Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa Mwisho
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • Sura Ya Kumi Na Saba

      Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa Mwisho

      1. Kulingana na Danieli sura ya 7, ni mambo gani yasiyo ya kawaida ambayo yangepata kikundi kidogo cha watu wasio na ulinzi leo?

      KIKUNDI kidogo cha watu wasio na ulinzi washambuliwa vikali na serikali ya ulimwengu yenye nguvu. Wasalimika na hata kuanza upya—si kwa sababu ya nguvu zao wenyewe lakini kwa sababu Yehova Mungu awathamini sana. Kitabu cha Danieli sura ya 7 kilitabiri matukio hayo, yaliyotokea mapema katika karne ya 20. Hata hivyo, watu hao walikuwa nani? Sura hiyohiyo ya Danieli iliwarejezea kuwa “watakatifu wake Aliye juu,” Yehova Mungu. Pia ilifunua kwamba watu hao hatimaye wangekuwa watawala wenzi katika Ufalme wa Kimesiya!—Danieli 7:13, 14, 18, 21, 22, 25-27.

      2. (a) Yehova huhisije juu ya watumishi wake watiwa-mafuta? (b) Lingekuwa jambo la hekima kufuata mwendo gani nyakati hizi?

      2 Kama tulivyojifunza kwenye Danieli sura ya 11, mfalme wa kaskazini atafikia kikomo chake baada ya kutisha makazi salama ya kiroho ya watu hao waaminifu. (Danieli 11:45; linganisha Ezekieli 38:18-23.) Naam, Yehova huwalinda sana waaminifu wake. Zaburi 105:14, 15 hutuambia hivi: “Hata wafalme [Yehova] aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, wala msiwadhuru nabii zangu.” Basi je, usingekubali kwamba katika nyakati hizi zenye misukosuko, lingekuwa jambo la hekima “umati mkubwa” unaoongezeka ushirikiane kwa ukaribu iwezekanavyo na watakatifu hao? (Ufunuo 7:9; Zekaria 8:23) Yesu Kristo alipendekeza kwamba watu walio mfano wa kondoo wafanye hivyohivyo—washirikiane na ndugu wa kiroho waliotiwa mafuta kwa kutegemeza kazi yao.—Mathayo 25:31-46; Wagalatia 3:29.

      3. (a) Kwa nini si rahisi kuwapata wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu na kushirikiana nao kwa ukaribu? (b) Danieli sura ya 12 itasaidiaje katika habari hii?

      3 Hata hivyo, Mpinzani wa Mungu, Shetani, amekuwa akipigana vita ya kufa na kupona dhidi ya watiwa-mafuta. Ameendeleza dini isiyo ya kweli, akipata mafanikio katika kujaza Wakristo bandia duniani. Kwa sababu hiyo, watu wamepotoshwa. Wengine wanakata tamaa wakiona kwamba hawatawatambua watu wanaowakilisha dini ya kweli. (Mathayo 7:15, 21-23; Ufunuo 12:9, 17) Hata wale ambao hupata “kundi dogo” na kushirikiana nalo lazima wajitahidi kwelikweli kudumisha imani, kwa kuwa ulimwengu huu hujitahidi kuidhoofisha imani daima. (Luka 12:32) Namna gani wewe? Je, umewapata “watakatifu wa Aliye juu,” na kushirikiana nao? Je, unajua kwamba kuna uthibitisho thabiti wa kwamba wale ambao umepata kwa kweli ndio wateule wa Mungu? Uthibitisho huo waweza kuimarisha imani yako. Pia waweza kukuwezesha kuwasaidia wengine waone waziwazi vurugu ya kidini ya ulimwengu wa leo. Danieli sura ya 12 ina habari nyingi zenye kuokoa uhai.

      JEMADARI MKUU ACHUKUA HATUA

      4. (a) Danieli 12:1 hutabiri mambo gani mawili tofauti juu ya Mikaeli? (b) Katika Danieli, yamaanisha nini mfalme ‘asimamapo’?

      4 Danieli 12:1 husema hivi: “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako.” Mstari huo watabiri mambo hayo mawili tofauti juu ya Mikaeli: kwanza, kwamba ‘anasimama,’ kuonyesha hali ya mambo inayochukua kipindi cha wakati; pili, kwamba “atasimama,” kuonyesha tukio katika kipindi hicho cha wakati. Kwanza, twataka kujua wakati ambapo Mikaeli ‘anasimama upande wa wana wa watu wa Danieli.’ Kumbuka kwamba akiwa Mtawala mbinguni, Yesu huitwa Mikaeli. Kurejezea ‘kusimama’ kwake kwatukumbusha jinsi neno hilo lilivyotumiwa kwingineko katika kitabu cha Danieli. Mara nyingi neno hilo hurejezea tendo la mfalme, kama vile kutwaa mamlaka ya kifalme.—Danieli 11:2-4, 7, 20, 21.

      5, 6. (a) Mikaeli asimama katika kipindi gani cha wakati? (b) Mikaeli “atasimama” lini na jinsi gani, na matokeo yatakuwa nini?

      5 Yaonekana kwamba malaika huyo alikuwa akirejezea kipindi cha wakati kinachotajwa kwingineko katika unabii wa Biblia. Yesu alikiita “kuwapo” kwake (Kigiriki, pa·rou·siʹa), wakati ambapo angetawala akiwa Mfalme mbinguni. (Mathayo 24:37-39) Kipindi hicho cha wakati pia huitwa “siku za mwisho” na “wakati wa mwisho.” (2 Timotheo 3:1; Danieli 12:4, 9) Tangu kipindi hicho kianze mwaka wa 1914, Mikaeli amekuwa akisimama akiwa Mfalme mbinguni.—Linganisha Isaya 11:10; Ufunuo 12:7-9.

      6 Ingawa hivyo, Mikaeli “atasimama” lini? Ainukapo kuchukua hatua muhimu. Yesu atafanya hivyo wakati ujao. Ufunuo 19:11-16 humfafanua Yesu kiunabii kuwa Mfalme wa Kimesiya mwenye nguvu akiongoza jeshi la malaika na kuangamiza adui za Mungu. Andiko la Danieli 12:1 laendelea kusema hivi: “Na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” Akiwa Mfishaji Mkuu wa Yehova, Kristo atakomesha mfumo wote mwovu wa mambo wakati wa ile “dhiki kubwa” iliyotabiriwa.—Mathayo 24:21; Yeremia 25:33; 2 Wathesalonike 1:6-8; Ufunuo 7:14; 16:14, 16.

      7. (a) Kuna tumaini gani kwa waaminifu wote “wakati [ujao] wa taabu”? (b) Kitabu cha Yehova ni nini, na kwa nini ni muhimu kuandikwa humo?

      7 Watu wanaodhihirisha imani watakuwa na hali gani nyakati hizo ngumu? Danieli akaendelea kuambiwa hivi: “Wakati huo watu wako wataokolewa; kila mmoja atakayeonekana ameandikwa katika kitabu kile.” (Linganisha Luka 21:34-36.) Kitabu hicho ni nini? Chawakilisha hasa kumbukumbu la Yehova Mungu la wale wanaofanya mapenzi yake. (Malaki 3:16; Waebrania 6:10) Wale ambao wameandikwa katika kitabu hicho cha uhai ndio watu salama zaidi ulimwenguni, kwa kuwa wanalindwa na Mungu. Dhara lolote liwapatalo, laweza kutanguliwa nalo litatanguliwa. Hata ikiwa watakufa kabla ya “wakati [ujao] wa taabu,” wangali salama kwenye kumbukumbu kubwa la Yehova. Atawakumbuka na kuwafufua wakati wa ule Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo.—Matendo 24:15; Ufunuo 20:4-6.

      WAAMINIFU ‘WAAMKA’

      8. Danieli 12:2 hutoa taraja gani lenye kupendeza?

      8 Tumaini la ufufuo ni lenye kufariji kwelikweli. Andiko la Danieli 12:2 hulizungumzia, lisemapo: “Wengi wa hao walalao katika mavumbi ya nchi wataamka, wengine wapate uzima wa milele, wengine aibu na kudharauliwa milele.” (Linganisha Isaya 26:19.) Huenda maneno hayo yakatukumbusha juu ya ahadi ya Yesu Kristo yenye kuchochea hisia juu ya ufufuo wa watu. (Yohana 5:28, 29) Ni tumaini lenye kusisimua kama nini! Hebu fikiria familia na marafiki wapendwa—ambao kwa sasa wamekufa—wakipewa fursa ya kuishi tena wakati ujao! Lakini kitabu hiki cha Danieli charejezea aina nyingine ya ufufuo—ufufuo ambao tayari umetukia. Yawezekanaje?

      9. (a) Kwa nini ni jambo lenye kupatana na akili kutarajia andiko la Danieli 12:2 litimizwe katika siku za mwisho? (b) Unabii huo warejezea ufufuo wa aina gani, nasi twajuaje hivyo?

      9 Ufikirie muktadha. Kama vile tumeona, mstari wa kwanza wa sura ya 12 wahusu mwisho wa mfumo huu wa mambo na pia kipindi chote cha siku za mwisho. Kwa hakika, sehemu kubwa ya sura hiyo yatimizwa katika wakati wa mwisho, wala si kwenye paradiso ya kidunia ijayo. Je, kumekuwa ufufuo wowote katika kipindi hiki? Mtume Paulo aliandika juu ya ufufuo wa “wale walio wa Kristo” kuwa watukia “wakati wa kuwapo kwake.” Hata hivyo, wanaofufuliwa wakaishi mbinguni wanafufuliwa “wakiwa wasioharibika.” (1 Wakorintho 15:23, 52) Hakuna yeyote kati yao anayefufuliwa ‘apate aibu na kudharauliwa milele’ kama ilivyotabiriwa kwenye Danieli 12:2. Je, kuna ufufuo wa aina nyingine? Katika Biblia, nyakati nyingine ufufuo una maana ya kiroho. Kwa kielelezo, kitabu cha Ezekieli na cha Ufunuo vina visehemu vya unabii vinavyohusu uhuisho, au ufufuo wa kiroho.—Ezekieli 37:1-14; Ufunuo 11:3, 7, 11.

      10. (a) Mabaki ya watiwa-mafuta walifufuliwaje katika wakati wa mwisho? (b) Hata hivyo, baadhi ya watiwa-mafuta waliofufuliwa waliamka wapate “aibu na kudharauliwa milele” jinsi gani?

      10 Je, watumishi wa Mungu wamefufuliwa kiroho kwa njia hiyo katika wakati wa mwisho? Ndiyo! Ni jambo halisi katika historia kwamba mwaka wa 1918 mabaki wachache wa Wakristo waaminifu walishambuliwa isivyo kawaida na hilo lilivuruga utaratibu wa huduma yao ya hadharani. Kisha, ingawa lilionekana kuwa jambo lisilowezekana, mwaka wa 1919 wakafufuliwa kiroho. Mambo hayo ya hakika yapatana na ufafanuzi wa ufufuo uliotabiriwa kwenye Danieli 12:2. Baadhi yao ‘waliamka’ kiroho wakati huo na baadaye. Ingawa hivyo, kwa kusikitisha si wote walioendelea kuwa hai kiroho. Wale ambao baada ya kuamshwa walimkataa Mfalme wa Kimesiya na ambao waliacha utumishi wa Mungu walijiletea “aibu na kudharauliwa milele” kama ifafanuliwavyo kwenye Danieli 12:2. (Waebrania 6:4-6) Hata hivyo, watiwa-mafuta waaminifu, wanaotumia vizuri hali yao baada ya kufufuliwa kiroho, walimtegemeza Mfalme wa Kimesiya kwa uaminifu-mshikamanifu. Kama vile unabii unavyotaarifu, uaminifu wao hatimaye huongoza kwenye “uzima wa milele.” Leo, nguvu zao katika utendaji wa kiroho wajapokabili upinzani hutusaidia kuwatambua.

      ‘WANG’AA KAMA NYOTA’

      11. Ni nani “walio na hekima” leo, nao wanang’aaje kama nyota?

      11 Mistari miwili inayofuata ya Danieli sura ya 12 yatusaidia kuwatambua vizuri zaidi “watakatifu wake Aliye juu.” Katika mstari wa 3 malaika amwambia Danieli hivi: “Walio na hekima watang’aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang’aa kama nyota milele na milele.” Ni nani “walio na hekima” leo? Uthibitisho wawaashiria walewale “watakatifu wa Aliye juu.” Kwani, ni nani isipokuwa mabaki watiwa-mafuta walio waaminifu waliokuwa na ufahamu wenye kina wa kutambua kwamba Mikaeli, Jemadari Mkuu, alianza kusimama akiwa Mfalme mwaka wa 1914? Kwa kuhubiri kweli za aina hiyo—na pia kwa kudumisha mwenendo wa Kikristo—wamekuwa ‘waking’aa wakiwa wamulikaji’ katika ulimwengu huu wenye giza kiroho. (Wafilipi 2:15; Yohana 8:12) Yesu alitabiri hivi juu yao: “Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua katika ufalme wa Baba yao.”—Mathayo 13:43.

      12. (a) Katika wakati wa mwisho, watiwa-mafuta wamehusikaje katika ‘kuongoza wengi watende haki’? (b) Watiwa-mafuta watawaongozaje wengi watende haki na ‘kung’aa kama nyota’ wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo?

      12 Hata andiko la Danieli 12:3 latuambia kazi ambayo Wakristo hao watiwa-mafuta wangekuwa wakifanya katika wakati wa mwisho. ‘Wangewaongoza wengi kutenda haki.’ Mabaki watiwa-mafuta walianza kukusanya waliosalia wa 144,000 walio warithi-washirika pamoja na Kristo. (Waroma 8:16, 17; Ufunuo 7:3, 4) Kazi hiyo ilipomalizika—yamkini miaka ya katikati ya 1930—walianza kukusanya “umati mkubwa” wa “kondoo wengine.” (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Wao pia hudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Kwa hiyo, wana msimamo safi mbele za Yehova. Wakijumlika kuwa mamilioni leo, wanathamini sana tumaini la kuokoka uharibifu ujao wa ulimwengu huu mwovu. Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, Yesu na wafalme na makuhani wenzake 144,000 watatumia manufaa kamili ya fidia kwa wanadamu watiifu duniani, na kwa hiyo, watawasaidia wote wanaodhihirisha imani kuondolea mbali dhambi zote zilizorithiwa kutoka kwa Adamu. (2 Petro 3:13; Ufunuo 7:13, 14; 20:5, 6) Katika maana kamili, wakati huo watiwa-mafuta watashiriki ‘kuongoza wengi kutenda haki’ nao “watang’aa kama nyota” mbinguni. Je, unathamini sana tumaini la kuishi duniani chini ya serikali tukufu ya kimbingu ya Kristo na watawala wenzake? Ni pendeleo lililoje kushiriki pamoja na “watakatifu” katika kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu!—Mathayo 24:14.

      ‘WAENDA MBIO HUKO NA HUKO’

      13. Ni katika maana gani maneno ya kitabu cha Danieli yalitiwa muhuri na kuwekwa yakiwa siri?

      13 Habari ambazo malaika amjulisha Danieli, kuanzia Danieli 10:20, sasa zamalizikia kwa maneno haya yenye kutia moyo: “Wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa [“ujuzi,” NW] yataongezeka.” (Danieli 12:4) Kwa kweli, mengi ya mambo ambayo Danieli alipuliziwa kuandika yaliwekwa yakiwa siri na kutiwa muhuri yasieleweke na watu. Kwani, Danieli mwenyewe aliandika hivi baadaye: “Nami nikasikia, lakini sikuelewa.” (Danieli 12:8) Katika maana hiyo, kitabu cha Danieli kilidumu kikiwa kimetiwa muhuri kwa karne nyingi. Vipi leo?

      14. (a) “Wakati wa mwisho,” ni nani ‘wameenda mbio huko na huko,’ nao wamekuwa wakienda wapi? (b) Kuna uthibitisho gani wa kwamba Yehova amebariki ‘huko kwenda mbio huko na huko’?

      14 Tuna pendeleo la kuishi katika “wakati wa mwisho” uliotabiriwa kwenye kitabu cha Danieli. Kama ilivyotabiriwa, waaminifu wengi ‘wameenda huko na huko’ katika kurasa za Neno la Mungu. Kumekuwa na matokeo gani? Ujuzi wa kweli umeongezeka, kwa sababu ya baraka za Yehova. Mashahidi watiwa-mafuta wa Yehova walio waaminifu wamebarikiwa na ufahamu wenye kina unaowawezesha kuelewa kwamba Mwana wa binadamu alikuwa Mfalme mwaka wa 1914, kuwatambua wanyama wa unabii wa Danieli, kuonya dhidi ya “chukizo la uharibifu”—na mengine mengi. (Danieli 11:31) Basi, ongezeko la ujuzi ni alama nyingine ya kuwatambulisha “watakatifu wa Aliye juu.” Lakini Danieli alipata uthibitisho zaidi.

      ‘WAVUNJWA’

      15. Malaika azusha swali gani sasa, na huenda swali hilo likatukumbusha juu ya nani?

      15 Twakumbuka kwamba Danieli alipata ujumbe mbalimbali kutoka kwa malaika kwenye ufuo wa “ule mto mkubwa” Hidekeli, pia uitwao Tigris. (Danieli 10:4) Hapa sasa aona malaika watatu na kusema: “Mimi, Danieli, nikatazama, na kumbe, wamesimama wengine wawili, mmoja ukingoni mwa mto upande huu, na mmoja ukingoni mwa mto upande wa pili. Na mmoja akamwuliza yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji ya mto, Je! itakuwa muda wa miaka mingapi hata mwisho wa mambo haya ya ajabu?” (Danieli 12:5, 6) Swali ambalo malaika huyo alizusha hapa laweza kutukumbusha tena juu ya “watakatifu wa Aliye juu.” Mwanzoni mwa “wakati wa mwisho,” mwaka wa 1914, walitaka sana kujua ingechukua muda gani kabla ya ahadi za Mungu kutimizwa. Jibu la swali lao laonyesha kwamba wao ni sehemu kubwa ya unabii huo.

      16. Malaika atoa unabii gani, naye anakaziaje uhakika wa kutimia kwake?

      16 Simulizi la Danieli laendelea kusema hivi: “Nami nikamsikia yule mtu aliyevikwa nguo za kitani, aliyekuwa juu ya maji ya mto, hapo alipoinua mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto kuelekea mbinguni; akaapa kwa yeye aliye hai milele na milele, ya kwamba itakuwa wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati; tena watakapokuwa wamekwisha kuvunja nguvu za hao watu watakatifu, ndipo mambo hayo yote yatakapotimizwa.” (Danieli 12:7) Hilo ni jambo zito. Malaika ainua mikono yote miwili akiapa, huenda ili tendo hilo lionekane na wale malaika wawili walio pande tofauti za mto huo mpana. Kwa hiyo, anakazia uhakika kamili wa kutimizwa kwa unabii huo. Hata hivyo, nyakati hizo ni lini? Jibu si gumu kama vile ambavyo huenda ukadhani.

      17. (a) Unabii mbalimbali uliorekodiwa katika Danieli 7:25, Danieli 12:7, na Ufunuo 11:3, 7, 9 walinganaje? (b) Zile nyakati tatu na nusu zina urefu gani?

      17 Unabii huo wafanana sana na nyingine mbili. Unabii mmoja, tuliouchunguza kwenye Sura ya 9 ya kichapo hiki, wapatikana kwenye Danieli 7:25; nao ule mwingine, kwenye Ufunuo 11:3, 7, 9. Ona mambo kadhaa yanayofanana. Kila mmoja ni wa wakati wa mwisho. Wote wahusu watumishi watakatifu wa Mungu, ukiwatambulisha kuwa wamenyanyaswa na hata kwa muda kuwa hawawezi kutekeleza utendaji wao wa kuhubiri hadharani. Kila unabii waonyesha kwamba watumishi wa Mungu wanafufuliwa na kuendelea na kazi yao, wakiwashinda wanyanyasaji wao. Kila unabii wataja kipindi cha wakati huu wa magumu kwa watakatifu. Unabii wote katika Danieli (7:25 na 12:7) warejezea “wakati, na nyakati mbili, na nusu wakati.” Kwa kawaida wasomi huziona hizo kuwa nyakati tatu na nusu. Ufunuo hurejezea kipindi hichohicho kuwa miezi 42, au siku 1,260. (Ufunuo 11:2, 3) Hilo lathibitisha kwamba nyakati tatu na nusu katika Danieli zarejezea miaka mitatu na nusu kila mwaka ukiwa na siku 360. Lakini siku hizo 1,260 zilianza lini?

      18. (a) Kulingana na Danieli 12:7, ni nini ambacho kingeonyesha mwisho wa zile siku 1,260? (b) ‘Nguvu za watakatifu zilivunjwa’ lini hatimaye, na hilo lilitukiaje? (c) Zile siku 1,260 zilianza lini, nao watiwa-mafuta ‘walitoaje unabii wakiwa wamevaa nguo ya gunia’ katika kipindi hicho?

      18 Unabii huo u dhahiri kabisa juu ya wakati ambapo zile siku 1,260 zingeisha—‘nguvu za watakatifu zitakapokuwa zimekwisha kuvunjwa.’ Katikati ya mwaka wa 1918, washiriki wakuu wa Watch Tower Bible and Tract Society, kutia ndani msimamizi wake, J. F. Rutherford, walishtakiwa kwa mashtaka yasiyo ya kweli, wakahukumiwa vifungo virefu na kufungwa gerezani. Kwa kweli watakatifu wa Mungu waliona kazi yao ‘ikivunjwa,’ nguvu zao zikivunjwa. Kuhesabu miaka mitatu na nusu kurudi nyuma kuanzia katikati ya mwaka wa 1918 huturudisha hadi mwisho wa mwaka wa 1914. Wakati huo kile kikundi kidogo cha watiwa-mafuta kilikuwa kikijitayarisha kwa ajili ya mnyanyaso ambao ungezuka. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa imezuka, nao upinzani dhidi ya kazi yao ulikuwa ukiongezeka. Mwaka wa 1915, hata andiko lao la mwaka lilitegemea swali ambalo Kristo aliwauliza wafuasi wake: “Je, mwaweza kukinywa kikombe ambacho mimi niko karibu kunywa?” (Mathayo 20:22) Kama ilivyotabiriwa kwenye Ufunuo 11:3, kile kipindi cha siku 1,260 kilichofuata kilikuwa wakati wa kuomboleza kwa watiwa-mafuta—ilikuwa kana kwamba walikuwa wakitoa unabii wakiwa wamevaa nguo za gunia. Mnyanyaso ukaongezeka. Baadhi yao wakatiwa gerezani, wengine wakapigwa na vikundi vya wafanya-ghasia, na bado wengine wakateswa. Wengi walivunjwa moyo na kifo cha msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, C. T. Russell, mwaka wa 1916. Hata hivyo, ni nini kingetukia baada ya kipindi hicho chenye giza kumalizika kwa kuuawa kwa watakatifu hao wakiwa tengenezo la kuhubiri?

      19. Unabii katika Ufunuo sura ya 11 watuhakikishiaje kwamba watiwa-mafuta hawataendelea kunyamaza kwa muda mrefu?

      19 Unabii sawa na huo upatikanao kwenye Ufunuo 11:3, 9, 11 huonyesha kwamba baada ya wale “mashahidi wawili” kuuawa, wanaendelea kuwa wafu kwa kipindi kifupi cha wakati—siku tatu na nusu—hadi wanapofufuliwa. Vivyo hivyo, unabii wa Danieli sura ya 12 waonyesha kwamba watakatifu hawangeendelea kunyamaza bali kwamba walikuwa na kazi nyingi zaidi ya kufanya.

      ‘WATAKASWA, WAFANYWA WEUPE, NA KUSAFISHWA’

      20. Kulingana na Danieli 12:10, watiwa-mafuta wangepata baraka zipi baada ya kupatwa na magumu?

      20 Kama tulivyoona awali, Danieli aliandika mambo hayo lakini hakuweza kuyaelewa. Hata hivyo, lazima awe alitaka kujua ikiwa watakatifu kwa hakika wangeharibiwa na wanyanyasaji, kwa kuwa aliuliza, “Mwisho wa mambo haya utakuwaje?” Malaika huyo alijibu hivi: “Enenda zako, Danieli; maana maneno haya yamefungwa, na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho. Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima ndio watakaoelewa.” (Danieli 12:8-10) Watakatifu walikuwa na tumaini hakika! Badala ya kuharibiwa, wangefanywa kuwa weupe, na kubarikiwa kuwa na msimamo safi mbele za Yehova Mungu. (Malaki 3:1-3) Ufahamu wao wenye kina wa mambo ya kiroho ungewawezesha kudumisha usafi machoni pa Mungu. Tofauti nao, waovu wangekataa kuelewa mambo ya kiroho. Lakini yote hayo yangetukia lini?

      21. (a) Kile kipindi cha wakati kilichotabiriwa katika Danieli 12:11 kingeanza wakati ambapo hali gani zingetokea? (b) Ile “sadaka ya kuteketezwa daima” ilikuwa nini, nayo iliondolewa lini? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 298.)

      21 Danieli aliambiwa hivi: “Tangu wakati ule ambapo sadaka ya kuteketezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapata siku elfu na mia mbili na tisini.” Kwa hiyo, kipindi hicho cha wakati kingeanza wakati ambapo hali fulani zingekuwa zimetokezwa. “Sadaka ya kuteketezwa ya daima”a ilikuwa imeondolewa. (Danieli 12:11) Malaika huyo alimaanisha dhabihu gani? Si dhabihu ya wanyama iliyotolewa kwenye hekalu lolote la kidunia. Kwani, hata hekalu ambalo wakati mmoja lilikuwa Yerusalemu lilikuwa “nakala ya uhalisi”—hekalu kuu la kiroho la Yehova, lililoanza kutumika wakati Kristo alipopata kuwa Kuhani wa Cheo cha Juu wa hekalu hilo mwaka wa 29 W.K.! Katika hekalu hilo la kiroho, lenye kuwakilisha mpango wa Mungu wa ibada safi, hakuna uhitaji wa matoleo yenye kuendelea ya dhambi, kwa kuwa ‘Kristo alitolewa mara moja kwa wakati wote ili kuchukua dhambi za wengi.” (Waebrania 9:24-28) Hata hivyo, Wakristo wote wa kweli hutoa dhabihu kwenye hekalu hilo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia [Kristo] acheni sikuzote tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.” (Waebrania 13:15) Kwa hiyo, hali hiyo ya kwanza ya unabii huo—kule kuondolewa kwa “sadaka ya kuteketezwa daima”—ilitimizwa katikati ya mwaka wa 1918 wakati ambapo kazi ya kuhubiri ilionekana kana kwamba ilikuwa imekomeshwa kwa muda.

      22. (a) “Chukizo” la uharibifu ni nini, nalo lilisimamishwa lini? (b) Kile kipindi kilichotabiriwa katika Danieli 12:11 kilianza lini, na kiliisha lini?

      22 Hata hivyo, vipi juu ya hali ya pili—‘kusimamishwa,’ au kuwekwa kwa “chukizo la uharibifu”? Kama tulivyoona tulipozungumzia Danieli 11:31, chukizo hilo mwanzoni lilikuwa Ushirika wa Mataifa na kisha likatokea tena likiwa Umoja wa Mataifa. Mashirika yote mawili yanachukiza kwa kuwa yatangazwa kuwa tumaini pekee la amani duniani. Kwa hiyo, mioyoni mwa watu wengi, mashirika hayo kwa hakika yametwaa mahali pa Ufalme wa Mungu! Ushirika wa Mataifa ulipendekezwa rasmi Januari 1919. Basi, wakati huo hali zote mbili za Danieli 12:11 zilitimizwa. Kwa hiyo, zile siku 1,290 zilianza mapema mwaka wa 1919 na kuendelea hadi vuli (kwenye Kizio cha Kaskazini) ya mwaka wa 1922.

      23. Watakatifu wa Mungu walielekeaje kupata msimamo safi wakati wa zile siku 1,290 zilizotabiriwa katika Danieli sura ya 12?

      23 Wakati huo, je, watakatifu walifanya maendeleo kuelekea kufanywa weupe na kutakaswa machoni pa Mungu? Bila shaka! Machi 1919 msimamizi wa Watch Tower Society na washiriki wake wa karibu walifunguliwa kutoka gerezani. Baadaye wakaondolewa mashtaka yote ambayo hayakuwa ya kweli. Wakijua kwamba bado walikuwa na kazi nyingi, mara moja wakaanza shughuli, wakipanga mkusanyiko wa Septemba 1919. Mwaka huohuo, gazeti-jenzi la The Watch Tower likachapishwa kwa mara ya kwanza. Mwanzoni likiitwa The Golden Age (sasa laitwa Amkeni!), sikuzote limetegemeza Mnara wa Mlinzi katika kufichua bila woga ufisadi wa ulimwengu huu na katika kusaidia watu wa Mungu wadumishe usafi. Kufikia mwisho wa zile siku 1,290 zilizotabiriwa, watakatifu walikuwa wakielekea kutakaswa na kuwa na msimamo mpya. Septemba 1922, wapata wakati barabara ambapo kipindi hicho kiliisha, walifanya mkusanyiko wa pekee huko Cedar Point, Ohio, Marekani. Ulichochea sana kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, bado kulikuwa na uhitaji wa kufanya maendeleo zaidi. Hayo yangefanywa katika kipindi cha pekee kilichofuata.

      FURAHA YA WATAKATIFU

      24, 25. (a) Ni kipindi gani cha wakati kinachotabiriwa kwenye Danieli 12:12, na yaonekana kilianza lini na kukoma lini? (b) Mabaki ya watiwa-mafuta walikuwa na hali gani ya kiroho mwanzoni mwa zile siku 1,335?

      24 Malaika wa Yehova amalizia unabii wake kuhusu watakatifu kwa maneno haya: “Heri [“Mwenye furaha ni yule,” NW] angojaye, na kuzifikilia [“kuzitarajia,” NW] siku hizo elfu na mia tatu na thelathini na tano.” (Danieli 12:12) Malaika hadokezi jambo lolote juu ya wakati ambapo kipindi hicho huanza au kumalizika. Historia yadokeza kwamba chafuatia karibu-karibu kile kipindi kilichokitangulia. Kwa hiyo, kingeanza vuli ya 1922 hadi mwisho-mwisho wa masika ya 1926 (kwenye Kizio cha Kaskazini). Je, watakatifu walifurahi mwishoni mwa kipindi hicho? Naam, katika njia muhimu za kiroho.

      25 Hata baada ya mkusanyiko mwaka wa 1922 (unaoonyeshwa kwenye ukurasa wa 302), baadhi ya watakatifu wa Mungu wangali walikuwa wakitamani nyakati zilizopita. Bado chanzo chao cha msingi cha habari za kujifunza kwenye mikutano kilikuwa Biblia na yale mabuku ya Studies in the Scriptures, yaliyoandikwa na C. T. Russell. Wakati huo, watu wengi walikuwa na maoni ya kwamba mwaka wa 1925 ndio mwaka ambao ufufuo ungeanza na Paradiso ingerejeshwa duniani. Kwa hiyo, wengi walitumikia wakiwa na tarehe fulani hususa akilini. Wengine walikataa kwa kiburi kushiriki katika kazi ya kuhubiria watu. Hali hiyo haikuwa yenye kufurahisha.

      26. Zile siku 1,335 zilipokuwa zikiendelea, hali ya kiroho ya watiwa-mafuta ilibadilikaje?

      26 Hata hivyo, zile siku 1,335 zilipoendelea, mambo yakaanza kubadilika. Kuhubiri kukatangulizwa, huku mipango ikifanywa ili kila mtu ashiriki katika huduma ya shambani. Mipango ilifanywa ili watu wajifunze The Watch Tower kwenye mikutano kila juma. Makala ya Machi 1, 1925, ilikuwa na makala ya kihistoria yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa,” ikiwaelewesha kikamili watu wa Mungu juu ya mambo yaliyotukia kipindi cha kati ya 1914 na 1919. Baada ya mwaka wa 1925 kupita, watakatifu hawakuendelea kumtumikia Mungu wakiwa na tarehe hususa akilini. Badala yake, kutakaswa kwa jina la Yehova kulikuwa jambo la kutangulizwa. Kweli hiyo muhimu ilikaziwa, kuliko wakati mwingine wowote, katika makala ya gazeti Watch Tower la Januari 1, 1926, yenye kichwa “Ni Nani Atakayemheshimu Yehova?” Kwenye mkusanyiko katika Mei 1926, kitabu Deliverance kilitolewa. (Ona ukurasa wa 302.) Hicho kilikuwa kitabu kimoja katika mfululizo wa vitabu vilivyokusudiwa kuchukua mahali pa Studies in the Scriptures. Watakatifu waliacha kutazama nyuma. Walikuwa wakitazamia kwa uhakika wakati ujao na kazi iliyokuwa mbele yao. Kwa hiyo, kama ilivyotabiriwa zile siku 1,335 zilikoma watakatifu wakiwa na furaha.

      27. Kuchunguza Danieli sura ya 12 hutusaidiaje kuwatambua kabisa watiwa-mafuta wa Yehova?

      27 Bila shaka, si wote waliovumilia kipindi hicho chenye msukosuko. Hapana shaka kwamba ndiyo sababu iliyomfanya malaika akazie umuhimu wa “kuzitarajia.” Wale waliovumilia na kuendelea kuwa na matarajio walibarikiwa sana. Kuchunguza Danieli sura ya 12 kwadhihirisha hilo. Kama ilivyotabiriwa, watiwa-mafuta walifufuliwa kiroho. Walipewa ufahamu wenye kina wa pekee wa Neno la Mungu, wakiwezeshwa ‘kwenda mbio huko na huko’ katika hilo, wakiongozwa na roho takatifu, na kufunua mambo ambayo yamekuwa mafumbo kwa muda mrefu. Yehova aliwatakasa na kuwafanya wang’ae kiroho, wakiwa waangavu kama nyota. Kwa hiyo, waliwasaidia wengi wawe na msimamo wenye uadilifu mbele za Yehova Mungu.

      28, 29. “Wakati wa mwisho” ukaribiapo, twapaswa kuazimia nini?

      28 Kwa kuwa kuna alama nyingi za kiunabii za kuwatambua “watakatifu wa Aliye juu,” twawezaje kushindwa kuwatambua na kushirikiana nao? Umati mkubwa unaojiunga na jamii inayopungua ya watiwa-mafuta katika kumtumikia Yehova, utapata baraka nzuri ajabu. Ni lazima sisi sote tuendelee kutarajia utimizo wa ahadi za Mungu. (Habakuki 2:3) Katika siku yetu Mikaeli, yule Jemadari Mkuu, amekuwa akisimama kwa niaba ya watu wa Mungu kwa makumi ya miaka. Hivi karibuni, atachukua hatua akiwa mfishaji aliyewekwa na Mungu wa mfumo huu wa mambo. Afanyapo hivyo, tutasimama wapi?

      29 Jibu la swali hilo lategemea ikiwa twachagua kuishi maisha ya uaminifu-maadili leo. Ili kuimarisha azimio letu la kufanya hivyo “wakati wa mwisho” ukaribiapo, acheni tuuchunguze mstari wa mwisho wa kitabu cha Danieli. Kuuzungumzia katika sura inayofuata kutatusaidia kuona jinsi Danieli alivyosimama mbele za Mungu wake na jinsi atakavyosimama mbele Zake wakati ujao.

      [Maelezo ya Chini]

      a Septuagint ya Kigiriki huitafsiri kuwa “dhabihu” tu.

  • Kuwatambua Waabudu wa Kweli Katika Wakati wa Mwisho
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • [Sanduku katika ukurasa wa 298]

      KUONDOLEWA KWA SADAKA YA KUTEKETEZWA DAIMA

      Katika kitabu cha Danieli, maneno “sadaka ya kuteketezwa daima” (au “sadaka ya kuteketezwa kila siku”) yapatikana mara tano. Yarejezea dhabihu ya sifa—“tunda la midomo”—ambayo watumishi wa Yehova Mungu humtolea kwa ukawaida. (Waebrania 13:15) Kuondolewa kwake kulikotabiriwa kwarejezewa kwenye Danieli 8:11, 11:31, na 12:11.

      Wakati wa vita viwili vya ulimwengu, watu wa Yehova walinyanyaswa vikali katika milki za “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini.” (Danieli 11:14, 15) “Sadaka ya kuteketezwa daima” iliondolewa kuelekea mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, wakati ambapo kazi ya kuhubiri ilikaribia sana kusimamishwa kwa muda katikati ya mwaka wa 1918. (Danieli 12:7) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, “sadaka ya kuteketezwa daima” vilevile ‘iliondolewa’ kwa siku 2,300 na Serikali ya Uingereza na Marekani. (Danieli 8:11-14; ona Sura ya 10 ya kitabu hiki.) Pia iliondolewa na “wenye silaha” wa Nazi kwa kipindi cha wakati kisichotajwa kwenye Maandiko.—Danieli 11:31; ona Sura ya 15 ya kitabu hiki.

      [Chati/Picha katika ukurasa wa 301]

      NYAKATI ZA KIUNABII KATIKA DANIELI

      Nyakati saba (miaka 2,520): Oktoba 607 K.W.K.

      Danieli 4:16, 25 hadi Oktoba 1914 W.K.

      (Ufalme wa Kimesiya wasimamishwa.

      Ona Sura ya 6 ya kitabu hiki.)

      Nyakati tatu na nusu Desemba 1914 hadi Juni 1918

      (Siku 1,260): (Wakristo watiwa-mafuta

      Danieli 7:25; 12:7 wasumbuliwa. Ona Sura ya 9

      ya kitabu hiki.)

      Jioni na asubuhi Juni 1 au 15, 1938, hadi

      2,300: Oktoba 8 au 22, 1944

      Danieli 8:14 (“Umati mkubwa” watokea,

      waongezeka. Ona Sura ya 10

      ya kitabu hiki.)

      Majuma 70 (miaka 490): 455 K.W.K. hadi 36 W.K.

      Danieli 9:24-27 (Kuja kwa Mesiya na huduma

      yake ya kidunia. Ona Sura ya 11

      ya kitabu hiki.)

      Siku 1,290: Januari 1919 hadi

      Danieli 12:11 Septemba 1922

      (Wakristo watiwa-mafuta waamka

      na kuendelea kiroho.)

      Siku 1,335: Septemba 1922 hadi Mei 1926

      Danieli 12:12 (Wakristo watiwa-mafuta

      wafurahi.)

      [Picha katika ukurasa wa 287]

      Watumishi mashuhuri wa Yehova walifungwa gerezani isivyo haki huko Atlanta, Georgia, Marekani. Kutoka kushoto kuelekea kulia: (wanaoketi) A. H. Macmillan, J. F. Rutherford, W. E. Van Amburgh; (wanaosimama) G. H. Fisher, R. J. Martin, G. DeCecca, F. H. Robison, na C. J. Woodworth

      [Picha katika ukurasa wa 299]

      Mikusanyiko muhimu ilifanywa huko Cedar Point, Ohio, Marekani, mwaka wa 1919 (juu) na mwaka wa 1922 (chini)

      [Picha katika ukurasa wa 302]

  • Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya Ajabu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • Sura Ya Kumi Na Nane

      Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya Ajabu

      1, 2. (a) Mkimbiaji anahitaji sifa gani muhimu ili afanikiwe? (b) Mtume Paulo alilinganishaje maisha ya uaminifu katika utumishi wa Yehova na shindano la mbio?

      MKIMBIAJI ang’ang’ana kufikia mwisho wa mbio. Amechoka sana, lakini yu karibu kuufikia mradi wake, atumia nguvu zote alizo nazo kupiga hatua hizo chache za mwisho. Akikaza misuli yake yote, avuka mstari wa mwisho hatimaye! Uso wake waonyesha utulivu na furaha ya ushindi. Kuvumilia hadi mwisho kumemthawabisha.

      2 Mwishoni mwa sura ya 12 ya Danieli, twamwona yule nabii mpendwa akielekea mwisho wa “shindano la mbio” lake mwenyewe—maisha yake akimtumikia Yehova. Baada ya kutaja vielelezo kadhaa vya imani miongoni mwa watumishi wa Yehova wa kabla ya Ukristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa hiyo, basi, kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi likituzingira, acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu, tumkaziapo macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu. Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:1, 2.

      3. (a) Ni nini kilichomchochea Danieli ‘akimbie kwa uvumilivu’? (b) Ni mambo gani matatu tofauti ambayo malaika wa Yehova alimwambia Danieli?

      3 Danieli alikuwa miongoni mwa ‘wingu hilo kubwa la mashahidi.’ Bila shaka alikuwa mtu aliyelazimika ‘kukimbia kwa uvumilivu,’ na kumpenda Mungu sana kulimchochea afanye hivyo. Yehova alikuwa amemfunulia Danieli mambo mengi juu ya wakati ujao wa serikali za ulimwengu, lakini sasa Alimpelekea kitia-moyo hiki cha kibinafsi: “Lakini enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule; maana wewe utastarehe, nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.” (Danieli 12:13) Malaika wa Yehova alikuwa akimwambia Danieli mambo matatu tofauti: (1) kwamba Danieli apaswa ‘kwenda hata awe mwisho ule,’ (2) kwamba ‘angestarehe,’ na (3) kwamba ‘angesimama’ tena wakati ujao. Maneno hayo yaweza kuwatiaje moyo Wakristo leo wavumilie hadi mwisho katika shindano la mbio la uhai?

      “ENENDA ZAKO HATA UTAKAPOKUWA MWISHO ULE”

      4. Malaika wa Yehova alimaanisha nini aliposema “enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule,” na kwa nini huenda hilo lilikuwa jambo gumu kwa Danieli?

      4 Malaika huyo alimaanisha nini alipomwambia Danieli: “Lakini enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule”? Mwisho wa nini? Kwa kuwa Danieli alikuwa akikaribia umri wa miaka 100, yaonekana hilo lilirejezea mwisho wa uhai wake mwenyewe, ambao yamkini ulikuwa karibu sana.a Malaika huyo alikuwa akimhimiza Danieli avumilie kwa uaminifu hadi kifo. Lakini hilo halimaanishi kwamba ingekuwa rahisi. Danieli aliona Babiloni ikipinduliwa na akaona mabaki ya wahamishwa Wayahudi wakirudi Yuda na Yerusalemu. Lazima mambo hayo yawe yalimfurahisha sana nabii huyo mzee. Hata hivyo, hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba alijiunga nao. Huenda alikuwa mzee sana na mdhaifu kufikia wakati huo. Au huenda Yehova alitaka abaki Babiloni. Vyovyote vile, mtu angetaka kujua ikiwa Danieli alikuwa na tamaa fulani huku wananchi wenzake walipokuwa wakiondoka kurudi Yuda.

      5. Ni mambo gani yanayodokeza kwamba Danieli alivumilia hadi mwisho?

      5 Haikosi Danieli alitiwa nguvu nyingi na taarifa ya fadhili ya malaika huyo: “Enenda zako hata utakapokuwa mwisho ule.” Huenda tukakumbuka maneno aliyosema Yesu Kristo karne sita hivi baadaye: “Yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:13) Yaonekana hivyo ndivyo alivyofanya Danieli. Alivumilia hadi mwisho, akikimbia shindano la mbio la uhai kwa uaminifu hadi mwisho kabisa. Huenda hiyo ni mojawapo ya sababu zinazomfanya arejezewe vizuri baadaye katika Neno la Mungu. (Waebrania 11:32, 33) Ni nini kilichomwezesha Danieli avumilie hadi mwisho? Rekodi ya maisha yake yatujibu.

      KUVUMILIA AKIWA MWANAFUNZI WA NENO LA MUNGU

      6. Twajuaje kwamba Danieli alijifunza Neno la Mungu kwa bidii?

      6 Kwa habari ya Danieli, kuvumilia hadi mwisho kulitia ndani kuendelea kujifunza na kutafakari sana ahadi zenye kusisimua za Mungu. Twajua kwamba Danieli alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu. La sivyo, angaliwezaje kujua kwamba Yehova alimwahidi Yeremia kwamba uhamisho ungedumu miaka 70? Danieli mwenyewe aliandika hivi: “Mimi . . . kwa kuvisoma vitabu, nalifahamu hesabu ya miaka.” (Danieli 9:2; Yeremia 25:11, 12) Huenda Danieli alivitafuta kwa bidii vitabu vya Neno la Mungu vilivyokuwako wakati huo. Maandishi ya Musa, Daudi, Solomoni, Isaya, Yeremia, Ezekieli—yoyote aliyoweza kupata—kwa hakika yalimwandalia Danieli saa nyingi nzuri za kusoma na kutafakari.

      7. Tunapolinganisha wakati wetu na siku za Danieli, twafaidikaje kwa kujifunza Neno la Mungu?

      7 Ili tusitawishe uvumilivu leo ni muhimu kujifunza Neno la Mungu, kuvama katika hilo. (Waroma 15:4-6; 1 Timotheo 4:15) Nasi tuna Biblia nzima, inayotia ndani rekodi iliyoandikwa ya jinsi baadhi ya unabii mbalimbali wa Danieli ulivyotimizwa karne nyingi baadaye. Isitoshe, tumebarikiwa kuishi “wakati wa mwisho,” uliotabiriwa kwenye Danieli 12:4. Leo, watiwa-mafuta wamebarikiwa kuwa na ufahamu wa kiroho wenye kina, waking’aa kama mienge ya kweli katika ulimwengu huu wenye giza. Kwa sababu hiyo, unabii mwingi wenye kina katika kitabu cha Danieli, ambao baadhi yake ulikuwa fumbo kwake, una maana nyingi kwetu leo. Kwa hiyo, acheni tuendelee kujifunza Neno la Mungu kila siku, bila kuyachukua mambo hayo kivivi hivi tu. Kufanya hivyo kutatusaidia kuvumilia.

      DANIELI ALISALI DAIMA

      8. Danieli aliweka kielelezo gani juu ya sala?

      8 Sala pia ilimsaidia Danieli avumilie hadi mwisho. Alimwendea Yehova Mungu katika sala kila siku na kuongea naye akiwa na moyo uliojaa imani na uhakika. Alijua kwamba Yehova ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW; linganisha Waebrania 11:6.) Moyo wa Danieli ulipolemewa na huzuni kwa sababu ya uasi wa Israeli, alimweleza Yehova hisia zake zote. (Danieli 9:4-19) Hata Dario alipoagiza kwamba watu wote wamwombe yeye peke yake kwa muda wa siku 30, Danieli hakuruhusu hilo limzuie asisali kwa Yehova Mungu. (Danieli 6:10) Je, mioyo yetu haiguswi kumwazia mzee huyo mwaminifu akijasiria kutupwa kwenye tundu lililojaa simba badala ya kuacha pendeleo lenye thamani la kusali? Hapana shaka kwamba Danieli alienda zake kwa uaminifu hata alipofikia mwisho, akisali kwa bidii kwa Yehova kila siku.

      9. Kwa nini hatupaswi kamwe kupuuza pendeleo la sala?

      9 Sala ni tendo sahili. Twaweza kusali karibu wakati wowote, mahali popote, kwa sauti au kimyakimya. Hata hivyo, tusilipuuze kamwe pendeleo hili lenye thamani. Biblia huhusianisha sala na uvumilivu, ustahimilivu, na kuendelea kuwa macho kiroho. (Luka 18:1; Waroma 12:12; Waefeso 6:18; Wakolosai 4:2) Je, si jambo lenye kutokeza kwamba twaweza kuwasiliana wakati wowote kwa uhuru na mtu mkuu zaidi ulimwenguni? Naye husikiliza! Kumbuka pindi ambayo Danieli alisali, na Yehova akatuma malaika. Malaika huyo alifika Danieli akiwa angali anasali! (Danieli 9:20, 21) Huenda leo tusitembelewe na malaika hao, lakini Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Vile tu alivyosikiliza sala ya Danieli, atasikiliza sala zetu. Na tusalipo, twamkaribia Yehova, tukifanyiza kifungo kitakachotusaidia kuvumilia hadi mwisho, kama alivyofanya Danieli.

      KUVUMILIA AKIWA MWALIMU WA NENO LA MUNGU

      10. Kwa nini kufundisha kweli ya Neno la Mungu kulikuwa jambo muhimu kwa Danieli?

      10 Danieli alipaswa ‘kuenda zake hata atakapokuwa mwisho ule’ katika maana nyingine. Alipaswa kuvumilia akiwa mwalimu wa kweli. Hakusahau kamwe kwamba alikuwa mmoja wa wateule ambao Maandiko yalikuwa yamesema hivi juu yao: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA, na mtumishi niliyemchagua.” (Isaya 43:10) Danieli alifanya yote aliyoweza ili kuutimiza utume huo. Yamkini kazi yake ilitia ndani kuwafundisha watu wake mwenyewe waliokuwa uhamishoni Babiloni. Hatujui mengi kuhusu shughuli zake na Wayahudi wenzake isipokuwa ushirika wake na wale vijana watatu waliorejezewa kuwa “wenzake”—Hanania, Mishaeli, na Azaria. (Danieli 1:7; 2:13, 17, 18) Bila shaka, urafiki wao wa karibu uliwasaidia sana wavumilie. (Mithali 17:17) Danieli, aliyebarikiwa kuwa na ufahamu wa pekee wenye kina kutoka kwa Yehova, alikuwa na mengi ya kuwafundisha rafiki zake. (Danieli 1:17) Lakini alikuwa na kazi nyingine pia ya kufundisha.

      11. (a) Kazi ya Danieli ilikuwaje ya pekee? (b) Danieli alikuwa na matokeo kadiri gani katika kuutekeleza mgawo wake usio wa kawaida?

      11 Danieli alikuwa na kazi kubwa ya kuwahubiria maofisa Wasio Wayahudi kuliko nabii mwingine yeyote. Ingawa mara nyingi aliwatolea ujumbe ambao haukuwapendeza, hakuwatendea watawala hao kana kwamba walikuwa wenye kukirihisha au kana kwamba walikuwa chini yake kwa njia fulani. Aliongea nao kwa heshima na ustadi. Baadhi yao—kama vile wale magavana wenye wivu waliopanga njama auawe—walitaka kumwangamiza Danieli. Hata hivyo, maofisa wengine walimheshimu. Kwa sababu Yehova alimwezesha Danieli afafanue siri zilizokuwa fumbo kwa wafalme na watu wenye hekima, nabii huyo alipata kuwa maarufu sana. (Danieli 2:47, 48; 5:29) Ni kweli kwamba alipozeeka, hangeweza kuwa mtendaji kama alipokuwa kijana. Lakini kwa hakika alienda zake hata mwisho ule, bado akitafuta kwa uaminifu njia yoyote ya kuwa shahidi wa Mungu wake mpendwa.

      12. (a) Sisi Wakristo hushiriki kazi gani ya kufundisha leo? (b) Twaweza kufuataje shauri la Paulo kwamba ‘tuendelee kutembea katika hekima kuelekea wale walio nje’?

      12 Katika kutaniko la Kikristo leo, huenda tukapata waandamani waaminifu watakaotusaidia tuvumilie, kama vile Danieli na washiriki wake watatu walivyosaidiana. Sisi hufundishana pia, tukiandaa “badilishano la kitia-moyo.” (Waroma 1:11, 12) Kama Danieli, tuna utume wa kuhubiria wasioamini. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa hiyo, twahitaji kuboresha stadi zetu ili tuweze ‘kulitumia sawasawa neno la ile kweli’ katika kuongea na watu juu ya Yehova. (2 Timotheo 2:15) Pia kutii shauri hili la mtume Paulo kutatusaidia: “Endeleeni kutembea katika hekima kuelekea wale walio nje.” (Wakolosai 4:5) Hekima hiyo hutia ndani mtazamo wenye usawaziko juu ya wale wenye imani tofauti. Hatuwadharau watu hao, tukijiona kuwa bora. (1 Petro 3:15) Badala yake, sisi hujaribu kuwavutia kwenye ile kweli, tukitumia Neno la Mungu kwa busara na ustadi ili tuifikie mioyo yao. Tunapofaulu kumfikia mtu, hilo hutupatia shangwe kama nini! Shangwe hiyo hutusaidia kuvumilia hadi mwisho, kama alivyofanya Danieli.

      “WEWE UTASTAREHE”

      13, 14. Kwa nini tazamio la kufa liliwaogofya Wababiloni wengi, na maoni ya Danieli yalikuwa tofauti jinsi gani?

      13 Kisha malaika huyo amhakikishia Danieli hivi: “Wewe utastarehe.” (Danieli 12:13) Maneno hayo yalimaanisha nini? Danieli alijua kwamba angekufa. Tangu wakati wa Adamu hadi leo wanadamu wote hufa, wapende wasipende. Kwa kufaa, Biblia hukiita kifo “adui.” (1 Wakorintho 15:26) Hata hivyo, kwa Danieli tazamio la kufa lilikuwa na maana tofauti kabisa na lile tazamio la kufa la Wababiloni waliomzunguka. Kwao, wakiabudu miungu 4,000 isiyo ya kweli, kifo kilimaanisha maogofyo mengi sana. Waliamini kwamba baada ya kifo, watu waliokuwa wameishi bila furaha au waliokufa kijeuri waligeuka wakawa roho zenye kulipiza kisasi zilizowasumbua walio hai. Pia Wababiloni waliamini katika ulimwengu wa wafu wenye kuogofya, uliojaa madubwana yenye maumbo kama ya wanadamu na ya wanyama.

      14 Kwa Danieli, kifo hakikumaanisha lolote la mambo hayo. Mamia ya miaka kabla ya wakati wa Danieli, Mfalme Solomoni alikuwa amepuliziwa na Mungu aseme hivi: “Wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Na juu ya mtu anayekufa, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4) Kwa hiyo, Danieli alijua kwamba maneno aliyoambiwa na malaika huyo yangetimia. Kifo ni pumziko. Hakuna mawazo, hakuna kughairi kwa uchungu, hakuna kuteswa-teswa—na bila shaka hakuna madubwana. Yesu Kristo alitaja mambo kwa njia hiyohiyo Lazaro alipokufa. Alisema: “Lazaro rafiki yetu ameenda kupumzika.”—Yohana 11:11.

      15. Siku ya kufa yawezaje kuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa?

      15 Fikiria sababu nyingine ambayo ilifanya tazamio la kufa lisimwogofye Danieli. Neno la Mungu husema hivi: “Heri sifa njema [“jina,” NW] kuliko marhamu nzuri; na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa.” (Mhubiri 7:1) Siku ya kufa, wakati wa kuomboleza, ikiwa ingalikuwapo, ingewezaje kuwa siku ya shangwe kuliko siku ya kuzaliwa? Jambo kuu ni “jina.” “Marhamu nzuri” ingeweza kuwa ya bei ghali mno. Maria, dada ya Lazaro alipaka miguu ya Yesu mafuta yenye marashi ambayo yaligharimu karibu mshahara wa mwaka mzima! (Yohana 12:1-7) Jina tu lingewezaje kuwa na thamani kubwa hivyo? Kwenye Mhubiri 7:1, Zaire Swahili Bible husema, “jina zuri.” Jambo muhimu si jina tu, lakini maana ya jina hilo. Mtu anapozaliwa, hakuna sifa yoyote, wala rekodi yoyote ya kazi nzuri, wala kumbukumbu lolote zuri la utu na sifa zake. Lakini mwishoni mwa maisha yake, jina huonyesha yote hayo. Na ikiwa ni jina zuri machoni pa Mungu, ni lenye thamani zaidi kuliko mali zozote za kimwili mtu anazoweza kupata.

      16. (a) Danieli alijitahidije kujifanyia jina zuri na Mungu? (b) Danieli angewezaje kwenda kupumzika akiwa na uhakika kabisa kwamba alikuwa amefanikiwa kujifanyia jina zuri na Yehova?

      16 Katika maisha yake yote, Danieli alifanya yote aliyoweza ili kujifanyia jina zuri na Mungu, naye Yehova hakupuuza yoyote ya mambo hayo. Alimtazama Danieli na kuuchunguza moyo wake. Mungu alikuwa amemfanyia Mfalme Daudi vivyo hivyo, aliyeimba hivi: “Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; umelifahamu wazo langu tokea mbali.” (Zaburi 139:1, 2) Ni kweli kwamba Danieli hakuwa mkamilifu. Alikuwa mzao wa Adamu mtenda-dhambi naye alikuwa mshiriki wa taifa lenye dhambi. (Waroma 3:23) Lakini Danieli alitubu dhambi zake na kuendelea kujaribu kutembea na Mungu wake kwa unyoofu. Kwa hiyo, mtume huyo mwaminifu angeweza kuwa na uhakika wa kwamba Yehova angemsamehe dhambi zake wala hangemwekea kinyongo. (Zaburi 103:10-14; Isaya 1:18) Yehova huchagua kukumbuka kazi nzuri za watumishi wake. (Waebrania 6:10) Kwa hiyo, malaika wa Yehova alimtaja Danieli mara mbili kuwa ‘mtu apendwaye sana.’ (Danieli 10:11, 19) Hilo lilimaanisha kwamba Mungu alimpenda Danieli. Danieli angeweza kupumzika akiwa ameridhika, akijua kwamba alijifanyia jina zuri na Yehova.

      17. Kwa nini ni muhimu tujifanyie jina zuri na Yehova leo?

      17 Kila mmoja wetu apaswa kujiuliza hivi, ‘Je, nimejifanyia jina zuri na Yehova?’ Twaishi nyakati zenye taabu. Kutambua kwamba twaweza kufa wakati wowote sio kuwaza mambo yenye kutisha bali ni kuona mambo kihalisi. (Mhubiri 9:11) Basi, ni muhimu kama nini kwamba kila mmoja wetu aazimie kujifanyia jina zuri na Mungu sasa hivi, bila kukawia. Tukifanya hivyo, hatuhitaji kuhofu kifo. Ni pumziko tu—kama usingizi. Na kama vile usingizi, chafuatwa na kuamka!

      “UTASIMAMA”

      18, 19. (a) Malaika alimaanisha nini alipomwambia Danieli kwamba ‘angesimama’ wakati ujao? (b) Danieli angewezaje kujua juu ya tumaini la ufufuo?

      18 Kitabu cha Danieli chamalizika kwa mojawapo ya ahadi nzuri sana ambazo Mungu amepata kumwahidi mwanadamu. Malaika wa Yehova alimwambia Danieli hivi: “Nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.” Malaika huyo alimaanisha nini? Basi, kwa kuwa ‘starehe’ aliyokuwa ametoka tu kurejezea ilikuwa kifo, ahadi ya kwamba Danieli ‘angesimama’ wakati fulani ujao, ingeweza kumaanisha kitu kimoja tu—ufufuo!b Hata wasomi fulani wamesisitiza kwamba Danieli sura ya 12 ina rejezo la kwanza lililo wazi kabisa juu ya ufufuo liwezalo kupatikana katika Maandiko ya Kiebrania. (Danieli 12:2) Hata hivyo, wamekosea. Danieli alijua vema juu ya tumaini la ufufuo.

      19 Kwa kielelezo, haikosi Danieli alijua maneno haya ambayo Isaya alikuwa amerekodi karne mbili mapema: “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana . . . ardhi itawatoa waliokufa.” (Isaya 26:19) Muda mrefu kabla ya hapo, Eliya na Elisha waliwezeshwa na Yehova kufufua watu kihalisi. (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37) Hata mapema zaidi, Hana, mama ya nabii Samweli, alikiri kwamba Yehova aweza kuleta watu juu kutoka kuzimu, kaburini. (1 Samweli 2:6) Isitoshe, hata mapema zaidi, Yobu mwaminifu alionyesha tumaini lake mwenyewe katika maneno haya: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu, hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. Wewe ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:14, 15.

      20, 21. (a) Kwa hakika Danieli atapata ufufuo gani? (b) Yamkini ufufuo katika Paradiso utafanywaje?

      20 Kama Yobu, Danieli alikuwa na sababu za kuwa na uhakika kwamba Yehova kwa kweli angetamani sana kumrudisha kwenye uhai siku fulani wakati ujao. Hata hivyo, bado lazima alitiwa moyo sana kusikia kiumbe-roho chenye nguvu kikimhakikishia tumaini hilo. Ndiyo, Danieli atasimama katika “ufufuo wa walio waadilifu,” utakaofanywa wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo. (Luka 14:14) Hilo litakuwaje kwa Danieli? Neno la Mungu hutuambia mengi zaidi juu yake.

      21 Yehova ni “Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Basi ni dhahiri kwamba ufufuo katika Paradiso utafanywa kwa utaratibu. Huenda wakati fulani utakuwa umepita tangu Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Mfumo wa mambo wa kale utakuwa umeondolewa kabisa, na bila shaka matayarisho ya kuwakaribisha wafu yatakuwa yamefanywa. Kwa habari ya utaratibu ambao wafu watafufuliwa, Biblia yatoa utaratibu huu: “Kila mmoja katika daraja lake mwenyewe.” (1 Wakorintho 15:23) Yaonekana kwamba wakati wa “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu,” waadilifu watafufuliwa kwanza. (Matendo 24:15) Kwa hiyo, watu waaminifu wa kale, kama vile Danieli, wataweza kusaidia katika kusimamia mambo ya kidunia, kutia ndani kufundisha mabilioni ya “wasio waadilifu” watakaofufuliwa.—Zaburi 45:16.

      22. Huenda Danieli atakuwa na hamu ya kujibiwa maswali gani?

      22 Kabla Danieli hajawa tayari kutwaa madaraka hayo, huenda atakuwa na maswali ya kuuliza. Kwani, alisema hivi kuhusu unabii mbalimbali mgumu aliokabidhiwa: “Nami nikasikia, lakini sikuelewa.” (Danieli 12:8) Atasisimuka kama nini kuweza kuelewa mafumbo hayo ya Mungu hatimaye! Huenda atataka kusikia yote juu ya Mesiya. Danieli atapata kujua na kustaajabia mfuatano wa serikali za ulimwengu tangu siku yake mwenyewe hadi leo, atajua ni nani “watakatifu wa Aliye juu”—waliovumilia licha ya minyanyaso katika “wakati wa mwisho”—na juu ya ule uharibifu wa mwisho wa falme zote utakaoletwa na Ufalme wa Kimesiya wa Mungu.—Danieli 2:44; 7:22; 12:4.

      KURA YA DANIELI NA YAKO KATIKA PARADISO!

      23, 24. (a) Ulimwengu ambao Danieli atajikuta ndani yake utakuwaje tofauti na ulimwengu alioujua? (b) Je, Danieli atakuwa na mahali katika Paradiso, nasi twajuaje?

      23 Danieli atataka kujua juu ya ulimwengu atakaojikuta ndani yake wakati huo—ulimwengu ulio tofauti sana na ule alioishi. Hakutakuwa na vita vyovyote wala uonezi wowote ambao uliharibu ulimwengu alioujua. Hakutakuwa majonzi yoyote, ugonjwa wowote, wala kifo chochote. (Isaya 25:8; 33:24) Lakini kutakuwa na wingi wa chakula, nyumba nyingi, na kazi yenye kuridhisha kwa watu wote. (Zaburi 72:16; Isaya 65:21, 22) Wanadamu watakuwa familia moja iliyoungana na yenye furaha.

      24 Ni dhahiri kwamba Danieli atakuwa na mahali katika ulimwengu huo. “Utasimama katika kura yako,” malaika alimwambia. (Italiki ni zetu.) Neno la Kiebrania ambalo latafsiriwa “kura” hapa ndilo lilelile ambalo hutumiwa kurejezea viwanja halisi vya shamba.c Huenda Danieli aliujua unabii wa Ezekieli juu ya kugawa nchi iliyorudishwa ya Israeli. (Ezekieli 47:13–48:35) Katika utimizo wake kwenye Paradiso, unabii wa Ezekieli wadokeza nini? Kwamba watu wote wa Mungu watakuwa na mahali katika Paradiso, hata nchi itagawanywa kwa utaratibu na kwa haki. Bila shaka, kura ya Danieli katika Paradiso itahusisha mengi zaidi ya nchi tu. Itatia ndani fungu lake katika kusudi la Mungu huko. Hakika Danieli atapata thawabu aliyoahidiwa.

      25. (a) Ni matazamio gani ya maisha katika Paradiso yanayokupendeza? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba Paradiso ni makao ya wanadamu?

      25 Hata hivyo, vipi juu ya kura yako? Wewe vilevile waweza kupata ahadi hizo. Yehova anataka wanadamu watiifu ‘wasimame’ kwa ajili ya kura zao, wawe na mahali katika Paradiso. Hebu wazia! Kwa kweli, lingekuwa jambo lenye kusisimua kwelikweli kukutana na Danieli ana kwa ana, pamoja na wanaume na wanawake wengine waaminifu wa nyakati za Biblia. Kisha kutakuwa na wengine wengi watakaofufuliwa, watakaohitaji kufundishwa ili wapate kumjua na kumpenda Yehova Mungu. Jiwazie ukitunza makao yetu ya kidunia na kusaidia kuyafanya yawe paradiso yenye unamna-namna mwingi na uzuri wenye kudumu. Wazia kufundishwa na Yehova, kujifunza kuishi alivyokusudia wanadamu waishi. (Isaya 11:9; Yohana 6:45) Naam, una mahali katika Paradiso. Ingawa huenda wengine wakaiona Paradiso kuwa kitu kipya, kumbuka kwamba mwanzoni Yehova alikusudia wanadamu waishi mahali pa aina hiyo. (Mwanzo 2:7-9) Katika maana hiyo, Paradiso ndiyo makao ya asili ya mabilioni ya wakazi wa dunia. Huko ndiko kwao. Kufikia Paradiso kutakuwa sawa na kurudi nyumbani.

      26. Yehova anakirije kwamba si rahisi kwetu kungojea mwisho wa mfumo huu wa mambo?

      26 Mioyo yetu hujaa shukrani tunapofikiria yote hayo, sivyo? Je, wewe mwenyewe hutamani sana kuwa huko? Basi, si ajabu kwamba Mashahidi wa Yehova wana hamu sana ya kutaka kujua wakati ambapo mwisho wa mfumo huu wa mambo utakuja! Si rahisi kungoja. Yehova akiri hivyohivyo, kwa kuwa anatuhimiza ‘tuungojee’ mwisho ‘ujapokawia.’ Anamaanisha kwamba huenda ukakawia machoni petu, kwa kuwa katika andiko hilohilo, twahakikishiwa kwamba: ‘Hautachelewa.’ (Habakuki 2:3, NW; linganisha Mithali 13:12.) Naam, mwisho utakuja wakati barabara.

      27. Wapaswa kufanya nini ili usimame mbele za Mungu kwa umilele wote?

      27 Wapaswa kufanya nini mwisho ukaribiapo? Kama Danieli, nabii mpendwa wa Yehova, vumilia kwa uaminifu. Jifunze Neno la Mungu kwa bidii. Sali kwa bidii. Shirikiana na waabudu wenzako kwa upendo. Wafundishe wengine kweli kwa bidii. Mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo ukaribiapo kila siku, endelea kuazimia kuwa mtumishi mwaminifu-mshikamanifu wa Aliye Juu na mteteaji mwaminifu wa Neno lake. Kwa hali na mali, sikiliza unabii wa Danieli! Na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova akupe pendeleo la kusimama mbele zake kwa shangwe kwa umilele wote!

      [Maelezo ya Chini]

      a Danieli alipelekwa uhamishoni Babiloni mwaka wa 617 K.W.K., yamkini akiwa tineja. Alipata ono hili mwaka wa tatu wa Koreshi, au mwaka wa 536 K.W.K.—Danieli 10:1.

      b Kulingana na The Brown-Driver-Briggs Hebrew and English Lexicon, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-simama” ambalo latumiwa hapa larejezea “kuhuishwa baada ya kifo.”

      c Neno hilo la Kiebrania lahusiana na neno “kijiwe cha mviringo,” kwa kuwa vijiwe vidogo vilitumiwa kupiga kura. Nyakati nyingine nchi iligawanywa hivyo. (Hesabu 26:55, 56) Kichapo A Handbook on the Book of Daniel chasema kwamba hapa neno hilo lamaanisha “kilichowekwa kando (na Mungu) kwa ajili ya mtu.”

  • Yehova Amwahidi Danieli Thawabu ya Ajabu
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • [Picha katika ukurasa wa 307]

      [Picha katika ukurasa wa 318]

      Kama Danieli, je, wasikiliza neno la Mungu la kiunabii?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki