-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUMCHAGUA AMA TOLSTOY AU YEHOVA
Vita vya ulimwengu vilipokuwa karibu kuanza, mgawanyiko ulitokea katika moja ya makutaniko makubwa zaidi katika Yugoslavia. Watu fulani kutanikoni walikuwa wameanza kueneza maoni ya Leo Tolstoy, mwandikaji Mrusi na mwanafalsafa wa dini. Tolstoy, ambaye zamani alikuwa mshiriki wa Kanisa Othodoksi la Urusi, alisadiki kwamba makanisa yote ya Kikristo yalikuwa yamepotoka na yalikuwa yameharibu kabisa sifa ya Ukristo. Ndugu fulani walifuata maoni hayo ya kutoamini dini zote na hawakutosheka na tengenezo la Yehova. Ndugu aliyekuwa akiongoza Kutaniko la Zagreb alitumia vibaya madaraka yake kuwashawishi wahubiri wengi wakubali maoni ya Tolstoy. Ndugu huyo alikuwa na uvutano mkubwa sana hivi kwamba watu wengi kutanikoni, zaidi ya watu 60, walipitisha azimio la kuacha tengenezo la Yehova.
Rudolf Kalle aliposikia hivyo, alisafiri haraka kutoka Belgrade mpaka Zagreb ili kukutana na kutaniko lote. Alizungumzia kweli za msingi za Biblia ambazo Yehova alikuwa amefunua kupitia jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. (Mt. 24:45-47) Kisha akauliza: “Ni nani aliyewafundisha kweli hizo? Ni Tolstoy au ni tengenezo la Yehova?” Rudolf alinukuu Yoshua 24:15, akawaomba wale waliotaka kubaki ndani ya tengenezo la Yehova wainue mikono yao. Ni wawili tu walioinua mikono.
Rudolf anasema, “Lilikuwa jambo lenye kutia uchungu sana.”
Ilionekana kana kwamba mambo yote mazuri yaliyotimizwa katika kutaniko hilo yalikuwa karibu kupotea.
Halafu Rudolf akawaita wale wawili waliokuwa waaminifu waje kwenye jukwaa, kisha akasema: “Tumebaki watatu tu. Sisi ndio tunaowakilisha watu wa Yehova katika jiji hili. Ninawaomba wengine wote waondoke kwenye jumba hili na kwenda zao. Tafadhali, tuacheni peke yetu! Tunataka kumtumikia Mungu wetu, Yehova, nanyi mnaweza kwenda kumtumikia Tolstoy wenu. Hatutaki kushirikiana nanyi tena.”
Kwa sekunde chache, kukawa na kimya kabisa. Kisha, mtu mmoja baada ya mwingine akaanza kuinua mkono wake na kusema: “Mimi pia ninataka kumtumikia Yehova.” Mwishowe, ni yule mtumishi wa kutaniko aliyeasi imani na wafuasi wake wachache tu ndio waliotoka na kwenda. Jaribu hilo la ushikamanifu liliwatia nguvu watumishi waaminifu wa Yehova na kuwatayarisha kwa ajili ya majaribu makali zaidi ambayo wangekabili baada ya muda mfupi.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ofisi ya Belgrade ilifungwa, na kazi ya kuwagawia akina ndugu chakula cha kiroho ilipangiwa Zagreb, Kroatia. Walihitaji kuwa wenye busara zaidi na kufanya mambo kwa siri zaidi kwa sababu badala ya kutozwa faini na kufungwa gerezani walipelekwa katika kambi za mateso na kuhukumiwa kifo.
Majeshi ya Ujerumani yalipoteka na kuigawanya Yugoslavia, kambi za mateso zilijengwa. Huko Kroatia, kambi hizo zilitumiwa kuwatenga na kuwaua watu wa makabila fulani madogo, na watu wachache wasio Wakatoliki, vilevile wafuasi wa dini yoyote ambao walipinga serikali.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Stevan Stanković, mfanyakazi wa reli, kutoka Serbia, alikuwa tayari kuwasaidia akina ndugu bila kujali malezi yao. Bila kujali hatari, Stevan alikubali kazi ya kupeleka vitabu kwa siri kutoka Kroatia mpaka nchi ya Serbia iliyokuwa chini ya ulinzi wa wanajeshi. Siku moja polisi waligundua vitabu katika sanduku alilobeba. Walitaka kujua vitabu hivyo vilitoka wapi. Hata hivyo, Stevan alikuwa mshikamanifu kwa ndugu zake, akakataa kuwapa habari hiyo. Polisi walimtia gerezani ili wamhoji halafu wakampeleka kwenye kambi ya mateso ya Jasenovac iliyo karibu. Ndugu yetu mwaminifu aliuawa katika kambi hiyo ambayo ilijulikana sana kwa sababu ya ukatili.
Mihovil Balković, ndugu mwenye busara na mwenye ubunifu, alikuwa fundi wa mabomba huko Kroatia katika nyakati hizo zenye taabu. Zaidi ya kufanya kazi yake, aliwatembelea akina ndugu ili kuwatia moyo na kuwapelekea vitabu. Mjukuu wake anasema hivi: “Pindi moja, alipata habari kwamba gari-moshi ambalo alikuwa amepanda lingekaguliwa katika mji unaofuata. Kwa hiyo, badala ya kushuka katika kituo alichotaka, alishuka katika kituo kilichotangulia. Mji wote ulizingirwa na seng’enge lakini alipata kijia katika shamba la mizabibu. Alibeba vitabu katika mfuko wake wa mgongoni, akaweka chupa mbili za pombe ya kienyeji (rakija) katika sehemu ya juu ya mfuko pamoja na mboga chache. Alipokuwa akitembea polepole katika shamba hilo la mizabibu, alipita handaki moja na kwa ghafula mwanajeshi mmoja akasema kwa sauti kubwa: ‘Simama! Wewe ni nani?’ Alipokaribia, mwanajeshi mmoja alimuuliza, ‘Umebeba nini?’
“‘Unga kidogo, maharagwe, na viazi vichache,’ akajibu.
“Alipoulizwa chupa alizobeba zilikuwa na nini, alisema, ‘Nusa na hata unaweza kuonja.’
“Mwanajeshi huyo alipoonja, Mihovil alisema, ‘Hii ni chupa yako, mwanangu, na iliyobaki ni yangu.’
“Kwa kuwa wanajeshi hao walitosheka na jibu lake na pombe ya rakija, wakasema, ‘Mzee, unaweza kwenda!’
Mjukuu wa Mihovil anamalizia hivi: “Kwa hiyo, vitabu vilifika bila tatizo.”
Bila shaka, Mihovil alikuwa jasiri. Alisafiri katika maeneo yaliyomilikiwa na wanajeshi wa pande mbili zilizopigana. Nyakati nyingine, Mihovil alikutana uso kwa uso na wanajeshi waliounga mkono Ukomunisti; na nyakati nyingine, alikutana na wanajeshi Wafashisti wa Ustašea au wanajeshi waasi wa Četnik. Badala ya kuogopa, alitumia nafasi hizo kutoa ushahidi na kuwaeleza kuhusu tumaini la wakati ujao ambalo linazungumziwa katika Biblia. Alihitaji ujasiri mkubwa sana kwa sababu sikuzote Mashahidi walikabili hatari ya kuuawa. Alikamatwa mara nyingi, akahojiwa, na kufungwa gerezani.
Vita vilipokaribia kwisha, usiku wa Novemba 9, 1944, wanajeshi Wakomunisti walivamia nyumba ya Mihovil, wakachukua vitabu, na kumkamata Mihovil. Inasikitisha kwamba Mihovil hakurudi tena. Baadaye iliripotiwa kwamba alikatwa kichwa.
Josip Sabo alikuwa mvulana tu alipokuwa akipeleka vitabu katika eneo la Slavonia huko Kroatia kwa baiskeli yake. Katika sehemu ya mizigo ya baiskeli yake, aliweka sanduku la kubebea vitabu, na alifunika vitabu kwa matunda ya pea. Wakati huo, kulikuwa na vizuizi na walinzi katika barabara za kuingia katika karibu kila kijiji.
Katika kila kizuizi wanajeshi walimuuliza hivi Josip: “Umebeba nini ndani ya sanduku hilo?”
“Nimebeba matunda ya pea ya mjomba wangu,” alijibu, na wanajeshi hao walichukua tunda moja au mawili. Alipokaribia mwisho wa safari, hakukuwa na matunda ya kutosha kufunika vitabu. Kwa hiyo, Josip alifuata njia isiyotumiwa ili matunda yaliyobaki yasichukuliwe na aweze kulinda vitabu vyenye thamani vilivyofichwa chini yake.
ALIKUWA MWAMINIFU MPAKA MWISHO
Lestan Fabijan, mjenzi wa nyumba kutoka Zagreb, aliwafundisha kweli Ivan Sever, Franjo Dreven, na Filip Huzek-Gumbazir. Wote walibatizwa katika muda wa miezi sita wakaanza kuhubiri na kufanya mikutano. Jioni ya Januari 15, 1943, wanajeshi waliokuwa wakilinda doria walifika kwenye nyumba ya Ivan Sever na kumkamata pamoja na Franjo Dreven na ndugu mwingine, Filip Ilić. Walipekua nyumba yake wakachukua vitabu vyote, na kuwakamata ndugu hao.
Lestan alipata habari kwamba walikuwa wamekamatwa, kwa hiyo akaenda pamoja na Filip Huzek-Gumbazir kumfariji mama na dada ya Franjo. Hata hivyo, wanajeshi Wakomunisti walisikia kuhusu ziara yao, wakawakamata Lestan na Filip. Ndugu hao watano walieleza wakitumia Biblia kwamba walimtumikia Yehova peke yake na kwamba wao ni askari-jeshi wa Kristo. Walihukumiwa kifo kwa sababu wote walikataa kuchukua silaha na kupigana katika vita. Basi, walishikwa mateka.
Usiku mmoja ndugu hao watano waliamshwa usingizini, wakavuliwa nguo zote, na kupelekwa msituni. Walipokuwa wakitembea, walipewa nafasi ya kubadili maoni yao. Wanajeshi walijaribu kuvunja azimio la ndugu hao kwa kuwashawishi wakitumia upendo wao kwa familia zao. Walizungumza kuhusu mke mjamzito wa Filip Huzek-Gumbazir na watoto wake wanne. Aliwajibu kwamba alikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova angewatunza. Franjo Dreven hakuwa na mke wala watoto, kwa hiyo, walimuuliza ni nani ambaye angemtunza mama yake na dada yake.
Walipofika, wanajeshi hao waliwaagiza ndugu hao wasimame katika baridi kali sana. Kisha wakaanza kuwaua. Kwanza, walimpiga risasi Filip Huzek-Gumbazir. Halafu wanajeshi walingoja na kuwauliza wale wengine ikiwa walitaka kubadili msimamo wao. Hata hivyo, ndugu hao walikuwa wameazimia kubaki thabiti. Kwa hiyo, wanajeshi hao walimuua Franjo, halafu Ivan, kisha Lestan. Mwishowe, Filip Ilić, aliyekuwa amebaki, alilegeza msimamo wake akakubali kujiunga na hao wanajeshi. Hata hivyo, miezi mitatu baadaye, alirudi nyumbani akiwa mgonjwa na kusimulia yaliyotendeka. Alijaribu kuokoa uhai wake kwa kulegeza msimamo wake lakini akafa ghafula kwa sababu ya ugonjwa.
-