Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Yehova alisifiwa pia katika kampeni ya majuma matatu ya ulimwenguni pote ya kuwakaribisha watu kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya “Ukombozi Unakaribia!” yaliyofanywa katika nchi 155 hivi. Mamilioni ya wahubiri wa ujumbe wa Ufalme katika makutaniko zaidi ya 99,000 walishiriki katika kampeni hiyo ya pekee. Ndugu wa Halmashauri moja ya Kusanyiko waliandika hivi: “Baadhi ya wanafunzi wa Biblia walichochewa kuanza kuhubiri, na baadhi ya ndugu wasiotenda walitiwa moyo wawe watendaji tena.” Ndugu mmoja ambaye alikuwa asiyetenda kwa miaka 35 alipewa mwaliko huo mlangoni na hajakosa hata mkutano mmoja tangu wakati huo! Yafuatayo ni baadhi ya mambo yaliyoonwa katika nchi mbalimbali.

      Ufaransa

      Mwanamke Mkatoliki na mume wake waliona karatasi ya kuwakaribisha watu kwenye kusanyiko nyumbani kwa mtu wa jamaa, na walivutiwa na maswali yaliyozushwa. Walihudhuria kusanyiko pamoja na watoto wao watatu. Walipofika, mkaribishaji mmoja aliwasalimu kwa uchangamfu, akawapa Biblia, na kuwaelekeza wakae karibu na familia ya Mashahidi wanaoishi umbali wa kilomita tatu tu kutoka kwao! Watu wa familia hizo mbili walishinda pamoja siku hiyo na wakafanya mpango wa kujifunza Biblia. Katika juma lililofuata kusanyiko, familia hiyo inayopendezwa ilihudhuria mkutano wa kutaniko wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko.

      India

      Mwimbaji mashuhuri anayeitwa Sunita alienda Kanada kuwatumbuiza watu. Alipokuwa huko Kanada alitembelewa na Mashahidi waliomwalika kwenye mkutano wa Kipunjabi. Alihudhuria mkutano huo na alivutiwa hasa kwa sababu Biblia ilitumiwa sana. Alipopewa karatasi ya kutangaza kusanyiko, alifuta mara moja mipango ya maonyesho ya mwisho wa juma hilo ili aweze kuhudhuria siku zote tatu. Sunita hakujutia uamuzi wake. Mwishoni mwa siku ya kwanza alisema, “Hii ndiyo kweli.” Aliporudi India, alienda kwenye Jumba la Ufalme lililo katika eneo lao pamoja na mamake, mwanawe, mpwa wake, na rafiki mmoja. Makasisi wa kanisa lake la zamani walipomuuliza kuhusu jambo hilo aliwaambia kwamba ameazimia kuwa Shahidi wa Yehova. Hata aliwaambia kwamba ingefaa wao pia waende kwenye Jumba la Ufalme!

      Serbia

      Mwanamke Mchina ambaye tutamwita Mei Li anaishi Belgrade. Alianza kusoma Mnara wa Mlinzi katika lugha yake mwaka wa 2006. Mei Li alipopokea karatasi ya kutangaza kusanyiko la Kichina jijini Leipzig, Ujerumani, aliazimia kuhudhuria ijapokuwa Leipzig liko umbali wa kilomita 1,000 kutoka Belgrade. Alipata kibali cha kukaa siku tatu nchini Ujerumani na akasafiri kwa ndege hadi Munich, kisha kwa gari-moshi hadi Leipzig. Safari hiyo ilimgharimu mishahara ya miezi miwili. Mambo aliyojifunza kusanyikoni na kwa kuzungumza na wengine waliohudhuria yalimgusa sana. Mei Li aliporudi Belgrade, yeye na mamake walikubali kujifunza Biblia na wakaanza kuhudhuria funzo la kitabu la Kichina.

      Marekani

      Ndugu wa Halmashauri moja ya Kusanyiko waliandika hivi: “Wageni walikuwapo siku zote tatu. Mwanamke mmoja aliyehudhuria, alipata karatasi ya kutangaza kusanyiko siku moja baada ya kumwomba Mungu amwongoze maishani mwake. Ili kuhudhuria, alisafiri kwa gari lake kwa muda wa saa mbili Jumamosi (Siku ya Posho) na Jumapili (Siku ya Yenga) pia, na akakubali kujifunza Biblia.” Ripoti hiyo inaongeza: “Mtu mmoja alitimua mbio ili amfikie ndugu aliyekuwa amemwachia mwana wa mtu huyo karatasi ya kutangaza kusanyiko. Ndugu hakujua yule mtu anataka nini, lakini alifurahi mtu huyo alipomwomba arudi nyumbani kwake ili wajadiliane. Mtu huyo aliuliza maswali mengi huku akishika Biblia mkononi, na funzo likaanzishwa.”

      Ndugu mmoja alimpa mtu fulani karatasi ya kutangaza kusanyiko kwenye kiwanja cha ujenzi. Mtu huyo aliuliza: “Je, ninaweza kuwaambia wengine kuhusu mwaliko huu?”

      “Bila shaka!” ndugu huyo akamjibu. Lakini hakujua kwamba mtu huyo anaongoza kipindi chake mwenyewe cha redio kila Jumamosi asubuhi. Kama alivyoahidi, mtu huyo aliwaambia wengine kuhusu mwaliko huo. Alifanya hivyo kwa kusoma karatasi ya kutangaza kusanyiko katika kipindi chake cha redio! Hilo lilifanya watu wengi watake kujua zaidi kuhusu karatasi hiyo.

      Morgan mwenye umri wa miaka 12 ni painia-msaidizi. Juma moja kabla ya kampeni hiyo ya pekee alikutana na mtu aliyeuliza maswali mengi kuhusu Biblia. Morgan alimwalika kusikiliza hotuba ya watu wote katika Jumba la Ufalme. Mtu huyo alikuja ijapokuwa ilimbidi kuondoka mara moja ili ahudhurie mazishi ya mtu wa jamaa. Kampeni ya pekee ilipoanza, Morgan alimpa mtu huyo anayependezwa karatasi ya kutangaza kusanyiko. Mtu huyo alisema: “Bila shaka nitahudhuria Jumamosi na Jumapili, lakini sina budi kwenda kazini Ijumaa (Siku ya 5).” Kisha akamuuliza Morgan jinsi Mashahidi wanavyoshughulikia hali kama hizo. Morgan akamjibu: “Kwa kawaida wanaomba ruhusa siku hiyo, lakini nyakati nyingine wanalazimika kuacha kazi.”

      Morgan alipomrudia, mtu huyo alisema kwamba alimwomba mwajiri wake apewe ruhusa siku ya Ijumaa na kumwambia kwamba kama hangepata ruhusa, angeacha kazi. Mwajiri wake alimwambia kwamba yeye ni mfanyakazi bora, kwa hiyo alipata ruhusa siku ya Ijumaa, na Alhamisi (Siku ya 4) pia ili ajitayarishe.

      Mtu huyo alihudhuria siku zote tatu lakini hakuja peke yake. Watu 8 wa familia yake waliandamana naye, na pia marafiki 12 pamoja na familia zao—jumla ya watu 35! Alipomwambia Morgan kwamba atakuja na watu 30 hivi, Morgan alisema: “Siwezi kuhifadhi viti vingi hivyo.”

      Mtu huyo alisema: “Si hoja, tutaketi popote pale.” Bila shaka wote walipata viti.

  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      Haukuwa Mwaliko Tu

      Karatasi ya kutangaza kusanyiko ilikuwa na sehemu ya kuomba funzo la Biblia, kitabu cha Biblia Inafundisha, au vyote viwili. Punde si punde ofisi za tawi kotekote duniani zilianza kupokea maombi hayo. Ofisi ya tawi ya Marekani inaripoti kwamba ilipokea maombi 2,000 hivi ya kitabu hicho, na maombi 300 ya funzo la Biblia. Bila shaka, jitihada za ndugu na dada zetu za kugawa karatasi hiyo ya kutangaza kusanyiko zitaendelea kuwa na matokeo mazuri.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki