Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Inavunja Moyo na Kuharibu Imani
    Amkeni!—2007 | Septemba
    • Inavunja Moyo na Kuharibu Imani

      “MIILI ilitapakaa kila mahali nasi hatungeweza kutambua mahali nyumba yetu ilipokuwa,” akasema mwanamume fulani huko Sri Lanka baada ya tsunami kuharibu kijiji chao mnamo Desemba 2004. Katika makala moja kuhusu misiba, mhariri wa mambo ya kidini alisema kwamba nyakati nyingine yeye hujikuta akisali kwa hasira.

      Watu wengi huona misiba ya asili kuwa ni adhabu kutoka kwa Mungu. Mwandishi mmoja alifafanua tufani moja kuwa “ngumi ya Mungu.” Nchini Marekani, viongozi fulani wa kidini walifafanua matukio kama ya Tufani Katrina kuwa “hasira ya Mungu” dhidi ya “majiji yaliyojaa dhambi.” Huko Sri Lanka, Wabudha wanaoshikilia sana imani waliwalaumu Wakristo kwa sababu ya tsunami, na hivyo kuongeza mgawanyiko wa kidini. Naye Mhindu mmoja mwenye cheo fulani hekaluni alisema kwamba mungu aitwaye Shiva alikuwa amekasirika kwa sababu watu hawakuwa wakiishi kwa njia inayofaa. Kiongozi wa dini ya Wabudha nchini Marekani alisema hivi kuhusu misiba ya asili: “Hatujui kwa nini mambo hayo hufanyika. Hata hatujui kwa nini tuko hapa.”

      Unapoona picha za nyumba zilizoharibiwa, watu waliokufa, na watu walio na huzuni, je, nyakati nyingine wewe hujiuliza, ‘Kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka kwingi hivyo?’ Au je, unafikiri ‘Mungu ana sababu nyingi za kuruhusu mambo kama hayo yatendeke lakini hajafunua sababu hizo’? Makala zinazofuata zitachunguza habari hiyo. Pia zitazungumzia hatua fulani ambazo watu wanaweza kuchukua ili kupunguza hatari ya kujeruhiwa na kufa wakati ambapo msiba wa asili unatokea.

  • Je, Mungu Anapaswa Kulaumiwa?
    Amkeni!—2007 | Septemba
    • Je, Mungu Anapaswa Kulaumiwa?

      “MUNGU ni upendo,” Biblia inasema. (1 Yohana 4:8) Pia, yeye ni mwenye haki na huruma. “Yeye Mwamba, kazi zake ni kamilifu, kwa maana njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki; yeye ni mwadilifu na mnyoofu.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.

      Kwa kuwa yeye ni Muumba, Yehova Mungu ana uwezo wa kuona mapema vitu vyote vinavyoweza kusababisha madhara, naye ana nguvu za kuingilia mambo. Kwa kufikiria mambo hayo na sifa za Mungu katika Biblia, inaeleweka kwamba wengi huuliza, “Kwa nini Mungu huruhusu misiba ya asili itukie?”a Mamilioni ya watu ambao wameuliza swali hilo wamegundua kwamba Mungu mwenyewe anatoa jibu linalopatana na akili katika Neno lake lililoandikwa. (2 Timotheo 3:16) Tafadhali fikiria mambo yafuatayo.

      Walikataa Upendo wa Mungu

      Biblia inatuambia kwamba Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza kila kitu walichohitaji ili waishi kwa furaha na usalama. Isitoshe, kadiri ambavyo wao na watoto wao wangeendelea kutii amri ya Mungu ya ‘kuzaa na kuwa wengi, waijaze dunia,’ familia ya wanadamu ingeweza kutazamia kwamba Mungu angeendelea kuwatunza.—Mwanzo 1:28.

      Hata hivyo, kwa kusikitisha Adamu na Hawa walimwasi kimakusudi Muumba wao kwa kutomtii na kuchagua kutomtegemea. (Mwanzo 1:28; 3:1-6) Kwa wazi wanadamu wengi wamefuata kielelezo chao. (Mwanzo 6:5, 6, 11, 12) Kwa ufupi, wanadamu wamechagua kujiongoza na kuimiliki dunia bila kuongozwa na Mungu. Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye upendo ambaye anaheshimu hiari ya watu wake, Yehova hawalazimishi wanadamu wajitiishe chini ya enzi yake kuu, hata ikiwa kuikaidi kunaweza kuwaletea madhara.b

      Hata hivyo, Yehova hakuiacha familia ya wanadamu. Hadi leo “yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Kwa kuongezea, Mungu alimpa mwanadamu uwezo wa kujifunza kuhusu dunia na mizunguko yake, na kwa kadiri fulani ujuzi huo umewasaidia wanadamu kutabiri hali mbaya sana ya hewa na hatari nyingine, kama vile milipuko ya volkano.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki