Kitabu cha Biblia Namba 53—2 Wathesalonike
Mwandikaji: Paulo
Mahali Kilipoandikiwa: Korintho
Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 51 W.K.
1. Ni nini chaonyesha wakati na mahali pa kuandikia, na ni nini kilichofanya barua ya pili kwa Wathesalonike iandikwe?
BARUA ya pili ya mtume Paulo kwa Wathesalonike ilifuata kwa ukaribu ile ya kwanza. Twajua kwamba iliandikwa muda mfupi baada ya barua ya kwanza, na pia kutoka jiji lile lile la Korintho, kwa ajili ya ndugu wale wale, Silwano na Timotheo, wajiunga tena na Paulo katika kusalimu kundi huko Thesalonike. Wote walikuwa watumishi wenye kusafiri wa kundi la mapema la Kikristo, na hakuna maandishi ya kuonyesha kwamba wote watatu walikuja pamoja tena baada ya ushirika huo katika Korintho. (2 The. 1:1; Mdo. 18:5, 18) Habari na asili ya mazungumzo yaonyesha kwamba Paulo alihisi uhitaji wa kufanya haraka kusahihisha kundi hilo kwa haraka kuhusu kosa fulani ambamo lilikuwa limetumbukia.
2. Ni nini hushuhudia uasilia wa Wathesalonike wa Pili?
2 Uasilia wa barua hii washuhudiwa vizuri kwa kadiri ile ile kama uasilia wa Wathesalonike wa Kwanza. Pia imenukuliwa na Irenaeus (karne ya pili W.K.) na pia na waandikaji wengine wa mapema, kutia na Justin Martyr (pia wa karne ya pili), ambaye yaonekana wazi arejezea 2 Wathesalonike 2:3, NW, anapoandika juu ya ‘mtu wa kuasi sheria’ [dhambi].’ Yaonekana katika orodha zile zile za mapema kama Wathesalonike wa Kwanza. Ingawa sasa yakosekana katika Chester Beatty Papyrus No. 2 (P46), yakaribia kuwa hakika kwamba ilikuwamo katika kurasa mbili za kwanza kati ya saba zenye kukosekana baada ya Wathesalonike wa Kwanza.
3, 4. (a) Ni tatizo gani lililokuwa limetokea katika kundi la Thesalonike? (b) Barua hii iliandikwa lini na wapi, na Paulo alitafuta kutimiza nini kwayo?
3 Kusudi la barua hii lilikuwa nini? Kutokana na shauri ambalo Paulo aliwatolea Wathesalonike, twajifunza kwamba watu fulani katika kundi walikuwa wakishindania kwamba kuwapo kwa Bwana kulikuwa karibu, kwamba wakisiaji hawa walikuwa wakihubiri kwa bidii nadharia (kisio) hii yao, na kwamba walikuwa wakikoroga sana mambo katika kundi. Yaonekana kwamba baadhi yao hata walikuwa wakitumia jambo hili kuwa udhuru wa kutofanya kazi ya kujipatia riziki. (2 The. 3:11) Katika barua yake ya kwanza, Paulo alikuwa amefanya marejezo ya kuwapo kwa Bwana, na bila shaka, wakisiaji hawa waliposikia barua hiyo ikisomwa, walifanya haraka kupotoa maneno ya Paulo na kusoma ndani yayo maana ambazo hazikukusudiwa kamwe. Pia yawezekana barua fulani iliyohesabiwa kuwa ya Paulo kwa makosa ilifasiriwa kuwa ilionyesha kwamba “siku ya Bwana [Yehova, NW] imekwisha kuwapo.”—2:1, 2.
4 Yaonekana kwamba Paulo alikuwa amepokea ripoti juu ya hali hii, labda kutoka kwa mtu aliyepeleka barua yake ya kwanza kwenye kundi hilo, na kwa hiyo angekuwa akitaka sana kusahihisha kufikiri kwa ndugu zake ambao alikuwa na shauku nyingi sana kwao. Kwa hiyo katika mwaka 51 W.K., Paulo, kwa kushirikiana na waandamani wake wawili, alipeleka barua kutoka Korintho kwa kundi katika Thesalonike. Zaidi ya kusahihisha maoni yenye makosa juu ya kuwapo kwa Kristo, Paulo awapa kitia-moyo kichangamfu ili wasimame imara katika ukweli.
YALIYOMO KATIKA WATHESALONIKE WA PILI
5. Paulo na waandamani wake wamtolea Mungu asante kwa jambo gani, wao watoa uhakikishio gani, na watoa sala juu ya nini?
5 Ule ufunuo wa Bwana Yesu (1:1-12). Paulo na waandamani wake wamtolea Mungu asante kwa sababu ya ukuzi mzuri wa imani ya Wathesalonike na upendo wao kuelekeana. Uvumilivu na imani yao chini ya minyanyaso ni uthibitisho wa hukumu adilifu ya Mungu kwamba wao wanahesabiwa kuustahili Ufalme. Mungu atalipa dhiki kwa wale wenye kuleta dhiki kwenye kundi, naye atawapa kitulizo wale wenye kuteseka. Hiyo itakuwa “wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake . . . atakapokuja ili kutukuzwa katika watakatifu wake.” (1:7, 10) Paulo na waandamani wake husali sikuzote kwa ajili ya Wathesalonike, ili kwamba Mungu apate kuwahesabu kuwa wenye kustahiki wito Wake na kwamba jina la Bwana Yesu lipate kutukuzwa katika wao, na wao katika muungano pamoja naye.
6. Ni nini ambacho lazima kije kabla ya siku ya Yehova, na jinsi gani?
6 Uasi-imani kuja kabla ya kuwapo kwa Yesu (2:1-12). Akina ndugu hawapaswi kusisimuliwa na ujumbe wowote kwamba siku ya Yehova imefika. “Haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu [uasi-imani, NW]; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu.” Sasa wao wajua lile “lizuialo,” lakini fumbo la huu uasi-sheria tayari lafanya kazi. Hili lizuialo liondolewapo, “hapo ndipo atakapofunuliwa yule mtu wa kuasi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo [udhihirisho, NW] wa kuwapo kwake.” Kuwapo kwa yule mtu wa kuasi ni kulingana na utendaji wa Shetani pamoja na kazi zenye nguvu na udanganyifu, na Mungu anaruhusu utendaji wa makosa uwaendee wale ambao hawakuukubali upendo wa ule ukweli ili wapate kuuamini uwongo.—2:3, 6, 8.
7. Ndugu hao wawezaje kusimama imara na kulindwa kutoka kwa yule mwovu?
7 Simameni imara katika imani (2:13–3:18). Paulo aendelea kusema hivi: ‘Imetupasa sisi kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, ndugu mliopendwa na Bwana [Yehova, NW], kwa kuwa Mungu amewachagua tangu mwanzo mpate wokovu, katika kutakaswa na roho, na kuiamini kweli.’ Kwa kusudi hilo habari njema zilijulishwa rasmi kwao. Kwa hiyo ndugu hao wapaswa kusimama imara na kudumisha mshiko wao juu ya mapokeo waliyofundishwa, kwamba Yesu Kristo na yule Baba, ambaye kwa upendo alitoa faraja na tumaini la milele, wapate kuwafanya “imara katika kila neno na tendo jema.” (2:13, 17) Paulo aomba sala zao, ili “neno la Bwana [Yehova, NW] liendelee, na kutukuzwa.” (3:1) Bwana, aliye mwaminifu, atawaimarisha na kuwazuia na yule mwovu, na ni sala ya Paulo kwamba Bwana aendelee kuelekeza mioyo yao kwa mafanikio ikaingie ndani ya upendo wa Mungu na ndani ya uvumilivu kwa ajili ya Kristo.
8. Ni onyo gani kali ambalo latolewa, na ni wapi ambamo Paulo na kikundi chake wameweka kielelezo?
8 Onyo kali lafuata: “Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu.” (3:6) Mtume awakumbusha juu ya kielelezo ambacho kikundi chake cha umisionari kiliweka, kikifanya kazi-jasho usiku na mchana ili kisiwe gharama kwao, hivi kwamba kikaweza kutoa agizo hili: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” Lakini sasa wao wasikia kwamba watu fulani wasio na utaratibu hawafanyi kazi na ni wenye kujiingiza katika mambo ya wengine. Hawa wapaswa kuanza kujipatia chakula chao wenyewe.—2 The. 3:10; 1 The. 4:11.
9. Paulo asema nini juu ya kufanya yafaayo na kumwaibisha asiye mtiifu, naye amaliziaje barua yake?
9 Akina ndugu hawapaswi kuchoka na kuacha kufanya yafaayo. Lakini ikiwa mmoja wao si mtiifu kwa barua ya Paulo, kundi lapaswa kumwaibisha kwa kumtia alama na kutoshirikiana naye tena, wakati ule ule likimwonya kama ndugu. Paulo atoa sala ya kwamba Bwana wa amani apate kuwapa “amani daima kwa njia zote,” na amalizia barua yake kwa salamu za mwandiko wake mwenyewe.—2 The. 3:16.
KWA NINI NI CHENYE MAFAA
10. Ni yapi baadhi ya mafundisho na kanuni za msingi zinazozungumzwa katika Wathesalonike wa Pili?
10 Barua hii fupi kwa Wathesalonike iliyopuliziwa na Mungu yagusia sehemu mbalimbali za kweli za Kikristo, zote zikiwa zina mafaa kwa ajili ya ufikirio. Fikiria mafundisho na kanuni za msingi zifuatazo ambazo zimezungumzwa: Yehova ndiye Mungu wa wokovu, naye hutakasa kwa roho na imani katika ukweli (2:13); lazima Mkristo avumilie kuteseka ili ahesabiwe astahili Ufalme wa Mungu. (1:4, 5); Wakristo watakusanywa pamoja kwa Bwana Yesu Kristo wakati wa kuwapo kwake (2:1); Yehova ataleta hukumu ya uadilifu juu ya wale wasiotii habari njema (1:5-8); wale walioitwa watatukuzwa katika umoja na Kristo Yesu, kwa kupatana na fadhili zisizostahilika za Mungu (1:12); wanaitwa kupitia kuhubiriwa kwa habari njema (2:14); imani ni takwa la muhimu (1:3, 4, 10, 11; 2:13; 3:2); yafaa kufanya kazi kwa ajili ya kujipatia riziki binafsi katika huduma; ikiwa mtu hafanyi kazi, aweza kuwa mvivu na kuanza kujiingiza katika mambo yasiyomhusu (3:8-12); upendo wa Mungu washirikishwa na uvumilivu (3:5). Jinsi hazina ya habari yenye kujenga inavyoweza kupatikana katika barua moja fupi iliyopuliziwa na Mungu!
11. Ni habari na uhakikisho gani wenye maana unaotolewa kwa kuhusiana na Ufalme?
11 Katika barua hii Paulo alionyesha hangaiko la kina kirefu kwa ajili ya hali njema ya kiroho ya ndugu zake katika Thesalonike na kwa ajili ya umoja na fanaka ya kundi. Aliwasahihisha juu ya wakati wa siku ya Yehova, akiwaonyesha kwamba kwanza lazima “mtu wa kuasi” atokee, aketi katika “hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu.” Hata hivyo, ‘waliohesabiwa wastahili kuuingia ufalme wa Mungu’ waweza kuwa na uhakikisho kamili kwamba Bwana Yesu kwa wakati wake atafunuliwa kutoka mbinguni, akilipa kisasi katika moto wenye kuwaka “atakapokuja ili kutukuzwa katika watakatifu wake, na kustaajabiwa katika wote waliosadiki katika siku ile.”—2:3, 4; 1:5, 10.