Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuijua “Akili ya Kristo”
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Februari 15
    • Kuijua “Akili ya Kristo”

      “‘Ni nani amekuja kuijua akili ya Yehova, kwamba apate kumfundisha?’ Lakini sisi tunayo akili ya Kristo.”—1 WAKORINTHO 2:16.

      1, 2. Katika Neno lake, Yehova aliona inafaa kufunua nini juu ya Yesu?

      YESU alikuwa na sura gani? Alikuwa na nywele zenye rangi gani? ngozi yenye rangi gani? na macho yenye rangi gani? Alikuwa mrefu kadiri gani? Alikuwa na uzito gani? Karne ambazo zimepita, Yesu amechorwa kwa njia zinazotofautiana, tokea michoro yenye kiasi hadi michoro yenye kupita kiasi. Wengine wamemchora akiwa mwanamume mwenye nguvu na mwenye utendaji sana, huku wengine wakimchora akiwa dhaifu na mwenye huzuni.

      2 Lakini Biblia haitilii mkazo sana sura ya Yesu. Badala yake, Yehova aliona inafaa kufunua jambo muhimu zaidi: utu wa Yesu. Masimulizi ya Gospeli hayataji tu maneno ya Yesu na matendo yake bali pia yanafunua kina cha hisia zake za moyoni na njia yake ya kufikiri ambazo zilichochea maneno yake na matendo yake. Masimulizi hayo manne yaliyopuliziwa hutuwezesha kuchunguza kile ambacho mtume Paulo alikiita “akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Ni muhimu tufahamu mawazo, hisia, na utu wa Yesu. Kwa nini? Kuna angalau sababu mbili.

      3. Kufahamu akili ya Kristo kwaweza kutufahamisha nini?

      3 Kwanza, akili ya Kristo inatuwezesha kuelewa akili ya Yehova Mungu. Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yake hivi kwamba angeweza kusema: “Mwana ni nani hakuna ajuaye ila Baba; na ya kwamba Baba ni nani, hakuna ajuaye ila Mwana, na yeye ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema, ‘Mkitaka kujua jinsi Yehova alivyo, mnitazame.’ (Yohana 14:9) Basi, tunapojifunza mambo ambayo Gospeli zinafunua kuhusu jinsi Yesu alivyofikiri na kuhisi, kwa kweli tunajifunza jinsi Yehova anavyofikiri na kuhisi. Ujuzi huo hutuwezesha kumkaribia Mungu wetu zaidi.—Yakobo 4:8.

      4. Ikiwa kwa kweli tunataka kutenda kama Kristo, ni lazima kwanza tujifunze nini, na kwa nini?

      4 Pili, kujua akili ya Kristo hutusaidia ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Kumfuata Yesu si kukariri tu maneno yake na kuiga matendo yake. Kwa kuwa usemi na matendo huchochewa na mawazo na hisia, kumfuata Kristo ni kusitawisha ‘mtazamo uleule wa akili’ aliokuwa nao. (Wafilipi 2:5) Yaani, ikiwa kwa kweli tunataka kutenda kama Kristo, ni lazima kwanza tujifunze kufikiri na kuhisi kama yeye kwa kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. Basi, kwa msaada wa waandikaji wa Gospeli, ebu tuchunguze akili ya Kristo. Kwanza tutazungumzia mambo ambayo yaliongoza mawazo na hisia za Yesu.

      Maisha Yake ya Kabla ya Kuwa Mwanadamu

      5, 6. (a) Watu tunaoshirikiana nao wanaweza kuwa na uvutano gani kwetu? (b) Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu alikuwa na ushirika gani mbinguni kabla ya kuja duniani, na ushirika huo ulikuwa na uvutano gani kwake?

      5 Watu tunaoshirikiana nao kwa ukaribu wanaweza kuwa na uvutano juu yetu, wakiathiri mawazo yetu, hisia zetu, na matendo yetu kwa mema au kwa mabaya.a (Mithali 13:20) Ebu fikiria mashirika ya Yesu huko mbinguni kabla ya kuja duniani. Gospeli ya Yohana yaonyesha Yesu akiwa “Neno,” au Msemaji wa Mungu, kabla ya kuwa mwanadamu. Yohana asema: “Hapo mwanzoni Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa mungu. Huyo alikuwa hapo mwanzoni pamoja na Mungu.” (Yohana 1:1, 2) Kwa kuwa Yehova hana mwanzo, kuwapo kwa Neno pamoja na Mungu tangu “mwanzoni” ni lazima kwarejezea mwanzo wa uumbaji wa Mungu. (Zaburi 90:2) Yesu ndiye “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” Kwa hiyo, alikuwapo kabla ya kuumbwa kwa viumbe wengine wa roho na ulimwengu halisi.—Wakolosai 1:15; Ufunuo 3:14.

      6 Kulingana na makadirio fulani ya kisayansi, ulimwengu halisi umekuwapo kwa angalau miaka bilioni 12. Ikiwa makadirio hayo yamekaribia ukweli, basi Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu alishirikiana kwa ukaribu na Baba yake kwa muda mrefu sana kabla ya Adamu kuumbwa. (Linganisha Mika 5:2.) Basi kukawa na uhusiano wa karibu sana na wenye upendo kati yao wawili. Akifananishwa na hekima, Mwana huyu mzaliwa wa kwanza aonyeshwa akisema hivi wakati wa maisha yake ya kabla ya kuwa mwanadamu: “Nikawa furaha [ya Yehova] kila siku; nikifurahi daima mbele zake.” (Mithali 8:30) Kwa kweli, kutumia muda mrefu sana akishirikiana kwa ukaribu sana na Chanzo cha upendo kulikuwa na uvutano mkubwa sana kwa Mwana wa Mungu! (1 Yohana 4:8) Mwana huyo akajua mawazo, hisia, na njia za Baba yake na kuzidhihirisha kwa njia ambayo hakuna mtu mwingine yeyote angeweza kuzidhihirisha.—Mathayo 11:27.

      Maisha Yake Duniani na Uvutano Mwingi

      7. Ni ipi mojawapo ya sababu zilizomfanya Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu aje duniani?

      7 Bado Mwana wa Mungu alikuwa na mengi ya kujifunza, kwa sababu kusudi la Yehova lilikuwa kumwandaa Mwana wake awe Kuhani wa Cheo cha Juu mwenye huruma, awezaye “kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali.” (Waebrania 4:15) Kutimiza matakwa ya daraka hilo ni mojawapo ya sababu zilizomfanya Mwana aje duniani akiwa binadamu. Hapa, akiwa mwanadamu mwenye nyama na damu, Yesu alijionea hali na uvutano mwingi ambao kabla ya wakati huo alikuwa ameyaona tu akiwa mbinguni. Sasa angeweza kuwa na hisia na hisia-moyo kama wanadamu. Nyakati nyingine alichoka, aliona kiu, na kuhisi njaa. (Mathayo 4:2; Yohana 4:6, 7) Hata zaidi, alivumilia magumu mengi na mateseko mengi. Basi “alijifunza utii,” akastahili kabisa daraka lake akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu.—Waebrania 5:8-10.

      8. Tunajua nini kuhusu maisha ya mapema ya Yesu duniani?

      8 Namna gani mambo yaliyompata Yesu akiwa mtoto duniani? Rekodi ya utoto wake ni fupi sana. Hata ni Mathayo na Luka tu waliosimulia mambo yaliyotukia yaliyohusu kuzaliwa kwake. Waandikaji wa Gospeli walijua kwamba Yesu alikuwa ameishi mbinguni kabla ya kuja duniani. Uhai wake wa kabla hajaja duniani ulidhihirisha sana utu wake kuliko jambo jingine lolote. Hata hivyo, Yesu alikuwa binadamu kamili. Ingawa alikuwa mkamilifu, bado ilikuwa lazima akue tokea utotoni, apitie ujana na hatimaye kuwa mtu mzima, akijifunza wakati huo wote. (Luka 2:51, 52) Biblia inafunua mambo fulani kuhusu maisha ya Yesu ya utotoni ambayo bila shaka yalikuwa na uvutano juu yake.

      9. (a) Ni nini kinachodokeza kwamba Yesu alizaliwa katika familia maskini? (b) Yaelekea Yesu alikulia katika hali za aina gani?

      9 Inaonekana Yesu alizaliwa katika familia maskini. Hilo linaonyeshwa na toleo ambalo Yosefu na Maria walileta kwenye hekalu siku 40 hivi baada ya kuzaliwa kwake. Badala ya kuleta mwana-kondoo mchanga awe toleo la kuteketezwa na hua mchanga au njiwa-tetere kwa ajili ya toleo la dhambi, wao walileta ama “jozi moja ya njiwa-tetere au hua wachanga wawili.” (Luka 2:24) Kulingana na Sheria ya Kimusa, toleo hilo lilipaswa kutolewa na maskini. (Mambo ya Walawi 12:6-8) Baada ya muda familia hii ya hali ya chini ilikua. Baada ya kumzaa Yesu kimuujiza, Yosefu na Maria walizaa angalau watoto wengine sita kwa njia ya kawaida. (Mathayo 13:55, 56) Basi, Yesu akakua katika familia kubwa na yaelekea katika nyumba yenye hali za kawaida.

      10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Maria na Yosefu walikuwa watu wenye kumcha Mungu?

      10 Yesu alilelewa na wazazi wenye kumcha Mungu ambao walimtunza. Mamake, Maria, alikuwa mwanamke wa kipekee. Kumbuka kwamba malaika Gabrieli alisema hivi alipomsalimu: “Siku njema, mwenye kupendelewa sana, Yehova yuko pamoja na wewe.” (Luka 1:28) Yosefu pia alikuwa mtu mwenye kumcha Mungu. Kwa uaminifu, yeye alifunga safari ya kilometa 150 kwenda Yerusalemu kila mwaka kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa. Maria pia alihudhuria, hata ingawa ni wanaume tu waliokuwa na wajibu wa kuhudhuria. (Kutoka 23:17; Luka 2:41) Katika pindi moja kama hiyo, Yosefu na Maria walimpata Yesu mwenye umri wa miaka 12 hekaluni akiwa katikati ya walimu baada ya kumtafuta sana. Yesu akawaambia wazazi wake waliokuwa na wasiwasi: “Je, hamkujua kwamba ni lazima mimi niwe katika nyumba ya Baba yangu?” (Luka 2:49) “Baba”—ni lazima neno hilo liwe lilitokeza hisia nzuri ya upendo kwa kijana Yesu. Kwanza, yaonekana alikuwa ameambiwa kwamba Yehova ndiye Baba yake halisi. Na zaidi, ni lazima Yosefu alikuwa baba-mlezi mzuri kwa Yesu. Kwa kweli Yehova hangemchagua mtu mkali wala mkatili amlee Mwana Wake mpendwa!

      11. Yesu alijifunza ufundi gani, na katika nyakati za Biblia, kazi hiyo ilihusisha nini?

      11 Katika miaka aliyokaa Nazareti, Yesu alijifunza useremala, yaelekea kutoka kwa babake mlezi, Yosefu. Yesu alikuwa stadi sana hivi kwamba yeye mwenyewe aliitwa “seremala.” (Marko 6:3) Katika nyakati za Biblia, seremala walijenga nyumba, walitengeneza vitu (kutia ndani meza, stuli, na benchi), na vifaa vya kilimo. Katika Dialogue With Trypho, Justin Martyr, wa karne ya pili W.K., aliandika hivi kumhusu Yesu: “Alizoea useremala alipokuwa miongoni mwa wanadamu, akitengeneza plau na nira.” Kazi hiyo haikuwa rahisi, kwa sababu huenda seremala wa wakati huo wa kale hangeweza kununua mbao. Yaelekea alitoka, akautafuta mti ufaao, akaukata, na kupeleka mbao nyumbani. Kwa hiyo, huenda Yesu aliyajua magumu ya kupata riziki, kushughulika na wateja, na kuiruzuku familia.

      12. Ni nini kinachoonyesha kwamba yaelekea Yosefu alikufa kabla ya Yesu, na jambo hilo lingemaanisha nini kwa Yesu?

      12 Akiwa mtoto wa kwanza, yaelekea Yesu alisaidia kutunza familia, hasa kwa sababu inaonekana Yosefu alikufa kabla ya Yesu.b Gazeti Zion’s Watch Tower la Januari 1, 1900, lilisema: “Mapokeo yanaonyesha kwamba Yosefu alikufa Yesu akiwa angali mchanga, na kwamba [Yesu] alianza useremala ili kuiruzuku familia. Jambo hilo laungwa mkono na ushuhuda wa Kimaandiko mahali ambapo Yesu mwenyewe anaitwa seremala, na mamake na ndugu zake wanatajwa, lakini Yosefu hatajwi. (Marko 6:3) . . . Basi inawezekana kwamba kile kipindi kirefu cha miaka kumi na minane ya maisha ya Bwana wetu, tokea wakati wa lile tukio [linalotajwa kwenye Luka 2:41-49] hadi wakati alipobatizwa, alikitumia kufanya mambo ya kawaida maishani.” Yaelekea Maria na watoto wake, kutia ndani Yesu, walihuzunishwa na kifo cha mume na baba mpendwa.

      13. Yesu alipoanza huduma yake, kwa nini alikuwa na ujuzi, ufahamu wa ndani, na hisia za moyoni ambazo hakuna mtu mwingine angeweza kuonyesha?

      13 Kwa wazi, Yesu hakuzaliwa katika maisha rahisi. Badala yake aliishi maisha ya watu wa kawaida. Kisha, mwaka wa 29 W.K., wakati ukafika wa Yesu kutekeleza mgawo aliopewa na Mungu uliokuwa ukimngoja. Katika vuli ya mwaka huo, alibatizwa katika maji na kuzaliwa akiwa Mwana wa roho wa Mungu. ‘Alifunguliwa mbingu,’ yaelekea ikimaanisha kwamba sasa angeweza kukumbuka maisha yake ya mbinguni ya kabla hajawa mwanadamu, kutia ndani mawazo na hisia alizokuwa nazo wakati huo. (Luka 3:21, 22) Basi Yesu alipoanza huduma yake, alikuwa na ujuzi, ufahamu wa ndani, na hisia za moyoni ambazo hakuna mtu mwingine angeweza kuonyesha. Kwa sababu nzuri, waandikaji wa Gospeli waliandika hasa juu ya matukio ya huduma ya Yesu. Na bado hata hawakuweza kuandika kila jambo alilosema na kufanya. (Yohana 21:25) Lakini mambo ambayo walipuliziwa kuandika yatuwezesha kuchunguza akili ya mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani.

      Utu wa Yesu Akiwa Mwanadamu

      14. Gospeli zaonyeshaje kwamba Yesu ni mtu mwenye upendo sana na mwenye hisia za moyoni?

      14 Gospeli zaonyesha kwamba Yesu ni mtu mwenye upendo sana na hisia za moyoni. Alionyesha hisia nyingi tofauti-tofauti: kumhurumia mwenye ukoma (Marko 1:40, 41); kuhuzunikia watu wasioitikia (Luka 19:41, 42); kuwa na hasira yenye uadilifu juu ya wavunja-fedha (Yohana 2:13-17). Yesu alikuwa na hisia-mwenzi na hata angeweza kutoa machozi, na hakuficha hisia zake. Rafiki yake mpendwa Lazaro alipokufa, Yesu aliguswa moyo sana alipomwona Maria, dadake Lazaro, akilia hivi kwamba hata yeye alianza kulia, tena mbele ya watu wengine.—Yohana 11:32-36.

      15. Hisia za moyoni za Yesu zilikuwaje dhahiri katika njia aliyowaona watu na kuwatendea?

      15 Hisia za moyoni za Yesu zilidhihirika hasa katika njia aliyowaona na kuwatendea wengine. Aliwafikia maskini na wale walionyanyaswa, akiwasaidia ‘kupata burudisho kwa ajili ya nafsi zao.’ (Mathayo 11:4, 5, 28-30) Yeye hakuwa mwenye shughuli sana asishughulikie mahitaji ya wenye taabu, awe ni mwanamke mwenye kuvuja damu aliyegusa vazi lake kisiri au awe ni mwombaji kipofu ambaye hangeweza kunyamazishwa. (Mathayo 9:20-22; Marko 10:46-52) Yesu alitafuta sifa nzuri za wengine na kuwapongeza; lakini pia alikuwa tayari kukaripia ikihitajika. (Mathayo 16:23; Yohana 1:47; 8:44) Wakati huo ambapo wanawake hawakuwa na haki nyingi, Yesu aliwatendea kwa usawaziko wenye adhama na staha. (Yohana 4:9, 27) Inaeleweka kwamba kikundi cha wanawake kilikuwa tayari kumhudumia kwa mali zao wenyewe.—Luka 8:3.

      16. Ni nini kinachodhihirisha kwamba Yesu alikuwa na usawaziko juu ya maisha na vitu vya kimwili?

      16 Yesu alikuwa na usawaziko juu ya maisha. Vitu vya kimwili havikuwa muhimu sana kwake. Inaonekana hakuwa na vitu vingi vya kimwili. Alisema kwamba “hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Kwa wakati uo huo, Yesu aliwafanya watu wafurahi hata zaidi. Alipohudhuria sherehe ya arusi—tukio ambalo kwa kawaida huwa na muziki, kuimba, na kushangilia—ni wazi kwamba yeye hakuenda huko kuzima tukio hilo. Yesu hata alifanya muujiza wa kwanza huko. Divai ilipokwisha, aliyageuza maji kuwa divai bora, ambayo ‘humfurahisha mtu moyo wake.’ (Zaburi 104:15; Yohana 2:1-11) Sasa sherehe zingeendelea, na inaelekea kwamba bwana-arusi na bibi-arusi hawakuaibika. Usawaziko wake waonekana hata zaidi kwa sababu pindi nyingi sana zimetajwa ambapo Yesu alifanya huduma kwa bidii na kwa muda mrefu.—Yohana 4:34.

      17. Kwa nini si jambo lenye kushangaza kwamba Yesu alikuwa Mwalimu Stadi, na mafundisho yake yalionyesha nini?

      17 Yesu alikuwa Mwalimu Stadi. Mafundisho yake mengi yalionyesha uhalisi wa maisha ya kila siku, ambayo aliyafahamu sana. (Mathayo 13:33; Luka 15:8) Njia yake ya kufundisha haikuwa na kifani—ilikuwa wazi kabisa, rahisi, na yenye kutumika. Aliyofundisha ndiyo muhimu hata zaidi. Mafundisho yake yalionyesha tamaa yake ya moyoni ya kuwafahamisha wasikilizaji wake mawazo, hisia, na njia za Yehova.—Yohana 17:6-8.

      18, 19. (a) Yesu alitumia mifano gani dhahiri kumfafanua Baba yake? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala ifuatayo?

      18 Akitumia vielezi mara nyingi, Yesu alitujulisha Baba yake kwa kutumia mifano ambayo si rahisi kusahau. Kuongea kwa ujumla juu ya rehema ya Mungu ni tofauti kabisa na kumfananisha Yehova na baba mwenye kusamehe ambaye anaguswa moyo sana na mtoto wake anayerudi hivi kwamba ‘akimbia na kuangukia shingo yake na kumbusu kwa wororo.’ (Luka 15:11-24) Akikataa utamaduni mgumu ambamo viongozi wa kidini waliwadharau watu wa kawaida, Yesu alieleza kwamba Baba yake ni Mungu anayeweza kufikiwa kwa urahisi na ambaye anapendezwa zaidi na maombi ya mkusanya-kodi mnyenyekevu kuliko sala ya kujionyesha ya Farisayo mwenye majivuno. (Luka 18:9-14) Yesu alionyesha kwamba Yehova ni Mungu mwenye kujali ajuaye wakati shore mdogo aangukapo chini. “Msiwe na hofu,” Yesu akawafariji wanafunzi wake, “nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Mathayo 10:29, 31) Inaeleweka kwamba watu walishangaa kwa jinsi ambavyo Yesu ‘alifundisha’ wakavutiwa naye. (Mathayo 7:28, 29) Kwani, kwenye pindi moja “umati mkubwa” ulibaki naye kwa siku tatu, hata bila chakula!—Marko 8:1, 2.

      19 Tushukuru kwamba Yehova amefunua katika Neno lake akili ya Kristo! Lakini tunaweza kusitawishaje akili ya Kristo na kuidhihirisha katika shughuli zetu na wengine? Jambo hili litazungumziwa katika makala ifuatayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Jambo la kwamba viumbe wa roho wanaweza kuathiriwa na mashirika yao linaonyeshwa kwenye Ufunuo 12:3, 4. Shetani ameonyeshwa hapo kuwa “joka” ambaye aliweza kutumia uvutano wake kuwafanya “nyota” wengine, au wana wa roho, waasi pamoja naye.—Linganisha Ayubu 38:7.

      b Mara ya mwisho ambapo Yosefu anatajwa moja kwa moja ni wakati Yesu mwenye umri wa miaka 12 alipopatikana hekaluni. Yosefu hatajwi kuwapo kwenye sherehe ya arusi kule Kana, mwanzoni mwa huduma ya Yesu. (Yohana 2:1-3) Mwaka wa 33 W.K., Yesu aliyetundikwa mtini alimkabidhi Maria kwa mtume mpendwa Yohana ili amtunze. Yaelekea Yesu hangalifanya hivyo kama Yosefu angalikuwa bado hai.—Yohana 19:26, 27.

  • Je, Una “Akili ya Kristo”?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Februari 15
    • Je, Una “Akili ya Kristo”?

      “Mungu apaye uvumilivu na faraja na awaruhusu . . . mwe na mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu.”—WAROMA 15:5.

      1. Yesu aonyeshwaje katika michoro mingi ya Jumuiya ya Wakristo, na kwa nini hiyo si picha ifaayo ya Yesu?

      “HAJAWAHI kuonekana akicheka.” Hivyo ndivyo Yesu anavyosemwa katika hati moja inayodai kwa uwongo kuwa iliandikwa na ofisa mmoja wa kale wa Roma. Inasemekana kwamba hati hiyo, ambayo imejulikana kuwa imedumu ikiwa katika hali hiyo tangu karne ya 11, imeshawishi wachoraji wengi.a Katika michoro kadhaa, Yesu aonekana kama mtu mwenye huzuni ambaye hatabasamu hata kidogo. Lakini hiyo si picha ifaayo ya Yesu, ambaye anaonyeshwa katika Gospeli akiwa mtu mchangamfu, mwenye fadhili na hisia za ndani.

      2. Tunaweza kusitawishaje “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu,” na huo utatuandaa kufanya nini?

      2 Kwa wazi, ili tumjue Yesu halisi, ni lazima tujaze akili zetu na mioyo yetu ufahamu sahihi juu ya utu wa kweli wa Yesu alipokuwa hapa duniani. Basi ebu tuchunguze masimulizi fulani ya Gospeli yanayotusaidia kufahamu kindani “akili ya Kristo”—yaani hisia zake, maoni yake, mawazo yake, na kusababu kwake. (1 Wakorintho 2:16) Tufanyapo hivyo, ebu tufikirie jinsi tuwezavyo kusitawisha “mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu.” (Waroma 15:5) Kwa kufanya hivyo, tunaweza kujiandaa vizuri maishani na katika shughuli zetu na wengine kufuata kiolezo alichotuwekea.—Yohana 13:15.

      Rahisi Kufikiwa

      3, 4. (a) Simulizi lililoandikwa kwenye Marko 10:13-16 lilisimuliwa katika mazingira gani? (b) Yesu alifanya nini wanafunzi wake walipojaribu kuwakataza watoto wachanga wasimwendee?

      3 Yesu aliwavutia watu. Mara nyingi watu wenye umri na malezi tofauti-tofauti walikuwa huru kumfikia. Ebu fikiria tukio moja lililoandikwa kwenye Marko 10:13-16. Lilitukia mwishoni mwa huduma yake alipokuwa akielekea Yerusalemu kwa mara ya mwisho kukabili kifo chenye maumivu makali.—Marko 10:32-34.

      4 Ebu wazia mazingira hayo. Watu wanaanza kuwaleta watoto wao, hata vitoto vichanga, wabarikiwe na Yesu.b Hata hivyo, wanafunzi wanajaribu kuwakataza watoto wasimwendee Yesu. Labda wanafunzi wanafikiri kwamba kwa hakika Yesu hataki kusumbuliwa na watoto katika majuma haya muhimu. Kumbe wamekosea. Yesu atambuapo wanachofanya wanafunzi, hafurahi. Yesu anawaita watoto hao, akisema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwakomesha.” (Marko 10:14) Kisha anafanya jambo linaloonyesha utu wake ambao kwa kweli ni wenye upendo na huruma. Simulizi hilo linasema: “Akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.” (Marko 10:16) Kwa wazi watoto hao wamestarehe Yesu awachukuapo mikononi mwake kwa upendo.

      5. Simulizi la Marko 10:13-16 latuambia nini juu ya utu wa Yesu?

      5 Simulizi hilo fupi latuarifu mengi juu ya utu wa Yesu. Ona kwamba ilikuwa rahisi kumfikia. Ijapokuwa alikuwa na cheo cha juu sana mbinguni, yeye hakuwa mwenye vitisho wala hakushusha hadhi ya wanadamu wasiokamilika. (Yohana 17:5) Je, si jambo muhimu kwamba hata watoto walistarehe wakiwa naye? Hakika hawangeweza kuvutiwa na mtu asiye mchangamfu, asiye na furaha na ambaye hatabasamu wala kucheka kamwe! Watu wenye umri tofauti-tofauti walimfikia Yesu kwa sababu walitambua kwamba yeye ni mchangamfu, mwenye kujali, na walikuwa na hakika kwamba hangewafukuza kamwe.

      6. Wazee wanaweza kufanyaje ili wafikiwe kwa urahisi?

      6 Tukifikiria simulizi hilo, twaweza kujiuliza, ‘Je, nina akili ya Kristo? Je, ninafikiwa kwa urahisi?’ Katika nyakati hizi za hatari, kondoo za Mungu wanahitaji wachungaji ambao wanafikiwa kwa urahisi, watu ambao ni kama “mahali pa kujificha na upepo.” (Isaya 32:1, 2; 2 Timotheo 3:1) Wazee, mkipendezwa kikweli na kwa moyo na ndugu zenu na kuwa tayari kujitoa kwa niaba yao, wao watatambua kwamba mnawajali. Wataona mnawajali kupitia sura zenu, sauti zenu, na hali zenu zenye fadhili. Uchangamfu wa kweli kama huo na kujali zaweza kutokeza hali zenye utumainifu ambazo wengine, hata watoto, wanaona ikiwa rahisi kuwafikia. Mwanamke mmoja Mkristo ataja kilichomfanya ajieleze kwa mzee fulani: “Alinizungumzia kwa upole na kwa huruma. Kama hangalifanya hivyo, labda nisingalisema jambo lolote. Alinifanya nihisi salama.”

      Kuwajali Wengine

      7. (a) Yesu alionyeshaje kwamba aliwajali wengine? (b) Huenda ni kwa nini Yesu alimponya kipofu mmoja hatua kwa hatua?

      7 Yesu alikuwa mwenye kujali. Alifahamu hisia za wengine. Kuona tu watu wenye taabu kulimgusa moyo sana hivi kwamba alisukumwa kuwaondolea taabu yao. (Mathayo 14:14) Pia alitambua mipaka na mahitaji ya wengine. (Yohana 16:12) Pindi moja, watu walimletea kipofu na kumwomba Yesu amponye. Yesu alimponya macho, lakini akafanya hivyo hatua kwa hatua. Kwanza mtu huyo aliweza kuona tu maumbo—‘yaonekanayo kama miti inayotembea huku na huku.’ Kisha, Yesu akamponya macho kabisa. Kwa nini alimponya mtu huyo hatua kwa hatua? Huenda alifanya hivyo ili kumwezesha mtu huyo ambaye alikuwa amezoea sana giza aweze kustahimili mshtuko wa kuona kwa ghafula ulimwengu mwangavu wenye kutatanisha.—Marko 8:22-26.

      8, 9. (a) Ni nini kilichotendeka punde tu baada ya Yesu na wanafunzi wake kuingia katika eneo la Dekapolisi? (b) Fafanua jinsi Yesu alivyomponya mtu aliyekuwa kiziwi.

      8 Pia fikiria jambo lililotukia baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 32 W.K. Yesu na wanafunzi wake walikuwa wameingia katika eneo la Dekapolisi, mashariki mwa Bahari ya Galilaya. Punde si punde umati mkubwa wa watu wakawapata huko, wakamletea Yesu watu wengi waliokuwa wagonjwa na walemavu, akawaponya wote. (Mathayo 15:29, 30) Jambo la kutokeza ni kwamba Yesu alimchukua mtu mmoja kwenye umati ili amwonyeshe kwamba anajali kwelikweli. Mwandikaji wa Gospeli, Marko, ambaye ndiye mwandikaji pekee aliyeandika tukio hili, aripoti yaliyotukia.—Marko 7:31-35.

      9 Mtu huyo alikuwa kiziwi na alikuwa na tatizo kubwa la kuongea. Huenda Yesu alitambua wasiwasi au aibu ya mtu huyo. Kisha Yesu akafanya jambo lisilo la kawaida. Alimwondoa mtu huyo kwenye umati, akampeleka faraghani. Kisha Yesu akatumia ishara fulani kumwambia mtu huyo jambo alilokusudia kufanya. “Akaweka vidole vyake ndani ya masikio ya yule mtu na, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi wake.” (Marko 7:33) Kisha, Yesu akatazama mbingu na kutweta kwa njia ya sala. Matendo hayo dhahiri yangemwonyesha mtu huyo, ‘Kile ninachotaka kukufanyia chatokana na nguvu ya Mungu.’ Hatimaye Yesu akasema: “Funguka.” (Marko 7:34) Basi, mtu huyo akaweza kusikia tena, akaweza kuzungumza kama kawaida.

      10, 11. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunajali hisia za wengine katika kutaniko? katika familia?

      10 Yesu aliwajali wengine kama nini! Alifahamu hisia zao, na hisia-mwenzi hiyo ikamfanya atende kwa njia yenye kujali hisia zao. Tukiwa Wakristo, ni vizuri tusitawishe na kuonyesha akili ya Kristo kuhusu jambo hili. Biblia inatuhimiza hivi: “Nyinyi nyote mwe wenye akili zenye kufanana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na shauku ya kidugu, wenye huruma kwa njia ya wororo, wanyenyekevu katika akili.” (1 Petro 3:8) Kwa hakika, hilo lamaanisha tuseme na kutenda katika njia ambazo zinajali hisia za wengine.

      11 Kutanikoni, tunaweza kujali hisia za wengine kwa kuwapa adhama, kuwatendea kama vile sisi tungependa kutendewa. (Mathayo 7:12) Hilo lamaanisha kwamba tuwe waangalifu kuhusu yale tusemayo na jinsi tuyasemavyo. (Wakolosai 4:6) Kumbuka kwamba ‘maneno yanenwayo bila kufikiri yanaweza kuchoma kama upanga.’ (Mithali 12:18) Namna gani katika familia? Mume na mke ambao wanapendana kikweli hujali hisia za kila mmoja. (Waefeso 5:33) Wao huepuka maneno makali, uchambuzi wa daima, na kejeli yenye kuumiza—na yote haya yanaweza kuumiza hisia na iwe vigumu kusuluhishwa. Watoto pia wana hisia, na wazazi wenye upendo huzifikiria pia. Rekebisho likihitajiwa, wazazi kama hao hulitoa kwa njia inayozingatia hadhi ya watoto wao na kutowafanya waaibike isivyofaa.c (Wakolosai 3:21) Basi, tukiwajali wengine, twadhihirisha kwamba tuna akili ya Kristo.

      Kuwa Tayari Kuwaitibari Wengine

      12. Yesu alikuwa na maoni gani halisi na yenye usawaziko juu ya wanafunzi wake?

      12 Yesu aliwaona wanafunzi wake kwa njia halisi na yenye usawaziko. Alijua vizuri kwamba hawakuwa wakamilifu. Kwani hata angeweza kusoma mioyo ya wanadamu. (Yohana 2:24, 25) Hata hivyo, yeye hakuona tu kutokamilika kwao bali aliona sifa zao nzuri. Pia aliona mambo ambayo watu hao waliokuwa wamevutwa na Yehova wangeweza kutimiza. (Yohana 6:44) Maoni mazuri ya Yesu juu ya wanafunzi wake yalikuwa dhahiri kwa jinsi alivyowashughulikia na kuwatendea. Jambo moja alilofanya ni kuwa tayari kuwaitibari.

      13. Yesu alionyeshaje kwamba aliwaitibari wanafunzi wake?

      13 Yesu alionyeshaje itibari hiyo? Alipoondoka duniani, aliwapa wanafunzi wake watiwa-mafuta daraka zito. Aliwapa daraka la kutunza masilahi ya duniani pote ya Ufalme wake. (Mathayo 25:14, 15; Luka 12:42-44) Wakati wa huduma yake, alionyesha hata katika mambo madogo-madogo na kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwamba aliwaitibari. Alipoongeza kiasi cha chakula kimuujiza ili kuulisha umati, aliwapa wanafunzi wake daraka la kugawa chakula.—Mathayo 14:15-21; 15:32-37.

      14. Ungesimuliaje kwa ufupi simulizi lililoandikwa kwenye Marko 4:35-41?

      14 Fikiria pia simulizi lililoandikwa kwenye Marko 4:35-41. Pindi hii Yesu na wanafunzi wake walipanda mashua na kusafiri kuelekea mashariki wakivuka Bahari ya Galilaya. Muda mfupi baada ya kuondoka, Yesu alijilaza kwenye tezi akalala fofofo. Lakini, punde tu “kukatokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi.” Dhoruba kama hizo zilikuwa za kawaida katika Bahari ya Galilaya. Kwa kuwa bahari hiyo iko chini sana (meta 200 hivi chini ya usawa wa bahari), hewa ya hapo ni joto sana kuliko hewa ya eneo lililo karibu, na hali hiyo hutokeza msukusuko wa hewa. Isitoshe, pepo zenye nguvu huteremka kwa kasi kwenye Bonde la Yordani kutoka Mlima Hermoni, ulioko upande wa kaskazini. Bahari shwari yaweza kugeuka kwa ghafula kuwa dhoruba kali. Ebu fikiria: Bila shaka Yesu alijua kwamba kuna dhoruba nyingi kwa kuwa alilelewa Galilaya. Lakini, yeye alilala kwa utulivu, akiitibari ustadi wa wanafunzi wake, ambao baadhi yao walikuwa wavuvi.—Mathayo 4:18, 19.

      15. Tunaweza kuigaje utayari wa Yesu wa kuitibari wanafunzi wake?

      15 Je, tunaweza kuiga utayari wa Yesu wa kuitibari wanafunzi wake? Ni vigumu kwa watu fulani kuwapa wengine madaraka. Ni kana kwamba sikuzote wao tu ndio lazima wafanye mambo hayo. Huenda wakafikiri hivi, ‘Nikitaka jambo lifanywe vizuri, ni lazima nilifanye mwenyewe!’ Lakini kama ni lazima tufanye kila kitu sisi wenyewe, kuna hatari ya kuchoka na labda kutumia isivyo lazima wakati ambao tungetumia na familia zetu. Isitoshe, tusipowapa wengine kazi na madaraka yafaayo, huenda tukawa tunawanyima uzoefu na mazoezi wanayohitaji. Ni vizuri kujifunza kuwaitibari wengine tukiwapa mambo fulani wafanye. Ni vizuri tujiulize hivi kwa unyofu, ‘Je, nina akili ya Kristo kuhusu jambo hili? Je, nawapa wengine kazi fulani-fulani, nikiitibari kwamba watafanya kadiri wawezavyo?’

      Alionyesha Kwamba Anawaamini Wanafunzi Wake

      16, 17. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwapa mitume wake uhakikishio gani, hata ingawa alijua kwamba wangemwacha?

      16 Yesu alikuwa na maoni mazuri juu ya wanafunzi wake katika njia nyingine muhimu. Aliwaonyesha kwamba ana uhakika nao. Jambo hilo lilikuwa dhahiri kabisa katika maneno yenye uhakikisho aliyowaambia mitume wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani. Ona jambo lililotukia.

      17 Yesu alikuwa na mambo mengi jioni hiyo. Aliwafunza wanafunzi wake somo la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Baadaye, akaanzisha mlo wa jioni ambao ungekuwa ukumbusho wa kifo chake. Kisha, mitume wakaanza kubishana tena vikali juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu. Akiwa na subira kama kawaida yake, Yesu hakuwakemea bali alisababu nao. Aliwaambia mambo yatakayotokea: “Nyinyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku huu, kwa maana imeandikwa, ‘Hakika nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanywa huku na huku.’” (Mathayo 26:31; Zekaria 13:7) Alijua kwamba waandamani wake wa karibu zaidi wangemwacha pindi hiyo yenye uhitaji. Lakini hata hakuwashutumu. Badala yake, aliwaambia hivi: “Lakini baada ya mimi kuwa nimefufuliwa hakika nitawatangulia kuingia katika Galilaya.” (Mathayo 26:32) Ndiyo, aliwahakikishia kwamba ingawa wangemwacha, yeye hangewaacha. Wakati ambapo masaibu hayo makali yangepita, angekutana nao tena.

      18. Huko Galilaya, Yesu aliwakabidhi wanafunzi wake utume gani mzito, na mitume walitimizaje utume huo?

      18 Yesu alitimiza maneno yake. Baadaye, katika Galilaya, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea mitume 11 waaminifu, ambao inaonekana walikusanyika pamoja na wengine wengi. (Mathayo 28:16, 17; 1 Wakorintho 15:6) Huko, Yesu aliwapa utume mzito: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kitabu cha Matendo chatupa uthibitisho wa wazi kwamba mitume walitii utume huo. Kwa uaminifu waliongoza kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza.—Matendo 2:41, 42; 4:33; 5:27-32.

      19. Matendo ya Yesu baada ya kufufuliwa yatufundisha nini kuhusu akili ya Kristo?

      19 Simulizi hilo lenye kufunua mambo linatufundisha nini kuhusu akili ya Kristo? Yesu alijua sifa mbaya za mitume wake, lakini “aliwapenda hadi mwisho.” (Yohana 13:1) Japo kasoro zao, aliwaonyesha kwamba aliwaamini. Ona kwamba Yesu hakukosea kuwaonyesha kwamba ana uhakika nao. Inaelekea kwamba uhakika na imani aliyokuwa ameonyesha kwao iliwaimarisha waazimie moyoni kutekeleza kazi ambayo alikuwa amewaamuru wafanye.

      20, 21. Tunaweza kuonyeshaje maoni mazuri juu ya waamini wenzetu?

      20 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna akili ya Kristo kuhusu jambo hili? Usiwe na maoni mabaya juu ya waamini wenzako. Ukifikiria tu mabaya, inaelekea maneno yako na matendo yako yatayafunua. (Luka 6:45) Hata hivyo, Biblia yatuambia kwamba upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Upendo hufikiria mema, wala si mabaya. Hujenga badala ya kubomoa. Watu huitikia kwa urahisi zaidi wakionyeshwa upendo na kutiwa moyo kuliko wanapotishwa. Tunaweza kuwajenga wengine na kuwatia moyo kwa kuonyesha kwamba tuna uhakika nao. (1 Wathesalonike 5:11) Ikiwa, kama Kristo, tuna maoni mazuri juu ya ndugu zetu, tutawatendea katika njia ambazo zinawajenga na kufanya watokeze sifa zao bora.

      21 Kusitawisha akili ya Kristo na kuidhihirisha kunatia ndani mengi zaidi kuliko kuiga tu mambo ambayo Yesu alifanya. Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, ikiwa kwa kweli tunataka kutenda kama Yesu, ni lazima kwanza tujifunze kuona mambo kama alivyoyaona. Gospeli hutusaidia kuona upande mwingine wa utu wake, mawazo yake na hisia zake juu ya kazi aliyopewa afanye, kama makala ifuatayo itakavyozungumzia.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika hati hiyo, mtu huyo mdanganyifu anataja ile isemekanayo kuwa eti sura ya Yesu, kutia ndani rangi ya nywele zake, ndevu, na macho. Mtafsiri mmoja wa Biblia Edgar J. Goodspeed aeleza kwamba udanganyifu huo “ulitayarishwa ili kuunga mkono ufafanuzi unaopatikana katika vitabu vya wachoraji kuhusu sura ya Yesu.”

      b Inaonekana kwamba watoto hao wana umri tofauti-tofauti. Neno lililotafsiriwa hapa “watoto wachanga” pia limetumiwa kumtaja binti Yairo mwenye umri wa miaka 12. (Marko 5:39, 42; 10:13) Hata hivyo, katika simulizi linalofanana na hilo, Luka atumia neno ambalo laweza kumaanisha pia vitoto vichanga.—Luka 1:41; 2:12; 18:15.

      c Ona makala “Je, Wewe Wastahi Adhama Yao?” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1998.

  • Je, Unasukumwa Kutenda Kama Yesu?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Februari 15
    • Je, Unasukumwa Kutenda Kama Yesu?

      “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha.”—MARKO 6:34.

      1. Kwa nini inaeleweka kwamba watu fulani huonyesha sifa nzuri?

      KATIKA historia watu wengi wameonyesha sifa nzuri. Na hiyo inaeleweka. Yehova Mungu ana upendo, fadhili, ukarimu na sifa nyinginezo tunazothamini naye huzionyesha. Wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu. Basi tunaweza kuelewa ni kwa nini watu wengi huonyesha kadiri fulani ya upendo, fadhili, huruma, na sifa nyinginezo za Mungu, na hata wengi huonyesha wana dhamiri. (Mwanzo 1:26; Waroma 2:14, 15) Lakini huenda unajua kwamba watu wengine huonyesha sifa hizi kwa urahisi kuliko wengine.

      2. Ni zipi kazi nzuri ambazo huenda watu wakafanya, labda wakifikiri kwamba wanamwiga Kristo?

      2 Labda unawafahamu wanaume na wanawake ambao mara nyingi huwazuru wagonjwa au kuwasaidia, huwaonyesha huruma walemavu, au kuwasaidia maskini kwa ukarimu. Pia, fikiria watu ambao huruma zao huwasukuma watoe maisha zao kufanya kazi katika makao ya kuwatunzia wagonjwa wa ukoma au katika makao ya kuwatunzia mayatima, wale wanaojitolea kufanya kazi katika hospitali au katika makao ya kutunzia watu wenye magonjwa yenye kufisha, au wale wanaojitahidi kuwasaidia watu wasio na makao au kuwasaidia wakimbizi. Yaelekea kwamba baadhi yao hufikiri wanamwiga Yesu ambaye aliwawekea Wakristo kielelezo cha kufuata. Twasoma katika Gospeli kwamba Kristo aliponya wagonjwa na kulisha wenye njaa. (Marko 1:34; 8:1-9; Luka 4:40) Upendo, wororo, na huruma za Yesu ni udhihirisho wa “akili ya Kristo,” ambaye naye alikuwa akimwiga Baba yake wa mbinguni.—1 Wakorintho 2:16.

      3. Twahitaji kufikiria nini ili tuwe na maoni yenye usawaziko juu ya kazi nzuri za Yesu?

      3 Lakini, je, umeona kwamba leo wengi ambao wamevutiwa na upendo na huruma za Yesu husahau sehemu kuu ya akili ya Kristo? Twaweza kufahamu kindani jambo hili kwa kuchunguza kwa makini Marko sura ya 6. Twasoma hapo kwamba watu walimletea Yesu wagonjwa ili awaponye. Katika muktadha huo, twajifunza pia kwamba alipoona maelfu ya watu waliokuwa wamemjia wakiwa na njaa, Yesu aliwalisha kimuujiza. (Marko 6:35-44, 54-56) Kuwaponya wagonjwa na kuwalisha wenye njaa kulionyesha kwa njia yenye kutokeza huruma yenye upendo, lakini je, hizo ndizo njia kuu ambazo Yesu aliwasaidia watu? Tunaweza kuigaje kwa njia bora kielelezo chake kikamilifu cha upendo, fadhili, na huruma, kama yeye naye alivyomwiga Yehova?

      Asukumwa Kushughulikia Mahitaji ya Kiroho

      4. Simulizi la Marko 6:30-34 lilisimuliwa katika mazingira gani?

      4 Yesu aliwasikitikia wale aliokuwa nao hasa kwa sababu ya mahitaji yao ya kiroho. Mahitaji hayo yalikuwa muhimu sana kuliko hata mahitaji ya kimwili. Ebu fikiria simulizi la Marko 6:30-34. Tukio lililotajwa katika simulizi hilo lilitukia kwenye ukingo wa Bahari ya Galilaya, karibu na wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 32 W.K. Na mitume walikuwa na sababu nzuri za kusisimka. Kwa kuwa walikuwa wamemaliza tu ziara kubwa, walimjia Yesu, yaonekana wakiwa na hamu ya kumwambia mambo yaliyoonwa. Lakini umati ukakusanyika. Umati ukawa mkubwa sana hivi kwamba Yesu na mitume wake hawangeweza kula wala kupumzika. Yesu akawaambia mitume: “Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.” (Marko 6:31) Wakipanda mashua, labda karibu na Kapernaumu, wao walisafiri kuvuka Bahari ya Galilaya kuelekea mahali patulivu. Lakini umati ukakimbia kandokando ya bahari na kufika mbele ya mashua. Sasa Yesu angefanya nini? Je, alikasirika kwamba anasumbuliwa? La hasha!

      5. Yesu alihisije juu ya umati mkubwa uliomjia, naye alifanya nini?

      5 Yesu aliguswa moyo alipouona umati wa maelfu ya watu, hata na wagonjwa, wakimngoja kwa hamu. (Mathayo 14:14; Marko 6:44) Akizingatia jambo lililotokeza huruma za Yesu na jinsi alivyotenda, Marko aliandika: “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Yesu hakuona tu umati wa watu. Aliona watu wenye mahitaji ya kiroho. Walikuwa kama kondoo wanaopotea, bila mchungaji wa kuwaongoza kwenye nyasi nzuri au kuwalinda. Yesu alijua kwamba viongozi wa kidini wasio na huruma, ambao walipaswa kuwa wachungaji wenye kujali, kwa kweli waliwadharau watu wa kawaida na kupuuza mahitaji yao ya kiroho. (Ezekieli 34:2-4; Yohana 7:47-49) Yesu alitaka kuwatendea kwa njia tofauti, akiwafanyia mema zaidi kwa kadiri alivyoweza. Akaanza kuwafundisha juu ya Ufalme wa Mungu.

      6, 7. (a) Gospeli zaonyesha ni mambo yapi yaliyotangulizwa wakati Yesu aliposhughulikia mahitaji ya watu? (b) Yesu alichochewa na nini kuhubiri na kufundisha?

      6 Ona jinsi mambo yalivyofuatana na jambo linalodokezwa katika mambo yaliyotangulizwa kama inavyoonekana katika simulizi linalolingana na hilo. Simulizi hili liliandikwa na Luka, ambaye alikuwa tabibu aliyependezwa sana na hali njema ya wengine. “Umati . . . ukamfuata [Yesu]. Naye akawapokea kwa fadhili na kuanza kuwaambia juu ya ufalme wa Mungu, naye akawaponya wale wenye kuhitaji ponyo.” (Luka 9:11; Wakolosai 4:14) Japo sivyo ilivyo na kila simulizi la muujiza, katika hali hii simulizi la Luka lililopuliziwa lilitaja nini kwanza? Kwamba Yesu aliwafundisha watu.

      7 Hilo lakubaliana na mkazo tunaopata katika Marko 6:34. Mstari huo waonyesha wazi jinsi Yesu alivyosukumwa hasa kuwasikitikia watu. Aliwafundisha watu, akitosheleza mahitaji yao ya kiroho. Mapema katika huduma yake, Yesu alisema: “Kwenye majiji mengine ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu kwa ajili ya hili nilitumwa.” (Luka 4:43) Lakini, ni kosa kufikiri kwamba Yesu alitangaza ujumbe wa Ufalme ili atimize tu wajibu, kana kwamba alihubiri kwa sababu tu ilikuwa lazima. La, kichocheo kikuu kilichofanya awahubirie watu habari njema ni huruma yake yenye upendo kwao. Jambo bora zaidi ambalo Yesu angeweza kufanya—hata kwa wagonjwa, wenye kupagawa na roho waovu, maskini, au wenye njaa—lilikuwa kuwasaidia kujua, kukubali, na kupenda kweli juu ya Ufalme wa Mungu. Kweli hiyo ilikuwa muhimu sana kwa sababu ya daraka ambalo Ufalme unatimiza katika kutetea enzi kuu ya Yehova na kuwabariki wanadamu daima.

      8. Yesu alionaje kazi yake ya kuhubiri na kufundisha?

      8 Sababu kuu iliyomfanya Yesu aje duniani ni kuhubiri kwa bidii juu ya Ufalme. Huduma yake duniani ilipokaribia mwisho, Yesu alimwambia Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli. Kila mtu aliye upande wa ile kweli husikiliza sauti yangu.” (Yohana 18:37) Tumeona katika makala mbili zilizotangulia kwamba Yesu alikuwa mtu mwenye hisia nyororo—mwenye kujali, rahisi kufikiwa, mwenye kufikiria hali za wengine, mwenye kuitibari, na zaidi ya yote, mwenye upendo. Tunapaswa kufahamu sifa hizo za utu wake ikiwa kwa kweli tunataka kuelewa akili ya Kristo. Ni muhimu vilevile kutambua kwamba akili ya Kristo yatia ndani jinsi alivyotanguliza kazi yake ya kuhubiri na kufundisha mbele ya mambo mengine.

      Aliwahimiza Wengine Watoe Ushahidi

      9. Ni nani waliopaswa kutanguliza kuhubiri na kufundisha?

      9 Si Yesu tu aliyepaswa kutanguliza kuhubiri na kufundisha ambako ni wonyesho wa upendo na huruma. Aliwahimiza wafuasi wake waige mambo yaliyomchochea, mambo aliyoyatanguliza, na matendo yake. Kwa mfano, baada ya Yesu kuteua mitume wake 12, wao walipaswa kufanya nini? Marko 3:14, 15 latuambia: “Akafanyiza kikundi cha kumi na wawili, ambao pia aliwaita jina ‘mitume,’ ili wapate kuendelea kuwa pamoja naye na kwamba apate kuwatuma wahubiri na kuwa na mamlaka ya kuwafukuza roho waovu.” Je, unaona jambo ambalo mitume walipaswa kutanguliza?

      10, 11. (a) Yesu alipowatuma mitume, aliwaambia wafanye nini? (b) Kuhusu kuwatuma mitume, ni jambo jipi lililotiliwa mkazo?

      10 Baadaye, Yesu aliwawezesha wale 12 kuponya wengine na kuwafukuza roho waovu. (Mathayo 10:1; Luka 9:1) Kisha akawatuma kuwaendea “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Wakafanye nini? Yesu aliwaagiza: “Mwendapo, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbingu umekaribia.’ Ponyeni wagonjwa, fufueni wafu, fanyeni wenye ukoma wawe safi, fukuzeni roho waovu.” (Mathayo 10:5-8; Luka 9:2) Nao walifanya nini? “Kwa hiyo wakaondoka na [1] kuhubiri ili watu wapate kutubu; nao [2] walikuwa wakitoa roho waovu wengi na kupaka mafuta watu wengi wagonjwa-wagonjwa na kuwaponya.”—Marko 6:12, 13.

      11 Kwa kuwa kufundisha hakutajwi mwanzoni katika kila hali, je, kuona mambo hayo kwa jinsi yanavyofuatana si kuzingatia mno mambo yanayotangulizwa au vichocheo vinavyohusika? (Luka 10:1-9) Hatupaswi kupuuza mara ambazo kufundisha kumetangulizwa mbele ya kuponya. Ebu ona muktadha huo. Kabla tu ya kuwatuma mitume 12, Yesu alikuwa ameguswa moyo na hali ya umati. Twasoma hivi: “Yesu akaondoka ili kutalii majiji na vijiji vyote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu. Alipouona umati alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo akawaambia wanafunzi wake: ‘Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.’”—Mathayo 9:35-38.

      12. Kazi za kimuujiza za Yesu na mitume zingeweza kutimiza kusudi gani jingine?

      12 Kwa sababu walikuwa pamoja na Yesu, mitume wangeweza kusitawisha sehemu ya akili ya Kristo. Wao walitambua kwamba kuwaonyesha watu upendo na huruma kikweli kunahusisha kuhubiri na kufundisha juu ya Ufalme—hilo ndilo lingekuwa jambo kuu la kazi zao njema. Kwa kupatana na jambo hilo, matendo mema ya kimwili, kama vile kuponya wagonjwa, yalitimiza mengi kuliko tu kuwasaidia wenye uhitaji. Kama ujuavyo, watu wengine wanaweza kuvutiwa na maponyo na chakula kinachoandaliwa kimuujiza. (Mathayo 4:24, 25; 8:16; 9:32, 33; 14:35, 36; Yohana 6:26) Lakini, zaidi ya kusaidia tu kimwili, kazi hizo hasa ziliwafanya watazamaji watambue kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu na “nabii” ambaye Musa alitabiri.—Yohana 6:14; Kumbukumbu la Torati 18:15.

      13. Unabii unaopatikana katika Kumbukumbu la Torati 18:18 wakazia daraka gani la “nabii” ajaye?

      13 Kwa nini ni jambo la maana kwamba Yesu alikuwa “nabii”? Ilitabiriwa kwamba angefanya jambo gani kuu? Je, “nabii” huyo angekuwa mashuhuri kwa kuponya watu kimuujiza au kuwaandalia wenye njaa chakula kwa huruma? Kumbukumbu la Torati 18:18 lilitabiri: “Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe [Musa], nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.” Vivyo hivyo, mitume walipojifunza kuwa na hisia nyororo na kuionyesha, wao wangeweza kukata kauli ya kwamba akili ya Kristo ilipaswa kuwa dhahiri pia katika utendaji wao wa kuhubiri na kufundisha. Hilo ndilo jambo bora zaidi ambalo wangeweza kuwafanyia watu. Kupitia njia hiyo, wagonjwa na maskini wangeweza kupata manufaa za kudumu, wala si manufaa zinazotusaidia tu katika maisha yetu mafupi au za muda mfupi.—Yohana 6:26-30.

      Sitawisha Akili ya Kristo Leo

      14. Kuwa na akili ya Kristo kwahusikaje na kuhubiri kwetu?

      14 Hatupaswi kuona akili ya Kristo kuwa jambo linalohusu karne ya kwanza tu—ikiwahusu Yesu na wanafunzi wa mapema ambao mtume Paulo aliwaandikia hivi: “Sisi tunayo akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Na tunakubali mara moja kwamba sisi tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Lakini, ni jambo linalofaa kufikiria mambo yanayotuchochea kufanya kazi hiyo. Haitupasi kuifanya kwa sababu ya kutimiza tu wajibu wetu. Kumpenda Mungu ni sababu ya msingi inayofanya tushiriki katika huduma, na kuwa kama Yesu kwa kweli kwatia ndani kusukumwa na huruma ili tuhubiri na kufundisha.—Mathayo 22:37-39.

      15. Kwa nini huruma ni sehemu ifaayo ya huduma yetu ya peupe?

      15 Ni kweli kwamba si rahisi nyakati zote kuwaonea huruma wale ambao hawana imani kama yetu, hasa tunapopata watu ambao hawapendezwi, watu wanapotukataa, au tunapopata upinzani. Lakini, tukikosa kuwapenda watu na kuwaonea huruma, tunaweza kupoteza kichocheo muhimu cha kushiriki katika huduma ya Kikristo. Basi tunaweza kusitawishaje huruma? Kwa kujaribu kuwaona watu kama Yesu alivyowaona, ‘wakiwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Je, wengi hawako hivyo leo? Wachungaji wa kidini wasio wa kweli wamewapuuza na kuwapofusha kiroho. Matokeo yakawa kwamba hawana mwongozo mzuri unaopatikana katika Biblia wala hawafahamu hali za Paradiso ambazo Ufalme wa Mungu utaleta duniani. Wanakabili matatizo ya maisha ya kila siku—kama vile umaskini, mzozo wa familia, ugonjwa, na kifo—bila kuwa na tumaini la Ufalme. Tuna mambo wanayohitaji: habari njema yenye kuokoa uhai ya Ufalme wa Mungu, ambao sasa umesimamishwa mbinguni!

      16. Kwa nini inafaa tuwaeleze wengine habari njema?

      16 Basi unapotafakari mahitaji ya kiroho ya wale walio karibu nawe, je, moyo wako haukusukumi utake kufanya yote uwezayo kuwaambia juu ya kusudi la Mungu lenye upendo? Ndiyo, kazi yetu ni yenye huruma. Tunapokuwa na hisia mwenzi kwa watu kama alivyofanya Yesu, jambo hilo litadhihirika katika sauti zetu, nyuso zetu, na njia yetu ya kufundisha. Yote hayo yatafanya ujumbe wetu uvutie zaidi wale ambao ‘wana mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’—Matendo 13:48.

      17. (a) Ni zipi baadhi ya njia ambazo tunaweza kuwaonyesha wengine upendo na huruma? (b) Kwa nini si suala la ama kufanya matendo mema ama kushiriki katika huduma ya peupe?

      17 Bila shaka, upendo wetu na huruma yetu zapaswa kudhihirika katika maisha yetu yote. Hiyo inatia ndani kuwa wenye fadhili kwa watu wasio na uwezo, wagonjwa, na maskini—tukifanya yote tuwezayo ili kuondoa taabu zao. Inatia ndani jitihada zetu katika maneno na katika matendo za kuwaondolea huzuni watu ambao wamefiwa na wapendwa wao. (Luka 7:11-15; Yohana 11:33-35) Lakini, kuonyesha upendo, fadhili, na huruma hakupaswi kuwa ndilo jambo kuu zaidi maishani, kama ilivyo na baadhi ya watu wenye kutoa msaada wa kibinadamu. Jitihada zinazochochewa na sifa za Mungu kama hizo ambazo zinadhihirika tunaposhiriki katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri na kufundisha ndizo zenye umuhimu wenye kudumu hata zaidi. Kumbuka jambo alilosema Yesu kuhusu viongozi wa kidini wa Kiyahudi: “Nyinyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na jira, lakini mmepuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu. Ilikuwa lazima mambo haya kuyafanya, na bado kutopuuza yale mambo mengine.” (Mathayo 23:23) Yesu hakuchagua kufanya jambo moja na kuacha jingine—ama kuwasaidia watu kwa mahitaji yao ya kimwili ama kuwafundisha mambo ya kiroho yenye kuleta uhai. Yesu aliyafanya yote. Lakini, ni wazi kwamba kazi yake ya kufundisha ilikuwa ndiyo jambo kuu kwa sababu mema aliyotimiza yangeweza kuwa yenye manufaa milele.—Yohana 20:16.

      18. Kuzungumzia akili ya Kristo kwapasa kutusukuma kufanya nini?

      18 Tunashukuru kama nini kwamba Yehova ametufunulia akili ya Kristo! Kupitia Gospeli, tunaweza kujua vizuri zaidi mawazo, hisia, sifa, utendaji, na mambo ambayo mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani alitanguliza. Ni juu yetu kusoma, kutafakari, na kutenda yale ambayo Biblia inafunua juu ya Yesu. Kumbuka kwamba ikiwa kwa kweli tunataka kutenda kama Yesu, ni lazima kwanza tujifunze kufikiri, kuhisi, na kuchanganua mambo kama alivyofanya kwa kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. Basi, na tuazimie kuisitawisha akili ya Kristo na kuidhihirisha. Hii ndiyo njia bora ya kuishi, kushughulika na watu, na pia ndiyo njia bora kabisa kwetu na kwa wengine kumkaribia yule ambaye Yesu alimwiga kikamilifu, Mungu wetu mwenye wororo, Yehova.—2 Wakorintho 1:3; Waebrania 1:3.

  • Je, Unasukumwa Kutenda Kama Yesu?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Februari 15
    • [Picha katika ukurasa wa 23]

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki