Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
Mashahidi Wenzetu wa Yehova:
Mtume Paulo alitumia kila nafasi kuwaonyesha waamini wenzake upendo na uthamini. Aliwaandikia hivi Wakristo huko Roma: “Namshukuru Mungu wangu kupitia Yesu Kristo kuhusu ninyi nyote, kwa sababu imani yenu inazungumzwa kotekote ulimwenguni.” (Rom. 1:8) Ndiyo, katika Milki yote ya Roma, Wakristo hao wa karne ya kwanza walijulikana kwa imani yao yenye nguvu na pia bidii yao katika kazi ya kuhubiri. (1 The. 1:8) Haishangazi kwamba Paulo aliwapenda sana ndugu hao!
Kama Paulo alivyofanya, sisi pia tunamshukuru Yehova kila wakati tunapowafikiria. Tunawapenda sana ninyi nyote! Na unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anawapenda ninyi nyote mmoja-mmoja. Wengine kati yenu mnakabili mateso makali, lakini mnaendelea kuhubiri. Moyo wa Yehova unashangilia kama nini anapoona roho ya ujasiri mnayoonyesha!—Met. 27:11.
Unaposoma kwa makini na kutafakari “Utendaji wa Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa” katika Kitabu cha Mwaka huu chenye mambo ya kusisimua na kujenga imani, utaona uthibitisho wa kwamba Bwana Yesu Kristo anaenda “akishinda na kukamilisha ushindi wake” na kwamba silaha yoyote itakayofanywa juu ya wafuasi wa Kristo haitafaulu.—Ufu. 6:2; Isa. 54:17.
Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Filipi: “Namshukuru Mungu wangu . . . kwa sababu ya mchango ambao mmeutoa kwa ajili ya habari njema.” (Flp. 1:3-5) Sisi washiriki wa Baraza Linaloongoza tunahisi vivyo hivyo kuwahusu. Katika mwaka wa utumishi wa 2007, wahubiri 6,691,790 walitumia saa 1,431,761,554 kuhubiri habari njema katika nchi 236 ulimwenguni pote. Mnajitahidi sana kuendeleza habari njema! Hebu fikiria mamia ya maelfu ya watu ambao wameguswa kwa sababu ya jitihada zetu zote. Sifa na zimwendee Yehova.
Wakati mwingine, Paulo aliwaonyesha ndugu zake hisia-mwenzi. Aliwaandikia hivi Wathesalonike: “Daima sisi hukumbuka akilini . . . uvumilivu wenu kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu wetu na Baba.” (1 The. 1:2, 3) Ndiyo, maisha hayakosi matatizo. Lakini matatizo yanapotokea, ni muhimu tuvumilie. Wewe binafsi unapata matatizo gani? Je, umevunjika moyo kwa sababu ugonjwa mbaya unakuzuia usitimize mengi katika utumishi wa Yehova? Je, mwenzi wako mpendwa wa ndoa wa miaka mingi amechukuliwa na adui asiyetosheka, Kaburi? (Met. 30:15, 16) Je, ni kana kwamba umekosa kupata mwenzi wa ndoa ambaye anampenda Yehova huku ukijitahidi kufuata shauri la Kimaandiko la kuoa katika Bwana tu? (1 Kor. 7:39) Je, unajitahidi kulea watoto katika hali mbaya sana za kiuchumi? Hata hali yako iwe gani, ukitanguliza mambo ya Ufalme akilini, unahakikishiwa kwamba Yehova ‘hatasahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ Tafadhalini akina ndugu na dada ‘msife moyo katika kufanya yaliyo mema’!—Ebr. 6:10; Gal. 6:9.
Ni nini kitakachokusaidia kuvumilia? Kama tu Wathesalonike, unaweza kuvumilia ukiwa na ‘tumaini katika Bwana wetu Yesu Kristo.’ Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kulinganisha “tumaini la wokovu” na kofia ya chuma ambayo inamlinda Mkristo kutokana na mawazo yasiyofaa na mashaka yoyote.—1 The. 5:8.
Kwa kweli, unapovumilia kwa shangwe unaandaa jibu kwa dhihaka za Shetani katika suala kuu la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima. Shetani anadai kwamba watumishi wa Mungu wana ubinafsi na kwamba ingawa wanaweza kuwa tayari kumtumikia Mungu kwa muda mfupi, watapunguza bidii yao katika ibada majaribu yakiongezeka au mfumo wa mambo ukiendelea kwa muda mrefu kuliko walivyotarajia. Una pendeleo la kuonyesha kwamba Ibilisi ni mwongo kabisa! Kila siku inayopita inakuleta karibu zaidi na kutimizwa kwa tumaini lako.
Kama vile Paulo alivyotumia nafasi zote kuwapongeza akina ndugu kwa imani yao yenye nguvu, michango yao ya ukarimu kwa kazi ya kuhubiri, na uvumilivu wao, sisi pia tunatumia nafasi hii kuwapongeza na kuwahakikishia kwamba tunawapenda sana. Endeleeni na roho hiyohiyo!
Ni tumaini letu kwamba mwaka ujao utakuwa na baraka nyingi za kiroho. Tunawatakia mema, sisi ni
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova