Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
RIPOTI kutoka duniani kote zinathibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova wamekuwa na shughuli nyingi sana za kuhubiri habari njema ya Ufalme “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Kwa sababu ya uvumilivu wao na kufanya kazi kwa umoja na kwa upendo bila ubinafsi, ‘neno la Yehova limevuma, na kila mahali imani yao kwa Mungu imeenea kotekote.’—1 The. 1:8.
IBADA YA FAMILIA INAYOJENGA NA KUFURAHISHA
Januari 1, 2009 (1/1/2009), Mashahidi wa Yehova walifanya mabadiliko makubwa katika ratiba yao ya mikutano ya kila juma. Jina Funzo la Kitabu la Kutaniko lilibadilishwa kuwa Funzo la Biblia la Kutaniko na lilipangwa kufanywa pamoja na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Wote walitiwa moyo wafanye Ibada ya Familia jioni ambayo hapo awali ilikuwa imetengwa kwa ajili ya Funzo la Kitabu la Kutaniko.
Watumishi wa Yehova wameitikiaje mabadiliko hayo yenye upendo? Wengi wana hisia sawa na za mume mmoja aliyeandika: “Asanteni, asanteni, asanteni. Ni vigumu kueleza jinsi ambavyo mimi na mke wangu tumenufaika na Ibada ya Familia. Upendo wetu kwa Yehova umeongezeka na tumekuwa na uhusiano wa karibu zaidi tukiwa mume na mke. Huu ni mpango mzuri na wenye hekima sana kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni!”
Familia zinafanya nini ili kutumia vizuri nafasi hii mpya na muhimu ya kujifunza pamoja? Mama mmoja aliandika: “Jioni fulani tunasoma pamoja ukurasa wa 31 wa Amkeni!, jioni nyingine tunatazama mojawapo ya video za Mashahidi wa Yehova. Watoto wanafanya utafiti wao wenyewe na wanafurahia kujifunza na kushiriki wakati wa Ibada ya Familia. Wanapewa mgawo wa kufanya utafiti mwezi mmoja kuhusu mtu fulani anayetajwa katika Biblia, kisha kutoa hotuba mwezi unaofuata. Mimi na mume wangu pia tunakuwa na migawo. Hotuba ya kwanza ya mwana wetu mwenye umri wa miaka kumi kumhusu Noa ilikuwa nzuri sana! Hata alitueleza jinsi tunavyoweza kutumia habari hiyo leo. Kisha akatuonyesha safina ndogo aliyokuwa ametengeneza ambayo inafanana na ile ya Noa. Binti yetu alikuwa na hotuba juma lililofuata kuhusu safari za umishonari za mtume Paulo. Alipomaliza, sote tulipiga makofi, kisha akatuuliza maswali katika sehemu aliyoiita, Je, Unakumbuka? Tulishangaa sana!” Familia hii imeona kwamba mpango wa Ibada ya Familia ni baraka kwelikweli kutoka kwa Yehova. “Mimi na mume wangu tulipatwa na hali ngumu sana mwaka uliopita,” mama huyo anasema, “na tulihitaji mpango huu ili kusonga mbele.”
Dada mwingine aliandika: “Ningependa kushukuru kwa mpango huu ambao umenichochea kiroho! Baada ya watoto wetu kukua na kuondoka nyumbani, mimi na mume wangu hatukufanya funzo la familia kwa ukawaida. Lakini sasa tunajifunza kwa ukawaida. Mara nyingi tunajifunza kwa muda wa saa mbili na wakati hupita haraka sana!”
Dhiki kubwa inapozidi kukaribia, wakati ambao umetenga kwa ajili ya Ibada ya Familia na ukusaidie kujifunza Neno la Mungu kwa undani zaidi na kukuimarisha kiroho kumpinga Ibilisi. Tumia vizuri nafasi hii muhimu ili ‘kumkaribia Mungu, naye atakukaribia.’—Yak. 4:7, 8.
JITIHADA NYINGI ZAIDI ZA KUANZISHA MAFUNZO YA BIBLIA
Kuanzia Januari 2009, makutaniko yalihimizwa kuteua Jumamosi (Siku ya Posho) au Jumapili (Siku ya Yenga) moja kila mwezi kwa kusudi la kuanzisha mafunzo ya Biblia. Matokeo yamekuwa nini? Wahubiri wengi wameshangaa na kufurahi sana. Wameshangaa kwa sababu kuanzisha funzo la Biblia ni rahisi kuliko vile walivyofikiri na wamefurahi kwa sababu watu tofauti-tofauti wamekubali kujifunza kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Waangalizi wanaosafiri wanasema kwamba makutaniko yanafurahia sana mpango huu mpya, na matokeo yaliyopatikana baada ya muda mfupi yanaonyesha tunaweza kutarajia matokeo mazuri zaidi. Kwa mfano, katika miezi mitano ya kwanza, mafunzo ya Biblia zaidi ya 8,000 yalianzishwa nchini Italia.
Wahubiri ambao hawajawahi kuongoza mafunzo ya Biblia sasa wanafanya ziara za kurudia na wanaanzisha mafunzo ya Biblia. Carolina, kutoka Peru, anasema: “Kabla ya mpango huu kuanzishwa sikuwa nikiongoza mafunzo yoyote ya Biblia, lakini pendekezo la kuteua siku moja kila mwezi ili kuanzisha mafunzo ya Biblia limenisaidia kuona uhitaji wa kujitahidi kuanzisha funzo la Biblia. Nimewaonyesha wenye nyumba kwamba kujifunza Biblia ni jambo rahisi lisilochukua wakati mwingi. Ninamshukuru Yehova kwa matokeo mazuri ambayo nimepata kwa kutumia mapendekezo yaliyotolewa; sasa ninaongoza mafunzo mawili ya Biblia.”
Satya, ambaye ni dada painia nchini Uingereza, alikuwa na wasiwasi kuhusu kuanzisha funzo la Biblia katika ziara ya kwanza. Lakini katika siku iliyoteuliwa kuanzisha mafunzo ya Biblia, aliazimia hatarudi nyumbani kabla ya kujaribu kuanzisha funzo la Biblia. Alifurahi mwanamke fulani alipokubali funzo la Biblia mara moja. Ilikuwa rahisi zaidi kuliko vile Satya alivyotarajia!
Luca, ndugu kijana huko Palermo, Sicily, alikuwa akimwachia mjane fulani magazeti kwa ukawaida. Mjane huyo aliogopa kumkaribisha yeyote nyumbani kwake. Jumamosi moja alasiri, siku iliyokuwa imeteuliwa kuanzisha mafunzo ya Biblia, Luca alienda kwa yule mjane huku akiwa amebeba kitabu Biblia Inafundisha kilichokuwa kimefunguliwa. Alimsomea mjane huyo sehemu fulani katika kitabu hicho. Mwanamke huyo alivutiwa na kitabu hicho na akazungumza na Luca kwa muda fulani. Luca alimwambia kwamba kitabu hicho kingemjibu maswali yake—kutia ndani swali alilokuwa ameuliza akitaka kujua kama atamwona tena mume wake aliyekufa. Luca alifungua kitabu hicho kwenye ukurasa wa 72, ambao unazungumza kuhusu wale watakaofufuliwa. Mwanamke huyo aliguswa moyo na tumaini la Biblia la ufufuo na akakubali funzo la Biblia. Sasa anajifunza kwa ukawaida, na anawakaribisha Mashahidi nyumbani kwake bila kuogopa.
Mwangalizi fulani wa mzunguko nchini Peru alisema, “Tangu uanzishwe, mpango huu umeyasaidia makutaniko mengi kuongeza idadi ya mafunzo ya Biblia yanayoongozwa. Katika muda wa mwezi mmoja, kutaniko moja huko Chiclayo lilianzisha mafunzo mapya 25, na mafunzo mapya 24 yakaanzishwa katika mji wa Chepén.”
Wahubiri vijana pia wamefaulu kuanzisha mafunzo ya Biblia. Giovanna, mwenye umri wa miaka 11 huko São Paulo, Brazili, anasema: “Jumamosi moja alasiri nilikuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba pamoja na mama yangu na tulijaribu kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa kutumia kitabu Biblia Inafundisha. Kwenye nyumba ya kwanza, nilimuuliza mwenye nyumba, ambaye ni mfanyabiashara mashuhuri, kama anaamini kwamba Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Akasema anaamini, kisha nikamwonyesha 2 Timotheo 3:16. Alisema aliguswa moyo kuona msichana mdogo akimweleza mambo mazuri kama hayo, na akachukua kitabu hicho.
“Nilipomrudia mtu huyo, niliandamana na babu yangu kwa sababu anajuana naye. Mwanamume huyo alitukaribisha, nami nikamwomba atazame ukurasa wa yaliyomo wa kitabu Biblia Inafundisha na achague habari inayompendeza zaidi. Alichagua sura ya 11, ‘Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?’ Baada ya kusoma mafungu ya kwanza mawili, yeye na mke wake waliuliza maswali mengi. Walifurahi sana kupata majibu yote katika Biblia, na wakakubali kujifunza kwa ukawaida. Nilifurahi kama nini kuanzisha funzo la Biblia kwenye nyumba ya kwanza ambapo tulihubiri!”
Bila shaka, si kila mtu atakayekubali funzo la Biblia, na sio wote wanaoanza kujifunza watakaoendelea. Lakini, kwa kuwa sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu, tunaendelea kujitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia na watu wengi iwezekanavyo, tukijua kwamba Yehova anawavuta watu wenye mfano wa kondoo kwenye tengenezo lake kabla ya kuharibiwa kwa mfumo wa mambo wa Shetani.—Yoh. 6:44; 1 Kor. 3:9.
TEKINOLOJIA YASAIDIA ‘KUHARAKISHA’ KAZI YA KUHUBIRI
Watu wa Yehova wanafurahia kutimia kwa unabii huu wenye kusisimua: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Isa. 60:22) Hapana shaka yoyote kwamba Yehova anaendelea kutumia vifaa vya kitekinolojia kuharakisha ukuzi wa kiroho nyakati hizi zenye kusisimua. Kwa hiyo, ndugu wa Baraza Linaloongoza waliwapa ndugu fulani mgawo wa kutayarisha programu ya kompyuta inayoweza kutumiwa na ofisi zote za tawi ulimwenguni.
Ndugu waliopewa mgawo huo, ambao mwanzoni walikuwa kwenye Ofisi ya Tawi ya Afrika Kusini, wamehamia Makao Makuu ya Ulimwengu huko Brooklyn, New York, ambako wanaendelea kuboresha na kutatua matatizo ya kiufundi ya programu hiyo. Ofisi za tawi zipatazo 20 zimeteuliwa kuwa vituo vya kuandaa usaidizi ili ofisi nyingine za tawi zilizo karibu zifaidike na programu hiyo nzuri ya kompyuta.
Programu hiyo ina manufaa gani? Kwa kuwa ofisi zote za tawi zinatumia programu ileile, ndugu wanaweza kupata habari kutoka ofisi nyingine. Kwa mfano, ndugu katika ofisi zote za tawi zinazofanya uchapaji wanaweza kujua vitabu ambavyo ofisi nyingine ziko navyo akibani. Ikiwa ofisi moja ina vitabu vya ziada, ofisi nyingine inaweza kuomba vitabu hivyo badala ya kuchapa vingine. Programu hiyo, iliyo na sehemu fulani zinazowawezesha ndugu kukadiria uhitaji wa vitabu wa wakati ujao kwa kutegemea maombi ya awali kutoka shambani, imesaidia ofisi zote za tawi kupunguza vitabu vya ziada.
Programu hiyo inawasaidia Wanabetheli kushughulikia vizuri maagizo ya vitabu na magazeti, kutayarisha ripoti za utumishi wa shambani za kila mwaka, kupanga makusanyiko, na kuweka rekodi zinazowahusu waangalizi wanaosafiri na mapainia wa pekee. Programu hiyo pia husaidia katika ununuzi, uwekaji wa hesabu za pesa, na kushughulikia fomu za orodha za vitabu. Kwa hiyo, hatutegemei sana programu za kompyuta za kibiashara ambazo zina gharama kubwa.
KUANGAZA NURU YA KIROHO KUPITIA INTANETI
Kama vile nuru ya kawaida inavyoweza kuangaza kwenye sehemu zenye giza, vivyo hivyo watu wa Mungu wanaendelea ‘kuacha nuru yao iangaze’ katika sehemu zote za dunia. (Mt. 5:16) Tovuti yetu rasmi kwenye Intaneti, www.watchtower.org, inatumiwa sana kuangaza nuru katika maeneo ya mbali sana. Tovuti hiyo ina makala mbalimbali za magazeti, trakti, na broshua katika lugha 383, na pia Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha 11. Kwa ujumla, kuna zaidi ya makala 700 kwenye tovuti yetu. Makala mpya kuhusu mambo yanayopendwa na watu wengi huwekwa kila juma kwenye kaya ya tovuti hiyo. Matokeo ya kuwa na habari katika lugha nyingi hivyo kwenye tovuti yetu ni nini?
Pat, anayeishi Florida, Marekani, ameona kwamba kwa kutumia tovuti hiyo anaweza kupata kwa haraka zaidi vitabu vyetu katika lugha za kigeni. Anaandika: “Tulipomaliza kugawa trakti Je, Ungependa Kujua Ukweli? nilianza kuchapa trakti hiyo katika lugha za watu ambao walichukua trakti ya Kiingereza ingawa wanazungumza lugha tofauti.” Matokeo yakawa nini?
Pat alichapa trakti ya Kithai kwa ajili ya mwanamke ambaye anamiliki kibanda katika soko fulani. Mwanamke huyo alifurahi na kushangaa kwamba Pat alipata trakti ya Kithai haraka hivyo. Mwanamke huyo na wateja wengine kwenye soko hilo walitaka kujua jina la tovuti yetu kwenye Intaneti ili waweze kupata habari hizo wenyewe. Mmoja wa wanawake hao alimwalika Pat amtembelee nyumbani kwake ili waendelee na mazungumzo yao. Kama Pat, wengi wanaona ni jambo linalofaa kuchapa kurasa kadhaa katika lugha mbalimbali kwa ajili ya watu wanaopendezwa wa mataifa mengine.
Mwaka uliopita, watu zaidi ya milioni 24 ulimwenguni pote walifungua tovuti yetu. Tangu mwaka wa 2007, wale wanaofungua tovuti yetu wameongezeka kwa asilimia 33. Watu kutoka duniani kote, na hata visiwa vya mbali, huomba funzo la Biblia au watembelewe na Mashahidi. Idadi ya wanaotuma maombi kupitia Intaneti imeongezeka kwa asilimia 55 hivi tangu 2007. Naam, nuru ya kiroho inaangaza katika sehemu za mbali zaidi za dunia, na kumletea sifa na utukufu Baba yetu wa mbinguni.—Mt. 5:16.
Zaidi ya tovuti ya www.watchtower.org, pia kuna tovuti ya www.jw.org iliyoanzishwa ili kuhakikisha kwamba vichapo fulani muhimu vinapatikana katika faili za sauti na video. Kwa nini tovuti hii ya pekee ni muhimu?
Ndugu wengi wana hisia kama za Trisha, kutoka Missouri, Marekani, aliyesema, “Ninatazamia kwa hamu sana siku ya Alhamisi (Siku ya 4).” Kwa nini? Kwa sababu Alhamisi ndiyo siku ambayo anaweza kupakua magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanayopatikana kwenye tovuti ya www.jw.org. Trisha ni mmoja kati ya maelfu ya akina ndugu na dada ulimwenguni pote ambao hufungua tovuti yetu ambayo ina chakula kingi cha kiroho. Wao hupakua faili za sauti za magazeti, Biblia, drama, vitabu, broshua, na trakti katika lugha 27. Pia chakula hicho kinaweza kupatikana katika faili mbili za video katika lugha ya ishara zinazotumiwa sana.
Ni nani wanaotumia tovuti hiyo kupakua habari katika vitabu vyetu? Inatumiwa hasa na ndugu na dada zetu wa kiroho, lakini watu wengine kutoka nchi zaidi ya 200, kutia ndani nchi kadhaa ambako kazi yetu iko chini ya vizuizi, wanaitumia pia. Watu kutoka maeneo ya Papua New Guinea, St. Helena, na hata Antaktika wanatumia tovuti yetu kwa ukawaida. Habari ambazo ndugu na dada zetu wanapakua kwenye tovuti hiyo zinawanufaishaje? Chukua kwa mfano Polinesia ya Ufaransa ambako mara nyingi magazeti yetu hufika yakiwa yamechelewa kwa sababu ya matatizo ya usafirishaji. Kwa kuwa hata wahubiri wanaoishi katika visiwa vya mbali kabisa wanaweza kutumia Intaneti, inawezekana kwao kusikiliza magazeti ya karibuni zaidi siku yanapowekwa kwenye tovuti hiyo.
Deborah, kutoka Illinois, Marekani, ana matatizo makubwa ya afya yanayofanya iwe vigumu kwake kushirikiana na kutaniko na pia kukumbuka mambo anayosoma. Sasa anapakua habari na kuzisikiliza, na anasema, “Uwezo wangu wa kukumbuka habari ninayosoma umeboreka, na ninaweza kuzungumzia mambo ambayo nimesikiliza nikiwa na uhakika.”
Mume na mke wanaoishi katika mji mdogo huko Texas, Marekani, wanajifunza Biblia na mwanamke fulani kutoka Siberia, na wanafurahi kwamba wanaweza kupakua faili za sauti za magazeti katika Kirusi kwa ajili ya mwanafunzi huyo. Ndugu fulani kutoka California, Marekani, hufurahia kukimbia asubuhi na mapema huku akisikiliza magazeti kwa kutumia kifaa cha kusikilizia habari zilizorekodiwa.
Kila juma mume na mke wanaoishi katika mji mdogo huko kaskazini mwa New Zealand hupakua habari kwenye faili za sauti kwa ajili ya mikutano. Wanapakua makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi, sura za vitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” na Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, na sehemu za Biblia zinazopaswa kusomwa kila juma. Wanasikiliza habari hizo kwa juma zima. Mume anasema, “Sasa tunaona kwamba tunazungumzia zaidi mambo ya kiroho badala ya matatizo tunayopata kazini.” Familia nyingi ulimwenguni kote zinafanya vivyo hivyo.
Kila juma, sura za Biblia zinazopaswa kusomwa hupakuliwa mara nyingi sana—hasa Jumanne (Siku ya 2). Makala ya Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya funzo la kila juma inapakuliwa mara nyingi sana kila Jumamosi na Jumapili. Isitoshe, wazee wa kutaniko wanaweza kuchapa fomu mbalimbali na mihtasari ya hotuba moja kwa moja kutoka katika tovuti yetu. Kwa ujumla, mipango hii inasaidia tengenezo kuokoa wakati, pesa, na inapunguza kazi.
“UTAKUWA USHAHIDI”
Ingawa Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuishi “maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili,” hawashangai wanapoteswa. (1 Tim. 2:1, 2) Yesu Kristo aliwaonya wanafunzi wake kuwa wangechukiwa na watu wote aliposema: “Watu watawakamata na kuwatesa, wakiwakabidhi ninyi kwenye masinagogi na magereza, mkikokotwa na kupelekwa mbele ya wafalme na magavana kwa ajili ya jina langu.” Lakini Yesu alisema kwamba mateso hayo yangekuwa na matokeo yaliyo kinyume na matarajio ya maadui wa ibada ya kweli. Alitabiri: “Utakuwa ushahidi kwenu.”—Luka 21:12, 13, 17.
Kupatana na unabii huo wa Yesu, Mashahidi wa Yehova wanakabili dhuluma katika maeneo mbalimbali. Ushindi mbalimbali ambao wamepata mahakamani katika nchi nyingi, umewasaidia kulinda uhuru wao wa kisheria, kutia ndani haki yao ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na kukutana bila vizuizi kwa ajili ya ibada. Ingawa bado kuna matatizo fulani ya kushughulikiwa, mwaka huu tumepata ushindi mbalimbali muhimu mahakamani unaothibitisha kuwa kazi yetu ni ya kidini.
Austria
Baada ya jitihada za akina ndugu za miaka 30, mnamo Mei (Mwezi wa 5) 2009, Wizara ya Elimu, Sanaa, na Utamaduni ya Austria, iliwatambua Mashahidi wa Yehova kuwa jamii ya kidini. Mashahidi ndilo shirika la 14 la kidini nchini Austria linalotambuliwa na wizara hiyo. Baada ya Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu kutoa uamuzi unaowaunga Mashahidi mkono mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2008, Mahakama hiyo ilitoa maamuzi mengine matatu yanayowaunga mkono akina ndugu nchini Austria, na kuthibitisha kabisa kwamba Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa kikamili kuwa shirika la kidini.
Afrika Kusini
Mwaka wa 2005, kesi dhidi ya Idara ya Wafanyakazi ya Afrika Kusini ilipelekwa kwenye Mahakama ya Wafanyakazi ya Afrika Kusini, kwa niaba ya shirika la Watch Tower Bible and Tract Society na Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova, ambao wanafanya kazi katika Betheli ya Afrika Kusini. Mashahidi walitaka mahakama itoe uamuzi unaothibitisha kwamba Wanabetheli hawapaswi kuhesabiwa kuwa wafanyakazi wa kuajiriwa kupatana na sheria za wafanyakazi za Afrika Kusini. Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 2009, Mahakama ya Wafanyakazi ilitoa uamuzi unaowaunga mkono Mashahidi ambao ulithibitisha kuwa Wanabetheli si wafanyakazi wa kuajiriwa na kwamba kazi wanayofanya Betheli ni ya kidini.
Uganda
Mwaka wa 2007, Idara ya Kodi ya Mapato ya Uganda ilitoa uamuzi kwamba ndugu wa Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova wanaotumika katika Betheli ya Uganda ni wafanyakazi wa kuajiriwa kupatana na Sheria ya Kodi ya Mapato ya Uganda. Kesi hiyo ilipelekwa kwenye Mahakama Kuu ya Uganda jijini Kampala kwa niaba ya Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia. Mnamo Juni (Mwezi wa 6) 2009, Mahakama Kuu ilitoa uamuzi kwamba Wanabetheli nchini Uganda si wafanyakazi wa kuajiriwa. Mahakama hasa ilizingatia kwamba Wanabetheli wote “wanapata msaada uleule hata wawe wanafanya kazi gani.” Mahakama hiyo ilimalizia kwa kusema kwamba Wanabetheli ni kikundi cha kidini na wanapokea chakula, makao, na pesa kidogo kwa ajili ya mahitaji ya kibinafsi wanapoendelea na kazi yao ya kujitolea na ya kidini nchini Uganda.
Armenia
Wenye mamlaka wanaendelea kuwakamata na kuwafunga gerezani ndugu zetu ambao wamefikia umri wa kujiunga na jeshi, na ambao wanakataa kufanya hivyo kwa sababu ya dhamiri. Kufikia Agosti (Mwezi wa 8) 2009, kulikuwa na ndugu 74 gerezani. Kwa kuwa mahakama zote nchini zimetoa maamuzi yasiyowaunga mkono, kesi nne zimepelekwa katika Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu ili ndugu hao waachiliwe. Serikali pia inaendelea kuvitoza kiwango cha juu cha Kodi ya Ongezeko la Thamani vitabu vya kidini ambavyo ndugu zetu hupokea kutoka nchi nyingine. Kama kodi hiyo isiyo halali itaendelea kutozwa au la, tuna hakika kwamba ndugu zetu wataendelea kupata chakula cha kiroho cha kutosha.—Isa. 65:13.
Azerbaijan
Uhuru wa kuabudu wa ndugu zetu nchini humo unaendelea kudidimia. Imekuwa vigumu kwao kupata vitabu na kukutanika kwa ajili ya ibada. Mashahidi wanatambuliwa kisheria katika mji mkuu Baku, lakini hawatambuliwi katika miji mingine. Kwa hiyo, mara nyingi polisi wanavamia kinyume cha sheria mikutano yao katika nyumba za akina ndugu, na kuwazuia kwenye vituo vya polisi kwa saa nyingi. Wanafanya hivyo ingawa kupatana na sheria si lazima watu wajiandikishe ili waweze kukutana katika nyumba za watu binafsi kwa ajili ya ibada. Aprili 9, 2009 (4/9/2009), ndugu zetu walipeleka ombi mahakamani wakitaka waandikishwe kisheria na serikali ya Azerbaijan. Tunatumaini kwamba wakiandikishwa kisheria, matatizo ambayo ndugu zetu wanakabili yatapungua.
Misri
Katika miaka mitatu iliyopita, ndugu kutoka Misri na pia kutoka Ubelgiji, Italia, na Marekani wamekutana mara kadhaa na wenye mamlaka nchini Misri wakitaka kazi yetu iandikishwe kisheria. Kwa hiyo, wenye mamlaka wamewapa ndugu zetu nchini Misri kibali cha kuabudu kwa amani katika nyumba za akina ndugu wakiwa vikundi vya watu 30. Hata hivyo, ndugu zetu bado wanaendelea kudhulumiwa kwa kadiri fulani. Maofisa wa Usalama wa Kitaifa wanaendelea kuwapeleleza ndugu zetu na mara kwa mara wanawahoji na kuwatisha washiriki wa kutaniko. Zaidi ya kukutana uso kwa uso na wenye mamlaka, ndugu zetu wanajitahidi kutumia njia za kisheria ili kazi yetu iandikishwe.
Eritrea
Wenye mamlaka wamepuuza kabisa haki za kimsingi za kibinadamu, na kuwakamata washiriki 23 wa kutaniko moja mnamo Juni 28, 2009, kutia ndani dada wazee na watoto wenye umri kati ya miaka miwili hadi miaka minne. Ingawa dada hao wazee wameshaachiliwa, watoto bado wako gerezani pamoja na mama zao. Baba zao walitiwa gerezani mapema kidogo. Kwa hiyo, familia nzima-nzima ziko gerezani. Sasa kuna ndugu na dada 64 gerezani. Idadi hiyo inatia ndani ndugu watatu ambao wamekuwa gerezani tangu 1994 kwa sababu ya kutojiunga na jeshi. Ndugu hao hawajawahi kuelezwa sheria ambazo inadaiwa walivunja.
India
Katika miaka michache iliyopita, Mashahidi wa Yehova nchini India wameshambuliwa na makundi ya watu wenye ghasia wanapohubiri. Pia wamevumilia matusi, kupigwa, kutishwa kufungwa gerezani, na kuteketezwa kwa vitabu vyao. Mara nyingi, baada ya kupigwa, ndugu zetu wanakamatwa na kutiwa gerezani, na wanashtakiwa kwa uhalifu. Makundi ya watu wenye hasira huwachochea wenye mamlaka katika maeneo fulani wawadhulumu ndugu zetu kwa kuwashtaki kwa uwongo kwamba wamevunja sheria.
Kwa mfano, mnamo Desemba (Mwezi wa 12) 2008, Mashahidi watatu (mama, binti yake, na mjukuu wake mwenye umri wa miaka kumi) walioishi Kundapura, Karnataka, walienda kumtembelea mwanamke wa Kijiji cha Koni aliyetaka kujifunza Biblia. Baadaye, wanaume watano au sita waliwapeleka kwa lazima Mashahidi hao watatu kwenye kituo cha polisi. Kikundi cha watu kilikusanyika, na polisi wakawashtaki dada hao kwa kosa la kuingia kwenye kijiji hicho bila ruhusa, kuchochea uadui kati ya jamii, na kutoheshimu dini nyingine. Mwishowe, Mashahidi hao waliruhusiwa kwenda nyumbani. Ndugu na dada zetu wanaokabili hali kama hizo wanasaidiwa kisheria.
Moldova
Ndugu zetu huko Transnistria, eneo la Moldova ambalo halijatambuliwa kimataifa, wanaendelea kufanya kwa bidii kazi ya Ufalme, ijapokuwa kwa miaka 12 hivi, wameendelea kupata vitisho kuwa watapigwa marufuku au kazi yao itasimamishwa. Ingawa kumekuwa na matatizo mengi, ndugu wameona baraka za Yehova na wamefaulu kwa kadiri fulani kutetea mahakamani kazi ya Ufalme. Ona visa hivi vitatu: Kasisi fulani wa Kanisa la Othodoksi ambaye aliwatukana na kuwapiga dada wawili walipokuwa wakihubiri katika kijiji cha Ordăşei alipatwa na hatia na kutozwa faini, mahakama ya jiji la Tiraspol ilitoa uamuzi mzuri kuhusiana na jitihada za akina ndugu za kutaka Mashahidi waandikishwe kisheria huko, na uamuzi mwingine ulitolewa kupinga hatua ya wakaguzi wa kodi wa jiji la Rîbniţa ya kutoza kodi chakula kilichotolewa kwa ajili ya wafanyakazi wa kujitolea waliokuwa wakijenga Jumba la Ufalme.
Kazakhstan
Ofisi ya Mwendesha-Mashtaka Mkuu wa Jamhuri ya Kazakhstan ilichochea malalamiko ambayo yalifanya mahakama itoe uamuzi uliowaunga mkono ndugu zetu. Mapema, mahakama za Kyzylorda, Shymkent, na Saryagash, zilikuwa zimeagiza kazi yetu ya kidini isimamishwe kwa miezi sita. Hata hivyo, baada ya uamuzi uliotolewa Novemba (Mwezi wa 11) 2008, ndugu katika Eneo la Kyzylorda, huko Shymkent, na eneo lote la kusini mwa Kazakhstan wanaweza kufurahia tena uhuru wa ibada. Isitoshe, mnamo Desemba 2008, mahakama ya jiji la Atyraū iliamua kuwa Mashahidi wa Yehova wana haki ya kuandikishwa kisheria katika jiji hilo, ingawa wenye mamlaka wa jiji hilo walikuwa wamepinga jambo hilo kwa miaka saba.
Urusi
Katika mwaka wa utumishi uliopita, Kituo chetu cha Usimamizi nchini Urusi kimechunguzwa tena na tena na mwendesha-mashtaka na wakuu mbalimbali serikalini, wakiwa na nia ya kusimamisha kazi yetu ya kidini isivyo haki. Ndugu na dada wanasumbuliwa na kufanyiwa uchunguzi mwingi usio na msingi. Katika kisa kimoja, mimba ya dada mmoja iliharibika baada ya polisi kuvamia mkutano wa kidini kinyume cha sheria. Mvulana wa miaka 15 aliyekuwa kwenye mkutano huo, alizuiliwa kinyume cha sheria pia. Wanaoendesha mashtaka wanatumia Sheria ya Kudhibiti Vikundi Vyenye Msimamo Mkali kama msingi wa kusimamisha kazi ya makutaniko kadhaa nchini Urusi na kupiga marufuku vitabu vyetu. Madai yasiyo na msingi kwamba Mashahidi ni kikundi chenye msimamo mkali yametumiwa na maofisa wa serikali kuwanyima akina ndugu uhuru wa ibada, kuwakamata bila sababu, kuwahamisha, na kuwazuia wasiingie nchini wawakilishi wanne wa kisheria wa Mashahidi wa Yehova kutoka nchi za kigeni waliokuwa wakiwatetea kuhusiana na madai hayo ya uwongo. Mmoja kati ya ndugu hao alitiwa kizuizini jijini Moscow kwa saa 23.
Maofisa wa Idara ya Kitaifa ya Usalama wameingilia mapatano mbalimbali ya kukodi mahali pa kufanyia mikutano na makusanyiko, na kufanya mapatano hayo yafutiliwe mbali. Wenye mamlaka pia wamezuia ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Mashahidi wanateswa wanapokuwa kwenye kizuizi cha polisi na kusingiziwa kutenda uhalifu mbalimbali.
Korea Kusini
Mnamo Juni 16, 2008, serikali ya Korea Kusini iliacha kuunga mkono tangazo ambalo ilitoa Mei 7, 2008, kwamba watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri wapewe nafasi ya kufanya utumishi wa kiraia. Serikali hiyo ilisema kwamba “suala la kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri linahitaji uchunguzi zaidi na makubaliano ya kitaifa.” Hadi leo hii, Bunge la Korea halijazungumzia mswada wowote kuhusu utumishi wa badala. Ndugu wanangoja maamuzi ya Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa, ambayo ilitoa uamuzi uliounga mkono Mashahidi kuhusiana na kesi mbili ilizoshughulikia. Mnamo Januari 2009, Tume ya Rais wa Korea ya Kuchunguza Vifo vya Wanajeshi Vinavyotiliwa Shaka ilikiri kuwa serikali ya Korea inalaumika kwa vifo vya kikatili vya Mashahidi watano ambao waliandikishwa jeshini kwa lazima kuanzia miaka ya 1970 hadi katikati ya miaka ya 1980. Huu ndio uamuzi wa kwanza muhimu unaoonyesha kwamba serikali inalaumika kwa vifo vinavyotokana na matendo ya kikatili jeshini.
Tajikistan
Shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova nchini Tajikistan lilipigwa marufuku mwaka wa 2007, na vitabu vyetu kutoka Ujerumani vikachukuliwa na maofisa wa forodha. Rufani ilikatwa kwenye mahakama ya kijeshi, na mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 2008, rufani hiyo ikakataliwa. Rufani nyingine ilikatwa kwenye Kamati ya Kijeshi ya Mahakama Kuu, ambayo pia ilikataliwa. Maamuzi hayo yanaunga mkono kupigwa marufuku kwa shirika letu na kuchukuliwa kwa vitabu vyetu. Hata hivyo, jitihada zaidi zinafanywa ili kuwasaidia ndugu zetu.
Uturuki
Ndugu nchini Uturuki wanakabili matatizo yanayohusiana na utumishi wa jeshi. Ndugu mmoja amekuwa gerezani kwa miaka miwili kwa sababu ya msimamo wake thabiti. Ndugu wengine wengi waliofikia umri wa kwenda jeshini wanaendelea kukabili vitisho vya kutozwa faini, kufungwa gerezani, na vilevile kufutwa kazi. Mnamo Machi 2009, ndugu walielezwa kwamba Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa ilikuwa imeanza kuchunguza kesi mbili zilizopelekwa kwenye kamati hiyo kwa niaba ya Mashahidi.
Isitoshe, mnamo Mei 2009, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu iliunganisha kesi tatu zinazongoja kusikizwa ili kuanza kuchunguza kama haki za kibinadamu za ndugu zetu sita zinavunjwa—wanne kati ya ndugu hao wamekaa gerezani kwa muda fulani. Watumishi wa Yehova wanashukuru kwa sababu mashirika hayo mawili ya kisheria yameonyesha nia ya kuwatetea Mashahidi, hivyo wanatumaini kwamba karibuni huenda hali zikawa bora.
Uzbekistan
Hali ya kisheria ya waabudu wa Yehova nchini Uzbekistan inaendelea kuzorota, huku ndugu zetu wakiendelea kukabili mateso yanayoungwa mkono na Serikali. Ndugu mmoja aliyeoa na ambaye ana wana wawili, aliachiliwa kutoka gerezani Mei 14, 2009, baada ya kumaliza kifungo cha miaka miwili kwa sababu ya kufundisha mambo ya dini. Siku iliyofuata alifukuzwa nchini na kurudi kwao, Tajikistan. Ndugu wengine watatu bado wamo gerezani kwa sababu ya kupanga “utendaji wa kidini kinyume cha sheria.” Mawakili wanaowakilisha ndugu hao watatu wanajitayarisha kukata rufani kwenye Mahakama Kuu ya Uzbekistan. Ndugu wa Uzbekistan na ujumbe wa ndugu kutoka nchi za nje wamekutana mara kadhaa na Kamati ya Mambo ya Dini ya Uzbekistan na wawakilishi wa kamati hiyo ili kusuluhisha mambo hayo.
MAHAKAMA YA ULAYA YA HAKI ZA KIBINADAMU
Mashahidi wa Yehova nchini Armenia, Austria, Azerbaijan, Georgia, Saiprasi, Serbia, Ufaransa, Urusi, na Uturuki wamepeleka maombi 22 ya kusikilizwa kwa kesi kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa. Maombi hayo yanataja uvunjaji wa haki za msingi za kibinadamu zinazopaswa kufurahiwa na raia wote chini ya mamlaka ya Mkataba wa Ulaya Unaohusu Haki za Kibinadamu. Maombi tisa kati ya hayo yanahusu haki ya mtu ya kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, saba zinahusu kuteswa na kubaguliwa kwa msingi wa kidini, nne zinahusu kupigwa marufuku kwa shirika la kisheria linalotumiwa na Mashahidi wa Yehova kupanga kazi yao, na mbili zinapinga hatua ya serikali ya kuingilia haki ya kukusanyika kwa amani ili kuabudu.
Mnamo Juni 17, 2008, mahakama hiyo ilianza kushughulikia ombi lililowasilishwa na shirika la Mashahidi wa Yehova (Association Les Témoins de Jéhovah) dhidi ya serikali ya Ufaransa. Ombi hilo linapinga hatua ya kibaguzi ya kuitoza kodi ya asilimia 60 michango yote ya kidini iliyopokewa kuanzia 1993 hadi 1996. Mahakama hiyo ilizusha maswali mengine ikitaka kujua kama serikali ya Ufaransa imevunja Kifungu cha 9 cha Mkataba wa Ulaya kinachohusiana na uhuru wa ibada. Sasa Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa na katika nchi nyingine ambazo ni wanachama wa Baraza la Ulaya wanangoja kuona kama mahakama hiyo itakubali kusikiliza kesi hiyo.
Ingawa Shetani anajaribu kuvuruga ibada ya kweli kwa ‘kutunga matatizo kwa njia ya amri,’ watumishi wa Yehova wanaendelea kuwa ‘imara katika imani, wakijua kwamba mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zao ulimwenguni.’ Waabudu wote wa kweli na waendelee kusimama imara kabisa kumpinga Shetani na kutupa mahangaiko yao yote kwa Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa, wakijua kwamba anawajali na atawafanya thabiti na imara.—Zab. 94:20; 1 Pet. 5:7-11.
“KUSTAHILI VYA KUTOSHA KUFUNDISHA WENGINE”
Tangu lianzishwe, kutaniko la Kikristo limekuwa likiwazoeza washiriki wake. Mtume Paulo alimwambia Timotheo: “Mambo hayo uwakabidhi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Nyakati hizi pia, tengenezo la Yehova lina programu mbalimbali za kuwazoeza watumishi wa Mungu. Kwa mfano, tangu mwaka wa 2008, wazee 6,528 kutoka maeneo yaliyo chini ya ofisi ya tawi ya Marekani—kutia ndani Alaska, Bermuda, na Visiwa vya Turks na Caicos—wamehudhuria madarasa 70 ya Shule ya Wazee wa Kutaniko kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York.
Shule hiyo inayochukua muda wa juma moja, inazingatia kwa undani sehemu mbalimbali za maisha ya wazee na kuwasaidia kuongoza katika kazi ya kuhubiri na kuwa walimu stadi zaidi kutanikoni. (2 Tim. 4:5; 1 Pet. 5:2, 3) Shule hiyo pia inawatia moyo kudumisha hali yao ya kiroho na ya familia zao ikiwa nzuri. Inawazoeza vilevile ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’ wanapowasaidia wengine. (2 Tim. 2:15) Yafuatayo ni maneno ya shukrani ya wazee wachache tu kati ya wengi waliotoa shukrani zao baada ya kuhudhuria shule hiyo.
“Walimu wetu walikuwa wanyenyekevu na hivyo, wakatuwekea kielelezo cha jinsi ya kuwatendea akina ndugu kutanikoni. Ninawashukuru sana ndugu wa Baraza Linaloongoza. Ninaona kwamba kualikwa kwenye shule hii ni pendeleo kubwa zaidi ambalo nimeonyeshwa tangu nijifunze kweli.”
“Mungu wetu Yehova anajua tunachohitaji na wakati wa kukiandaa. Imani yangu imetiwa nguvu, na hali yangu ya kiroho imeimarishwa. Shule hii imenisaidia kuthamini yale ambayo Yehova amefanya kupitia sehemu inayoonekana ya tengenezo lake na pia kuona jinsi anavyowajali watu wake wote.”
“Nimefurahia sana kuhudhuria shule hiyo. Kadiri nilivyojifunza, ndivyo nilivyotambua kuwa kuna mambo mengi sana ambayo sikuwa ninajua. Nimeanza kulithamini zaidi funzo la kibinafsi na nimetambua kwamba ni lazima mimi binafsi nifuate mambo yote niliyojifunza.”
“Mazoezi niliyopata yamenisaidia kushughulikia familia na kutaniko nikiwa na akili ya Kristo. (1 Kor. 2:16) Yamenisaidia kujichunguza mimi ni mtu wa aina gani.”
“Mambo ambayo nimejifunza kwa juma moja kupitia walimu ambao Yehova ameandaa ni muhimu kuliko elimu ya chuo kikuu.”
“Shule hii imenichochea na kuninufaisha sana! Imenitia nguvu kuendelea na utumishi wa Yehova, kujidhabihu, na kuwa mwenye kuburudisha kwa ndugu na dada zetu. (Isa. 32:2) Asante Yehova!”
“Kupitia shule hii, tumetambua jinsi Yehova anavyotupenda. Ni kana kwamba ametufanyia ziara ya uchungaji.”
“Ninamshukuru Yehova kwa pendeleo hili la kujifunza jinsi ninavyoweza kushughulikia mgawo wangu vizuri zaidi na kumletea sifa na utukufu.”
Baada ya muda, Baraza Linaloongoza litatangaza mipango kwa ajili ya wazee wa maeneo mengine ili wao pia wanufaike na mafunzo haya ya wakati unaofaa.
KUWEKWA WAKFU KWA OFISI ZA TAWI KWALETA SHANGWE
Samuel Herd wa Baraza Linaloongoza ndiye aliyekuwa msemaji anayezuru wakati ofisi mpya ya tawi ya nchi ya Tanzania, iliyoko Afrika Mashariki, ilipowekwa wakfu mnamo Januari 24, 2009. Wageni 779 wenye shangwe kutoka nchi 22 walilengwalengwa na machozi walipotafakari jinsi ambavyo kazi imesonga mbele tangu marufuku iondolewe nchini humo mwaka wa 1987. “Ni Yehova tu anayeweza kufanya jambo kama hili liwezekane nchini humu,” akasema ndugu mmoja wa zamani. Sasa kazi ya kuhubiri imepiga hatua kubwa, na wahubiri zaidi ya 14,000 wanashangilia, wanamshukuru Yehova, na kulipigia jina lake muziki.—Zab. 92:1, 4.
Jumamosi Mei 2, 2009, ndugu na dada wapatao 600 kutoka nchi 31 walisikiliza hotuba ya kuweka wakfu kwenye ofisi ya tawi ya Uholanzi iliyotolewa na Theodore Jaracz wa Baraza Linaloongoza. Sehemu ya makao iliongezwa kwenye jengo lililojengwa 1983, nayo majengo yaliyotumiwa kuchapa magazeti yakafanyiwa marekebisho na kuwa ofisi na Kituo cha Kutayarisha na Kurekodi CD na DVD. Kituo hicho kinatumiwa kutayarisha CD na DVD katika lugha 24, na nyingi kati ya hizo zinazungumzwa barani Ulaya. Isitoshe, ndugu kwenye kituo hicho wanasaidia kutayarisha video katika lugha 20 za ishara. Kazi hiyo inahusisha kusimamia utayarishaji wa CD barani Ulaya, Afrika, na Visiwa vya Bahari ya Pasifiki, na utayarishaji wa DVD ulimwenguni kote. Ofisi ya tawi ya Uholanzi pia hununua na kusafirisha vifaa vinavyohitajiwa na ofisi katika sehemu nyingine za ulimwengu, na majengo hayo yaliyofanyiwa marekebisho yanafaa sana kwa kazi hiyo.
“JITUNZENI KATIKA UPENDO WA MUNGU”
Kwa kweli, tuna sababu nyingi za kushangilia. Tumebarikiwa sana kuishi nyakati hizi zenye kusisimua! Naam, kama ilivyotabiriwa, “siku za mwisho” ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Lakini kwa kuwa ukombozi umekaribia sana, ni muhimu kila mmoja wetu aazimie kutii himizo hili la Yuda: “Ninyi, wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi, na kusali mkiwa na roho takatifu, jitunzeni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.”—Yuda 20, 21.
[Grafu katika ukurasa wa 13]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
IDADI YA WATU WANAOFUNGUA www.watchtower.org KILA SIKU
70,000
50,000
30,000
10,000
1999 2001 2003 2005 2007 2009
[Ramani katika ukurasa wa 21]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Maeneo Ambako Mambo Muhimu ya Kisheria Yameshughulikiwa Hivi Karibuni
AUSTRIA
MISRI
ERITREA
UGANDA
AFRIKA KUSINI
MOLDOVA
ARMENIA
UTURUKI
AZERBAIJAN
URUSI
KAZAKHSTAN
UZBEKISTAN
TAJIKISTAN
INDIA
KOREA KUSINI
[Picha katika ukurasa wa 11]
Hata wahubiri wachanga hufurahia kuanzisha mafunzo ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 27]
Shule ya Wazee wa Kutaniko huwasaidia kutimiza majukumu yao ya kiroho
[Picha katika ukurasa wa 28]
Ndugu Jaracz akitoa hotuba ya kuweka wakfu kwenye ofisi ya tawi ya Uholanzi
[Picha katika ukurasa wa 29]
Ndugu Herd akitoa hotuba ya kuweka wakfu ofisi ya tawi ya Tanzania