Wewe Ni Mfuasi wa Mfano wa Kristo au Wewe Ni Mkristo wa Kujifanya Tu?
—Ujumbe mbalimbali wa Paulo kwa Wathesalonike
MTUME Paulo alikuwa Mkristo mwenye kuweka mfano mwema. Kwa sababu yenye alifuata mfano wa Yesu kwa juhudi angeweza kupendekeza kwa kufaa ili wenzake walio katika imani wafanye hivi: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Mwendo wa maisha ya Paulo na kufundisha kwake ulisaidia wengi wa watu wa siku zake waipate ile “Njia” ya Ukristo wa kweli na kuendelea kuifuata.—Matendo 9:2.
Paulo alihangaikia wengine kwa upendo. Kwa kufaa sana, wakati Mungu alipoagiza Paulo na Sila waliache eneo la Asia na kuanza kazi ya misionari katika Makedonia, Yeye alimpa Paulo njozi akaona mwanamume wa huko aliyekuwa akimtolea ombi kwa bidii na kusema: “Vuka . . . utusaidie.” Wakiwa na imani pamoja na kujitia katika hali za wanadamu wenzao, Paulo na Sila walitii kwa nia ya kupenda, wakafunga safari kwa merikebu kutoka Troa.—Matendo 16:6-10.
Walipokwisha kufika Neapoli, Paulo na wenzake walitembelea Filipi kwanza. Kutoka huko wakasonga mbele kando-kando ya ile njia kuu ya Waroma, Via Egnatia, kupitia Amfipoli na Apolonia na kufika Thesalonike, hiyo ikiwa ni jumla ya kilometa 121. (Matendo 16:11, 12; 17:1) Katika Thesalonike Paulo aliyatumia makusanyiko ya Wayahudi ya kushika siku ya Sabato wakiwa katika sinagogi la huko akahubiri “habari njema.” Kwa sababu hiyo, “wengine” wa Wayahudi, pamoja na ‘Wayunani wengi sana,’ wakawa waamini.—Matendo 17:2-4.
Kwa kuona wivu juu ya mafanikio ya Paulo, Wayahudi wasioamini walijiunga wakawa kundi lenye ghasia na kuleta fujo katika mji wa Thesalonike, basi akina ndugu wakatuma Paulo na Sila wasonge mbele mpaka Beroya. Ujumbe wa Ufalme wa Mungu wenye kupita kwa Yesu Kristo ulikuwa umekuwa jiwe la kukwaza Wayahudi. Hata walitokeza shtaka juu ya Paulo na Sila na wale Wathesalonike waliojishirikisha nao, wakisema: “Hawa wote wanatenda mambo yaliyo kinyume cha amri za Kaisari, wakisema [ya] kwamba yupo mfalme mwingine, aitwaye Yesu.”—Matendo 17:5-10.
Hangaiko la Paulo kwa Wakristo Wathesalonike
Alipofika Korintho, Paulo alimwagiza Timotheo mfanya kazi mwenzake kijana alirudie kundi la huko Thesalonike lililokuwa limeanzishwa majuzi. Timotheo alipomrudia Paulo, alimpokeza habari nzuri za kwamba wale Wakristo waliokuwa wamebatizwa majuzi walikuwa imara katika imani na wakawa wakizidi kukua, ijapokuwa mateso yaliendelea kuwako. Wao walikuwa wamekuwa wafuataji wa mifano ya Wakristo wengine waaminifu katika kuvumilia dhiki. (1 Wathesalonike 2:14-16; 3:6, 7) Paulo alitaka sana kuwajulisha Wathesalonike namna alivyojisikia kuwaelekea na akataka kuwapa kitia-moyo na mashauri zaidi. Kwa hiyo akaliandikia kundi barua mbili. Inaelekea kuwa kwamba hizo ndizo zilizokuwa barua za kwanza za Paulo zinazokubalika kuwa kati ya maandiko matakatifu. Ziliandikwa katika miaka ya 50 na 51 W.K. Zinaeleza vizuri sana mambo yanayohusika katika Ukristo wa kweli.
Lakini, je! ripoti ya Luka katika Matendo 17:11, 12 haiwataji Wathesalonike hao kwa kuwapa sifa mbaya, kwa kusema hawakulipokea lile neno kwa bidii ya moyoni kama Waberoya? Hapana, kwa maana hapo Luka hawataji Wakristo, bali anawataja Wayahudi. Ingawa matokeo ya mahubiri ya Paulo na Sila yalikuwa machache sana kati ya Wayahudi, “wengi” walioenda kwenye sinagogi la Wayahudi katika Beroya wakawa waamini.
Wale waliokuwa wamegeuzwa huko Thesalonike wakawa Wakristo muda mchache tu uliopita walijifunza Neno la Mungu na wakalifuata sana. Paulo anawasifu katika barua yake ya kwanza kwa kusema walikuwa wamefuata mfano wake na wa Bwana kwa ‘kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya roho takatifu.’ (1 Wathesalonike 1:6) Walikuwa wamezikubali “habari njema” kuwa “neno la Mungu,” na sasa lilikuwa ‘likifanya kazi,’ yaani, likizaa matunda, katika waamini hao. (1 Wathesalonike 2:3-5, 13, NW) Kwa njia yo yote hawakuwa Wakristo wa kujifanya tu.
Paulo mwenyewe alikuwa mfuasi wa mfano wa Kristo mwenye bidii. Ingawa ziara yake ya kwanza huko Thesalonike huenda ikawa ilikuwa fupi sana, washiriki wa kundi la huko waliachiwa naye mfano wa kujinyima ukabaki ukiwa umekazika kikiki katika akili zao. Walikuwa wameacha kuabudu sanamu “ili kumtumikia Mungu aliye hai,” halafu wao pia wakawa mfano wa imani kwa waamini wote wa huko Makedonia na Akaya. (1 Wathesalonike 1:7, 9) Kati yao walikuwako waangalizi waliokuwa ‘wakijitaabisha’ kutunza mahitaji ya kundi, na ndivyo inavyopasa kuwa katika makundi yote ya Wakristo wa kweli.—1 Wathesalonike 5:12; 1 Petro 5:2, 3.
Ndiyo, Paulo na wenzi wake walikuwa wametoa vyote vilivyokuwa vyao kwa faida ya Wathesalonike, wakafanya kazi usiku na mchana, wakijulisha watu ile kweli pasipo woga na kulisha kundi kwa huruma pole “kama wakati mama mlezi anapotunza sana watoto wake mwenyewe.” (1 Wathesalonike 2:3-11, NW; 2 Wathesalonike 3:7, 8) Walikuwa na kusudi gani akilini? Ni kusudi la kwamba ndugu hao waliokuwa wapya katika imani waweze ‘kuenenda kama ilivyo wajibu wao kwa Mungu’ na ‘mtu ye yote asifadhaishwe na dhiki.’ Paulo alitaka kuwachochea ‘wakeshe’ kiroho, “kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema.” Aliwataka ‘wavumilie kwa ajili ya Kristo,’ ili wakati wo wote ‘wasikate tamaa katika kutenda mema.’—1 Wathesalonike 2:12;3:3;5:6; 2 Wathesalonike 2:17; 3:5, 13.
Hangaiko kubwa sana la Paulo la kutaka kuona Wathesalonike wakiwa na hali nzuri limetiwa katika maandishi ili kututia moyo sisi leo, tupate kuendelea kutembea pamoja na Mungu tukiwa tunampendeza. (Amosi 3:3) Mtu anayejiita Mkristo akifanya jambo jingine lo lote linalotofautiana na hilo angekuwa Mkristo ovyo, wa kujifanya tu.—1 Wathesalonike 4:1.
Hatari Kutokea Ndani!
Wayahudi wasioamini walikuwa wameleta mateso juu ya kundi changa hilo kutokea nje, lakini sasa hatari kubwa zaidi ilikuwa ikielekea kutokea humo ndani! Inaonekana wengine kundini walikuwa wakieneza maoni yaliyopotoka ya kwamba siku ya Yehova ilikuwa ikikaribia sana. Paulo alifanya haraka akanyosha mambo, akisema hivi juu ya “siku” hiyo: “Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu.”—2 Wathesalonike 2:1-3.
Wakati Paulo alipolionya kundi katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike juu ya kuja kwa huyo “mtu wa kuasi,” maelezo marefu ya mwendo wa mwasi huyo yalikuwa yangali “siri,” au siri ya kidini. Lakini, mtume anataja kwamba hata alipokuwa angali nao ‘alikuwa akiwaambia’ habari za ukengeufu (uasi-imani) huo ambao ungetokea baadaye na za ‘kizuizi’ kilichokuwa kikiuzuia.—2 Wathesalonike 2:5-7.
Kufikia hapo, tukifungua Biblia zetu kwenye 2 Wathesalonike 2:3-12 na kuchunguza habari zinazoyatangulia na kuyafuata maneno ya Paulo, hata sisi tunaweza kufahamu jambo ambalo lilikuwa akilini mwa Paulo. “Ukengeufu” ambao ungetokea ungeletwa na ukosefu wa “kuipenda ile kweli.” Ungetokana na ‘kuuamini uongo’ na ‘kujifurahisha katika udhalimu.’ Ungetokeza kwa ujasiri uonekane waziwazi mara tu baada ya kile ‘kizuizi’ kilichotajwa na Paulo kuondolewa. Ungeendelea kuwako moja kwa moja mpaka wakati wa ‘kudhihirishwa kwa ufunuo wa kuwapo’ kwa Yesu Kristo. Wakati huo Kristo atamfunua wazi na kumharibu huyo “asi,” aumalize kabisa ukengeufu huo.—Linganisha 2 Wathesalonike 2:8 pamoja na Isaya 11:4 na Ufunuo 19:11, 14, 15.
Kumtambua “Mtu wa Kuasi”
Ilikuwa ni lazima huyo “mtu wa kuasi” awe ni jamii ya watu wala si mtu mmoja tu, kwa sababu urefu wa maisha ya mtu huyo ulianza siku za Paulo na kuendelea mpaka kuwapo kwa Kristo. Kwa kuwa asi huyo ‘anajiinua nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa,’ matumizi ya neno hilo yanaelekeza fikira kwenye viongozi wa ukengeufu (uasi-imani) huo. Wao wangekuwa ndio wenye kufanya “ajabu” kwa jina la Kristo. (Linganisha 2 Wathesalonike 2:9 pamoja na Mathayo 7:22, 23.) Umati wa watu ungejiunga nao wafuate hiyo njia rahisi zaidi ya kidini, njia yenye kuburudisha dhamiri lakini isiyowekea watu mzigo wo wote wa kuepuka njia ya maisha ya kichoyo, ya kilimwengu na hata ya ufisadi. Watu hao wenye Ukristo wa bandia walikuwa ‘wakitenda kazi kati ya wenye kujiita Wakristo katika siku za Paulo.—1 Wathesalonike 4:3-8, 5:6-9, 14, 15, 19-22; 2 Wathesalonike 3:6-15 linganisha Mathayo 25:41-46.
Paulo na mitume wengine na wanaume wazee wa kundi la Kikristo walikuwa ndio ‘kizuizi’ cha kupinga nguvu hizo zenye msukumo, wakalichunga kundi kulingana na mfano uliowekwa na Kristo. Kwa sababu ya hatari iliyoelekea kuwako ya uasi-imani, Paulo aliwaonya Wathesalonike kwa upole akawaambia hivi: “Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa.” Baada ya Paulo na mitume wale wengine kufa, watu wenye kujitafutia faida zao wenyewe waliisukuma kweli kando, wakajisimamisha wawe viongozi na kulipoteza kundi. Ni wale tu walioitikia mashauri ya Paulo walio fanywa “imara katika kila neno na tendo jema.” Yule “mtu wa kuasi” akatambulishwa kuwa ni viongozi wa kidini wa Ukristo wa bandia tu.—2 Wathesalonike 2:15-17; linganisha Mathayo 13:24-30, 37-43.a
Kungojea Siku ya Yehova
Ilimlazimu Paulo kuonya Wakristo Wathesalonike juu ya hatari nyingine bado: Ile ya kuwa na kinaya (kutosheka kabisa) au ya kusinzia kiroho kuhusu siku ya Yehova. Waandikaji wengine wa kidini wa wakati wetu wamejaribu kupuza umaana na uharaka wa ujumbe wa Maandiko unaohusu ‘kuwapo kwa Yesu na wa umalizio wa mfumo wa mambo’ wakitumia maneno ambayo Paulo alitaja baada ya hapo: “Msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka . . . kana kwamba siku ya [Yehova] imekwisha kuwapo.”—Mathayo 24:3, NW; 2 Wathesalonike 2:1, 2.
Sasa, je! kweli inaweza kuwa Paulo alitaka Wakristo wenye mioyo myeupe wasijali sana habari za kuwapo kwa Bwana wao na za siku ya Yehova? Badala ya hivyo, aliwataka waendeleze usawaziko katika jambo hilo, ‘waendelee kuwa na fahamu zao’ kwa ‘kuhakikisha mambo yote.’ Kwa kufanya hivyo, ujumbe wa namna mbalimbali usio na msingi wa kwamba siku ya Yehova ilikuwa karibu haungewakosesha usawaziko wala hawangekaa bila kujitayarisha, wakiwa wazembe na bila kuijali.—1 Wathesalonike 5:8, 21, NW; linganisha 2 Petro 3:3, 10-12 na 1 Yohana 4:1.
Hapa inatupasa tukumbuke kwamba Wathesalonike hao walijua sana kwamba siku ya Yehova ingekuja “kama vile mwivi ajavyo usiku.” Hiyo haikuwa kamwe sababu ya kukaa bila kujali, bali ya ‘kukesha,’ wakiwa kama watu waliowekewa ‘wokovu, si hasira.’ Uasi imani ukiisha kuonekana wazi kabisa, siku ya Yehova ingekuja. Ingekuja katika wakati ambao wale wenye kupinga Ufalme wa Yehova—kutia ndani yule “mtu wa kuasi” pasipo shaka—wangekuwa wakisema: “Kuna amani na salama”! Hicho kingekuwa kiishara cha kwamba watapatwa na uharibifu wa ghafula, wa papo kwa hapo. (1 Wathesalonike 5:1-11) Katika siku hiyo ya kufikilizwa kwa hukumu ya uadilifu, wenye furaha watakuwa ni wale ‘wanaomjua Mungu na wale wanaotii habari njema juu ya Bwana Yesu’!—2 Wathesalonike 1:8, NWb
Ni Wafuasi wa Mfano au Ni wa Kujifanya tu
Barua za Paulo zilizoonyesha hangaiko la upendo kwa kundi la Kikristo la huko Thesalonike zinapanga mambo ambayo wafuasi wa kweli wa Kristo Yesu lazima watimize leo, na yale ambayo ni lazima wayaamini na kuyatenda. Lakini namna gani juu ya watu na vikundi vinavyodai kwamba ni vya Kikristo lakini havifuati mfano wa Kristo, wala wa Paulo wala wa Wathesalonike waaminifu? Watu hao wanaonekana wazi kuwa ni Wakristo wa kujifanya tu! (2 Wathesalonike 3:6, 7; 2 Petro 2:1-3) Paulo anakazia kwamba ni wale tu ‘wanaotii habari njema’ watakaohesabiwa kuwa ‘wanastahili kuuingia ufalme wa Mungu.’ Yesu alisema maneno yanayofanana na hayo juu ya “kondoo” waadilifu watakaorithi makao ya Ufalme hapa duniani.—2 Wathesalonike 1:4-10; linganisha Mathayo 7:21 na 25:31-34.
Habari njema, zilizojulishwa na Paulo katika barua alizoandikia Wathesalonike, zinapasa kutuchochea tujibidiishe katika utumishi wa Mungu, tufuate viwango bora vya adili katika maisha ya Kikristo, ndiyo, tuwe na uvumilivu katika kuishi maisha yenye kujawa na furaha na kujawa na sala, maisha ya kuthamini, ya kuwa na roho ya kujikaza sana, maisha yasiyo na lawama yatakayotupendekeza kwa wengine ndani na nje ya kundi la watu wa Yehova. (1 Wathesalonike 5:16-23) Unaombwa ufikirie kwa moyo mweupe mfano uliowekwa na Paulo na barua alizoandika na hata ile imani ya Wakristo wa Thesalonike, kisha kufikiri kwako na kukufaidi wewe ufuate mfano wa Kristo ‘kwa kuzidi sana.’ Nako kufanya hivyo kukuletee ukombozi usipatwe na “ghadhabu itakayokuja,” kisha upate wokovu wa kuwa na uzima wa milele chini ya utawala mtukufu wa Ufalme wa Mungu.—1 Wathesalonike 1:10; 4:1; Waebrania 12:2, 3; Ufunuo 21:1, 3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate mazungumzo marefu juu ya “mtu wa kuasi,” ona kichapo chetu kinachoitwa God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, kurasa 364-397.
b Habari zaidi juu ya matukio yanayoelekeza kwenye ‘siku ya Yehova’ zinaweza kupatikana katika Mnara wa Mlinzi wa Juni 15, 1982, kurasa 10-22.
[Picha katika ukurasa wa 14]
Paulo anaandika habari za kutokea kwa “mtu wa kuasi” ambaye ni viongozi wa kidini