Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb07 kur. 6-30
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
  • 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “KITABU HICHO . . . KINAFUNDISHA KAMA YESU ALIVYOFUNDISHA”
  • JITIHADA ZA KUHUBIRI KATIKA LUGHA YA KIGENI
  • KUTAFSIRI KWA AJILI YA VIZIWI
  • MAMBO YA KISHERIA
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb07 kur. 6-30

Matukio Muhimu ya mwaka uliopita

“NITAMSIFU Yehova muda wote wa maisha yangu. Nitampigia Mungu wangu muziki maadamu nipo.” (Zab. 146:2) Mtunga-zaburi angefurahi sana kama angeishi katika siku zetu na kuona Yehova akisifiwa kuliko nyakati nyingine zozote! Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinachangia sifa hiyo. Kitabu hicho kinafikia mioyo ya wengi wanaotaka kujua kweli kumhusu Mungu.—Mdo. 17:27.

Ili Yehova asifiwe hata zaidi, ofisi nyingi za tawi zimepanga masomo ya lugha ili wahubiri na mapainia waweze kuwahubiria watu wengi zaidi habari njema. Huenda ukatiwa moyo kupanua utumishi wako kwa kujifunza lugha ya kigeni.

Yehova alisifiwa pia katika kampeni ya majuma matatu ya ulimwenguni pote ya kuwakaribisha watu kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya “Ukombozi Unakaribia!” yaliyofanywa katika nchi 155 hivi. Mamilioni ya wahubiri wa ujumbe wa Ufalme katika makutaniko zaidi ya 99,000 walishiriki katika kampeni hiyo ya pekee. Ndugu wa Halmashauri moja ya Kusanyiko waliandika hivi: “Baadhi ya wanafunzi wa Biblia walichochewa kuanza kuhubiri, na baadhi ya ndugu wasiotenda walitiwa moyo wawe watendaji tena.” Ndugu mmoja ambaye alikuwa asiyetenda kwa miaka 35 alipewa mwaliko huo mlangoni na hajakosa hata mkutano mmoja tangu wakati huo! Yafuatayo ni baadhi ya mambo yaliyoonwa katika nchi mbalimbali.

Ufaransa

Mwanamke Mkatoliki na mume wake waliona karatasi ya kuwakaribisha watu kwenye kusanyiko nyumbani kwa mtu wa jamaa, na walivutiwa na maswali yaliyozushwa. Walihudhuria kusanyiko pamoja na watoto wao watatu. Walipofika, mkaribishaji mmoja aliwasalimu kwa uchangamfu, akawapa Biblia, na kuwaelekeza wakae karibu na familia ya Mashahidi wanaoishi umbali wa kilomita tatu tu kutoka kwao! Watu wa familia hizo mbili walishinda pamoja siku hiyo na wakafanya mpango wa kujifunza Biblia. Katika juma lililofuata kusanyiko, familia hiyo inayopendezwa ilihudhuria mkutano wa kutaniko wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko.

India

Mwimbaji mashuhuri anayeitwa Sunita alienda Kanada kuwatumbuiza watu. Alipokuwa huko Kanada alitembelewa na Mashahidi waliomwalika kwenye mkutano wa Kipunjabi. Alihudhuria mkutano huo na alivutiwa hasa kwa sababu Biblia ilitumiwa sana. Alipopewa karatasi ya kutangaza kusanyiko, alifuta mara moja mipango ya maonyesho ya mwisho wa juma hilo ili aweze kuhudhuria siku zote tatu. Sunita hakujutia uamuzi wake. Mwishoni mwa siku ya kwanza alisema, “Hii ndiyo kweli.” Aliporudi India, alienda kwenye Jumba la Ufalme lililo katika eneo lao pamoja na mamake, mwanawe, mpwa wake, na rafiki mmoja. Makasisi wa kanisa lake la zamani walipomuuliza kuhusu jambo hilo aliwaambia kwamba ameazimia kuwa Shahidi wa Yehova. Hata aliwaambia kwamba ingefaa wao pia waende kwenye Jumba la Ufalme!

Serbia

Mwanamke Mchina ambaye tutamwita Mei Li anaishi Belgrade. Alianza kusoma Mnara wa Mlinzi katika lugha yake mwaka wa 2006. Mei Li alipopokea karatasi ya kutangaza kusanyiko la Kichina jijini Leipzig, Ujerumani, aliazimia kuhudhuria ijapokuwa Leipzig liko umbali wa kilomita 1,000 kutoka Belgrade. Alipata kibali cha kukaa siku tatu nchini Ujerumani na akasafiri kwa ndege hadi Munich, kisha kwa gari-moshi hadi Leipzig. Safari hiyo ilimgharimu mishahara ya miezi miwili. Mambo aliyojifunza kusanyikoni na kwa kuzungumza na wengine waliohudhuria yalimgusa sana. Mei Li aliporudi Belgrade, yeye na mamake walikubali kujifunza Biblia na wakaanza kuhudhuria funzo la kitabu la Kichina.

Marekani

Ndugu wa Halmashauri moja ya Kusanyiko waliandika hivi: “Wageni walikuwapo siku zote tatu. Mwanamke mmoja aliyehudhuria, alipata karatasi ya kutangaza kusanyiko siku moja baada ya kumwomba Mungu amwongoze maishani mwake. Ili kuhudhuria, alisafiri kwa gari lake kwa muda wa saa mbili Jumamosi (Siku ya Posho) na Jumapili (Siku ya Yenga) pia, na akakubali kujifunza Biblia.” Ripoti hiyo inaongeza: “Mtu mmoja alitimua mbio ili amfikie ndugu aliyekuwa amemwachia mwana wa mtu huyo karatasi ya kutangaza kusanyiko. Ndugu hakujua yule mtu anataka nini, lakini alifurahi mtu huyo alipomwomba arudi nyumbani kwake ili wajadiliane. Mtu huyo aliuliza maswali mengi huku akishika Biblia mkononi, na funzo likaanzishwa.”

Ndugu mmoja alimpa mtu fulani karatasi ya kutangaza kusanyiko kwenye kiwanja cha ujenzi. Mtu huyo aliuliza: “Je, ninaweza kuwaambia wengine kuhusu mwaliko huu?”

“Bila shaka!” ndugu huyo akamjibu. Lakini hakujua kwamba mtu huyo anaongoza kipindi chake mwenyewe cha redio kila Jumamosi asubuhi. Kama alivyoahidi, mtu huyo aliwaambia wengine kuhusu mwaliko huo. Alifanya hivyo kwa kusoma karatasi ya kutangaza kusanyiko katika kipindi chake cha redio! Hilo lilifanya watu wengi watake kujua zaidi kuhusu karatasi hiyo.

Morgan mwenye umri wa miaka 12 ni painia-msaidizi. Juma moja kabla ya kampeni hiyo ya pekee alikutana na mtu aliyeuliza maswali mengi kuhusu Biblia. Morgan alimwalika kusikiliza hotuba ya watu wote katika Jumba la Ufalme. Mtu huyo alikuja ijapokuwa ilimbidi kuondoka mara moja ili ahudhurie mazishi ya mtu wa jamaa. Kampeni ya pekee ilipoanza, Morgan alimpa mtu huyo anayependezwa karatasi ya kutangaza kusanyiko. Mtu huyo alisema: “Bila shaka nitahudhuria Jumamosi na Jumapili, lakini sina budi kwenda kazini Ijumaa (Siku ya 5).” Kisha akamuuliza Morgan jinsi Mashahidi wanavyoshughulikia hali kama hizo. Morgan akamjibu: “Kwa kawaida wanaomba ruhusa siku hiyo, lakini nyakati nyingine wanalazimika kuacha kazi.”

Morgan alipomrudia, mtu huyo alisema kwamba alimwomba mwajiri wake apewe ruhusa siku ya Ijumaa na kumwambia kwamba kama hangepata ruhusa, angeacha kazi. Mwajiri wake alimwambia kwamba yeye ni mfanyakazi bora, kwa hiyo alipata ruhusa siku ya Ijumaa, na Alhamisi (Siku ya 4) pia ili ajitayarishe.

Mtu huyo alihudhuria siku zote tatu lakini hakuja peke yake. Watu 8 wa familia yake waliandamana naye, na pia marafiki 12 pamoja na familia zao—jumla ya watu 35! Alipomwambia Morgan kwamba atakuja na watu 30 hivi, Morgan alisema: “Siwezi kuhifadhi viti vingi hivyo.”

Mtu huyo alisema: “Si hoja, tutaketi popote pale.” Bila shaka wote walipata viti.

“KITABU HICHO . . . KINAFUNDISHA KAMA YESU ALIVYOFUNDISHA”

Ripoti mbalimbali zinaonyesha kwamba kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinasaidia sana katika kazi ya kuhubiri. Mwanafunzi mmoja wa Biblia alisema: “Kinafumbua macho na kinalisha moyo na akili.” Mwangalizi mmoja wa wilaya anasema: “Kitabu hicho kinavutia sana kwa sababu kinafundisha kama Yesu alivyofundisha. Kinaeleza mambo kifupi, moja kwa moja, na kwa njia rahisi kuelewa, na pia kinachangamsha moyo sana.” Fikiria mambo yaliyoonwa yafuatayo.

Australia

Ndugu fulani aliyekuwa akifanya ukarabati nyumbani kwa mwanamke mgonjwa, alimweleza kuhusu tumaini la Ufalme. Siku chache baadaye alipomtembelea pamoja na dada painia, mwanamke huyo aliuliza kuhusu siku za mwisho. Mashahidi hao walizungumza naye sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha yenye kichwa, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?” Mwanamke huyo alistaajabishwa na mambo aliyojifunza katika Biblia, na kusema: “Kanisa langu halijanifundisha lolote.”

Ndugu huyo aliandika: “Tuliporudi tulijifunza sura ya 1, ‘Ukweli Kumhusu Mungu’ na sehemu ya nyongeza inayoeleza kwa nini jina la Mungu limeondolewa katika Biblia fulani. Mwanamke huyo aliposoma katika utangulizi wa Biblia yake kwamba watafsiri walitumia neno ‘Bwana’ badala ya jina ‘Yehova’ alikasirika kwa sababu alikuwa ameambiwa kwamba Biblia yake ni tafsiri nzuri. Mwanamke huyo amesema anataka kuhudhuria mikutano ya Kikristo.

Ubelgiji

Dada anayeitwa Ingrid alikutana na mwanamke Mwafrika aliyewachukia Mashahidi wa Yehova. Ingrid alipomwonyesha kwa fadhili kitabu Biblia Inafundisha, mtazamo wake ulibadilika kwa sababu alikuwa na hamu ya kuelewa Neno la Mungu. Hata alikubali kujifunza Biblia, lakini akasisitiza wasome maandiko yote. Mwanamke huyo huhudhuria mikutano, anatoa maelezo mara nyingi, na anataka kuwa mhubiri wa ujumbe wa Ufalme.

Brazili

Paulo alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi alipokuwa kijana. Alipokuwa na miaka 16, mama na baba yake walitengana. Ili kumsaidia mama yake, Paulo alijiunga na kikundi kinachopiga muziki wa kienyeji. Muda si muda alianza kunywa kupindukia na kuishi maisha yasiyo ya maadili. Hata hivyo, hakusahau mambo yote aliyokuwa amejifunza. Kwa mfano, alisikia vibaya alipolazimika kufanya maonyesho ya muziki kwenye kituo cha uchawi. Alitambua kwamba maisha yake hayana kusudi. Ndugu mmoja kijana alipomwonyesha Paulo kitabu Biblia Inafundisha katika mwaka wa 2005, alianza kujifunza tena. Muda mfupi baadaye aliacha kikundi hicho cha wanamuziki na sasa anahudhuria mikutano ya Kikristo.

Uingereza

Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, Marilyn alikutana na mama fulani anayeitwa Melanie, aliyetaka kujua mengi zaidi kuhusu Biblia. Marilyn alimwachia trakti na kumwahidi atarudi. Baada ya kumkosa mara kadhaa, hatimaye Marilyn alimpata Melanie nyumbani. Marilyn anasema: “Niliamua kuanzisha funzo moja kwa moja kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha, na funzo hilo la Biblia linaendelea vizuri. Kabla tu ya Krismasi, Melanie alinishangaza aliponiambia kwamba hii ni mara ya mwisho kwake kuleta mti wa Krismasi nyumbani. Alikuwa amesoma kitabu hicho kimbele na kujua kweli kuhusu Krismasi.”

Kolombia

Consuelo alimwomba msimamizi wake ruhusa ili ahudhurie kusanyiko la wilaya. Consuelo aliporudi kazini, msimamizi wake alimuuliza kuhusu kusanyiko, na walikuwa na mazungumzo mazuri. Consuelo alipomwonyesha kitabu Biblia Inafundisha, msimamizi huyo aliomba kukisoma. Siku mbili baadaye alimrudishia Consuelo kitabu hicho na kusema ni kizuri. “Kitabu hiki hakikusudiwi kusomwa tu bali kwa ajili ya funzo,” Consuelo alimwambia, kisha akamwonyesha jinsi funzo linavyofanywa. Msimamizi akamuuliza: “Unamaanisha ninaweza kujifunza kitabu hiki?” Bila shaka walipanga kujifunza, na muda si muda, mwanamke huyo akaanza kuwahubiria watu wa familia yake na marafiki wake. Alianza pia kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na nyakati nyingine aliandamana na mwanawe na nyanya yake.

Guyana

Joseph, ambaye ni painia wa kawaida, alianza kujifunza kitabu Biblia Inafundisha pamoja na mtu aliyekuwa amekutana na Mashahidi miaka kadhaa iliyopita katika mji mkuu, Georgetown. Joseph aliporudi ili wajifunze kwa mara ya kwanza, mtu huyo alikuwa akimngojea pamoja na wanawe wawili na wake zao. Wao pia walipata kitabu hicho. Juma lililofuata yule mtu alisema kwamba mwalimu wa shule ameomba nakala yake ya kitabu Biblia Inafundisha na alikuwa amekisoma. “Kitabu hiki kina mafundisho ya kweli,” mwalimu huyo alisema na akajiunga na funzo hilo. Jirani mmoja alisikia kuhusu funzo hilo naye pia akaomba kuhudhuria. Wakati huo Joseph aliwaalika wote kwenye Ukumbusho. Ijapokuwa yule mtu ambaye alianza kujifunza kwanza hakuweza kuhudhuria kwa sababu ya ugonjwa, familia yake ilihudhuria Ukumbusho, na vilevile yule mwalimu na familia yake. Wote wanafanya maendeleo.

Poland

Lucjan alipokuwa akihubiri barabarani alikutana na Jan mwenye umri wa miaka 50. Jan alikuwa rafiki yake walipokuwa shuleni na hakuwa amemwona kwa miaka mingi. Katika mazungumzo yao, yaliyohusisha pia mambo fulani katika kitabu Biblia Inafundisha, Jan alieleza kwamba baada ya kufiwa na mkewe alianza kuvuta sigara na kuwa mlevi sugu. Lucjan anasema: “Mimi na rafiki wangu mmoja tulipomtembelea siku chache baadaye, Jan alikuwa akitungojea. Aliomba tujifunze kitabu Biblia Inafundisha, na tukaanza mara moja.” Kweli inafikia moyo wake, na anajitahidi kuacha mazoea sugu na lugha chafu.

Hispania

Kwa nini mtaalamu wa damu alimshauri mgonjwa aliyeshuka moyo ajifunze Biblia? Ndugu wawili wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali walimtembelea mtaalamu huyo na kumwachia kitabu Biblia Inafundisha. Mtaalamu huyo na mgonjwa wake mmoja walikuwa wameshuka moyo kwa sababu wote ni wagonjwa sana. Alivutiwa na kitabu Biblia Inafundisha na akamwonyesha mgonjwa huyo kitabu hicho na kumhakikishia kwamba wote wawili watapata tumaini kama watajifunza pamoja na Mashahidi. Baada ya siku chache, dada painia aliyekuwa akitoa ushahidi barabarani alikutana na mwanamke huyo, na akakubali kujifunza. Yule mtaalamu wa damu alianza pia kujifunza na tayari anahudhuria mikutano ya Kikristo.

Zambia

Goliath ni mkuu wa kijiji aliye na watoto kumi, na hapo awali alikuwa na wake wawili. Yeye na familia yake wamefanya maendeleo makubwa ya kiroho. Goliath alianza kufanya mabadiliko muda mfupi baada ya kusoma kitabu Biblia Inafundisha. Yeye na watu wa familia yake walianza kuhudhuria mikutano katika mwezi wa Januari (Mwezi wa 1) 2006, na katika mwezi wa Februari (Mwezi wa 2) alimwomba mke wake wa pili aondoke, kisha akafunga ndoa na mke wake wa kwanza. (Mt. 19:4-6; 1 Tim. 3:2) Katika mwezi wa Machi (Mwezi wa 3) aliacha cheo chake kijijini, na katika mwezi wa Aprili (Mwezi wa 4) yeye na mkewe Esther, wakawa wahubiri ambao hawajabatizwa. Yaelekea mashetani hawakufurahia uamuzi wao wa kumtumikia Yehova nao wakaanza kumsumbua Esther. Hata hivyo, aliwapinga kama andiko la Yakobo 4:7 linavyohimiza. Esther alisema hivi kuhusu jambo hilo: “Sasa mimi na mume wangu ni watu huru.”

JITIHADA ZA KUHUBIRI KATIKA LUGHA YA KIGENI

Katika nchi kadhaa kuna wahamiaji wengi wanaoongea lugha ya kigeni, na wengi wao wanatoka nchi ambako kazi ya kuhubiri imezuiwa. Kwa hiyo, ‘mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji umefunguliwa,’ na ndugu na dada wengi wanaingia kupitia mlango huo kwa kujifunza lugha ya kigeni. (1 Kor. 16:9) Isitoshe, katika nchi fulani kuna makabila ya wenyeji wanaoongea lugha ambazo wenyeji wengine katika nchi hizo hawazijui. Wahubiri wa ujumbe wa Ufalme wanajifunza lugha hizo pia na wanapata matokeo mazuri.

Ili kuendeleza kazi ya kuwahubiria watu hao, ofisi kadhaa za tawi zimepanga masomo ya lugha. Wanafunzi wanajua lugha haraka kwa sababu masomo hayo yanakazia hali ambazo wanakabili katika utumishi. Elisa anayejifunza Kialbania anasema hivi: “Masomo hayo yanamsaidia mtu kujihusisha kabisa na lugha anayojifunza.”

Ubelgiji

Ofisi ya tawi inaripoti kwamba wahubiri 300 wamehudhuria madarasa 17 ya lugha kumi tofauti-tofauti. Umri wa wanafunzi ni kati ya miaka 9 na 71. Enora anasema: “Nimejifunza Kituruki na ninawapenda watu hao.” Annelies anayejifunza Kichina alihojiwa na mtoa habari wa kituo cha televisheni cha kitaifa. Mtoa habari huyo alitaka kutayarisha kipindi kumhusu mtu anayefanya jambo jipya maishani. Ni wazi kwamba Annelies alimweleza kwa nini anajifunza Kichina. Mtoa habari huyo aliporudi mwaka mmoja baadaye, Annelies alimweleza kuhusu matokeo mazuri aliyopata katika utumishi wake. Yaelekea yule mtoa habari alivutiwa, kwa sababu kipindi hicho kilionyeshwa kotekote nchini wakati ambapo wengi hutazama televisheni. Annelies alionyeshwa akihojiwa na pia akiwa kwenye kituo cha basi akihubiri katika Kichina.

Uholanzi

Ofisi ya tawi iliandika hivi: “Kwa sababu ya masomo hayo ya lugha, tuna wahubiri wengi zaidi wanaoweza kuwahubiria watu wanaoongea lugha za kigeni na ndugu wengi wanaoweza kusaidia makutaniko hayo.” Nchini Uholanzi kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wanaojua Kirumania. Ofisi ya tawi ilikuwa imepanga mikutano mara mojamoja, lakini ndugu mmoja tu ndiye aliyeweza kuiongoza, naye alikuwa na afya mbaya. Sasa ndugu wengine wanaweza kusaidia kwa sababu wamehudhuria masomo ya lugha. Ndugu mmoja huongoza funzo la kitabu kila juma, mwingine huongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi, na mwingine tayari anaweza kutafsiri hotuba za Kiholanzi.

Hispania

Tangu mwaka wa 2003, ofisi ya tawi imepanga madarasa 48 ya lugha kumi tofauti-tofauti, na kwa sababu hiyo idadi ya mafunzo ya Biblia imeongezeka sana hadi 50,000 hivi. Juan na Mari Paz, mume na mke ambao ni mapainia wa pekee, walialikwa nyumbani kwa familia kutoka Rumania. Punde si punde, watu 16 walikuja kusikiliza, akiwemo Mario mwenye umri wa miaka 19 aliyekuwa makini kuliko wote. Ijapokuwa hakujua Kihispania na mapainia hao hawakujua Kirumania, alichukua kitabu Anataka katika lugha yake. Juma lililofuata, Mario aliomba kujifunza Biblia na akahudhuria kusanyiko la siku ya pekee ingawa hakuelewa mengi. Baada ya majuma machache alikuwa akihudhuria mikutano yote ya kutaniko, na alianza kutoa maelezo mafupi katika Kihispania. Alianza kuvalia nadhifu na kuwaeleza wengine kuhusu mambo aliyojifunza. Sasa anaongoza funzo la Biblia pamoja na mume na mke Warumania, ambao wanafanya maendeleo.

Wakati uo huo, Juan na Mari walianza kujifunza Kirumania, na muda si mrefu walikuwa wakiongoza mafunzo 30 katika lugha hiyo! Pia, Juan anaongoza funzo la kitabu katika Kirumania. Baada ya funzo, wahubiri kumi hujifunza Kirumania na mwalimu wao ni yule kijana aliyekuwa wa kwanza kujifunza Biblia, yaani, Mario.

Marekani

Wakaaji zaidi ya milioni 50 nchini humo hawaongei Kiingereza nyumbani kwao. Kuna makutaniko 3,052 na vikundi 53 vya Kihispania nchini humo vyenye wahubiri 254,000. Isitoshe, kuna makutaniko na vikundi 690 vya lugha nyingine vyenye wahubiri 26,000. Ili kuwahubiria watu wengi wanaoongea lugha za kigeni, ofisi ya tawi ilipanga madarasa 450 ya masomo ya lugha 29 tofauti-tofauti. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema hivi: “Katika miaka miwili iliyopita makutaniko manne yalianzishwa katika mzunguko wetu. Matatu kati ya hayo yalianzishwa kwa sababu ya masomo ya Kifaransa.”

Ndugu mmoja aliyejifunza Kihispania anasema hivi: “Tamaa yetu imetimizwa. Kwa miaka mingi mimi na mke wangu tulitamani kuwa wamishonari, lakini tulikuwa na watoto wawili. Sasa watoto wetu ni watu wazima nami nimestaafu. Kwa hiyo, miezi mitatu iliyopita, mimi na mke wangu tulijiunga na kutaniko la Kihispania, na tayari tumepewa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Pia, tuna marudio mengi na huenda tukaweza kuripoti mafunzo matano ya Biblia. Sisi tuna umri wa miaka 67 na 64, na tumetambua kwamba hakuna aliye mzee sana asiweze kujifunza lugha ya kigeni.”

Ikiwa hakuna ongezeko la wanafunzi katika eneo lenu, huenda ukajifunza lugha nyingine hali zikikuruhusu, na hatimaye kuhamia eneo ambako watu wanaongea lugha hiyo. Fikiria jambo hilo na usali kulihusu, kwa sababu hatua kama hiyo inaweza kuwa na matokeo mazuri sana na kufanya utumishi wako uwe wenye kufurahisha zaidi.

Ujerumani

Masomo ya lugha yalianzishwa miaka 30 iliyopita katika nchi hiyo, na wanafunzi zaidi ya 1,000 wamejifunza lugha tisa tofauti-tofauti, kama vile Kialbania na lugha ya Vietnam. Dada mmoja alisema: “Masomo hayo ni bora sana kuliko masomo yangu ya chuo kikuu.” Wanafunzi wanaweza kuwafikia watu mioyo wanapohubiri kwa sababu wanajifunza pia jinsi watu kutoka nchi nyingine wanavyofikiri.

Paula aliye na miaka 82 alianza kujifunza lugha ya Vietnam naye husafiri kilomita 150 hivi ili ahudhurie mikutano. Anasema hivi: “Mimi sina kipawa cha kujifunza lugha, lakini ninamshukuru Yehova kwa kunipa shangwe kubwa sana.” Paula alijifunza na familia moja kutoka Vietnam. Mume ndiye aliyependezwa na kweli kwanza kisha mke wake. Sasa wote wawili wamebatizwa.

Baada ya kubatizwa, mume huyo na mke wake pamoja na binti yao, walifanikiwa kutimiza tamaa yao ya kumtumikia Yehova nchini kwao. Walijenga nyumba iliyo na nafasi ya kutosha ya kufanyia mikutano ya kutaniko. Mume ni mzee wa kutaniko na painia-msaidizi. Mke wake ni painia wa kawaida. Paula alifurahi sana alipopokea barua kutoka kwa familia hiyo iliyoeleza kwamba baba alimbatiza binti yake. Binti huyo alimwandikia Paula hivi: “‘Nyanya’ Mpendwa. Ninatamani kukuona. Ninakufikiria mara nyingi. Wewe ni nyanya yangu wa kiroho milele. Ninakupenda.” Wazia jinsi jambo hilo lilivyomtia moyo dada yetu mpendwa aliyejifunza lugha ngumu akiwa mzee!

Kanada

Tangu mwaka wa 2002, wanafunzi 554 wamehudhuria madarasa 31 katika majiji kumi. Paul mwenye miguu iliyopooza, ni mzee wa kutaniko, na alikuwa akijifunza Kichina cha Mandarin. Muuguzi wake Linda ni Mchina. Kwa sababu kanisa lake lilikuwa limewachafulia Mashahidi jina, Linda hakutaka kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Siku moja Paul alimwomba ampeleke kwenye Jumba la Ufalme ili asikilize hotuba ya watu wote katika Kichina cha Mandarin. Alikubali kumpeleka lakini akajitenga na wengine na hakuonyesha dalili ya kupendezwa. Muda mfupi baadaye alimpeleka Paul kwenye funzo la kitabu. Wakati huo Linda ambaye ni mzazi alisikiliza kwa makini kwa sababu funzo lilihusu maisha ya familia. Baada ya funzo, dada painia alijitolea kujifunza pamoja naye, na Linda akakubali. Alifanya maendeleo ya kiroho haraka na sasa yeye ni dada yetu.

Nchini Kanada kuna makabila mengi ya wenyeji wanaozungumza lugha mbalimbali. Miaka michache iliyopita dada anayeitwa Carma, ambaye anaishi katika eneo la kabila la Blackfoot pamoja na wazazi wake, alimhubiria mtu ambaye ni wa kabila hilo. Carma anasema: “Nilipojaribu kumhubiria katika Kiingereza alikataa kunisikiliza. Alisema kwamba mimi ni mfuasi wa dini ya Wazungu na Biblia ni kitabu cha Wazungu. Carma aliwaza: ‘Iwapo ningejua lugha ya kabila la Blackfoot na utamaduni wao, labda angenisikiliza.’” Carma aliazimia kujifunza lugha hiyo na baadaye akawasaidia wahubiri 23 waliohudhuria masomo ya lugha ya kabila hilo.

Mwanafunzi mmoja alimhubiria mume na mke wa kabila hilo waliokuwa wanamtembelea mwana wao aliyelazwa hospitalini. Mume na mke hao walivutiwa kwa sababu dada huyo alijitahidi kujifunza lugha yao na wakamweleza mahali wanapoishi. Carma alitambua kwamba mume huyo ndiye yule mtu aliyekutana naye mwaka mmoja uliopita! Basi aliandamana na yule dada alipofanya ziara ya kurudia. Carma anasema: “Walisikiliza na pia kuamini mafundisho ya Biblia. Dada huyo aliwapa Biblia na kitabu cha kujifunzia Biblia. Mwanamke huyo alishika vitabu hivyo kifuani akitokwa na machozi, na mume wake alionyesha kibali chake kwa kuinamisha kichwa. Kwa sasa mwanamke huyo anajifunza huku mume wake akisikiliza.”

Ili kuonyesha matokeo mazuri ya masomo ya lugha hiyo, ofisi ya tawi inaripoti kwamba watu 34 wa kabila la Blackfoot walihudhuria Ukumbusho wa mwaka wa 2006 uliofanywa katika lugha yao.

Italia

Wahubiri 7,200 wamejifunza lugha 18 tofauti-tofauti. Mmoja wa wanafunzi hao alikutana na Samson anayetoka nchi ambako kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme imepigwa marufuku. Alipokuwa na miaka 24, Samson alifunga safari ambayo aliiita safari ya tumaini. Kwanza alivuka jangwa, kisha akasafiri kwa meli hadi Italia. Samson alipofika Italia alikutana na yule mwanafunzi ambaye alikuwa amejifunza lugha yake. Samson alisikiliza kwa makini na hata akahudhuria mkutano wa Kikristo. Baada ya kupoteana kwa miezi kumi walikutana tena, na yule ndugu akaanza kujifunza Biblia pamoja na Samson. Walijifunza katika mikahawa, vituo vya gari-moshi vya chini ya ardhi, na maegesho ya magari. Baada ya kuhudhuria Ukumbusho, Samson alianza kufanya mabadiliko maishani, hata alivunja uhusiano na mwanamke aliyekuwa ameishi naye kwa mwaka mmoja. Sasa yeye ni ndugu yetu.

Nikaragua

Katika mwaka wa 2006 ndugu walifaulu kwa mara ya kwanza kuwahubiria kikamili watu wa kabila la Mayangna. Watu wengi wa kabila hilo ni waumini wa Kanisa la Moravia. Hilo ni kanisa la Kiprotestanti, na katika miji mingi kasisi wa kanisa hilo anatumika kama meya ijapokuwa hajawekwa rasmi. Mmoja wa makasisi hao alivunja desturi na kuwaruhusu mapainia Hamilton na Abner kukaa mjini mwake. Hata aliwatafutia makao na akawapa Biblia kamili katika lugha ya Mayangna. Ndugu hao walijifunza lugha hiyo na muda si muda walikuwa na mafunzo kadhaa ya Biblia. Hata waliweza kutafsiri hotuba katika ziara ya kwanza ya mwangalizi wa mzunguko wakati watu 13 walipohudhuria mkutano, na pia wakati watu 90 walipohudhuria Ukumbusho. Ndugu hao walitafsiri pia nyimbo mbili zilizoteuliwa kwa ajili ya Ukumbusho, na wote waliimba kwa shangwe.

Kwa sababu watu wengi wanapendezwa, ofisi ya tawi ilikubali ndugu hao wabaki katika eneo hilo. Lakini, je, wenye mamlaka walikubali? Katika mkutano wa baraza la mji, watu fulani waliwashtaki Mashahidi wa Yehova kwamba wao ni mpinga-Kristo. Hata hivyo, mtu mmoja aliyekuwa amejifunza na Mashahidi, na ambaye ni mwanachama wa baraza hilo, alisema: “Tangu vijana hao walipofika mjini kwetu, sijawahi kumwona mtu yeyote akiwapikia wala kuwafulia nguo. Wanajishughulikia wenyewe. Hata wamejifunza lugha yetu! Isitoshe, wametufundisha mambo ya Biblia ambayo hatukujua. Ikiwa watu hao hawangekuwa wametumwa na Mungu, hakika wangekuwa tayari wamechoka.” Ndugu hao waliruhusiwa kubaki huko.

KUTAFSIRI KWA AJILI YA VIZIWI

Marekani

Seti ya DVD yenye Injili ya Mathayo (The Good News According to Matthew) ilitolewa katika Lugha ya Ishara ya Marekani mwaka wa 2006. Sasa wahubiri viziwi wanaweza kusoma sura nzima-nzima za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yao. Mzee mmoja wa kutaniko ambaye ni kiziwi alisema hivi: “Hii ni barua bora ambayo nimepokea kutoka kwa Yehova.” Mwingine alisema: “Sasa ninaweza kuona jinsi kila mstari unavyopatana na muktadha.” Dada mmoja aliye na lengo la kusoma sura moja kila siku aliandika hivi: “Ninajikuta niko karibu kuchelewa kufanya mambo mengine, kwa sababu nimesoma sura nne au tano na kusahau wakati kabisa!”

Brazili

Kuna ongezeko kubwa sana miongoni mwa watu wanaotumia lugha ya ishara. Kwa sasa kuna makutaniko 232 ya lugha ya ishara katika wilaya moja yenye mizunguko kumi. Kuna wazee wa kutaniko na watumishi wa huduma zaidi ya 1,000 katika makutaniko ya lugha ya ishara. Mapainia wa pekee 146 hutumia lugha ya ishara, na 8 kati yao ni viziwi. Kati ya wale wazee wa kutaniko na watumishi wa huduma, zaidi ya 100 wanasema kwamba vitabu ambavyo tengenezo la Yehova linaandaa katika lugha ya ishara vimewasaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Vitabu hivyo ni Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, Endeleeni Kukesha!, Mungu Anataka Tufanye Nini?, Mnara wa Mlinzi, na vinginevyo. Kuanzia mwaka wa 2006, ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilirekebishwa kwa ajili ya makutaniko ya lugha ya ishara. Ratiba hiyo ina marejeo ya vitabu vya lugha hiyo pekee.

Mwalimu mmoja mwenye umri wa miaka 30 alisema hivi: “Nimehudhuria ibada katika makanisa mbalimbali, lakini sasa ninaona kwamba ni Mashahidi wa Yehova tu wanaoweza kuwafundisha viziwi Biblia.” Alisema kwamba yale ambayo kanisa lake linafundisha hayapatani na akili wala hayamsaidii mtu. Licha ya upinzani wa marafiki wake ameazimia kuendelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Yehova na aendelee kuwavuta watu wanyoofu kama hao kwa Mwana wake!—Yoh. 6:44; Ufu. 14:6.

MAMBO YA KISHERIA

Eritrea

Amri ya rais ilifuta uraia wa Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1994 kwa sababu hawakupiga kura katika uchaguzi wa kitaifa. Ndugu zetu walilemewa sana kifedha kwa sababu ya uamuzi huo, na mamia wakakimbilia nchi nyingine. Wengine walibaki, kutia ndani familia zenye watoto wa shule. Wanapokuwa katika darasa la tisa, wanafunzi wote, wavulana kwa wasichana, huandikishwa kufanya mazoezi ya kijeshi. Kwa hiyo, vijana wengi wameamua kuacha shule baada ya darasa la nane.

Kuhudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri ni hatari. Katika visa fulani wote waliohudhuria mkutano walikamatwa na kufungwa! Hata hivyo, ndugu na dada zetu wenye moyo mkuu wanaendelea ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Mdo. 5:29) Kwa sasa, ndugu na dada 31 wamefungwa, akiwemo ndugu mmoja mwenye miaka 73 ambaye ni raia wa Uholanzi. Wengine wamefungwa kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Ndugu watatu, Paulos Eyassu, Isaac Mogos, na Negede Teklemariam, wamekuwa gerezani tangu mwaka wa 1994.

Ufaransa

Februari 25, 2005, malalamiko kuhusu kodi iliyotozwa isivyo haki juu ya Shirika la Mashahidi wa Yehova yaliwasilishwa kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Watu zaidi ya 874,000 walitia sahihi hati ya kulalamikia utozaji huo wa kodi, na hati hiyo ikapelekwa kwenye Mahakama hiyo. Hata hivyo, mwezi wa Januari 2006 mamlaka ya utozaji wa kodi iliwaamuru ndugu walipe kodi hiyo.

Mashahidi wa Yehova walijulisha Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu kuhusu jambo hilo mara moja. Mahakama hiyo ilianza kuchunguza malalamiko yao bila kuchelewa. Mnamo Mei 4 (Mwezi wa 5), 2006, Mahakama hiyo iliomba serikali ya Ufaransa iwasilishe hoja zake kwa maandishi. Lengo ni kuchunguza kama uhuru wa ibada ya Mashahidi wa Yehova umeingiliwa na kama kisa hicho kinahusisha ubaguzi.

Ujerumani

Februari 10, 2006, Mahakama ya Utawala jijini Leipzig ililiamuru Jimbo la Berlin liandikishe Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani kama shirika la umma. Mnamo Julai 15, 2006, Jimbo la Berlin liliandikisha shirika hilo, kisha likawapa ndugu wawili wa Halmashauri ya Tawi hati ya uandikishaji. Hivyo, kesi iliyokuwa imeendelea kwa miaka 15 ikamalizika. Sasa Shirika hilo la Kidini limesamehewa kodi na lina haki nyingine ambazo dini kuu zinazo.

Ugiriki

Miaka nenda miaka rudi, maombi ya kibali cha kujenga au kutumia Majumba ya Ufalme yaliahirishwa au kukataliwa, kwa sababu maombi hayo yalipaswa kuidhinishwa na askofu wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki. Mnamo Mei 30, 2006, bunge liliamuru kwamba Wizara ya Elimu ya Taifa na Dini pekee ishughulikie maombi hayo ya dini zisizo za Othodoksi.

Julai 15, 2005, wasimamizi wa uwanja fulani huko Loutraki, Corinth, walibadili uamuzi wao wa kuwaruhusu ndugu wakodishe uwanja huo kwa ajili ya kusanyiko la wilaya. Wasimamizi walitilia shaka kama Mashahidi wa Yehova ni “dini inayojulikana.” Mchunguzi wa malalamiko ya wananchi aliingilia kati, na mnamo Februari 2006, wasimamizi wa uwanja huo wakaahidi kushughulikia maombi mapya wakijua kwamba dini ya Mashahidi wa Yehova imekubaliwa kisheria.

Nepal

Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kama shirika la kidini Oktoba (Mwezi wa 10) 2005. Lengo moja la shirika hilo ni “kuendeleza elimu ya kiroho.” Kibali hicho cha kisheria kinatarajiwa kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema katika nchi hiyo yenye Wahindu wengi.

Rumania

Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria mwaka wa 1990, waliondolewa katika orodha ya Serikali ya dini zinazokubaliwa kisheria ya mwaka wa 1997. Kwa hiyo, ndugu hawakuwa na haki ambazo dini nyingine zilizoandikishwa kisheria zinazo, kama vile kujenga Majumba ya Ufalme na haki ya kukataa kujiunga na jeshi. Mahakama Kuu ya Rumania iliamuru tena na tena serikali iandikishe dini ya Mashahidi wa Yehova kisheria, lakini serikali ikakataa. Hatimaye, Machi 2006, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ilisaidia serikali kufanya mapatano na Mashahidi wa Yehova, na kesi hiyo ya miaka tisa ikamalizika. Serikali ilikubali kwamba Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa na “haki zote za kisheria na wajibu wote” ambao dini zilizoandikishwa kisheria zinazo.

Uturuki

Baada ya ofisi ya tawi kuwasilisha ombi la kuandikishwa kisheria, serikali ilisema kwamba haiwezekani kuandikisha dini ya Mashahidi, ijapokuwa sheria za nchi hiyo zimepatanishwa na sheria za Muungano wa Ulaya. Sasa kesi hiyo inasikilizwa na mahakama nchini humo, lakini huenda hatimaye ikawasilishwa kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.

Tatizo lingine linahusisha jeshi. Ndugu huitwa wajiandikishe jeshini mara tatu au nne kila mwaka hadi wapite umri wa kuitwa. Kila mara wanahukumiwa. Baadhi yao wametozwa faini tena na tena, na wengine wamefungwa. Mwaka wa 2004, Yunus Erçep aliwasilisha kesi kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Ijapokuwa alikuwa ametozwa faini mara nyingi, Ndugu Erçep alihukumiwa kifungo cha miezi 12 na akafungwa Oktoba 2005. Aliachiliwa baada ya kufungwa kwa miezi mitano. Siku alipoachiliwa aliitwa tena mahakamani na kutozwa faini kwa kukataa kujiunga na jeshi mara kadhaa kabla ya kufungwa.

Uzbekistan

Katika miaka minne iliyopita kumekuwa na visa 1,100 vya ndugu kukamatwa, kufungwa, kutozwa faini, au kupigwa. Visa zaidi ya 800 kati ya hivyo vilitukia wakati wa Ukumbusho mwaka wa 2005 na 2006. Katika sehemu nyingi polisi wenye rungu waliosafiri kwa mabasi walifika na kuwakamata wote waliohudhuria. Wengi walitozwa faini, na wengine wakapigwa kikatili.

Hata hivyo, ushahidi mzuri umetolewa. Fikiria kisa cha ndugu na dada walioshtakiwa kwa uhalifu kwa sababu walikuwa wamehudhuria mikutano ya kutaniko na kuhubiri. Wakili wao aliomba vitabu vilivyochukuliwa walipokamatwa visomwe mahakamani. Kitabu Ujuzi na broshua Mungu Anataka vilisomwa kwa sauti, hata hakimu alisoma sehemu fulani. Kwa sababu alipendezwa sana na sura ya 5 ya kitabu Ujuzi, yenye kichwa “Ni Ibada ya Nani Anayoikubali Mungu?” hakimu aliagiza usomaji uendelee wakati wa mapumziko ya mchana.

Wakati andiko la Mathayo 28:19, 20 liliposomwa, hakimu huyo alisema kwa mshangao, “Kumbe, hiyo ndiyo sababu inayowafanya mhubiri!” Alipouliza kwa nini Mashahidi wa Yehova waliteswa chini ya utawala wa Nazi wa Hitler, alipewa video hizi tatu: Purple Triangles, Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault, na The Bible—Accurate History, Reliable Prophecy. Ijapokuwa yule ndugu na dada walitozwa faini, waliwahubiria maofisa wa mahakama na polisi kwa njia ambazo hawakutarajia.—Luka 21:12, 13.

Sudan

Kufikia Juni (Mwezi wa 6) 2006, Mashahidi wa Yehova walikuwa wameandikishwa kisheria katika majimbo manane. Ndugu wamejenga Majumba ya Ufalme katika maeneo hayo na wamefanya makusanyiko makubwa hadharani. Vitabu vyetu vinaingizwa nchini humo bila vizuizi na kuna ofisi jijini Khartoum.

Urusi

Mnamo Aprili 12, 2006, ndugu 200 huko Moscow walikuwa wakiadhimisha Ukumbusho katika jumba walilokuwa wamekodi wakati polisi 50 hivi wenye silaha walipoingia. Mkuu wa Idara ya Polisi ya Lyublino alivunja mkutano huo, na kudai kwamba mikutano kama hiyo imekatazwa kwa sababu Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku jijini Moscow. Polisi hao walichunguza vitambulisho vya wahudhuriaji, wakachukua vitabu, na kuwapeleka ndugu 14 kwenye kituo cha polisi cha Lyublino, ambako walizuiliwa kwa muda wa saa nne. Ndugu fulani alipoenda kwenye kituo cha polisi ili kuwasaidia kisheria, aliangushwa chini na kutishwa kwa kisu. Aliambiwa asiwasilishe malalamiko. Hata hivyo, ndugu 4 kati ya wale ndugu 14 waliwasilisha malalamiko dhidi ya Idara ya Polisi ya Lyublino mnamo Aprili 17.

Hakimu Z. V. Zubkova alianza kusikiliza kesi hiyo Mei 16, katika Mahakama ya Wilaya ya Lyublino, jijini Moscow. Hakuna polisi hata mmoja kati ya wale waliovamia akina ndugu aliyekuwapo ila wakili wao tu. Bila kutoa sababu yoyote hakimu alifuta malalamiko 50 ya mawakili wa akina ndugu na kukataa karibu hoja zao zote. Lakini hakimu huyo alikubali hoja ya wakili wa idara ya polisi ya kuwasilisha nakala ya uamuzi wa Mahakama ya Manispaa ya Wilaya ya Golovinsky wa kuwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova jijini Moscow. Alikubaliwa pia kuwasilisha maoni ya daktari wa akili L. V. Kulikov aliyetoa ushahidi dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika kesi iliyotangulia.

Mnamo Juni 15, 2006, hakimu huyo alitoa uamuzi kwamba kuzuiliwa kwa walalamishi hakupatani na sheria lakini akakosa kutoa uamuzi kuhusu kusimamishwa kwa Ukumbusho. Uamuzi huo unadai pia kwamba jumba lililokodiwa na ndugu halistahili kwa ajili ya ibada. Mashahidi wa Yehova walikata rufani kwenye Mahakama ya Rufaa ya Moscow Juni 30, 2006, na kutaja kwamba Mahakama ya Wilaya ya Lyublino haikufuata utaratibu unaofaa kesi hiyo iliposikilizwa, na mambo mengineyo. Ukumbusho uliadhimishwa katika sehemu nyingine 22 jijini Moscow bila matatizo yoyote.

Katika fungu la kwanza la masimulizi haya ya Matukio Muhimu tamaa ya mtunga-zaburi ilitajwa: “Nitampigia Mungu wangu muziki maadamu nipo.” (Zab. 146:2) Mamilioni ya watumishi wa Yehova leo, wanaonyesha wazi kwamba wao pia wanataka kufanya hivyo kwa moyo wote. Naam, maadamu ulimwengu huu mwovu ungalipo, tusiruhusu kamwe kuta za magereza, amri za wenye mamlaka, wala lugha za kigeni, zituzuie tusimpigie Baba yetu wa mbinguni muziki!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Haukuwa Mwaliko Tu

Karatasi ya kutangaza kusanyiko ilikuwa na sehemu ya kuomba funzo la Biblia, kitabu cha Biblia Inafundisha, au vyote viwili. Punde si punde ofisi za tawi kotekote duniani zilianza kupokea maombi hayo. Ofisi ya tawi ya Marekani inaripoti kwamba ilipokea maombi 2,000 hivi ya kitabu hicho, na maombi 300 ya funzo la Biblia. Bila shaka, jitihada za ndugu na dada zetu za kugawa karatasi hiyo ya kutangaza kusanyiko zitaendelea kuwa na matokeo mazuri.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Watu Wengi Wanataka Kitabu Biblia Inafundisha!

Mwishoni mwa Julai (Mwezi wa 7) 2006, nakala zaidi ya milioni 47 za kitabu Biblia Inafundisha zilikuwa zimechapwa katika lugha 155, bila kuhesabu chapa 10 za lugha ya vipofu. Katika mwezi mmoja, makutaniko nchini Marekani yaliomba kwa wastani, vitabu 42,000 kila siku. Thuluthi moja ya idadi hiyo ilitumwa kabla ya maombi ya kawaida kwa sababu ya uhitaji. Familia ya Betheli ya ulimwenguni pote huliona kuwa pendeleo kufanya kazi kwa bidii ili ndugu na dada zetu wapate vitabu kama hivyo.

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Ofisi za Tawi Zawekwa Wakfu

Albania

Marufuku ya miaka 50 juu ya kazi yetu iliondolewa mwaka wa 1992. Ndugu na dada 325 walihudhuria kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya ya tawi iliyoko kwenye vitongoji vya Tiranë. Kati ya waliohudhuria kulikuwa na Mashahidi wanne wazee waliomtumikia Mungu katika miaka hiyo ya marufuku. Wageni kutoka nchi za kigeni 32 walikuwapo pia. Wamishonari walipofika mwaka wa 1992, kulikuwa na wahubiri tisa tu waliobatizwa nchini humo. Sasa kuna wahubiri 3,617 nchini Albania. Ndugu wa Baraza Linaloongoza Theodore Jaracz na Gerrit Lösch walikuwa na sehemu katika programu ya kuweka wakfu ofisi hiyo mnamo Juni 3, 2006. Siku iliyofuata, walitoa hotuba katika uwanja usio na paa, na wahudhuriaji 5,153 walisikiliza kwa makini licha ya mvua kubwa.

Kroatia

Katika mwaka uliopita nchi hiyo ilibarikiwa katika njia mbili. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kikroatia ilitolewa katika kusanyiko la wilaya, na sehemu mpya ya ofisi ya tawi huko Zagreb ikawekwa wakfu. Ijumaa, Agosti 11 (Mwezi wa 8), watu 142 walisikiliza hotuba ya kuweka wakfu iliyotolewa na Ndugu Jaracz. Sehemu ya kwanza ya ofisi hiyo iliwekwa wakfu miaka saba iliyopita, yaani, mwaka wa 1999.

Slovenia

Mnamo Jumamosi, Agosti 12, Ndugu Jaracz alitoa hotuba ya kuweka wakfu ofisi mpya ya tawi huko Kamnik, mji ulio umbali wa kilomita 20 kaskazini ya mji mkuu Ljubljana, na umbali wa kilomita 130 magharibi ya Zagreb, Kroatia. Kabla ya hapo Wanabetheli walikuwa wakiishi huku na huku katika mji mkuu, kwa hiyo, wanafurahi sana kukaa pamoja hatimaye! Wale wasikilizaji 144 walitoka nchi 20.

[Picha]

Jengo la ofisi ya tawi nchini Albania

Watu 5,153 walihudhuria mkutano wa pekee

Ofisi ya tawi iliyopanuliwa nchini Kroatia

Ofisi ya tawi ya Slovenia

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kumhubiria mwanamke kiziwi, Brazili

[Picha katika ukurasa wa 17]

Darasa la kwanza la Kihindi, Ujerumani

[Picha katika ukurasa wa 19]

Linda na Paul

[Picha katika ukurasa wa 19]

Carma akihubiri katika lugha ya kabila la Blackfoot

[Picha katika ukurasa wa 20]

Darasa la Kihispania, Rome, Italia

[Picha katika ukurasa wa 20]

Samson akihubiriwa

[Picha katika ukurasa wa 21]

Hamilton na Abner wakifundisha Biblia katika lugha ya Mayangna

[Picha katika ukurasa wa 27]

Jumba la Ufalme kusini mwa Sudan

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki