Mwe Tayari kwa Ajili ya Siku ya Yehova!
Mambo Makuu Kutokana na Wathesalonike wa Kwanza
SIKU ya Yehova! Wakristo katika Thesalonike la kale waliifikiria kuwa karibu. Je! walifikiri vizuri? Ingekuja lini? Hilo lilikuwa jambo moja muhimu lililoshughulikiwa katika barua ya kwanza ya mtume Paulo kwa Wathesalonike, iliyopelekwa kutoka Korintho katika karibu mwaka 50 wa Wakati wa Kawaida wetu.
Paulo na Sila walianzisha kundi katika Thesalonike, kiti cha usimamizi cha jimbo la Kiroma la Makedonia. (Matendo 17:1-4) Baadaye, katika barua yake ya kwanza kwa Wathesalonike, Paulo alitoa pongezi, akaandaa onyo la upole, na kuzungumzia siku ya Yehova. Sisi pia twaweza kunufaika kutokana na barua hii, hasa kwa kuwa siku ya Yehova sasa i karibu sana.
Pongeza na Kutia Moyo
Paulo aliwapongeza Wathesalonike kwanza. (1:1-10, NW) Pongezi ilikuwa kwa sababu ya kazi yao ya uaminifu na uvumilivu. Lilikuwa jambo la kupongezeka, pia, kwamba ‘walilipokea lile neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu.’ Je! wewe hupongeza wengine, kama Paulo alivyofanya?
Mtume alikuwa ameweka kielelezo kizuri. (2:1-12) Ijapokuwa kutendwa ufidhuli katika Filipi, yeye alikuwa ‘amethubutu katika Mungu kuinena Injili ya Mungu kwa’ Wathesalonike. Alikuwa ameepuka urairai, choyo, na kutafuta utukufu. Paulo hakuwa amekuwa mzigo wa gharama nyingi bali alikuwa mwanana kwao kama vile mama mlezi alivyo kwa mtoto wake. Ni mfano mzuri kama nini kwa wazee leo!
Maneno ya Paulo yafuatayo yaliwatia moyo Wathesalonike wabaki imara wanyanyaswapo. (2:13–3:13) Walikuwa wamevumilia mnyanyaso kutoka kwa wananchi wenzao, na Timotheo alikuwa amemletea Paulo ripoti njema juu ya hali yao ya kiroho. Mtume alisali kwamba wawe na wingi wa upendo na kwamba mioyo yao iimarishwe. Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova sasa husali kwa ajili ya waamini wenzao, huwatia moyo ikiwezekana, na hushangilia katika ripoti za uaminifu wao.
Baki Ukiwa Macho Kiroho!
Ndipo Wathesalonike wakapokea shauri. (4:1-18) Walipaswa kutembea kwa ukamili zaidi katika mwendo unaopendeza Mungu, wakionyesha upendo mwingi zaidi wa kidugu na kufanya kazi kwa mikono yao ili kutimiza mahitaji yao. Zaidi ya hilo, walipaswa kufarijiana kwa tumaini la kwamba kwenye kuwapo kwa Yesu waamini waliozaliwa kwa roho ambao walikuwa wamekufa wangeinuliwa kwanza na kuunganishwa naye. Baadaye, wakati ambapo wapakwa mafuta waliobaki hai wangekufa na kufufuliwa wangejiunga na Kristo na wale waliokwisha kufufuliwa kwenye uhai wa kimbingu.
Halafu Paulo alizungumzia siku ya Yehova na kutoa shauri zaidi. (5:1-28) Siku ya Yehova ingekuja kama mwivi, kukiwa na hakika ya kutokea uharibifu wa ghafula baada ya ule mpaazo wa sauti: “Kuna amani na salama”! Hivyo basi Wathesalonike walipaswa kubaki macho kiroho, wamelindwa na bamba la chuma la kifuani lililo la imani na upendo na kulindwa na tumaini la wokovu likiwa kofia ya chuma. Walipaswa kuwa na heshima ya kina kirefu kwa wale wanaosimamia katika kundi na walipaswa kushika mwiko wa uovu, kama vile ilivyo lazima kwetu.
Barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakristo yapasa kutuharakisha tutoe pongezi na kitia-moyo kwa waamini wenzetu. Pia yapasa kutusukuma tuwe mfano mwema katika mwenendo na mtazamo. Na kwa uhakika shauri layo laweza kutusaidia tuwe tayari kwa ajili ya siku ya Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Bamba la Kifuani na Kofia ya Chuma: Akihimiza kuwa macho kiroho, Paulo aliandika hivi: “Tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani imani na upendo, na chapeo [helmeti, NW] yetu iwe tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Bamba la kifua lilikuwa kinga ya kifua ya shujaa mwenye silaha, likiwa na magamba, minyororo, au chuma kigumu. Vivyo hivyo, bamba la kifua la imani hutulinda kiroho. Namna gani ile kofia ya chuma ya kale? Mara nyingi ikiwa imefanyizwa kwa chuma, ilikuwa kifunika-kichwa cha kijeshi kilichoundwa kwa njia ya kulinda mpiganaji wakati wa pigano. Kama vile kofia ya kichwa ilivyolinda kichwa cha mwana-vita, ndivyo tumaini la wokovu linavyolinda nguvu za kiakili, hivyo likiwezesha Mkristo kudumisha ukamilifu. Ni jambo muhimu kama nini kwamba watu wa Yehova wavae silaha hizo za kiroho!—Waefeso 6:11-17.