Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Kaeni Katika Neno Langu’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • ‘Kaeni Katika Neno Langu’

      “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.”—YOHANA 8:31.

      1. (a) Yesu aliporudi mbinguni, aliacha nini duniani? (b) Tutazungumzia maswali gani?

      YESU KRISTO, yule Mwanzilishi wa Ukristo, hakuacha ameandika vitabu vyovyote, wala kujenga minara yoyote ya ukumbusho, wala kuacha amelundika mali hapa duniani aliporudi mbinguni. Hata hivyo, aliacha wanafunzi na vilevile matakwa hususa ya kuwa mwanafunzi. Kwa kweli, katika Injili ya Yohana, tunaona kwamba Yesu alitaja matakwa matatu muhimu ambayo mtu yeyote anayetaka kuwa mwanafunzi wake anapaswa kuyatimiza. Hayo ni matakwa gani? Tunaweza kufanya nini ili kuyatimiza? Nasi tunaweza kuhakikishaje kwamba tuna sifa zinazotustahilisha kuwa wanafunzi wa Kristo leo?a

      2. Kama lilivyoandikwa katika Injili ya Yohana, ni lipi takwa muhimu la kuwa mwanafunzi?

      2 Miezi sita hivi kabla ya kifo chake, Yesu alienda Yerusalemu na kuhubiria umati wa watu waliokuwa wamekusanyika huko kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda iliyosherehekewa kwa muda wa juma moja. Sherehe hiyo ilipokuwa katikati, “wengi wa umati waliweka imani katika yeye” kwa sababu ya mahubiri yake. Yesu aliendelea kuhubiri hivi kwamba siku ya mwisho ya sherehe hiyo, “wengi waliweka imani katika yeye.” (Yohana 7:10, 14, 31, 37; 8:30) Wakati huo, Yesu alielekeza fikira zake kwa waamini wapya na kutaja takwa moja muhimu la kuwa mwanafunzi ambalo liliandikwa na mtume Yohana: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.”—Yohana 8:31.

      3. Ni sifa gani inayohitajiwa ili mtu ‘akae katika neno la Yesu’?

      3 Yesu hakusema maneno hayo ili kuonyesha kwamba waamini wapya hawakuwa na imani. Badala yake, alikuwa akisema kwamba walikuwa na fursa ya kuwa wanafunzi wake wa kweli—mradi wangekaa katika neno lake na kuwa wavumilivu. Walikuwa wamekubali neno lake, lakini sasa walipaswa kukaa katika neno hilo. (Yohana 4:34; Waebrania 3:14) Kwa kweli, Yesu aliona uvumilivu kuwa sifa muhimu kwa wafuasi wake hivi kwamba alipozungumza na mitume wake mara ya mwisho, kama tusomavyo katika Injili ya Yohana, Yesu aliwasihi mara mbili hivi: ‘Endeleeni kunifuata mimi.’ (Yohana 21:19, 22) Wakristo wengi wa mapema walifanya hivyo. (2 Yohana 4) Ni nini kilichowasaidia kuvumilia?

      4. Ni nini kilichowawezesha Wakristo wa mapema kuvumilia?

      4 Mtume Yohana, aliyekuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo kwa miaka 70 hivi, alitaja jambo fulani muhimu. Aliwapongeza Wakristo waaminifu kwa kusema: “Nyinyi ni wenye nguvu na neno la Mungu hukaa katika nyinyi na mmemshinda mwovu.” Wanafunzi hao wa Kristo walivumilia, au walikaa katika neno la Mungu, kwa sababu neno la Mungu lilikaa ndani yao. Walilithamini sana. (1 Yohana 2:14, 24) Vivyo hivyo leo, ili ‘kuvumilia hadi mwisho,’ tunahitaji kuhakikisha kwamba neno la Mungu linakaa ndani yetu. (Mathayo 24:13) Tunawezaje kufanya hivyo? Tunapata jibu katika kielezi kimoja cha Yesu.

      “Anayelisikia Neno”

      5. (a) Yesu anataja aina gani tofauti za udongo katika mojawapo ya vielezi vyake? (b) Katika kielezi cha Yesu mbegu na udongo zinawakilisha nini?

      5 Yesu alitaja kielezi cha mpanzi anayepanda mbegu, ambacho kinapatikana katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka. (Mathayo 13:1-9, 18-23; Marko 4:1-9, 14-20; Luka 8:4-8, 11-15) Unaposoma masimulizi hayo, utaona kwamba jambo kuu katika kielezi hicho ni kwamba mbegu ileile inaanguka kwenye udongo mbalimbali na matokeo yakawa tofauti. Udongo wa kwanza ni mgumu, wa pili hauna kina, nao wa tatu umejaa miiba. Udongo wa nne ni “bora” na “mzuri,” tofauti na aina hizo tatu. Kulingana na ufafanuzi wa Yesu, mbegu ni ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu, nao udongo unawakilisha watu wenye hali mbalimbali za moyoni. Ingawa kuna mambo yanayofanana kuhusu watu wanaowakilishwa na aina hizo tofauti-tofauti za udongo, wale wanaowakilishwa na udongo ulio bora wana sifa fulani inayowatofautisha na wengine.

      6. (a) Aina ya nne ya udongo unaotajwa katika kielezi cha Yesu unatofautianaje na zile aina nyingine tatu, na hilo linamaanisha nini? (b) Ni nini kilicho muhimu ili kuonyesha uvumilivu tukiwa wanafunzi wa Kristo?

      6 Simulizi linalopatikana katika andiko la Luka 8:12-15 linaonyesha kwamba katika hali zote nne, watu ‘husikia neno.’ Hata hivyo, wale wenye “moyo ulio bora na mwema” huchukua hatua zaidi baada ya “kusikia lile neno.” ‘Wanalihifadhi na kuzaa matunda kwa uvumilivu.’ Kwa kuwa udongo ulio bora na mzuri ni wenye kina na si mgumu, mizizi ya mbegu hupenya ndani na kwa hiyo mbegu huota na kuzaa matunda. (Luka 8:8) Vivyo hivyo, wale wenye mioyo iliyo bora huelewa, huthamini, na kuvama katika neno la Mungu. (Waroma 10:10; 2 Timotheo 2:7) Neno la Mungu hukaa ndani yao. Kwa hiyo, wao huzaa matunda kwa uvumilivu. Hivyo basi, ni muhimu kulithamini sana Neno la Mungu ili tuweze kuonyesha uvumilivu tukiwa wanafunzi wa Kristo. (1 Timotheo 4:15) Hata hivyo, tunawezaje kusitawisha uthamini huo wa Neno la Mungu?

      Hali ya Moyoni na Kutafakari kwa Makini

      7. Ni jambo gani linalohusianishwa sana na moyo mzuri?

      7 Ona jambo ambalo Biblia inahusianisha na moyo ulio bora na mzuri. “Moyo wa mwenye haki hufikiri [“hutafakari,” NW] jinsi atakavyojibu.” (Mithali 15:28) “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya [“kutafakari kwa,” NW] moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA.” (Zaburi 19:14) “Kinywa changu kitanena hekima, na fikira za [“kutafakari kwa” NW] moyo wangu zitakuwa na busara.”—Zaburi 49:3.

      8. (a) Tunapaswa kuepuka nini tunaposoma Biblia, na tunapaswa kufanya nini? (b) Tunapata manufaa gani kwa kutafakari Neno la Mungu kwa sala? (Tia ndani sanduku “Mmewekwa Imara Katika Kweli.”)

      8 Kama waandikaji hao wa Biblia, sisi pia tunahitaji kutafakari Neno la Mungu na utendaji wake kwa njia inayofaa na kwa sala. Tunaposoma Biblia au vitabu vinavyozungumzia Biblia, hatupaswi kuwa kama watalii wenye haraka-haraka ambao hutoka kwenye mandhari moja yenye kuvutia huku wakipiga picha bila hata kufurahia mandhari hizo. Badala yake, tunapojifunza Biblia tungependa kutenga wakati wa kutosha kufurahia usomaji wetu.b Neno la Mungu huathiri moyo wetu tunapotafakari mambo tunayosoma. Neno la Mungu hugusa hisia zetu na kuelekeza fikira zetu. Pia hutuchochea kumweleza Mungu mawazo yetu ya ndani katika sala. Kwa hiyo, tunampenda Yehova zaidi, na upendo wetu kwake hutuchochea tuendelee kumfuata Yesu hata chini ya hali ngumu. (Mathayo 10:22) Bila shaka, ni muhimu kutafakari yale ambayo Mungu anasema iwapo tunataka kudumu tukiwa waaminifu hadi mwisho.—Luka 21:19.

      9. Tunawezaje kuhakikisha kwamba moyo wetu unaendelea kupokea neno la Mungu?

      9 Pia kielezi cha Yesu kinaonyesha kwamba kuna mambo yanayozuia mbegu ya neno la Mungu isikue. Kwa hiyo, ili tudumu tukiwa wanafunzi waaminifu, tunapaswa (1) kutambua vizuizi vinavyowakilishwa na hali mbalimbali zisizofaa za udongo katika kielezi hicho na (2) kuchukua hatua ya kurekebisha au kuepuka vizuizi hivyo. Kwa kufanya hivyo, tutahakikisha kwamba mioyo yetu inaendelea kupokea mbegu ya Ufalme na kuzaa matunda.

      “Kando ya Barabara” Yamaanisha Wale Wanaokengeushwa

      10. Fafanua aina ya kwanza ya udongo katika kielezi cha Yesu na ueleze udongo huo unamaanisha nini.

      10 Mbegu inaanguka kwanza kwenye udongo ulio “kando ya barabara,” ambapo mbegu hiyo ‘inakanyagwakanyagwa.’ (Luka 8:5) Udongo ulio kando ya barabara inayopita katikati ya shamba la nafaka ni mgumu kwa sababu ya kukanyagwa-kanyagwa na watu. (Marko 2:23) Vivyo hivyo, wale ambao huruhusu hekaheka za ulimwengu ziwakoseshe wakati na nguvu huenda wakajikuta wamekengeushwa na hivyo kukosa kulithamini neno la Mungu. Wanasikia neno hilo, lakini hawalitafakari. Kwa hiyo, mioyo yao inashindwa kulipokea. Kabla hawajaanza kulipenda, “Ibilisi huja na kuliondoa lile neno kutoka mioyoni mwao ili wasipate kuamini waokolewe.” (Luka 8:12) Je, jambo hilo linaweza kuepukwa?

      11. Tunaweza kuzuiaje hali yetu ya moyoni isiwe kama udongo mgumu?

      11 Kuna mengi yanayoweza kufanywa ili kuzuia moyo usiwe kama udongo ulio kando ya barabara ambao hautokezi mazao. Udongo ambao umekanyagwa-kanyagwa na kuwa mgumu unaweza kuwa laini ukilimwa na watu wakiacha kuukanyaga. Vivyo hivyo, kutafuta wakati wa kujifunza na kutafakari Neno la Mungu kunaweza kufanya moyo uwe kama udongo mzuri unaotokeza mazao. Siri ni kutokengeushwa na mambo ya kawaida maishani. (Luka 12:13-15) Badala yake, hakikisha kwamba unatenga wakati wa kutafakari “mambo yaliyo ya maana zaidi” maishani.—Wafilipi 1:9-11.

      “Juu ya Tungamo-Mwamba” Yamaanisha Kuwa Mwoga

      12. Sababu halisi ni ipi ambayo inafanya mche katika aina ya pili ya udongo unaotajwa kwenye kielezi cha Yesu unyauke?

      12 Mbegu inapoanguka kwenye aina ya pili ya udongo, haibaki hapo, kama ilivyokuwa katika aina ya kwanza ya udongo. Inaota mizizi na kuchipuka. Lakini jua linapotokea, mche huo unachomwa na joto la jua na kunyauka. Hata hivyo, ona jambo hili muhimu. Mche huo haunyauki hasa kwa sababu ya joto. Kwani, mmea unaomea katika udongo mzuri unapigwa na jua pia, lakini haunyauki—unasitawi. Mbona kuwe na tofauti hiyo? Yesu anasema, mmea huo unanyauka “kwa sababu ya kutokuwa na kina cha udongo” na “kutokuwa na unyevunyevu.” (Mathayo 13:5, 6; Luka 8:6) “Tungamo-mwamba,” lililo chini ya udongo wa juu, linazuia mbegu hiyo isipenyeze mizizi vya kutosha na kupata unyevu na kuimarika. Mche huo unanyauka kwa sababu udongo huo hauna kina.

      13. Ni watu gani walio kama udongo usio na kina, na ni nini hasa ambacho hufanya waogope?

      13 Sehemu hii ya kielezi inahusu watu ambao “hulipokea lile neno kwa shangwe” na kumfuata Yesu kwa bidii “kwa majira.” (Luka 8:13) Wanapokabili “dhiki au mnyanyaso” mkali, wanaogopa sana hivi kwamba wanapoteza shangwe na nguvu na kuacha kumfuata Kristo. (Mathayo 13:21) Hata hivyo, sababu hasa inayofanya waogope si upinzani. Kwa kuwa kuna mamilioni ya wanafunzi wa Kristo wanaovumilia dhiki mbalimbali na bado wanadumu wakiwa waaminifu. (2 Wakorintho 2:4; 7:5) Sababu halisi inayofanya wengine waogope na kuacha kweli ni kwamba hali yao ya moyoni iliyo kama mwamba huwazuia wasitafakari vya kutosha mambo yanayofaa ya kiroho. Kwa hiyo, hawapendezwi kikweli na Yehova na neno lake na hivyo hawana nguvu za kuvumilia mnyanyaso. Mtu anawezaje kuepuka hali hiyo?

      14. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani ili kuzuia hali ya moyo wake isiwe kama udongo usio na kina?

      14 Mtu anapaswa kuhakikisha kwamba moyo wake hauna vizuizi vilivyo kama mwamba, kama vile kuweka kinyongo kwa muda mrefu, hali ya ubinafsi isiyo dhahiri, au hisia fulani zisizofaa. Ikiwa kuna vizuizi kama hivyo, nguvu za neno la Mungu zinaweza kuvivunja. (Yeremia 23:29; Waefeso 4:22; Waebrania 4:12) Baada ya hapo, kutafakari kwa sala kutachochea “kupandwa kwa neno” ndani kabisa ya moyo wa mtu. (Yakobo 1:21) Kufanya hivyo kutatokeza nguvu za kukabiliana na nyakati zenye kuvunja moyo na kutokeza ujasiri wa kudumisha uaminifu licha ya majaribu.

      “Katikati ya Miiba” Yamaanisha Kuwa na Moyo Nusu-nusu

      15. (a) Kwa nini tuzingatie aina ya tatu ya udongo iliyotajwa na Yesu? (b) Ni nini kinachotokea hatimaye kuhusiana na udongo wa aina ya tatu, na kwa nini?

      15 Tunapaswa kuzingatia aina ya tatu ya udongo, yaani udongo wenye miiba, kwa sababu unafanana kwa njia fulani na udongo mzuri. Mbegu iliyoanguka kwenye udongo wenye miiba inatoa mizizi na kuota sawa na ile inayoanguka kwenye udongo mzuri. Mwanzoni, hakuna tofauti katika ukuzi wa mmea mpya katika aina hizi mbili za udongo. Hata hivyo, baada ya muda hali fulani inatokea ambayo hatimaye inasonga mmea. Tofauti na udongo mzuri, udongo huu umejaa miiba. Mmea mchanga unapochipuka kutoka udongoni, unasongwa na ‘miiba inayokua pamoja nao.’ Kwa muda fulani mimea hiyo inapigania lishe, nuru, na nafasi, lakini hatimaye miiba inashinda mmea huo na ‘kuusonga.’—Luka 8:7.

      16. (a) Ni watu gani wanaofanana na udongo wenye miiba? (b) Kulingana na masimulizi ya vitabu vitatu vya Injili, miiba huwakilisha nini?—Ona kielezi-chini.

      16 Ni watu gani wanaofanana na udongo wenye miiba? Yesu anaeleza hivi: “Hawa ndio ambao wamesikia, lakini, kwa kuchukuliwa na mahangaiko na mali na raha za maisha haya, wao husongwa kabisa na hawakamilishi kitu.” (Luka 8:14) Kama vile mbegu za mpanzi na miiba inavyokua katika udongo kwa wakati uleule, ndivyo watu fulani hujaribu kujifunza neno la Mungu na wakati uleule kufuatia “raha za maisha haya.” Ukweli wa neno la Mungu hupandwa katika mioyo yao, lakini unakabili ushindani kutoka kwa mambo mengine wanayohitaji kuyashughulikia. Moyo wao wa mfano umegawanyika. (Luka 9:57-62) Hilo huwazuia wasiwe na wakati wa kutosha kutafakari neno la Mungu kwa sala na kwa njia inayofaa. Wanashindwa kuvama katika neno la Mungu na hivyo wanakosa kuonyesha uthamini unaohitajiwa ili kuvumilia. Hatua kwa hatua, ufuatiaji wa mambo ya kimwili huzuia na hata ‘husonga kabisa’ mambo ya kiroho.c Wale wasiompenda Yehova kwa moyo wote wanapatwa na matokeo ya kuhuzunisha kama nini!—Mathayo 6:24; 22:37.

      17. Tunapaswa kufanya maamuzi gani maishani ili tusisongwe na miiba ya mfano inayotajwa katika kielezi cha Yesu?

      17 Kwa kutanguliza mambo ya kiroho badala ya mambo ya kimwili, tunaepuka kusongwa na matatizo na raha za ulimwengu huu. (Mathayo 6:31-33; Luka 21:34-36) Hatupaswi kupuuza kusoma na kutafakari yale tunayosoma katika Biblia. Tutapata wakati zaidi wa kutafakari kwa makini na kwa sala tukifanya maisha yetu yawe sahili kadiri tuwezavyo. (1 Timotheo 6:6-8) Watumishi wa Mungu ambao kwa njia ya mfano wameng’oa miiba kutoka kwenye udongo ili mmea unaozaa matunda upate lishe, nuru na nafasi zaidi, wanabarikiwa na Yehova. Sandra mwenye umri wa miaka 26 anasema hivi: “Ninapotafakari baraka ambazo nimepata kwa kujifunza kweli, ninaona kwamba ulimwengu hauwezi kutoa kitu chochote kinacholingana na kweli!”—Zaburi 84:11.

      18. Tunawezaje kukaa katika neno la Mungu na kuvumilia tukiwa Wakristo?

      18 Bila shaka, sisi sote, wakubwa kwa wadogo, tutakaa katika neno la Mungu na kuvumilia tukiwa wanafunzi wa Kristo mradi tu neno la Mungu linakaa ndani yetu. Kwa hiyo, na tuhakikishe kwamba udongo wa moyo wetu wa mfano hautakuwa mgumu, usio na kina, au wenye miiba, bali utabaki ukiwa mwepesi na wenye kina. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kuvama katika neno la Mungu na “kuzaa matunda kwa uvumilivu.”—Luka 8:15.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika makala hii, tutazungumzia takwa la kwanza. Matakwa yale mengine mawili yatazungumziwa katika makala zinazofuata.

      b Kwa mfano, ili kutafakari kwa sala sehemu fulani uliyosoma katika Biblia, unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, sehemu hii inafunua sifa moja au sifa zaidi za Yehova? Inahusianaje na kichwa cha Biblia? Ninawezaje kuitumia maishani mwangu au kuitumia kuwasaidia wengine?’

      c Kulingana na masimulizi ya mfano wa Yesu katika vitabu vitatu vya Injili, mbegu inasongwa na matatizo na raha za ulimwengu huu: “Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo,” “nguvu za udanganyifu wa mali,” “tamaa za mambo yale mengine,” na “raha za maisha haya.”—Marko 4:19; Mathayo 13:22; Luka 8:14; Yeremia 4:3, 4.

  • ‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • ‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’

      “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.”—YOHANA 13:35.

      1. Yesu alikazia sifa gani muda mfupi tu kabla ya kifo chake?

      “WATOTO wadogo.” (Yohana 13:33) Kwa kutumia maneno hayo ya upendo, Yesu alizungumza na mitume wake usiku wa kuamkia kifo chake. Masimulizi ya Injili hayaonyeshi kwamba Yesu alikuwa amewahi kutumia maneno hayo ya upendo kuzungumza na mitume wake. Hata hivyo, usiku huo wa pekee, alichochewa kuzungumza nao kwa upendo ili kuwaonyesha wafuasi wake kwamba aliwapenda sana. Kwa kweli, Yesu alizungumza kuhusu upendo mara 30 hivi usiku huo. Kwa nini alikazia sana sifa hiyo?

      2. Kwa nini ni muhimu sana kwa Wakristo kuonyesha upendo?

      2 Yesu alieleza ni kwa nini upendo ni muhimu sana. “Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe,” akasema. (Yohana 13:35; 15:12, 17) Kuwa mfuasi wa Kristo huambatana sana na kuonyesha upendo wa kidugu. Wakristo wa kweli hutambuliwa kwa upendo mchangamfu wanaoonyeshana wala si mavazi ya aina fulani, au desturi fulani zisizo za kawaida. Upendo huo wa pekee ndio takwa la pili kati ya matakwa matatu ya kuwa mwanafunzi wa Kristo yaliyotajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia. Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kutimiza takwa hili?

      “Kufanya Hilo kwa Kipimo Chenye Kujaa Zaidi”

      3. Mtume Paulo alitoa onyo gani kuhusu upendo?

      3 Wanafunzi wa kweli wa Kristo leo huonyesha upendo huo wa pekee kama wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza hivi: “Kuhusu upendo wa kidugu, hamhitaji sisi tuwe tukiwaandikia nyinyi, kwa maana nyinyi wenyewe hufundishwa na Mungu kupendana; na, kwa kweli, nyinyi mnafanya hilo kwa ndugu wote.” Hata hivyo, Paulo aliongeza kusema hivi: “Mwendelee kufanya hilo kwa kipimo chenye kujaa zaidi.” (1 Wathesalonike 3:12; 4:9, 10) Sisi pia tunahitaji kutii onyo la Paulo na kujitahidi kuonyeshana upendo “kwa kipimo chenye kujaa zaidi.”

      4. Kulingana na Paulo na Yesu, tunapaswa kuwafikiria nani hasa?

      4 Katika barua hiyohiyo iliyoongozwa na roho ya Mungu, Paulo aliwatia moyo waamini wenzake ‘waseme kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo,’ na ‘kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) Pindi nyingine, aliwakumbusha Wakristo kwamba ‘wale walio na nguvu, wanapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu.’ (Waroma 15:1) Yesu pia alitoa maagizo kuhusu kuwasaidia walio dhaifu. Yesu alimwambia Petro hivi baada ya kutabiri kwamba Petro angemwacha usiku ambao angekamatwa: “Mara uwapo umerudi, watie nguvu ndugu zako.” Kwa nini? Kwa sababu wao pia wangekuwa wamemwacha Yesu na hivyo wangehitaji msaada. (Luka 22:32; Yohana 21:15-17) Kwa hiyo, Neno la Mungu hutuambia tuwaonyeshe upendo wale ambao ni dhaifu kiroho na ambao huenda hawashirikiani tena na kutaniko la Kikristo. (Waebrania 12:12) Kwa nini tufanye hivyo? Tunapata jibu kutokana na vielezi viwili dhahiri vilivyotolewa na Yesu.

      Kondoo Aliyepotea na Sarafu Iliyopotea

      5, 6. (a) Yesu alisimulia vielezi gani viwili vifupi? (b) Vielezi hivyo vinaonyesha nini kuhusu Yehova?

      5 Ili kuwafundisha wasikilizaji wake jinsi Yehova anavyowaona wale ambao wamepoteza mwelekeo, Yesu alisimulia vielezi viwili vifupi. Kielezi kimoja kilihusu mchungaji. Yesu alisema: “Ni mtu gani kati yenu mwenye kondoo mia, apotezapo mmoja wao, hataacha nyuma wale tisini na tisa nyikani na kwenda kumtafuta aliyepotea mpaka ampate? Na akiisha kumpata humweka juu ya mabega yake na kushangilia. Naye afikapo nyumbani huita marafiki wake na majirani wake pamoja, akiwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’ Mimi nawaambia nyinyi kwamba ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye kuliko juu ya waadilifu tisini na tisa wasio na uhitaji wa toba.”—Luka 15:4-7.

      6 Kielezi cha pili kilihusu mwanamke fulani. Yesu alisema: “Ni mwanamke gani mwenye sarafu za drakma kumi, ikiwa apoteza sarafu moja ya drakma, asiyewasha taa na kufagia nyumba yake na kutafuta kwa uangalifu mpaka aipate? Naye akiisha kuipata huwaita wanawake walio marafiki wake na majirani pamoja, akisema, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimeipata sarafu ya drakma niliyoipoteza.’ Hivyo, mimi nawaambia nyinyi, ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.”—Luka 15:8-10.

      7. Tunaweza kujifunza mambo gani mawili kutokana na kielezi cha kondoo aliyepotea na sarafu iliyopotea?

      7 Tunaweza kujifunza nini kutokana na vielezi hivyo vifupi? Vinatuonyesha (1) tunavyopaswa kuhisi kuelekea wale walio dhaifu na (2) mambo tunayopaswa kufanya ili kuwasaidia. Na tuchunguze mambo hayo.

      Kilipotea Lakini Kilithaminiwa

      8. (a) Mchungaji na mwanamke walihisije vitu vyao vilipopotea? (b) Tunajifunza nini kutokana na jinsi walivyohisi kuhusu vitu vilivyopotea?

      8 Katika vielezi vyote viwili, kitu fulani kilipotea, lakini ona jinsi wenye vitu hivyo walivyohisi. Mchungaji hakusema: ‘Kondoo mmoja ana faida gani, je, sina kondoo 99? Simhitaji kondoo huyo.’ Mwanamke huyo hakusema: ‘Kwa nini nihangaikie sarafu moja? Zile tisa nilizo nazo zanitosha.’ Badala ya kusema hivyo, mchungaji alimtafuta kondoo aliyepotea kana kwamba alikuwa na kondoo huyo mmoja tu. Naye mwanamke huyo aliona kwamba amepata hasara kwa kupoteza sarafu moja kana kwamba hakuwa na sarafu nyingine. Katika visa vyote viwili, wenye vitu hivyo vilivyopotea waliviona kuwa vyenye thamani. Tunajifunza nini?

      9. Ni nini kinachoonyeshwa na hangaiko la mchungaji na mwanamke?

      9 Ona jinsi Yesu alivyomalizia vielezi vyote viwili: “Ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye” na “ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.” Kwa hiyo, hangaiko lililoonyeshwa na mchungaji na mwanamke huyo linatufundisha kwa kiwango kidogo jinsi Yehova na viumbe wake walio mbinguni wanavyohisi. Kwa hiyo, wale ambao wamepoteza mwelekeo na kuacha kushirikiana na watu wa Mungu ni wenye thamani machoni pa Yehova kama vile vitu vilivyopotea vilivyokuwa na thamani kwa mchungaji na mwanamke. (Yeremia 31:3) Huenda watu hao wakawa dhaifu kiroho, lakini huenda wasiwe waasi. Licha ya udhaifu wao, huenda kwa kadiri fulani wakawa wanajitahidi kutimiza matakwa ya Yehova. (Zaburi 119:176; Matendo 15:29) Kwa hiyo, kama ilivyokuwa zamani, Yehova hafanyi haraka ‘kuwatupa usoni pake.’—2 Wafalme 13:23.

      10, 11. (a) Tungependa kuwaonaje wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko? (b) Kulingana na vielezi viwili vya Yesu, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali?

      10 Kama Yehova na Yesu, sisi pia tunawajali sana wale walio dhaifu na ambao hawashirikiani na kutaniko la Kikristo. (Ezekieli 34:16; Luka 19:10) Tunamwona mtu aliye dhaifu kiroho kama kondoo aliyepotea—si mtu asiyeweza kusaidiwa. Hatusemi: ‘Kwa nini tujishughulishe na mtu aliye dhaifu? Kutaniko linaendelea vizuri bila yeye.’ Badala yake, tunawaona wale ambao wameacha njia na wanaotaka kurudi kama Yehova anavyowaona—kuwa wenye thamani.

      11 Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali? Vielezi viwili vya Yesu vinaonyesha kwamba tunaweza kufanya hivyo (1) kwa kuonyesha kwamba tunapendezwa nao, (2) kwa kuwa wenye fadhili, na (3) kuwa wenye bidii. Na tuchunguze mambo hayo moja baada ya jingine.

      Pendezwa Nao

      12. Maneno ‘kwenda kumtafuta aliyepotea’ yanaonyesha nini kuhusu mtazamo wa mchungaji?

      12 Katika kielezi cha kwanza kati ya vielezi hivyo viwili, Yesu anasema kwamba mchungaji ‘atakwenda kumtafuta aliyepotea.’ Mchungaji anaonyesha upendezi na kujitahidi kutafuta kondoo aliyepotea. Mchungaji huyo hazuiwi na magumu, hatari, wala umbali. Badala yake anaendelea na jitihada yake “mpaka ampate.”—Luka 15:4.

      13. Wanaume wa kale wenye imani walichukua hatua gani kuelekea walio dhaifu, nasi tunawezaje kuiga mifano hiyo ya Biblia?

      13 Vivyo hivyo, ili kusaidia mtu anayehitaji kutiwa moyo mara nyingi mwenye nguvu anapaswa kuonyesha upendezi. Wanaume waaminifu wa kale walifahamu jambo hilo. Kwa mfano, Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli alipotambua kwamba rafiki yake wa chanda na pete, Daudi, alihitaji kutiwa moyo, Yonathani “akainuka akamwendea Daudi huko Horeshi, akamtia nguvu mkono wake katika Mungu.” (1 Samweli 23:15, 16) Karne kadhaa baadaye, Gavana Nehemia alipoona kwamba baadhi ya ndugu zake Wayahudi walikuwa wamevunjika moyo, yeye pia ‘mara moja alisimama’ na kuwatia moyo ‘wamkumbuke Yehova.’ (Nehemia 4:14, NW) Leo, sisi pia tungependa ‘kusimama—kuonyesha upendezi—kuimarisha walio dhaifu. Lakini ni nani wanaopaswa kufanya hivyo kutanikoni?

      14. Ni nani anayepaswa kusaidia walio dhaifu katika kutaniko la Kikristo?

      14 Wazee Wakristo hasa wana daraka la ‘kutia nguvu mikono iliyo dhaifu na kufanya imara magoti yaliyolegea’ na ‘kuwaambia walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope.’ (Isaya 35:3, 4; 1 Petro 5:1, 2) Hata hivyo, shauri la Paulo juu ya ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ na ‘kutegemeza walio dhaifu’ halikutolewa kwa wazee peke yao. Badala yake, maneno ya Paulo yalihusu ‘kutaniko lote la Wathesalonike.’ (1 Wathesalonike 1:1; 5:14) Kwa hiyo Wakristo wote wana daraka la kusaidia walio dhaifu. Kama yule mchungaji katika kielezi cha Yesu, kila Mkristo anapaswa kuchochewa “kwenda kumtafuta aliyepotea.” Bila shaka, tunaweza kutoa msaada huo kwa njia inayofaa kwa kushirikiana na wazee. Je, unaweza kufanya jambo fulani kusaidia mtu aliye dhaifu katika kutaniko lenu?

      Uwe Mwenye Fadhili

      15. Ni nini ambacho huenda kilifanya mchungaji atende jinsi alivyotenda?

      15 Mchungaji anafanya nini hatimaye anapompata kondoo aliyepotea? “Humweka juu ya mabega yake.” (Luka 15:5) Hiyo ni hatua muhimu na yenye kugusa hisia kama nini! Huenda kondoo huyo alitangatanga siku nyingi, usiku na mchana, katika eneo asilolijua, na labda akakabili hatari ya kunyemelewa na simba. (Ayubu 38:39, 40) Bila shaka kondoo huyo amedhoofika kwa sababu ya kukosa chakula. Kondoo huyo ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali anapokuwa njiani kurudi zizini. Kwa hiyo, mchungaji anainama, anamwinua kondoo kwa wororo, anambeba na kumrudisha zizini. Tunawezaje kuonyesha hangaiko kama la mchungaji huyo?

      16. Kwa nini tuwe na fadhili kama yule mchungaji mwenye kondoo aliyepotea?

      16 Huenda mtu ambaye ameacha kushirikiana na kutaniko akawa amechoka kiroho. Kama kondoo aliyetenganishwa na mchungaji, huenda mtu huyo alirandaranda bila kusudi katika ulimwengu huu wenye uadui. Bila ulinzi kutoka katika kundi, kutaniko la Kikristo, anakabili hatari kubwa sana ya kushambuliwa na Ibilisi, ambaye “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Isitoshe, amedhoofika kwa kukosa chakula cha kiroho. Kwa hiyo, bila kusaidiwa yaelekea yeye ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali akiwa safarini kurudi kutanikoni. Kwa hiyo, tunapaswa kuinama kwa njia ya mfano, kumwinua aliye dhaifu, na kumbeba hadi kutanikoni. (Wagalatia 6:2) Tunawezaje kufanya hivyo?

      17. Tunawezaje kumwiga mtume Paulo tunapomtembelea mtu aliye dhaifu?

      17 Mtume Paulo alisema: “Kama mtu yeyote ni dhaifu, nami pia ni dhaifu.” (2 Wakorintho 11:29, Biblia Habari Njema; 1 Wakorintho 9:22) Paulo aliwahurumia watu, kutia ndani walio dhaifu. Sisi pia tungependa kuwahurumia wale walio dhaifu. Unapomtembelea Mkristo aliye dhaifu kiroho, mhakikishie kwamba ana thamani machoni pa Yehova na kwamba Mashahidi wenzake wanamkosa sana. (1 Wathesalonike 2:17) Mjulishe kwamba Mashahidi wangependa kumtia moyo na wako tayari kuwa ‘ndugu aliyezaliwa siku ya taabu.’ (Mithali 17:17; Zaburi 34:18) Mazungumzo yetu machangamfu yanaweza kumtia moyo hatua kwa hatua na anaweza kurudi tena kwenye kundi. Tunapaswa kufanya nini baada ya hapo? Tunapata mwongozo kutokana na kielezi cha mwanamke na sarafu iliyopotea.

      Uwe Mwenye Bidii

      18. (a) Kwa nini mwanamke anayesimuliwa katika kielezi hakukata tamaa? (b) Mwanamke huyo alionyesha jitihada gani yenye bidii, na matokeo yakawaje?

      18 Mwanamke aliyepoteza sarafu anajua kwamba anakabili hali ngumu lakini hakati tamaa. Iwapo sarafu hiyo ingeanguka kichakani au kutumbukia ndani ya ziwa lenye tope, labda mwanamke huyo angekata tamaa kabisa. Hata hivyo, kwa kuwa anajua kwamba sarafu hiyo iko mahali fulani nyumbani mwake, ambapo anaweza kuipata, anaitafuta kwa makini na kwa bidii. (Luka 15:8) Kwanza, anawasha taa ili kuangaza nyumba. Kisha anafagia sakafu kwa ufagio akitumaini kusikia mlio fulani. Hatimaye, anapekua kwa bidii kila pembe na nyufa za nyumba hadi anapoona kitu chenye kumetameta. Mwanamke huyo anathawabishwa kwa sababu ya jitihada yake yenye bidii!

      19. Hatua zilizochukuliwa na mwanamke katika kielezi cha sarafu iliyopotea zinaweza kutufunza nini kuhusu kuwasaidia walio dhaifu?

      19 Habari hiyo inayohusu kielezi hicho, inatukumbusha kwamba sote tunaweza kutimiza daraka la Kimaandiko la kusaidia Mkristo aliye dhaifu. Wakati huohuo, tunatambua kwamba jitihada inahitajiwa. Kwa kweli, mtume Paulo aliwaambia wazee wa Efeso hivi: “Kwa kufanya kazi ya jasho hivyo ni lazima msaidie wale walio dhaifu.” (Matendo 20:35a) Kumbuka kwamba mwanamke huyo hatafuti sarafu hiyo nyumbani mwake pasipo mpango. La, anafaulu kwa sababu anaitafuta kwa makini “mpaka aipate.” Vivyo hivyo, tunapojitahidi kumsaidia mtu aliye dhaifu kiroho, tunahitaji tuwe na bidii na kusudi. Tunaweza kufanya nini?

      20. Walio dhaifu wanaweza kusaidiwaje?

      20 Tunawezaje kumsaidia mtu aliye dhaifu awe na imani na shukrani? Huenda ikatubidi kujifunza Biblia pamoja naye tukitumia kichapo kinachofaa cha Kikristo. Kwa kweli, kujifunza Biblia pamoja na mtu aliye dhaifu hutuwezesha kumsaidia hatua kwa hatua na kikamilifu. Huenda mwangalizi wa utumishi akaamua ni nani anayeweza kutoa msaada unaohitajiwa. Anaweza kupendekeza habari ambazo mtu huyo anaweza kujifunza na ni kichapo gani kinachofaa zaidi. Kama yule mwanamke anayetajwa katika kielezi anavyotumia vifaa vinavyofaa ili kutimiza kazi yake, sisi leo tuna vifaa vinavyotusaidia kutimiza kazi tuliyopewa na Mungu ya kusaidia walio dhaifu. Vichapo vipya tulivyopata hivi karibuni vitatusaidia sana kutimiza kazi hiyo. Vitabu hivyo ni, Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli na Mkaribie Yehova.a

      21. Kusaidia walio dhaifu huletaje baraka kwa wote?

      21 Kusaidia walio dhaifu huleta baraka kwa wote. Mtu anayesaidiwa hupata furaha ya kuungana tena na marafiki wa kweli. Tunapata furaha ya kweli ambayo hutokana tu na kutoa. (Luka 15:6, 9; Matendo 20:35b) Kutaniko lote huwa na uchangamfu kila mshiriki anapopendezwa na wengine. Zaidi ya yote, Wachungaji wetu wanaojali, Yehova na Yesu, hupata sifa watumishi wao walio duniani wanapoiga nia ya kusaidia walio dhaifu. (Zaburi 72:12-14; Mathayo 11:28-30; 1 Wakorintho 11:1; Waefeso 5:1) Kwa hiyo, tuna sababu nzuri kama nini ya kuendelea ‘kuwa na upendo miongoni mwetu’!

  • ‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • ‘Fulizeni Kuzaa Matunda Mengi’

      “Mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu.”—YOHANA 15:8.

      1. (a) Yesu aliwatajia mitume wake takwa gani la kuwa mwanafunzi? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

      ULIKUWA usiku wa kuamkia kifo chake. Yesu alikuwa ametumia muda wa kutosha kuwatia moyo mitume wake kwa kuzungumza nao waziwazi. Kufikia sasa, yaonekana ilikuwa baada ya saa sita usiku, lakini Yesu aliendelea kuzungumza na hao rafiki zake wa karibu kwa sababu aliwapenda. Kisha, alipokuwa akizungumza nao, aliwakumbusha takwa jingine walilopaswa kutimiza ili kuendelea kuwa wanafunzi wake. Alisema: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu.” (Yohana 15:8) Je, leo sisi tunatimiza sifa hiyo ya kuwa wanafunzi? Inamaanisha nini kuwa wenye “kuzaa matunda mengi”? Ili kupata jibu, na tuchunguze mazungumzo ya Yesu jioni hiyo.

      2. Yesu asimulia kielezi gani kuhusu matunda jioni kabla ya kifo chake?

      2 Shauri la kuzaa matunda limetajwa katika kielezi kimoja ambacho Yesu alisimulia mitume wake. Alisema: “Mimi ndio mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mlimaji. Kila tawi katika mimi lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali, na kila linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi. Tayari nyinyi ni safi kwa sababu ya neno ambalo nimewaambia. Kaeni katika muungano nami, na mimi katika muungano nanyi. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa matunda likiwa pekee isipokuwa likae katika mzabibu, katika njia hiyohiyo wala nyinyi hamwezi, isipokuwa mkae katika muungano nami. Mimi ndio mzabibu, nyinyi ndiyo matawi. . . . Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu. Kama vile Baba amenipenda mimi nami nimewapenda nyinyi, kaeni katika upendo wangu. Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu.”—Yohana 15:1-10.

      3. Wafuasi wa Yesu wanapaswa kufanya nini ili kuzaa matunda?

      3 Katika kielezi hicho, Yehova ndiye Mlimaji, Yesu ndiye mzabibu, nao mitume ambao Yesu alikuwa akizungumza nao ndio matawi. Mitume wangezaa matunda maadamu wangejitahidi ‘kukaa katika muungano’ na Yesu. Kisha Yesu alieleza jinsi ambavyo mitume hao wangefaulu kudumisha muungano huo muhimu: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu.” Baadaye, mtume Yohana aliandika maneno kama hayo kwa Wakristo wenzake: “Yeye ambaye hushika amri [za Kristo] hukaa katika muungano na yeye.”a (1 Yohana 2:24; 3:24) Kwa hiyo, kwa kushika amri za Kristo, wafuasi wake hukaa katika muungano naye, na muungano huo huwawezesha kuzaa matunda. Tunapaswa kuzaa matunda ya aina gani?

      Fursa ya Kukua

      4. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uhakika wa kwamba Yehova “huliondolea mbali” kila tawi lisilozaa matunda?

      4 Katika kielezi cha mzabibu, Yehova “huliondolea mbali,” tawi lisipozaa matunda. Jambo hilo linatufunza nini? Linatufunza kwamba wanafunzi wote wanatakiwa wazae matunda kwa kuwa wanaweza kufanya hivyo licha ya hali zao na udhaifu wao. Kwa kweli, ingekuwa kinyume cha njia za upendo za Yehova ‘kuondolea mbali,’ mwanafunzi wa Kristo kwa sababu ya kushindwa kutimiza jambo linalozidi uwezo wake.—Zaburi 103:14; Wakolosai 3:23; 1 Yohana 5:3.

      5. (a) Kielezi cha Yesu kinaonyeshaje kwamba tunaweza kufanya maendeleo katika kuzaa matunda? (b) Tutazungumzia aina gani mbili za matunda?

      5 Pia kielezi cha Yesu cha mzabibu kinaonyesha kwamba chini ya hali zetu, tunapaswa kutafuta fursa za kufanya maendeleo katika utendaji wetu tukiwa wanafunzi. Ona jinsi Yesu anavyosema: “Kila tawi katika mimi lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali, na kila linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yohana 15:2) Akimalizia kielezi hicho, Yesu aliwahimiza wafuasi wake wazae “matunda mengi.” (Mstari wa 8) Hilo linamaanisha nini? Tukiwa wanafunzi, hatupaswi kuridhika tu na yale ambayo tumetimiza. (Ufunuo 3:14, 15, 19) Badala yake, tunapaswa kutafuta njia za kuendelea kuzaa matunda. Tunapaswa kujitahidi kuzaa kwa wingi matunda ya aina gani? Kuna aina mbili (1) “matunda ya roho” na (2) matunda ya Ufalme.—Wagalatia 5:22, 23; Mathayo 24:14.

      Matunda ya Sifa za Kikristo

      6. Yesu Kristo alikaziaje umuhimu wa kuonyesha tunda la kwanza la roho?

      6 Sifa ya kwanza inayotajwa kati ya “matunda ya roho” ni upendo. Roho takatifu ya Mungu huwawezesha Wakristo waonyeshe upendo kwa kuwa wanatii amri ambayo Yesu alitoa muda mfupi kabla ya kusimulia kielezi cha mzabibu unaozaa matunda. Aliwaambia mitume wake hivi: “Ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane.” (Yohana 13:34) Kwa kweli, alipokuwa akizungumza na mitume wake usiku huo wa mwisho duniani, Yesu aliwakumbusha tena na tena kuhusu uhitaji wa kuonyesha upendo.—Yohana 14:15, 21, 23, 24; 15:12, 13, 17.

      7. Mtume Petro alionyeshaje kwamba kuzaa matunda kunahusiana na kuonyesha sifa kama za Kristo?

      7 Petro aliyekuwako usiku huo, alifahamu kwamba wanafunzi wa kweli wa Kristo wanapaswa kuonyesha upendo kama wa Kristo na sifa nyingine zinazohusiana na upendo. Miaka kadhaa baadaye, Petro aliwatia moyo Wakristo wasitawishe sifa kama vile kujidhibiti, shauku ya kidugu, na upendo. Aliongeza kusema kwamba kufanya hivyo hutuzuia “kuwa ama wasiotenda ama wasiozaa matunda.” (2 Petro 1:5-8) Hata hali zetu ziweje, tunaweza kuonyesha matunda ya roho. Hivyo basi, na tujitahidi kuonyesha upendo, fadhili, upole, na sifa nyingine za Kikristo kwa kiwango kikubwa zaidi kwa kuwa “dhidi ya mambo ya namna hiyo hakuna sheria,” wala kikomo. (Wagalatia 5:23) Naam, na tuzae “matunda zaidi.”

      Kuzaa Matunda ya Ufalme

      8. (a) Kuna uhusiano gani kati ya matunda ya roho na matunda ya Ufalme? (b) Tunapaswa kufikiria swali gani?

      8 Matunda yenye kupendeza na yenye ladha nzuri huupamba mti. Hata hivyo, matunda hayo yana manufaa zaidi ya kupamba mti. Pia matunda ni muhimu kwa kuwa hueneza mbegu na kuzidisha idadi ya miti. Vivyo hivyo, matunda ya roho hufanya mengi zaidi ya kupamba utu wetu wa Kikristo. Sifa kama vile upendo na imani hutuchochea kueneza ujumbe wa Ufalme ulio kama mbegu ambayo hupatikana katika Neno la Mungu. Ona jinsi mtume Paulo anavyokazia uhusiano muhimu uliopo kati ya matunda ya roho na matunda ya Ufalme. Anasema: “Sisi pia hudhihirisha imani [sehemu ya matunda ya roho] na kwa hiyo twasema.” (2 Wakorintho 4:13) Kwa kufanya hivyo, Paulo anazidi kueleza kwamba ‘tunamtolea Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo’—tunda la pili tunalohitaji kuonyesha. (Waebrania 13:15) Je, tuna fursa maishani mwetu za kuzaa “matunda zaidi,” tukiwa watangazaji wa Ufalme wa Mungu?

      9. Je, kuzaa matunda ni kufanya wanafunzi? Eleza.

      9 Ili tujibu kwa usahihi, kwanza tunahitaji kuelewa kinachomaanishwa na matunda ya Ufalme. Je, ni sahihi kusema kwamba kuzaa matunda kunamaanisha kufanya wanafunzi? (Mathayo 28:19) Je, matunda tunayozaa ni watu tunaowasaidia kuwa waabudu waliobatizwa wa Yehova? La. Ikiwa ingekuwa hivyo, jambo hilo lingewavunja moyo sana Mashahidi wenzetu wapendwa ambao kwa miaka mingi wametangaza ujumbe wa Ufalme kwa uaminifu katika maeneo yasiyo na matokeo sana. Naam, ikiwa matunda ya Ufalme tunayozaa yanawakilishwa tu na wanafunzi wapya, Mashahidi hao wanaofanya kazi kwa bidii wangekuwa kama matawi yasiyozaa katika kielezi cha Yesu! Bila shaka, hivyo sivyo ilivyo. Hivyo, basi matunda ya Ufalme ya huduma yetu ni nini hasa?

      Kuzaa Matunda kwa Kueneza Mbegu ya Ufalme

      10. Kielezi cha Yesu cha mpanzi na aina mbalimbali za udongo kinaonyeshaje matunda ya Ufalme?

      10 Tunapata jibu katika kielezi cha Yesu cha mpanzi na aina mbalimbali za udongo. Jibu hilo linawatia moyo Mashahidi wanaohubiri maeneo yasiyo na matokeo sana. Yesu alisema kwamba mbegu ni ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu, na kwamba udongo ni moyo wa mfano. Baadhi ya mbegu ‘zilianguka juu ya udongo mzuri, na, baada ya kuota, zikatokeza matunda.’ (Luka 8:8) Matunda gani? Baada ya bua la ngano kuota na kukomaa, linazaa matunda, yaani mbegu mpya, wala halizai mabua madogo ya ngano. Vivyo hivyo, matunda ambayo Mkristo hutokeza si lazima yawe ni wanafunzi wapya, bali ni mbegu mpya ya Ufalme.

      11. Matunda ya Ufalme yanaweza kufasiriwaje?

      11 Kwa hiyo, matunda si wanafunzi wapya wala sifa nzuri za Kikristo. Kwa kuwa mbegu inayopandwa ni neno la Ufalme, basi matunda ni mbegu zaidi za ufalme. Kwa habari hii, kuzaa matunda kunamaanisha kuzungumza juu ya Ufalme huo. (Mathayo 24:14) Je, sote tunaweza kuzaa matunda hayo ya Ufalme, yaani, kutangaza habari njema ya Ufalme hata hali zetu ziweje? Ndiyo! Katika kielezi hichohicho, Yesu anaeleza sababu.

      Kutoa Yaliyo Bora ili Kumtukuza Mungu

      12. Je, Wakristo wote wanaweza kuzaa matunda ya Ufalme? Eleza.

      12 ‘Kwa habari ya yule aliyepandwa juu ya udongo ulio bora, hutokeza, huyu mara mia, yule sitini, yule mwingine thelathini.’ (Mathayo 13:23) Huenda nafaka zilizopandwa shambani zisitokeze kiasi kilekile cha mazao ikitegemea hali. Vivyo hivyo, kwa sababu ya hali huenda yale tunayoweza kutimiza katika kutangaza habari njema yasilingane na ya wengine, na Yesu alionyesha kwamba anatambua jambo hilo. Huenda wengine wakawa na fursa zaidi, wengine wakawa na afya bora na nguvu zaidi. Hivyo, huenda tukafanya mengi au machache kuliko wengine. Hata hivyo, Yehova anafurahi iwapo tunatoa yaliyo bora zaidi. (Wagalatia 6:4) Hata ikiwa uzee au ugonjwa unaodhoofisha unatuzuia tusishiriki sana kazi ya kuhubiri, Yehova, Baba yetu mwenye huruma hutuhesabu miongoni mwa wale ‘wanaofuliza kuzaa matunda mengi.’ Kwa nini? Kwa sababu tunampa ‘vyote tulivyo navyo’—utumishi wa nafsi yote.b—Marko 12:43, 44; Luka 10:27.

      13. (a) Ni sababu gani kuu zaidi inayofanya ‘tuendelee na kufuliza’ kuzaa matunda ya Ufalme? (b) Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kuzaa matunda katika maeneo yasiyo na matokeo sana? (Ona sanduku katika ukurasa wa 21.)

      13 Hata tuwe tunazaa matunda ya Ufalme kadiri gani, tutachochewa ‘tuendelee na kufuliza kuzaa matunda’ tunapokumbuka sababu ya kufanya hivyo. (Yohana 15:16) Yesu alitaja sababu kuu zaidi: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi.” (Yohana 15:8) Naam, kazi yetu ya kuhubiri hulitukuza jina la Yehova mbele ya watu wote. (Zaburi 109:30) Honor, Shahidi mwaminifu mwenye umri wa miaka 70 na kitu anasema: “Ni pendeleo kumwakilisha Aliye Juu Zaidi Sana, hata katika maeneo yasiyo na matokeo sana.” Wakati Claudio, Shahidi mwenye bidii tangu 1974, alipoulizwa kwa nini anaendelea kuhubiri hata ingawa ni wachache wanaoitikia katika eneo lao, alinukuu Yohana 4:34, ambapo tunasoma maneno haya ya Yesu: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.” Claudio aliongeza kusema: “Kama Yesu, ningependa kuanza na pia kumaliza kazi yangu ya kutangaza Ufalme.” (Yohana 17:4) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanakubaliana naye.—Ona sanduku “Jinsi ya ‘Kuzaa Matunda kwa Uvumilivu,’” katika ukurasa wa 21.

      Kuhubiri na Kufundisha

      14. (a) Kazi ya Yohana Mbatizaji na ya Yesu ilikuwa na makusudi gani mawili? (b) Ungeelezaje utendaji wa Kikristo leo?

      14 Yohana Mbatizaji ndiye mtangazaji wa kwanza wa Ufalme anayetajwa katika vitabu vya Injili. (Mathayo 3:1, 2; Luka 3:18) Kusudi lake kuu lilikuwa ‘kutoa ushahidi,’ naye alifanya hivyo kwa imani kubwa na kwa tumaini kwamba “watu wa namna zote wapate kuamini.” (Yohana 1:6, 7) Kwa kweli, baadhi ya watu waliohubiriwa na Yohana walikuja kuwa wanafunzi wa Kristo. (Yohana 1:35-37) Kwa hiyo, Yohana alihubiri na vilevile kufanya wanafunzi. Yesu pia alikuwa mhubiri na mwalimu. (Mathayo 4:23; 11:1) Kwa hiyo haishangazi kwamba Yesu aliwaamuru wafuasi wake wahubiri ujumbe wa Ufalme na pia wawasaidie watu wanaokubali ujumbe huo kuwa wanafunzi wake. (Mathayo 28:19, 20) Kwa hiyo kazi yetu leo inatia ndani kuhubiri na kufundisha.

      15. Kuna ufanani gani kati ya namna watu wanavyoitikia habari njema sasa na walivyoitikia katika karne ya kwanza W.K.?

      15 Kati ya watu waliomsikia Paulo akihubiri na kufundisha katika karne ya kwanza W.K., ‘wengine walianza kuamini mambo yaliyosemwa na wengine wakawa hawaamini.’ (Matendo 28:24) Leo, watu wanaitikia vivyo hivyo. Kwa kusikitisha, mbegu nyingi za Ufalme huanguka katika udongo usiofaa. Hata hivyo, mbegu nyingine bado huanguka kwenye udongo mzuri, hutoa mizizi, na kuota, kama Yesu alivyotabiri. Kwa kweli, ulimwenguni pote, kwa wastani watu zaidi ya 5,000 huwa wanafunzi wa kweli wa Kristo kila juma! Wanafunzi hao wapya ‘huamini mambo yaliyosemwa,’ ijapokuwa watu wengine wengi hawaamini. Ni nini kilichofanya mioyo yao ipokee ujumbe wa Ufalme? Mara nyingi ni upendezi walioonyeshwa na Mashahidi. Mashahidi walipata matokeo mazuri kwa kutia maji mbegu mpya kwa njia ya mfano. (1 Wakorintho 3:6) Fikiria mifano miwili tu kati ya mifano mingi.

      Kupendezwa Kibinafsi na Watu Huwa na Matokeo Mazuri

      16, 17. Kwa nini ni muhimu tupendezwe na watu tunaokutana nao katika huduma?

      16 Karolien, Shahidi mchanga anayeishi Ubelgiji, alimtembelea mwanamke mzee ambaye hakupendezwa na ujumbe wa Ufalme. Kwa kuwa mwanamke huyo alikuwa amefungwa bendeji mkononi, Karolien na mwenzake walitaka kumsaidia, lakini mwanamke huyo akakataa. Siku mbili baadaye Mashahidi hao walirudi nyumbani kwa mwanamke huyo ili kumjulia hali. “Kukawa na matokeo mazuri,” akasema Karolien. “Alishangaa kuona kwamba tulipendezwa naye kikweli. Alitualika nyumbani kwake, na tukaanza kujifunza Biblia pamoja naye.”

      17 Sandi, Shahidi anayeishi Marekani, pia hupendezwa na watu anaowahubiria. Yeye hutazama matangazo ya kuzaliwa kwa watoto katika gazeti moja la kwao na kuwatembelea wazazi waliojifungua hivi karibuni akiwa na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.c Kwa kuwa akina mama waliojifungua huwa nyumbani na hupenda kuwaonyesha wageni mtoto wao mchanga, mara nyingi mazungumzo huanzia hapo. “Mimi huzungumza na wazazi kuhusu umuhimu wa kuwa na uhusiano wa karibu na mtoto wao mchanga kupitia kusoma,” asema Sandi. “Baadaye ninazungumzia magumu ya kulea watoto katika ulimwengu wa sasa.” Hivi karibuni, baada ya kumtembelea mama mmoja, yeye na watoto wake sita walianza kumtumikia Yehova. Tunaweza kufurahia matokeo mazuri katika huduma yetu kwa kuchukua hatua ya kwanza na kupendezwa kibinafsi na watu.

      18. (a) Kwa nini sisi sote tunaweza kutimiza takwa la “kuzaa matunda mengi”? (b) Ni matakwa gani matatu ya kuwa mwanafunzi yanayotajwa katika Injili ya Yohana ambayo umeazimia kutimiza?

      18 Inatia moyo kama nini kujua kwamba tunaweza kutimiza takwa la ‘kufuliza kuzaa matunda mengi’! Iwe tu wachanga au wazee, tuna afya nzuri au mbaya, tunahubiri maeneo yenye matokeo au yasiyo na matokeo sana, sote tunaweza kuzaa matunda mengi. Jinsi gani? Kwa kuonyesha matunda ya roho kwa kadiri kubwa zaidi na kwa kueneza ujumbe wa Ufalme wa Mungu kwa kadiri tuwezavyo. Wakati huohuo, tunajitahidi ‘kukaa katika neno la Yesu’ na ‘kuwa na upendo miongoni mwetu.’ Naam, kwa kutimiza matakwa hayo matatu muhimu ya kuwa mwanafunzi ambayo yametajwa katika Injili ya Yohana, tunathibitisha kwamba sisi ‘kwa kweli sisi ni wanafunzi wa Kristo.’—Yohana 8:31; 13:35.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa matawi ya mzabibu katika kielezi hicho yanawakilisha mitume wa Yesu na Wakristo wengine watakaorithi Ufalme wa kimbingu wa Mungu, kielezi hicho kina kweli zinazoweza kuwanufaisha wafuasi wa Kristo leo.—Yohana 3:16; 10:16.

      b Wale ambao hawawezi kutoka nyumbani mwao kwa sababu ya uzee au ugonjwa wanaweza kutoa ushahidi kwa kuandika barua, au inapowezekana wanaweza kutumia simu, au labda kuwahubiria watu wanaokuja kuwatembelea.

      c Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki