Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
ZAMANI, katika maono ya kinabii, mtume Yohana aliona umati mkubwa usio na hesabu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Watu hao walitambuliwa kuwa wale wanaookoka “dhiki kuu” na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufu. 7:9, 14) Tarakimu na mambo yaliyoonwa yaliyo katika kurasa zifuatazo yanaonyesha kwamba, mbali na kukusanywa, umati mkubwa unaendelea kuwa mkubwa hata zaidi. Je, hilo haliimarishi hata zaidi imani yako katika ahadi za Yehova?
AFRIKA
IDADI YA NCHI 57
IDADI YA WATU 949,533,064
IDADI YA WAHUBIRI 1,267,314
IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,819,310
BARUA YAKE ILIMFARIJI. Iris, anayeishi Afrika Kusini, huandika barua za kuwafariji wale ambao wamefiwa na wapendwa wao. Katika barua hizo yeye huambatanisha trakti Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni! na Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa? Hivi karibuni, alipokea majibu kutoka kwa mtu anayeitwa Sidney, ambaye alifiwa na mke wake baada ya ndoa yenye furaha ya miaka 38. Sidney aliandika, “Ingawa wataalamu wa kitiba walinieleza kuwa hatimaye mke wangu mpendwa angekufa, kifo chake kimenifanya niwe bila tumaini, nichanganyikiwe, niwe na uchungu mwingi, na kuvunjika moyo sana. Ninamshukuru Bwana kwa watu kama ninyi. Muda na jitihada unazotumia kuwaeleza watu usiowajua kabisa kuhusu ahadi za Mungu ni jambo bora, na njia ambayo unaeleza imani yako itaendelea kuwa kitu chenye thamani moyoni mwangu katika kipindi kigumu kilicho mbele. Barua na trakti ulizonitumia zimenisaidia kuelewa mambo na kwa mara ya kwanza, nimepata utulivu.”
WAAMUA KUTOTOA MIMBA. Gloria, dada mchanga kutoka Benin, alimhubiria Arnaud, mwanafunzi wa chuo kikuu. Mazungumzo yalipokuwa yanaendelea, Arnaud alipigiwa simu, akaomba aondoke kwa sababu rafiki yake aliyempigia simu alihitaji msaada wake. Mara moja Gloria akatoa gazeti la kwanza alilopata mkobani na kumpa. Arnaud akalichukua bila kuliangalia na akaondoka.
Rafiki ya Arnaud aliyepiga simu alisema kwamba mpenzi wake alikuwa na mimba na alitaka kumlazimisha aitoe. Akiwa njiani, Arnaud aliangalia gazeti alilopewa. Baadaye alisema: “Sikuamini macho yangu nilipoona maneno ‘kutoa mimba’ kwenye jalada.” Gloria alikuwa amempa gazeti la Amkeni! la Juni 2009 lenye kichwa “Kutoa Mimba—Kwa Nini ni Suala Linalobishaniwa?” Baada ya rafiki ya Arnaud kusoma gazeti hilo, aliamua kuwa mimba haipaswi kutolewa. Baadaye mpenzi wa rafiki ya Arnaud alijifungua mtoto mrembo wa kike.
HATUKUWA NA SABABU YA KUOGOPA MCHAWI. King, ambaye ni painia wa kawaida, alihamia eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi nchini Zimbabwe. Alipokuwa akihubiri pamoja na dada wengine, alifika katika nyumba ya mchawi mmoja aliyejulikana sana. Ingawa dada hao waliogopa kuzungumza na mwanamke huyo, King aliamua kumweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani. Mchawi huyo alipoona King na dada mmoja wakikaribia, alifikiri ni wateja wake na akawauliza walichotaka. King akamwonyesha kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? na kumweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia nyumbani. Mwanamke huyo alikubali kujifunza. “Tulishangaa kujua kwamba alikuwa na maswali mengi,” King akasema. “Kwa hiyo tukapanga kurudi ili kujifunza Biblia.” Majuma matatu baadaye walimwalika kwa mikutano, na akahudhuria. Aliharibu vyombo vyake vyote vya kuwasiliana na pepo na akafanya maendeleo ya kiroho haraka. Mwanamke huyo alibatizwa miezi michache baadaye.
“TAFADHALI SALI WANITEMBELEE!” Miaka kumi iliyopita Patrick alihamia Marekani kutoka Angola. Lakini aliendelea kuwasiliana na mama yake, Felicidade, kwa njia ya simu. Hivi majuzi, waliweza kuonana kupitia simu ya Intaneti yenye video. Walipokuwa wanazungumza, Patrick alimwona mtu fulani akiwa na mama yake na akataka kumjua. Felicidade, ambaye ni Shahidi wa Yehova, akasema: “Ni dada wa kutaniko letu ambaye amenitembelea.”
Patrick akauliza: “Kwa nini Mashahidi hawanitembelei? Nimekuwa hapa kwa miaka kumi, na hawajawahi kunitembelea. Tafadhali sali wanitembelee!”
Felicidade na dada aliyekuwa pamoja naye wakajibu hivi kwa mshangao: “Sawa, tutasali kwa ajili yako.”
Siku tatu tu baadaye, Shahidi mmoja wa Yehova alimtembelea Patrick. Alishangaa sana hivi kwamba akamuuliza mama yake iwapo alifanya mipango mtu fulani huko Marekani amtembelee. Hakuwa amefanya hivyo. Alikata kauli kuwa ziara hiyo ilikuwa jibu kutoka kwa Mungu na akakubali kujifunza Biblia. Mara moja, akaanza kuhudhuria mikutano yote. Alipomwona mama yake tena kupitia simu ya video, alimwonyesha kwa shangwe sura aliyokuwa akijifunza katika kitabu Biblia Inafundisha. Pia, alimweleza mama yake kuwa amenunua suti kwa ajili ya mikutano.
OMBI LA UBATIZO LENYE KUTATANISHA. Mwanzoni mwa kusanyiko la wilaya mjini Brazzaville, katika Jamhuri ya Kongo mwaka wa 2010, kijana anayeitwa Edvard alisema kuwa anataka kubatizwa. Alipoulizwa yeye ni wa kutaniko gani, alijibu: “Mossaka.” Kwa sababu hakukuwa Mashahidi katika kijiji hicho cha mbali, akina ndugu walishangaa na wakataka kujua jinsi alivyofikia hatua ya kutaka kubatizwa.
Edvard aliwaeleza wazee kwamba mwaka wa 2007, babu yake alijifunza naye broshua Anataka na vilevile sura 14 za kitabu Biblia Inafundisha mjini Brazzaville. Kisha Edvard akahamia Mossaka ili kuishi na wazazi wake. Kwa sababu hakukuwa na Mashahidi watendaji huko, Edvard alimwomba baba yake amsaidie kujifunza sehemu iliyosalia ya kitabu Biblia Inafundisha. Baba yake angeuliza maswali, na Edvard angejibu. Kwa njia hiyo Edvard alimaliza kujifunza kitabu hicho. Kisha akaona umuhimu wa kufundisha wengine mambo aliyokuwa amejifunza. Hivyo, mwezi wa Oktoba 2009, akaanza kuhubiri akiwa peke yake katika eneo la Mossaka akitumia broshua Anataka. Aliandika muda aliotumia katika utumishi wa shambani na kutuma ripoti zake kwa ukawaida kwa babu yake huko Brazzaville. Lakini, babu yake hakutoa ripoti hizo kwa kutaniko.
Baadaye, bila kujua lolote kuhusu Edvard, ofisi ya tawi iliwatuma mapainia wa pekee wa muda huko Mossaka kwa miezi mitatu. Siku mbili tu kabla waondoke huko, Daniel, mmoja wa mapainia hao wa pekee, alimwona Edvard akiongoza funzo la Biblia kwa kutumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Kwa hiyo, Daniel akamfikia Edvard na kuzungumza naye. Edvard akamwambia: “Ninahubiri. Mimi ni mhubiri. Unaweza kumuuliza baba yangu.” Daniel alikutana na baba ya Edvard ambaye alimhakikishia kuwa mambo aliyosema Edvard yalikuwa ya kweli. Mapainia hao wa pekee wa muda walitumia siku mbili zilizosalia kabla ya kumaliza mgawo ili kumzoeza Edvard katika huduma. Baada ya wao kuondoka, Edvard aliendelea kuhubiri kwa bidii, na kuongoza zaidi ya mafunzo kumi ya Biblia. Pia alijiweka wakfu kwa Yehova.
Wakiwa na habari hizo kumhusu, wazee wawili walikutana na Edvard siku ya Ijumaa ya kusanyiko lililotajwa hapo awali, na kupitia maswali ya wanaotaka kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Majibu yake sahihi yaliwashangaza. Wazee walipata habari kutoka kwa mapainia wa pekee kwamba mwenendo wa Edvard ni mzuri na tayari alikuwa amehubiri kwa miezi tisa. Kwa sababu hiyo, akawekwa rasmi kuwa mhubiri ambaye bado hajabatizwa. Kwa sababu kungekuwa na kusanyiko la wilaya la lugha ya Lingala mwishoni mwa juma lililofuata, wazee walifanya mipango ili Edvard apitie maswali ya ubatizo siku chache kabla ya kusanyiko. Ilionekana wazi kuwa anaielewa kweli vizuri na akabatizwa katika kusanyiko hilo mnamo Julai 2010. Kisha, juma moja tu baada ya kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, wazee wakatangaza kuwa Edvard ni ndugu aliyebatizwa.
Baada ya kubatizwa, alifanya upainia msaidizi kwa miezi miwili mjini Brazzaville. Wazee walifanya mipango ili ajifunze kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” halafu akarudi Mossaka. Hivi majuzi, painia wa pekee alitumwa katika eneo hilo. Mwezi wa Aprili, Edvard—ambaye wakati huo alikuwa painia msaidizi—pamoja na painia huyo wa pekee, waliwakaribisha watu 182 waliopendezwa kwenye Ukumbusho. Edvard ana mafunzo 16, na 7 kati yao wanahudhuria mikutano ambayo inaongozwa na ndugu hao wawili. Kufikia mwaka wa 2011, Edvard alikuwa na umri wa miaka 15.
AMERIKA
IDADI YA NCHI 55
IDADI YA WATU 941,265,091
IDADI YA WAHUBIRI 3,780,288
IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 4,139,793
‘HAIKUWA MAKOSA KUKUPIGIA.’ Sundie, dada anayeishi Marekani, alikuwa nyumbani simu ilipolia na mwanamke fulani akaomba kuongea na mtu ambaye Sundie hakumfahamu. Alimwambia mwanamke huyo aliyepiga simu kwamba amekosea. Mwanamke huyo akasema kwamba alikuwa na tatizo la kuona na mara nyingine hukosea anapopiga simu. Walianza kuongea, na mwanamke huyo akasema kuwa alitaka kuzungumza na mwanaye ili amweleze habari fulani zenye kuhuzunisha. Madaktari walikuwa wamegundua kwamba ana kansa. Mwanamke huyo alikuwa amehuzunika sana na alimlaumu Mungu kwa kuruhusu jambo hilo limpate. Sundie akatambua kwamba anapaswa kumweleza ujumbe wa Biblia. Baada ya kutoa sala fupi, Sundie alimsomea maandiko machache ili kumfariji na kumpa tumaini. Alimfafanulia kwamba Mungu ana jina na akamtia moyo alitumie anaposali, na ataje matatizo yake hususa. Mwanamke huyo akamshukuru Sundie kwa kumsikiliza na kumtia moyo. “Sidhani ilikuwa makosa kukupigia,” akasema.
Sundie alichukua anwani za mwanamke huyo, akamtumia rekodi ya kitabu Biblia Inafundisha, na akafanya mipango ili mwanamke huyo atembelewe na dada painia anayeishi katika eneo hilo. Sundie anasema, “Nafurahi kwamba Yehova ametufundisha mambo mengi sana kuhusu jinsi ya kuwafariji watu walio na matatizo ya kila aina.”
TRAKTI ILIJIBU SWALI LAO. Akina dada fulani huhubiri barabarani katika eneo fulani lenye hospitali nyingi nchini Puerto Riko. Mmoja wao aliwafikia wanaume wawili waliokuwa wakitembea haraka kuelekea hospitali moja. Alipoona jinsi walivyokuwa na haraka, aliwapa trakti Je, Una Roho Isiyoweza Kufa? Kwa kawaida, hatolei watu trakti hiyo anapohubiri barabarani, lakini hakuwa na trakti nyingine isipokuwa hiyo. Baadaye, wanaume hao walimfikia dada mwingine na kumweleza kuwa waliipokea trakti hiyo walipokuwa wanaenda kumwona mtu wa familia yao ambaye ni mgonjwa sana. Walisema kwamba kabla ya kupata trakti hiyo walikuwa wakijadiliana ikiwa roho huendelea kuishi baada ya kifo, na trakti hiyo ikajibu swali lao. Walisema kwamba iliwasaidia sana.
BARUA KWA YEHOVA. Joshua, mvulana mwenye umri wa miaka saba ni mwanafunzi wa shule nchini Marekani. Katika mwezi wa Desemba, yeye na wanafunzi wenzake waliambiwa na mwalimu wao wamwandikie barua Baba Krismasi. Joshua alipomwambia mwalimu kwa upole kwamba hatamwandikia Baba Krismasi, mwalimu alimwambia, “Andikia mtu yeyote.” Joshua akaamua kumwandikia Yehova. Aliandika hivi: “Asante kwa kutuahidi paradiso. Asante kwa Mwana wako, anayeitwa Yesu, ambaye alitoa uhai wake. Asante kwa kuumba vitu vinavyotufurahisha. Ninakupenda, Yehova Mungu.” Barua hiyo, pamoja na za wanafunzi wengine, ilichapishwa kwenye gazeti moja la habari.
WATU WA FAMILIA WALIPENDEZWA. Alejandro, ndugu anayeishi Kolombia, alitaka kuwahubiria watu wa familia yao. Kwa sababu wanaishi mbali, aliwaandikia barua na kuwatumia nakala kadhaa za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Pablo, mtu wa familia yao, aliposoma magazeti na maandiko yaliyomo, alitambua kwamba mafundisho ya Kanisa Katoliki ni ya uwongo. Akiwa na furaha nyingi, aliwaeleza watu wengine wa familia mambo aliyojifunza nao pia wakatambua kwamba ni ya kweli, na hivyo wakaacha kushirikiana na Kanisa Katoliki.
Muda si muda, watu 15 wa familia hiyo wakaanza kukutana kila usiku ili kujifunza Biblia wakitumia magazeti hayo. Kwa kuwa walitaka kujua zaidi, walitafuta Mashahidi katika miji iliyo karibu lakini hawakuwapata. Wakati huohuo, walianza kuwaeleza majirani wao mambo waliyokuwa wamejifunza. Hatimaye, wakatambua kwamba kuna Jumba la Ufalme katika mji uliokuwa umbali wa kilomita 80 hivi. Mara moja wakaenda huko na kuwaomba ndugu wawasaidie kujua mengi kuhusu Biblia.
Sasa painia wa kawaida huenda huko mara moja kwa juma ili kuongoza funzo moja la Biblia lenye watu 26, yaani, familia ya Alejandro na watu wengine 11. Wao hukodi gari ili wengi wao waweze kuhudhuria hotuba ya watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi.
JE, KWELI WALIENDA HUKO KIMAKOSA? Siku moja dada fulani alikuwa mgonjwa na hivyo akawatuma Mashahidi wengine wakajifunze Biblia pamoja na familia fulani katika eneo la watu wanaozungumza lugha ya Quichua nchini Ekuado. Ndugu hao hawakujua kabisa mahali ambapo familia hiyo iliishi na hivyo wakaulizia katika nyumba fulani. Familia hiyo iliwapokea ndugu hao kana kwamba walikuwa wakiwatarajia. Ni baada tu ya funzo ndipo ndugu hao walipogundua kwamba familia hiyo haikuwa imewahi kujifunza! Familia hiyo ilikuwa imefurahi sana kwamba wanaweza kujifunza Biblia na hivyo wakatenda kana kwamba wamekuwa wakijifunza Biblia kwa muda. Sasa wanaendelea kujifunza Biblia, na hata familia iliyokuwa inajifunza na yule dada inaendelea pia kujifunza.
KEKI YAONGOZA KWENYE USHAHIDI. Caleb ana umri wa miaka sita. Katika siku ya kwanza ya shule nchini Kanada, mmoja wa wanafunzi wenzake alikuwa anasherehekea siku yake ya kuzaliwa na hivyo Natalie, mama yake, akaleta keki kwa ajili ya darasa lote. Caleb alikataa keki hiyo kwa upole. Natalie akamuuliza ikiwa ana mizio yoyote inayosababishwa na chakula. Caleb akajibu, “Hapana, mimi namtumikia Yehova.”
Baada ya masomo, Natalie alimuuliza mama ya Caleb, “Wewe ni Shahidi wa Yehova?” Aliposema ndiyo, Natalie alisisimka. Alikuwa amejifunza Biblia pamoja na Mashahidi alipokuwa tineja, lakini akaacha kwa sababu ya upinzani kutoka kwa familia. Alipoulizwa ikiwa angependa kuanza kujifunza tena, Natalie alikubali.
HAYAKUWA MAPENZI YA MUNGU. Laly, anayeishi nchini Peru, alizaliwa akiwa kiziwi. Alipouliza kwa nini alizaliwa hivyo, mama yake alimwambia ni mapenzi ya Mungu. Jambo hilo lilimhuzunisha Laly na likamfanya amkasirikie Mungu. Aliwaza, ‘Kwa nini Mungu ananitesa?’
Miaka ilisonga na Laly akaolewa na mwanamume kiziwi. Mtoto wao wa kwanza alizaliwa akiwa na ugonjwa wa Down syndrome. Akiwa na wasiwasi na hasira alimuuliza mama yake, “Kwa nini mwana wangu amezaliwa na ugonjwa huu?” Mama yake akamwambia aende amuulize kasisi fulani. Kasisi huyo alimpa jibu lilelile alilopewa na mama yake, “Ni mapenzi ya Mungu.”
Akiwa ameghadhibika, Laly alisema: “Kwa nini Mungu ni mkatili hivyo? Nakubali kwamba mimi ni kiziwi na Mungu ameniadhibu kwa njia hiyo, lakini kwa nini amwadhibu mwanangu? Ni mtoto tu. Amefanya dhambi gani?” Kutoka wakati huo, Laly hakutaka kusikia chochote kumhusu Mungu na akaachana na kanisa.
Miaka michache baadaye, Shahidi wa Yehova anayejua lugha ya ishara alimtembelea na kumweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia. Laly alikataa kujifunza na akasema kwamba hamwamini Mungu. Kwa subira, dada huyo alimweleza Laly kuwa Mungu ambaye hakutaka kumjua anaitwa Yehova, na kwamba yuko tayari kumpa uwezo wa kusikia na kunena. Laly hakumwamini, na hivyo akamwambia athibitishe jambo hilo. Dada huyo alimsomea andiko la Isaya 35:5: “Macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.” Hilo lilimshangaza Laly, ambaye alikubali funzo la Biblia, akafanya maendeleo, na akabatizwa. Mwana wake huandamana naye kwenye mikutano yote na amejifunza lugha ya ishara. Anazidi kuthamini ahadi za Biblia na sasa yeye ni painia wa kawaida.
ASIA NA MASHARIKI YA KATI
IDADI YA NCHI 47
IDADI YA WATU 4,194,127,075
IDADI YA WAHUBIRI 664,650
IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 629,729
MASWALI MAWILI AMBAYO HAWAKUWEZA KUJIBU. Katika nchi moja ya Asia ambapo kazi yetu iko chini ya vizuizi, kijana mmoja mwenye umri wa miaka 24 alikubali kujifunza Biblia ili kuthibitisha kwamba mafundisho ya Mashahidi si ya kweli na kwamba mafundisho ya dini yake ya Katoliki ndiyo ya kweli. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli.
Familia yao ilipojua kwamba anajifunza Biblia, walimwita kwenye mkutano wa familia na kumshinikiza arudi katika Kanisa Katoliki. Kwa sababu kijana huyo alikataa, familia yao ilikusanya watu wote wa ukoo walio kijijini ili kumlazimisha aache imani yake mpya. Ingawa walimpiga, hakulegeza msimamo wake. Kisha wakamshtaki kwa kasisi, aliyempeleka mbele ya mwenyekiti wa baraza la kanisa. Kijana huyo aliliambia baraza hilo kwamba atarudi kanisani iwapo kasisi huyo atajibu maswali mawili: Jina la Mungu ni nani? Kwa nini kanisa linawaruhusu washiriki wake wale damu ilhali inakatazwa katika Biblia? Kasisi aliposhindwa kujibu maswali hayo, alimpiga kofi usoni kijana huyo, eti ili “kufukuza pepo iliyo ndani yake.” Kisha, mkutano huo ukaisha.
Baada ya hayo, familia ya kijana huyo ilitafuta marafiki wao wote wamlazimishe aipigie magoti sanamu ya Maria. Ijapokuwa walimpiga tena, alikataa kulegeza msimamo wake. Familia hiyo ikatafuta msichana mrembo amwambie angekubali aolewe naye iwapo angerudi kanisani. Kijana huyo akamwambia atarudi ikiwa yeye pia atajibu yale maswali mawili aliyouliza kasisi. Msichana huyo akaondoka na hakurudi tena. Hatimaye, baada ya kuzuiliwa kinyume cha mapenzi yake kwa miezi saba, kijana huyo alitoroka kijijini, akarudi mjini, ambapo aliwasiliana na akina ndugu. Mwezi mmoja baadaye, akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Mnamo Machi 2011, akabatizwa katika kusanyiko la mzunguko.
OFISA WA GEREZA AMTETEA DADA. Dada ambaye ni painia wa kawaida alikuwa anamtembelea mwana wake aliyefungwa gerezani nchini Korea Kusini kwa sababu ya msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Akiwa katika eneo la mapokezi, alimpa trakti mwanamume fulani aliyeketi kando yake. Mwanamume huyo akapaaza sauti, akimwambia, “Kwa nini ninyi watu wa hii dini ya uwongo mnahubiri hapa?” Watu wote karibu 30 au 40 waliokuwa hapo wakasikia kilichokuwa kinaendelea. Ofisa wa gereza akaingilia kati na kumkemea mwanamume huyo, akisema: “Hawa ndio watu wa dini ya kweli. Dini nyingine zote ni za uwongo. Kwa miaka mingi ambayo nimefanya kazi katika gereza hili, nimewachunguza watu hawa na nimekuja kutambua kwamba ni wao tu wanaoishi kulingana na mambo wanayofundishwa.” Mwanamume huyo mwenye matusi akanyamazishwa.
MAANDISHI UKUTANI. Harindra alipoanza kujifunza Biblia, alikuwa ameishi peke yake kwa miaka kumi kwa sababu alifanya kazi katika mji mkubwa nchini Nepal, ili aitegemeze familia yake iliyokuwa kijijini. Kwa kuwa hakujua kusoma na kuandika, Shahidi aliyemfundisha Biblia alitumia broshua Furahia Milele Maisha Duniani! Kwa kuwa broshua hiyo haikupatikana katika Kinepali wakati huo, walitumia ya Kiingereza. Siku moja, mke wa mwanamume huyo alikuja kumtembelea. Alishangaa kuona mume wake akijifunza broshua ya Kiingereza. Isitoshe, alikuwa ameacha kunywa pombe na hakuwa mjeuri. Alipojua kwamba Harindra alifanya mabadiliko hayo kwa sababu ya kujifunza Biblia, yeye pia alianza kujifunza na kuhudhuria mikutano kijijini mwao. Harindra alitamani kujifunza mengi kumhusu Yehova, hivyo akaamua kujifunza kusoma na kuandika. Alimwomba mwalimu wake wa Biblia amwandikie herufi za Kinepali kwenye vipande vya karatasi, ambavyo alibandika kwenye kuta za chumba chake hivi kwamba hakukuwa na nafasi iliyobaki. Kisha akafanya mazoezi ya kusoma maneno yote mapya na herufi mpya mpaka pole kwa pole akajua kusoma. Baada ya muda, alifanya mipango familia yake ihamie mjini ili wamwabudu Yehova pamoja. Katika kipindi cha miaka miwili, akabatizwa. Sasa, Harindra na familia yake wanahudhuria mikutano, naye hushughulikia migawo ya usomaji wa Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Anasema: “Maisha yetu yamekuwa mazuri zaidi na tunamshukuru Yehova kwa kutufundisha.”
ALIKATAA DOLA 200,000. Zarkhanum, anayeishi Azerbaijan, alijiingiza sana katika mambo ya ushirikina. Kwa miaka 15 alionwa kuwa ana nguvu zisizo za kawaida na angeweza kutabiri mambo ya wakati ujao. Pia, watu waliamini kwamba alikuwa na uwezo wa kuponya na wa kuondoa laana. Zarkhanum alijulikana sana, na kwa kuwa wateja wake wengi walikuwa maofisa wa ngazi za juu pamoja na wake zao, walilipa kati ya dola 2,000 na 4,000 za Marekani ili awasiliane na wafu kwa niaba yao. Hivyo, kutokana na kazi hiyo, alitajirika. Ingawa alikuwa na uwezo wa kuwasiliana na pepo, alihisi kwamba hana uhusiano mzuri na Mungu, na alikuwa na maswali mengi yaliyomsumbua. Ndoa yake ilivunjika, na hakuwa na kusudi maishani. Siku moja, alipokuwa akisali, alisikia mlango ukibishwa. Alifungua mlango, na dada wawili wakaanza kumhubiria. Zarkhanum aliguswa moyo aliposikia wakisema kuhusu kumpendeza Mungu si kwa maneno tu bali pia kwa matendo. Alijua watu wengi wa dini waliokuwa na mwenendo mbaya. Alijua pia kwamba anakosea kwa kuwasiliana na pepo. Akakubali kujifunza Biblia. Baada ya muda, alianza kusali akitumia jina la Yehova na akaona jinsi sala zake zilivyojibiwa. Hata hivyo, haikuwa rahisi kuacha mazoea yake—nyakati zote roho waovu walimsumbua na hata kumpiga. Hatimaye, kwa msaada wa Yehova, alijitenga na dini ya uwongo, akajinasua kutoka kwa uvutano wa roho waovu, na kuharibu vitu alivyotumia kuwasiliana na pepo.
Punde si punde, Zarkhanum akawa mhubiri mwenye bidii wa habari njema, na akabatizwa mnamo Mei 2011. Mara tu baada ya kubatizwa, akawa painia msaidizi. Hakuwa na tatizo kutimiza takwa la saa kwani hata kabla ya kubatizwa alikuwa akihubiri zaidi ya saa 70 kila mwezi, licha ya matatizo ya afya. Miezi miwili kabla ya kubatizwa, mke wa ofisa mmoja wa serikali aliahidi kumlipa dola 200,000 za Marekani ili amwondolee laana. Mwanamke huyo aliamini kwamba laana hiyo ilimletea ugonjwa uliosababisha akatwe mguu. Zarkhanum alikataa na badala yake, akawatuma Mashahidi wawili waende kumhubiria mwanamke huyo hospitalini. Huyo dada yetu mwenye bidii amekuwa akiwahubiria waliokuwa wateja wake, akiwaambia kwamba mambo aliyofanya awali yalikuwa mabaya machoni pa Mungu. Matokeo yakawa kwamba, mmoja wao, yule aliyemjulisha kwa yule mke wa ofisa wa serikali, alikubali kujifunza Biblia na akaanza kuhudhuria mikutano.
KUTOA USHAHIDI NDANI YA JELA. Nchini India, dada zetu wawili walikamatwa kwa sababu ya kuhubiri na wakafungwa jela kwa siku tano. Mmoja wao anaeleza: “Mara tu tulipotiwa kifungoni, maofisa wa polisi walitaka kujua sababu iliyofanya tutiwe mbaroni, na hivyo tukapata fursa ya kuwahubiria. Kwa kuwa tulipelekwa kwenye kituo cha polisi moja kwa moja kutoka utumishi wa shambani, tulikuwa na magazeti mengi na trakti nyingi. Tuliwahubiria wote na kuwaachia machapisho mengi. Tulitiana moyo, tukasali, na kusoma machapisho tuliyokuwa nayo.
“Baadaye, tulihamishiwa jela nyingine mjini. Mara moja, wafungwa wenzetu wakataka kujua ni kwa nini tulifungwa. Hilo lilitupa fursa ya kuwaeleza mambo tuliyohubiri na kujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Askari wa kike wa jela alisikia na kusema, ‘Mlikamatwa kwa kuhubiri, na sasa mnahubiri ndani ya jela!’” Sasa dada zetu wanapanga kuwarudia wafungwa waliopendezwa na kweli.
POLISI ALITAMBUA UPENDO WAO. Dada wawili walikuwa wanajitayarisha kuhubiri katika maduka fulani madogo mjini Bethlehemu. Ghafula, wanawake wawili wakaja kwao upesi na kuwauliza kwa Kihispania ikiwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Wanawake hao ni Mashahidi kutoka Mexico waliotembea Israeli wakiwa katika kikundi fulani cha watalii, na walitambua machapisho ambayo akina dada walikuwa wamebeba. Dada hao wanne walikumbatiana, wakapiga picha, na kubadilishana anwani. Baada ya hayo, wale dada kutoka Mexico walijiunga na watalii wenzao, na dada wenyeji wakaenda kuhubiri madukani.
Saa chache baadaye, ofisa mmoja wa polisi aliwafikia wale dada wenyeji na kuwauliza ikiwa wao ni Wahispania. Dada hao wakamwambia la. Ofisa huyo akasema kwamba alikuwa anawatazama wote wanne walipokutana na akafikiri kwamba lazima wawe marafiki wa muda mrefu au watu wa familia moja. Dada hao wakamweleza kuwa wote ni Mashahidi wa Yehova na kwamba hata wakati ambapo Mashahidi wa Yehova ni wa nchi nyingine au hawajawahi kukutana, wao huhisi kuwa kama familia kwa sababu wanapendana. Polisi huyo alivutiwa sana, akachukua machapisho na akataka kujua ni wapi angeweza kupata habari zaidi kuhusu Mashahidi. Dada hao wakafanya mipango atembelewe.
“HUENDA KUNA MTU FULANI ATAKAYESIKILIZA.” Yusuke ni kijana painia katika kikundi cha Kiingereza nchini Japani. Siku moja alipata habari kwamba meli fulani yenye abiria kutoka nchi mbalimbali itatia nanga asubuhi inayofuata. Hivyo, akaamka mapema, na licha ya mvua kubwa akaendesha gari kwa saa mbili hadi bandari ya Nagasaki. Akiwa amesimama peke yake kwenye gati akinyeshewa, abiria wengi waliokuwa wakishuka walifikiri kimakosa kwamba yeye ni mwelekezi na hivyo wakamfikia. Hali hiyo ilimwezesha Yusuke kuwaachia watu magazeti 70 na broshua 50 katika lugha mbalimbali kwa muda wa nusu saa.
Alirudi kwenye gari lake kuchukua machapisho zaidi, na aliporejea, alimwona abiria mmoja wa kiume akiwa amesimama peke yake. Yusuke alipomkaribia, kijana huyo alimuuliza kwa Kiingereza, “Wewe ni Shahidi wa Yehova?” Yusuke aliposema ndiyo, kijana huyo alianza kulia. Yusuke akampeleka mkahawani ili wazungumze.
Kijana huyo, Jason, alikuwa na umri wa miaka 21. Alieleza kwamba wazazi wake ni Mashahidi, na alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa mpaka alipokaribia umri wa miaka 20. Miezi sita kabla ya hapo, aliacha kushirikiana na Mashahidi wa Yehova na akaamua kutembelea nchi kadhaa za Asia, akifikiri kwamba hatakutana na Mashahidi. Hata hivyo, kwa sababu tumbo lake lilikuwa linamsokota, hakuweza kutoka ndani ya meli nchini Thailand, Vietnam, au Taiwan. Alishuka meli kwa mara ya kwanza nchini Japani, na mtu wa kwanza aliyezungumza naye ni Shahidi wa Yehova! Aliwaza hivi mara moja, ‘Siwezi kamwe kumkimbia Yehova,’ na jambo hilo ndilo lililofanya aanze kulia.
Wakiwa mkahawani, Yusuke alizungumzia mafungu fulani ya kitabu “Upendo wa Mungu” kumhakikishia kwamba Yehova bado anampenda. Yusuke alimsihi Jason asiliache tengenezo. Inasikitisha kwamba hawakuwa na muda mwingi pamoja. Jason aliondoka kwa meli hiyo jioni hiyohiyo kwenda Inchon, Korea Kusini, ambapo alipanga kutembelea maeneo mbalimbali kwa siku kadhaa.
Yusuke alifikiria kile ambacho angeweza kufanya ili kumsaidia Jason zaidi. Kisha akakumbuka ndugu fulani aliyekutana naye katika kusanyiko la kimataifa nchini Korea Kusini. Ndugu huyo aliishi Inchon na anazungumza Kiingereza. Usiku huo, Yusuke akampigia simu. Bila shaka, Jason hakuwa na habari kuhusu mawasiliano hayo. Jason aliposhuka meli asubuhi iliyofuata, aliona bango lenye maandishi “Karibu Korea, Jason!” Bango hilo lilikuwa limebebwa na Mashahidi watano waliokuwa wakitabasamu. Jason akavunja mipango yake yote na kutumia muda huo na akina ndugu. Aliguswa sana aliposikia kuhusu vijana kama yeye wanaofungwa gerezani kwa sababu ya imani yao. Pia, alihudhuria Ukumbusho huko.
Jason alirudi Marekani, akawa mhubiri mwenye bidii tena, na akawaomba wazee wajifunze naye mara nne kwa juma. Alimaliza kujifunza kitabu Biblia Inafundisha na “Upendo wa Mungu” na akastahili kubatizwa. Alibatizwa siku 107 baada ya Yusuke kuzungumza naye mara ya kwanza. Akafanya upainia msaidizi mwezi uliofuata.
Yusuke anakumbuka kwamba asubuhi hiyo yenye baridi na mvua, alitamani sana kwenda Nagasaki, ingawa hakuwa na yeyote wa kuandamana naye. Aliwaza, “Huenda kuna mtu fulani atakayesikiliza.”
ULAYA
IDADI YA NCHI 47
IDADI YA WATU 736,505,919
IDADI YA WAHUBIRI 1,589,052
IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 843,405
WALIPATA KITU CHA PEKEE SANA. Ani, kutoka Bulgaria, alienda nchini Uholanzi kufanya kazi kwa miezi michache. Siku moja, alihisi amevunjika moyo na akasimama kando ya barabara na kumwomba Mungu amtumie mtu wa kanisa lao. Alipokuwa akisali, dada wawili walisimama ili kumhubiria. Ani aliona hilo kuwa jibu la sala yake, kwa hiyo akawasikiliza na akaanza kuhudhuria mikutano. Ingawa hakuelewa mambo yaliyozungumziwa kwenye mikutano, alijionea wazi upendo miongoni mwa Mashahidi. Hilo lilikuwa tofauti na mfarakano ulio katika kanisa lao nchini Bulgaria, na akasadiki kwamba amepata kitu cha pekee sana. Aliporudi Bulgaria, dada aliyemfunza aliambatana naye ili kumsaidia kuwatafuta Mashahidi mjini Sofia. Hilo lilimvutia Ani zaidi, na kufanya aone kwamba ameipata dini ya kweli.
Punde baadaye, Ani na mume wake, Ivo, walianza kujifunza na kuhudhuria mikutano. Wakati wa funzo lao, watu wengine walijiunga nao ili kusikiliza mambo waliyojifunza. Assen, mmoja wa watu hao, alikuwa kasisi wa kikundi kimoja cha kidini. Alikuwa ameenda kwa Ani na Ivo ili kuwathibitishia kwamba Mashahidi wa Yehova hawafundishi kweli, lakini akagundua sivyo. Aliuliza maswali ya Biblia yenye kina. Alielezwa kuhusu mpango wa kujifunza Biblia na akakubali yeye na familia yake wafundishwe. Kwa muda fulani, Assen aliendelea kuongoza mikutano ya kidini na kikundi chake, ingawa sasa alifundisha kweli ambazo alijifunza katika kitabu Biblia Inafundisha. Muda si muda, Dencho, shemasi wa kikundi hicho, alitaka kujifunza Biblia. Muda mfupi baadaye, familia tatu pia za kikundi hicho zikaanza kujifunza Biblia. Kwa kuwa wengi katika kikundi hicho walikuwa wanajifunza Biblia, waliamua kuachana na kikundi hicho, na wakaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Dencho akawa mhubiri na akaanza kuwafundisha Biblia baadhi ya rafiki zake. Hivyo, kutokana na Ani kuhubiriwa nchini Uholanzi, watu 30 hivi wameanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano.
ALISOMA MAANDIKO YANAYOHUSU NDOA TU. Ndugu fulani na mke wake katika Jamhuri ya Cheki walijifunza Biblia katika Jumba la Ufalme pamoja na wenzi fulani wa ndoa kutoka Mongolia. Ingawa ndugu huyo na mke wake walijitahidi kujifunza Kimongolia, bado ilikuwa vigumu kuwasiliana katika lugha hiyo. Hata hivyo, wenzi hao wachanga kutoka Mongolia walikubali kweli ya Biblia kwa unyenyekevu na subira. Jioni moja, mwanamke huyo alifika mikutanoni bila mume wake. Alisema kwamba alitaka kumwacha mume wake kwa sababu hawaelewani. Dakika chache baadaye, mume akawasili, lakini hata hakumtazama mkewe. Ilionekana wazi kwamba walikuwa na tatizo kubwa. Ndugu alimpeleka mume huyo katika chumba cha maktaba ya Jumba la Ufalme ili wazungumze. Lakini kwa sababu hakufahamu Kimongolia vizuri, hakuelewa tatizo la wenzi hao, kwa hiyo hangetoa shauri hususa. Hivyo basi, aliamua kusoma maandiko tu. Alisoma maandiko yote aliyokumbuka kuhusu ndoa na mawasiliano. Mwanamume huyo alionekana kuguswa moyo na kila andiko. Ghafula, akakimbia hadi alipokuwa mke wake na kumbusu. Walipokuwa wanaondoka kwenye Jumba la Ufalme, mume huyo alisisitiza kubeba kipochi cha mke wake kwa kuwa alijifunza kwamba anapaswa kumsaidia.
Siku iliyofuata, wenzi hao walionekana kama maarusi wapya na wakiwa wenye furaha walieleza jinsi wanavyomshukuru Yehova kwa mashauri ya kimaandiko na yenye hekima waliyopata kuhusu ndoa. Baadaye, walirudi Mongolia kuwatunza watoto wao wawili. Familia hiyo inaishi katika mji usio na kutaniko. Mke alibatizwa mwezi wa Oktoba, na mume anafanya maendeleo ili astahili kubatizwa.
“MBONA ALIFANYA HIVYO?” Olha, dada painia, alimhubiria dereva wa gari la kusafirisha chakula nchini Ukrainia. Alimwuliza, “Je, kuna mtu yeyote tunayeweza kumwamini?”
“Hapana,” dereva huyo akajibu. “Mke wangu aliniacha na akaenda na mwana wetu mwenye umri wa miaka miwili. Alitaka nini zaidi? Nilifanya kazi kwa bidii kila siku—yote niliyofanya yalikuwa kwa faida yake. Alipotaka pete, nilimpa! Alipotaka viatu, nilimpa. Alipotaka mkufu, nilimpa. Alipata kila kitu alichotaka, mbona alifanya hivyo?”
Dada huyo alimwuliza mwanamume huyo kwa upole ikiwa alitumia wakati pamoja na mke wake na mwana wao. Mwanamume huyo akajibu: “Nitapata wapi wakati wa kuwa pamoja nao ilhali ninapaswa kufanya kazi hadi saa sita usiku? Mimi huanza kazi saa kumi asubuhi. Ninafanya kazi hata Jumamosi na Jumapili.”
Olha alimwonyesha gazeti la Amkeni! la Oktoba 2009 ambalo lilikuwa na mfululizo wa makala yenye kichwa “Siri ya Kufanikiwa kwa Familia.” Alimwonyesha siri ya kwanza, “Kutanguliza Mambo Yanayofaa.” Baada ya kupitia habari hizo, mwanamume huyo alipendezwa na akasema: “Nilidhani kwamba kuwa na pesa ndio siri ya furaha ya familia na vitu vingine vyote si muhimu. Sasa naona kwamba furaha ya familia haitegemei pesa. Naona kile ambacho mke wangu anahitaji.”
Juma moja baadaye, Olha alikutana na dereva huyo aliyemwambia kuwa alilisoma gazeti hilo, akafikiria sana, na kuona mambo mengi kwa njia tofauti. Alimtafuta mkewe na wakapatana. Olha akampa kitabu Furaha ya Familia. Juma lililofuata, Olha aliona gari hilohilo lakini lilikuwa na dereva mwingine. Dereva huyo mpya alisema kwamba dereva wa zamani alikuwa ameacha kazi na kuhamia eneo lingine pamoja na familia yake. Hata hivyo, alimwachia Olha ujumbe huu: “Nataka kukushukuru sana wewe, Olha, na Mungu wako, Yehova, kwa sababu ulinisaidia kuiokoa familia yangu. Nikikutana na Mashahidi wa Yehova, bila shaka nitazungumza nao.”
ALITAKA ISHARA KUTOKA KWA MUNGU. Kijana mmoja nchini Latvia alivutiwa na ujumbe wa Biblia alipohubiriwa na Mashahidi miaka 15 iliyopita. Alijifunza mara kwa mara, lakini hakuamini kwamba Biblia—ambayo ni kitabu “tu”—ingemsaidia kumjua Mungu. Alitarajia kwamba Mungu angejifunua kwake binafsi, labda kwa njia isiyo ya kawaida au ya kimuujiza. Hivyo, akaacha kujifunza na baadaye hakuwasiliana hata kidogo na Mashahidi. Miaka kadhaa baadaye, alipambana na matatizo makubwa na akamwomba Mungu amsaidie. Bado hakupata muujiza lakini kupitia dirishani, aliwaona dada wawili wakihubiri. Aliposali tena majuma machache baadaye, aliwaona dada walewale tena kupitia dirishani. Juma moja baadaye, alisali na kwa mara ya tatu akawaona dada hao wakihubiri. Akakata kauli kwamba hiyo ilikuwa ishara kutoka kwa Mungu! Alikimbia nje na kuwaambia dada hao waliokuwa wameshangaa kwamba anataka kuanza kujifunza Biblia tena baada ya kuacha kwa miaka mingi. Hatimaye, alipata nguvu za kutatua matatizo yake na akamkaribia Mungu. Jinsi gani? Kwa msaada wa Biblia! Alibatizwa katika kusanyiko la wilaya la mwaka wa 2010.
HATA VYUNGU VIDOGO VINA MASIKIO. Nchini Denmark, msemo huo humaanisha kwamba watoto hujifunza mengi kuliko inavyodhaniwa wanaposikiliza mazungumzo ya watu wazima. Miaka 16 hivi iliyopita, dada mmoja wa Denmark ambaye mume wake pia ni Shahidi, alijifunza Biblia pamoja na mwanamke aliyekuwa na watoto watatu wavulana. Mara nyingi watoto hao waliandamana na mama yao alipoenda kujifunza nyumbani kwa dada huyo. Mwanamke huyo aliacha kujifunza wakati Ronnie, mwana mdogo zaidi alipokuwa na umri wa miaka minane. Alipoendelea kukua, Ronnie alikabili matatizo mengi. Hata hivyo, siku moja mwaka wa 2008, akiwa na umri wa miaka 22, aliona magazeti yetu nyumbani kwa mama yake na akawa na hamu ya kuwatembelea Mashahidi waliojifunza na mama yake hapo awali. Dakika 15 baadaye, mlango wa wenzi hao Mashahidi ulibishwa, na mume alipofungua, Ronnie aliingia. Ilichukua muda kumtambua Ronnie, lakini alifurahi kumwona tena. Ronnie alipewa kitabu Biblia Inafundisha na akakubali kujifunza Biblia. Funzo likaendelea vizuri. Kwa kuwa Ronnie alipenda sana michezo ya kompyuta, ambayo baadhi yake ilihusu uchawi na jeuri, mara nyingi alihusianisha mambo aliyojifunza na michezo hiyo. Lakini Mashahidi hao wakamfundisha kwamba michezo ya kompyuta haipaswi kuwa msingi wa kuelewa mambo ya kiroho. Ronnie alielewa na akasema: “Tafadhali unikomeshe ninapoanza kuongea juu ya upuuzi huo!” Tangu wakati huo, amefanya maendeleo. Kijana huyo alisikia kweli kwa mara ya kwanza akiwa tu ‘chungu kidogo chenye masikio’ mama yake alipokuwa anajifunza. Sasa ni mhubiri ambaye hajabatizwa.
FARAJA KUTOKA KWA MAANDIKO. Katika eneo moja la makaburini nchini Uingereza, ndugu mmoja alimwona mwanamume aliyekuwa amepiga magoti kando ya kaburi akilia. Ndugu huyo akaomba aketi naye. Mwanamume huyo anayeitwa Alf, akakubali. Alf alisema: “Binti yangu amekufa. Alikuwa na umri wa miaka 42 tu. Sasa mke wangu na binti yangu wamezikwa hapa.” Alikuwa ameiomba serikali impe msaada wa mshauri lakini akaambiwa angojee miezi mitatu. “Mimi ni tajiri na nina biashara nyingi,” akasema Alf, “lakini hivyo vyote ni bure bila familia yangu. Ninaweza kutoa mali yangu yote ili niwapate tena.” Alf alisema kwamba anamwamini Mungu, anaiheshimu Biblia, anaenda kanisani, lakini hajapata majibu yenye kuridhisha. Huko kanisani, alipoomba kufarijiwa aliambiwa awashe mshumaa au aandike ujumbe kwenye karatasi na kuining’niza juu ya mti. “Lakini karatasi haiwezi kutoshea ujumbe ninaotaka kusema,” akasema. Ndugu huyo alimfariji kwa Maandiko. Sasa Alf anajifunza Biblia.
OCEANIA
IDADI YA NCHI 29
IDADI YA WATU 38,162,658
IDADI YA WAHUBIRI 94,309
IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 58,465
WALIMWALIKA MUME AJIUNGE NAO. Ndugu mmoja nchini New Zealand anaripoti kwamba alipokuwa akimpeleka mke wake kujifunza na mama fulani, walitambua kwamba mume wa mwanamke huyo alikuwa nyumbani, hivyo wakaamua kumwalika katika funzo. Mume huyo alikubali, na wakapanga kwamba wakati ujao watajifunza siku ambayo mume huyo anapatikana. Mwanamume huyo na mke wake walikubali kuhudhuria mkutano wa Jumapili, ambapo walipokelewa kwa uchangamfu na wakafurahia mambo waliyojifunza. Jumapili iliyofuata, mume huyo alitoa maelezo wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi. Makala ya funzo ilizungumzia ibada ya familia, na huyo mume akataka kujua jinsi anavyoweza kujifunza pamoja na mke wake na mwana wao mwenye umri wa miaka minne. Pia, alionyesha kwamba anataka kutumia mambo mengine aliyojifunza mkutanoni. Wenzi hao wanaendelea kujifunza, kuhudhuria mikutano, na kufanya maendeleo ya kiroho. Ndugu huyo anasema: “Tunashukuru kama nini kwamba tuliamua kumwalika mume huyo katika funzo!”
KUADHIMISHA UKUMBUSHO KATIKA KISIWA CHA MBALI. Kisiwa cha Reao, chenye wakaaji 362 tu, kiko chini ya Kutaniko la Vaiete, ambalo ni mojawapo ya makutaniko 18 nchini Tahiti. Kisiwa hicho kiko karibu kilomita 1,350 mashariki ya Tahiti. Mashahidi hawakuwa wametembelea kisiwa hicho kwa miaka 30 na maadhimisho ya Ukumbusho hayajawahi kufanywa katika kisiwa hicho cha mbali. Manoah, mwangalizi wa utumishi wa Kutaniko la Vaiete, alitaka kufanya mipango ili kikundi kidogo kiende kuhubiri katika kisiwa hicho wakati wa juma la Ukumbusho na kufanya maadhimisho hayo. Lakini, ili kwenda huko yeye na mke wake walihitaji faranga 65,000 hivi (dola 740 za Marekani) kwa ajili ya nauli, kiasi kilichozidi pesa walizokuwa nazo. Hata hivyo, alipata malipo ya ziada kutoka kazini, faranga 65,000! Mara moja wakakata kauli kwamba Yehova anabariki mpango wao. Mwishowe, wahubiri saba walienda Reao, na watu 47 wakahudhuria Ukumbusho. Sasa, wahubiri nchini Tahiti hujifunza Biblia kwa simu pamoja na watu wanaopendezwa huko Reao.
HAKUNA WAKATI WA KIAMSHA-KINYWA. Habari nyingine kama hiyo inatoka Vanuatu, ambapo kutaniko moja linasaidia kikundi cha wahubiri 11 katika kisiwa cha mbali cha Ambrym. Wazee wa kutaniko hilo waliwaomba wahubiri wenye uzoefu wafikirie kwenda Ambrym kwa siku chache ili kusaidia kikundi hicho kabla ya Ukumbusho. Marinette, painia mwenye uzoefu ambaye ni mwalimu aliyestaafu, alikubali mwito huo. Yeye, pamoja na wengine kadhaa, wakaamua kwenda huko wakiwa na lengo la kuanzisha mafunzo ya Biblia. Baada ya kuhubiri kwa siku chache tu, alishangaa kuona kwamba haikuwa rahisi kuondoka katika makao yake. Marinette akumbuka: “Sikuwa hata na wakati wa kuoga au kula kiamsha-kinywa kwa sababu watu walikuwa tayari wanangoja nje wakiwa wamepiga foleni ili wajifunze Biblia. Nilihubiri siku nzima bila kwenda popote! Niliongoza mafunzo ya Biblia 31 juma hilo.” Wahubiri hao walikaa huko kwa juma moja wakihubiri kwa bidii, na watu 158 wakahudhuria Ukumbusho. Hawakutaka kuondoka. Marinette alisema: “Kwa nini tuondoke mahali hapa ilhali kuna watu wengi walio na kiu ya kweli za Biblia?” Ofisi ya tawi imepanga kutuma mapainia wa pekee wa muda ili kuwasaidia watu wenye kupendezwa katika eneo hilo.
MWALIMU MKUU AKUBALI MAONI YAO. Katika shule moja ya sekondari kwenye Visiwa vya Solomon, wanafunzi hulazimishwa kusimama na kuimba nyimbo za Kanisa la Kiinjili la South Seas. Dada wawili vijana walimwomba mwalimu mkuu awape ruhusa ya kutoimba, kwa kuwa nyimbo za aina hiyo zinachafua dhamiri zao. Mwalimu mkuu aliwashukuru kwa kuzungumza naye kwa heshima na akawaambia kwamba si lazima waimbe lakini wanaweza kuketi kama watoto wengine Mashahidi.
Kisha akawauliza ikiwa mtu fulani kutoka kutanikoni anaweza kutembelea na kumweleza mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova na elimu. Mmishonari mmoja alimtembelea na kuzungumza naye kwa karibu saa moja na nusu kuhusu imani yetu na vilevile matatizo yanayowakumba vijana. Mwalimu huyo alisema kwamba yeye hufurahia kusoma magazeti ya Amkeni! na huyaacha mengine katika chumba cha walimu. Mmishonari huyo alipompa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, aliomba nakala 16 kwa ajili ya walimu na nakala 367 kwa ajili ya wanafunzi. Kwa jumla, walipelekewa vitabu 400.
Kwa sababu ya ujasiri wa hao dada wawili, ushahidi mzuri ulitolewa na mambo mengi mazuri yamesemwa kuhusu kitabu hicho. Msichana mmoja, ambaye wazazi wake walikuwa wameachana hivi karibuni, alisema kwamba alihitaji kitabu hicho ili kukabiliana na matatizo. Dada hao wawili wanafanya upainia msaidizi mfululizo, naye mwalimu mkuu hupokea magazeti kwa ukawaida kutoka kwao.
MWAMINIFU LICHA YA UPINZANI. Kwingineko katika Visiwa vya Solomon, mmishonari mmoja alijifunza Biblia na mwanamke tutakayemwita Lisa. Alifanya maendeleo licha ya kwamba alilazimika kutembea kwa zaidi ya saa mbili kwenda kwenye Jumba la Ufalme akiwa na wavulana wake mapacha na wasichana wake wachanga wawili. Pia, alivumilia upinzani mkali kutoka kwa mume wake. Alimpiga na kuteketeza nguo zake za mikutano, Biblia, na machapisho ya Biblia. Isitoshe, alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwingine. Hata hivyo, licha ya yote hayo, Lisa alibatizwa na anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.
Mwaka uliopita, mume wa Lisa akichochewa na jinsi ambavyo Lisa alikuwa anamtendea licha ya yote aliyomfanyia, alimwacha yule mwanamke mwingine na akaomba afundishwe Biblia. Kama unavyoweza kuwazia, dada yetu, Lisa, anafurahia sana badiliko hilo. Isitoshe, kikundi kimoja kilianzishwa karibu na kwake, na hivyo kurahisisha mambo hata zaidi kwa kuwa anatembea kwa muda unaopungua saa moja tu kufika mikutanoni. Kwa msaada wa mume wake, ameweza pia kufanya upainia msaidizi.
[Blabu katika ukurasa wa 66]
“Kwa nini Mungu ni mkatili hivyo? . . . kwa nini amwadhibu mwanangu? Ni mtoto tu. Amefanya dhambi gani?”
[Blabu katika ukurasa wa 68]
Aliliambia baraza la kanisa atarudi kanisani iwapo kasisi atajibu maswali mawili
[Blabu katika ukurasa wa 72]
“Mlikamatwa kwa kuhubiri, na sasa mnahubiri ndani ya jela!”
[Picha katika ukurasa wa 84]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Tahiti → → → Kilomita 1,350 → → → Reao
[Picha katika ukurasa wa 56]
Juu: Kuongoza funzo la Biblia katika Jamhuri ya Kongo (ona ukurasa wa 59)
[Picha katika ukurasa wa 61]
Edvard (kulia) pamoja na Daniel katika soko fulani
[Picha katika ukurasa wa 64]
Samaniego, Nariño, Kolombia
[Picha katika ukurasa wa 67]
Sasa machapisho ya lugha ya Ishara yanapatikana katika lugha 59
São Paulo, Brazili