Kitabu cha Biblia Namba 52—1 Wathesalonike
Mwandikaji: Paulo
Mahali Kilipoandikiwa: Korintho
Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 50 W.K.
1. (a) Wathesalonike wa Kwanza ilikujaje kuandikwa? (b)Hiyo ilikuwa wakati gani, na hivyo barua hiyo ina upekee gani?
ILIKUWA karibu mwaka 50 W.K. kwamba mtume Paulo, wakati wa ziara yake ya pili ya kuhubiri, akatembelea jiji la Makedonia la Thesalonike na huko akaanzisha kundi la Kikristo. Katika muda wa mwaka mmoja, akiwa katika Korintho akiandamana na Silwano (Sila wa kitabu cha Matendo) na Timotheo, Paulo alichochewa kuandika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike ili kuwafariji na kuwajenga katika imani. Yaelekea ilikuwa mwishoni-mwishoni mwa 50 W.K. Yaonekana kwamba barua hii ndiyo yenye upekee wa kuwa ya kwanza kati ya miandiko ya Paulo kuwa sehemu yenye kukubalika ya Biblia na, isipokuwa labda Gospeli (Injili) ya Mathayo, ndicho kitabu cha kwanza cha Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kutiwa katika maandishi.
2. Kuna uthibitisho gani juu ya uandikaji na uasilia wa Wathesalonike wa kwanza?
2 Ushuhuda wenye kuunga mkono uasilia na ukamilifu wa barua hii ni mwingi mno. Paulo ajitambulisha mwenyewe kwa jina kuwa ndiye mwandikaji, na kitabu hiki kina upatano wa kindani pamoja na sehemu nyingine yote ya Neno lililopuliziwa na Mungu. (1 The. 1:1; 2:18) Waraka huu watajwa kwa jina katika orodha za mapema kabisa za Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu, kutia na Muratorian Fragment.a Wathesalonike wa Kwanza ama imenukuliwa au kutajwa na wengi wa waandikaji wa mapema wa makundi, kutia na Irenaeus (karne ya pili W.K.), ambaye aitaja kwa jina. Chester Beatty Papyrus No. 2 (P46), la karibu 200 W.K., lina Wathesalonike wa Kwanza, na funjo jingine la karne ya tatu (P30), ambalo sasa liko katika Ghent, Ubelgiji, lina vipande vya Wathesalonike wa Kwanza na wa Pili pia.b
3, 4. Ni nini kilichotokana na mafanikio ya mapema ya huduma ya Paulo huko Thesalonike?
3 Kutupia jicho historia fupi ya kundi la kule Thesalonike, kabla ya kuandikwa kwa barua hii, huthibitisha hali zilizofanya Paulo awahangaikie kwa kina kirefu akina ndugu katika jiji hilo. Kuanzia pale pale mwanzoni, kundi lilipatwa na mnyanyaso mkali na upinzani. Katika Matendo sura ya 17, Luka huripoti kuwasili kwa Paulo na Sila huko Thesalonike, “ambapo palikuwa na sinagogi la Wayahudi.” Kwa Sabato tatu, Paulo aliwahubiri, akisababu nao kutokana na Maandiko, na kuna vionyeshi vya kwamba alibaki huko muda mrefu hata zaidi ya huu, kwa maana alikuwa na wakati wa kujiimarisha katika biashara yake na, juu ya yote, kusimamisha na kupanga kundi kitengenezo.—Mdo. 17:1; 1 The. 2:9; 1:6, 7.
4 Maandishi katika Matendo 17:4-7 husimulia waziwazi sana tokeo la kuhubiri kwa mtume katika Thesalonike. Wakiwa na wivu juu ya mafanikio ya huduma ya Kikristo ya Paulo, Wayahudi walipanga kitengenezo kundi lenye ghasia na kufanya jiji lile lijawe na fujo. Walishambulia nyumba ya Yasoni na kumburuta yeye na ndugu wengine mpaka kwa watawala wa jiji, huku wakipaaza sauti hivi: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako, na Yasoni amewakaribisha; na hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema [ya] kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.” Yasoni na wale wengine walishurutika kutoa dhamana kabla hawajaachiliwa. Kwa ajili ya akina ndugu katika kundi, na pia kwa ajili ya usalama wao wenyewe kibinafsi, Paulo na Sila walisafirishwa usiku waende Beroya. Lakini kundi huko Thesalonike lilikuwa sasa limesimamishwa imara.
5. Paulo alionyeshaje hangaiko lake na upendezi wenye upendo katika kundi la Thesalonike?
5 Upinzani mkali kutoka kwa Wayahudi ulifuatia Paulo kule Beroya na kutisha kusimamisha kuhubiri kwake huko. Ndipo yeye akahamia Athene, katika Ugiriki. Bado alitamani sana kujua jinsi ndugu zake katika Thesalonike walivyokuwa wakiendelea chini ya dhiki. Alijaribu mara mbili kuwarudia, lakini kila wakati ‘Shetani alizuia safari yake.’ (1 The. 2:17, 18, NW) Kwa kujawa na hangaiko kwa kundi hilo changa na akijua sana dhiki ile waliyokuwa wakipitia, Paulo alimtuma Timotheo arudi Thesalonike kufariji akina ndugu na kuwaimarisha katika imani. Timotheo aliporudi na ripoti yake ya kuchangamsha moyo, Paulo aliona shangwe nyingi mno kwa kupata habari juu ya ukamilifu wao usiotikisika katikati ya mnyanyaso wenye jeuri. Kwa sasa kumbukumbu ya matendo yao ilikuwa imekuwa kielelezo kwa waamini kotekote katika Makedonia na Akaya. (1:6-8; 3:1-7) Paulo alimtolea asante Yehova Mungu kwa uvumilivu wao wa uaminifu, lakini pia akatambua kwamba walipokuwa wakiendelea kukua mpaka ukomavu, wangehitaji mwongozo na shauri zaidi. Kwa hiyo, akiwa katika Korintho pamoja na Timotheo na Silwano, Paulo aliandika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike.
YALIYOMO KATIKA WATHESALONIKE WA KWANZA
6. Paulo awapongeza Wathesalonike kwa jambo gani?
6 Wathesalonike ni kielelezo kwa waamini wengine (1:1-10). Paulo aanza barua yake kwa Wathesalonike kwa pongezi changamfu kwa kazi yao ya uaminifu, kazi-jasho yenye upendo, na uvumilivu katika tumaini. Habari njema zilizohubiriwa miongoni mwao hazikuwa zimekuwa kwa uneni tu bali ‘pia kwa nguvu na usadikisho imara.’ Kwa kuiga kielelezo walichopewa, Wathesalonike walikuwa wamelikubali neno ‘wakiwa na shangwe ya roho takatifu’ na wao wenyewe walikuwa wamekuwa kielelezo kwa waamini wote katika Makedonia, Akaya, na hata ng’ambo ya huko. Walikuwa wamegeuka kabisa kutoka kwenye sanamu zao, “ili kutumikia Mungu aliye hai na wa kweli, na kungojea Mwana wake kutoka kwenye mbingu.”—1:5, 6, 9, 10, NW.
7. Paulo na waandamani wake walikuwa wameonyesha mtazamo gani walipokuwa miongoni mwa Wathesalonike, na walikuwa wamewahimiza kufanya nini?
7 Hangaikio lenye upendo la Paulo kwa Wathesalonike (2:1–3:13). Baada ya kutendewa kwa ufidhuli katika Filipi, Paulo na waandamani wake walijipa ujasiri kuwahubiri Wathesalonike. Walifanya hivyo, si wakiwa wapendeza wanadamu wala wenye kusifu-sifu wala wenye kutafuta utukufu kutoka kwa wanadamu. Kinyume cha hilo, Paulo asema, “tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho [nafsi, NW] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (2:7, 8) Waliendelea kuwahimiza Wathesalonike, kama vile baba hufanyia watoto wake, ili wazidi kutembea kama istahilivyo Mungu, aliyekuwa akiwaita kwenye Ufalme na utukufu wake.
8. Wathesalonika wamekuwaje shangwe kubwa kwa Paulo, naye asali nini kwa ajili yao?
8 Paulo awapongeza kwa upesi wao wa kukubali habari njema kama ilivyo, “neno la Mungu.” Hawako peke yao katika kunyanyaswa na wananchi wa kwao wenyewe, kwa maana waamini wa kwanza katika Yudea walipata minyanyaso kama hiyo mikononi mwa Wayahudi. Akiwa na wasiwasi wa kujua hali njema yao, katika pindi mbili Paulo alitaka kuwajia yeye mwenyewe lakini akazuiwa na Shetani. Kwa Paulo na wafanya kazi wenzake, ndugu Wathesalonike ni taji ya furaha, “utukufu na shangwe” yao. (2:13, 20, NW) Alipokuwa hawezi kuvumilia tena ukosefu wa kupata habari kuwahusu, Paulo alimtuma Timotheo aende Thesalonike ili kuimarisha imani yao na kuwafariji. Timotheo ametoka tu kurudi akiwa na habari njema za ufanisi wao wa kiroho na upendo, na hii imemletea mtume faraja na shangwe. Paulo ampa Mungu asante na asali kwamba Bwana apate kuwapa ongezeko, ili kwamba wao wapate kuwa na wingi katika kupendana, na kwamba mioyo yao ipate kuwa ‘isiyolaumika katika utakatifu’ mbele za Mungu Baba wakati wa kuwapo kwa Bwana Yesu.—3:13, NW.
9. Paulo ahimiza nini kuhusu utakaso na kupendana?
9 Kutumikia katika utakaso na heshima (4:1-12). Paulo awapongeza Wathesalonike kwa kuwa na mwenendo wenye kupendeza Mungu, naye awahimiza waendelee kufanya hivyo kwa ukamili zaidi. Kila mmoja “ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima; si katika hali ya tamaa mbaya [hamu ya kutamani ngono, NW].” Katika hili, hakuna mmoja apaswaye kuingilia haki za ndugu yake. Kwa maana Mungu hakuwaitia ‘uchafu, bali wawe katika utakaso. Basi yeye anayekataa, hakatai mwanadamu bali Mungu.’ (4:4, 5, 7, 8) Paulo awapongeza Wathesalonike kwa sababu wanaonyeshana upendo, na awahimiza waendelee kufanya hivyo kwa kipimo kamili zaidi, wakifanya iwe shabaha yao kuishi kwa utulivu na kushika lao wenyewe na kufanya kazi kwa mikono yao. Kwa maana ni lazima watembee kama inavyostahili “habari ya watu walio nje.”—4:12, NW.
10. Akina ndugu wapaswa kuwa na mtazamo gani kwa habari ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo?
10 Tumaini la ufufuo (4:13-18). Kwa habari ya wale wanaolala katika kifo, ni lazima akina ndugu wasiwe na sikitiko kama wafanyavyo wale wasio na tumaini. Ikiwa imani yao ni kwamba Yesu alikufa na kuinuka tena, vivyo, pia, Mungu kupitia Yesu atawainua wengine ambao wamelala usingizi katika kifo. Wakati wa kuwapo kwa Bwana, atashuka kutoka mbinguni kwa wito wenye nguvu, “na wale walio wafu katika muungano pamoja na Kristo watainuka kwanza.” Baadaye, wale wenye kubaki hai ‘watanyakuliwa katika mawingu ili kulaki Bwana katika hewa,’ wakawe pamoja na Bwana sikuzote.—4:16, 17, NW.
11. Kwa nini yawapasa Wathesalonike wakae macho, na yawapasa wafulize kufanya nini?
11 Kuemdlea kuwa macho huku siku ya Yehova ikaribiapo (5:1-28). “Siku ya Bwana [Yehova, NW] yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.” Ni wakati ambapo watu wasema “Kuna amani na salama”! kwamba uharibifu wa ghafula utakuwa juu yao papo hapo. Kwa hiyo, acheni Wathesalonike wakae macho kama “wana wa nuru, na wana wa mchana,” wakiwa waangalifu katika fahamu zao na ‘kujivika kifuani imani na upendo, na chapeo ya tumaini la wokovu.’ (5:2, 3, 5, 8) Huu ni wakati wao wa kuendelea kufarijiana na kujengana. Acheni wote wawape “ufikirio uzidio ule wa kawaida katika upendo” wale wanaofanya kazi kwa bidii na kusimamia miongoni mwao. Kwa upande mwingine, ni lazima wasio na utaratibu waonywe kwa upole, walio dhaifu wajengwe, na lazima wote waonyeshwe ustahimilivu. Ndiyo, aandika Paulo, “sikuzote fuatieni lililo jema nyinyi kwa nyinyi na kwa wengine wote.”—5:13, 15, NW.
12. Mwishowe Paulo atoa shauri juu ya mambo gani muhimu, naye amaliziaje barua yake kwa Wathesalonike?
12 Mwishowe, Paulo ashauri juu ya mambo kadhaa yaliyo muhimu: ‘Sikuzote shangilieni. Salini bila kukoma, toeni asante kwa kila jambo. Dumisheni moto wa roho. Mwe na staha kwa mambo yaliyosemwa kwa unabii. Hakikisheni mambo yote na mshike sana lililo zuri. Shikeni mwiko wa kila namna ya uovu.’ (5:16-22, NW) Kisha asali ili yule yule Mungu wa amani awatakase kabisa na kwamba wabaki bila lawama katika roho, nafsi, na mwili wakati wa kuwapo kwa Bwana Yesu Kristo. Yeye amalizia barua yake kwa maneno machangamfu ya kitia-moyo na kwa agizo la uzito kwamba ndugu wote wasomewe barua hii.
KWA NINI NI CHENYE MAFAA
13. Paulo na waandamani wake walikuwa kielelezo bora katika nini, na wonyesho wenye nia wa upendo una tokeo gani katika kundi?
13 Katika barua hii Paulo alionyesha roho ya hangaiko la upendo kwa ajili ya ndugu zake. Yeye na wahudumu wenzake walikuwa wameweka kielelezo bora cha shauku nyororo, wakitoa si habari njema tu za Mungu bali pia nafsi zao wenyewe kwa ajili ya ndugu zao wapendwa katika Thesalonika. Acheni waangalizi wote wajitahidi kufanyiza vifungo hivyo vya upendo pamoja na makundi yao! Wonyesho huo wa upendo utachochea wote waonyeshe upendo kwa ajili ya mmoja na mwenzake, sawa na alivyosema Paulo: “Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu.” Upendo huo unaoonyeshwa kwa nia miongoni mwa watu wa Mungu ni wenye kujenga sana. Hufanya mioyo iwe ‘imara bila lawama katika utakatifu mbele za Mungu, Baba yetu, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu pamoja na watakatifu wake wote.’ Huwaweka Wakristo kando na ulimwengu uliopotoka usio na adili ili waweze kutembea katika utakatifu na utakato na hivyo kumpendeza Mungu.—3:12, 13; 2:8; 4:1-8.
14. Wathesalonike wa Kwanza ni kielelezo bora cha shauri lenye busara na upendo katika njia gani?
14 Barua hii yatoa kigezo bora cha shauri lenye busara, lenye upendo ndani ya kundi la Kikristo. Ingawa ndugu Wathesalonike walikuwa wenye bidii na waaminifu, kulikuwako mambo ya kusahihiswa yaliyotaka kufanywa. Hata hivyo, katika kila kisa, Paulo aliwapongeza akina ndugu kuhusu sifa zao nzuri. Kwa kielelezo, katika kuonya juu ya uchafu wa kiadili, yeye kwanza awapongeza juu ya kutembea ili kumpendeza Mungu na kisha awasihi wafanye hilo kwa “kuzidi sana,” kila mmoja akitunza chombo chake katika utakato na heshima. Kisha, baada ya kuwapongeza juu ya upendo wao wa kidugu, yeye awahimiza waendelee katika njia hiyo kwa ‘kuzidi sana,’ wakishika yao na kuishi maisha ya adabu mbele za wale walio nje. Kwa busara Paulo aelekeza ndugu zake ‘wafuatie lililo jema, wao kwa wao na kwa watu wote.’—4:1-7, 9-12; 5:15.
15. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo alihubiri kwa bidii tumaini la Ufalme alipokuwa Thesalonike, na ni shauri gani zuri alilotoa kuhusiana na hilo?
15 Katika pindi nne Paulo ataja “kuwapo” (NW) kwa Yesu Kristo. Kwa wazi Wakristo hao waliotoka kuongolewa karibuni kule Thesalonika walipendezwa sana na fundisho hilo. Alipokuwa katika jiji lao, bila shaka Paulo alikuwa amehubiri kwa ujasiri kuhusu Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo, kama inavyoonyeshwa na shtaka lililoelekezwa kwake na kwa waandamani wake: “Hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema na kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.” (Mdo. 17:7; 1 The. 2:19; 3:13; 4:15; 5:23) Ndugu hao Wathesalonike walikuwa wameweka tumaini lao juu ya Ufalme na, wakiwa na imani kuelekea Mungu, walikuwa wakingojea “Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu,” ili awakomboe na hasira ambayo ingekuja. Vivyo hivyo, wote wanaotumainia Ufalme wa Mungu leo wahitaji kutii shauri zuri la Wathesalonike wa Kwanza wazidi sana katika upendo, mioyo ikiwa imara na isiyo na lawama, ili waendelee ‘kuenenda kama ilivyo wajibu wao kwa Mungu, mwenye kuwaita ili waingie katika ufalme wake na utukufu wake.’—1 The. 1:8, 10; 3:12, 13; 2:12.
[Maelezo ya Chini]
a Ona chati “Orodha Zenye Kutokeza za Mapema za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo,” ukurasa 303.
b The Text of the New Testament, cha Kurt na Barbara Aland, kilichotafsiriwa na E. F. Rhodes, 1987, kurasa 97, 99.