa ni kana kwamba anapakia mizigo yake ili ahame. Akiwa tineja, anajichunguzia viwango ambavyo amelelewa navyo, na anaamua ni viwango gani atahama navyo atakapokuwa mtu mzima.a

      Huenda ukaogopa unapofikiri kwamba mtoto wako anafanya maamuzi kama hayo. Lakini unaweza kuwa na hakika kwamba atakapokuwa mtu mzima, atafuata tu viwango ambavyo yeye anaona kuwa ni vyenye thamani. Kwa hiyo, sasa—wakati ambapo kijana wako bado yuko nyumbani—ndio wakati anapaswa kuchunguza kwa undani viwango atakavyofuata maishani.—Matendo 17:11.

      Kwa kweli, kijana wako atafaidika sana kwa kufanya hivyo. Ikiwa sasa atakubali viwango vyako bila kujichunguzia, huenda baadaye akakubali viwango vya wengine bila kufikiri. (Kutoka 23:2) Biblia inaeleza kwamba kijana kama huyo hushawishika kwa urahisi kwa sababu “amepungukiwa moyoni”—maneno yanayomaanisha kwamba anakosa utambuzi, pamoja na sifa nyingine muhimu. (Methali 7:7) Kijana ambaye hana uhakika wa mambo anayoamini anaweza ‘kurushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kupitia udanganyifu wa watu.’—Waefeso 4:14.

      Unaweza kufanya nini ili kijana wako asipatwe na hali kama hiyo? Hakikisha kwamba ana mambo haya matatu muhimu:

      1 NGUVU ZA UFAHAMU

      Mtume Paulo aliandika kwamba ‘nguvu za ufahamu za watu wakomavu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Huenda ukasema, ‘Lakini nilimfundisha mtoto wangu yaliyo sawa na yaliyo makosa miaka mingi iliyopita.’ Ni kweli, na bila shaka elimu hiyo ilimfaidi wakati huo na kumtayarisha kwa ajili ya kipindi kilichofuata cha ukuzi maishani mwake. (2 Timotheo 3:14) Hata hivyo, Paulo alisema kwamba nguvu za ufahamu zinahitaji kuzoezwa. Ingawa watoto wadogo wanaweza kupata ujuzi kuhusu yaliyo sawa na yaliyo makosa, matineja wanahitaji kuwa “watu wazima katika nguvu za uelewaji.” (1 Wakorintho 14:20; Methali 1:4; 2:11) Hungependa kijana wako atii tu bila kufikiri, bali atumie uwezo wake wa kufikiri. (Waroma 12:1, 2) Unaweza kumsaidia afanye hivyo jinsi gani?

      Njia moja ya kufanya hivyo ni kumruhusu ajieleze. Usimkatize anapozungumza, na usimwonyeshe kwamba umekasirika kupita kiasi, hivi kwamba aache kuzungumza—hata anaposema jambo la kushtua. Biblia inasema hivi: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19; Methali 18:13) Zaidi ya hilo, Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Ikiwa utamsikiliza, utaweza kujua mambo ambayo kwa kweli yanamhangaisha kijana wako.

      Unapoongea, jaribu kumwuliza maswali badala ya kumwambia mambo moja kwa moja. Nyakati nyingine Yesu aliuliza, “Mnaonaje?” ili kuwasaidia watu wajieleze waziwazi na kwa unyoofu, si wanafunzi wake tu, bali hata wale waliokuwa wakaidi. (Mathayo 21:23, 28) Unaweza kufanya hivyo unaposhughulika na kijana wako anayebalehe, hata anapotoa maoni yanayotofautiana na yako. Kwa mfano:

      Kijana wako anaposema: “Sidhani ninaamini kwamba kuna Mungu.”

      Badala ya kumjibu: “Si tulikufundisha kwamba kuna Mungu—lazima uamini kwamba Mungu yuko!”

      Unaweza kusema: “Kwa nini unasema hivyo?”

      Kwa nini unapaswa kumtia moyo kijana wako ajieleze? Kwa sababu hata ingawa unasikia anachosema, unahitaji kujua yale anayofikiri. (Methali 20:5) Huenda akawa na tatizo na viwango vya Mungu si eti haamini kuna Mungu.

      Kwa mfano, huenda kijana ambaye anashawishiwa kuvunja sheria za Mungu za maadili akaamua kutoamini kwamba kuna Mungu ili iwe rahisi kuzivunja. (Zaburi 14:1) Huenda akajiambia, ‘Ikiwa hakuna Mungu, basi si lazima niishi kulingana na viwango vya Biblia.’

      Ikiwa kijana wako ana maoni kama hayo, msaidie afikirie swali hili, Je, kweli ninaamini kwamba viwango vya Mungu vina faida kwangu? (Isaya 48:17, 18) Ikiwa anaamini kwamba vinaweza kumfaidi, basi mtie moyo atambue kwamba anapaswa kufanya kila awezalo kudumisha hali yake nzuri.—Wagalatia 5:1.

      Kijana wako anaposema: “Hii ni dini yako, si lazima iwe dini yangu.”

      Badala ya kumjibu: “Hii ni dini yetu, wewe ni mtoto wetu, na ni lazima uamini yale tunayokufundisha.”

      Unaweza kusema: “Hayo kwa kweli ni maneno makali. Ikiwa hukubaliani na imani yangu, lazima uwe na imani nyingine tofauti. Kwa hiyo, unaamini nini? Unafikiri ni viwango gani bora vya kufuata maishani?”

      Kwa nini unapaswa kumtia moyo kijana wako ajieleze? Kwa sababu unapotumia maswali kwa njia hiyo ili kuufikia moyo wake, utamsaidia achunguze maoni yake mwenyewe. Huenda akashangaa anapotambua kwamba imani yake ni sawa na yenu ila tu anahangaishwa na jambo lingine tofauti kabisa.

      Kwa mfano, huenda kijana wako hajui jinsi ya kuwaeleza wengine mambo anayoamini. (Wakolosai 4:6; 1 Petro 3:15) Au huenda amevutiwa kimapenzi na mtu wa jinsia tofauti ambaye hana imani kama yake. Tafuta kiini cha tatizo, na umsaidie kijana wako kufanya hivyo pia. Kadiri anavyotumia nguvu zake za ufahamu, ndivyo atakavyojitayarisha vizuri zaidi kuwa mtu mzima.

      2 MWONGOZO WA MTU MZIMA

      Katika tamaduni fulani leo, hakuna “mahangaiko na mkazo” mwingi ambao wanasaikolojia fulani wanadai ungetarajiwa wakati wa ujana. Watafiti wamegundua kwamba katika maeneo kama hayo watoto wanakomaa wakiwa na umri mdogo. Wao hushirikiana na kufanya kazi na watu wazima, na hata kupewa majukumu ya watu wazima. Maneno kama vile “utamaduni wa vijana,” “vijana wasio na adabu,” na hata “kubalehe” hayatumiki katika maeneo hayo.

      Tofauti na hilo, hebu wazia kuhusu vijana katika maeneo fulani ambao husoma katika shule zilizosongamana ambako wanashirikiana tu na vijana wenzao. Wanaporudi nyumbani, hawapati mtu. Baba na Mama wako kazini. Watu wa ukoo wanaishi mbali. Watu wanaoshirikiana nao kwa ukaribu mara nyingi ni vijana wenzao tu.b Je, unaona hatari iliyopo? Tatizo si kuwa tu ataanza kushirikiana na vijana watundu. Watafiti wanasema kwamba hata vijana wenye mwenendo mzuri hushawishiwa na kuingia kwenye mwenendo mbaya wasiposhirikiana na watu wazima.

      Jamii moja ambayo haikuwatenga vijana kutoka kwa watu wazima ni ile ya Israeli la kale.c Kwa mfano, Biblia inaeleza kumhusu Uzia, aliyewekwa kuwa mfalme wa Yuda alipokuwa bado tineja. Ni nini kilichomsaidia Uzia kuutimiza mgawo huo mzito? Ni wazi kwamba ilikuwa kwa sababu ya uvutano wa mtu mzima aliyeitwa Zekaria, ambaye Biblia inasema ‘alikuwa akiwafundisha watu kumwogopa Mungu wa kweli.’—2 Mambo ya Nyakati 26:5.

      Je, kijana wako ana mshauri mmoja au kadhaa walio na umri mkubwa na walio na viwango kama vyako? Usione wivu ikiwa kijana wako ana marafiki kama hao. Wanaweza kumsaidia kijana wako afanye lililo sawa. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—Methali 13:20.

      3 KUTEGEMEKA

      Katika nchi fulani, sheria zinawazuia vijana wasifanye kazi ya kuajiriwa kwa zaidi ya saa fulani kila juma au wasifanye kazi za aina fulani. Vizuizi hivyo viliwekwa ili kuwalinda watoto kutokana na kazi hatari—viliwekwa wakati wa ule mvuvumko wa kiviwanda wa karne ya 18 na 19.

      Ingawa sheria hizo zinawalinda vijana kutokana na hatari na kutumiwa vibaya, wataalamu fulani wanasema kwamba zinawazuia wasiwajibike. Kwa sababu hiyo, kinasema kitabu Escaping the Endless Adolescence, vijana wengi wamesitawisha “mtazamo wa kudai vitu kwa nguvu, eti wanastahili kila kitu wanachopata bila hata kufanya kazi yoyote.” Waandishi wa kitabu hicho wanasema kwamba inaonekana mtazamo huo “unatokana na ulimwengu unaopendelea hasa kuwatumbuiza vijana badala ya kutazamia wafanye jambo lolote.”

      Tofauti na hilo, Biblia inaeleza kuhusu vijana ambao walichukua madaraka mazito walipokuwa wangali wachanga. Fikiria kisa cha Timotheo, ambaye huenda alikuwa tineja tu alipokutana na mtume Paulo—mtu mzima ambaye alikuwa na uvutano mkubwa juu yake. Wakati mmoja, Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Uichochee kama moto zawadi ya Mungu iliyo ndani yako.” (2 Timotheo 1:6) Huenda muda fulani kabla au baada ya kutimia miaka 20, Timotheo aliondoka nyumbani na kusafiri pamoja na mtume Paulo, akisaidia kuanzisha makutaniko na kuimarisha akina ndugu. Baada ya kufanya kazi pamoja na Timotheo kwa miaka kumi hivi, Paulo aliwaambia hivi Wakristo huko Filipi: “Sina mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu.”—Wafilipi 2:20.

      Mara nyingi, vijana wana hamu ya kuchukua madaraka, hasa wanapotambua kwamba watafanya kazi ya maana na inayowasaidia watu. Kufanya hivyo hakuwasaidii tu wawe watu wazima wenye kutegemeka katika maisha ya baadaye bali pia kunawasaidia kusitawisha sifa nzuri hata sasa.

      Kuzoea Hali Mpya

      Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa habari hii, ikiwa wewe ni mzazi wa kijana anayebalehe, huenda ukahisi kwamba unakabili hali tofauti na ile uliyokabili miaka michache tu iliyopita. Uwe na hakika kwamba unaweza kubadilikana na hali hiyo, kama vile tu ulivyofanya katika hatua nyingine zote za ukuzi wake.

      Ona miaka ya utineja ya mtoto wako kuwa nafasi ya (1) kumsaidia kukuza nguvu zake za ufahamu, (2) kumsaidia apate mwongozo wa mtu mzima, na (3) kumsaidia awe mwenye kutegemeka. Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukimtayarisha kijana wako anayebalehe kwa ajili ya maisha ya utu uzima.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kitabu kimoja kinasema kwamba umri wa kubalehe ni “kipindi cha kujitayarisha kuwaaga wazazi.” Kwa habari zaidi, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2009 (1/5/2009), ukurasa wa 10-12, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Burudani ambazo zimekusudiwa hasa kwa ajili ya vijana huendeleza wazo la kwamba wanapaswa kushirikiana na vijana wenzao tu, kwa kuwa wana utamaduni ambao watu wazima hawawezi kuuelewa.

      c Maneno “kubalehe” na “tineja” hayapatikani katika Biblia. Ni wazi kwamba vijana waliokuwa miongoni mwa watu wa Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo na katika enzi za Ukristo walikomaa wakiwa na umri mdogo kuliko ilivyo katika jamii nyingi leo.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

      “SIWEZI KUWAZIA KUWA NA WAZAZI BORA KULIKO HAWA”

      Kwa maneno na matendo, wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova huwafundisha watoto wao kuishi kupatana na kanuni za Biblia. (Waefeso 6:4) Hata hivyo, hawawalazimishi kufanya hivyo. Wazazi ambao ni Mashahidi wanatambua kwamba kila mtoto, anapofikia umri wa kujiamulia, lazima aamue viwango atakavyofuata maishani.

      Aislyn, mwenye umri wa miaka 18, ameamua kufuata viwango alivyofundishwa tangu utotoni. Anasema hivi: “Kwa maoni yangu, dini yangu si kitu cha kufuatwa siku moja tu kwa juma. Ni njia yangu ya maisha. Inahusisha kila kitu ninachofanya na kila uamuzi ninaofanya—iwe ni marafiki wangu, masomo nitakayochagua, na vitabu nitakavyosoma.”

      Aislyn anathamini sana jinsi ambavyo wazazi wake Wakristo wamemlea. Anasema hivi: “Siwezi kuwazia kuwa na wazazi bora kuliko hawa, na ninafurahi kwamba wamenifundisha kuwa na tamaa ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kudumu nikiwa hivyo. Wazazi wangu wataendelea kuwa na uvutano mkubwa katika maisha yangu yote.”

      [Picha katika ukurasa wa 17]

      Mruhusu kijana wako azungumze

      [Picha katika ukurasa wa 18]

      Mshauri aliye na umri mkubwa anaweza kuwa na uvutano mzuri kwa mtoto wako

      [Picha katika ukurasa wa 19]

      Kazi yenye kuridhisha inawasaidia vijana kuwa watu wazima wenye kutegemeka

  • Maoni ya Wazazi
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Maoni ya Wazazi

      Miaka ya kubalehe huwaletea wazazi wengi magumu mpya. Ni kwa njia gani unaweza kumsaidia mtoto wako afaulu kupitia kipindi hiki kigumu maishani—ambacho huenda kinaweza kuwa chenye kutatanisha kwake kama kilivyo kwako? Ona mambo ambayo wazazi fulani kutoka sehemu zote ulimwenguni wamesema.

      MABADILIKO

      “Mwanangu alipokuwa mchanga, alikuwa akikubali mashauri yangu bila ubishi. Lakini alipofikia umri wa utineja, alianza kutilia shaka mamlaka yangu. Alishuku mambo niliyoyasema na jinsi nilivyoyasema.”—Frank, Kanada.

      “Mvulana wangu haongei sana kama zamani. Ni lazima nimuulize anafikiria nini badala ya kungoja anieleze. Si rahisi kumfanya akupe jibu. Atajibu—lakini si upesi.”—Francis, Australia.

      “Subira ni muhimu sana. Nyakati nyingine, tunaweza kushawishiwa kuwafokea watoto wetu, lakini inafaa zaidi tunapojituliza kwanza kisha tunazungumza nao!” —Felicia, Marekani.

      MAWASILIANO

      “Nyakati nyingine, binti yangu huwa na mwelekeo wa kujitetea, na wakati mwingine anafikiria ninamwonea. Ni lazima nimkumbushe kwamba ninampenda, na kwamba ninajaribu kumsaidia na ningependa afanikiwe!”—Lisa, Marekani.

      “Watoto wangu walipokuwa wachanga, walikuwa tayari kujieleza. Ilikuwa rahisi kujua mambo wanayofikiria. Lakini sasa lazima niwaelewe na niwaonyeshe kuwa ninawaheshimu. Hiyo ndiyo njia pekee inayoweza kufanya wanieleze yaliyo moyoni.”—Nan-hi, Korea.

      “Haitoshi tu kuwazuia vijana wasifanye mambo fulani. Ni lazima tuwaeleze sababu zetu na tuwe na mazungumzo yatakayogusa mioyo yao. Tukitaka kuwachochea wajieleze, ni lazima tuwe tayari kusikiliza chochote watakachosema, hata kama ni mambo ambayo hatutaki kuyasikia.”—Dalila, Brazili.

      “Ikiwa ni lazima nimtie nidhamu binti yangu, mimi hujaribu kufanya hivyo faraghani, badala ya mbele ya watu wengine.”—Edna, Nigeria.

      “Nyakati nyingine ninapozungumza na kijana wangu, ninaanza kukengeushwa na shughuli nyingine za nyumbani na sikazii fikira anachosema. Anatambua hilo mara moja na nafikiri hiyo ni sababu moja inayomfanya asizungumze na mimi mara nyingi. Ninahitaji kumsikiliza kwa makini zaidi tunapoongea ili aendelee kujieleza.”—Miriam, Mexico.

      KUJITEGEMEA

      “Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kuwapa vijana wangu uhuru zaidi, na hilo limesababisha matatizo kati yetu. Tulizungumzia jambo hilo waziwazi pamoja. Niliwaeleza kwa nini nilikuwa na hofu, nao wakanieleza kwa nini walitaka kuwa na uhuru zaidi. Tulikubaliana kwamba wangeweza kuwa na uhuru zaidi lakini wasivuke mipaka niliyowawekea.” —Edwin, Ghana.

      “Mwana wangu alitaka pikipiki. Sikukubaliana kabisa na wazo hilo na bila hata kumpa nafasi ya kutoa maoni yake, nilimkemea na kumtajia madhara yote ya kununua pikipiki. Jambo hilo lilimkasirisha na akaazimia hata zaidi kununua pikipiki! Niliamua kutumia mbinu nyingine. Nilimtia moyo kijana wangu afanye utafiti kuhusu jambo hilo, achunguze hatari, gharama, na matakwa ya kupata na kuandikisha upya leseni ya pikipiki. Nilimwambia pia atafute ushauri kutoka kwa Wakristo wakomavu kutanikoni. Nilikuja kugundua kwamba badala ya kumnyima uhuru, ni afadhali kama ningemtia moyo awe huru kueleza yaliyo moyoni mwake. Kwa njia hiyo, ningeufikia moyo wake.”—Hye-young, Korea.

      “Tuliweka mipaka, lakini hatua kwa hatua tuliwapa uhuru. Kadiri walivyotumia uhuru huo vizuri, ndivyo walivyopata uhuru zaidi. Tuliwapa nafasi ya kupata uhuru zaidi, na tukawaonyesha kwamba tulitaka waweze kuupata; lakini hatukukosa kutoa nidhamu walipotumia uhuru huo vibaya.”—Dorothée, Ufaransa.

      “Sikulegeza viwango vyangu. Lakini watoto wangu walipokuwa watiifu, nilikuwa tayari kuwaruhusu wafanye mambo fulani. Kwa mfano, mara kwa mara ningewaruhusu warudi nyumbani saa zikiwa zimesonga kuliko kawaida. Lakini kama wangerudi nyumbani wakiwa wamechelewa zaidi ya mara moja, wangelipia kosa hilo.” —Il-hyun, Korea.

      “Kadiri mfanyakazi anavyokuwa mtiifu na kuwajibika, ndivyo mwajiri wake anavyompa madaraka zaidi. Vivyo hivyo, mwanangu anaweza kuona kwamba kadiri anavyotii na kuhakikisha kwamba hapiti mipaka tuliyomwekea, ndivyo anavyopata uhuru zaidi. Mwanangu anajua kwamba kama vile mfanyakazi anavyoadhibiwa asipotimiza majukumu yake, anaweza pia kupoteza uhuru wake iwapo hatakuwa mwenye kuwajibika.”—Ramón, Mexico.

      [Blabu katika ukurasa wa 22]

      “Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.”—Methali 22:6, Biblia Habari Njema

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

      MASIMULIZI YA FAMILIA

      “Kuwalea Vijana Wanaobalehe Ni Jambo Zuri Ajabu”

      Joseph: Binti zangu wawili wakubwa wana umri wa miaka 17 na 13, na ninaona ni muhimu kuwasikiliza na kukubali maoni yao. Kukubali udhaifu wangu—na kuwaheshimu binti zangu ninapoongea nao—husaidia tuweze kuwasiliana vizuri zaidi. Kwa ufupi, ninahisi kwamba kuwalea vijana wanaobalehe ni jambo zuri ajabu, hasa kwa sababu ya mwongozo tunaopata katika Neno la Mungu, Biblia.

      Lisa: Niligundua kwamba binti yetu mkubwa alipoanza kubalehe, alihitaji nitumie wakati mwingi zaidi naye. Ninakumbuka nikitumia wakati wangu mwingi sana kumsikiliza, kuzungumza naye, na kumtia moyo. Mimi na mume wangu tunahakikisha binti zetu wanajua kwamba wanaweza kutuambia jambo lolote na tutaheshimu maoni yao. Ninajaribu kufuata shauri lenye hekima la Yakobo 1:19, linalotuambia tuwe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’

      Victoria: Mama yangu ndiye rafiki yangu mkubwa zaidi. Sijawahi kukutana na mtu yeyote aliye mzuri na anayejali kuliko yeye—naye humtendea kila mtu hivyo. Ninahisi kwamba mama yangu anawajali watu wengine kikweli. Siwezi kupata mama mwingine kama huyu.

      Olivia: Baba yangu anawajali watu wengine na ni mkarimu. Yeye huwa tayari sikuzote kuwasaidia wengine kimwili hata wakati ambapo familia yetu ina uhitaji. Anajua jinsi ya kuchukua mambo kwa uzito, lakini pia anajua kufurahia maisha kwelikweli. Yeye ni baba wa pekee, na ninafurahi sana kwamba yeye ni baba yangu!

      “Hatuna Wakati wa Kuchoshwa na Maisha!”

      Sonny: Binti zetu wanapokuwa na tatizo, tunaketi tukiwa familia na kulizungumzia. Kila mmoja wetu hujieleza waziwazi, na maamuzi tunayofanya yanategemea kanuni za Biblia. Mimi na Ynez tunajaribu kuhakikisha kwamba binti zetu wana marafiki wazuri waliokomaa kiroho. Rafiki zetu ni rafiki zao, na rafiki zao ni wetu pia.

      Ynez: Sisi huwa na mengi ya kufanya, na tunafanya mambo yote tukiwa familia. Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tunashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri, funzo la kibinafsi na la familia, na kujitolea kufanya kazi nyingine—kutia ndani kutoa msaada wakati wa misiba na ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Tunasawazisha mambo yote hayo na tafrija. Hatuna wakati wa kuchoshwa na maisha!

      Kellsie: Baba yangu ni msikilizaji mzuri, na sikuzote yeye hutafuta maoni ya familia yote kabla ya kufanya uamuzi mzito. Mama yangu yuko tayari kunisikiliza ninapohitaji msaada—au mtu wa kuzungumza naye.

      Samantha: Mama yangu hunifanya nijihisi kuwa mtu wa pekee sana, anayependwa, na wa maana sana—hata kama yeye hatambui jambo hilo. Yeye hunisikiliza na ananijali. Nisingependa kubadilisha urafiki wetu na kitu kingine chochote.

      [Picha]

      Familia ya Camera: Joseph, Lisa, Victoria, Olivia, na Isabella

      Familia ya Zapata: Kellsie, Ynez, Sonny, na Samantha

      [Picha katika ukurasa wa 22]

      Wazazi wanaweza kutoa uhuru kwa kiasi fulani, ingawa pia wanaweka mipaka yenye usawaziko

  • Lengo la Mzazi Ni Nini?
    Amkeni!—2011 | Oktoba
    • Lengo la Mzazi Ni Nini?

      UNGEPENDA kijana wako awe mtu wa aina gani?

      A. Awe kama wewe.

      B. Awe mwasi ambaye lengo lake ni kutenda kinyume cha jinsi unavyotenda.

      C. Awe mtu mzima anayefanya maamuzi ya hekima.

      Ingawa wazazi fulani wangependa kijana wao awe mtu anayetajwa mwisho (C) huenda wakajaribu kumfanya awe mtu anayetajwa mwanzoni (A). Wao hujaribu kumlazimisha kijana wao afuate viwango vyao, kama vile kwa kumchagulia kazi atakayofanya. Matokeo yanakuwa nini? Mara tu anapoanza kujitegemea, kijana hutenda kinyume kabisa na jinsi wazazi walivyotaka. Vijana wengi ambao wazazi wao wangependa kuwaona wakiwa kama mtu anayetajwa kwenye alama A, huwa kama mtu anayetajwa kwenye alama ya B.

      Huwezi Kuwadhibiti Vijana Kabisa

      Unataka kijana wako awe mtu mzima anayefanya maamuzi ya hekima. Lakini unaweza kufikia lengo hilo jinsi gani? Jambo moja ni hakika: Kujaribu kumdhibiti kabisa si suluhisho. Fikiria sababu mbili zifuatazo.

      1. Kujaribu kumdhibiti kabisa hakupatani na maandiko. Yehova Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uhuru wa kuchagua. Anawaruhusu watu wachague njia watakayofuata maishani, iwe nzuri au mbaya. Kwa mfano, Kaini alipokuwa na hasira na kutaka kumuua ndugu yake Abeli, Yehova alimwambia hivi: “Ukigeuka utende mema, je, hutainuliwa? Lakini usipogeuka utende mema, kuna dhambi inayovizia katika mwingilio, nayo inakutamani wewe. Je, wewe utaishinda?”—Mwanzo 4:7.

      Ona kwamba ingawa Yehova alimpa Kaini shauri la wazi, hakumlazimisha alifuate. Kaini alipaswa kuchagua ikiwa angeshinda hasira yake au la. Tunajifunza nini? Ikiwa Yehova hajaribu kudhibiti kabisa viumbe wake ili wamtii, basi wewe hupaswi kujaribu kuwadhibiti kabisa vijana wako.a

      2. Unapojaribu kumdhibiti kabisa atatenda kinyume na unachotaka. Hebu wazia kwamba mwuzaji fulani anajaribu kukulazimisha ununue bidhaa fulani. Kadiri anavyosisitiza, ndivyo unavyokataa katakata. Hata ikiwa unahitaji bidhaa hiyo, huenda usipende jinsi anavyojaribu kukushinikiza uinunue. Unataka kumwepuka kabisa mwuzaji huyo.

      Hali inaweza kuwa hivyo ukijaribu kumlazimisha kijana wako afuate viwango, imani, na miradi yako. Je, atakubali? La! Kwa kweli, huenda kufanya hivyo kukamfanya kijana wako achukie viwango vyako. Mara nyingi, wazazi wanapojaribu kuwadhibiti kabisa watoto wao, watoto huasi. Basi unaweza kufanya nini?

      Badala ya kujaribu kudhibiti kabisa maisha ya kijana wako, kwa kumlazimisha afuate viwango vyako kama ulivyofanya alipokuwa mchanga, msaidie aone hekima ya kufanya lililo sawa. Kwa mfano, ikiwa wewe ni Mkristo, mwonyeshe kwamba kufuata kanuni za Mungu kutamletea uradhi katika maisha yake yote.—Isaya 48:17, 18.

      Unapofanya hivyo, mwekee mfano mzuri. Sitawisha sifa ambazo unataka kijana wako awe nazo. (1 Wakorintho 11:1) Onyesha wazi viwango ambavyo umechagua kufuata. (Methali 4:11) Kijana wako anapompenda Mungu na viwango vyake, basi atafanya maamuzi ya hekima, hata wakati haupo.—Zaburi 119:97; Wafilipi 2:12.

      Mfundishe Stadi Zitakazomfaidi

      Kama ilivyotajwa kwenye ukurasa wa 2 wa gazeti hili, siku moja—ambayo huenda kwa maoni yako ikaja haraka sana—mtoto wako ambaye amekuwa mtu mzima “atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ukiwa mzazi, unataka kuhakikisha kwamba amepata stadi zitakazomsaidia kujitegemea akiwa mtu mzima. Fikiria kuhusu stadi unazoweza kumfundisha sasa akiwa bado nyumbani.

      Kazi za Nyumbani. Je, kijana wako anaweza kupika chakula? kuosha na kupiga pasi nguo zake? kusafisha chumba chake na kuhakikisha kwamba ni nadhifu? kufanya marekebisho madogo ya gari? Kuwa na ustadi wa kufanya mambo kama hayo kutamsaidia mwana au binti yako kusimamia nyumba yake siku moja. Mtume Paulo alisema hivi: “Nimejifunza kuwa mwenye kujitosheleza katika hali zozote nilizo nazo.”—Wafilipi 4:11.

      Kushirikiana na Wengine. (Yakobo 3:17) Je, kijana wako ana uhusiano mzuri na watu wengine? Je, anaweza kusuluhisha ugomvi kwa utulivu na fadhili? Je, umemzoeza kuwaheshimu wengine na kusuluhisha mizozo kwa amani? (Waefeso 4:29, 31, 32) Biblia inasema: “Waheshimuni watu wa namna zote.”—1 Petro 2:17.

      Kupangia Matumizi ya Pesa. (Luka 14:28) Je, unaweza kumsaidia kijana wako ajifunze ufundi fulani, kupanga na kufuata bajeti, na kuepuka madeni? Je, umemfundisha kuweka pesa akiba ili anunue vitu anavyohitaji na kuepuka kununua vitu ambavyo hakupangia na kuridhika na mahitaji ya lazima? (Methali 22:7) Paulo aliandika hivi: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika.”—1 Timotheo 6:8.

      Vijana ambao wamejifunza kufuata viwango vya maadili na wamejifunza stadi fulani wanazoweza kutumia wako tayari kuishi kama watu wazima. Wazazi wamefikia lengo lao!—Methali 23:24.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi, ona Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2011, (1/2/2011) ukurasa wa 18-19.

      JE, UMEJIULIZA HIVI?

      ● Lengo lako ni nini ukiwa mzazi?—Waebrania 5:14.

      ● Kijana wako atakabili uamuzi gani atakapokuwa mtu mzima? —Yoshua 24:15.

      [Picha katika ukurasa wa 25]

      Ungependa kijana wako awe mtu wa aina gani?

      Awe kama wewe . . .

      Awe mwasi . . .

      Awe mtu mzima mwenye kutegemeka

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki