Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb08 kur. 6-29
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
  • 2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MWISHO WA DINI YA UWONGO UNAKARIBIA!”
  • KAMPENI YA PEKEE YA KUTANGAZA UKUMBUSHO
  • KUTHIBITISHA KISHERIA HABARI NJEMA
  • UAMINIFU NA UTIMILIFU
  • “FANYA MAHALI PA HEMA LAKO PAWE NA NAFASI KUBWA ZAIDI”
  • “YEHOVA AMEFANYA JAMBO KUU”
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya mwaka uliopita
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2012 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb08 kur. 6-29

Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita

MATUKIO ya mwaka uliopita yanatoa uthibitisho zaidi kwamba tunaishi mwisho kabisa wa “siku za mwisho” ambazo Neno la Mungu linazieleza kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Hata hivyo, siku za mwisho zinapozidi kuwa ngumu, baraka za Yehova kwa watumishi wake waaminifu ulimwenguni pote zinazidi kuonekana. Iwe Mashahidi wa Yehova wanapatwa na misiba ya asili, uhalifu na jeuri, magonjwa, mshuko wa moyo, uzee, upinzani, au ubaridi, kwa nguvu za Yehova wao huendelea ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yao.’—Ebr. 12:1.

“MWISHO WA DINI YA UWONGO UNAKARIBIA!”

Mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) na Novemba (Mwezi wa 11) 2006, Mashahidi wa Yehova waliongeza utendaji wao wa kuhubiri ulimwenguni pote kwa kugawa trakti Habari za Ufalme Na. 37, yenye kichwa, “Mwisho wa Dini ya Uwongo Unakaribia!” Ujumbe huo wenye kuchochea umekuwa na matokeo gani?

“Ujumbe wake ni sahihi kabisa!” akasema mwanamume fulani nchini Sweden ambaye amehangaishwa na unafiki katika dini ya uwongo. Kama mwanamume huyo, watu wengi walianza kujifunza Biblia kwa sababu ya trakti Habari za Ufalme.

Nepal

Huko Kathmandu, Dil alimpa mwanamume fulani ambaye alienda kanisani kwa ukawaida trakti Habari za Ufalme lakini mke wa mwanamume huyo alikuwa amemwacha miezi miwili hivi iliyotangulia kwa sababu ya ulevi. Dil alirudi na mume wake, Buddha, ili wazungumzie trakti Habari za Ufalme. Mwanamume huyo aliwaambia kwamba hapendi mwenendo wa washiriki fulani wa kanisa na kwamba mambo aliyosikia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova yalikuwa tofauti na yale aliyosikia kanisani. Walimwonyesha Ufunuo 18:2-4 na kukazia umuhimu wa kutoka katika “Babiloni Mkubwa.” Kwenye ziara ya tatu, walianza kujifunza somo la 13 katika broshua Anataka. Kwenye ziara ya tano, walimkuta mke wake, ambaye alikuwa amerudi nyumbani. Aliwajua Mashahidi wa Yehova na alipenda ujumbe wetu. Kwenye ziara ya saba, mume huyo na mke wake walijifunza broshua hiyo pamoja. Mke wake alisema, “Sasa mume wangu hanywi kileo.”

Brazili

Dereva wa teksi ya pikipiki ambaye alipokea trakti Habari za Ufalme aliibandika nyuma ya koti lake kwa siku kadhaa na hivyo watu wengi wakaiona. Abiria walilazimika kusoma ukurasa wa kwanza walipokuwa wakisafirishwa.

Dada wawili nchini Brazili walipokaribia nyumba fulani walishtuka kuona kibandiko kilichosema, “Unaweza kuingia, lakini hutatoka ukiwa hai.” Wakiwa na woga waliwauliza ndugu wawili wafanye nini. Ndugu hao waliamua kwenda kwenye nyumba hiyo. Baada ya kusali wapate mwongozo wa Yehova, ndugu hao walipiga makofi ili mwenye nyumba awasikie. Mwenye nyumba, ambaye alikuwa polisi, alikubali trakti Habari za Ufalme. Alieleza kwamba alikuwa akikarabati nyumba yake na alikuwa na vifaa vingi vya ujenzi upande wa nyuma wa nyumba. Kwa hiyo aliweka kibandiko hicho ili kuwaogopesha wezi. Wahubiri hao waliporudi kumtembelea, alikubali kujifunza Biblia.

Mongolia

Tsetsegmaa alijaribu kumhubiria dada yake mkubwa mara nyingi. Ingawa dada yake alihudhuria mikutano michache na akahudhuria Ukumbusho mara mbili, hakupendezwa sana na alikataa kujifunza Biblia. Lakini alipoona trakti Habari za Ufalme Na. 37 katika nyumba ya Tsetsegmaa, upendezi wake uliamshwa. Katika mazungumzo yaliyoendelea kwa saa mbili, aliuliza maswali mengi ambayo Tsetsegmaa aliyajibu kwa kutumia Biblia. Dada yake mkubwa alishangazwa na yale aliyojifunza, akataka kujifunza mengi zaidi, na sasa anafurahia kujifunza Biblia kwa ukawaida.

Georgia

Mashahidi walimpa mwanamke fulani trakti Habari za Ufalme naye aliuliza ikiwa ni ya kidini. Alipoambiwa kuwa ni ya kidini, aliichukua na akaahidi kuisoma. Mashahidi hao waliporudi, mwanamke huyo aliuliza ikiwa alikuwa amedanganywa na Kanisa Othodoksi. Alihangaishwa na hali za ulimwengu na kuzorota kwa viwango vya maadili kati ya vijana. Alisema kwamba haikuwa rahisi kupata mambo ya kuzungumzia na watoto wake. Mashahidi hao walimsomea 2 Timotheo 3:1-5, na akakubali kitabu Biblia Inafundisha. Mashahidi hao walipokuwa wakiondoka, aliwaambia hivi: “Ninasadiki kwamba dini yenu ndiyo ya kweli. Sina budi kuwapongeza vijana wenu kwa kuvalia kwa njia nzuri na kwa unyoofu wao na viwango vyao vya juu vya maadili.” Mwanamke huyo anafurahia kusoma magazeti yetu kwa ukawaida.

Bangladesh

Richel mwenye umri wa miaka 19 aligawa trakti Habari za Ufalme Na. 37 katika eneo ambalo halijawahi kuhubiriwa. Ingawa eneo hilo lilikuwa mbali na mahali ambapo Richel aliishi, bado alihisi kwamba anapaswa kwenda kwa sababu ilikuwa kampeni ya pekee. Kwenye nyumba ya pili aliyohubiri, aliwakuta wasichana wawili waliodai kuwa Wakristo ambao baba yao alikuwa amekufa miezi miwili iliyotangulia. Walimwuliza hivi: “Kwa nini Mungu aliruhusu jambo hilo litupate?” Richel aliwajibu kwa kutumia Biblia, na wasichana hao wakakubali trakti Habari za Ufalme, kisha wakamwambia, “Mungu amekutuma nyumbani kwetu.” Akitambua uhitaji wa kiroho wa wasichana hao, Richel aliwauliza ikiwa wangependa ajifunze Biblia pamoja nao. Wasichana hao walikubali mara moja. Wao ni wanafunzi wenye bidii na wana maswali mengi. Richel anahitaji kufanya utafiti mwingi, lakini anafurahia uradhi unaotokana na kuwafunza kweli watu wenye njaa ya kiroho.

Armenia

Painia wa kawaida anayeitwa Eliza alipigiwa simu na Lilit ambaye hapo awali alikuwa akijifunza naye Biblia. Alimwambia hivi: “Lazima uache mambo yote uliyopangia kesho ili uje tuanze kujifunza tena.” Kwani nini kilikuwa kimetukia? Lilit alipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, mume wake alimwambia: “Chagua utamwacha nani, mimi au Yehova.” Kwa hiyo akaacha kujifunza. Sasa, miaka miwili baadaye, alipokea trakti Habari za Ufalme Na. 37 alipokuwa akiwatembeza watoto wake bustanini. Trakti hiyo ilimfanya apendezwe sana hivi kwamba akamwambia hivi mume wake kwa ujasiri, “Huenda ukatosheka kuishi miaka 50 ukiwa na afya njema kisha ufe, lakini mimi ninataka mengi zaidi.” Kisha akamwahidi mume wake kwamba kujifunza Biblia kutamsaidia abadili utu wake usiofaa, kwa hiyo akaacha kumpinga. Sasa anafurahia kujifunza bila kupingwa na mume wake ambaye huwatunza watoto Lilit anapojifunza.

Kambodia

Wakati wa kampeni ya pekee, mmishonari anayeitwa Hugues alimtembelea mwanamume Mwislamu. Aliposoma trakti Habari za Ufalme, mwanamume huyo alikubali kuwa dini hazipaswi kujihusisha katika vita. Alisema anasikitishwa sana na dini yake kwa sababu watu wanaoshikilia sana dini waliiletea jina mbaya. Hugues alimsomea Zaburi 46:9 na kumwonyesha ahadi ya Mungu ya ulimwengu usiokuwa na vita. Juma lililofuata Hugues alimwonyesha kitabu Biblia Inafundisha. Sasa mwanamume huyo anathamini sana Biblia na anajifunza Biblia kwa kawaida.

Urusi

“Ninajua kwamba ninyi mnafundisha kweli,” akasema kasisi wa Kanisa Othodoksi ambaye alipokea nakala ya trakti Habari za Ufalme kutoka kwa dada wawili, “na kwamba Mungu wenu, Yehova, ataharibu dini zote za uwongo na kuacha yenu.” Kisha akawaambia mambo aliyojua kuhusu tumaini la kimbingu na paradiso duniani. Dada hao walimwuliza kwa nini hakuiacha dini yake ikiwa alijua kwamba itaharibiwa. Akajibu, “Ni kwa sababu ya kazi yangu. Nina nyumba tatu na magari manne. Siwezi kuacha vitu hivyo vyote.”

KAMPENI YA PEKEE YA KUTANGAZA UKUMBUSHO

Jumatatu (Siku ya 1), Aprili 2, 2007 (2/4/2007), Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walionyesha uthamini wao kwa fadhili zisizostahiliwa na upendo wa Mungu kwa kuadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Ili kujitayarisha kwa ajili ya tukio hilo muhimu, mwaliko wa pekee ulisambazwa ulimwenguni pote kuanzia Machi (Mwezi wa 3) 17 mpaka Aprili 2. Wanafunzi wengi wa Biblia na watoto walitumia kipindi hicho cha utendaji ulioongezeka kuanza kuhubiri habari njema.

Marekani

Kwa saa mbili hivi jioni ya Ukumbusho, ndugu aliyekuwa kwenye mapokezi ya makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, alipokea simu nyingi kutoka kwa watu waliokuwa wakiuliza mahali ambapo wanaweza kuhudhuria Ukumbusho. Simu kadhaa zilitoka kwa watu waliopokea mwaliko wa kuhudhuria Ukumbusho. Mwanamke mmoja alisema: “Nimefika nyumbani muda mfupi uliopita na kupata mwaliko wa kuhudhuria sherehe yenu leo. Ningependa kuhudhuria, lakini sijui itakuwa saa ngapi.”

Jacquelin mwenye umri wa miaka 16 alimpa mwalimu wake mwaliko wa Ukumbusho na kumweleza umuhimu wa tukio hilo. Alishangaa mwalimu wake alipohudhuria. Kwa kuwa programu hiyo ilikuwa ikifanyiwa kwenye Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, Jacquelin alimtembeza mwalimu wake kwenye jumba hilo baada ya Ukumbusho. Mwalimu wake alivutiwa sana na usafi na utaratibu wa kila kitu na hasa jinsi jengo hilo lilivyojengwa na kudumishwa na wajitoleaji. Baada ya kueleza jinsi alivyofurahia hotuba hiyo, mwalimu aliuliza, “Ninaweza kupata jinsi gani funzo la Biblia ambalo msemaji alitaja?” Jacquelin akamjibu kwa furaha, “Niko tayari kujifunza nawe!” Jacquelin alianza kujifunza Biblia na mwalimu wake kila Jumatatu baada ya shule.

Afrika Kusini

Kutaniko la wahubiri tisa katika eneo moja la mbali walishangaa kupokea mwaliko mmoja tu wa Ukumbusho ilhali walikuwa wameagiza mialiko 500 kutoka kwenye ofisi ya tawi. Baadaye waligundua kwamba shirika la posta lilishindwa kutambua mahali pa kupeleka furushi lililotumwa na ofisi ya tawi kwa sababu kibandiko cha anwani kilikuwa kimetoka. Wafanyakazi wa posta walifungua furushi hilo ili wajaribu kujua lilitoka wapi na lilikuwa likienda wapi. Walipoona mialiko ya Ukumbusho, waliamua kwamba ilihitaji kusambazwa, kwa hiyo wafanyakazi hao walitia mwaliko mmoja katika kila sanduku la posta, na hivyo wakagawa mialiko yote. Akina ndugu walitambua jambo hilo walipopokea, si mialiko yote bali mwaliko mmoja tu kwenye sanduku la posta la kutaniko. Wahubiri hao tisa walifurahi kama nini kuona watu 42 wakihudhuria Ukumbusho, wengi wao wakija na nakala yao ya mwaliko waliokuwa wamepata kwenye sanduku lao la posta!

Italia

Patrizia alimpa Gabriella, mwanafunzi wake wa Biblia, mwaliko na kumweleza umuhimu wa kuhudhuria Ukumbusho. Mwana wa Gabriella anayeitwa Mattia ambaye ana umri wa miaka mitano, alikuwa akisikiliza kwa makini na akaomba mwaliko ampelekee mwalimu wake. Siku iliyofuata, Mattia alimpa mwalimu wake mwaliko huo na kumweleza umuhimu wa Ukumbusho na kwamba angependa sana ahudhurie. Siku chache baadaye kulipokuwa na mkutano wa walimu na wazazi, mwalimu wa Mattia alimweleza Gabriella kwamba alivutiwa sana na usadikisho wa Mattia hivi kwamba aliamua kuhudhuria Ukumbusho. Aliandamana na Gabriella na Mattia kwenye Ukumbusho. Mwalimu alisikiliza hotuba kwa makini na akapendezwa sana na tabia nzuri ya watoto wote. Baadaye, alisema kwamba sasa anaelewa ni kwa nini Ukumbusho ni tukio muhimu, kama tu Mattia alivyosema. Tangu wakati huo, Mattia amempa mwalimu wake Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kwa ajili ya mtoto wake, na Gabriella na Patrizia wamepanga kuwa na mazungumzo pamoja naye.

Mexico

Mzee mmoja alimhubiria kasisi wa Kanisa Presbiteri na kumwalika kwenye Ukumbusho. Kasisi huyo alikubali mwaliko huo kwa furaha. Mzee huyo alishangaa kasisi huyo alipomwomba mialiko ya kuwapa waumini wa kanisa lake. Akina ndugu walifurahi kuona kasisi huyo akifika kwenye Ukumbusho akiwa na washiriki 40 wa kanisa lake, kila mmoja wao akiwa na mwaliko wake ili auonyeshe mlangoni. Kasisi huyo alisema kwamba wengine walitaka kuja lakini walifikiri kwamba hawangeruhusiwa kuingia bila mwaliko wao. Kutaniko hilo lenye wahubiri 11 lilifurahi kama nini kuwa na hudhurio la watu 191 kwenye Ukumbusho!

Australia

Kijana mmoja anayejifunza Biblia na Mashahidi alianza kuwaeleza wengine katika ukumbi wa mazoezi ambapo anafanya kazi kuhusu mambo anayojifunza. Mwanamke mmoja kati yao alikubali mwaliko wa kuhudhuria Ukumbusho. Alipokuwa kijana, mwanamke huyo aliwasikia Mashahidi wa Yehova wakiimba katika Jumba la Ufalme na akawaomba wazazi wake ruhusa ya kuhudhuria lakini wazazi wake walimkataza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, alihudhuria mikutano kadhaa lakini walipohama kutoka eneo hilo hakuwaona Mashahidi tena. Alipohudhuria Ukumbusho, alijulishwa kwa dada mmoja ambaye alianza kujifunza naye Biblia. Alianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko, na mume wake akaanza kupendezwa pia. Kwa sasa, kijana yule anayefanya kazi kwenye ukumbi wa mazoezi amestahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa na anajitahidi kufikia ubatizo.

Kazakhstan

Mwanamke mmoja aliyekuwa akipendezwa alisema kwamba hangeweza kuhudhuria Ukumbusho kwa kuwa ana watoto wadogo. Hata hivyo, siku ya Ukumbusho, binti yake mwenye umri wa miaka mitano alivalia vizuri na kwenda kwenye Jumba la Ufalme peke yake. Mwanamke huyo alipogundua kwamba binti yake hayuko, alianza kumtafuta. Alikisia kwamba huenda binti yake amehudhuria Ukumbusho na alipofika huko akamkuta kwenye Jumba la Ufalme. Sasa kwa kuwa hata yeye alikuwa amefika kwenye Ukumbusho, mama huyo aliamua kuketi kando ya binti yake na kumsikiliza msemaji kwa makini.

KUTHIBITISHA KISHERIA HABARI NJEMA

Ufaransa

Tangu 1996 watu fulani wenye mamlaka huko Ufaransa waliamua kwamba ofisi ya tawi inapaswa kulipa ushuru kwa rudishio la gharama ambalo Wanabetheli huko Louviers hupata. Hata hivyo, Machi 28, 2007, Mahakama ya Utawala ya Paris ilitoa uamuzi wa kwamba Wanabetheli hawapaswi kutozwa ushuru kwani wao hawapati mshahara. Mahakama hiyo ilisema kwamba “Mashahidi wa Yehova ambao ni Wanabetheli wanafanya kazi huko Louviers kwa sababu ya uhusiano wao wa kiroho na Mashahidi wenzao.” Uamuzi huo unathibitisha kwamba familia ya Betheli hufanya kazi ya kidini na unapatana na uamuzi mwingine uliopitishwa huko Brazili.

Katika kesi tofauti, maofisa wa jiji la Lyon walikataa kuwakodisha Mashahidi wa Yehova jumba la manispaa kwa ajili ya Ukumbusho. Hata hivyo, Machi 15, 2007, hakimu wa mahakama ya utawala aliwaamuru maofisa wa jiji hilo wawakodishe Mashahidi wa Yehova jumba hilo. Maofisa hao walikata rufaa kwa Baraza la Nchi, lakini uamuzi wa mahakama ya utawala uliungwa mkono na Baraza la Nchi, ambao ulisema kwamba uamuzi uliochukuliwa na jiji hilo ulikuwa “mzito na ulivunja sheria ya uhuru wa kukutana, ambao ni uhuru wa msingi.” Pia Baraza la Nchi liliwaamuru maofisa wa jiji hilo walipe shirika la Mashahidi wa Yehova gharama za kesi.

Licha ya uamuzi huo mzuri huko Lyon, Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa wanaendelea kupingwa na watu mmoja-mmoja, vyombo vya habari, na hata maofisa wa serikali. Kwa mfano, mnamo 2005 mbunge mmoja wa Bunge la Ufaransa aliwashutumu Mashahidi wa Yehova “kuwa wanatenda kama wahalifu kwa kuwa wao huwaachia watu wengine mzigo wa kuwalipia kodi.” Mashahidi wa Yehova walipeleka madai hayo ya uchongezi mahakamani, na mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2007 Mahakama ya Rufaa ya Rouen ilitoa uamuzi uliowaunga mkono Mashahidi, na ikasema kwamba maneno ya mbunge huyo “hayakufaa hata kidogo, na yalipita mipaka.” Serikali ya Ufaransa inaendelea kusisitiza kwamba Shirika la Mashahidi wa Yehova lilipe kodi ambazo si za haki na zilizo kinyume cha sheria. Jambo hilo limepelekwa kwenye Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR), na akina ndugu wana hakika kwamba Yehova anawategemeza.

Uzibekistani

Kumekuwa na visa zaidi ya elfu moja vilivyorekodiwa vya akina ndugu na dada kukamatwa, kutiwa mbaroni, au kushambuliwa. Wengi walikamatwa wakati wa maadhimisho ya Ukumbusho ya 2005 na 2006. Hata hivyo, tunafurahi kuripoti kwamba katika mwaka wa 2007 hakujawa na matatizo yoyote kuhusiana na Ukumbusho. Lakini kipindi hicho cha utulivu hakikudumu. Muda mfupi baadaye, ndugu na dada mmoja walikamatwa na kufungwa kwa sababu wa kufundisha mambo ya kidini. Ndugu huyo ambaye ana mke na watoto wawili alihukumiwa kifungo cha miaka miwili na akafungwa mara moja. Dada huyo alihukumiwa miaka miwili ya kifungo cha nje cha kurekebisha tabia, ambacho kinatia ndani asilimia 20 ya mshahara wake kuchukuliwa na serikali kama adhabu.

Georgia

Mei 3, 2007 (3/5/2007), ECHR ilitoa hukumu dhidi ya serikali ya Georgia kwa kuunga mkono jeuri dhidi ya Mashahidi wa Yehova na serikali hiyo ikaamuriwa iwalipe Mashahidi fidia. Kutoka Oktoba 1999 mpaka Novemba 2002, kumekuwa na mashambulizi 138 ya kijeuri dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Katika visa fulani, polisi walikuwepo lakini walikataa kuwalinda Mashahidi. Mahakama hiyo ilisema kwamba serikali ya zamani ya Georgia ilivunja Mkataba wa Ulaya Unaohusu Haki za Kibinadamu na pia ilivunja uhuru wa kidini wa ndugu zetu kwa kukataa kuwalinda dhidi ya watu wenye msimamo mkali wa kidini. Uamuzi huo ulithibitisha kwamba ECHR inaona kwamba uhuru wa kidini hauwezi kupuuzwa na kwamba lazima Mashahidi wa Yehova walindwe hata ikiwa watu wengi wanawapinga.

Eritrea

Miaka mitano baada ya serikali kuchukua msimamo mkali dhidi dini zote ambazo haziko kwenye orodha ya dini nne zinazokubaliwa na serikali, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kupingwa vikali. Hata wanapoabudu katika nyumba zao, akina ndugu hukamatwa, huteswa, na kushinikizwa wakane imani yao. Kufikia Aprili 2007, Mashahidi wa Yehova 24 walikuwa gerezani kwa sababu ya kuhudhuria mikutano, kuhubiri, au kukataa kwenda jeshini kwa sababu ya dhamiri. Mashahidi watatu walio gerezani wana umri wa miaka 60 au zaidi, kumi kati yao wamefungwa katika magereza yenye hali mbaya sana, na watatu kati yao wamekuwa gerezani tangu 1994. Ingawa jitihada za kuwasaidia akina ndugu hazijafua dafu, tunatumaini kwamba hivi karibuni watapata utulivu, na tunaendelea kutafuta mwongozo wa Yehova ambaye anawakomboa watumishi wake “kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.”—Zab. 72:14.

Andorra

Baada ya kutafuta kuandikishwa kisheria tangu 1973, hatimaye ndugu zetu waliandikishwa kisheria Desemba 14, 2006 (14/12/2006). Kuna wahubiri wa Ufalme zaidi ya 150 nchini Andorra.

Korea

Kwa zaidi ya miaka 50, akina ndugu huko Korea Kusini wamefungwa kwa kukataa kwenda kwenye jeshi. Watano kati yao wamekufa kwa sababu hiyo. Baada ya kutumia njia zote za kisheria huko Korea Kusini, Ndugu Yoon na Choi walikata rufaa kwa Kamati ya Haki za Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa. Novemba 3, 2006, kamati ilitoa hukumu dhidi ya Korea Kusini kwa kuvunja haki za kibinadamu na ikaamuru kwamba ndugu hao walipwe fidia. Pia kamati hiyo iliiambia Korea Kusini ihakikishe kwamba wanaokataa kushiriki vita kwa sababu ya dhamiri wasilazimishwe kuamua kati ya kuvunja viwango vyao na kifungo cha gereza. Kwa kawaida, ndugu 70 wanafungwa gerezani kila mwezi.

Wakati uliopita, ndugu wengi waliokabili suala hilo waliamua kukubali maamuzi ya mahakama ya kufungwa gerezani kwa mwaka mmoja na nusu. Hata hivyo, nyakati za karibuni ndugu wengi wameamua kukata rufaa na hivyo kuna kesi nyingi mahakamani. Kwa sababu hiyo, serikali ya Korea imetangaza kwamba ina mipango ya kufanya kuwe na utumishi wa badala kwa ajili ya wale ambao hawataki mazoezi ya kijeshi. Baada ya muda, tutajua ikiwa mpango huo utatekelezwa na, ikiwa mpango wenyewe utapatana na dhamiri za wale wanaoukubali.

Argentina

Mnamo Julai 2007, waziri wa masuala ya sheria na haki za kibinadamu alitia sahihi azimio lililosema kwamba Daniel Victor Guagliardo alifungwa isivyo haki kwa kukataa kwenda jeshini kwa sababu ya dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Uamuzi huo utawanufaisha wengine ambao wamefungwa isivyo haki kwa sababu ya uamuzi wao wa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu za dhamiri.

Armenia

Ndugu kumi na tisa wameshtakiwa kwa kukataa kufanya utumishi wa badala, ambao kwa kweli ungewafanya walegeze msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo. Kisha, mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 2006 barua kutoka kwa mwendesha-mashtaka mkuu iliwaambia ndugu hao kwamba kesi yao ilikuwa imetupiliwa mbali. Lakini serikali bado haijaanzisha utumishi wa badala unaomfaa Mkristo. Hivyo, kufikia katikati ya mwaka wa 2007, akina ndugu 71 hivi vijana walikuwa wanatumikia vifungo vya kufikia miaka mitatu.

Vahan Bayatyan ni mmoja wa vijana Mashahidi walioshtakiwa na kufungwa nchini Armenia. Baada ya kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja na nusu, mwendesha-mashtaka aliomba kwamba Ndugu Bayatyan apewe adhabu kali zaidi, akidai kwamba kukataa kwake utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri “hakukuwa na msingi na ni hatari.” Mahakama ya rufaa ilikubali ombi lake na ikaongeza kifungo cha Ndugu Bayatyan kwa mwaka mmoja zaidi na uamuzi huo uliungwa mkono na mahakama kuu ya nchi hiyo. Ndugu Bayatyan aliwasilisha kesi yake kwa ECHR, na mahakama hiyo ikakubali kuichunguza kesi hiyo. Tunatumaini kwamba matokeo mazuri katika kesi hiyo yatamsaidia Ndugu Bayatyan na ndugu wengine ambao wanakabili mashtaka kama yake.

Azerbaijan

Ingawa Mashahidi wa Yehova wameandikishwa kisheria nchini Azerbaijan, ndugu na dada zetu wanaendelea kukabili hali ngumu. Kwa mfano, Desemba 24, 2006, zaidi ya akina ndugu na dada na watu waliopendezwa 200 walikusanyika pamoja kwa amani huko Baku kwa mazungumzo ya Biblia wakati polisi wenye bunduki pamoja na waandishi wa habari na maofisa wa eneo hilo walipowasili mahali hapo ili kuvunja mkutano huo. Polisi ambao hawakuwa na hati ya upekuzi walivunja mlango wa jumba hilo lililokodiwa na kuwazuia wote waliokuwepo kuondoka. Watu wawili hivi waliohudhuria walipigwa. Polisi walichukua vichapo vingi vya Biblia, sanduku la michango na pesa zilizokuwamo, hati za kisheria, na kompyuta zinazotumiwa kutafsiri Biblia na vichapo vya Biblia. Wengi wa waliofungiwa waliachiliwa mwishoni mwa siku hiyo. Hata hivyo, kati yao kulikuwa na wajitoleaji sita kutoka nchi nyingine, nao walirudishwa makwao kwa madai ya kwamba walikuwa “wanafuatia propaganda ya kidini.” Akina ndugu huko wanaweza kufungwa kwa sababu ya kukataa kufanya utumishi jeshini. Pia ndugu huko wanapata matatizo ya kuingiza vichapo nchini.

Israeli

Februari 5, 2007 (5/2/2007), Mahakama ya Wilaya ya Haifa ilitoa uamuzi wa kwamba wasimamizi wa Jumba la Mikutano la Haifa (ICC) walikuwa wamewabagua Mashahidi wa Yehova kwa kukataa kuwaruhusu watumie jumba hilo kufanyia kusanyiko. Mahakama hiyo iliamuru kwamba wasimamizi hao walipe gharama za kesi kama fidia. Mkuu wa sheria alisema kwamba wasimamizi wa jumba hilo wana “wajibu wa msingi wa kushughulikia . . . wateja wao wote kwa usawa lakini hawakutekeleza wajibu wao.” Uamuzi huo utafanya iwe rahisi kwa ndugu zetu nchini Israeli kukutana katika vikundi vikubwa kwa ajili ya ibada.

Tajikistan

Vichapo vingi vilivyokuwa vikiingizwa nchini vilizuiliwa na maofisa wa forodha na wizara ya utamaduni ilihimizwa ipige marufuku vichapo vyetu na shirika letu. Kukiwa na chuki hiyo, wamishonari waliozoezwa Gileadi walilazimishwa waondoke nchini. Kisha katika Oktoba 11, 2007, wenye mamlaka walipiga marufuku utendaji wa Mashahidi wa Yehova. Akina ndugu wamekata rufaa kuhusu ukosefu huo wa haki, na tunasali kwamba Yehova atafungua njia ili kazi ya kuhubiri iendelee katika eneo hilo lenye matokeo, ambalo lilikuwa na ongezeko la asilimia 14 katika mwaka wa utumishi wa 2007.

Ukrainia

Siku moja kabla ya hotuba ya pekee kutolewa kwenye Uwanja wa L’viv Mei 12, 2007, wapinzani waliwachochea wasimamizi wa uwanja huo wawazuie Mashahidi wasiutumie. Akina ndugu waliwasiliana na maofisa wa serikali ya Ukrainia na Marekani na kuwaomba wawasadikishe wasimamizi wa uwanja wa michezo kwamba Mashahidi wa Yehova si tisho kwa jiji hilo. Bado mazungumzo hayo yalikuwa yakiendelea wakati maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipoanza kuwasili huko L’viv kwa ajili ya hotuba hiyo. Walisafiri kutoka sehemu mbalimbali za Ukrainia kwa gari, basi, na gari-moshi. Akina ndugu walikusanyika kwa amani nje ya malango yaliyofungwa ya uwanja huo wakisubiri huku wakifurahia ushirika mchangamfu na hata wakiimba nyimbo za Ufalme. Kisha, dakika 20 tu kabla ya programu kuanza, wasimamizi wa uwanja walisadikishwa wafungue malango na kuwaruhusu akina ndugu waingie. Zaidi ya ndugu na dada 27,000 walimiminika kwenye uwanja ili kufurahia hotuba yenye kutia moyo ya mwangalizi wa eneo la dunia.

Turkmenistan

Mashahidi wa Yehova hawajaandikishwa kisheria nchini humo. Baada ya muda wa utulivu, wenye mamlaka wameanza tena kuwatesa akina ndugu. Hata hivyo, ndugu na dada wanaendelea kukutana kwa busara na kuwahubiria habari njema majirani wao. (Mt. 10:16) Ndugu watatu walikamatwa kwa kukataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri. Wote walihukumiwa; wawili walipewa kifungo cha nje, lakini ndugu mmoja alihukumiwa mwaka mmoja na nusu gerezani. Kwa kuwa hali gerezani ni mbaya, akina ndugu ulimwenguni pote wamekazia fikira hali ya huyo ndugu. Ndugu ambao ni mawakili kutoka nje ya nchi hiyo walinyimwa viza ya kuingia nchini humo ili kuwakilisha akina ndugu mahakamani. Hata hivyo, serikali za kibinadamu haziwezi kuzuia sala kwa niaba ya ndugu zetu kumfikia Aliye Juu Zaidi.—1 Tim. 2:1, 2.

Kazakhstan

Maofisa sita kutoka kwa ofisi ya mwendesha-mashtaka walikatiza mkutano uliokuwa ukiongozwa katika nyumba ya dada fulani katika eneo ambalo Mashahidi wa Yehova hawajaandikishwa kisheria. Ndugu mmoja ambaye hata hakuhudhuria mkutano huo na dada watano walitozwa faini ya pesa nyingi. Wote walikata rufaa.

Uturuki

Julai 31, 2007, ofisi ya tawi ya Uturuki ilifurahi kupata barua kutoka kwa wenye mamlaka kwamba Shirika la Kuwategemeza Mashahidi wa Yehova limeandikishwa kisheria. Kuandikishwa huko kulitukia baada ya miaka miwili ya mvutano ambao ulitia ndani serikali kupeleka shirika hilo mahakamani ikidai kwamba mkataba wake ulipingana na katiba ya nchi hiyo. Baada ya mahakama ndogo huko Istanbul kuthibitisha kwamba mkataba huo haukuwa na hitilafu yoyote kisheria, serikali ilikata rufaa kwa mahakama kuu. Lakini mahakama kuu iliunga mkono uamuzi wa mahakama hiyo ndogo, na hivyo kuwezesha shirika hilo kuandikishwa kisheria. Shirika hilo jipya linawezesha kisheria ofisi ya tawi kununua na kumiliki ardhi, kukodi mahali pa kukutania kwa ajili ya kusanyiko, kupokea michango, na kutetea haki za Mashahidi wa Yehova mahakamani.

Mashahidi wa Yehova wawili walishtakiwa kwa “kuwasumbua watu” walipokuwa wakigawa trakti Habari za Ufalme Na. 37. na wakatozwa faini. Hata hivyo, Mahakama ya Amani ya Sisli huko Istanbul ilifutilia mbali faini hiyo ikisema kwamba “kuwatolea watu vichapo vya Mashahidi wa Yehova . . . ni sehemu ya uhuru wa kufikiri na kuamini” na raia wa Uturuki “wana uhuru wa kueneza imani yao.” Bado ndugu zetu Waturuki wanakabili matatizo mengine, kama vile suala la kutokuwamo, ambalo hufanya ndugu zetu ambao wamefikia umri wa kwenda jeshini wakabili hatari ya kufungwa na kutozwa faini.

Baadhi ya mambo hayo yaliyoonwa yanaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hukata rufaa kwa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu wakati nchi za Ulaya zinapopinga haki yetu ya kuabudu Mungu. Kufikia katikati ya 2007, kulikuwa na kesi 22 mbele ya mahakama hiyo zinazohusu mambo kama vile kutokuwamo, kuandikishwa kisheria, na mateso. Bila shaka, ndugu na dada zetu wanaokabili matatizo hayo, iwe ni Ulaya au kwingineko, wanahitaji sala zetu.—2 Kor. 1:10, 11.

UAMINIFU NA UTIMILIFU

Katika sehemu ya Kitabu cha Mwaka inayozungumzia mambo ya kihistoria, utasoma jinsi ndugu zetu nchini Urusi walivyodumisha utimilifu wakati wa Muungano wa Sovieti Mashahidi wa Yehova walipokuwa wamepigwa marufuku. Waliteswa kinyama. Hata hivyo, hata katika nchi ambako tuna uhuru wa kuhubiri, Shetani na uzao wake wanajaribu kuvunja utimilifu wetu kwa njia za ujanja. Lakini watumishi wa Yehova huufanya moyo wake ushangilie wanapodumisha uaminifu! (Met. 27:11) Mambo yafuatayo yaliyoonwa yanaonyesha jinsi watu wa Mungu ulimwenguni pote wanavyoendelea kuwa waaminifu na washikamanifu katika hali mbalimbali.

Sweden

Dada mmoja painia anayefanya kazi katika hospitali ya kibinafsi huwa na wakati mgumu kushinda vishawishi vya kingono kutoka kwa wafanyakazi wa hospitali hiyo. Hata hivyo, amegundua mbinu za kukabiliana na hali hiyo. Kwanza, anawaambia wafanyakazi wapya kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na mara nyingi yeye husema kwamba ameolewa. Anatumia nafasi zote anazopata kuwaambia wafanyakazi wenzake kuhusu mambo ambayo yeye na mume wake hufanya pamoja, akikazia kwamba wana uhusiano wa karibu. Anapohitaji kuzungumza na daktari kuhusu mgonjwa fulani, yeye hupanga wakutane kwenye chumba cha kulia mahali ambapo kuna watu. Ikiwa mtu anaingia ghafula kwenye chumba anachofanyia kazi na kufunga mlango, mara moja yeye husali kwa Yehova na kuwa mwenye urafiki lakini imara.

Ujerumani

Marian amefanya kazi katika kampuni moja iliyo kaskazini mwa Ujerumani kwa miaka 13. Kwa kuwa yeye hufanya kazi alasiri na jioni katikati ya juma, inakuwa vigumu kwake kuhudhuria mikutano ya jioni. Anaeleza hivi: “Jambo hilo lilinihuzunisha sana kwani nilifurahia kuhudhuria mikutano. Nilimwomba Yehova mara nyingi anisaidie nipate njia ya kuhudhuria mikutano yote.” Alisali ili apate ujasiri wa kuzungumza na mkubwa wake kazini, naye alimruhusu atoke kazini mapema siku za mikutano, mradi amemaliza kazi yake. Mpango huo ulifaulu mpaka wakati mkubwa wa Marian alibadilishwa na akapata mkubwa ambaye hakumruhusu kutoka mapema. Marian angefanya nini? Anasema: “Kwa heshima nilimwambia mkubwa wangu mpya kwamba nitazungumza na meneja wa kampuni.” Katika mazungumzo hayo na meneja, Marian alimhubiria na kumweleza sababu zake za kuhudhuria mikutano. Meneja huyo alimruhusu Marian kuondoka mapema siku za mkutano iwapo tu wafanyakazi wenzake wangekubali. Kwa hiyo Marian aliwaita wafanyakazi wenzake na kuwaeleza kuhusu mazungumzo hayo, na pia akawahubiria. Sasa Marian anaweza kuhudhuria mikutano yote ya katikati ya juma. Marian anasema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kuhudhuria mikutano, lakini kusali kwa Yehova kutoka moyoni kulinisaidia nipate nguvu zinazopita zile za kawaida.”

Uingereza

Sophie, mwenye umri wa miaka 16, anashinikizwa kwenda kwenye karamu za shule na hilo limejaribu imani yake. Anasema: “Ingawa karamu fulani zinasikika kuwa nzuri, ninajua kwamba nitajuta iwapo nitaenda kwa sababu zitatokeza hali zinazoweza kunidhuru baadaye. Msichana mmoja alinikaribisha kwenye karamu, akisema kwamba ingekuwa karamu ya kawaida tu. Lakini baadaye niligundua kwamba ilikuwa karamu ya siku yake ya kuzaliwa. Nilifurahi kwamba sikwenda kwani baadaye nilisikia kwamba wazazi wake hawakuwapo usiku huo na wengi wa marafiki wake wa shuleni walilewa. Hiyo ndiyo sababu ninafurahia zaidi kushirikiana katika tafrija na wengi wa umri mbalimbali walio katika kweli ambao wataninufaisha kiroho. Mimi na ndugu yangu huwaalika vijana na wazee nyumbani kwetu ili kucheza muziki, kuchoma nyama, au kwenda matembezi. Ninapoalikwa kwenda kwenye karamu, mimi hujiuliza jinsi karamu hiyo itakavyoathiri uhusiano wangu na Yehova. Nimekuja kugundua kwamba hukosi chochote unapofanya yaliyo mema.”

Italia

Wasichana shuleni walijaribu mara kadhaa kumtongoza Giovanni mwenye umri wa miaka 17, lakini msichana mmoja hasa ndiye aliyefanya hivyo kwa kuendelea. Alipoona kwamba Giovanni hajishughulishi naye, alimwandikia barua iliyosema: “Ninafikiri kwamba tunafaana. Ninavutiwa sana na wewe. Ninapenda utu wako na mambo mengine kukuhusu. Ninatumaini utafanya uamuzi unaofaa. Ni mimi mpenzi wako.” Barua hiyo ilimalizia kwa jina lake na akaifunga kwa kuibusu kwa midomo yake iliyopakwa rangi. “Lazima niseme kwamba siku chache zilizofuata hazikuwa rahisi,” anasema Giovanni. “Nilijiuliza ikiwa nitawahi kupata msichana mwingine mrembo kama huyo. Wanafunzi wenzangu walipogundua hilo walinitia moyo nimkubali. Waliniambia, ‘Usipoteze nafasi hii, ukimkataa wewe ni mjinga.’ Hata hivyo, nilihisi kana kwamba ninapoteza utambulisho wangu wa Kikristo. Nilisali kwa Yehova na kuzungumza na wazazi wangu ambao mwanzoni walishangaa kwa kuwa hawakufikiri ningeweza kupatwa na hali kama hizo. Tulifanya utafiti mwingi wa Biblia pamoja, hasa kwa kutumia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Nilizungumza pia na ndugu wakomavu kutanikoni. Mwishowe, nilifanya uamuzi unaofaa na kumkataa msichana huyo. Sasa wanafunzi wenzangu wananiheshimu zaidi kwa sababu ya uthabiti wangu.”

Mexico

“Nilipokuwa na umri wa miaka 19,” anasema Antonio mwenye umri wa miaka 59, ambaye amebatizwa kwa miaka 37, “iligunduliwa kwamba nina ugonjwa wa yabisi-kavu. Inahuzunisha sana kuwa na ugonjwa ambao umenifanya nisiweze kufanya chochote na nikae tu kwenye kiti chenye magurudumu kwa miaka 35. Nyakati nyingine mimi huvunjika moyo. Lakini mimi huimarishwa kwa kufanya mengi katika utendaji wa Kikristo kadiri afya yangu inavyoniruhusu.” Miaka saba iliyopita, mama ya Antonio alikufa na hivyo kufanya hali ya Antonio kuwa ngumu zaidi kwani yeye ndiye aliyekuwa akimtunza. Antonio angefanya nini? “Tangu wakati huo,” anasema, “nimeona jinsi Yehova anavyowasaidia watumishi wake badala ya kuwaacha. Kutaniko lilifanya mipango ili ndugu mmoja anitunze na ndugu fulani husaidia kulipia mahitaji yangu ya lazima.” Antonio anatamani wakati ambapo ahadi zote za Ufalme zitatimia.

“FANYA MAHALI PA HEMA LAKO PAWE NA NAFASI KUBWA ZAIDI”

“Fanya mahali pa hema lako pawe na nafasi kubwa zaidi. Nao wanyooshe hema la maskani yako kuu.” (Isa. 54:2) Utimizo mkubwa wa maneno hayo ya kinabii unaweza kuonekana katika uhitaji wa mahali pa ibada na ofisi kubwa zaidi za tawi. Mbali na ujenzi mwingine uliofanywa ulimwenguni pote mwaka uliopita, kuwekwa wakfu kwa ofisi sita za tawi zifuatazo kulikuwa chanzo cha shangwe kubwa kwa Mashahidi wa Yehova.

Puerto Riko

Miaka 13 tu baada ya ujenzi wa ofisi ya tawi kumalizika, kulikuwa na uhitaji wa upanuzi kwa sababu idara kadhaa zilikuwa zimepanuka. Hotuba ya kuwekwa wakfu ilitolewa Jumamosi (Siku ya Posho), Septemba 16, 2006 na ndugu David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

Kolombia

Akina ndugu na dada kutoka nchi 30 walikusanyika kwenye ofisi ya tawi ya Kolombia Novemba 11, 2006, ili kufurahia kuwekwa wakfu kwa majengo yaliyopanuliwa huko Facatativá, kilomita 42 kaskazini-magharibi ya Bogotá. Watu 3,605 walihudhuria tukio hilo. Wengi ambao hawakuwa wameonana kwa miaka 30 au 40 walikumbatiana kwa upendo, na wote walifurahia hotuba ya wakfu iliyotolewa na ndugu Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

Fiji

Dakika tano tu kutoka katikati ya Suva, mji mkuu wa Fiji, kuna ofisi maridadi ya tawi, karibu na bandari. Jumamosi, Novemba 11, 2006, ndugu Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya wakfu mbele ya wasikilizaji 410.

Burundi

Novemba 25, 2006, ilikuwa siku isiyoweza kusahauliwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi hii maridadi ya Afrika ya kati. Watu 1,141 kutoka nchi 11 walifurahi kushiriki na ndugu Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, katika kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya maridadi ya tawi. Baraka za Yehova zinaonekana wazi na kuna uwezekano wa watu wengi zaidi kujiunga nasi katika kumwabudu Yehova.

Rwanda

Baada ya miaka 30 yenye msukosuko, kutia ndani kupigwa marufuku na vita vya wenyewe kwa wenyewe, ndugu na dada nchini Rwanda walifurahi kuwa na ndugu Guy Pierce kwenye kuwekwa wakfu kwa ofisi mpya maridadi ya tawi ambayo imejengwa katika bustani zenye kupendeza.

Licha ya matukio yenye kusikitisha ya mauaji ya kikabila, ambayo yalisababisha ndugu kadhaa kuuawa, kazi ya Yehova imeendelea kunawiri katika nchi hii inayojulikana kama Nchi ya Milima Elfu Moja. Watu 553 ambao walifurahia programu ya wakfu Jumamosi, Desemba 2, 2006, walitia ndani wajumbe 112 kutoka nchi 15.

Uganda

Ofisi mpya ya tawi iliyo kusini mwa mji mkuu, Kampala, iliwekwa wakfu Jumamosi, Januari 20, 2007 (20/1/2007). Watu 665 waliohudhuria walitia ndani wajumbe 170 kutoka ofisi 20 za tawi kutia na ndugu Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliyetoa hotuba ya wakfu.

“YEHOVA AMEFANYA JAMBO KUU”

Bila shaka, tuna sababu ya kuwa na shangwe tunapofikiria utendaji wa ajabu wa Yehova mwaka uliopita. Kwa umoja, tunarudia maneno yenye uthamini ya mtunga-zaburi aliyesema: “Yehova amefanya jambo kuu katika yale ambayo ametufanyia. Tumekuwa na shangwe.”—Zab. 126:3.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kweli Ilikuwa Kampeni ya Ulimwenguni Pote

Watu kadhaa katika sehemu mbalimbali walijiuliza ikiwa kweli trakti Habari za Ufalme ilikuwa ikisambazwa ulimwenguni pote. Kwa mfano, mwenye nyumba fulani huko Brazili ambaye alikuwa na shaka alimwambia mhubiri angoje ampigie simu rafiki yake huko Marekani ili ajue ikiwa alikuwa ameipata. Rafiki yake akamjibu, “Ndiyo, nimepata nakala moja dakika kumi zilizopita.” Akiwa ameshangaa, mwenye nyumba huyo alikubali trakti Habari za Ufalme na akaahidi kuisoma kwa makini.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kulikuwa na mwaliko mmoja tu katika sanduku la posta la kutaniko

[Picha katika ukurasa wa 25]

Antonio akiwa tayari kwenda kuhubiri

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Ofisi za Tawi Zilizowekwa Wakfu

Puerto Riko

Rwanda

Kolombia

Burundi

Fiji

Uganda

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki