-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Zaidi ya hayo, wenzi wa ndoa kutoka nchi nyingine za Ulaya ambao walikuwa wamejifunza lugha ya eneo hilo walialikwa watumikie Kroatia.
Wenzi fulani wa ndoa, Heinz na Elke Polach, kutoka Austria, walikuwa mapainia wa pekee huko Denmark katika eneo lenye watu wa Yugoslavia, walipoalikwa kutumika Kroatia mwaka wa 1991. Vita vilianza walipokuwa tu wanaanza kazi ya kutembelea makutaniko. Mzunguko wao wa kwanza ulitia ndani maeneo ya pwani ya Dalmatia na sehemu fulani za Bosnia, na maeneo yote hayo yalikumbwa na vita. Heinz alisema hivi: “Ilikuwa vigumu kutembelea Bosnia wakati wa vita. Kwa sababu ya hatari, hatungeweza kutumia gari letu la kibinafsi, kwa hiyo ilitubidi tutumie mabasi ambayo hayakutegemeka. Hatungeweza kubeba vitu vingi, tulibeba mifuko michache na taipureta tu.
“Tulihitaji kutumia akili ili tufanikiwe. Wakati fulani, tulipokuwa tukisafiri kati ya Tuzla na Zenica, wanajeshi walisimamisha basi letu. Walituambia ni hatari sana kuendelea na safari. Ilimbidi kila mtu katika basi ashuke. Lakini tulijua kwamba ndugu zetu huko Zenica wanatusubiri, kwa hiyo tulianza kuwaomba watu wengine watupeleke huko. Mwishowe, msafara wa malori ya mafuta yaliyokuwa na kibali yalikubali kutubeba. Tulipokuwa njiani tulimhubiria dereva, akatusikiliza sana.
“Kwa mara nyingine, tulilazimika kusimama njiani kwa sababu ya vita, na ilitubidi tutumie barabara za kandokando. Barabara hizo zilikuwa mbovu, na theluji ilifanya safari iwe ngumu hata zaidi. Tulisimama mara nyingi ili kusukuma malori mengine yaliyokwama. Katika eneo fulani, tulishambuliwa na ilibidi tukimbie. Tulifika Vareš, kilomita 50 hivi kutoka mahali tulipokuwa tukienda, tukasimamisha safari yetu hapo usiku huo.
“Dereva alilala kwenye viti, nami na Elke tukalala tukiwa tumejikunja nyuma ya kiti cha dereva tukijaribu kupata joto. Ni kana kwamba muda ulijikokota sana usiku huo! Hata hivyo, siku iliyofuata, tulipofika mwishowe Zenica, ndugu walifurahi sana kutuona! Safari yetu haikuwa ya bure! Ingawa hawakuwa na maji ya bomba wala umeme, walijitahidi wawezavyo kututendea kwa ukarimu. Ingawa walikuwa maskini kimwili, walikuwa tajiri kiroho nao walionyesha kwamba wanaipenda sana kweli.”
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 215]
Elke na Heinz Polach
-