Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb13 kur. 8-41
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
  • 2013 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mali Zilizonunuliwa na Kuuzwa
  • Kueneza Neno la Mungu
  • Msaada kwa Ajili ya Watu wa Namna Zote
  • Nyimbo za Sifa Katika Lugha Nyingi
  • Ofisi za Utafsiri
  • Habari Fupi Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni
  • Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi Kunamletea Yehova Heshima
  • Ripoti ya Mambo ya Kisheria
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2013 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb13 kur. 8-41

Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

Sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova inasonga mbele bila kuzuiwa! Tunakualika usome kuhusu matukio yenye kusisimua ambayo yametukia katika miezi iliyopita.

Mali Zilizonunuliwa na Kuuzwa

Eneo Jipya la Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote

Mnamo Julai 2009, Mashahidi wa Yehova walinunua kiwanja kwenye jimbo la New York, Marekani, wakiwa na lengo la kuhamisha makao yao makuu. Kiwanja hicho chenye ukubwa wa ekari 253 kipo umbali wa kilometa 80 hivi kaskazini-magharibi mwa eneo la Brooklyn, New York, mahali ambapo makao makuu hayo yamekuwapo tangu mwaka wa 1909.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wanabetheli wapatao 800 wataishi na kufanya kazi katika makao hayo mapya, yatakayotia ndani jengo la ofisi mbalimbali na jengo la huduma mbalimbali, majengo ya udumishaji, na majengo manne ya makazi. Pia, kutakuwa na jumba dogo la makumbusho lenye historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova.

Majengo hayo yatajengwa kwenye eneo la ekari 45 za kiwanja hicho, na kuacha msitu na maeneo yenye majimaji yaliyo katika eneo hilo kama yalivyo. Bustani hazitakuwa na maeneo makubwa yenye nyasi. Badala yake, mazingira ya asili ya eneo hilo yatadumishwa. Wasanifu-majengo wamechora ramani za majengo yatakayohifadhi nishati na kupunguza gharama, na hivyo, kuepuka kuharibu mazingira isivyo lazima. Kwa mfano, juu ya paa za majengo hayo kutakuwa na mimea itakayopunguza kuchuruzika kwa maji ya mvua na kudumisha kiwango kinachofaa cha halijoto ndani ya majengo. Ofisi zitajengwa kwa njia ambayo mwanga wa asili utaweza kutumika kwa kiasi kikubwa. Pia, uhifadhi wa maji utazingatiwa.

Ni nini kilichochochea mabadiliko hayo? Ofisi za tawi katika sehemu nyingine za ulimwengu sasa zinashiriki katika kazi ya uchapaji wa Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia, kazi iliyokuwa ikifanywa huko Brooklyn. Katika mwaka wa 2004, kazi ya uchapaji na usafirishaji nchini Marekani ilihamishiwa huko Wallkill, New York, kilometa 145 hivi kaskazini-magharibi mwa Brooklyn. Gharama pia zilifikiriwa. Inagharimu sana kuendesha na kudumisha majengo ya zamani na yaliyotawanyika yaliyo Brooklyn. Kuhamia mahali pamoja kutatufanya tutumie vizuri zaidi michango ya hiari.

Kuunganishwa kwa Ofisi za Tawi

Kuanzia Septemba 2012, usimamizi wa ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova 30 hivi ulihamishiwa kwenye ofisi za tawi kubwa zaidi. Kuna sababu mbili kuu za mabadiliko hayo:

1. Teknolojia imerahisisha kazi. Katika miaka ya karibuni, maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano na uchapaji yamepunguza idadi ya wafanyakazi wanaohitajika kwenye ofisi kubwa za tawi. Kwa kuwa ni watu wachache zaidi wanaofanya kazi katika ofisi kubwa za tawi, nafasi ilipatikana kwa ajili ya wale waliokuwa wakitumika kwenye ofisi ndogo za tawi katika nchi nyingine.

[Chati katika ukurasa wa 13]

Sasa, kutoka kwenye ofisi hizo kubwa za tawi, kikundi cha Mashahidi wenye uzoefu wanashughulikia kazi ya elimu ya Biblia. Kwa mfano, kazi ya kuhubiri nchini Kosta Rika, El Salvador, Guatemala, Honduras, Nicaragua, na Panama sasa inasimamiwa na ofisi ya tawi ya Mexico. Matokeo ni kwamba, ofisi za tawi katika nchi hizo sita zilifungwa. Washiriki arobaini wa familia ya Betheli kutoka katika ofisi hizo za tawi walipewa mgawo wa kutumika kwenye ofisi ya tawi ya Mexico. Wengine 95 hivi walibaki kwenye nchi walimozaliwa wakifanya utumishi wa wakati wote.

Wengine katika nchi hizo za Amerika ya Kati waliendelea kufanya kazi kwenye ofisi za utafsiri chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Mexico. Kwa mfano, watafsiri 20 hivi nchini Panama hutafsiri machapisho ya Biblia katika lugha za wenyeji. Nchini Guatemala Mashahidi 16 hutafsiri machapisho katika lugha nne za wenyeji. Jitihada hizo za kupanga kazi upya katika Amerika ya Kati zimefanya idadi ya Wanabetheli ipungue kutoka 300 hadi 75 hivi.

2. Kuongezeka kwa wahubiri wa wakati wote. Kwa sababu ya kuunganishwa kwa ofisi za tawi, ndugu waliokuwa wakitumika kwenye ofisi ndogo za tawi sasa wanaweza kukazia fikira kazi ya kuhubiri habari njema. Ndugu mmoja barani Afrika, aliyepewa mgawo wa kuhubiri, aliandika: “Katika miezi michache ya kwanza, haikuwa rahisi kubadili mtindo wangu wa maisha ili ufae hali mpya. Hata hivyo, nimepata shangwe na baraka nyingi sana kwa kushiriki katika utumishi kila siku. Kwa sasa, ninajifunza Biblia na watu 20, na baadhi yao wanahudhuria mikutano ya kutaniko.”

Alama ya Muda Mrefu Katika Jiji la Brooklyn

Usiku na mchana kwa zaidi ya miaka 40, wakaaji wa New York City wamekuwa wakiona maandishi mekundu yenye urefu wa meta 4.6 yaliyo juu ya makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Wengi wao hutegemea kujua kiwango cha halijoto na wakati unaoonyeshwa katika alama hiyo.

Alama hiyo iliwekwa miaka 70 iliyopita na mmiliki wa awali wa jengo hilo. Mashahidi wa Yehova walibadili muundo wa alama hiyo baada ya kununua jengo hilo mwaka wa 1969.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ndugu wakisimamisha herufi za alama ya “Watchtower” mwaka wa 1970

Alama hiyo imerekebishwa mara kadhaa, ili ifanye kazi vizuri na kwa usahihi zaidi. Katikati ya miaka ya 1980, kiwango cha halijoto kinachoonyeshwa kwa Selsiasi kiliongezwa kwenye sehemu inayoonyesha wakati na kiwango cha halijoto kwa Fahrenheit.

Eboni, anayeweza kuona alama hiyo kutoka mahali anapoishi huko Brooklyn, alisema: “Inapendeza kutazama tu nje ya dirisha na kuona wakati na kiwango cha halijoto kabla ya kwenda kazini. Inanisaidia nitunze wakati na kuvaa mavazi kulingana na hali ya hewa iliyopo.”

Je, alama hiyo itabaki hapo kwa miaka mingine 40? Kwa sababu ya mipango ya kuhamishwa kwa makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova, uamuzi huo utategemea wale watakaomiliki jengo hilo wakati ujao.

Kueneza Neno la Mungu

Jambo Jipya Manhattan

Mnamo Novemba 2011, kikundi cha Mashahidi wa Yehova kilianza kuwajulisha watu ujumbe wa Biblia katika eneo la Manhattan kwa kutumia meza na vigari vya kukokotwa vyenye kuvutia. Mpango huo unaendelea katika sehemu ya kusini ya Manhattan, eneo lenye shughuli nyingi na la zamani zaidi la New York City. Eneo hilo liligawanywa katika sehemu nne. Kila sehemu ina vituo kadhaa ambapo wapita-njia wanaweza kupata machapisho yaliyopangwa vizuri kwenye meza au katika vigari vya kukokotwa vyenye machapisho ya Biblia vinavyosimamiwa na painia mmoja. Meza nyingi zipo kwenye au karibu na vituo vya usafiri, ambapo makumi ya maelfu ya watu hupita kila siku.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wenzi wa ndoa mapainia wakitoa magazeti kwenye meza ya machapisho huko Grand Central Station, New York City

Katika vituo hivyo, watu wanaweza kupata majibu ya maswali mengi ya Biblia. Watu wenye haraka wanaweza kuchukua chapisho na kujisomea baadaye. Machapisho yanapatikana katika lugha nyingi. Ikiwa chapisho halipatikani katika lugha fulani, linaweza kuagizwa na kuchukuliwa siku chache baadaye.

Watu kwa ujumla na pia wenye mamlaka wameufurahia mpango huo. Polisi mmoja alisema: “Mmekuwa wapi sikuzote? Kwa kweli mna kitu ambacho watu wanahitaji.” Mwanaume mmoja alisimama ghafla alipokiona kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Alisema kwamba aliona watu wakikisoma kwenye treni naye hakujua mahali walipokipata. Sasa anajua.

Kijana mmoja alipita mbele ya mojawapo ya meza hizo kila siku kwa majuma sita akienda kazini. Mwishowe, alisimama na kusema, “Ninahitaji msaada.” Wale waliokuwa wakisimamia meza hiyo walifurahi kumsaidia. Walimpa Biblia na kumwonyesha jinsi anavyoweza kufaidika kutokana nayo. Wapita-njia wengi wamefurahia kusimama na kuzungumzia mambo ya kiroho, na kwa muda wa miezi nane, watu 1,748 wameonyesha tamaa ya kujifunza Biblia. Kufikia Juni 2012, mpango huo umewawezesha watu kupata magazeti 27,934 na vitabu 61,019.

Magazeti Yetu—Kurasa Chache Zaidi, Lugha Nyingi Zaidi

Kuanzia Januari 2013, kurasa za gazeti la Amkeni! na Mnara wa Mlinzi toleo la watu wote la mwezi huo, zilipunguzwa kutoka kurasa 32 hadi 16. Kwa sababu magazeti hayo yana habari chache zaidi, vikundi vya watafsiri vitaweza kutafsiri magazeti hayo katika lugha nyingi zaidi. Kwa sasa, gazeti la Amkeni! linatafsiriwa katika lugha 98 na Mnara wa Mlinzi katika lugha 204. Toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi litaendelea kuwa na kurasa 32.

Baadhi ya habari zilizokuwa kwenye magazeti hayo sasa zinapatikana tu katika Tovuti ya www.jw.org. Habari hizo zinatia ndani “Kwa Ajili ya Vijana,” “Masomo Yangu ya Biblia,” na ripoti ya kuhitimu kwa madarasa ya Gileadi kutoka katika gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la watu wote na “Mazungumzo ya Familia” na “Vijana Huuliza” kutoka katika gazeti la Amkeni!

Kwa kuongezea, mfululizo wa makala zinazopatikana kwenye mtandao katika Tovuti hiyo, sasa zinatoa majibu mafupi, yaliyo wazi ya maswali kuhusu Mashahidi wa Yehova na Biblia. Pia, machapisho kama vile vitabu, broshua, trakti na mengineyo yanaweza kupakuliwa kutoka kwenye Tovuti. Kwa kutumia kompyuta au kifaa kinachobebeka, wenye vifaa hivyo wanaweza kupata kwa urahisi machapisho yetu kwenye Tovuti ya www.jw.org katika lugha zaidi ya 440.

Tovuti Yetu Yaboreshwa

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Katika miezi michache iliyopita, kikundi kikubwa cha Mashahidi wa Yehova kwenye makao makuu ya ulimwenguni pote huko New York kimekuwa kikifanya kazi ya kuboresha Tovuti ya www.jw.org iwe yenye kuvutia na rahisi zaidi kutumia kwenye kompyuta au kifaa kinachobebeka. Kwa kuongezea, wamebadili na kuboresha Tovuti hiyo kwa makusudi mawili:

1. Kuunganisha Tovuti zetu. Tovuti tatu zinazosimamiwa na Mashahidi wa Yehova zimeunganishwa katika Tovuti moja rasmi ya www.jw.org. Tovuti nyingine mbili, www.watchtower.org na www.jw-media.org, hazitatumiwa tena. Kuunganishwa kwa Tovuti hizo kumewawezesha wale wanaotafuta habari kuhusu Mashahidi wa Yehova au machapisho yao, kupata habari zote katika Tovuti moja. Kwa mfano, unaweza kusoma, kusikiliza, au kuchapa kurasa za Biblia na za machapisho mengine ya Biblia katika lugha nyingi.

Mnamo Agosti 28, 2012, Tovuti iliyobadilishwa muundo ya www.jw.org ilizinduliwa

2. Kuongeza habari. Tovuti hiyo iliyoboreshwa ina majibu ya maswali ya Biblia na habari kuhusu kazi ya kuhubiri, ofisi za tawi, Majumba ya Ufalme na makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Sehemu ya “Habari” inaripoti matukio yanayowaathiri ndugu zetu ulimwenguni pote. Pia, kuna sehemu kwa ajili ya familia, vijana, na watoto.

Kwa siku, mamia ya maelfu kadhaa ya watu husoma machapisho yetu kwenye mtandao. Pia, hupakua karibu nusu milioni ya faili za kusikiliza, faili za muundo wa EPUB, PDF, au video za lugha ya ishara. Kila siku, mamia ya watu huomba kujifunza Biblia.

Msaada kwa Ajili ya Watu wa Namna Zote

Biblia ya Futi Sita

Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yenye maandishi ya vipofu, ambayo inapatikana katika Kiingereza, Kihispania, na Kiitaliano ina jumla ya mabuku kati ya 20 hadi 28 ambayo yanahitaji nafasi ya angalau mita mbili (futi 6 na inchi 5) kwenye rafu ya vitabu! Biblia nyingine za muundo wa maandishi ya vipofu hazichukui nafasi kubwa kama Biblia hiyo. Kwa mfano, mashine ya kupiga chapa maandishi ya vipofu huwawezesha vipofu kuandika na pia kusoma habari zilizohifadhiwa kielektroni kupitia kifaa cha mkononi chenye pini zinazoinuka na kushuka na kutokeza maandishi ya vipofu. Pia, vipofu wanaweza kupata na kusikiliza machapisho kwa kutumia programu zinazoweza kusoma maandishi kwenye skrini, ambazo hubadili maandishi kuwa sauti.

Kwa zaidi ya miaka 100, Mashahidi wamekuwa wakichapisha machapisho yanayozungumzia Biblia kwa ajili ya vipofu, na machapisho hayo sasa yanapatikana katika lugha 19. Ingawa vipofu wanaopenda kujifunza Biblia wanaweza kupata machapisho hayo bila malipo, wengi wao hutoa mchango wa hiari.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ndugu Anthony Bernard huko Sri Lanka akitumia Biblia ya Kiingereza yenye maandishi ya vipofu kuongoza ibada ya familia

Mashahidi wamebuni programu ya kompyuta inayoweza kubadili maandishi ya kawaida yawe maandishi ya vipofu katika lugha nyingi. Baada ya kutayarisha jedwali lenye herufi za lugha fulani na pia herufi za maandishi ya vipofu katika lugha hiyo, programu hiyo inaweza kubadili maandishi ya kawaida yawe maandishi ya vipofu. Pia, hutumia mpangilio ambao hufanya iwe rahisi kwa vipofu kusoma maandishi hayo. Programu hiyo itafanya iwezekane kutayarisha machapisho ya vipofu, kutia ndani Biblia, katika lugha yoyote ile yenye herufi za maandishi ya vipofu, hata zile zisizotumia herufi za Kiroma.

Awali, chapisho jipya lilipotolewa kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, wahudhuriaji walijulishwa kwamba wanaweza kuagiza baadaye machapisho yenye maandishi ya vipofu. Mwaka uliopita, ofisi ya tawi ya Marekani ilifanya uchunguzi katika makutaniko ili kujua watu ambao ni vipofu wanapanga kuhudhuria kusanyiko lipi la wilaya na chapa wanayopendelea (karatasi yenye maandishi ya vipofu, kifaa cha kupiga chapa maandishi ya vipofu, au programu ya kusoma maandishi kwenye skrini).

Nakala zenye maandishi ya vipofu zilisafirishwa hadi mahali pa makusanyiko ambayo vipofu walihudhuria, jambo lililofanya iwezekane kwao kupata machapisho mapya wakati uleule wengine walipoyapata. Juma moja baada ya kusanyiko nakala za kielektroni zilitumwa kupitia barua-pepe kwa kila mmoja aliyehitaji.

Dada mmoja kipofu alisema hivi: “Nilifurahi sana kupokea machapisho pamoja na wengine wote. Zaburi 37:4 inasema kwamba Yehova atatupa maombi ya moyo wetu. Amefanya hivyo mwisho juma huu!” Ndugu mwingine kipofu alianza kulia na kusema, “Tunamshukuru Yehova kwa kutujali sana!”

Maelfu Wajifunza Kusoma na Kuandika

Katika mwaka wa 2011, Mashahidi wa Yehova waliwasaidia zaidi ya watu 5,700 kujua kusoma na kuandika. Hivi ndivyo mambo yamekuwa katika baadhi ya nchi:

Ghana: Katika kipindi cha miaka 25 iliyopita, tumewasaidia watu 9,000 kujua kusoma na kuandika.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Darasa la kujifunza kusoma na kuandika nchini Zambia

Msumbiji: Katika kipindi cha miaka 15 iliyopita zaidi ya watu 19,000 wamejifunza kusoma. Mwanafunzi mmoja anayeitwa Felizarda alisema: “Ninafurahi sana kwa kuwa sasa ninaweza kuwasomea wengine maandiko ya Biblia. Hapo awali ilikuwa vigumu sana kwangu.”

Visiwa vya Solomon: Ofisi ya tawi inaandika hivi: “Hapo awali, watu wengi wanaoishi maeneo ya mashambani au vijijini hawakupata nafasi ya kwenda shule. Pia, ni wasichana wachache sana waliopokea elimu. Kwa hiyo, wanawake hasa ndio wamefaidika kutokana na madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika. Baada ya kukamilisha masomo hayo, wengi hujiamini zaidi.”

Zambia: Tangu mwaka wa 2002, karibu watu 12,000 wameboresha uwezo wao wa kusoma na kuandika. Agnes, mwenye umri wa miaka 82 anasema: “Wakati madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika kutanikoni yalipotangazwa, nilifurahi kujiandikisha. Katika somo la kwanza, nilijifunza kuandika jina langu mwenyewe!”

Nyimbo za Sifa Katika Lugha Nyingi

Mashahidi wa Yehova tayari wanatafsiri machapisho ya Biblia katika lugha 600 hivi. Kutafsiri kitabu kizima cha nyimbo 135 ni kazi ngumu sana. Licha ya hilo, kwa kipindi cha miaka mitatu kitabu chote kipya cha nyimbo, Mwimbieni Yehova, kilitafsiriwa katika lugha 116. Toleo la kitabu cha nyimbo 55 limetafsiriwa katika lugha za ziada 55, na vitabu vingi vya nyimbo katika lugha nyingine vinatafsiriwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Visiwa vya Solomon: Kutaniko likiimba katika Kipijini cha Visiwa vya Solomon

Watafsiri wa nyimbo hukusudia kutokeza maneno ya nyimbo yenye maana, mazuri na yanayoweza kukumbukwa. Kwa kuongezea, maneno yanayotumiwa katika nyimbo ya sifa yanapaswa kuwa rahisi ili mwimbaji apate maana na kusudi la kila mstari. Katika kila lugha, maneno yanahitaji kuingiana na muziki na kusikika kwa njia ya kawaida, kana kwamba ni maneno ya mwimbaji.

Watafsiri hutimizaje lengo hilo? Badala ya kutafsiri maneno moja kwa moja kutoka katika kitabu cha Mwimbieni Yehova cha lugha ya Kiingereza, wao huandika upya maneno ya nyimbo yanayokazia mambo muhimu ya wimbo wanaotafsiri. Watafsiri hutumia maneno yanayotumiwa kwa ukawaida katika lugha yao ambayo yanaeleweka na kukumbukwa kwa urahisi, huku wakijaribu kushikamana kwa ukaribu na wazo la Kimaandiko la kila wimbo.

Hatua ya kwanza ni kutafsiri wimbo wa Kiingereza neno kwa neno. Kisha, Shahidi mwenye ustadi wa kutunga maneno ya nyimbo hufanya kazi ya kugeuza wimbo uliotafsiriwa kuwa maneno ya wimbo yenye kupendeza lakini yenye maana katika lugha hiyo mpya. Halafu, kikundi cha watafsiri na wasahihishaji huchunguza kazi hiyo, wakati wote wakiwa makini kudumisha usahihi wa Kimaandiko wa maneno ya nyimbo. Ijapokuwa si kazi rahisi kutafsiri kitabu chetu cha nyimbo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamefurahia sana kuimba nyimbo za ufalme katika lugha zao wenyewe.

Ofisi za Utafsiri

Kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba katika siku zetu watiwa mafuta wangewaalika watu waje ‘wachukue maji ya uzima bure.’ (Ufu. 22:17) Wangewaalika watu kutoka ‘vikundi vyote vya watu na lugha.’ (Ufu. 7:9) Kwa muda mrefu, watafsiri wengi walifanya kazi katika ofisi zao za tawi, hata ingawa lugha yao ilizungumzwa katika maeneo mengine ya nchi. Haikuwa rahisi kwao kuendelea kujifunza lugha yao na kufikia mioyo ya wasomaji wa machapisho waliyotafsiri. Hata hivyo, sasa vikundi vingi vya watafsiri vinahamishiwa katika ofisi zilizo kwenye maeneo ambayo lugha yao inazungumzwa. Jambo hilo limeleta baraka katika njia nyingi, kama maelezo yafuatayo ya watafsiri yanavyoonyesha.

Mtafsiri wa Kimaya kutoka Mexico alieleza: “Nilihisi kama mmea mchanga uliopandwa tena katika udongo wake, kwenye mazingira yake ya asili.” Mtafsiri kutoka Urusi kusini alisema: “Watafsiri hufurahia sana kuwa na ofisi kwenye eneo ambalo watu huzungumza lugha wanayotafsiri. Jinsi lugha inavyotumiwa kwenye televisheni, vitabu, na Intaneti ni tofauti kabisa na jinsi watu wanavyozungumza lugha hiyo katika maisha ya kila siku. Kwa upande wetu, njia pekee ya kutafsiri kwa njia inayoeleweka ni kusikiliza lugha hiyo inapozungumzwa.”

“Nilihisi kama mmea mchanga uliopandwa tena katika udongo wake, kwenye mazingira yake ya asili”

Mtafsiri wa Kitshiluba huko Kongo alieleza hivi: “Tunazungumza lugha yetu kila siku—katika shughuli zetu za kila siku, kama vile tunaponunua vitu dukani na tunapozungumza na jirani zetu, tunapofanya kazi ya kuhubiri, na kwenye mikutano ya Kikristo. Tunajifunza kile tulichotafsiri, na tunatumia machapisho ya Kitshiluba kwenye huduma, kwa hiyo tunaweza kuona moja kwa moja ikiwa watu wanaelewa lugha inayotumiwa na watafsiri.”

Mtafsiri wa Kilhukonzo kutoka Uganda alisema: “Huwezi kuwazia furaha yetu tunapohudhuria mikutano inayoongozwa katika lugha tunayozungumza na kutafsiri. Pia, tunafurahia zaidi huduma ya shambani, kwa kuwa sasa tunazungumza na watu kwa lugha yetu ya asili.”

[Ramani katika ukurasa wa 27]

Pia, makutaniko yamenufaika kwa kushirikiana na watafsiri walio katika makutaniko yao. Dada mmoja alisema hivi kuhusu watafsiri wa Kimaya: “Watafsiri hututia moyo kwa maneno na mfano wao mzuri. Ni kama kuwa na sehemu ya Betheli pamoja nasi, na hilo ni jambo la pekee sana.”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kikundi cha watafsiri cha Kijaluo, Kisumu, Kenya

Badilishano hilo linawatia moyo wote. Ndugu mmoja mtafsiri kutoka Kenya alisema: “Kwa sababu ya kuwa na machapisho machache tu katika Kijaluo, watu hapa hawakuwahi kuwazia kwamba wangeona machapisho yenye ubora kama huu katika lugha yao. Kwa hiyo, wengi wanasisimuka kuyapokea. Ninapoona jinsi wanavyofurahia, ninatiwa moyo sana na ninapata sababu zaidi za kuendelea katika mgawo wangu na kufanya kila niwezalo.”

Wengi kati ya watafsiri hao wametumika kwenye ofisi ya tawi kwa miaka kadhaa na wengine kwa miongo mingi. Utayari wao wa kutanguliza faida za kondoo wa Yehova badala ya faida zao wenyewe unathaminiwa sana, na wanaendelea kupata baraka nyingi kwa kufanya hivyo. Ndugu mtafsiri wa lugha ya Xhosa huko Afrika Kusini alielezea kwa ufupi hisia za wengi: “Uamuzi wa kuanzisha ofisi za utafsiri ni uamuzi bora uliofanywa na Baraza Linaloongoza. Tulifurahi kuwa Betheli, lakini tunafurahi zaidi kuwa kwenye ofisi ya utafsiri.”

Habari Fupi Kutoka Sehemu Mbalimbali Ulimwenguni

“Ndugu Walishughulikia Vizuri Mahitaji Yetu”

Mnamo Jumapili, Juni 3, 2012, kulikuwa na aksidenti mbaya sana ya ndege huko Nigeria. Ndege iliyokuwa imebeba abiria 153 ilianguka katika kitongoji kimoja chenye watu wengi katika jiji kubwa zaidi la Nigeria, Lagos, na kuwaua abiria wote na idadi isiyojulikana ya watu ardhini.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Lagos, Nigeria: Baada ya ndege kuanguka

Collins Eweh na familia yake waliishi katika ghorofa ya juu kwenye jengo la ghorofa tatu lenye nyumba za kupanga lililogongwa na ndege hiyo. Aksidenti hiyo ilipotukia, familia hiyo ilikuwa ikihudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme.

Saa tisa na dakika thelathini na tano alasiri wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, Collins na mke wake Chinyere, waligundua kwamba walikuwa wamepigiwa simu mara kadhaa, lakini hawakupokea. Mikutano ilipoisha tu, Chinyere akapiga simu. Majirani walimjulisha kwamba jengo lao lilikuwa likiungua. Walipofika hapo, familia ya Eweh iliona kwamba ndege hiyo ilikuwa imegonga jengo lao na kuanguka katika jengo lililokuwa karibu ambapo ndege hiyo ilishika moto.

Chinyere anasema: “Ikiwa tungekuwa nyumbani, kwa kweli tungekufa. Baada ya msiba huo, tulibaki tu na nguo zetu za mkutano, lakini angalau tuko hai. Mwangalizi wa mzunguko alianzisha halmashauri ya kutoa msaada na ndugu walishughulikia vizuri mahitaji yetu. Tunashukuru sana.”

Collins anasema: “Watu wangu wa ukoo ambao walipinga uamuzi wangu wa kuwa Shahidi wamebadili mtazamo wao. Mmoja wao aliniambia: ‘Yehova wako hujibu sala. Shikamana sana na Mungu wako kwa sababu hukusaidia.’ Mwanamke mwingine alisema: ‘Chochote ambacho umefanya ili kumtumikia Mungu, endelea kukifanya kwa moyo wote.’ Kwa kweli tumeona msaada wa Yehova katika kisa chetu. Nina furaha sana.”

Bunge Laidhinisha Usajili wa Kanisa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Budapest, Hungaria: Ndugu zetu wakiwatolea wageni ushahidi popote wanapopatikana

Mnamo Februari 27, 2012, serikali ya Hungaria ilitumia Sheria ya Kanisa kuwatambua Mashahidi wa Yehova kama kikundi cha kidini kilichosajiliwa. Jambo hilo litasaidia sana kuhubiriwa kwa habari njema nchini Hungaria. Pia, kutambuliwa rasmi kwa Mashahidi wa Yehova kunawaruhusu kupokea michango, kutotozwa kodi, na kutembelea magereza na hospitali ili kufundisha Biblia.

Ukumbusho Uliofanywa Katika Mandhari ya Pekee

Painia mmoja wa pekee kutoka Rundu, Namibia, anaeleza kuhusu Ukumbusho aliohudhuria katika kijiji kilichokuwa karibu. Kulikuwa na watu waliopendezwa huko, na kwa hiyo akina ndugu wakaamua kwa mara ya kwanza kufanya Ukumbusho kwa kutumia lugha ya wenyeji inayoitwa Rumanyo. Aliandika: “Mandhari ilikuwa yenye kupendeza. Kulikuwa na mbalamwezi nje. Tulikuwa na taa za mafuta na tochi mbili zinazotumia betri.” Hilo liliwafanya wahisi wakiwa karibu na Yehova. Mhubiri pekee katika eneo hilo alianza kuhubiri katika mwezi wa Machi, lakini Ukumbusho ulihudhuriwa na watu 275!

Kuwekwa Wakfu kwa Ofisi za Tawi Kunamletea Yehova Heshima

Novemba 19, 2011, ni siku ya pekee katika historia ya tengenezo la Yehova katika Jamhuri ya Afrika ya Kati na Chad. Siku hiyo, ndugu na dada 269 walikusanyika mbele ya ofisi mpya ya tawi iliyokamilika. Ilipendeza kwamba Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikuwepo ili kuweka wakfu kwa Yehova Betheli hiyo mpya itumiwe kwa ajili ya utumishi Wake. Katika programu, historia ya kazi ya kuhubiri katika nchi hizo mbili ilisimuliwa. Katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kazi ya kuhubiri ilianza mwaka wa 1947 na nchini Chad ilianza mwaka wa 1959. Hotuba iliyofuata ilikuwa na maelezo hususa ya ujenzi wa ofisi na mambo yote yaliyohusika katika kukamilisha majengo hayo. Baada ya salamu kutoka nchi nyingi kusomwa, wasikilizaji walifurahia hotuba iliyotolewa na Ndugu Herd. Washiriki 42 wa familia ya Betheli wanathamini kuwa na ofisi 8 za utafsiri, jiko, chumba cha kulia, na dobi. Familia ya Betheli inaweza kufanya kazi vizuri sana kwa kuwa ina vyumba 22 vya makazi, sehemu ya mapokezi, ofisi za usimamizi, na eneo la upakizi na usafirishaji.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa ofisi ya tawi kuwekwa wakfu nchini Kongo

[Picha katika ukurasa wa 32]

Ndugu Jackson akitoa hotuba ya kuweka wakfu ofisi ya tawi, Kinshasa, Kongo

Jumamosi, Mei 26, 2012, kulikuwa na tukio la pekee sana lililoshuhudiwa na Mashahidi wa Yehova nchini Kongo (Kinshasa). Baada ya miaka minane ya ujenzi na marekebisho, ofisi ya tawi iliwekwa wakfu. Lilikuwa tukio la pekee kwa sababu, ijapokuwa ofisi ya tawi imekuwepo nchini Kongo kwa karibu miaka 50, hiyo ilikuwa programu ya kwanza kuwahi kufanywa nchini humo ya kuwekwa wakfu kwa ofisi ya tawi. Geoffrey Jackson wa Baraza Linaloongoza aliwatolea wasikilizaji 2,422 hotuba hiyo ya wakfu, na wengi wao walikuwa wamebatizwa kwa zaidi ya miaka 40. Kulikuwa na wageni 117 kutoka nchi 23. Baadhi ya wamishonari waliokuwa wametumika Kongo kwa miaka mingi walisimulia mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo. Wote walisisimuka kwa shangwe na kuazimia kutumia majengo hayo kwa ajili tu ya ibada ya Yehova.

Ripoti ya Mambo ya Kisheria

Mnamo Juni 30, 2011, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) iliamua kwamba serikali ya Ufaransa ilikiuka haki za Mashahidi wa Yehova ilipotoza kodi ya asilimia 60 ya michango yote ya Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa kati ya mwaka wa 1993 na 1996. Ingawa Mahakama hiyo iliwaruhusu wahusika wa pande zote mbili wasuluhishe suala hilo kwa njia ya kirafiki, serikali ilisisitiza kwamba kiwango hicho cha kodi kilikuwa halali na hivyo njia hiyo ya kusuluhisha mambo haikufaulu. Kwa hiyo, katika uamuzi uliofikiwa Julai 5, 2012, mahakama ya ECHR iliamuru serikali ya Ufaransa iondoe “madhara yote” ya kodi hiyo. Pamoja na kurudisha dola 5,749,440 za Marekani (euro 4,590,295) ambazo zilikuwa zimechukuliwa wakati kodi hiyo ilipotozwa (kutia ndani riba iliyopatikana tangu pesa hizo zilipochukuliwa), serikali ya Ufaransa inapaswa pia kuwalipa Mashahidi wa Yehova dola 68,890 za Marekani (euro 55,000) kwa ajili ya gharama za kushughulikia kesi hiyo.

Watumishi washikamanifu wa Yehova huko Eritrea wamenyang’anywa uraia wao kwa sababu ya msimamo wao imara wa kutounga mkono upande wowote. (Isa. 2:4) Katika kipindi cha miaka 17 iliyopita, Mashahidi wengi wamekamatwa, na kwa sasa ndugu na dada 50 kutia ndani dada waliozeeka na watoto wadogo wenye umri wa hata miaka miwili, wako gerezani. Kwa kusikitisha, mnamo Julai 2011, Ndugu Misghina Gebretin-sae alikuwa Shahidi wa kwanza kufa katika magereza ya Eritrea. Kabla ya kifo chake, alifungwa kifungo cha upweke ndani ya kontena la chuma kwa juma moja; inasemekana kwamba alikufa katika mazingira “yanayotatanisha.” Ndugu zetu wanaendelea kufanya jitihada za kukutana na wenye mamlaka ili kuwasaidia waelewe kwamba hali yetu ya kutojihusisha na vita na tamaa yetu ya kutounga mkono upande wowote haimaanishi kwamba hatuheshimu serikali ya Eritrea.

[Picha katika ukurasa wa 34]

India: Mmoja wa ndugu zetu akiwa amesimama nje ya jengo la mahakama kabla ya kupelekwa gerezani

Mashahidi wa Yehova huko India wanaendelea kuvumilia jeuri kutoka kwa vikundi vya watu wenye fujo wanaposhiriki katika huduma. Wanaume, wanawake, watoto na hata pia nyanya mwenye umri wa miaka 60 na mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu wamepigwa na kutukanwa. Wengine wamevuliwa nguo na hata kutishiwa kuuawa. Mashahidi wa Yehova wameendelea kuteseka kwa sababu ya ubaguzi na polisi kutochukua hatua. Badala ya kuwafungulia mashtaka wahalifu hao, polisi wamewakamata Mashahidi kwa mashtaka ya uwongo ya uhalifu. Mara kwa mara, wale wanaokamatwa huachiliwa kwa dhamana kubwa sana na hutukanwa na kupigwa na polisi na pia hunyimwa matibabu, chakula, na maji. Baada ya hapo, wao huvumilia miaka kadhaa ya kushtakiwa kortini kama wahalifu kabla ya kuondolewa mashtaka. Malalamishi kadhaa yamewasilishwa kwenye Halmashauri ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu kukiwa na matumaini ya kwamba Halmashauri hiyo itawasaidia ndugu zetu.

[Picha katika ukurasa wa 37]

Uturuki: Licha ya hali ngumu ambayo amekabili, Ndugu Feti Demirtaş anaendelea kuhubiri kwa bidii

Novemba 2011, mahakama ya ECHR ilifikia uamuzi usiopingwa kwamba serikali ya Uturuki ilikuwa imekiuka haki ya uhuru wa dhamiri ya Yunus Erçep, mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyeshtakiwa na kufungwa gerezani kwa kukataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Tangu mwezi wa Machi 1998, Ndugu Erçep amekuwa akiitwa ajiunge na utumishi wa kijeshi mara 39 na ameshtakiwa zaidi ya mara 30. Ndugu Erçep ametozwa faini, amefungwa jela, na kuwekwa katika hospitali ya walio na magonjwa ya akili.

Mnamo Oktoba 2004, Ndugu Erçep aliwasilisha kesi hiyo kwenye mahakama ya ECHR. Katika uamuzi uliofikiwa, mahakama ilisema: “Mshtakiwa, akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliomba asihusishwe katika utumishi wa kijeshi kwa sababu ya kushikilia imani yake ya kidini.”

Mwingine ni Feti Demirtaş, mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoka Uturuki ambaye alikataa kupokea mazoezi ya kijeshi mwaka wa 2005. Alikamatwa, akapigwa, akashtakiwa, na kufungwa gerezani kwa siku 554 hadi alipoachiliwa mnamo Juni 2007. Kwa sababu Ndugu Demirtaş hangekana imani yake inayotegemea Biblia, ripoti ilitayarishwa iliyosema kuwa ana ugonjwa wa akili. Katika uamuzi wake dhidi ya serikali ya Uturuki mahakama ya ECHR iligundua kwamba Ndugu Demir-taş aliteswa kikatili mikononi mwa wenye mamlaka wa Uturuki na kwamba haki yake ya uhuru wa dhamiri ilikuwa imekiukwa.

Maamuzi yaliyofikiwa na mahakama ya ECHR kuhusu kesi hizo mbili yanakaribiana na uamuzi mkubwa wa kihistoria wa Julai 2011 (Bayatyan v. Armenia) ambapo Baraza Kuu la ECHR lilihakikisha kwamba Mkataba wa Ulaya unalinda haki za wanaokataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Uamuzi huo unatumika katika nchi zote ambazo ni wanachama wa Baraza la Ulaya, kutia ndani Uturuki.

Mnamo Januari 2012, mahakama ya ECHR ilitoa uamuzi dhidi ya serikali ya Armenia kuhusiana na kesi ya Bukharatyan v. Armenia na Tsaturyan v. Armenia, kwamba serikali hiyo ilikuwa imepuuza uhuru wa kidini wa Mashahidi hao wawili wa Yehova ambao walikataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Mahakama hiyo ilitoa uamuzi wake mkubwa wa kihistoria kuhusiana na kesi ya Bayatyan v. Armenia.

Licha ya maamuzi hayo ya kihistoria dhidi ya serikali ya Armenia, bado serikali hiyo inaendelea kuwafungulia mashtaka, kuwahukumu, na kuwafunga gerezani wale wanaokataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Bunge halijashughulikia marekebisho ya Sheria kuhusu Utumishi wa Badala, yaliyoidhinishwa na serikali ya Armenia katika mwezi wa Machi 2012. Tunatumaini kwamba serikali ya Armenia itatumia maamuzi yaliyofikiwa na mahakama ya ECHR kwa kuwaachilia kutoka gerezani ndugu ambao wamefungwa kwa kukataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri.

Mashahidi wa Yehova huko Azerbaijan wanaendelea kukabiliana na mkazo kutoka kwa serikali: kuvamiwa na kukamatwa kwa sababu ya kuhudhuria mikutano ya kidini, kupigwa marufuku kwa machapisho ya kidini, kufukuzwa nchini kwa washiriki wa kidini ambao si wenyeji, kupigwa na kutukanwa na polisi, na kupigwa marufuku. Kuanzia wakati ambao Kamati ya Kitaifa ya Kazi Pamoja na Mashirika ya Kidini ilikataa maombi ya Mashahidi wa Yehova ya kusajiliwa tena, polisi wameendelea kuvuruga mikutano yao ya ibada, kuvuruga huduma yao, na kuzuia kuingizwa na kusambazwa kwa machapisho ya Biblia nchini humo. Mahakama zimewatoza Mashahidi wa Yehova faini kubwa kwa sababu ya kusambaza machapisho ya kidini na kuhudhuria mikutano ya kidini. Kwa mfano, dada mmoja alitozwa faini ya dola 1,909 za Marekani kwa sababu ya kuhudhuria mkutano katika jiji la Ganja. Kwa sababu matendo hayo yanakiuka haki ya uhuru wa ibada kama ilivyo katika Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu, kesi kadhaa zimewasilishwa katika mahakama ya ECHR kukiwa na matumaini ya kukomesha kuteswa na kudhulumiwa kwa Mashahidi wa Yehova huko Azerbaijan.

Maofisa wenye kutekeleza sheria kutoka sehemu mbalimbali za Urusi wanaendelea kuwadhulumu na kuwatesa Mashahidi wa Yehova na kushinikiza mahakama ziwazuie Mashahidi kumwabudu Mungu kwa uhuru. Kwa msingi wa sheria inayoshutumiwa sana ya msimamo mkali wa kidini, mahakama za Urusi zimetangaza wazi kuwa machapisho 64 ya Mashahidi wa Yehova yanachochea watu kuwa na msimamo mkali wa kidini. Hivi karibuni, mwendesha mashtaka mmoja alipendekeza kwamba kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kinachowafundisha watoto kuhusu Yesu, kitangazwe kuwa kinawachochea watu kuwa na msimamo mkali. Pia, katika sehemu nyingi za Urusi, mahakama imezuia matumizi ya Tovuti rasmi ya Mashahidi wa Yehova. Wamewaruhusu maofisa wenye kutekeleza sheria kuwapeleleza kisiri washiriki wa kutaniko, kutia ndani kutumia video ili kuwapeleleza kisiri na kuchunguza barua zao kabla hawajazipokea. Matokeo ni kwamba, polisi huwahoji kwa ukawaida majirani ambao huwapinga Mashahidi wa Yehova, hupekua nyumba za Mashahidi, na kuchukua machapisho ya kidini na vitu vingine vya kibinafsi. Mashahidi wamekamatwa wanapotembea barabarani, wanapoendesha magari yao, au wanaposhuka kutoka katika gari-moshi. Polisi wamekuwa wakikatiza mikutano ya Kikristo, na wazee wameshtakiwa kwa sababu ya kufanya ziara za uchungaji za kiroho katika kutaniko. Katika maeneo fulani, waendesha mashtaka wanajitahidi kushawishi mahakama zifutilie mbali Shirika la Kidini (LRO) la Mashahidi wa Yehova.

Kwa sababu tu ya imani yao, mnamo Mei 2012 katika jiji la Taganrog, Mashahidi wa Yehova 17 walishtakiwa kwa kupanga na kujihusisha katika uhalifu. Ilikuwa katika jiji hilo ambapo Shirika la Kidini la Mashahidi wa Yehova lilipigwa marufuku mwaka wa 2009 na Jumba la Ufalme likachukuliwa kwa amri ya mahakama kwa madai ya kwamba Mashahidi wana msimamo mkali wa kidini. Kwa kuwa walikatazwa kutumia Jumba la Ufalme, Mashahidi walikutana katika nyumba za kibinafsi au katika majumba ya kukodiwa, lakini sasa wenye mamlaka wanajitahidi kukomesha kabisa ibada. Mnamo Julai 2012, wenzi wa ndoa mapainia walipokuwa wakihubiri katika jiji moja la Siberia linaloitwa Chita, walipatikana na hatia ya uchochezi wa chuki kwa sababu ya kugawanya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kinachodaiwa kuwachochea watu kuwa na msimamo mkali wa kidini. Kila mmoja alihukumiwa saa 200 za kazi ngumu ya lazima, lakini wanakata rufaa kwa sababu ya hukumu waliyopewa.

Ingawa mahakama ya ECHR imewasaidia Mashahidi wa Yehova kupata ushindi mkubwa dhidi ya serikali ya Urusi, kama katika kesi ya Kuznetsov and Others v. Russia ya mwaka wa 2007 na kesi ya Jehovah’s Witnesses of Moscow v. Russia ya mwaka wa 2010, wenye mamlaka nchini Urusi wanaendelea kupuuza maamuzi haya ya mahakama hiyo inayoheshimiwa. Hivyo, Mashahidi wa Yehova wana kesi nyingine 19 zinazosubiri kushughulikiwa katika mahakama ya ECHR wakiwa na matumaini ya kwamba mahakama hiyo itawachochea wenye mamlaka wa Urusi waache kuwatesa watu wa Yehova na kuwaruhusu ‘waendelee kuishi maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.’—1 Tim. 2:2.

[Picha katika ukurasa wa 41]

Serikali ya Korea Kusini inaendelea kuwafunga gerezani ndugu vijana kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Kila mwezi, ndugu vijana wapatao 45 hivi hushtakiwa na kuhukumiwa mwaka mmoja na nusu gerezani. Matokeo ni kwamba, kwa sasa ndugu 750 hivi wamefungwa gerezani huko Korea. Hiyo ni idadi kubwa zaidi ya Mashahidi wa Yehova waliowahi kufungwa gerezani kwa sababu ya imani yao katika nchi yoyote ile duniani. Tangu mwaka wa 1950, Mashahidi wa Yehova 17,000 hivi wamehukumiwa kwa jumla ya zaidi ya miaka 32,000 gerezani.

Katika mwaka wa 2012, wenye mamlaka walizidisha ukandamizaji kwa Mashahidi waliokataa kujiunga na utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri, kwa kuwafunga gerezani, kwa mara ya kwanza, wale waliokataa kuwa wanajeshi wa akiba. Hapo awali, watu hao walitozwa tu faini kwa kukataa kuzoezwa kama wanajeshi wa akiba. Kwa kuwa kwa miaka mingi watu wamekuwa wakiitwa mara kadhaa ili kuzoezwa kama wanajeshi wa akiba, wale wanaokataa kujiunga na utumishi huo watakabili mashtaka mengi. Kwa mfano, mnamo Novemba 2011, Ho-jeong Son alihukumiwa kifungo cha miezi nane gerezani. Kisha, mwezi wa Juni 2012, alirudishwa mahakamani na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani. Alizuiliwa mara tu baada ya kusikilizwa kwa kesi yake ya pili na kuachiliwa kwa dhamana baada ya siku 29, huku akisubiri matokeo ya rufaa aliyokata. Kwa sasa anakabili kifungo cha miezi 14 gerezani.

Katika Korea Kusini, ndugu vijana 45 hushtakiwa na kuhukumiwa vifungo vya mwaka mmoja na nusu gerezani

Katika matukio kadhaa, Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa, imekashifu Korea Kusini kwa kukiuka haki ya kuwa na uhuru wa dhamiri. Kwa sasa, kesi kadhaa zinasubiri kushughulikiwa na Kamati hiyo na pia Mahakama ya Katiba ya Korea Kusini katika jitihada za kusuluhisha jambo hilo.

kwa Muziki Katika Mioyo Yenu” (1970)

Mwimbieni Yehova Sifa (1986)

Mwimbieni Yehova (2009)

0 50 100 150

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki