Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Kuujua Upendo wa Kristo”
    Mkaribie Yehova
  • “Kuujua Upendo wa Kristo”
    Mkaribie Yehova
    • ‘Alisukumwa na Sikitiko’

      8. Neno la Kigiriki ambalo linatumiwa na Biblia kufafanua huruma ya Yesu linamaanisha nini?

      8 Yesu alikuwa na huruma kama Baba yake. Maandiko yanaonyesha jinsi ambavyo Yesu alijitahidi kuwasaidia watu waliotaabika kwa sababu aliwahurumia sana. Biblia inafafanua huruma ya Yesu kwa kutumia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “sukumwa na sikitiko.” Msomi mmoja anasema hivi: ‘Neno hilo linafafanua hisia ya ndani sana ambayo inamchochea mtu kutoka moyoni. Hakuna neno jingine la Kigiriki linalofafanua hisia ya huruma kwa mkazo sana kama neno hilo.’ Ebu ona pindi fulani-fulani ambapo huruma ilimchochea Yesu kutenda.

      9, 10. (a) Ni kwa nini Yesu na mitume wake walitafuta mahali pa faragha? (b) Yesu alihisije umati ulipovuruga faragha yake, na kwa nini?

      9 Alichochewa kuwasaidia watu kiroho. Simulizi la Marko 6:30-34 laonyesha sababu iliyomfanya Yesu awasikitikie watu. Wazia hali ilivyokuwa. Mitume walifurahi sana baada ya kuhubiri kotekote. Walirudi kwa Yesu na kumsimulia kwa shauku mambo yote waliyoona na kusikia. Lakini umati mkubwa ukakusanyika, na Yesu na mitume wake wakakosa hata nafasi ya kula. Daima akiwa makini, Yesu akafahamu kwamba mitume wamechoka. Akawaambia: “Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.” Walipanda mashua na kuvuka upande wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya hadi mahali pa faragha. Lakini umati uliwaona wakienda. Wengine walipata habari hizo pia. Watu hao wote walikimbia kuzunguka ufuko wa kaskazini wa bahari hiyo na kufika ng’ambo nyingine kabla ya ile mashua!

      10 Je, Yesu alikasirika kwa sababu watu walivuruga faragha yake? La hasha! Alisikitika sana alipoona umati huo wa maelfu ya watu ukimsubiri. Marko aliandika hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Yesu alitambua kwamba watu hao walikuwa na mahitaji ya kiroho. Walikuwa kama kondoo wanaozurura huku na huku bila mchungaji wa kuwaongoza au kuwalinda. Yesu alijua kwamba watu wa kawaida walipuuzwa na viongozi wa kidini ambao badala ya kuwa wachungaji wenye kujali, waliwatendea bila huruma. (Yohana 7:47-49) Aliwasikitikia sana watu, akaanza kuwafundisha “juu ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:11) Ona kwamba Yesu aliwasikitikia watu hata bila kujua jinsi ambavyo wangeitikia mafundisho yake. Yaani, Yesu hakuwahurumia watu kwa sababu tu walikubali mafundisho yake bali aliwafundisha kwa sababu alichochewa na huruma yake nyororo.

      Kwa huruma Yesu anamgusa mwenye ukoma na kumponya

      “Akanyoosha mkono wake akamgusa”

      11, 12. (a) Wenye ukoma walitendewaje nyakati za Biblia, lakini Yesu alitendaje alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma”? (b) Huenda mtu mwenye ukoma aliyeguswa na Yesu alihisije, na kisa halisi cha daktari mmoja kinathibitishaje jambo hilo?

      11 Alichochewa kukomesha mateso. Watu wenye magonjwa mbalimbali walivutiwa na Yesu kwa sababu walijua yeye ni mwenye huruma. Jambo hilo lilionekana wazi wakati Yesu huku akifuatwa na umati alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma.” (Luka 5:11, 12) Katika nyakati za Biblia, wenye ukoma walitengwa ili wasiwaambukize wengine. (Hesabu 5:1-4) Lakini baada ya muda, marabi wasio na huruma walikuwa na maoni mabaya kuhusu ukoma, hivyo wakatunga sheria zao wenyewe zenye kukandamiza.a Ingawa hivyo, hebu ona jinsi Yesu alivyomtendea yule mtu mwenye ukoma: “Huko pia mwenye ukoma akaja kwake, akimsihi sana hata kwa kukunja magoti, akimwambia: ‘Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.’ Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’ Na mara hiyo ule ukoma ukamtoka.” (Marko 1:40-42) Yesu alijua kwamba mtu huyo mwenye ukoma hakupaswa kuwa miongoni mwa watu. Hata hivyo, badala ya kumfukuza, Yesu alimsikitikia sana hivi kwamba alifanya jambo la kushangaza. Yesu alimgusa!

      12 Wafikiri mtu huyo alihisije alipoguswa na Yesu? Kwa mfano, hebu fikiria kisa hiki halisi. Dakt. Paul Brand, mtaalamu wa ukoma, asimulia kuhusu mtu mmoja mwenye ukoma ambaye alimtibu nchini India. Alipokuwa akimpima, daktari huyo alimshika begani na kumweleza kupitia mkalimani matibabu ambayo angepewa. Mtu huyo alianza kulia ghafula. Daktari akamwuliza, “Nimesema jambo baya?” Mkalimani akamwuliza kijana huyo swali hilo katika lugha yake kisha akajibu: “La, daktari. Anasema analia kwa sababu umemshika begani. Hajapata kamwe kuguswa na yeyote kwa miaka mingi isipokuwa wewe.” Yule mtu mwenye ukoma aliyemfikia Yesu alifaidika hata zaidi alipoguswa naye. Baada ya kuguswa mara moja tu, ugonjwa uliomfanya atengwe na watu ulitoweka kabisa!

      13, 14. (a) Yesu alikutana na msafara gani alipokaribia jiji la Naini, na kwa nini kisa hicho kilihuzunisha sana? (b) Yesu alichochewaje na huruma kumsaidia yule mjane wa Naini?

      13 Alichochewa kuondoa huzuni. Yesu alisikitishwa sana na huzuni ya wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Luka 7:11-15. Jambo hilo lilitukia alipokuwa anakaribia kumaliza nusu ya huduma yake duniani. Yesu alikuwa amekaribia jiji la Naini huko Galilaya alipokutana na msafara wa mazishi karibu na lango la jiji hilo. Kilikuwa kisa chenye kuhuzunisha sana. Mwana pekee wa mjane mmoja alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba mjane huyo aliwahi kuwa katika msafara mwingine kama huo wakati wa mazishi ya mume wake. Sasa mwanaye ambaye huenda ndiye tu aliyemruzuku alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba miongoni mwa umati ulioandamana naye mlikuwa na waombolezaji walioimba nyimbo za maombolezo na wanamuziki waliocheza miziki ya maombolezo. (Yeremia 9:17, 18; Mathayo 9:23) Hata hivyo, Yesu alimtazama sana mama huyo aliyekuwa na majonzi tele, ambaye yaelekea alifuata kwa ukaribu jeneza lililobeba maiti ya mwanaye.

      14 Yesu ‘alimsikitikia’ mama huyo. Kwa sauti yenye kutia moyo, akamwambia hivi: “Koma kutoa machozi.” Akalikaribia jeneza na kuligusa. Wale waliokuwa wamelibeba—na labda umati wote—wakasimama tuli. Kwa sauti yenye nguvu, Yesu akamwambia hivi yule maiti: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” Halafu ikawaje? “Huyo mfu akaketi na kuanza kusema” kana kwamba ameamshwa kutoka kwa usingizi mzito! Maneno yanayofuata yanagusa moyo sana: “Naye [Yesu] akampa huyo kwa mama yake.”

      15. (a) Masimulizi ya Biblia yanayoeleza jinsi Yesu alivyowasikitikia watu, yanaonyesha kuna uhusiano gani kati ya huruma na matendo? (b) Tunawezaje kumwiga Yesu?

      15 Twajifunza nini kutokana na visa hivyo? Katika kila kisa, angalia uhusiano uliopo kati ya huruma na matendo. Sikuzote Yesu aliwahurumia watu waliokuwa wakitaabika, na huruma hiyo ilimchochea kutenda. Tunawezaje kuiga mfano wake? Tukiwa Wakristo, tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Upendo wetu kwa Mungu ndio hasa unaotuchochea. Na tukumbuke kwamba kazi ya kuhubiri ni njia ya kuwaonyesha watu huruma. Tukiwahurumia watu kama alivyofanya Yesu, moyo wetu utatuchochea kujitahidi tuwezavyo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:37-39) Tutawaonyeshaje huruma waamini wenzetu ambao wanateseka au wamefiwa? Hatuwezi kukomesha mateso yao kimuujiza au kufufua wafu. Lakini, tunaweza kuwahurumia kwa matendo kwa kuwaonyesha kwamba tunawajali au kwa kuwapa msaada wanaohitaji.—Waefeso 4:32.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki