Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
Ndugu na Dada Wapendwa:
Baba yetu wa mbinguni, Yehova, ni mfano bora zaidi wa upendo. Hivyo, Biblia inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Ingawa Yehova ndiye Mweza-yote, Neno lake halisemi, “Mungu ni nguvu” au, “Mungu ni uwezo.” Anatawala akiongozwa na sifa ya upendo. Hilo linafanya tuvutiwe naye!
Inafurahisha kwamba Yehova hatulazimishi tumtumikie. Yeye si dikteta Anataka tumtumikie kwa sababu tunampenda kutoka moyoni. Tukifanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunakubali utawala wake kwa sababu tunaamini anatawala kwa haki na upendo. Hilo limeonekana tangu mwanzo wa historia ya wanadamu.
Badala ya kuwalazimisha Adamu na Hawa wamtii, Yehova aliwapa nafasi ya kujiamulia. Ikiwa kwa kweli walimpenda Yehova na kuthamini kile alichowafanyia, wangempinga Shetani alipowashawishi kuasi.
Baadaye, katika hotuba yake ya mwisho kwa taifa la Israeli, Musa alisema: “Tazama, naweka mbele yako leo uzima na mema, na kifo na mabaya.” (Kum. 30:15) Watu walikuwa na uhuru wa kuamua jinsi walivyotaka kuishi. Vivyo hivyo, Yoshua aliwaambia Waisraeli: “Ikiwa mnaona ni vibaya machoni penu kumtumikia Yehova, jichagulieni leo yule mtakayemtumikia.” Watu wakamjibu Yoshua hivi: “Ni jambo lisilowaziwa, kwa upande wetu, kumwacha Yehova.” (Yos. 24:15, 16) Sisi pia tunahisi hivyo. Kwa sababu tunampenda Yehova, ni jambo “lisilowaziwa” kwetu kumwacha.
Katika kutaniko la Kikristo, tunajua wazi kwamba kuna mambo yanayohusu dhamiri. Ingawa wazee wameruhusiwa kutoa ushauri na hata kutia nidhamu, hawatawali au kudhibiti maisha na imani ya wengine. Mtume Paulo aliandika: “Si kwamba sisi ndio mabwana juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba ninyi mnasimama.”—2 Kor. 1:24.
Jinsi inavyoburudisha kufanya jambo kwa sababu tunataka kulifanya badala ya kulazimishwa! Yehova anatualika tufanye yaliyo mema tukichochewa na upendo. Umuhimu wa jambo hilo unaonekana katika maneno haya ya Paulo yaliyoongozwa na roho: “Nikitoa mali zangu zote ili kuwalisha wengine, nami nikiutoa mwili wangu, ili nijisifu, lakini sina upendo, sipati faida hata kidogo.”—1 Kor. 13:3.
Yehova anapata shangwe na sifa kwelikweli anapoona mamilioni ya ndugu na dada zetu wakimtumikia kwa sababu wanampenda kwa moyo wote!
Naye Yehova, anawapenda sana watumishi wake wote, kutia ndani ninyi watoto na vijana ambao mnaonyesha kwamba mnampenda Yehova badala ya ulimwengu na mtazamo wake wa kibinafsi. Muwe na hakika kwamba sisi pia tunawapenda sana.—Luka 12:42, 43.
Kwa sababu mnampenda Yehova, mwa-ka jana ninyi ndugu, dada, na vijana mlitumia saa 1,748,697,447 mkihubiri habari njema. Wakichochewa na upendo, wahubiri 7,782,346 walishiriki katika huduma ya shambani ulimwenguni pote. Tunashangilia kwamba wapya 268,777 kutia ndani vijana wengi, walionyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa. Hilo linamaanisha kwamba watu 5,168 walibatizwa kila mwisho-juma. Jambo hilo linagusa sana mioyo yetu!
Katika wakati huu wa mwisho, watu wa Mungu wanakabiliana na matatizo, majaribu, mateso, magonjwa, na wengine wanapambana na uzee. Lakini tumeazimia ‘kutorudi nyuma’ au ‘kufa moyo.’ Tunawapenda sana nyote.—Ebr. 10:39; 2 Kor. 4:16.
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova