Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ufisadi—Umeenea Kwa Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 1
    • Ufisadi—Umeenea Kwa Kadiri Gani?

      “Kampuni yetu inatoa huduma kwa mamlaka ya mji fulani. Mara nyingi tunasuburi kwa miezi miwili au mitatu ili kupata malipo ya huduma tunazotoa. Hata hivyo, hivi karibuni nilipigiwa simu na mmoja wa wafanyakazi wa mamlaka hiyo. Alitaka kunisaidia kupata malipo yetu bila kuchelewa ikiwa ningekubali kumpa kiasi fulani cha pesa kama rushwa.”—JOHN.a

      JE, UMEWAHI kuathiriwa na ufisadi? Labda si ufisadi kama uliotajwa hapo juu, lakini bila shaka ulipatwa na matokeo mabaya ya ufisadi.

      Kulingana na Orodha ya 2011 ya Makadirio ya Ufisadi,b iliyotolewa na shirika la Transparency International (TI), ‘Nyingi kati ya nchi 183 zilizoorodheshwa zilikuwa na kiwango cha ufisadi kisichozidi 5. Kulingana na makadirio hayo, kiwango cha 0 kiliwakilisha nchi zenye ufisadi mwingi na kiwango cha 10 kiliwakilisha nchi zisizo na ufisadi.’ Miaka miwili mapema, shirika la TI lilitaja katika ripoti yake ya kila mwaka ya 2009 kuwa ufisadi umeenea sana liliposema: “Ni wazi kwamba hakuna sehemu yoyote ulimwenguni ambayo haijaathiriwa na ufisadi.”

      “Ufisadi ni matumizi mabaya ya mamlaka ili kupata faida za kibinafsi. Ufisadi huathiri kila mtu ambaye maisha yake, riziki yake au furaha yake inategemea unyoofu wa watu wenye mamlaka.”​—SHIRIKA LA TRANSPARENCY INTERNATIONAL

      Katika hali fulani, matokeo ya ufisadi yanaweza kuwa mabaya sana. Kwa mfano, gazeti Time lilisema kwamba “ufisadi na kutojali” ndiyo mambo yaliyosababisha kwa kiasi fulani vifo vya watu wengi baada ya tetemeko kubwa la ardhi lililoikumba nchi ya Haiti mwaka wa 2010. Liliendelea kusema: “Majengo hujengwa kwa usaidizi mdogo au bila usaidizi wa wahandisi, na wale wanaoitwa wakaguzi wa serikali hupokea rushwa kwa wingi.”

      Je, inawezekana kukomesha kabisa ufisadi? Ili tupate jibu, tunahitaji kuelewa mambo ya msingi yanayosababisha ufisadi. Tutachunguza mambo hayo katika makala inayofuata.

      a Jina limebadilishwa.

      b “Orodha ya Makadirio ya Ufisadi hupanga nchi kulingana na kiwango cha ufisadi kinachodhaniwa katika idara za umma.”—Transparency International.

  • Kwa Nini Ufisadi Unazidi Kuongezeka?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 1
    • Kwa Nini Ufisadi Unazidi Kuongezeka?

      “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—MHUBIRI 8:9.

      MANENO ya andiko hilo yanaonyesha kikamili historia ya utawala wa wanadamu. Utawala huo umesababisha kuteseka na huzuni nyingi. Kwa muda mrefu, jitihada za watu wenye nia nzuri ambao wamejaribu kutokeza jamii iliyo na haki, sikuzote zimezuiwa na tamaa na ufisadi. Kwa nini hali iko hivyo? Kwa nini ufisadi unazidi kuongezeka? Kwa ujumla, ni kwa sababu ya mambo matatu yafuatayo ambayo husababisha uvutano usiofaa.

      1. Uvutano wa dhambi.

      Biblia inataja waziwazi kwamba ‘sote tuko chini ya dhambi.’ (Waroma 3:9) Kama tu ugonjwa wa kurithiwa usioweza kutibiwa, dhambi ‘inakaa’ ndani yetu. Kwa maelfu ya miaka, dhambi ‘imewatawala’ wanadamu kama mfalme. “Sheria” yake imeendelea kufanya kazi ndani yetu. Mwelekeo wa kutenda dhambi umewafanya watu wengi watangulize mapendezi yao au kutafuta mali na mamlaka huku wakiwaumiza watu wengine.—Waroma 5:21; 7:17, 20, 23, 25.

      2. Uvutano wa ulimwengu mwovu tunamoishi.

      Ulimwengu wetu umejaa pupa na ubinafsi. Watu wengi wanaona kuwa ni vigumu kujiendesha kwa njia tofauti na watu wanaowazunguka. Wakisukumwa na ubinafsi wanakuwa wenye njaa ya kutaka mamlaka. Pia, wanakuza tamaa ya kupata pesa na mali kwa wingi hata kuliko wanavyohitaji. Jambo la kusikitisha ni kwamba wako tayari kujihusisha na ukosefu wa haki ili watimize malengo yao. Badala ya kukataa uvutano usiofaa, watu kama hao “[wanafuata] umati kwa ajili ya makusudio maovu.”​—Kutoka 23:2.

      3. Uvutano wa Shetani Ibilisi.

      Shetani, kiumbe mwasi wa kiroho, ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Anafurahia kuwapotosha wanadamu. Kwa ujanja anaweza kumshawishi mtu atumie vibaya tamaa ya asili ya kutaka kuwa na vitu vya kimwili na pesa na hata kumfanya atende kwa udanganyifu.

      Je, hilo linamaanisha sisi ni kama vikaragosi ambavyo vinaongozwa na Shetani, yaani, tunapaswa kutii kila jambo analotuamuru? Tutapata jibu katika makala inayofuata.

  • Je, Inawezekana Kuwa Mnyoofu Katika Ulimwengu Wenye Ufisadi?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 1
    • Je, Inawezekana Kuwa Mnyoofu Katika Ulimwengu Wenye Ufisadi?

      “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—WAEBRANIA 13:18.

      INGAWA tunasukumwa na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, ulimwengu tunamoishi, na Ibilisi, bado tunaweza kushinda uvutano huo wote! Jinsi gani? Kwa kumkaribia Mungu na kufuata kanuni za Neno lake, Biblia, ambazo kwa muda mrefu zimethibitika kuwa zenye faida. Fikiria mifano miwili.

      KANUNI YA BIBLIA: “Msiige tabia ya ulimwengu huu.”​—Waroma 12:2, New Jerusalem Bible.

      Jambo lililoonwa: Guilherme ni mfanyabiashara mwenye mafanikio nchini Brazili. Anakubali kwamba si rahisi kuwa mnyoofu. Anasema hivi: “Ni rahisi kwa mfanyabiashara kuanza kukosa unyoofu, labda kwa sababu ya mkazo wa kutaka kutimiza malengo ya kampuni au ili afaulu katika ulimwengu wenye ushindani mkali. Watu wengi wanaona kuwa jambo la kawaida kutoa na kupokea hongo. Ni vigumu kuwa mnyoofu ukiwa mwekezaji aliye na majukumu mengi ya kifedha.”

      Hata hivyo, Guilherme amefaulu kuendelea kuwa mnyoofu ingawa anakabili mkazo wa kukosa unyoofu. Anasema: “Hata unapofanya biashara ambayo watu huona ni sawa kuvunja sheria, inawezekana kuwa mnyoofu. Lazima uwe na viwango thabiti vya maadili. Biblia imenisaidia kutambua faida za kuwa mnyoofu. Mtu mnyoofu ana dhamiri safi, ana utulivu wa moyoni, na anajiheshimu. Anaweza kuwachochea watu wengine wamwige.”

      KANUNI YA BIBLIA: “Watu wanaotamani kuwa na mali kwa haraka haraka huanguka kwenye majaribu na wamenaswa na tamaa nyingi za kipumbavu, zenye kudhuru zinazowazamisha watu katika uharibifu na maangamizi. Kwa maana kupenda fedha ndiyo shina moja la maovu ya kila namna.”—1 Timotheo 6:9, 10, Neno Biblia Takatifu.

      Jambo lililoonwa: André ana kampuni ya kuweka mifumo ya usalama. Kati ya watu anaowahudumia ni klabu fulani kubwa ya mpira wa miguu. Wakati fulani, baada ya shindano kubwa, André alienda kwenye ofisi ya usimamizi na kupeleka karatasi ya kudai malipo ya kazi aliyokuwa amefanya. Wafanyakazi katika idara ya fedha bado walikuwa na kazi nyingi ya kuhesabu pesa walizopokea kutokana na tiketi zilizouzwa. Kwa sababu usiku ulikuwa unaingia, msimamizi wa idara hiyo aliwalipa haraka haraka watu waliotoa huduma mbalimbali, kutia ndani André.

      “Nilipokuwa njiani nikienda nyumbani, niligundua kwamba yule msimamizi alikuwa amenilipa pesa nyingi zaidi,” anaeleza André. “Nilijua kwamba huenda hangejua ni nani aliyepokea pesa hizo. Lakini nilijua pia mtu huyo angelazimika kulipa pesa hizo zilizopotea! Hivyo niliamua kurudi. Nilifaulu kupita katikati ya mashabiki wengi na nikarudisha pesa hizo. Yule msimamizi alishangazwa sana na tendo hilo. Hakuna mtu aliyewahi kumrudishia pesa.”

      “Tendo hilo la unyoofu lilifanya msimamizi huyo aniheshimu,” André anaendelea kusema. “Miaka mingi imepita, na kati ya watu wengi waliokuwa wakitoa huduma mbalimbali katika klabu hiyo, mimi tu ndiye niliyebaki. Ninafurahi kwamba kwa kutumia kanuni za juu za Biblia nimejulikana kuwa na sifa nzuri.”

      Inatia moyo kujua kwamba kupitia msaada wa Mungu tunaweza kushinda mkazo wa kujihusisha na ufisadi. Hata hivyo, tukiwa mtu mmoja-mmoja hatuwezi kumaliza ufisadi kabisa. Mambo yanayosababisha ufisadi ni magumu sana hivi kwamba wanadamu hawawezi kuyaondoa wenyewe. Je, hilo linamaanisha kwamba ufisadi hautakwisha kamwe? Makala ya mwisho katika mfululizo huu inaonyesha jibu la Biblia lenye kutia moyo.

  • Ufisadi Utakwisha!
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Oktoba 1
    • Ufisadi Utakwisha!

      “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake . . . Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”​—ZABURI 37:34.

      JE, WEWE pia, kama watu wengine, unahisi kwamba ufisadi hauwezi kuepukika na kwamba hautawahi kuondolewa kabisa? Inaeleweka ikiwa unahisi hivyo. Katika historia yote, wanadamu wamejaribu mifumo mbalimbali ya serikali. Lakini hawajafaulu kamwe kuondoa ufisadi kabisa. Je, tunaweza kutumaini kwamba kuna wakati ambapo watu wote watashirikiana kwa unyoofu?

      Jambo la kufurahisha ni kwamba Biblia inajibu ndiyo! Inasema kuwa hivi karibuni Mungu atachukua hatua na kuondoa ufisadi wote katika dunia yetu. Atafanyaje hivyo? Kupitia Ufalme wake ambao ni serikali ya mbinguni ataibadilisha dunia yetu kabisa. Huo ndio Ufalme ambao Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali uje. Katika ile sala ambayo inajulikana kama Sala ya Bwana au Baba Yetu, Yesu alisema hivi: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani.”​—Mathayo 6:10, Union Version.

      Kuhusu Mtawala wa Ufalme huo, Yesu Kristo, Biblia ilitabiri hivi: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.” (Zaburi 72:12-14) Ona kwamba Yesu anaelewa hali ya watu wanaoathiriwa na ufisadi, na atachukua hatua ya kuondoa ukandamizaji! Jambo hilo ni lenye kufariji kwelikweli!

      Chini ya utawala wa Mfalme huyo mwenye huruma na nguvu, Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa ufisadi duniani. Jinsi gani? Kwa kuondoa mambo matatu yanayosababisha ufisadi.

      Uvutano wa Dhambi

      Wakati huu, sote tunalazimika kushindana na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, ambao unatuchochea tutende kwa ubinafsi. (Waroma 7:21-23) Hata hivyo, bado kuna watu wazuri wanaotaka kutenda mema. Wanaonyesha imani katika thamani ya damu ya fidia ya Yesu iliyomwagwa, na hivyo wanasamehewa dhambi zao.a (1 Yohana 1:7, 9) Watu kama hao watapata fursa ya kufaidika kutokana na tendo kubwa zaidi la upendo wa Mungu, kama tunavyosoma katika Yohana 3:16: “Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”

      Mungu atawafanyia watu waaminifu jambo fulani lenye kustaajabisha. Katika ulimwengu mpya unaokuja, mwishowe ataondoa dhambi zote, hatua kwa hatua atawarudishia wanadamu waaminifu ukamilifu na msimamo wa uadilifu. (Isaya 26:9; 2 Petro 3:13) Kamwe uvutano wa dhambi hautamchochea tena mtu yeyote atende kwa ufisadi. Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, wanadamu waaminifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu au ufisadi.’—Waroma 8:20-22.

      Uvutano wa Ulimwengu Mwovu Tunamoishi

      Inasikitisha kwamba leo watu wengi wanawanyanyasa wenzao kimakusudi. Wanawatendea isivyo haki watu wa hali ya chini na maskini, na wanawachochea wengine watende kwa ufisadi. Biblia inawahimiza hivi watu kama hao: “Mtu mwovu aiache njia yake, na mtu mwenye madhara ayaache mawazo yake.” Watu hao wafisadi wakitubu, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atasamehe kwa njia kubwa.”​—Isaya 55:7.

      Hata hivyo, Mungu atalazimika kuwaondoa watu wanaokataa kishupavu kubadili mwenendo wao. Kupitia Ufalme wa Mungu, ahadi hii ya Biblia itatimia: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake . . . Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”b (Zaburi 37:34) Watu waovu wasiotaka kubadilika watakapoondolewa, waabudu waaminifu wa Mungu hawataathiriwa tena na ufisadi.

      Uvutano wa Shetani Ibilisi

      Shetani ndiye mtenda dhambi sugu zaidi kati ya watenda dhambi wasiotaka kubadilika. Jambo la kupendeza ni kwamba hivi karibuni Yehova atamzuia Shetani asiwachochee wanadamu. Mwishowe, Yehova atamharibu Shetani kabisa. Jitu hilo katili halitaweza tena kuwachochea watu watende kwa ufisadi.

      Huenda wazo la kwamba Mungu ataondoa kabisa ufisadi likaonekana kuwa ndoto. Huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli Mungu ana uwezo wa kuleta mabadiliko kama hayo? Ikiwa ndivyo, mbona hajachukua hatua?’ Hayo ni maswali mazuri, na Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha.c Tunakutia moyo uchunguze mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao ulio karibu, wakati ambapo ufisadi wote utakuwa umeondolewa.

      a Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi kifo cha Yesu kinavyoweza kutukomboa, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Yehova ni jina la Mungu kama inavyoonyeshwa katika Biblia.

      c Kwa habari zaidi ona, sura ya 3, 8, na 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki