“Msikate Tamaa Katika Kutenda Mema”
Mambo Makuu Kutokana na Wathesalonike wa Pili
HANGAIKO la mtume Paulo kwa Wakristo katika jiji la Makedonia la Thesalonike lilimsukuma awaandikie barua yake ya pili, karibu mwaka 51 W.K. Watu fulani katika kundi walikuwa wakisema kimakosa kwamba kuwapo kwa Yesu Kristo kulikaribia. Labda hata barua moja iliyohesabiwa bila usahihi kuwa ya Paulo ilifasiriwa kuonyesha kwamba “siku ya Bwana [Yehova, NW]” ilikuwa imewasili.—2 Wathesalonike 2:1, 2.
Kwa hiyo kufikiri kwa Wathesalonike fulani kulitaka rekebisho. Katika barua yake ya pili, Paulo aliwapongeza kwa imani yao yenye kukua, upendo wenye kuongezeka, na uvumilivu wenye uaminifu. Lakini pia alionyesha kwamba uasi-imani ungekuja kabla ya kuwapo kwa Yesu. Hivyo basi kulikuwa na nyakati ngumu huko mbele, na barua ya mtume ingewasaidia kutii hili onyo la upole: “Msikate tamaa katika kutenda mema.” (2 Wathesalonike 3:13) Maneno ya Paulo yaweza kutusaidia sisi katika njia iyo hiyo.
Ufunuo na Kuwapo kwa Kristo
Kwanza Paulo alisema juu ya kupata kitulizo kutoka kwenye dhiki. (1:1-12) Hicho kingekuja “wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake.” Ndipo uharibifu wa milele ungeletwa juu ya wale wasiotii habari njema. Inafariji kukumbuka jambo hili tupatwapo na dhiki mikononi mwa wanyanyasi.
Halafu, Paulo alionyesha wazi kwamba “yule mtu wa kuasi” angefunuliwa kabla ya kuwapo kwa Kristo. (2:1-17) Wathesalonike hawakupaswa kusisimuliwa na ujumbe wowote wenye kudokeza kwamba “siku ya Bwana [Yehova, NW]” ilikuwa tayari juu yao. Kwanza, uasi-imani ungetukia na yule mtu wa kuasi angefunuliwa. Baada ya hapo, Yesu angemfanya kuwa si kitu, akifanya hivyo kwenye udhihirisho wa kuwapo Kwake. Kwa sasa, Paulo alisali kwamba Mungu na Kristo wafariji mioyo ya Wathesalonike na kuwafanya “imara katika kila neno na tendo jema.”
Kushughulika na Wasio na Utaratibu
Kati ya maneno zaidi ya Paulo kulikuwa na maagizo juu ya kushughulika na watu wasio na utaratibu. (3:1-18) Alionyesha uhakika kwamba Bwana angewaimarisha Wathesalonike na kuwazuia na yule mwovu, Shetani Ibilisi. Lakini walihitaji kuchukua hatua fulani-fulani kwa ajili ya manufaa yao wenyewe ya kiroho. Walipaswa kujitenga na wasio na utaratibu, wale wenye kuingilia mambo yasiyowahusu na kukataa kufanya kazi. “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” Watu wa jinsi hiyo walipaswa kutiwa alama, na hakukupaswa kuwe kushirikiana nao, ingawa walipaswa kuonywa kama akina ndugu. Wakristo Wathesalonike waaminifu hawakupaswa kukata tamaa katika kufanya yaliyo mema, na Paulo alitamani kwamba fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja nao wote.
Barua ya pili ya Paulo kwa Wathesalonike huwapa Mashahidi wa Yehova uhakikisho wa kwamba kitulizo cha kuwatoa kwenye dhiki yao kitakuja wakati Kristo na malaika zake waletapo kisasi juu ya wale wasiotii habari njema. Pia inaimarisha imani kujua kwamba “yule mtu wa kuasi” (jamii ya makasisi wa Jumuiya ya Wakristo) na dini bandia yote atakomeshwa karibuni. Kwa sasa, acheni sisi tutii onyo pole la Paulo na tusikate tamaa katika kufanya yaliyo mema.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Neno la Yehova Linasonga Kasi: “Tuombeeni,” akaandika Paulo, “neno la Bwana [Yehova, NW] liendelee [kasi, NW, au, “liwe likikimbia”], na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu.” (2 Wathesalonike 3:1; Kingdom Interlinear) Wanachuo fulani wamedokeza kwamba mtume alikuwa akidokeza wakimbiaji wenye kwenda kasi katika mbio. Ingawa hilo halina uhakika, Paulo aliomba sala za Wakristo Wathesalonike ili yeye na wafanya kazi wenzake waweze kueneza neno la ukweli kwa hima na bila kizuizi. Kwa sababu Mungu hujibu sala za jinsi hiyo, neno lake ‘linaendelea [kasi, NW]’ wakati habari njema zihubiriwapo hima katika hizi siku za mwisho. Pia neno la Yehova ‘linatukuzwa,’ linapewa staha nyingi na waamini kuwa “uweza wa Mungu uuletao wokovu,” kama lilivyokuwa kati ya Wathesalonike waliolikubali. (Warumi 1:16; 1 Wathesalonike 2:13) Sisi tunafurahi kama nini kwamba Mungu anabariki wapiga mbiu ya Ufalme na kwamba anaongeza kasi idadi za waabudu wake!—Isaya 60:22.