Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
TUNA kila sababu ya kushangilia baada ya mwaka mwingine wenye baraka katika utumishi mtakatifu. Tunapopitia baadhi ya matukio muhimu ya kazi kubwa ambayo Mungu wetu anafanya kupitia watumishi wake, tunaweza kusema hivi kwa hakika: “Umeuvika taji mwaka kwa wema wako”!—Zab. 65:11.
“HABARI NJEMA” KATIKA INTANETI
Sisi Mashahidi wa Yehova tunachukua kwa uzito daraka letu la ‘kuhubiri hii habari njema ya ufalme katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote’ kabla ya mwisho kufika. (Mt. 24:14) Kwa miaka mingi, maendeleo ya kitekinolojia yamesaidia kuharakisha kuhubiriwa kwa “neno la ufalme.” (Mt. 13:18-23) Katika miaka 11 iliyopita, tumetumia kituo chetu rasmi cha Intaneti, www.watchtower.org, kufikishia watu ujumbe wa Biblia. Watu wanaofungua kituo hicho wanaweza kujifunza kweli za Biblia katika mojawapo ya lugha 314, na wanaweza kufungua vichwa kama vile “Beliefs and Activities,” “Current Topics,” “God and Your Future,” “Medical Care and Blood,” na “Publications Available.”
Watu wengi wanaofungua kituo chetu cha www.watchtower.org, wanafanya hivyo ili kusoma Biblia. Kila siku watu zaidi ya 6,300 wanasoma Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika mojawapo ya lugha kumi zilizo kwenye kituo hicho. Vitabu vya Biblia vinavyopendwa sana ni Zaburi, Methali, na masimulizi ya Injili ya maisha ya Yesu.
Kila juma, makala zilizoteuliwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinaongezwa kwenye kituo chetu cha Intaneti katika lugha 12—hasa makala zilizochapishwa kwa ajili ya watu wote. Watu wengi wanataka kujua mambo tunayoamini, jinsi mikutano yetu inavyofanywa, na jinsi kazi yetu ya kuhubiri inavyogharimiwa. Watu wanaofungua kituo chetu cha Intaneti wanapata majibu ya maswali hayo kwa kufungua broshua Mashahidi wa Yehova—Wao Ni Nani? Wanaamini Nini? Trakti Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia! inapatikana kwenye kituo cha www.watchtower.org katika lugha 252, kutia ndani sehemu fulani zilizorekodiwa kwenye video katika lugha tano za ishara.
KUPATA KWELI KATIKA INTANETI
Kuwa na vichapo hivyo kwenye Intaneti kumekuwa na matokeo gani? Kwa wastani watu zaidi ya 60,000 wanafungua kituo cha www.watchtower.org kila siku! Wengi wa watu hao wanaishi mahali ambako Mashahidi ni wachache au katika nchi ambako kazi yetu imepigwa marufuku au imezuiwa. Hata hivyo, wale walio na kiu ya kupata kweli wanaweza kupata maji ya kukata kiu hiyo kwenye kituo chetu cha Intaneti.
Bryon anasema: “Sikuzote nimetamani kujifunza Biblia, lakini kila nilipoenda kanisani na marafiki wangu, waliimba nyimbo au kucheza tu.” Bryon aliendelea na masomo yake na riadha. Alijifunza lugha tano na hata akalipiwa masomo ya chuo, lakini hakuridhika kiroho. Kwa hiyo akasali apate kweli.
“Nilitamani sana kupata majibu ya maswali yangu,” Bryon anasema. “Niliamua kutafuta kituo cha Mashahidi wa Yehova kwenye Intaneti kwa sababu Mashahidi fulani tuliokuwa marafiki shuleni waliniambia kwamba jina la Mungu ni Yehova. Nilifungua kituo chao na kuanza kusoma broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Hatimaye, maswali yangu yalijibiwa.” Bryon aliomba funzo la Biblia, akafanya maendeleo haraka, na kujiweka wakfu kwa Yehova mwaka wa 2004. Sasa yeye ni painia wa kawaida na anatumaini kuwa mmishonari aliyepata mazoezi ya Biblia na hivyo kutumia lugha alizojifunza.
“MUNGU YUPO PAMOJA NANYI”
Inafurahisha kama nini kujua kwamba kila siku maelfu ya watu “kutoka katika lugha zote za mataifa” wanafungua kituo cha www.watchtower.org! Kila siku, wastani wa watu 94 wanajaza fomu iliyo kwenye kituo chetu cha Intaneti inayojazwa na wale wanaotaka kutembelewa.—Zek. 8:23.
Denise alikuwa na maswali kuhusu imani ya Mashahidi wa Yehova, lakini alisita kwenda kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu na kwao. Badala yake, aliamua kutafuta habari kuhusu Mashahidi kwenye Intaneti, na akapata kituo cha www.watchtower.org. Habari alizopata zilimsadikisha kwamba alikuwa amepata kweli, lakini akasita kuomba funzo la Biblia kwa sababu alijua kuwa atahitaji kubadili maisha yake yapatane na viwango vya Biblia. Alijaza mara nne ile fomu inayojazwa na watu wanaotaka kutembelewa, lakini kila alipoijaza, alishindwa kuituma.
Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 2007, Denise alijaza fomu hiyo kwa mara ya tano na wakati huu akatuma ombi lake la kutaka atembelewe. Ombi hilo lilitumwa katika kutaniko lililo karibu na kwao, na wazee wakamwomba dada Vonnie amtembelee. Katika juma la kwanza baada ya Vonnie kumtembelea, Denise alianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme.
Kufikia mwisho wa Septemba (Mwezi wa 9), Denise alikuwa ameharibu vitu vyake vya kidini, akakatiza uhusiano wake na dini, na kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Yeye na wanawe wawili walifanya maendeleo haraka, na mwana wake mwenye umri wa miaka minane akajiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Denise alibatizwa Januari 2008, na miezi miwili baadaye akawa painia msaidizi. Hayo yalitendeka mwaka mmoja tu baada ya kutuma fomu ya kutaka atembelewe. Denise anasema: “Kama singalifungua kituo hicho cha Intaneti, singalikuwa nikiwaeleza mambo haya.”
Mnamo Januari 2008, baadhi ya vichapo vyetu vilivyorekodiwa viliongezwa kwenye kituo chetu cha Intaneti na vinaweza kunakiliwa katika lugha 17. Watu wanapendezwa sana na mpango huo, na vichapo pamoja na makala mojamoja zaidi ya milioni moja zinanakiliwa kila mwezi! Wahubiri wengi wanasikiliza makala za magazeti hayo wanaposafiri kwenda kazini au shuleni.
TAFSIRI ZINAZOTIMIZA UHITAJI
Inafurahisha kama nini kutegemezwa na malaika tunapowahimiza watu wa “kila taifa na kabila na lugha” kumtukuza Mungu! (Ufu. 14:6, 7) Ili kuwasaidia watu waitikie ujumbe wa Biblia kwa utayari zaidi katika lugha ambazo wanaelewa vizuri, sasa Mashahidi wa Yehova wanachapisha vichapo katika lugha 450 hivi.
Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilitolewa hivi karibuni katika Kitetum, lugha ya kienyeji ya Timor Mashariki, lakini nakala zilizotolewa hazikutosha. Maria, mwanafunzi mpya aliyekuwa akitumia kitabu Biblia Inafundisha katika Kiindonesia, hakupata nakala ya Kitetum. Alimwomba mwalimu wake wa Biblia amwazime kitabu chake cha Kitetum kwa siku mbili. Katika siku zilizofuata, alirudia kwa shauku mambo yote aliyokuwa amejifunza. Kwa kuwa sasa Maria alikuwa akijifunza kweli katika lugha ya mama, alielewa mambo mengi vizuri zaidi ya vile alivyoyaelewa alipokuwa akijifunza katika Kiindonesia. Mwalimu wake alishindwa kumwambia amrudishie kitabu chake cha Kitetum. Maria anaendelea kujifunza na kuhudhuria mikutano.
Nchini Kenya, Kiingereza na Kiswahili ni lugha zinazotumiwa kwa ukawaida serikalini na katika biashara. Hata hivyo, mamilioni ya Wakenya wanapendelea kuzungumza Kikuyu, Kikamba, Kijaluo, na lugha nyingine za kienyeji. Kwa hiyo, kuchapisha vichapo katika lugha hizo kumewachochea wengi wapendezwe na ibada ya Yehova. Wazee wa Kutaniko la Siaya waliandika hivi baada ya kuanza kutumia vichapo na kufanya mikutano katika Kijaluo: “Sasa akina ndugu wanaweza kuelewa vizuri zaidi mambo wanayofundishwa na watoto wanasikiliza kwa makini zaidi. Tangu tulipoanza kutoa hotuba katika Kijaluo, hudhurio kwenye mikutano limeongezeka kwa asilimia 60.”
Nchini Nikaragua, watu wengi wanazungumza lugha ya Miskito badala ya Kihispania. Watu zaidi ya 200 walihudhuria kusanyiko la wilaya katika lugha ya Miskito. Baadhi yao walijidhabihu sana kuhudhuria. Kwa mfano, ndugu 13 kutoka mji mdogo wa Asang, kando ya Mto Coco, walitengeneza chelezo la magogo walilotumia kusafiria kwenye mto huo kwa siku mbili hadi mji wa Waspam. Kisha wakasafiri kwa lori kwa muda wa saa tano ili kufika katika jiji la kusanyiko. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa ndugu wengi katika kikundi hicho kuhudhuria kusanyiko. Walifurahia kusikiliza programu katika lugha yao ya kienyeji. Kwa sababu walitumia pesa zote kufika kwenye jiji la kusanyiko, wahudhuriaji wengine walichanga ili ndugu hao wapate pesa za kurudi nyumbani.
Waliohudhuria kusanyiko hilo la lugha ya Miskito walifurahi wakati kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilipotolewa katika lugha yao. Mapainia hasa walikithamini sana. Kabla ya hapo, walikuwa wakitumia kitabu Biblia Inafundisha katika Kihispania na walilazimika kutafsiri mafungu na maswali katika lugha ya Miskito walipofundisha wanafunzi wa Biblia. Sasa wanakazia fikira kufundisha kweli za Biblia badala ya kufikiria vile watakavyotafsiri.
Lugha ya Quechua inazungumzwa na Wenyeji wa Asili wa Amerika Kusini. Wahubiri fulani wanaozungumza lugha ya Quechua nchini Peru waliandika: “Tunapomalizia mazungumzo na wenye nyumba tunawaeleza kwamba tuna vichapo katika lugha ya Quechua. Baadhi yao wameguswa moyo sana kupata vichapo katika lugha yao hivi kwamba wamelia na kuvibusu.” Ofisi ya tawi huko Peru iliandika: “Akina ndugu wanaoishi mahali ambapo lugha ya Quechua inazungumzwa wamejitahidi sana kuonyesha uthamini wao. Baada ya kusoma kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? katika lugha ya Quechua, ndugu mmoja alisema kwamba hatimaye anaelewa maana na thamani ya fidia ya Kristo. Wasomaji wamewaletea ndugu kwenye ofisi ya tawi viazi, pai, matunda, na vitu vingine ili kuonyesha uthamini wao.”
Pia, tengenezo linajitahidi sana kutafsiri vichapo katika lugha zinazozungumzwa katika visiwa vya mbali vya Pasifiki. Dada mmoja alimwambia hivi mmishonari fulani katika kisiwa cha Micronesia kinachoitwa Pohnpei: “Ninamshukuru Yehova kwa kutukumbuka. Hapo mbeleni tulikuwa tukipata Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Ponapea miezi kadhaa baada ya gazeti la Kiingereza.” Aliongeza kusema hivi kwa ucheshi: “Tulifikiri kwamba labda Har–Magedoni ingetufikia ikiwa imechelewa. Lakini sasa tunajifunza gazeti hilo wakati uleule na watu wengine ulimwenguni, na linavutia kama vile tu gazeti la Kiingereza. Tunathamini sana kwamba Baraza Linaloongoza linatutunza.”
Ndugu na dada katika Visiwa vya Marshall huko kaskazini mwa Pasifiki walifurahia kupata toleo jipya la watu wote la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Marshall. Ndugu hao wanapenda kusoma masimulizi ya maisha, lakini matoleo ya awali ya Mnara wa Mlinzi hayakuwa na nafasi kwa ajili ya masimulizi hayo, kwa hiyo ilibidi yatafsiriwe kutoka gazeti la Kiingereza. Kwa hiyo, walifurahi sana walipopata simulizi la kwanza la maisha katika toleo la watu wote la lugha yao. Msomaji mmoja mwenye umri wa miaka 16 alisema: “Kwa miaka mingi ningeangalia magazeti ya Kiingereza na kuona picha katika masimulizi ya maisha, na ingawa nilitamani kuyasoma singeweza. Sasa ninaweza kuyasoma.”
Hata kusoma kichapo kimoja tu katika lugha fulani, kunaweza kubadili maisha ya watu. Katika nchi moja ya Asia ya Kati ambako kazi yetu imezuiwa, broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? imesambazwa sana. Mwanamume mmoja kijana alipata broshua hiyo, akaisoma peke yake, na kuguswa moyo sana hivi kwamba alienda kwenye mto uliokuwa karibu na “kujibatiza.” Alipojua kwamba alipaswa kufundishwa Biblia, alikubali mara moja, na muda si muda akabatizwa kwa njia inayofaa. Sasa anatumia wakati wake mwingi akiwahubiria wengine habari njema.
MAENDELEO KATIKA KUTAFSIRI BIBLIA
Mashahidi wa Yehova wanathamini sana Neno la Mungu, Biblia, na pia wanathamini sana tafsiri iliyo sahihi na rahisi kueleweka. Kwa sababu hiyo, sasa watu wa Mungu wanafurahia kuwa na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, ikiwa nzima, au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 70. Watu wanafurahia wanapopata tafsiri hiyo kwa mara ya kwanza, lakini jambo linalogusa mioyo yao hasa na kuwasaidia kuwa na mawazo yanayofaa, ni kuitumia kila siku katika funzo la kibinafsi, katika mikutano ya kutaniko, na katika utumishi wa shambani.
Ofisi ya tawi nchini Urusi imekuwa ikipokea barua nyingi za kushukuru kwa sababu ya kutolewa kwa Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kirusi. Mwanamke mmoja aliandika: “Ingawa nimeisoma Biblia mara nyingi, kuisoma tafsiri hii ni kama kuisoma Biblia kwa mara ya kwanza! Nyakati nyingine machozi yananilengalenga, nami ninasisimka sana ninapoguswa moyo na ujumbe wa Biblia.”
Msomaji mwingine alipoona jinsi tafsiri hiyo inavyoeleweka wazi alisema: “Baada ya kusoma Mwanzo sura ya 18 leo, nimechochewa kuwaandikia barua hii. Mazungumzo kati ya Abrahamu na Yehova, yaliyo katika mstari wa 23-32, yalinigusa moyo sana. Ijapokuwa ninasoma Biblia kwa mara ya tano, hii ilikuwa mara ya kwanza kufikiria kwa undani kuhusu mazungumzo hayo. Nilimhurumia Abrahamu na “kusikiliza” kwa makini mazungumzo yake na Yehova. Machozi yalinilengalenga kuona jinsi Yehova alivyomsikiliza Abrahamu. Tafsiri hii ilifanya tukio hilo liwe halisi. Niliona sifa za Yehova na kuguswa nazo kibinafsi.”
“Asanteni sana kwa Biblia nzima Tafsiri ya Ulimwengu Mpya!” akaandika Svetlana kutoka Moscow. “Hatimaye hatuchanganyikiwi tunaposoma ‘Agano la Kale.’ Awali hatungeweza kuelewa vizuri sehemu hiyo ya Biblia kwa sababu tulikuwa na tafsiri ya zamani isiyoeleweka! Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni rahisi kueleweka!”
Msomaji mwingine aliandika: “Nikiwa kazini nilikuwa nikizungumza na mfanyakazi mwenzangu, Irina, kuhusu kweli. Mwanzoni nilikuwa ninanukuu maandiko tu. Lakini nilipofungua Biblia yangu na kumwonyesha sala ya mfano ya Yesu, aliniuliza, ‘Hii ndiyo Sala ya Bwana?’ Aliposoma maneno ya Yesu, macho yake yaling’aa kwa shangwe naye akasema hivi kwa mshangao: ‘Inapendeza kama nini! Mambo yametajwa waziwazi sana! Nimesikia sala hii mara nyingi lakini sijawahi kuielewa. Hapa imeelezwa waziwazi na kwa urahisi! Ninataka Biblia kama hii. Nitafutie moja! Nitafutie Biblia kama hii!’ Nilimwambia hivi: ‘Tunawapa Biblia watu wanaotamani kikweli kuisoma.’ Naye akanijibu hivi kwa uzito: ‘Sikuwa ninataka kusoma Biblia mbeleni. Ijapokuwa nilikuwa na Biblia kadhaa wakati uliopita, niliwapa watu zote, lakini sasa kwa kweli ninataka kuisoma!’”
Ndugu mmoja aliandika hivi kuhusu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiukrainia: “Ninataka kutoa shukrani zangu kwa kupokea zawadi hii nzuri kutoka kwa Yehova na tengenezo lake. Ninafurahia kusoma kila ukurasa nami ninaibeba kila mahali ninapoenda. Imetafsiriwa katika lugha rahisi na inayoeleweka. Ninaguswa moyo ninapoisoma na ninaweza kuelewa kwa urahisi mafundisho ya Biblia.”
Tafsiri katika Kiserbia na Kikroatia pia zimefurahiwa sana. Dada mmoja Mkroatia aliandika: “Ni rahisi sana kuisoma tafsiri ya Kikroatia, inaeleweka kwa urahisi zaidi kuliko Biblia ambayo tumetumia kwa miaka mingi. Mashauri ya Kimaandiko yananigusa moyo kwa urahisi zaidi, na ninahisi kwamba ninaendelea kumjua Yehova zaidi kuliko hapo awali.”
Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kisamoa ilitolewa na Ndugu Geoffrey Jackson wa Baraza Linaloongoza, Novemba 2, 2007, (2/11/2007). Biblia za zamani za Kisamoa hazipatikani kwa urahisi na ni za bei ya juu, kwa hiyo akina ndugu wanafurahi sana kwamba tafsiri hiyo mpya inapatikana kwa urahisi. Baada ya kutumia Biblia hiyo kwa miezi kadhaa, mhubiri mmoja alisema, “Biblia ya zamani inafunika maana, lakini Biblia mpya inafunua mambo na inatusaidia kuyaelewa vizuri zaidi.”
Dada mmoja anaeleza kuhusu funzo la Biblia ambapo walizungumzia andiko la Yakobo 4:8 katika kitabu walichokuwa wakijifunza. Dada huyo anasema, “Nilimwambia mwenye nyumba hata kama tunajua andiko hilo, ni vizuri tulisome katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Mwanzoni tulifikiri tunasoma andiko tofauti, lakini baada ya kuchunguza tukaona ni andiko lilelile. Dada niliyekuwa naye katika funzo hilo alisema kwa mshangao, ‘Andiko hilo limebadilika.’ Sasa tungeweza kuelewa vizuri kwamba neno ‘kukaribia’ linamaanisha tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Jambo hilo halikuwa wazi katika Biblia ya zamani. Hilo lilitugusa moyo sana na kutuchochea kusitawisha uhusiano wa karibu na Yehova.”
Muda fulani baada ya kutolewa kwa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kichina, wamishonari wanaotumika huko Taiwan waliandika: “Tulimpa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya mwanasheria fulani anayependa kusoma magazeti yetu kwa ukawaida. Alitaka kujua ni kwa nini tafsiri mpya ilihitajika. Baada ya kumwonyesha mistari michache tu, alivutiwa sana, na kusema kwamba tafsiri hiyo mpya ni rahisi zaidi kueleweka kuliko Biblia ya Union Version, aliyokuwa akisoma.” Wamishonari hao pia walimpa mbunge fulani Biblia hiyo, naye akaiacha ofisini mwake. Mtangazaji fulani wa redio aliyewachambua Mashahidi wa Yehova aliiona Biblia hiyo kwenye ofisi ya mbunge huyo, akaichukua, na kusoma sehemu fulani. Alivutiwa sana hivi kwamba aliwapigia wamishonari hao simu akiomba Biblia yake mwenyewe.
Dada mmoja kutoka Kirghiz ambaye hawezi kusoma vizuri kwa sababu ya tatizo la macho, alifikiri kusoma Biblia ni jambo gumu sana. Hata hivyo, maoni yake yalibadilika alipopata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Kirghiz. Sasa anafurahia sana kusoma tafsiri hiyo kwa sababu ni rahisi kueleweka.
Dada mwingine alisema: “Hii ni tafsiri nzuri sana! Sikosei ninaposoma kwa sauti. Ninataka kuisoma tena na tena. Ninahisi ni kama nimeanza kujifunza kweli tena.”
Dada aliye na tatizo la kusikia, aliandikia Baraza Linaloongoza hivi: “Ninapenda Injili ya Mathayo katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Sasa mambo ninayosoma katika Biblia yanakuwa halisi na yananigusa moyo. Ninaweza kuona utu wa Yesu, ishara zake za uso, fadhili zake, na upendo wake mwingi kwa watu. Ninapenda nakala yangu ya kitabu cha Mathayo katika lugha ya ishara. Lakini . . . mnaweza kuharakisha kutafsiri vitabu vingine vya Biblia katika lugha ya ishara?”
Bila shaka, Biblia iliyotafsiriwa vizuri inaweza kuwasaidia watu kuelewa Neno la Mungu vizuri, na kufanya ujumbe wake wa kweli ufikie moyo wa msomaji. Kwa sababu hiyo, wale wanaotamani kumkaribia Baba yao wa mbinguni wanashangilia wanapopata Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yao ya mama—lugha inayowachochea.
WAFANYAKAZI ZAIDI WATUMWA KATIKA MAVUNO
Wanabetheli kadhaa katika Betheli ya Marekani wameombwa kutumika katika migawo mingine kwa sababu ya kurahisisha mambo kwenye ofisi ya tawi. Baadhi yao wametumwa kwenye ofisi nyingine za tawi na mamia kadhaa wakatumwa kama mapainia wa pekee na wa kawaida nchini kote. Walihisi namna gani walipopewa migawo hiyo? Wamekabiliana jinsi gani na matatizo katika migawo yao mipya? Makutaniko yamenufaika jinsi gani?
Todd na Leslie wanasema: “Kwa miaka mingi, tulimwomba ‘Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.’ Lakini hatukujua kwamba Yehova angetutumia kujibu sala hiyo! Sasa tunaweza kuona kuwa mkono wa Yehova unaongoza mambo, na tunahisi ni pendeleo kwamba Kristo ‘ametuona kuwa waaminifu kwa kutugawia huduma.’”—Mt. 9:37, 38; 1 Tim. 1:12.
Franco anasema hivi anapokumbuka miezi michache ya kwanza katika mgawo mpya pamoja na mke wake: “Hatukujua kabisa kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa nchini Marekani. Tulipofika kwenye mgawo wetu, tulipata watu wengi sana waliotaka kujifunza Biblia.” Mapainia wengi wanahisi kama Curtis na Karolynne ambao walisema: “Tunafurahia sana mgawo wetu mpya! Tumepata nafasi ya kumwonyesha Yehova kwamba tulijikana kikweli tulipojiweka wakfu kwake.”
KUMTUMAINI “BWANA WA MAVUNO”
Wanabetheli wengi walikuwa na wasiwasi walipopata migawo mipya baada ya kutumika Betheli kwa miaka mingi. Mume na mke fulani waliuliza, “Je, tutapata nyumba ya bei rahisi? Je, tutaweza kufanya mabadiliko na kuhubiri kwa muda wa saa 120 au 130 kwa mwezi badala ya kuhubiri saa za mhubiri wa kawaida, na vilevile kulitia moyo kutaniko?” Wenzi hao wa ndoa na Wanabetheli wengine walikabiliana jinsi gani na hali hiyo mpya?
Baadhi yao walipata nyumba kwa bei rahisi siku ya mwisho ambayo wangeweza kutafuta nyumba katika eneo walikotumwa. Kwa mfano, Jessica ambaye ni dada mseja, alienda katika eneo alikotumwa na kutafuta nyumba kwa majuma mawili bila mafanikio. Siku moja kabla ya kurudi Betheli kuchukua vitu vyake, alifurahi sana wakati mzee wa kutaniko katika eneo hilo alipojitolea kumkodisha nyumba ndogo kwa bei nafuu.
Jeff na Cynthia walimweleza msimamizi wa nyumba za kukodi kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova. “Ninawajua Mashahidi wa Yehova,” msimamizi huyo akasema, “na ninajua sipaswi kuwa na wasiwasi kuwahusu. Yehova anahakikisha kwamba mnapata pesa za kulipia kodi ya nyumba!”
Eric na Melonie walisema, “Mambo tuliyojionea yanatukumbusha kwamba tunahitaji kumtegemea Yehova nyakati zote. Tunaona uthibitisho kwamba Yehova anatutegemeza kila siku na hilo limeimarisha imani yetu kwelikweli.”
MAKUTANIKO YAMEWATEGEMEZA
Makutaniko yaliwakaribisha mapainia hao kwa upendo na hilo liliwasaidia sana kuzoeleana na hali katika migawo yao mipya. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema kwamba ndugu katika makutaniko mengi wanaeleza kwa shauku kuhusu “mapainia wetu wa pekee.” Anaendelea kusema: “Mzunguko mzima uliwakaribisha na kuwasaidia kwa upendo.” Ndugu fulani katika mzunguko huo aliandika hivi kwa uthamini: “Ningependa kuwaambia akina ndugu katika ofisi ya tawi, ‘Asanteni sana.’ Mapainia hao ni baraka kwetu!”
Kutaniko moja huko Kansas lilikuwa na maeneo 100 ambayo hayakuwa yamehubiriwa kwa miezi mingi. Kwa kuwa sasa kuna mume na mke ambao ni mapainia wa pekee, maeneo mengi yanahubiriwa kwa ukawaida. Wazee wa kutaniko hilo waliandika hivi: “Hatungewazia jinsi ambavyo mpango huu ungetufaidi.”
Ingawa makutaniko yamekuwa ‘msaada wenye kuwatia nguvu’ mapainia hao, hata wahubiri wenyewe wamefaidika. (Kol. 4:11) Mwangalizi mmoja wa mzunguko anasema, “Bidii ya mapainia hao imewatia moyo na kuwachochea sana ndugu na dada zetu.” Mwangalizi mwingine wa mzunguko aliandika, “Unachotambua waziwazi kuhusu mapainia hao ni upendo na shangwe yao, na wengine wamechochewa kuiga sifa hizo.”
Wenzi fulani wa ndoa walifurahia kuwasaidia wahubiri kumi wasiotenda wawe watendaji tena. Pia, baadhi ya mapainia wanaotumika wakiwa wazee wana matokeo mazuri. “Katika kutaniko, tumepata msaada kwa kuwa na ndugu mwenye usawaziko na aliyezoezwa,” akaandika mzee mmoja. “Kutaniko na baraza la wazee walihitaji kuwa na ndugu kama huyo.”
“WAFANYAKAZI WENZI WA MUNGU”
Yehova amewabariki wahubiri wa Ufalme kwa mambo mengi yenye kufurahisha. Kwa mfano, Steve na Gaye walienda kuhubiri nyumba kwa nyumba siku moja yenye baridi kali. Kwenye nyumba ya kwanza, walianzisha funzo la Biblia na mzee mmoja aliyeshuka moyo. Katika muda wa majuma mawili, alihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme ambapo Steve na Gaye walitaja kwamba mzee huyo alionyesha fadhili kwa kuwakaribisha walipomtembelea mara ya kwanza. Mzee huyo aliwajibu, “Sikuwakaribisha kwa sababu nilikuwa mtu mzuri, bali ni kwa sababu nilijua mngekuja. Nilikuwa nimesali kwa siku tatu nipate msaada.” Sasa anahudhuria mikutano kwa ukawaida na anafanya maendeleo ili abatizwe.
Wakati Ray na Jill walipokuwa wakiendesha gari asubuhi moja, walimwona mtu aliyekuwa akitembea upande ule mwingine wa barabara na wakaamua kuongea naye. Walimpa vichapo na kujitolea kujifunza Biblia pamoja naye. Alichukua magazeti na kueleza kwamba amekuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alikuwa amehamia eneo hilo karibuni na alikubali kwa furaha walipojitolea kuendelea kujifunza Biblia pamoja naye.
Wote wanaojidhabihu wanapomtumikia Yehova wanajua kwamba ‘Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yao na upendo walioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Ebr. 6:10) Kama vile mwili wa mwanadamu una sehemu nyingi zinazotimiza kinachohitajiwa, kila ndugu anaweza kuchangia ukuzi na hali nzuri kutanikoni. “Mungu ameviweka viungo katika [kutaniko], kila kimoja, kama vile alivyopenda,” na kila kiungo kikijitahidi kushirikiana na vingine, “vile viungo vingine vyote hushangilia.” (1 Kor. 12:18, 26) Ushirikiano huo wenye upatano kati ya “wafanyakazi wenzi wa Mungu” unamletea Yehova utukufu ambaye ‘anaendelea kulikuza’ kutaniko.—1 Kor. 3:6, 9.
KUITHIBITISHA KISHERIA HABARI NJEMA
Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” (Mt. 10:22) Wanafunzi wa kweli wangetarajia wapinzani ‘waseme kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yao kwa ajili yake.’ (Mt. 5:11) Wanafunzi wa Kristo wa siku hizi wamefanya nini ili “kuithibitisha kisheria habari njema”?—Flp. 1:7.
Armenia
Kati ya Aprili (Mwezi wa 4) 2007 na Aprili 2008, maofisa wa forodha nchini Armenia walikataa kuachilia zaidi ya tani saba za Biblia na vichapo vya Biblia wakidai walipwe kiasi kikubwa sana cha ushuru. Hatimaye, mnamo Aprili 2008, akina ndugu waliruhusiwa kuchukua shehena ya kwanza ya vichapo hivyo baada ya kulipa shingo upande ushuru waliodaiwa, lakini shehena nyingine bado zimezuiliwa. Akina ndugu wamechukua hatua za kisheria ili kutatua tatizo hilo.
Kazakhstan
Ndugu wawili kutoka makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova, waliokuja kuwatia moyo kiroho waabudu wenzao nchini Kazakhstan, walikamatwa baada ya mkutano wa pekee huko Almaty. Walizuiliwa kwenye kituo cha polisi, wakahojiwa, na kupelekwa mbele ya hakimu wa mahakama ya utawala, ambaye aliwapata na hatia ya “kufanya kazi ya umishonari.” Ijapokuwa waliachiliwa baadaye, jitihada zinafanywa ili kuthibitisha kwamba ndugu hao wawili hawakuwa na hatia. Hivi karibuni, wenye mamlaka wamekuwa wakivamia nyumba za ndugu zetu na kuvuruga mikutano inayofanywa kwa ajili ya sala na funzo la Biblia. Mahakama zimesimamisha utendaji wa kiroho wa makutaniko matatu yaliyoandikishwa kisheria, na maofisa wa kutekeleza sheria wamevuruga tena na tena utendaji wa kiroho katika eneo lililo kaskazini ya Bahari ya Kaspiani.
Tajikistan
Jumuiya ya Kidini ya Mashahidi wa Yehova nchini Tajikistan iliandikishwa kisheria mnamo 1994, na hivyo kuwaruhusu Mashahidi kukutana pamoja kwa ajili ya ibada. Hata hivyo, Oktoba 11, 2007 (11/10/2007), wizara ya utamaduni ilifikia uamuzi wa kupiga marufuku ibada ya Mashahidi wa Yehova. Jitihada zinafanywa ili kuwathibitishia wenye mamlaka kwamba Mashahidi wa Yehova wanapenda amani na hawasababishi vurugu.
Uzibekistani
Hali ya Mashahidi wa Yehova nchini Uzibekistani inaendelea kuzorota. Mapema katika mwaka wa 2008, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alifungwa miaka minne katika kambi ya kazi ngumu kwa sababu ya imani yake. Mashahidi wengine wamekamatwa, wakazuiliwa, wakahukumiwa, na kutozwa faini kwa kuvunja sheria zinazohusu mashirika na mafundisho ya kidini. Mikutano imevamiwa, nyumba zikapekuliwa, vichapo vikachukuliwa, na wahubiri wakazuiliwa. Polisi wamewatusi na kuwatesa ndugu na dada wengi.
Maofisa kadhaa kutoka eneo hilo wamefunua kwamba makasisi katika nchi hizo ndio wanaochochea matendo hayo maovu. Tunaendelea kusali kwamba karibuni wenye mamlaka watatambua kwamba matendo yao hayafai na hivyo kuwaruhusu ndugu na dada zetu ‘waendelee kuishi maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.’—1 Tim. 2:1, 2.
Ugiriki
Katika kesi mbili zilizowasilishwa katika mahakama kuu nchini Ugiriki, mahakama hiyo ilikata uamuzi unaofaa kuhusu haki ya mtu ya kutojiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri inayotegemea imani. Konstantinos Kotidis alikuwa mwanajeshi katika jeshi la Muungano wa Sovieti miaka kadhaa kabla ya kuhamia Ugiriki na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wenye mamlaka walipotaka Ndugu Kotidis ajiunge na jeshi, hawakumruhusu afanye utumishi wa kiraia badala yake. Walidai kwamba kwa kuwa alikuwa mwanajeshi zamani, hakuwa na msingi wa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Hata hivyo, Baraza la Serikali liliamua kwamba mtu ambaye alikuwa mwanajeshi zamani na ambaye dhamiri yake ilibadilika baadaye kwa sababu za kidini, anaweza kukubaliwa kufanya utumishi wa kiraia badala ya kujiunga na jeshi.
Katika kisa kingine, taasisi fulani ya umma ilikataa kumwajiri Stylianos Ioannidis kwa kuwa alikuwa amefungwa alipokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Kwa maoni yao hakuwa ametimiza wajibu wake wa kijeshi. Lakini Baraza la Serikali liliamua kuwa mtu anayekataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri hangelazimishwa kujiunga na jeshi baada ya kumaliza kifungo chake. Pia mahakama hiyo ilisema kwamba baada ya kifungo suala la utumishi wa kijeshi litakuwa limeshughulikiwa kabisa, kwa hiyo hilo halipasi kumzuia mtu asiajiriwe katika ofisi ya umma. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa Baraza la Serikali kutoa uamuzi unaotegemea misingi ileile ya uhuru wa kidini iliyotumiwa na Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu katika kesi nyingine ambapo Shahidi wa Yehova alikosa kuajiriwa alipopatikana na hatia ya kutojiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.
Eritrea
Ndugu na dada zetu nchini Eritrea wanaendelea kuteswa kikatili. Wenye mamlaka wamewazuilia Mashahidi kadhaa wa Yehova gerezani, wengine chini ya hali mbaya sana. Mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2008, ndugu sita walikamatwa kutia ndani wazee fulani wanaosimamia kazi katika nchi hiyo. Ingawa jitihada nyingi zimefanywa na watu kutoka mataifa mbalimbali wameomba hali ziboreshwe, serikali imesimama kidete kupinga ibada ya watu wa Mungu wa kweli, Yehova.
Korea Kusini
Maendeleo yanafanywa nchini Korea Kusini ambako serikali imekataa kutambua haki ya msingi ya kutojiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Katika miaka 50 iliyopita, ndugu zetu zaidi ya 13,000 wamefungwa, na kwa sasa ndugu 500 hivi wako gerezani. Msimamo na mwenendo wao wa Kikristo umekuwa ushahidi mzuri kwa wenye mamlaka gerezani na katika serikali, jambo linalompendeza Mungu wetu Yehova. (1 Pet. 2:20) Kufikia sasa, kesi 488 zimepelekwa kwenye Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa na mnamo 2006 mahakama hiyo ilikata uamuzi unaofaa katika kesi mbili. Wakati huu ndugu zetu wanatumaini kwamba serikali itatimiza nia yake ya kupitisha sheria inayoruhusu watu wanaokataa kujiunga na jeshi wafanye utumishi wa kiraia unaokubalika.
Rwanda
Mnamo Aprili 2008 walimu wote nchini Rwanda, kutia ndani wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova, walitakiwa kuhudhuria mkutano fulani. Ilikuwa lazima kwa kila mwalimu kushiriki katika mambo yaliyokuwa yakifanywa huko hata kama yalipingana na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Kwa hiyo, Mashahidi 215 hivi waliokataa kuhudhuria mkutano huo walifutwa kazi, na dada wawili wakafungwa kwa majuma kadhaa. Mkutano huo ulihusisha mambo ya kisiasa na kijeshi, na waliohudhuria waliamriwa washiriki mambo ya kisiasa na sherehe za kizalendo. Yeyote aliyejaribu kuondoka katika mkutano huo alizuiwa na wanajeshi. Tangu wakati huo, watoto 90 wa Mashahidi wa Yehova wamefukuzwa shuleni kwa kukataa kuimba wimbo wa taifa au kusalimu bendera. Tuna hakika kwamba Yehova atawatia nguvu ndugu na dada zetu na watoto wao ili waendelee kushika utimilifu wao wanapokabili mateso hayo yaliyotokea hivi karibuni.
Hispania
Serikali ya Hispania ilikubali agizo la mfalme kuhusu Mashahidi wa Yehova ambao ni watumishi wa pekee wa wakati wote, kama Wanabetheli na waangalizi wanaosafiri. Taarifa ya serikali iliwatambua watumishi wa pekee wa wakati wote kuwa “wahudumu waliowekwa rasmi . . . ambao wanajitolea kabisa kufanya kazi ya umishonari au huduma ya Kikristo, kufundisha mambo ya dini, au kufanya mambo mengine yanayotegemeza dini yao.” Agizo hilo lilitolewa wakati ambapo wenye mamlaka katika nchi fulani hawawaoni watumishi wa pekee wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova kuwa wahudumu wa kweli ambao wanastahili kupokea huduma fulani kama wahudumu wa dini nyingine.
MAHAKAMA YA ULAYA YA HAKI ZA KIBINADAMU
Mashahidi wa Yehova nchini Armenia, Austria, Azerbaijan, Georgia, Ufaransa, Ukrainia, Urusi, na Uturuki wamepeleka kesi 24 mbele ya Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) huko Strasbourg, Ufaransa. Kesi hizo zinahusu haki za msingi za raia walio chini ya mamlaka ya Mkataba wa Ulaya Unaohusu Haki za Kibinadamu, kama haki ya mtu kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Kesi nyingine zinahusu kuteswa na kubaguliwa kwa misingi ya kidini, kuondolewa katika orodha ya dini zilizoorodheshwa rasmi, au kupigwa marufuku kwa shirika la kisheria linalotumiwa na Mashahidi wa Yehova kupanga kazi yao, serikali kuingilia haki ya kukutana kwa amani ili kuabudu, na haki ya mzazi Shahidi kumlea mtoto kama Shahidi wa Yehova.
Austria
Katika kesi ya Mashahidi wa Yehova dhidi ya serikali ya Austria (Jehovah’s Witnesses v. Austria), ECHR ilikata uamuzi unaofaa Julai 31, 2008. Mahakama ilisema kwamba sheria za Austria kuhusu dini zinavunja haki ya Mashahidi wa Yehova ya kuabudu kwa uhuru kwa sababu dini zinaandikishwa katika vikundi viwili. Hilo linafanya dini fulani zionekane kuwa duni, na hivyo kufanya raia fulani waonekane duni. Uamuzi huo umetolewa baada ya ndugu zetu kujitahidi kwa miaka 30 kutambuliwa kuwa shirika la kidini huko Austria. Mahakama ilisema: “Haifai vikundi vya kidini, kama Mashahidi wa Yehova, ambavyo vimekuwapo kwa muda mrefu katika mataifa mbalimbali, na ambavyo pia vimekuwa nchini kwa muda mrefu na hivyo kujulikana na wenye mamlaka wanaoshughulikia uandikishaji wa dini, [kungoja kwa muda mrefu].” Sasa serikali ya Austria inatakiwa kubadili sheria ya sasa. Ikifanya hivyo, ndugu zetu wanaweza kuwa na haki sawa na dini zilizo kubwa nchini Austria.
Azerbaijan
Mnamo Novemba 2007 kesi ilipelekwa mbele ya ECHR kulalamikia jinsi polisi wanavyovunja haki yetu ya uhuru wa ibada. Ijapokuwa Mashahidi wa Yehova wameandikishwa kisheria nchini Azerbaijan, kumekuwa na visa vingi vyenye kutia wasiwasi vya ndugu zetu kukamatwa na kuteswa. Vikundi vikubwa vya polisi wenye silaha wamevamia mikutano yenye amani ya Mashahidi wa Yehova, wakachukua vichapo na mali za watu binafsi, wakakamata na kuwazuilia waliohudhuria, na kuwatusi na kuwapiga ndugu na dada. Kwa sababu polisi wameendelea na uvamizi wao, mahakama hiyo imekubali kwamba kesi hiyo inapaswa kushughulikiwa upesi na hivyo wameharakisha kuchunguzwa kwake. Tunatumaini kwamba karibuni ndugu zetu wataruhusiwa kukutana kwa amani bila kuogopa kwamba wataingiliwa na polisi.
Ufaransa
Mnamo Februari (Mwezi wa 2) 2005 kesi ilipelekwa mbele ya ECHR kulalamikia hatua isiyo ya haki na isiyo ya kisheria ya serikali ya Ufaransa kulitoza kodi shirika letu (Association of Jehovah’s Witnesses) nchini humo. Bado tunangoja kuona kama mahakama hiyo itafikiria kesi hiyo. Wakati huu, wapinzani wamepotosha mafundisho yetu sana hivi kwamba katika mwaka uliopita kulikuwa na visa 70 hivi vya Majumba ya Ufalme kuharibiwa. Hata hivyo, ndugu nchini Ufaransa wanatumaini kwamba karibuni mahakama hiyo itawaletea kitulizo Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo kwa kuamua kwamba serikali ilitenda kwa ubaguzi.
Urusi
Mnamo Desemba (Mwezi wa 12) 2001, Mashahidi wa Yehova nchini Urusi walipeleka kesi katika ECHR wakilalamikia kukamatwa na kupelekwa mahakamani kwa watu katika jumuiya ya kidini ya Mashahidi wa Yehova kwa mashtaka ya uhalifu na mengineyo. Mnamo Juni (Mwezi wa 6) 2004, Mahakama ya Jiji la Moscow iliunga mkono uamuzi wa mahakama ya chini wa kupiga marufuku utendaji wa Mashahidi wa Yehova jijini Moscow na kufutilia mbali shirika lao la kisheria. Kwa ujumla, ndugu jijini Moscow bado wanaweza kukutana kwa ajili ya ibada na kuhubiri habari njema za Ufalme. Hata hivyo, jijini Moscow na katika maeneo mengine ya Urusi, mara nyingi wenye mamlaka wamekuwa wakivuruga mikutano na makusanyiko na pia kuwatesa ndugu na dada zetu. Kwa mfano, mnamo Julai katika mji wa Chekhov ulio kilomita 60 hivi kusini mwa Moscow, watu waliteketeza Jumba la Ufalme. Ingawa wazima-moto waliitwa mara moja, watu walisema kwamba hawakujitahidi kuuzima moto huo, nao polisi wamekataa kufanya uchunguzi. Ijapokuwa ndugu na dada zetu nchini Urusi wanakabili matatizo na upinzani, wanaendelea kuwa waaminifu na kumtegemea Yehova.
Yehova anaahidi kwamba hakuna silaha yoyote itakayofanywa juu ya watumishi wake itakayofanikiwa. (Isa. 54:17) Hata hali zilizo ngumu zaidi zinaweza kuchangia ‘kuendelezwa mbele kwa habari njema.’ Kwa hiyo, watumishi wa Mungu wameazimia kuendelea ‘kusimama imara katika roho moja, kwa nafsi moja wakikazana pamoja kwa ajili ya imani ya habari njema, nao hawawaogopi hata kidogo wapinzani wao.’ (Flp. 1:12, 16, 18, 27, 28) Tafadhali “endeleeni kusali” kwa ajili ya ndugu na dada zetu duniani pote wanapoendelea kumtumaini Yehova, ‘ngome yao na Mwokoaji wao.’—2 The. 3:1; Zab. 18:2.
OFISI ZA TAWI ZAWEKWA WAKFU
Kulikuwa na shangwe kubwa kwenye ofisi ya tawi ya Afrika Kusini Jumamosi (Siku ya Posho), Novemba 10, 2007, wakati ndugu na dada 4,000 hivi walipokusanyika kwa ajili ya kuwekwa wakfu kwa kiwanda cha uchapishaji kilichopanuliwa, chumba cha kulia chakula, na jengo la makao.
Waliotembelea kiwanda hicho walifurahia kuona mashini za uchapaji zinazoitwa MAN Roland Lithoman zikichapisha makumi ya maelfu ya Biblia na vichapo vya Biblia. Mashini mpya ya kujalidi vitabu tayari imejalidi nakala zaidi ya milioni moja za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha 16 za Afrika. Wageni walionyeshwa jengo la idara ya upakizi na usafirishaji lililopanuliwa ambapo ofisi inaweka vichapo vya Biblia vinavyotumiwa na makutaniko 8,000 hivi katika nchi kumi kusini mwa Afrika.
Ofisi ya tawi iliyopanuliwa nchini Nigeria, iliwekwa wakfu Juni 7, 2008 jijini Lagos, umbali wa kilomita 360 kusini-magharibi ya Betheli ya Igieduma. Ofisi ya Lagos ina jengo la makao lenye vyumba 24, bohari, na jengo la ofisi. Mambo mengi yanayohusu ofisi ya tawi yanashughulikiwa huko Lagos, mji mkuu wa biashara wa nchi hiyo. Wanabetheli wanaochukua vitu kutoka bandarini na kununua vitu vinavyohitajiwa kwenye ofisi ya tawi, na pia ndugu wanaowasili na kuondoka kwenye uwanja wa ndege, wanalala katika ofisi hiyo. Ofisi ya Lagos pia inatumika kwa ajili Shule ya Mazoezi ya Kihuduma mpaka upanuzi wa ofisi ya tawi ya Igieduma ukamilike. Kwa kweli, Yehova anabariki kazi ya kuhubiri barani Afrika, kama anavyofanya duniani kote.
TUMEPEWA VIFAA ILI KUFANYA MAPENZI YA MUNGU
Tunamshukuru Yehova sana kwamba ametupa “vifaa vyema vya kila namna ili kufanya mapenzi yake, akifanya katika sisi kupitia Yesu Kristo lile ambalo linapendeza vema machoni pake.” (Ebr. 13:21) Kwa sababu Yehova amethibitisha kwamba yeye ndiye anayeweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri,” tunasema hivi kwa moyo wote: “Kwake kuwe na utukufu kwa njia ya kutaniko na kwa njia ya Kristo Yesu kwa vizazi vyote milele na milele.”—Efe. 3:20, 21.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Dini Zinaandikishwa kwa Nini na Jinsi Gani?
Dini zinaandikishwa kwa njia tofauti katika nchi mbalimbali. Nchi fulani, kama Armenia na Azerbaijan, zina sheria hususa zinazoruhusu mashirika ya kidini kuomba yaandikishwe kisheria. Nchi ikikubali ombi hilo, shirika la kidini linatambuliwa kuwa dini rasmi. Katika nchi nyingine, dini zinaandikishwa katika vikundi viwili. Kikundi cha kwanza kinatia ndani dini maarufu. Dini katika kikundi hicho zinapata faida nyingi kama vile kutolipa kodi. Kwa kawaida kikundi cha pili kinatia ndani dini ndogo, mpya, na zisizo maarufu.
Nchi nyingine, kama Georgia na Marekani, hazina sheria hususa kuhusu kuandikishwa kwa dini. Katika visa kama hivyo, sheria inawaruhusu watu wote wawe na uhuru wa kidini. Ingawa dini mojamoja hazitambuliwi rasmi, dini yoyote inaweza kuomba kuandikisha shirika lake kisheria. Dini inapofanya hivyo, inaweza kutumia shirika hilo kwa mambo mbalimbali, kutia ndani kuchapisha na pia kununua ardhi au nyumba.
[Ramani katika ukurasa wa 21]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
AUSTRIA
UFARANSA
HISPANIA
UGIRIKI
ERITREA
RWANDA
ARMENIA
AZERBAIJAN
URUSI
KAZAKHSTAN
UZIBEKISTANI
TAJIKISTAN
KOREA KUSINI
[Picha katika ukurasa wa 11]
Kutaniko la Kijaluo la Siaya
[Picha katika ukurasa wa 13]
“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” ikiwa nzima au kwa sehemu, inapatikana katika lugha zaidi ya 70
[Picha katika ukurasa wa 22]
Konstantinos Kotidis
[Picha katika ukurasa wa 22]
Stylianos Ioannidis
[Picha katika ukurasa wa 29]
Jengo jipya la makao jijini Lagos, Nigeria
[Picha katika ukurasa wa 29]
Kiwanda cha uchapishaji, ofisi ya tawi ya Afrika Kusini