-
Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
OMBI LA UBATIZO LENYE KUTATANISHA. Mwanzoni mwa kusanyiko la wilaya mjini Brazzaville, katika Jamhuri ya Kongo mwaka wa 2010, kijana anayeitwa Edvard alisema kuwa anataka kubatizwa. Alipoulizwa yeye ni wa kutaniko gani, alijibu: “Mossaka.” Kwa sababu hakukuwa Mashahidi katika kijiji hicho cha mbali, akina ndugu walishangaa na wakataka kujua jinsi alivyofikia hatua ya kutaka kubatizwa.
Edvard aliwaeleza wazee kwamba mwaka wa 2007, babu yake alijifunza naye broshua Anataka na vilevile sura 14 za kitabu Biblia Inafundisha mjini Brazzaville. Kisha Edvard akahamia Mossaka ili kuishi na wazazi wake. Kwa sababu hakukuwa na Mashahidi watendaji huko, Edvard alimwomba baba yake amsaidie kujifunza sehemu iliyosalia ya kitabu Biblia Inafundisha. Baba yake angeuliza maswali, na Edvard angejibu. Kwa njia hiyo Edvard alimaliza kujifunza kitabu hicho. Kisha akaona umuhimu wa kufundisha wengine mambo aliyokuwa amejifunza. Hivyo, mwezi wa Oktoba 2009, akaanza kuhubiri akiwa peke yake katika eneo la Mossaka akitumia broshua Anataka. Aliandika muda aliotumia katika utumishi wa shambani na kutuma ripoti zake kwa ukawaida kwa babu yake huko Brazzaville. Lakini, babu yake hakutoa ripoti hizo kwa kutaniko.
Baadaye, bila kujua lolote kuhusu Edvard, ofisi ya tawi iliwatuma mapainia wa pekee wa muda huko Mossaka kwa miezi mitatu. Siku mbili tu kabla waondoke huko, Daniel, mmoja wa mapainia hao wa pekee, alimwona Edvard akiongoza funzo la Biblia kwa kutumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kwa hiyo, Daniel akamfikia Edvard na kuzungumza naye. Edvard akamwambia: “Ninahubiri. Mimi ni mhubiri. Unaweza kumuuliza baba yangu.” Daniel alikutana na baba ya Edvard ambaye alimhakikishia kuwa mambo aliyosema Edvard yalikuwa ya kweli. Mapainia hao wa pekee wa muda walitumia siku mbili zilizosalia kabla ya kumaliza mgawo ili kumzoeza Edvard katika huduma. Baada ya wao kuondoka, Edvard aliendelea kuhubiri kwa bidii, na kuongoza zaidi ya mafunzo kumi ya Biblia. Pia alijiweka wakfu kwa Yehova.
Wakiwa na habari hizo kumhusu, wazee wawili walikutana na Edvard siku ya Ijumaa ya kusanyiko lililotajwa hapo awali, na kupitia maswali ya wanaotaka kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Majibu yake sahihi yaliwashangaza. Wazee walipata habari kutoka kwa mapainia wa pekee kwamba mwenendo wa Edvard ni mzuri na tayari alikuwa amehubiri kwa miezi tisa. Kwa sababu hiyo, akawekwa rasmi kuwa mhubiri ambaye bado hajabatizwa. Kwa sababu kungekuwa na kusanyiko la wilaya la lugha ya Lingala mwishoni mwa juma lililofuata, wazee walifanya mipango ili Edvard apitie maswali ya ubatizo siku chache kabla ya kusanyiko. Ilionekana wazi kuwa anaielewa kweli vizuri na akabatizwa katika kusanyiko hilo mnamo Julai 2010. Kisha, juma moja tu baada ya kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, wazee wakatangaza kuwa Edvard ni ndugu aliyebatizwa.
Baada ya kubatizwa, alifanya upainia msaidizi kwa miezi miwili mjini Brazzaville. Wazee walifanya mipango ili ajifunze kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” halafu akarudi Mossaka. Hivi majuzi, painia wa pekee alitumwa katika eneo hilo. Mwezi wa Aprili, Edvard—ambaye wakati huo alikuwa painia msaidizi—pamoja na painia huyo wa pekee, waliwakaribisha watu 182 waliopendezwa kwenye Ukumbusho. Edvard ana mafunzo 16, na 7 kati yao wanahudhuria mikutano ambayo inaongozwa na ndugu hao wawili. Kufikia mwaka wa 2011, Edvard alikuwa na umri wa miaka 15.
-
-
Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 56]
Juu: Kuongoza funzo la Biblia katika Jamhuri ya Kongo (ona ukurasa wa 59)
[Picha katika ukurasa wa 61]
Edvard (kulia) pamoja na Daniel katika soko fulani
-