-
Kutendewa Kama Mtu Asiye na MaanaAmkeni!—2009 | Agosti
-
-
Kutendewa Kama Mtu Asiye na Maana
“Katika mwaka wangu wa kwanza katika shule ya msingi nchini Hispania watoto wengine darasani walinibandika majina kwa sababu nilikuwa mfupi sana. Kila siku nilikuwa nikienda nyumbani nikilia.”—Jennifer, binti ya wahamiaji Wafilipino.
“Nilipohamia shule mpya, wanafunzi wenzangu wazungu waliniita majina ya kunishushia heshima. Nilijua walitaka nipigane nao. Hata hivyo, nilijidhibiti lakini nilihisi vibaya na kwamba sifai.”—Timothy, Mmarekani mwenye asili ya Kiafrika.
“Nilipokuwa na umri wa miaka saba, Waigbo na Wahausa nchini Nigeria walikosana. Chuki yao iliniathiri, na nikaanza kumdhihaki mvulana darasani mwetu ambaye ni Mhausa, ingawa mbeleni tulikuwa marafiki wakubwa.”—John, wa kabila la Igbo.
“Mimi na mmishonari mwenzangu tulikuwa tukiwahubiria majirani ujumbe wa Biblia wakati watoto waliochochewa na viongozi wa kidini wa eneo hilo walipoanza kutufuata na kututupia mawe. Viongozi wa kidini walitaka tuondoke.”—Olga.
JE, UMEWAHI kushushiwa heshima kwa kubaguliwa isivyo haki? Huenda ilikuwa kwa sababu ya rangi, dini, hali ya kiuchumi, jinsia, au umri wako. Wale ambao hubaguliwa kwa ukawaida wanaishi wakiogopa kutendewa vibaya hata zaidi. Huenda wakashikwa na wasiwasi mwingi sana wanapotembea mahali palipo na kikundi fulani cha watu, wanapoingia ndani ya duka, wanapohamia shule mpya, au wanapoalikwa kwenye sherehe fulani.
Isitoshe, watu wanapochukiwa na kubaguliwa inaweza kuwa vigumu kupata kazi, au wapate matibabu na masomo ya hali ya chini, au wanyimwe huduma au haki wanazopewa raia wengine. Wenye mamlaka wanapounga mkono ubaguzi, mambo mabaya kama vile mauaji ya kikabila na maangamizi ya jamii nzimanzima yanaweza kutokea. Mfano mmoja wa kale wa jaribio la kuangamiza jamii nzima unapatikana katika kitabu cha Biblia cha Esta. Ona jinsi chuki na ubaguzi zilivyochangia jambo hilo.—Esta 3:5, 6.
Ubaguzi na chuki unaweza kuendelezwa hata katika maeneo ambako kuna sheria zinazoupinga. Aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa anasema hivi: “Miaka 60 baada ya Azimio la Haki za Kibinadamu kwa Wote . . . , bado ulimwengu haujawa na usawa na watu hawajaacha kuwa na ubaguzi.” Hilo ni jambo la kusikitisha, kwa kuwa wahamiaji na wakimbizi wameongezeka na kubadili sana idadi ya watu katika nchi nyingi.
Je, kweli inawezekana kuwa na jamii yenye usawa? Au je, ubaguzi unaweza kumalizwa? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.
-
-
Chuki na Ubaguzi—Kufichua Mizizi YakeAmkeni!—2009 | Agosti
-
-
Chuki na Ubaguzi—Kufichua Mizizi Yake
“Wanadamu wote wanazaliwa wakiwa huru na sawa katika adhama na haki. Wamejaliwa uwezo wa kusababu na dhamiri pia, nao wapaswa kutendeana kwa roho ya udugu.”—Kifungo cha 1 cha Azimio la Haki za Kibinadamu kwa Wote.
LICHA ya malengo hayo mazuri, bado chuki na ubaguzi unaendelea kuwakumba wanadamu. Hali hiyo yenye kusikitisha inaonyesha mambo yanayotukia sasa na pia hali ya kutokamilika kwa wanadamu. (Zaburi 51:5) Lakini kuna matumaini. Ni kweli kwamba huenda tusiweze kuondoa ubaguzi kutoka kwa watu wengine, lakini sisi wenyewe tunaweza kujitahidi kuondoa mawazo yoyote ya ubaguzi yaliyo mioyoni mwetu.
Jambo la kwanza tunalopaswa kujua ni kwamba sote tunaweza kuonyesha ubaguzi. Kitabu Understanding Prejudice and Discrimination kinasema hivi: “Huenda mambo muhimu zaidi ambayo tumejifunza katika utafiti kuhusu ubaguzi ni haya: (1) kila mwanadamu aliye na uwezo wa kufikiri na kusema anaweza kuwa na ubaguzi, (2) kwa kawaida lazima mtu atambue anaweza kuonyesha ubaguzi na ajitahidi sana ili asifanye hivyo, na (3) mtu akichochewa inavyofaa anaweza kufaulu.”
Imesemwa kwamba “njia bora zaidi” ya kukabiliana na ubaguzi ni kuwaelimisha watu. Kwa mfano, elimu inayofaa inaweza kufichua mizizi ya ubaguzi, kutuwezesha tuchunguze mitazamo yetu vizuri zaidi, na kutusaidia kutenda kwa hekima tunapobaguliwa.
Kufichua Mizizi
Ubaguzi huwafanya watu wapotoshe, waelewe vibaya, au wapuuze mambo hakika yanayopingana na maoni yao. Lakini chanzo cha ubaguzi ni nini? Mtu anapochunguza kwa uangalifu, anaweza kugundua kwamba huenda ubaguzi ukatokana na viwango vya familia vilivyopotoshwa lakini vinavyoonekana kuwa sawa, au unaweza kupandwa na watu wanaoendeleza maoni yasiyofaa kuhusu watu wa jamii au utamaduni mwingine. Ubaguzi unaweza kuchochewa pia na utaifa na mafundisho ya dini za uwongo. Unaweza kutokezwa na kiburi. Unapofikiria mambo yafuatayo na kanuni zinazofaa za Biblia, mbona usichunguze mitazamo yako mwenyewe na uone ikiwa unahitaji kufanya mabadiliko?
Marafiki. Kwa kawaida, wanadamu wanapenda kushirikiana na wengine na hilo ni jambo zuri. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba “mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe” na hata atashindana na hekima inayotumika. (Methali 18:1) Hata hivyo, tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima kwa kuwa wanaweza kuwa na uvutano mkubwa kwetu. Kwa hiyo, wazazi wenye hekima wanapendezwa sana kujua marafiki wa watoto wao. Uchunguzi umeonyesha kwamba hata watoto wenye umri wa miaka mitatu wanaweza kuwa na ubaguzi wa rangi, kwa sababu ya mtazamo, maneno, na mambo ambayo wengine wanafanya. Bila shaka, wazazi wanapaswa kufanya yote wanayoweza ili wawe na uvutano mzuri kwa watoto wao, kwa kuwa wazazi ndio huchangia sehemu kubwa katika ukuzi wa mtoto.
◼ Biblia inasema nini? “Mfunze mtoto namna ya kuishi vizuri, naye hatasahau njia hiyo hata uzeeni.” (Methali 22:6, Biblia Habari Njema) “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Ikiwa wewe ni mzazi, jiulize hivi: ‘Je, ninawaelekeza watoto wangu katika njia ya kweli na iliyo sawa machoni pa Mungu? Je, ninashirikiana na watu walio na uvutano mzuri kwangu? Je, nina uvutano mzuri kwa wengine?’—Methali 2:1-9.
Uzalendo. Kamusi moja inafafanua uzalendo kuwa “kutukuza taifa moja juu ya mataifa mengine yote na kusisitiza kuendelezwa kwa utamaduni wake na mapendezi ya taifa hilo badala ya yale mataifa mengine.” Ivo Duchacek, profesa wa siasa, alisema hivi katika kitabu chake Conflict and Cooperation Among Nations: “Uzalendo hugawanya wanadamu katika visehemu visivyoweza kuvumiliana. Kwa sababu hiyo, watu hujiona kuwa Wamarekani, Warusi, Wachina, Wamisri, Waperu, au watu wa taifa lingine, kisha wanajiona kuwa wanadamu—ikiwa kwa vyovyote wao hujifikiria hivyo.” Aliyekuwa katibu mkuu wa UM aliandika hivi: “Matatizo mengi tunayokabili leo ni kwa sababu ya, au yanatokana na mitazamo isiyofaa ambayo tumesitawisha, mengine bila kujua. Mawazo hayo yanatia ndani wazo la kwamba ‘nitaitetea nchi yangu iwe imekosea au la.’”
◼ Biblia inasema nini? “Mungu aliupenda ulimwengu [wanadamu wote] sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Jiulize hivi, ‘Ikiwa Mungu anawapenda bila ubaguzi watu wa mataifa yote kutia ndani mimi, je, sipaswi kumwiga, hasa ikiwa ninadai kwamba ninamwabudu?’
Ubaguzi wa rangi. Watu wenye ubaguzi wa rangi wanaamini “kwamba rangi ya mtu inaamua tabia au uwezo wake na kwamba watu wa rangi fulani ni bora kuliko wengine,” inasema kamusi moja. Hata hivyo, kulingana na The World Book Encyclopedia, watafiti “hawajagundua msingi wowote wa kisayansi wa kuthibitisha madai kama hayo kwamba [watu wa rangi fulani] ni bora kuliko wengine.” Ukosefu mkubwa sana wa haki unaochochewa na ubaguzi wa rangi, kama vile kuwanyima wanadamu wenzao haki zao, ni uthibitisho wenye kusikitisha kwamba ubaguzi wa rangi unatokana na maoni ya uwongo.
◼ Biblia inasema nini? “Kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Matendo 17:26) “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Jiulize hivi: ‘Je, mimi hujaribu kuwaona wanadamu wote kama Mungu anavyowaona? Je, mimi hujaribu kuwaelewa na kuwafahamu kabisa watu wa rangi au utamaduni mwingine?’ Tunapowafahamu watu vizuri, inakuwa rahisi zaidi kuwa na maoni yanayofaa kuwahusu.
Dini. Kitabu The Nature of Prejudice kinasema: “Chuki hutokea watu wanapotumia dini yao kutetea [ubinafsi] na mapendezi ya kikabila. Hapo ndipo dini na ubaguzi hupatana.” Kitabu hichohicho kinasema kwamba jambo linaloshangaza zaidi ni jinsi watu wengi wanaodai kufuata dini “wanavyopoteza sifa zao za kiroho kwa urahisi na kuwa na ubaguzi.” Jambo hilo linaonekana wazi katika dini za watu wa rangi moja, chuki na jeuri kati ya vikundi vya kidini, na ugaidi unaochochewa na dini.
◼ Biblia inasema nini? “Hekima inayotoka juu [kwa Mungu] . . . ni . . . yenye kufanya amani, yenye usawaziko, . . . haifanyi tofauti zenye ubaguzi.” (Yakobo 3:17) “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli.” (Yohana 4:23) ‘Wapendeni adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.’ (Mathayo 5:44) Jiulize hivi: ‘Je, dini yangu inanichochea kuwapenda watu wote kikweli, kutia ndani hata wale ambao huenda wakataka kuniumiza? Je, dini yangu inamkaribisha kila mtu bila kujali taifa, rangi, jinsia, hali yake ya kiuchumi, au ya kijamii?’
Kiburi. Mtu anapoanza kujivuna au kujiona kuwa mtu wa maana kupita kiasi, kiburi kinaweza kumfanya aanze kuonyesha ubaguzi. Kwa mfano, kiburi kinaweza kumfanya mtu ajione kuwa bora kuliko wengine au awadharau watu ambao hawana elimu kama yake au walio maskini. Huenda pia kikamfanya aamini propaganda zinazotukuza taifa au kabila lake. Watu walio na ustadi wa kueneza propaganda kama vile dikteta wa Nazi Adolf Hitler, wamechochea kimakusudi watu wajivunie taifa na rangi yao ili kutafuta wafuasi na kuwaharibia jina wale wanaoonwa kuwa tofauti au hawafai.
◼ Biblia inasema nini? “Kila mtu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova.” (Methali 16:5) ‘Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mwaone wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.’ (Wafilipi 2:3) Jiulize hivi: ‘Je, moyoni mwangu mimi hufurahi watu wanaposifu rangi au kabila langu na kuwadharau wengine? Je, nina mwelekeo wa kuwaonea wivu watu walio na vipawa ambavyo mimi sina, au mimi hufurahia kutoka moyoni uwezo wao?’
Hiyo ndiyo sababu Biblia inatuonya hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa, kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Hivyo, ona moyo wako kuwa kitu cha thamani na usiache kitu chochote kiupotoshe! Badala yake, ujaze hekima kutoka kwa Mungu. Ni kwa kufanya hivyo tu ndipo ‘uwezo wa kufikiri na utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya, na kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu.’—Methali 2:10-12.
Lakini unaweza kufanya nini ikiwa unachukiwa au kubaguliwa? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
Tunapowafahamu watu vizuri, inakuwa rahisi zaidi kuwa na maoni yanayofaa kuwahusu
-
-
Upendo Hushinda ChukiAmkeni!—2009 | Agosti
-
-
Upendo Hushinda Chuki
“Jamii mpya ya kidini ilitokea kwa mara ya kwanza katika historia: si kikundi fulani kinachoendeleza utaifa, lakini kikundi cha wajitoleaji ambao wameshinda tofauti za kijamii, rangi, na kitaifa: wanaume kwa wanawake wakiungana kwa usawa mbele ya mungu wao.”—Kitabu cha Paul Johnson, A History of Christianity.
UKRISTO wa kweli ulipoenea kotekote katika Milki ya Roma, watu waliona jambo la kushangaza—familia ya kimataifa ya watu wanaomwabudu Mungu ambao wamejifunza kuishi pamoja kwa amani ya kweli na umoja. Siri ya “familia” hiyo kuwa na amani ilikuwa upendo wa kweli uliotegemea kanuni za Mungu wala si hisia tu.
Yesu Kristo alifundisha kanuni hizo kwa maneno na matendo, ingawa yeye mwenyewe alibaguliwa sana na kuchukiwa. (1 Petro 2:21-23) Kwanza, alitoka eneo la Galilaya, na Wagalilaya ambao wengi wao walikuwa wakulima na wavuvi walidharauliwa na viongozi wa kidini Wayahudi huko Yerusalemu. (Yohana 7:45-52) Pia, Yesu alikuwa mwalimu stadi ambaye alipendwa na kuheshimiwa na watu wa kawaida. Kwa sababu hiyo, viongozi wa kidini walimwonea wivu hivi kwamba wakaeneza habari za uwongo kumhusu na hata wakapanga njama ya kumwua!—Marko 15:9, 10; Yohana 9:16, 22; 11:45-53.
Hata hivyo, Yesu ‘hakulipa uovu kwa uovu.’ (Waroma 12:17) Kwa mfano, Mafarisayo—waliokuwa washiriki wa dini ya Kiyahudi iliyompinga Yesu—walipomwendea wakiwa mmoja-mmoja kwa unyoofu na kumwuliza maswali, aliwajibu kwa fadhili. (Yohana 3:1-21) Hata alikula pamoja na Mafarisayo, kutia ndani mmoja ambaye alimbagua Yesu. Jinsi gani? Katika siku hizo ilikuwa kawaida kuosha miguu ya mgeni; lakini Farisayo huyo hakumwosha Yesu miguu. Je, Yesu alikasirika? Hapana. Alitumia jioni hiyo kuwafundisha jambo muhimu kuhusu huruma na kusamehe.—Luka 7:36-50; 11:37.
Yesu Aliwapenda Waliodharauliwa
Moja kati ya mifano ya Yesu inayojulikana zaidi, ni ile ya Msamaria mwema ambaye alitoa pesa zake mwenyewe kumsaidia Myahudi ambaye alikuwa amepigwa na kunyang’anywa mali zake. (Luka 10:30-37) Kwa nini tendo la Msamaria huyo lilikuwa jema sana? Wayahudi na Wasamaria walidharauliana. Kwa kweli, neno “Msamaria” mara nyingi lilitumiwa na Wayahudi kumshushia mtu heshima, hata Yesu mwenyewe aliitwa hivyo wakati mmoja. (Yohana 8:48) Chini ya hali hizo, mfano wa Yesu wa kuwapenda majirani bila ubaguzi ulikuwa wenye nguvu kama nini.
Matendo ya Yesu yalithibitisha jambo hilo kwa kumponya Msamaria mwenye ukoma. (Luka 17:11-19) Isitoshe, Yesu alizungumza kwa muda mrefu na mwanamke Msamaria, na hilo lilikuwa tukio la maana sana. (Yohana 4:7-30, 39-42) Kwa nini? Marabi Wayahudi walioshikilia sana sheria hawangezungumza na mwanamke yeyote hadharani, hata awe mtu wa ukoo wa karibu, sembuse mwanamke Msamaria!
Lakini, Mungu anamwonaje mtu mwenye ubaguzi anayejitahidi kuondoa hisia hizo moyoni mwake? Biblia inasema mambo yenye kufariji kuhusu jambo hilo.
Mungu Ni Mwenye Subira Kwetu
Katika karne ya kwanza, Wakristo wengi Wayahudi waliathiriwa na maoni yenye ubaguzi kuelekea watu wasio Wayahudi, ambao wengi wao waligeuka na kuwa waamini. Yehova Mungu alishughulikiaje jambo hilo ambalo lingeweza kuwagawanya watu? Alilifundisha kutaniko la Kikristo kwa subira. (Matendo 15:1-5) Subira hiyo ilikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa kama ilivyotajwa mwanzoni mwa makala hii, ‘walishinda tofauti za kijamii, rangi, na kitaifa.’ Kwa sababu hiyo, “makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.”—Matendo 16:5.
Tunajifunza nini? Usikate tamaa, lakini endelea kumwomba Mungu msaada kwa kuwa yeye anawapa hekima na nguvu za kufanya yaliyo sawa wale ‘wanaoendelea kuomba kwa imani.’ (Yakobo 1:5, 6) Je, unawakumbuka Jennifer, Timothy, John, na Olga waliotajwa katika makala ya kwanza ya mfululizo huu? Jennifer alipoenda kwenye shule ya sekondari, alikuwa amekomaa kiroho na alikuwa amejifunza kupuuza matusi kuhusu rangi na kimo chake. Muda mfupi baadaye, msichana mwingine alipotukanwa mara nyingi na wanafunzi wenzake, Jennifer alimtetea na kumfariji.
Ni nini kilichomsaidia Timothy kuwa mtulivu wanafunzi wenzake walipomtukana kwa sababu ya rangi yake? Anasema: “Sikutaka kuliletea suto jina la Yehova Mungu. Pia nilikumbuka kwamba tunapaswa ‘kuendelea kuushinda uovu kwa wema’ na kutoruhusu uovu utushinde.”—Waroma 12:21.
John alishinda hisia zake za ubaguzi dhidi ya mwanafunzi mwenzake ambaye ni Mhausa. “Nilipokuwa kijana,” anasema, “nilikutana na wanafunzi Wahausa na tukawa marafiki. Nilifanya mradi mmoja wa shule pamoja na mmoja wao, na tulipatana sana. Sasa ninajitahidi kuwaona watu jinsi walivyo, si kwa kutegemea rangi au kabila lao.”
Olga na mmishonari mwenzake hawakuogopa walipoteswa na wapinzani wenye chuki, lakini waliendelea kuwa imara, wakiwa na uhakika kwamba watu fulani watathamini ujumbe wa Biblia. Wengi waliuthamini. “Miaka 50 hivi baadaye,” anasema Olga, “mwanamume mmoja alinipa mfuko maridadi sana. Ndani yake kulikuwa na mawe madogo yaliyokuwa yameandikwa sifa za Kikristo kama vile wema, fadhili, upendo, na amani. Kisha aliniambia kwamba alikuwa mmoja wa wale wavulana walionitupia mawe na sasa yeye ni ndugu yangu Mkristo. Yeye na mke wake wakanipa maua meupe 24 ya waridi pamoja na ule mfuko wenye mawe.”
Wakati Ubaguzi Hautakuwapo Tena!
Hivi karibuni hakutakuwa na chuki na ubaguzi. Hilo litawezekanaje? Kwanza, dunia itakuwa na Mtawala mmoja, yaani, Yesu Kristo, ambaye alionyesha kwamba “hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu.” (Isaya 11:1-5) Isitoshe, raia wa kidunia wa Yesu wataiga kikamilifu mtazamo wake, kwa kuwa yeye na Baba yake, Yehova Mungu, watakuwa wamewafundisha.—Isaya 11:9.
Elimu hiyo ya kiroho inaendelea sasa, ikiwatayarisha watu wa Mungu kwa ajili ya maisha katika mfumo mpya kabisa wa mambo. Kwa hiyo, tunakutia moyo ujiunge na mpango huo wa kujifunza Biblia bila malipo.a Naam, Mungu hana ubaguzi; ni mapenzi yake kwamba watu wa namna zote “waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Ikiwa ungependa kujifunza Biblia bila malipo wakati na mahali panapokufaa, twakualika uwasiliane na Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme au mojawapo ya ofisi za tawi zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5. Au uwasiliane na Mashahidi wa Yehova kwenye kituo cha Intaneti www.watchtower.org.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Hivi karibuni wanadamu hawatatatizwa na chuki na ubaguzi
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa8, 9]
KANUNI ZA MUNGU TUNAZOPASWA KUFUATA
◼ “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:17-21) Tunajifunza nini? Wengine wakikutendea mambo mabaya, jifunze kuwatendea kwa njia nzuri. “Walinichukia bila sababu,” alisema Yesu Kristo. Hata hivyo, yeye hakuwachukia.—Yohana 15:25.
◼ “Na tusiwe wenye kujisifu, . . . tukioneana wivu.” (Wagalatia 5:26) Wivu na kiburi hudhuru hali ya kiroho, na mara nyingi humfanya mtu awe na chuki na ubaguzi.—Marko 7:20-23.
◼ “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Jiulize, ‘Ningependa kutendewa jinsi gani?’ Watendee watu wengine kwa njia hiyo, haidhuru wana umri, rangi, utamaduni au wanazungumza lugha gani.
◼ “Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi.” (Waroma 15:7) Je, wewe hujaribu kuwafahamu watu wa malezi na utamaduni mbalimbali, hasa ikiwa wao ni watumishi wenzako wa Mungu?—2 Wakorintho 6:11.
◼ “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zaburi 27:10) Hata wengine wakutendee namna gani, Mungu hatakuacha kamwe ukiendelea kuwa mshikamanifu kwake.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Msamaria mwenye ujirani anamsaidia Myahudi ambaye amevamiwa na wanyang’anyi
-