-
Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?Mnara wa Mlinzi—2003 | Mei 1
-
-
Faraja ya Kweli Inaweza Kupatikana Wapi?
“Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo . . . hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 WAKORINTHO 1:3, 4.
1. Ni hali zipi zinazoweza kuwafanya watu wahisi kwamba wanahitaji sana faraja?
UGONJWA wenye kudhoofisha unaweza kumfanya mtu ahisi kwamba maisha yake yameharibika. Matetemeko ya ardhi, dhoruba, na njaa huwaacha watu katika hali ya ufukara. Huenda vita vikasababisha vifo vya washiriki wa familia, vikaharibu nyumba, au kufanya watu waache nyumba na mali zao. Ukosefu wa haki unaweza kuwafanya watu wahisi kwamba hakuna mahali pa kupata kitulizo. Wale wanaopatwa na taabu hizo, wanahitaji sana faraja. Inaweza kupatikana wapi?
2. Kwa nini faraja inayotolewa na Yehova haina kifani?
2 Watu na mashirika fulani hujitahidi kutoa faraja. Maneno yenye fadhili yanathaminiwa. Misaada inayotolewa hutimiza mahitaji kwa muda mfupi. Lakini Yehova pekee, Mungu wa kweli, ndiye anayeweza kuondoa madhara yote na kutoa msaada unaohitajiwa ili misiba kama hiyo isitokee tena. Biblia inasema hivi kumhusu: “Mbarikiwa na awe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo kwayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Yehova hutufariji jinsi gani?
Kuondoa Mambo Yanayosababisha Matatizo
3. Faraja ambayo Mungu hutoa inaonyeshaje mambo yanayosababisha matatizo ya wanadamu?
3 Kwa sababu ya dhambi ya Adamu, wanadamu wote wamerithi hali ya kutokamilika na hiyo husababisha matatizo mengi ambayo hatimaye huleta kifo. (Waroma 5:12) Hali hiyo inakuwa mbaya zaidi kwa sababu Shetani Ibilisi ndiye “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Yehova hakusikitishwa tu na hali mbaya inayowakabili wanadamu. Alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuwa fidia ili atoe ukombozi, naye alituambia kwamba tunaweza kusamehewa dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu iwapo tutadhihirisha imani katika Mwana Wake. (Yohana 3:16; 1 Yohana 4:10) Mungu pia alitabiri kwamba Yesu Kristo, ambaye amepewa mamlaka yote mbinguni na duniani, atamharibu Shetani na ulimwengu wake wote mwovu.—Mathayo 28:18; 1 Yohana 3:8; Ufunuo 6:2; 20:10.
4. (a) Yehova ameandaa nini ili kuimarisha tumaini letu katika ahadi zake za kutukomboa? (b) Yehova anatusaidiaje kujua wakati atakapotukomboa?
4 Ili kuimarisha tumaini letu katika ahadi zake, Mungu ameandikisha uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba yote anayotabiri hutimia. (Yoshua 23:14) Katika simulizi la Biblia alitia ndani mambo ambayo amefanya ili kuwakomboa watumishi wake kutoka katika hali ambazo kwa maoni ya wanadamu haingewezekana kuwakomboa. (Kutoka 14:4-31; 2 Wafalme 18:13–19:37) Kupitia kwa Yesu Kristo, Yehova alionyesha kwamba kusudi lake linatia ndani kuwaponya watu “kila namna ya maradhi,” hata kuwafufua wafu. (Mathayo 9:35; 11:3-6) Mambo hayo yote yatatimizwa lini? Biblia inajibu kwa kueleza kuhusu siku za mwisho za ulimwengu huu wa kale zitakazofuatwa na mbingu mpya na dunia mpya ya Mungu. Yale ambayo Yesu alitabiri kuhusu siku hizo yanatimia wakati huu wetu.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5.
Faraja kwa Watu Wanaoteseka
5. Alipowafariji Waisraeli wa kale, Yehova alitaka wafikirie mambo gani?
5 Tunajifunza jinsi Yehova alivyowafariji Waisraeli wa kale kutokana na namna alivyoshughulika nao. Aliwakumbusha sifa zake. Hilo liliimarisha tumaini lao katika ahadi zake. Yehova aliwafanya manabii wake waonyeshe waziwazi tofauti iliyopo kati yake akiwa Mungu wa kweli aliye hai, na sanamu, zisizoweza kujisaidia wala kuwasaidia waabudu wake. (Isaya 41:10; 46:1; Yeremia 10:2-15) Yehova alipomwambia Isaya, ‘Wafariji, wafariji watu wangu,’ alimhimiza nabii wake atumie mifano na ufafanuzi mbalimbali kuhusu uumbaji Wake ili kukazia ukuu wa Yehova aliye Mungu wa pekee wa kweli.—Isaya 40:1-31, ZSB.
6. Yehova alitaja nini nyakati nyingine ili kuonyesha wakati ambapo ukombozi ungetazamiwa?
6 Pindi fulani, Yehova aliwafariji watu wake kwa kutaja wakati hususa ambapo wangekombolewa, iwe ni baada ya muda mfupi au mrefu. Wakati wa kuwakomboa Waisraeli walioteseka Misri ulipokaribia, aliwaambia hivi: “Liko pigo moja bado, nitakaloleta juu ya Farao na juu ya Misri; baadaye atawapa ninyi ruhusa mtoke huku.” (Kutoka 11:1) Wakati mataifa matatu yalipoungana na kuvamia Yuda katika siku za Mfalme Yehoshafati, Yehova aliwaambia kwamba angewakomboa “kesho.” (2 Mambo ya Nyakati 20:1-4, 14-17) Kwa upande mwingine, kukombolewa kwao kutoka Babiloni kulikuwa kumetabiriwa na Isaya miaka 200 mapema, na habari zaidi zilitolewa na nabii Yeremia miaka 100 hivi kabla ya ukombozi huo. Unabii huo uliwatia moyo sana watumishi wa Mungu wakati kukombolewa kwao kulipokaribia!—Isaya 44:26–45:3; Yeremia 25:11-14.
7. Mara nyingi ahadi za ukombozi zilitia ndani nini, na Waisraeli waaminifu walitendaje kuhusiana nazo?
7 Jambo la kupendeza ni kwamba ahadi zilizowafariji watu wa Mungu mara nyingi zilitia ndani habari kumhusu Mesiya. (Isaya 53:1-12) Habari hiyo iliwapa watu waaminifu tumaini walipokabili majaribu mbalimbali, kizazi baada ya kizazi. Tunasoma hivi katika Luka 2:25: “Tazama! palikuwa na mtu mmoja katika Yerusalemu aliyeitwa jina Simeoni, na mwanamume huyu alikuwa mwadilifu na mwenye kumstahi Mungu, akingojea liwazo la Israeli [au, faraja; yaani, kuja kwa Mesiya], na roho takatifu ilikuwa juu yake.” Simeoni alijua tumaini la Maandiko kumhusu Mesiya, na alionyesha katika maisha yake kwamba alitarajia kuona utimizo wa ahadi hizo. Hakuelewa jinsi ahadi hizo zingetimizwa, naye alikufa kabla ya kuona wokovu uliokuwa umetabiriwa, lakini alifurahi alipomtambua Yule ambaye angekuwa ‘njia ya Mungu ya kuokoa.’—Luka 2:30.
Faraja Iliyotolewa Kupitia Kristo
8. Msaada ambao Yesu alitoa ulitofautianaje na msaada ambao watu wengi walifikiri walihitaji?
8 Yesu Kristo alipokuwa akiendelea na huduma yake duniani, mara nyingi hakutoa msaada ambao watu walifikiri walihitaji. Baadhi yao walitazamia kwamba Mesiya angewakomboa kutoka katika utawala wa Roma waliouchukia. Lakini Yesu hakuunga mkono mapinduzi; aliwaambia, “mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari.” (Mathayo 22:21) Kusudi la Mungu lilihusisha mengi zaidi ya kuwakomboa watu kutoka katika utawala fulani wa kisiasa. Watu walitaka kumfanya Yesu awe mfalme, lakini alisema kwamba ‘angetoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28; Yohana 6:15) Wakati wake wa kuwa mfalme haukuwa umefika, na Yehova ndiye angempa mamlaka ya kutawala wala si wanadamu wasioridhika.
9. (a) Yesu alihubiri ujumbe gani wa faraja? (b) Yesu alionyeshaje kwamba ujumbe aliohubiri ulihusu hali mbalimbali ambazo watu walikabili? (c) Huduma ya Yesu ingekuwa na matokeo gani ya baadaye?
9 Yesu alileta faraja kupitia “habari njema ya ufalme wa Mungu.” Huo ndio ujumbe ambao Yesu alihubiri popote alipoenda. (Luka 4:43) Alikazia jinsi ujumbe huo ulivyohusu matatizo ya kawaida ya watu kwa kuonyesha yale atakayowafanyia wanadamu akiwa Mesiya, chini ya Utawala wake wa Ufalme. Aliwapa watu walioteseka kusudi maishani kwa kuwarudishia uwezo wao wa kuona na kusema (Mathayo 12:22; Marko 10:51, 52), kuwaponya vilema (Marko 2:3-12), kuwaponya Waisraeli wenzake magonjwa yenye kuchukiza (Luka 5:12, 13), na magonjwa mengine mabaya sana. (Marko 5:25-29) Kwa kuwafufua watoto waliokuwa wamekufa, aliwafariji sana watu wa familia zao waliokuwa wakiomboleza. (Luka 7:11-15; 8:49-56) Alidhihirisha uwezo wake wa kudhibiti dhoruba hatari na kutosheleza mahitaji ya umati wa watu waliohitaji chakula. (Marko 4:37-41; 8:2-9) Isitoshe, Yesu aliwafundisha kanuni za maisha ambazo zingeweza kuwasaidia kushughulikia matatizo kwa njia inayofaa na ambazo zingewapa tumaini la kupata utawala wa haki chini ya Mesiya. Kwa hiyo, Yesu alipoendelea na huduma yake, mbali na kuwafariji waliomsikiliza kwa imani, huduma yake ingewapa watu kitia-moyo maelfu ya miaka baadaye.
10. Ni mambo gani yanayowezekana kupitia dhabihu ya Yesu?
10 Zaidi ya miaka 60 baada ya Yesu kutoa uhai wake wa kibinadamu kuwa dhabihu na kufufuliwa kwenda mbinguni, mtume Yohana aliongozwa na roho kuandika hivi: “Watoto wangu wadogo, nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi. Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi, tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo, aliye mwadilifu. Na yeye ni dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu, lakini si kwa ajili ya zetu tu bali pia kwa ajili ya zile za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:1, 2) Tunapata faraja kubwa kutokana na dhabihu kamilifu ya kibinadamu ya Yesu. Tunajua kwamba tunaweza kupata msamaha wa dhambi, dhamiri safi, uhusiano mzuri pamoja na Mungu, na tumaini la kuishi milele.—Yohana 14:6; Waroma 6:23; Waebrania 9:24-28; 1 Petro 3:21.
Roho Takatifu Hutoa Faraja
11. Kabla ya kifo chake, Yesu aliahidi kwamba angefanya mpango gani mwingine wa kutoa faraja?
11 Alipokuwa pamoja na mitume wake jioni ya mwisho kabla ya kutoa uhai wake kuwa dhabihu, Yesu alisema kuhusu mpango mwingine ambao Baba yake wa kimbingu alikuwa amefanya ili kuwapa faraja. Yesu alisema hivi: “Nami hakika nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji mwingine [mfariji; pa·raʹkle·tos, katika Kigiriki] awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.” Yesu aliwahakikishia hivi: “Msaidiaji, roho takatifu, . . . itawafundisha nyinyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yohana 14:16, 17, 26) Roho takatifu iliwapa faraja jinsi gani?
12. Watu wengi wamepataje faraja kwa sababu roho takatifu iliwasaidia wanafunzi wa Yesu kukumbuka mambo?
12 Mitume walikuwa wamefundishwa mambo mengi na Yesu. Bila shaka hawakusahau kamwe kwamba aliwafundisha, lakini je, walikumbuka yale aliyosema? Je walisahau mafundisho muhimu kwa sababu ya kutokamilika? Yesu aliwahakikishia kwamba roho takatifu ‘ingewakumbusha mambo yote aliyowaambia.’ Kwa hiyo, miaka minane hivi baada ya Yesu kufa, Mathayo aliandika Injili ya kwanza, inayotia ndani Mahubiri ya Mlimani ya Yesu yenye kuchangamsha, mifano mingi aliyotoa kuhusu Ufalme, na habari kamili kuhusu ishara ya kuwapo kwake. Zaidi ya miaka 50 baadaye, mtume Yohana aliandika masimulizi yanayoaminika yenye habari nyingi kuhusu siku chache za mwisho za maisha ya Yesu duniani. Masimulizi hayo yaliyoandikwa chini ya uongozi wa roho yamewafariji watu sana mpaka siku zetu.
13. Roho takatifu iliwafundishaje Wakristo wa mapema?
13 Mbali na kuwakumbusha tu maneno ya Yesu, roho takatifu iliwafundisha na kuwaongoza wanafunzi hao waelewe kusudi la Mungu vizuri zaidi. Yesu alipokuwa na wanafunzi wake, aliwaambia mambo ambayo hawakuyaelewa waziwazi wakati huo. Hata hivyo, baadaye Yohana, Petro, Yakobo, Yuda, na Paulo, waliongozwa na roho takatifu kueleza katika maandishi yao mambo mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu. Kwa hiyo, roho takatifu iliwafundisha na hivyo kuwapa wanafunzi uhakikisho mzuri kwamba waliongozwa na Mungu.
14. Roho takatifu iliwasaidiaje watu wa Yehova?
14 Uwezo wa kufanya miujiza kupitia kwa roho ulionyesha wazi kwamba sasa kibali cha Mungu kilikuwa juu ya kutaniko la Kikristo wala si juu ya taifa la Israeli la asili. (Waebrania 2:4) Jambo jingine muhimu lililowatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu ni kwamba walidhihirisha matunda ya roho maishani mwao. (Yohana 13:35; Wagalatia 5:22-24) Pia, roho hiyo iliwaimarisha washiriki wa kutaniko hilo watoe ushahidi kwa ujasiri, bila woga.—Matendo 4:31.
Msaada Wakati wa Mateso Makali
15. (a) Wakristo wamekabili magumu gani zamani na wakati huu? (b) Kwa nini wale wanaotoa kitia-moyo huenda nyakati nyingine wakahitaji kutiwa moyo?
15 Wote waliojitoa kwa Yehova na walio waaminifu kwake watanyanyaswa kwa njia fulani. (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, Wakristo wengi wamepatwa na mateso makali sana. Wakati wetu, baadhi yao wameshambuliwa na watu wenye ghasia na kupelekwa kwenye kambi za mateso, magereza, kambi za kazi ngumu, ambako wametendwa kinyama. Serikali nyingine zimewatesa au kuruhusu watu fulani wasiotii sheria wawatende Wakristo kwa jeuri pasipo kuwaadhibu. Isitoshe, Wakristo wamekabili matatizo mabaya ya afya au ya familia. Mkristo mkomavu anaweza pia kukabili magumu anapowasaidia waamini wenzake kushughulikia matatizo mazito. Katika hali kama hizo, yule anayetoa kitia-moyo huenda akahitaji kutiwa moyo pia.
16. Daudi alipata msaada gani alipokabili magumu?
16 Mfalme Sauli alipotaka kumwua Daudi, Daudi alimwendea Mungu ili kupata msaada: “Ee Mungu, uyasikie maombi yangu,” aliomba. “Nitaukimbilia uvuli wa mbawa zako.” (Zaburi 54:2, 4; 57:1) Je, Daudi alipata msaada? Ndiyo. Pindi hiyo, Yehova alimtuma nabii Gadi na kuhani Abiathari kumpa Daudi mwongozo, na Yonathani, mwana wa Sauli, amwimarishe mwanamume huyo kijana. (1 Samweli 22:1, 5; 23:9-13, 16-18) Yehova aliwaruhusu pia Wafilisti kushambulia nchi hiyo, hivyo alimkengeusha Sauli asimfuate Daudi.—1 Samweli 23:27, 28.
17. Yesu alipata wapi msaada alipokabili mateso makali?
17 Yesu Kristo mwenyewe aliteswa vikali alipokaribia kufa. Alijua kabisa matokeo ambayo mwenendo wake ungeleta kwa jina la Baba yake wa mbinguni na wakati ujao wa wanadamu wote. Alisali kwa bidii, hata ‘aliingia katika maumivu makali.’ Mungu alihakikisha kwamba Yesu alipata msaada aliohitaji wakati huo mgumu.—Luka 22:41-44.
18. Mungu aliwapa Wakristo wa mapema walioteswa vikali faraja gani?
18 Baada ya kutaniko la karne ya kwanza kuanzishwa, Wakristo waliteswa vikali sana hivi kwamba wote walitawanyika, na mitume peke yao ndio waliobaki Yerusalemu. Wanaume na wanawake waliburutwa kutoka katika nyumba zao. Mungu aliwafariji jinsi gani? Aliwahakikishia kupitia Neno lake kwamba walikuwa na “miliki bora na yenye kudumu,” yaani, urithi wa milele wa mbinguni pamoja na Kristo. (Waebrania 10:34; Waefeso 1:18-20) Walipoendelea kuhubiri, waliona uthibitisho kwamba roho ya Mungu ilikuwa pamoja nao, na yale waliyojionea yaliwapa sababu nyingine ya kufurahi.—Mathayo 5:11, 12; Matendo 8:1-40.
19. Ingawa Paulo aliteswa vikali, alihisije kuhusu faraja ambayo Mungu hutoa?
19 Hatimaye, Sauli (Paulo), aliyekuwa mtesi mkali, aliteswa pia kwa sababu alikuwa amegeuka na kuwa Mkristo. Kwenye kisiwa cha Saiprasi, kulikuwa na mlozi aliyejaribu kumzuia Paulo asiendelee na huduma yake kwa kutumia ulaghai na udanganyifu. Huko Galatia, watu walimpiga Paulo kwa mawe na kumwacha wakiwazia alikuwa amekufa. (Matendo 13:8-10; 14:19) Huko Makedonia alipigwa kwa fito. (Matendo 16:22, 23) Baada ya kushambuliwa na watu wenye ghasia huko Efeso aliandika hivi: “Tulikuwa chini ya mkazo mkali mno upitao nguvu yetu, hivi kwamba tulikuwa bila hakika kabisa hata juu ya uhai wetu. Kwa kweli, tulihisi ndani yetu wenyewe kwamba tulikuwa tumeipokea hukumu ya kifo.” (2 Wakorintho 1:8, 9) Lakini katika barua hiyohiyo, Paulo aliandika maneno yenye kufariji yaliyonukuliwa katika fungu la 2 la makala hii.—2 Wakorintho 1:3, 4.
20. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
20 Unawezaje kutoa faraja kama hiyo? Kuna watu wengi leo wenye huzuni wanaohitaji faraja kwa sababu ya misiba inayowaathiri maelfu ya watu kwa ghafula, au kwa sababu ya taabu wanazokabili. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi ya kutoa faraja katika hali hizo mbili.
-
-
Wafariji Wale WanaohuzunikaMnara wa Mlinzi—2003 | Mei 1
-
-
Wafariji Wale Wanaohuzunika
“BWANA amenitia mafuta . . . kuwafariji wote wanaoomboleza.” —ISAYA 61:1, 2, Zaire Swahili Bible.
1, 2. Tunapaswa kuwafariji nani, na kwa nini?
YEHOVA, ambaye ni Mungu wa faraja yote ya kweli, hutufundisha kuwajali wengine wanapopatwa na msiba. Yeye hutufundisha ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ na kuwafariji wote wanaoomboleza. (1 Wathesalonike 5:14) Inapohitajika, sisi huwasaidia waabudu wenzetu. Sisi pia huwaonyesha upendo watu wengine ambao si washiriki wa kutaniko, hata wale ambao huenda hapo awali hawakutuonyesha upendo.—Mathayo 5:43-48; Wagalatia 6:10.
2 Yesu Kristo alisoma na kusema kwamba kazi hii ya kiunabii ilimhusu: “Roho ya Bwana Mungu ni juu yangu; kwa sababu BWANA amenitia mafuta, kuhubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma niwaponyeshe wenye kuvunjika kwa moyo, . . . kuwafariji wote wanaoomboleza.” (Isaya 61:1, 2, ZSB; Luka 4:16-19) Kwa muda mrefu, Wakristo watiwa-mafuta wa leo wametambua kwamba wao pia wanapaswa kufanya kazi hiyo, nao “kondoo wengine” wanajiunga nao kwa furaha kuifanya.—Yohana 10:16.
3. Tunawezaje kuwasaidia watu wanapouliza, “Kwa nini Mungu huruhusu misiba itokee”?
3 Misiba inapotokea watu huvunjika moyo na mara nyingi huuliza, “Kwa nini Mungu huruhusu misiba itokee?” Biblia hujibu swali hilo waziwazi. Hata hivyo, huenda ikachukua muda kwa mtu ambaye hajajifunza Biblia kuelewa kikamili jibu la swali hilo. Msaada unaweza kupatikana katika vichapo vya Mashahidi wa Yehova.a Lakini wengine wamefarijika kwa kusoma tu andiko fulani katika Biblia kama vile Isaya 61:1, 2, kwa kuwa linaonyesha kwamba Mungu anataka wanadamu wapate faraja.
4. Shahidi mmoja huko Poland alimsaidiaje msichana fulani aliyeshuka moyo, na jambo hilo linaweza kukusaidiaje uwasaidie wengine?
4 Vijana na vilevile wazee wanahitaji faraja. Tineja mmoja nchini Poland aliyekuwa ameshuka moyo alimwomba rafiki yake ushauri. Baada ya rafiki huyo ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova kumwuliza maswali kwa fadhili, alitambua kwamba msichana huyo alikuwa na maswali na shaka nyingi: “Kwa nini kuna uovu mwingi? Kwa nini watu huteseka? Kwa nini dada yangu aliyelemaa anateseka? Kwa nini nina ugonjwa wa moyo? Tunaambiwa kanisani kwamba hayo ni mapenzi ya Mungu. Lakini ikiwa ndivyo ilivyo, basi, mimi nitaacha kumwamini Mungu!” Shahidi huyo alisali kwa Yehova kimoyomoyo kisha akasema: “Ninafurahi kwamba umeniuliza kuhusu mambo hayo. Nitajaribu kukusaidia.” Shahidi huyo alisema kwamba alipokuwa mdogo, yeye pia alikuwa na shaka lakini Mashahidi wa Yehova wakamsaidia. Alisema: “Nilijifunza kwamba Mungu hafanyi watu wateseke. Yeye anawapenda na anawatakia mema, na hivi karibuni ataleta mabadiliko makubwa duniani. Ataondoa magonjwa, matatizo ya uzee, na kifo, nao watu watiifu wataishi milele papa hapa duniani.” Alimwonyesha msichana huyo andiko la Ufunuo 21:3, 4; Ayubu 33:25; Isaya 35:5–7 na 65:21-25. Baada ya mazungumzo marefu, msichana huyo alisema hivi akionekana kuwa amefarijika: “Sasa nimepata kusudi la maisha. Je, nije kukuona tena?” Shahidi huyo alianza kujifunza Biblia pamoja naye mara mbili kila juma.
Kwa Faraja Ambayo Mungu Hutoa
5. Tunapoonyesha huruma, ni nini kitakachotoa faraja ya kweli?
5 Bila shaka, inafaa kutumia maneno ya huruma tunapowafariji wengine. Kwa maneno na kwa sauti yetu, tunajitahidi kumwonyesha mtu mwenye huzuni kwamba tunamjali sana. Hatuwezi kufanya hivyo kwa kusema kijuujuu tu. Biblia hutuambia kwamba ‘kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tunapata kuwa na tumaini.’ (Waroma 15:4) Kwa sababu hiyo, tunaweza kutafuta wakati unaofaa kuwaeleza Ufalme wa Mungu ni nini, na kuonyesha katika Biblia jinsi ufalme huo utakavyosuluhisha matatizo ya sasa. Kisha tuwaeleze kinachofanya tumaini hilo litegemeke. Kwa njia hiyo, tutawafariji wengine.
6. Tunapaswa kuwasaidia watu waelewe nini ili waweze kunufaika kabisa na faraja inayopatikana katika Maandiko?
6 Ili mtu anufaike kabisa na faraja tunayotoa, anahitaji kumjua Mungu wa kweli, utu wake, na kwamba ahadi zake zinategemeka. Tunapotaka kumsaidia mtu ambaye si mwabudu wa Yehova, inafaa tumweleze mambo yafuatayo. (1) Faraja inayopatikana katika Biblia inatoka kwa Yehova Mungu wa kweli. (2) Yehova ndiye Mweza Yote, Muumba wa mbingu na dunia. Yeye ni Mungu wa upendo na mwingi wa fadhili-upendo na kweli. (3) Tunaweza kuimarishwa ili kuvumilia hali mbalimbali iwapo tutamkaribia Mungu kwa kutwaa ujuzi sahihi wa Neno lake. (4) Biblia ina maandiko yanayozungumzia majaribu fulani hususa yaliyowapata watu mbalimbali.
7. (a) Ni nini kinachoweza kutimizwa kwa kukazia kwamba faraja ambayo Mungu hutoa ‘huzidi kupitia Kristo’? (b) Unawezaje kumfariji mtu ambaye anatambua kwamba mwenendo wake umekuwa mbaya?
7 Wengine wamewafariji kiroho watu wenye huzuni ambao tayari wanaijua Biblia kwa kuwasomea andiko la 2 Wakorintho 1:3-7. Wanapofanya hivyo, wanakazia maneno kwamba ‘faraja tupatayo huzidi kupitia Kristo.’ Andiko hilo linaweza kumsaidia mtu atambue kwamba Biblia inaweza kumfariji na anapaswa kuichunguza zaidi. Biblia pia inaweza kutumiwa kwa mazungumzo zaidi, labda katika pindi nyingine. Ikiwa mtu anafikiri kwamba matatizo yake yanasababishwa na maovu ambayo amefanya, basi tunaweza kumweleza bila kumlaumu kwamba atafarijika kujua yale yaliyoandikwa kwenye 1 Yohana 2:1, 2 na Zaburi 103:11-14. Kwa kufanya hivyo tunawafariji wengine kikweli kwa faraja ambayo Mungu hutoa.
Kuwafariji Watu Waliokumbwa na Jeuri au Hali Ngumu za Kiuchumi
8, 9. Faraja inaweza kutolewaje kwa njia inayofaa kwa watu waliokumbwa na jeuri?
8 Watu wengi sana wamekumbwa na jeuri—inayotokea katika jumuiya au inayosababishwa na vita. Tunaweza kuwafariji namna gani?
9 Wakristo wa kweli huwa waangalifu kutounga mkono kwa maneno au kwa matendo upande wowote katika mapigano ya ulimwengu. (Yohana 17:16) Lakini wao hutumia Biblia ifaavyo kuonyesha kwamba hali ngumu za sasa hazitaendelea milele. Huenda wakasoma andiko la Zaburi 11:5, NW kuonyesha jinsi Yehova huhisi kuhusu wale wapendao jeuri au Zaburi 37:1-4 kuonyesha jinsi Mungu anavyotutia moyo tusilipize kisasi bali tumtumaini. Maneno ya Zaburi 72:12-14 yanaonyesha jinsi Sulemani Mkuu, Yesu Kristo, ambaye sasa ni Mfalme mbinguni, anavyohisi kuhusu watu wasio na hatia wanaokumbwa na jeuri.
10. Ikiwa umekabili mapigano kwa miaka mingi, maandiko yaliyotajwa yanaweza kukufariji namna gani?
10 Watu wengine wamekabili mapigano mengi huku vikundi mbalimbali viking’ang’ania kuchukua mamlaka. Wanafikiri vita na matokeo yake ni kawaida ya maisha. Wanaona kwamba kukimbilia nchi nyingine ndilo tumaini pekee la kuwa na maisha bora. Lakini wengi wao hawafaulu kukimbia nchi zao, na baadhi yao wamekufa wakijaribu kufanya hivyo. Mara nyingi wale wanaofaulu kukimbia matatizo katika nchi zao hupata kwamba kuna matatizo ya aina nyingine katika nchi wanazokimbilia. Andiko la Zaburi 146:3-6 linaweza kutumiwa kuwasaidia watu kama hao kuweka tumaini lao katika jambo jingine lenye kutegemeka zaidi kuliko kuhama nchi zao. Unabii kwenye Mathayo 24:3, 7, 14 au 2 Timotheo 3:1-5 unaweza kuwasaidia waelewe mambo vizuri zaidi na pia waelewe kwamba hali hizo zinawapata kwa sababu tunaishi katika umalizio wa mfumo huu wa mambo wa kale. Maandiko kama vile Zaburi 46:1-3, 8, 9 na Isaya 2:2-4 yanaweza kuwasaidia watambue kwamba kwa kweli kuna tumaini la kuwa na wakati ujao wenye amani.
11. Mwanamke fulani huko Afrika Magharibi alifarijiwa na Maandiko gani, na kwa nini?
11 Wakati vita ilipokuwa ikiendelea huko Afrika Magharibi, mwanamke mmoja na familia yake walitoroka nyumbani kwao huku risasi zikirushwa hewani kwa wingi. Alianza kuishi maisha yaliyojawa na woga, huzuni, na akavunjika moyo sana. Baadaye, familia hiyo ilipokuwa ikiishi katika nchi nyingine, mume wake aliamua kuteketeza cheti chao cha ndoa, akamfukuza mke wake aliyekuwa mjamzito, pamoja na mwana wao mwenye umri wa miaka kumi, kisha akawa kasisi. Hatimaye mwanamke huyo alipata faraja na kusudi maishani baada ya kusomewa andiko la Wafilipi 4:6, 7 na Zaburi 55:22 pamoja na makala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinazozungumzia Biblia.
12. (a) Maandiko hutoa kitulizo gani kwa wale wanaokabili hali ngumu sana za kiuchumi? (b) Shahidi mmoja huko Asia alimsaidiaje mnunuzi fulani?
12 Maisha ya watu wengi yameharibika kwa sababu ya kuzorota kwa uchumi. Wakati mwingine hali hiyo husababishwa na vita na matokeo yake. Nyakati nyingine, watu wamepoteza akiba zao za pesa na mali zao kwa sababu ya sera zisizofaa za serikali, pupa, na ukosefu wa unyofu wa wale wanaotawala. Wengine hata hawajawahi kuwa na mali. Wote hao wanaweza kufarijika kujua kwamba Mungu anawahakikishia wale wanaomtumaini kuwa watapata kitulizo na pia kuishi katika ulimwengu wenye uadilifu ambapo watu watafurahia kazi ya mikono yao. (Zaburi 146:6, 7; Isaya 65:17, 21-23; 2 Petro 3:13) Baada ya kumsikia mnunuzi akilalamika kuhusu hali ya kiuchumi, Shahidi fulani anayefanya kazi kwenye duka katika nchi moja ya Asia alimweleza mnunuzi huyo kwamba hali hiyo ni mojawapo ya mambo yanayotokea ulimwenguni pote. Funzo la Biblia la kawaida lilianzishwa baada ya kuzungumzia andiko la Mathayo 24:3-14 na Zaburi 37:9-11.
13. (a) Watu wanapokatishwa tamaa na ahadi za uwongo, tunawezaje kuwasaidia kwa kutumia Biblia? (b) Ikiwa watu wanafikiri kwamba hali mbaya zinathibitisha kwamba hakuna Mungu, unaweza kuwasaidiaje watambue kwamba hivyo sivyo ilivyo?
13 Watu wanapoteseka kwa miaka mingi au kukatishwa tamaa na ahadi nyingi za uwongo, wanaweza kuwa kama Waisraeli huko Misri ambao hawakusikiliza “kwa ajili ya uchungu wa moyo.” (Kutoka 6:9) Katika hali kama hizo, huenda ikafaa kukazia njia ambazo Biblia inaweza kuwasaidia wafanikiwe kutatua matatizo wanayokabili na kujiepusha na mitego ambayo huharibu isivyo lazima maisha ya wengi. (1 Timotheo 4:8b) Huenda wengine wakafikiri kwamba hali mbaya wanazokabili maishani ni uthibitisho kwamba hakuna Mungu au hajali. Unaweza kutumia maandiko yafaayo ili kuwasaidia watambue kwamba Mungu ametoa msaada lakini wengi wameukataa.—Isaya 48:17, 18.
Kuwafariji Wale Waliokumbwa na Dhoruba na Matetemeko ya Ardhi
14, 15. Mashahidi wa Yehova walionyeshaje kwamba wanawajali wengine baada ya msiba fulani kuwashtua wengi?
14 Huenda msiba ukasababishwa na dhoruba, matetemeko ya ardhi, moto, au mlipuko, na huenda watu wengi wakapatwa na huzuni. Ni nini kinachoweza kuwafariji waokokaji?
15 Watu wanahitaji kujua kwamba kuna mtu anayejali. Baada ya shambulio la kigaidi katika nchi fulani, wengi walishtuka. Wengi wao walipoteza washiriki wa familia zao, watafuta-riziki, na marafiki. Wengine walipoteza kazi na hali ya usalama waliyofikiri walikuwa nayo. Mashahidi wa Yehova waliwasaidia majirani wao, wakawapa pole kwa yale yaliyowapata, na kuwafariji kwa kutumia Biblia. Wengi waliwashukuru Mashahidi sana kwa kuwajali.
16. Msiba ulipotokea katika eneo moja huko El Salvador, kwa nini Mashahidi wa Yehova nchini humo walikuwa na matokeo sana katika kazi ya kuhubiri?
16 Huko El Salvador tetemeko kubwa la ardhi lililotokea mwaka wa 2001 lilifuatiwa na maporomoko makubwa ya matope yaliyowaua watu wengi. Mwanamume mmoja mwenye umri wa miaka 25, aliyekuwa mtoto wa Shahidi, alikufa pamoja na dada wawili wa mchumba wake. Mama ya mwanamume huyo kijana pamoja na mchumba wake waliendelea kuhubiri kwa bidii baada tu ya msiba huo. Wengi walisema kwamba Mungu ndiye aliyewachukua wale waliokufa au kwamba hayo yalikuwa mapenzi ya Mungu. Mashahidi hao walitaja andiko la Mithali 10:22 ili kuonyesha kwamba Mungu hataki tuumie. Walisoma andiko la Waroma 5:12 kuonyesha kwamba kifo si mapenzi ya Mungu, bali husababishwa na dhambi ya mwanadamu. Pia walitaja ujumbe wa faraja unaopatikana katika andiko la Zaburi 34:18, Zaburi 37:29, Isaya 25:8, na Ufunuo 21:3, 4. Wanawake hao wawili walianzisha mafunzo mengi ya Biblia kwa sababu watu walikuwa tayari kuwasikiliza, hasa kwa sababu wao pia walikuwa wamepoteza washiriki wa familia zao katika msiba huo.
17. Tunaweza kutoa misaada ya aina gani wakati wa msiba?
17 Msiba unapotokea, huenda ukapata mtu anayehitaji kusaidiwa haraka. Huenda ikakubidi kutafuta daktari, kumsaidia mtu huyo afike hospitalini, au kufanya yote uwezayo ili apate chakula na makao. Msiba ulipotokea huko Italia mwaka wa 1998, mwandishi mmoja wa habari alisema kwamba Mashahidi wa Yehova “huwasaidia kimatendo watu wanaoteseka bila kujali wao ni wa dini gani.” Mambo yaliyotabiriwa kutukia katika siku za mwisho husababisha mateseko makubwa katika maeneo fulani. Katika maeneo hayo, Mashahidi wa Yehova hueleza unabii wa Biblia, na kuwafariji watu kwa uhakikisho ulio katika Biblia kwamba Ufalme wa Mungu utawaletea wanadamu usalama wa kweli.—Mithali 1:33; Mika 4:4.
Kutoa Faraja Mshiriki wa Familia Anapokufa
18-20. Huenda ukasema au ukafanya nini kuifariji familia iliyofiwa?
18 Kila siku watu wengi huhuzunika mpendwa wao anapokufa. Huenda ukakutana na watu wanaoomboleza unaposhiriki katika huduma ya Kikristo au unapokuwa katika shughuli zako za kawaida. Unaweza kusema au kufanya nini ili kuwafariji?
19 Je, mtu huyo amevurugika kihisia-moyo? Je, nyumba yake imejaa watu wa ukoo wenye huzuni? Huenda ukataka kusema mengi, lakini unahitaji kuwa mwenye utambuzi. (Mhubiri 3:1, 7) Labda jambo linalofaa ni kuwapa pole, kuwaachia kichapo kifaacho kinachozungumzia Biblia (broshua, gazeti, au trakti), kisha urudi baada ya siku kadhaa kuona kama unaweza kuwasaidia zaidi. Tafuta wakati unaofaa ili kuzungumza nao mambo yenye kutia moyo kutoka katika Biblia. Kufanya hivyo kunaweza kuwatuliza sana. (Mithali 16:24; 25:11) Huwezi kuwafufua wafu kama Yesu alivyofanya. Lakini unaweza kuwaeleza wengine yale ambayo Biblia husema kuhusu hali ya wafu, ingawa huenda huo usiwe wakati unaofaa kupinga maoni yao yenye makosa. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Unaweza kusoma pamoja nao ahadi za Biblia kuhusu ufufuo. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Huenda ukazungumzia maana ya Maandiko hayo, labda ukitumia masimulizi fulani ya Biblia kuhusu ufufuo. (Luka 8:49-56; Yohana 11:39-44) Pia kazia sifa za Mungu mwenye upendo anayetupatia tumaini hilo. (Ayubu 14:14, 15; Yohana 3:16) Eleza jinsi ambavyo umenufaishwa na mafundisho hayo na kinachofanya uyatumaini.
20 Kumwalika mtu mwenye huzuni kwenye Jumba la Ufalme kunaweza kumsaidia apate kuwajua watu wanaowapenda majirani wao kikweli na wanaojua kujengana. Mwanamke mmoja nchini Sweden alisema kwamba hao ndio watu aliokuwa akitafuta maishani mwake.—Yohana 13:35; 1 Wathesalonike 5:11.
21, 22. (a) Tunahitaji kufanya nini ili kuwafariji wengine? (b) Unawezaje kumfariji mtu ambaye tayari anajua Maandiko vizuri?
21 Unapojua kwamba mtu fulani ana huzuni, awe ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo au la, je, wakati mwingine unashindwa la kusema au kufanya? Neno la Kigiriki ambalo mara nyingi hutafsiriwa “faraja” katika Biblia, humaanisha “kumkaribisha mtu aje upande wako.” Ili uwe mfariji wa kweli, unahitaji kuwa mtu anayeweza kufikiwa kwa urahisi na wale wenye huzuni.—Mithali 17:17.
22 Namna gani ikiwa mtu unayetaka kumfariji tayari anajua yale Biblia husema kuhusu kifo, fidia, na ufufuo? Kuwapo tu kwa rafiki mwenye imani sawa na yake kunaweza kumfariji. Akitaka kuzungumza, msikilize kwa makini. Usihisi kwamba unahitaji kuzungumza sana. Ikiwa utasoma Maandiko, yaone kuwa maneno ya Mungu yanayowaimarisha nyote wawili. Onyesha kwamba nyote wawili mna hakika kabisa na ahadi ambayo Maandiko hayo yanatoa. Unaweza kuwasaidia wale wenye huzuni wapate faraja kutoka kwa Yehova, “Mungu wa faraja yote” kwa kuwaonyesha huruma kama ya Mungu na kuwaeleza kweli zenye thamani za Neno la Mungu.—2 Wakorintho 1:3.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, sura ya 8; Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko ukurasa wa 131-138, 369-373; Je, Kuna Muumba Anayekujali? sura ya 10; na broshua Je! Kweli Mungu Anatujali?
-