-
Ukurasa wa Kichwa/Ukurasa wa WachapishajiMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Ukurasa wa Kichwa/Ukurasa wa Wachapishaji
Mashahidi wa Yehova na Elimu
Broshua hii haiuzwi. Ni sehemu ya kazi ya elimu ya Biblia ya ulimwenguni pote inayotegemezwa kwa michango ya hiari.
Ikiwa ungependa kutoa mchango, tafadhali tembelea donate.jw.org.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya Maandiko yametoka katika Biblia ya Union Version ya Kiswahili
Chapa ya Januari 2019
Swahili (ed-SW)
© 1995, 2002, 2015 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
-
-
Kusudi la Broshua HiiMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Kusudi la Broshua Hii
MWANAFALSAFA Mholanzi Spinoza aliandika hivi: “Nimejaribu kutoyacheka matendo ya binadamu, kutoyatolea machozi, wala kutoyachukia, bali kuyaelewa.” Ukiwa mwelimishaji, wewe hukabili ugumu wa kujaribu kuelewa maoni, malezi, na masadikisho ya wanafunzi unaowatunza, kutia na wanafunzi ambao ni watoto wa Mashahidi wa Yehova. Nyakati nyingine, wanafunzi hao huenda wakachukua msimamo ambao waonekana si wa kawaida juu ya masuala fulani. Lakini inapokuwa wazi kwamba matendo hayo yatokana na masadikisho ya mwanafunzi ya kidini na ya kiadili, yanastahili uangalifu wako. Broshua hii imetolewa na Watch Tower Bible and Tract Society (shirika la utangazaji la Mashahidi wa Yehova) na imekusudiwa kukusaidia uwaelewe vizuri zaidi wanafunzi Mashahidi. Twatumaini utachukua wakati kuisoma kwa uangalifu.
Kuelewa itikadi za kidini za mtu mwingine hakutaki kwamba uzikubali au uzifuate, na kumjulisha mtu si kumgeuza imani. Broshua hii haijaribu kukulazimisha wewe wala wanafunzi wako kukubali maoni fulani ya kidini. Tamaa yetu ni kukujulisha tu kanuni na itikadi ambazo baadhi ya wanafunzi wako wanafundishwa na wazazi wao ili iwe rahisi kwako kuwaelewa watoto Mashahidi na pia kushirikiana nao. Bila shaka, yale ambayo watoto wanafundishwa na yale wanayofanya hayapatani sikuzote, kwa kuwa kila mtoto anajifunza kusitawisha dhamiri yake mwenyewe.
Kama vile wazazi walio wengi, Mashahidi wa Yehova hutaka watoto wao wanufaike kikamili na elimu yao. Kwa kusudi hilo, wao huwafundisha watoto wao washirikiane na walimu wao. Kisha, wazazi Mashahidi na watoto wao huthamini wakati waelimishaji wanapowatendea kwa uelewevu na staha.
Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wanaojulikana ulimwenguni pote. Hata hivyo nyakati nyingine watu huwaelewa vibaya. Kwa hiyo, tumaini letu ni kwamba broshua hii itakusaidia uwaelewe vizuri zaidi watoto Mashahidi unaowatunza. Hasa, twatumaini utaona ni kwa nini, katika hali fulani hususa, huenda wakadai haki ya kuwa tofauti.
-
-
Jinsi Mashahidi wa Yehova Huona ElimuMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Jinsi Mashahidi wa Yehova Huona Elimu
Kama vile wazazi wote, Mashahidi wa Yehova wanahangaikia wakati ujao wa watoto wao. Kwa hiyo wao huiona elimu kuwa ya maana sana. “Elimu yapaswa kusaidia watu wawe washiriki wa jamii wenye mafaa. Yapaswa pia kuwasaidia wasitawishe ufahamu wa urithi wao wa kitamaduni na kuishi maisha yenye kuridhisha zaidi.”
KAMA vile nukuu hili kutoka katika The World Book Encyclopedia lidokezavyo, mojapo makusudi makuu ya elimu ni kuzoeza watoto kwa ajili ya maisha ya kila siku, ambalo latia ndani kuwawezesha kutunza mahitaji ya familia siku moja. Mashahidi wa Yehova huamini kwamba hili ni daraka takatifu. Biblia yenyewe husema hivi: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” (1 Timotheo 5:8) Miaka inayotumiwa shuleni hutayarisha watoto kwa ajili ya madaraka watakayopata maishani. Kwa hiyo, Mashahidi huhisi kwamba elimu yapasa kuchukuliwa kwa uzito sana.
“Elimu yapaswa kusaidia watu wawe washiriki wa jamii wenye mafaa. Yapaswa pia kuwasaidia wasitawishe ufahamu wa urithi wao wa kitamaduni na kuishi maisha yenye kuridhisha zaidi.” —The World Book Encyclopedia
Mashahidi hujitahidi kuishi kulingana na amri hii ya Biblia: “Lolote mfanyalo, mlifanye kwa moyo wenu wote, kana kwamba mwamfanyia Bwana na si wanadamu.” (Wakolosai 3:23, Today’s English Version) Kanuni hiyo yatumika kuhusu sehemu zote za maisha ya kila siku, kutia ndani shule. Hivyo Mashahidi hutia moyo vijana wao wasome kwa bidii na kuchukua kwa uzito kazi wanazogawiwa shuleni.
“Lolote mfanyalo, mlifanye kwa moyo wenu wote, kana kwamba mwamfanyia Bwana.”—Wakolosai 3:23, Today’s English Version
Biblia hufundisha pia kutii sheria za nchi ambako mtu aishi. Kwa hiyo elimu inapokuwa ya lazima hadi umri fulani, Mashahidi wa Yehova hutii sheria hiyo.—Warumi 13:1-7.
Starehe ifaayo, muziki, mambo ya kujifurahisha, mazoezi ya kimwili, na kuzuru maktaba na nyumba za kuhifadhi mambo ya kale yote ni sehemu ya maana katika elimu yenye usawaziko
Bila kupunguza umaana wa mazoezi kwa ajili ya maisha ya kila siku, Biblia huonyesha kwamba hili si lengo pekee wala lengo kuu la elimu. Elimu yenye mafanikio yapasa pia ikuze ndani ya watoto shangwe ya kuishi, na kuwasaidia wachukue mahali pao katika jamii wakiwa watu mmoja-mmoja wenye usawaziko mzuri. Hivyo, Mashahidi wa Yehova huhisi kwamba chaguo la utendaji wa ziada baada ya masomo ya darasani ni la maana sana. Wao huamini kwamba starehe ifaayo, muziki, mambo ya kujifurahisha, mazoezi ya kimwili, kuzuru maktaba na nyumba za kuhifadhi mambo ya kale, na kadhalika, ni sehemu ya maana katika elimu yenye usawaziko. Kwa kuongezea, wao hufundisha watoto wao wastahi watu wenye umri mkubwa na kutafuta fursa za kuwasaidia.
Namna Gani Elimu ya Ziada?
Kwa sababu ya tekinolojia mpya, fursa za kupata kazi zinabadilika daima. Likiwa tokeo, vijana wengi watalazimika kufanya kazi katika sehemu au katika ufundi mbalimbali ambao hawajapata mazoezi hususa juu yao. Hali ikiwa ni hivyo, tabia zao za kufanya kazi na mazoezi yao ya kibinafsi, na hasa uwezo wao wa kubadilikana na hali, utakuwa wenye thamani zaidi kwao. Kwa hiyo, kama ilivyoelezwa na Montaigne, aliyekuwa mwandikaji-insha wa nyakati za Mfufuo wa Harakati, ni bora zaidi kwa wanafunzi kuwa watu wazima wenye ‘vichwa vilivyofundishwa jinsi ya kutumia ujuzi kuliko kuwa wenye vichwa vilivyojaa ujuzi.’
Ukosefu wa kazi za kuajiriwa, unaoathiri nchi zenye utajiri na pia zilizo maskini, mara nyingi hutisha vijana ambao hawana mazoezi ya kutosha. Kwa hiyo, ikiwa fursa za kupata kazi zahitaji mtu awe na mazoezi yanayozidi yale ya msingi yanayotakiwa na sheria, ni daraka la wazazi kuongoza watoto wao katika kufanya uamuzi juu ya elimu ya ziada, wakipima manufaa zinazoweza kupatikana na pia dhabihu ambazo masomo hayo ya ziada yaweza kuhusisha.
Hata hivyo, yaelekea utakubali kwamba mafanikio maishani hutia ndani mengi zaidi ya ufanisi wa kimwili tu. Katika nyakati za karibuni wanaume na wanawake waliotumia maisha zao zote katika kazi-maisha zao walipoteza kusudi lao la kuishi walipopoteza kazi zao. Wazazi fulani wamedhabihu maisha yao ya familia na wakati ambao wangaliweza kutumia pamoja na watoto wao, wakikosa fursa ya kuwasaidia wafikie hali ya kuwa watu wazima, kwa sababu walitumia wakati wote kazini.
Kwa wazi, elimu yenye usawaziko yapasa izingatie kwamba mengi zaidi kuliko ufanisi wa kimwili yanahitajiwa ili kutufurahisha kikweli. Yesu Kristo alisema hivi: “Imeandikwa: ‘Mwanadamu haishi kwa mkate pekee, bali kwa kila neno litokalo kinywani mwa Mungu.’” (Mathayo 4:4, New International Version) Wakiwa Wakristo, Mashahidi wa Yehova huthamini umaana wa kusitawisha sifa za kiadili na za kiroho na pia kujitayarisha ili kutunza mahitaji yao ya kimwili.
-
-
Programu za ElimuMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Programu za Elimu
Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa ajili ya kazi yao ya elimu ya Biblia.
KWA SABABU ya wao kuiona kazi yao ya elimu ya Biblia kuwa ya maana sana, huenda wengine wakafikiri kwamba hawapendezwi na elimu ya kilimwengu. Lakini sivyo. Ili kufundisha wengine, lazima mwalimu ajifunze kwanza, na hilo lataka mazoezi na maagizo yafaayo. Kwa hiyo zaidi ya kutumia ifaavyo elimu ya kilimwengu, Mashahidi wa Yehova wamenufaika kwa miaka mingi na programu za elimu na shule mbalimbali zinazoendeshwa na Watch Tower Society. Hizi zimewasaidia Mashahidi na wengine wajiboreshe kiakili, kiadili, na kiroho.
Kwa kielelezo, katika nchi nyingi Mashahidi wamekabili ugumu wa pekee—jinsi ya kufundisha watu ambao wamekuwa na fursa ndogo au hawajawa na fursa yoyote ya kupokea elimu ifaayo na hivyo hawajui jinsi ya kusoma au kuandika. Ili kutimiza uhitaji huo, Watch Tower Society imepanga programu za kufundisha watu kusoma na kuandika.
Mathalani, katika Nigeria madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika yameendeshwa na Mashahidi wa Yehova tangu 1949. Kupitia madarasa kama hayo, makumi ya maelfu nchini Nigeria wamejifunza kusoma. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia zaidi ya 90 ya Mashahidi wa Yehova katika Nigeria walijua kusoma na kuandika, wakilinganishwa na asilimia isiyozidi 50 ya watu wengine wa nchi hiyo. Katika Mexico, Mashahidi wa Yehova wameendesha madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika tangu 1946. Katika mwaka mmoja, watu zaidi ya 6,500 walifundishwa kusoma na kuandika. Kufikia sasa, tayari watu zaidi ya 100,000 wamesaidiwa kujua kusoma na kuandika. Madarasa ya kufundisha watu kusoma na kuandika yamepangwa pia katika nchi nyingine nyingi, kama vile Bolivia, Kamerun, Nepal, na Zambia. Mashahidi wa Yehova wamechapisha nakala zaidi ya millioni saba za broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika, katika lugha zaidi ya 100.
Mara nyingi programu hizo za kufundisha watu kusoma na kuandika zimepewa utambuzi na wenye mamlaka wa elimu katika nchi ambako zimeendeshwa. Kwa kielelezo, katika Mexico mfanyakazi mmoja wa serikali aliandika hivi: “Nashukuru kwa ajili ya ushirikiano wenu, na kwa niaba ya serikali ninawapitishia hongera yao yenye moyo mweupe sana kwa ajili ya kazi yenu bora yenye maendeleo kwa manufaa ya watu katika kuleta nuru ya ujuzi kwa wale wasiojua kusoma na kuandika. . . . Nawatakia mafanikio katika kazi yenu ya elimu.”
Mazoezi ya Ziada
Wanafunzi hupokea mazoezi katika usomaji na usemaji wa hadharani
Kwa sababu wao huiona kazi yao ya elimu ya Biblia kuwa ya maana sana, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuboresha uwezo wao wa kueleza wengine juu ya mafundisho ya Biblia. Kwa mfano, katika kila kutaniko, zaidi ya makutaniko 119,000 ulimwenguni pote, wanafunzi hupokea mazoezi katika stadi za usomaji na usemaji wa hadharani. Hata wale wachanga zaidi, mara wanapojua jinsi ya kusoma, waweza kujiandikisha na kupokea mazoezi hayo, ambayo huthibitika kuwa yenye mafaa kwao pia katika mambo mengine, na pia katika elimu yao ya kilimwengu. Waelimishaji wengi wamesema kwamba wanafunzi Mashahidi huelekea kujieleza wenyewe vizuri sana.
Kusoma hutiwa moyo sana katika makutaniko yao, na kila familia hutiwa moyo vilevile kuwa na maktaba ya familia yenye vichapo vingi mbalimbali
Kwa kuongezea, kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova linatiwa moyo liwe na maktaba yenye misaada ya kujifunza Biblia, kamusi, na vitabu vingine vya marejezo, katika Jumba la Ufalme lalo, au mahali palo pa kukutania. Maktaba hiyo inaweza kutumiwa na wote wanaohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Kusoma hutiwa moyo sana katika makutaniko yao, na kila familia hutiwa moyo vilevile kuwa na maktaba ya familia yenye vichapo vingi mbalimbali ili kutimiza mahitaji ya watoto na ya watu wazima.
Mazoezi ya Kiwango cha Juu
Watch Tower Society huendesha pia shule za kuzoeza wamishonari wa jinsia zote mbili, na pia shule za kuzoeza wanaume walio na madaraka ya kihuduma katika makutaniko ya mahali-mahali. Shule hizo ni uthibitisho zaidi wa kwamba Mashahidi wa Yehova huiona elimu kuwa ya maana sana.
-
-
Ugumu wa Utofautiano wa KidiniMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Ugumu wa Utofautiano wa Kidini
Ukiwa mwelimishaji, wewe wakabili ugumu ambao waelimishaji katika karne zilizotangulia walikabili mara haba—utofautiano wa kidini.
MUDA wote wa Enzi za Kati, kwa kawaida raia wa nchi ileile walifuata dini ileile. Karibuni zaidi kufikia mwisho wa karne ya 19, Ulaya ilijua dini chache tu zilizo kuu: Ukatoliki na Uprotestanti katika magharibi, Uorthodoksi na Uislamu katika mashariki, na Dini ya Kiyahudi. Bila shaka, utofautiano wa kidini ni jambo la kawaida zaidi leo katika Ulaya na kotekote ulimwenguni. Dini zisizojulikana zimeanzishwa, ama kwa kufuatwa na baadhi ya wenyeji wenyewe wa nchi ama kwa kuletwa na wahamiaji na wakimbizi.
Hivyo, leo katika nchi kama vile Australia, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, na Marekani, twapata Waislamu, Wabuddha, na Wahindu wengi. Wakati uleule, Mashahidi wa Yehova, wakiwa Wakristo, wanahudumu kwa bidii katika nchi zaidi ya 239. Katika kila moja ya nchi 14, washiriki wao watendaji wafikia idadi ya zaidi ya 150,000.—Ona sanduku, “Mashahidi wa Yehova—Dini ya Ulimwenguni Pote.”
Utofautiano wa mazoea ya kidini ya mahali-mahali waweza kutokeza ugumu kwa mwelimishaji. Kwa kielelezo, huenda maswali fulani ya maana yakatokezwa kuhusu sherehe zinazopendwa na wengi: Je, kila mwanafunzi alazimishwe kufuata miadhimisho yote—awe yeye ni wa dini gani? Huenda walio wengi wasione ubaya wowote katika sherehe hizo. Hata hivyo, je, maoni ya familia zilizo washiriki wa kikundi kidogo cha kidini hayapasi kustahiwa pia? Na kuna jambo jingine pia la kufikiriwa: Katika nchi ambazo sheria yatenganisha dini na mambo ya Serikali na mafundisho ya kidini hayatiwi ndani ya utaratibu wa masomo, je, wengine wasingeliona kuwa jambo lisilopatana kufanya sherehe hizo kuwa za lazima shuleni?
Siku za Kuzaliwa
Kutoelewana kwaweza hata kutokea kuhusiana na sherehe zinazoonekana kuwa na uhusiano mdogo wa kidini ikiwa kuna wowote. Hilo ni kweli kuhusu siku za kuzaliwa, zinazosherehekewa katika shule nyingi. Ingawa Mashahidi wa Yehova hustahi haki za wengine za kusherehekea siku za kuzaliwa, bila shaka wewe wajua vema kwamba wao huchagua kutoshiriki katika sherehe hizo. Lakini labda hujui sababu kwa nini wao na watoto wao wameamua kutoshiriki katika sherehe hizi.
Le livre des religions (Kitabu cha Dini Mbalimbali), ambayo ni ensaiklopedia iliyogawanywa sana Ufaransa, yaita desturi hii sherehe na yaiorodhesha miongoni mwa “mazoea ya kilimwengu.” Ingawa zaonwa leo kuwa desturi ya kilimwengu isiyodhuru, kwa kweli sherehe za siku za kuzaliwa zilitokana na upagani.
The Encyclopedia Americana (Chapa ya 1991) yasema hivi: “Ulimwengu wa kale wa Misri, Ugiriki, Roma, na Uajemi ulisherehekea siku za kuzaliwa kwa miungu, wafalme, na wakuu.” Watungaji wa vitabu Ralph na Adelin Linton wafunua sababu ya msingi ya kufanya hivyo. Katika kitabu chao The Lore of Birthdays, wao waliandika hivi: “Mesopotamia na Misri, vyanzo vya ustaarabu, vilikuwa pia nchi za kwanza ambazo watu walikumbuka na kuheshimu siku za kuzaliwa kwao. Kuweka rekodi za siku ya kuzaliwa kulikuwa jambo la maana katika nyakati za kale kwa sababu hasa tarehe ya kuzaliwa ilikuwa muhimu kwa ajili ya kupigwa kwa falaki.” Uhusiano huo wa moja kwa moja na unajimu ni chanzo cha hangaiko kubwa kwa wowote ambao huepuka unajimu kwa sababu ya yale ambayo Biblia husema juu ya huo.—Isaya 47:13-15.
Basi, haishangazi tusomapo hivi katika The World Book Encyclopedia: “Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku ya kuzaliwa Kwake [Kristo] kwa sababu waliiona sherehe ya kuzaliwa kwa mtu yeyote kuwa desturi ya wapagani.”—Buku 3, ukurasa 416.
Mashahidi hufurahia kuwa na nyakati nzuri wakiwa pamoja
Wakizingatia habari hiyo iliyo juu, Mashahidi wa Yehova huchagua kutoshiriki katika karamu za siku za kuzaliwa. Kwa hakika, kuzaliwa kwa mtoto ni jambo lenye furaha, lililo zuri ajabu. Kwa asili, wazazi wote hushangilia watoto wao wanapokua na kusitawi kila mwaka upitapo. Mashahidi wa Yehova hupata pia shangwe nyingi katika kuonyesha upendo wao kwa familia na rafiki zao kwa kutoa zawadi na kuwa na nyakati nzuri wakiwa pamoja. Hata hivyo, kwa sababu ya chanzo cha sherehe za siku za kuzaliwa, wao hupendelea kufanya hivyo katika nyakati nyinginezo muda wote wa mwaka.—Luka 15:22-25; Matendo 20:35.
Krismasi
Krismasi husherehekewa ulimwenguni pote, hata katika nchi nyingi zisizo za Kikristo. Kwa kuwa sikukuu hiyo inakubaliwa na dini zilizo nyingi za Jumuiya ya Wakristo, huenda ikaonekana kuwa jambo la kushangaza sana kwamba Mashahidi wa Yehova huchagua kutoisherehekea. Kwa nini ni hivyo?
Kama vile ensaiklopedia nyingi zisemavyo kwa wazi, siku ya kuzaliwa kwa Yesu iliwekwa bila kufuata kanuni yoyote kuwa Desemba 25 ili ilingane na sikukuu ya kipagani ya Kiroma. Ona taarifa zifuatazo zilizochukuliwa kutoka katika vitabu tofauti-tofauti vya marejezo:
“Tarehe ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani. Gospeli hazionyeshi wala siku wala mwezi.”—New Catholic Encyclopedia, Buku 3, ukurasa 656.
“[Sherehe ya] Saturnalia katika Roma ilitolea mfano desturi zilizo nyingi zenye furaha za wakati wa Krismasi.”—Encyclopædia of Religion and Ethics
“Nyingi kati ya desturi za Krismasi zinazoenea sasa katika Ulaya, au zilizorekodiwa kutoka nyakati zilizopita, si desturi za Kikristo zilizo za kweli, bali ni desturi za kipagani ambazo zimefuatwa au kuvumiliwa na Kanisa. . . . [Sherehe ya] Saturnalia katika Roma ilitolea mfano desturi zilizo nyingi zenye furaha za wakati wa Krismasi.”—Encyclopædia of Religion and Ethics (Edinburgh, 1910), iliyohaririwa na James Hastings, Buku 3, kurasa 608-609.
“Krismasi imesherehekewa mnamo Desemba 25 katika makanisa yote ya Kikristo tangu karne ya nne. Wakati huo, hiyo ilikuwa ni tarehe ya sikukuu ya kipagani iliyoitwa ‘Kuzaliwa (Kilatini, natale) kwa Jua,’ ya kusherehekea majira ya baridi kali ya upeo wa jua, kwa kuwa jua lilionekana kuzaliwa upya siku zilipoanza tena kuwa ndefu zaidi. Katika Roma, Kanisa lilianza kufuata desturi hii iliyopendwa sana . . . kwa kuipa maana mpya.”—Encyclopædia Universalis, 1968, (ya Kifaransa) Buku 19, ukurasa 1375.
“Ukuzi wa sikukuu ya Krismasi uliathiriwa na utofautiano wayo na sherehe za kipagani za Sol Invictus (Mithra). Kwa upande ule mwingine, Desemba 25, ikiwa ndiyo siku ya majira ya baridi kali ya upeo wa jua, ilionwa kuwa yafanana na ile nuru iliyotokea ghafula ulimwenguni kupitia Kristo, hivyo ule ufananisho wa Sol Invictus ukapitishwa kwa Kristo.”—Brockhaus Enzyklopädie, (ya Kijerumani) Buku 20, ukurasa 125.
Wanapojifunza mambo ya hakika juu ya Krismasi, wengine wameitikiaje? The Encyclopædia Britannica ilionelea hivi: “Katika 1644 warekebishaji wa kidini Waingereza walikataza kusiwe na sherehe yoyote wala ibada za kidini kupitia amri ya Bunge, kwa msingi wa kwamba [Krismasi] ilikuwa sikukuu ya kipagani, nao wakaamuru isherehekewe kwa kufunga. Charles wa 2 alianzisha tena sikukuu hiyo, lakini watu wa Scotland walishikamana na maoni ya Warekebishaji wa Kidini.” Wakristo wa mapema hawakusherehekea Krismasi, wala Mashahidi wa Yehova hawaisherehekei leo wala kushiriki katika utendaji mbalimbali unaoshirikishwa na Krismasi.
Hata hivyo, Biblia husema kwa upendeleo juu ya kutoa zawadi au kualika familia na marafiki kwa ajili ya mlo wenye shangwe kwenye pindi nyinginezo. Hiyo hutia moyo wazazi wazoeze watoto wao wawe na ukarimu wenye moyo mweupe, badala ya kutoa zawadi wanapotazamiwa tu kufanya hivyo kijamii. (Mathayo 6:2, 3) Watoto wa Mashahidi wa Yehova hufundishwa kuvumilia na kuwa wenye staha, na hilo latia ndani kutambua haki ya wengine ya kusherehekea Krismasi. Kisha, wao huthamini wakati uamuzi wao wa kutoshiriki katika sherehe za Krismasi unapostahiwa.
Sherehe Nyinginezo
Mashahidi wa Yehova huchukua msimamo uo huo kuelekea sikukuu nyinginezo za kidini au zinazohusiana na dini ambazo hutukia katika mwaka wa shule katika nchi mbalimbali, kama vile sikukuu za Juni katika Brazili, Epiphany katika Ufaransa, Carnival katika Ujerumani, Setsubun katika Japani, na Halloween katika Marekani. Kwa habari ya sherehe hizi au nyingine yoyote hususa isiyotajwa hapa, wazazi Mashahidi au watoto wao wangefurahi kwa hakika kujibu maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo.
-
-
Kanuni za Adili Zinazostahili StahaMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Mashahidi wa Yehova hujaribu kukaza katika watoto wao kanuni za Kikristo zilizo za kweli
Kanuni za Adili Zinazostahili Staha
Muda wote wa historia, wanaume na wanawake hodari wamechukua msimamo ulio kinyume cha fikira za wengi katika nyakati zao. Wamevumilia udhalimu wa kisiasa, wa kidini, na wa ubaguzi wa rangi, mara nyingi wakitoa uhai wao kwa ajili ya madhumuni yao.
WAKRISTO wa mapema walikuwa wenye moyo mkuu hasa. Wakati wa ile minyanyaso mibaya ya karne tatu za kwanza, wengi wao waliuawa na Waroma wapagani kwa sababu ya kukataa kumwabudu maliki. Nyakati nyingine, madhabahu ilijengwa katika uwanja wa michezo. Ili kupata uhuru wao, Wakristo walihitaji tu kuchoma kiasi kidogo sana cha uvumba kuonyesha utambuzi wa hali ya kimungu ya maliki. Hata hivyo, ni wachache walioacha imani yao. Walio wengi walipendelea kufa badala ya kukana imani yao.
Katika nyakati za kisasa, Mashahidi wa Yehova wa Kikristo huchukua msimamo uo huo kwa habari ya kutokuwamo kwa kisiasa. Kwa kielelezo, msimamo wao imara walipokabili Unazi waweza kuthibitishwa katika rekodi za kihistoria. Kabla ya, na wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, karibu robo ya Mashahidi Wajerumani walipoteza uhai wao, hasa katika kambi za mateso, kwa sababu waliendelea kutokuwamo nao walikataa kusema “Heil Hitler.” Watoto wachanga walitenganishwa kwa nguvu kutoka kwa wazazi wao Mashahidi. Ujapokuwa mbano huo, vijana waliendelea kuwa imara nao wakakataa kuchafuliwa na mafundisho yasiyo ya kimaandiko ambayo wengine walijaribu kuwalazimisha wakubali.
Kusalimu Bendera
Kwa ujumla Mashahidi wa Yehova si shabaha ya mnyanyaso mkali wa jinsi hiyo leo. Hata hivyo, nyakati nyingine kuelewa vibaya hutokea kwa sababu ya uamuzi wenye kudhamiria wa Mashahidi wachanga wa kutoshiriki katika sherehe za kizalendo kama vile kusalimu bendera.
“Rudishieni Kaisari vilivyo vya Kaisari—na Mungu vilivyo vya Mungu”—Mathayo 22:21, Jerusalem Bible
Watoto wa Mashahidi wa Yehova hufundishwa wasizuie wengine kusalimu bendera; hilo ni jambo la kuamuliwa na kila mtu mmoja-mmoja. Hata hivyo, msimamo wa Mashahidi wenyewe ni imara: Wao hawasalimu bendera ya taifa lolote. Hilo kwa hakika halina nia ya kuonyesha ukosefu wa staha. Wao huistahi bendera ya nchi yoyote wanamoishi, nao huonyesha staha hiyo kwa kutii sheria za nchi hiyo. Hawashiriki kamwe katika aina yoyote ya utendaji wa kupinga serikali. Kwa kweli, Mashahidi huamini kwamba serikali za binadamu zilizopo hufanyiza “mpango wa Mungu” ambao yeye ameruhusu uweko. Kwa hiyo wao hujiona kuwa chini ya amri ya kimungu ya kulipa kodi na kustahi “mamlaka [hizo] zilizo kubwa.” (Warumi 13:1-7, NW) Hilo lapatana na taarifa maarufu ya Kristo: “Rudishieni Kaisari vilivyo vya Kaisari—na Mungu vilivyo vya Mungu.”—Mathayo 22:21, Jerusalem Bible ya Katoliki.
‘Lakini, kwa nini,’ huenda wengine wakauliza, ‘Mashahidi wa Yehova hawaiheshimu bendera kwa kuisalimu?’ Ni kwa sababu wao huona kusalimu bendera kuwa tendo la ibada, na ibada ni ya Mungu; hawawezi kwa kudhamiria kuabudu yeyote au chochote isipokuwa Mungu. (Mathayo 4:10; Matendo 5:29) Kwa hiyo, wao huthamini wakati waelimishaji wanapostahi sadikisho hili na kuruhusu watoto Mashahidi wafuate itikadi zao.
Haishangazi kwamba si Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoamini kwamba kusalimu bendera kuna uhusiano na ibada, kama vile maelezo yafuatayo yaonyeshavyo:
“Bendera za mapema karibu zilikuwa za aina ya kidini kabisa. . . . Msaada wa dini ulikuwa daima ukitafutwa ili kuzipa utakatifu bendera za kitaifa.” (Italiki ni zetu.)—Encyclopædia Britannica.
“Bendera ni takatifu, kama vile msalaba. . . . Kanuni na amri zinazohusu mtazamo wa binadamu kuelekea viwango vya kitaifa hutumia maneno yenye nguvu na yaliyo dhahiri, kama vile, ‘Utumishi kwa Bendera,’ . . . ‘Kicho kwa Bendera,’ ‘Ujitoaji kwa Bendera.’” (Italiki ni zetu.)—The Encyclopedia Americana.
“Wakristo walikataa . . . kutolea dhabihu roho ya kimungu ya maliki [Mroma]—karibu na vile leo kukataa kusalimu bendera au kurudia kiapo cha uaminifu wa kiraia.”—Those About to Die (1958), cha Daniel P. Mannix, ukurasa 135.
Vijana Waebrania watatu walikataa kuinamia sanamu iliyojengwa na mfalme Mbabiloni Nebukadreza
Tena, Mashahidi wa Yehova hawana nia ya kutostahi serikali yoyote wala watawala wayo kwa kukataa kusalimu bendera. Ni kwamba tu, hawatainamia wala kusalimu sanamu inayowakilisha Serikali katika tendo lolote la ibada. Wanaona hilo kuwa sawa na msimamo uliochukuliwa katika nyakati za Biblia na vijana Waebrania watatu waliokataa kuinamia ile sanamu iliyojengwa katika uwanda wa Dura na mfalme Mbabiloni Nebukadreza. (Danieli, sura ya 3) Kwa hiyo basi, ingawa wengine husalimu na kuapa uaminifu wa kiraia, watoto wa Mashahidi wa Yehova wanafundishwa kufuata dhamiri zao zilizozoezwa na Biblia. Hivyo, kwa ukimya na kwa staha wao huepuka kushiriki. Kwa sababu zizo hizo, watoto Mashahidi huchagua kutoshiriki wakati nyimbo za kitaifa zinapoimbwa au kupigwa.
Haki ya Wazazi
Siku hizi, nchi zilizo nyingi hustahi haki ya wazazi ya kuwapa watoto wao maagizo ya kidini kwa kupatana na masadikisho yao. Dini zote huunga mkono haki hiyo, kama vile ionyeshwavyo na sheria iliyo halali bado katika Kanisa Katoliki: “Wakiwa wamewapa watoto wao uhai, wazazi wako chini ya ule wajibu imara wa kuwaelimisha, nao wana haki ya kufanya hivyo; hiyo ndiyo sababu ni lazima hasa waandalie watoto wao elimu ya Kikristo kulingana na fundisho la Kanisa.”—Sheria 226.
Watoto wanatiwa moyo wapendezwe na wengine
Mashahidi wa Yehova hawaombi jambo jingine zaidi. Wakiwa wazazi wenye kujali, wao hujaribu kukaza kikiki kanuni za Kikristo zilizo za kweli katika watoto wao na kukaza ndani yao upendo kwa jirani na staha kwa mali za watu wengine. Wao hutamani kufuata lile shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo katika Efeso: “Wazazi, msiwatende watoto wenu kwa njia ya kuwakasirisha. Badala ya hivyo, waleeni kwa nidhamu na maagizo ya Kikristo.”—Waefeso 6:4, Today’s English Version.
Nyumba Zilizogawanyika Kidini
Katika familia fulani, mzazi mmoja tu ni Shahidi wa Yehova. Katika hali ya jinsi hiyo, mzazi Shahidi anatiwa moyo atambue haki ya yule mzazi ambaye si Shahidi ya kuagiza pia watoto kulingana na masadikisho yake ya kidini. Watoto wanaofunuliwa kwa maoni tofauti ya kidini hupatwa na madhara machache, ikiwa kuna yoyote.a Kwa kweli, ni lazima watoto wote wachague ni dini gani watakayofuata. Kwa asili, si vijana wote wanaochagua kufuata kanuni za kidini za wazazi wao, wawe ni Mashahidi wa Yehova au la.
Haki ya Watoto ya Kuwa na Uhuru wa Dhamiri
Wapaswa kujua pia kwamba Mashahidi wa Yehova huiona dhamiri ya Kikristo ya mtu mmoja-mmoja kuwa ya maana sana. (Warumi, sura ya 14) Kanuni juu ya Haki za Mtoto, iliyokubaliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa katika 1989, ilitambua haki ya mtoto ya kuwa na “uhuru wa fikira, dhamiri na dini” na haki ya “kueleza maoni yake kwa uhuru na maoni hayo kufikiriwa ifaavyo katika jambo lolote au taratibu yoyote inayomwathiri mtoto huyo.”
Hakuna watoto wawili walio sawasawa kabisa. Kwa hiyo, waweza kutazamia ifaavyo tofauti fulani katika maamuzi ambayo Mashahidi wachanga au wanafunzi wengine wanafanya kwa habari ya utendaji na migawo fulani shuleni. Twatumaini kwamba wewe wakubaliana pia na kanuni ya uhuru wa dhamiri.
a Kuhusu watoto wa ndoa zenye dini tofauti, Steven Carr Reuben, Ph.D., katika kitabu chake Raising Jewish Children in a Contemporary World, aonelea hivi: “Watoto hufadhaika wakati wazazi wanapoishi maisha ya kujikana, ya kufadhaika, ya kisiri, na ya kuepuka masuala ya kidini. Wazazi wanapokuwa wazi, wanyoofu, dhahiri juu ya itikadi, kanuni, na njia zao wenyewe za kusherehekea, watoto hukua wakiwa na ile aina ya usalama na hisi ya kuwa wao ni wa maana katika mambo ya kidini ambayo ni ya maana sana kwa habari ya ukuzi wa hali yao ya ujumla ya kujistahi na kujua mahali pao ulimwenguni.”
-
-
Daraka la WazaziMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Daraka la Wazazi
Bila shaka, kulea watoto kuwa watu wazima wenye usawaziko katika jamii ya leo si jambo rahisi.
Waelimishaji wana daraka kuu katika kutokeza watu wazima vijana waliorekebishwa vizuri
TAASISI ya Kitaifa ya Afya ya Akilini ya Marekani ilitangaza matokeo ya uchunguzi fulani wa wazazi walioonwa kuwa wenye mafanikio—wale ambao watoto wao, wenye umri wa miaka zaidi ya 21, “walikuwa watu wazima wenye matokeo ambao walionekana kuwa wenye kubadilikana vizuri na jamii yetu.” Wazazi hao waliulizwa hivi: ‘Kwa msingi wa ono lenu kibinafsi, ni shauri gani zuri zaidi mwezalo kutolea wazazi wengine?’ Majibu ya kawaida zaidi yalikuwa haya: ‘Onyesha upendo mwingi,’ ‘toa nidhamu kwa njia ya kujenga,’ ‘tumia wakati pamoja nao,’ ‘fundisha watoto wako tofauti kati ya mema na mabaya,’ ‘sitawisha hali ya kustahiana,’ ‘wasikilize kikweli,’ ‘toa mwongozo badala ya hotuba,’ na ‘mwe wenye maoni ya kihalisi.’
Hata hivyo, wazazi hawako peke yao katika kujitahidi kutokeza watu wazima vijana waliorekebishwa vizuri. Waelimishaji pia wana daraka katika hilo. Mshauri fulani wa shule mwenye uzoefu alionelea hivi: “Kusudi hasa la elimu rasmi ni kutegemeza wazazi katika kutokeza watu wazima vijana wenye kuchukua madaraka ambao wamesitawishwa vizuri kiakili, kimwili, na kihisiamoyo.”
Kwa hiyo wazazi na waelimishaji wana lengo lilelile—kutokeza vijana ambao baadaye watakuwa watu wazima wakomavu na wenye usawaziko wanaofurahia maisha na wawezao kuona mahali pao katika jamii wanamoishi.
Wafanyakazi Wenzao, Si Washindani
Hata hivyo, matatizo hutokea wakati wazazi wanaposhindwa kushirikiana na waelimishaji. Kwa kielelezo, wazazi fulani hawajali hata kidogo elimu ya watoto wao; wengine hujaribu kushindana na walimu. Likizungumzia hali hii, jarida moja la Kifaransa lilisema hivi: “Mwalimu hawi tena peke yake katika kusimamia mambo. Wazazi, wanaokazia kupita kiasi mafanikio ya watoto wao, huchanganua vitabu vya shule, huamua na kuchambua njia za kufundisha, nao hukasirika mara iyo hiyo kwa sababu ya maksi mbaya za kwanza za mtoto wao.” Matendo hayo yaweza kuingilia haki za walimu.
Mashahidi wa Yehova huhisi kwamba watoto wao wanatumikiwa vizuri zaidi wakati wazazi wanaposhirikiana na waelimishaji, wakipendezwa na elimu ya watoto wao kwa bidii na kwa njia yenye kusaidia
Mashahidi wa Yehova huhisi kwamba watoto wao wanatumikiwa vizuri zaidi wakati wazazi wanaposhirikiana na waelimishaji, wakipendezwa na elimu ya watoto wao kwa bidii na kwa njia yenye kusaidia. Wao huamini kwamba ushirikiano huo ni wa maana hasa kwa sababu kazi yako ukiwa mwelimishaji imezidi kuwa ngumu.
Matatizo ya Shule Leo
Zikionyesha hali ya jamii ambayo hizo ni sehemu yayo, shule hazilindwi dhidi ya matatizo ya jamii kwa ujumla. Matatizo ya kijamii yameongezeka upesi kwa muda wa miaka ambayo imepita. Likifafanua hali katika shule moja Marekani, The New York Times liliripoti hivi: “Wanafunzi hulala darasani, wao hutishana kwenye vijia vya shule vilivyojaa michoro na maandishi, wao huwashusha wale wanafunzi wema. . . . Karibu wanafunzi wote wanakabiliana na matatizo kama vile kutunza watoto, kushughulika na wazazi walio gerezani, na kuponyoka ujeuri wa magenge. Katika siku yoyote ile, karibu mmoja kati ya watano hukosa shule.”
Lenye kutia hofu zaidi ni lile tatizo la kimataifa lenye kuongezeka la ujeuri shuleni. Mahali pa mapigano ya mara kwa mara yanayohusisha kusukumana pamechukuliwa na ufyatuaji-risasi na uchomaji-visu ulio wa kawaida. Silaha zimekuja kuwa za kawaida zaidi, mashambulio yamekuwa mabaya zaidi, watoto wakielekea kuwa wajeuri upesi zaidi na wakiwa wachanga zaidi.
Bila shaka, si kila nchi inayokabili hali hizo za kuhuzunisha. Hata hivyo, waelimishaji wengi ulimwenguni pote hukabili ile hali itajwayo katika lile gazeti la Kifaransa la kila juma Le Point: “Mwalimu hastahiwi tena; yeye hana mamlaka.”
Wazazi wenye mafanikio hutumia wakati pamoja na watoto wao
Kutostahi huko kwa mamlaka kwatokeza hatari halisi kwa watoto wote. Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova hujaribu kukaza kikiki katika watoto wao utii na staha kwa mamlaka, sifa ambazo mara nyingi hukosekana katika maisha ya shuleni leo.
-
-
UmalizioMashahidi wa Yehova na Elimu
-
-
Umalizio
KUSUDI la broshua hii haikuwa kuzungumzia itikadi zote za kidini za Mashahidi wa Yehova. Badala ya hivyo, tumejitahidi kueleza baadhi ya kanuni ambazo Mashahidi huamini na kuonyesha wazi aina za uvutano mbalimbali wa familia unaoathiri mwanafunzi wako ikiwa mzazi mmoja au wote wawili ni Mashahidi.
Mashahidi wa Yehova hukazia sana ukuzi wa kiroho wa watoto wao. Nao wahisi uhakika kwamba huo huendeleza ukuzi wa watoto wao katika mambo mengine. Itikadi wanazokubali na kanuni wanazofuata huzipa maisha zao maana nazo huwasaidia washughulike na matatizo yao ya kila siku. Kwa kuongezea, itikadi na kanuni hizo zapasa kuwasukuma wajaribu kuwa wanafunzi wenye bidii na raia wema muda wote wa maisha.
Mashahidi hujitahidi kuona maisha kihalisi, kwa hiyo wao huiona elimu kuwa ya maana sana. Kwa hiyo, ni tamaa yao kushirikiana nawe kwa uwezo wao wote. Kwa upande wao, wakiwa nyumbani mwao na katika mahali pao mbalimbali pa ibada kotekote ulimwenguni, wao wataendelea kuwatia moyo watoto wao watimize daraka lao katika ushirikiano huu wenye matokeo.
-