-
Muungano wa Ulimwengu—Je, Utapata Kuwa Uhalisi Wakati Wowote?Mnara wa Mlinzi—1997 | Novemba 1
-
-
Muungano wa Ulimwengu—Je, Utapata Kuwa Uhalisi Wakati Wowote?
“TUKIWEZA kufaulu katika vizazi vichache vyenye kufuata, kuugeuza umbo ulimwengu wa mataifa huru ambamo twaishi, kuwa namna fulani ya jamii ya kweli ya kimataifa, . . . basi tutakuwa pia tumebatilisha kwa matokeo shirika la kale la shughuli za vita . . . Hata hivyo tukishindwa, labda kutakuwa . . . hakuna ustaarabu.” Hivyo ndivyo asemavyo mwanahistoria wa kijeshi Gwynne Dyer katika kitabu chake chenye kichwa War.
Rekodi za historia, asema Dyer, zajawa na masimulizi ya mataifa na vikundi vingine vyenye nguvu vilivyoishia kupigana vita ili kusuluhisha tofauti zao. Ukosefu wao wa muungano uliangamiza kabisa uhai wa mamilioni ya wahasiriwa. Ufafanuzi wa Mfalme Solomoni wa jinsi jambo hilo lilivyoathiri watu katika siku yake bado wafaa leo. Aliandika hivi: “Nikarudi na kuona madhalimu yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji.”—Mhubiri 4:1.
Siku hizi, kama mwanahistoria aliyetajwa juu aonyeshavyo, mbali na kuhurumia “machozi yao waliodhulumiwa,” kuna sababu zaidi ya kupata njia fulani ya kugeuza umbo ulimwengu wa mataifa huru kuwa namna fulani ya jamii ya kweli ya kimataifa: Kule kuokolewa kwenyewe kwa ustaarabu kumo hatarini! Shughuli za vita za kisasa hutoa msingi wa kutarajia kuangamizwa kwa kila taifa liishialo kwenye shughuli hizo na hazitaacha washindi wowote.
Muungano wa Ulimwengu Wakaribia?
Muungano wa ulimwengu una matazamio gani? Je, jamii ya kibinadamu yaweza kushinda kani zenye kutenganisha ambazo zatisha kuokolewa kwa dunia? Watu fulani hufikiri hivyo. Mhariri wa mambo ya ulinzi wa gazeti la habari la Daily Telegraph la Uingereza, John Keegan, aandika hivi: “Kujapokuwa vurugu na ukosefu wa uhakika, yaonekana kuwa jambo liwezekanalo kwa mmoja kuweza kuona kule kutokea hatua kwa hatua kwa kile kionekanacho kuwa ulimwengu usio na vita.”
Ni nini limtolealo mtazamo huo wenye matumaini mema? Kwa nini watu wengi waonekana kuwa wenye tumaini ijapokuwa historia ndefu ya kibinadamu ya shughuli za vita na kuonekana kwa mwanadamu kuwa bila uwezo wa kujiongoza kwa mafanikio? (Yeremia 10:23) ‘Wanadamu wanasonga mbele. Historia yaonyesha kiolezo cha maendeleo yasiyokoma,’ watu fulani walibisha wakati mmoja. Hata leo, wengi huamini kwamba wema wa asili wa mwanadamu utashinda uovu kwa njia fulani. Je, hilo ni tumaini halisi? Au ni danganyo tu litakaloongoza kwenye kukata tamaa zaidi? Katika kitabu chake History of the World, mwanahistoria J. M. Roberts aliandika hivi kwa uhalisi: “Wakati ujao wa ulimwengu haungeweza kufafanuliwa kuwa salama salimini. Wala sasa mwisho wowote wa kuteseka kwa kibinadamu hauonekani kuwa karibu, wala hakuna msingi wowote wa kuamini kwamba kutakuwa na mwisho wa kuteseka kwa kibinadamu.”
Je, kuna sababu za kweli za kuamini kwamba watu na mataifa kwa kweli watashinda kutokuwa kwao na itibari kati yao na tofauti zenye kutenganisha? Au jambo fulani zaidi ya jitihada za kibinadamu lahitajiwa? Makala yenye kufuata itazungumzia maswali hayo.
-
-
Muungano wa Ulimwengu—Utakujaje?Mnara wa Mlinzi—1997 | Novemba 1
-
-
Muungano wa Ulimwengu—Utakujaje?
KAMA jengo lililochakaa ambalo limeharibiwa vibaya na wapangaji wasiojali, mfumo wa ulimwengu wa sasa wafaa kwa jambo moja tu—kubomolewa na mwingine kuchukua mahali pake. Haya si maoni mengine tu ya wenye kutabiri juu ya kukaribia kwa maafa. Kulingana na Biblia, hayo ndiyo maoni pekee ya kihalisi. Kwa nini?
Misingi ya utaratibu wa ulimwengu wa sasa si salama. Jengo lote limejawa na mchwa na mbao zenye kuoza. Miimo ya feleji inashika kutu. Kuta zinazotegemeza zimedhoofika. Paa inabonyea. Ufundibomba wavuja. Mfumo wa umeme una kasoro na ni hatari. Wakaaji hupigana bila kukoma na husababisha uharibifu katika jengo lote wakiwa na nia ya kudhuru wengine. Rasilimali yote na mazingira yake yamejaa wadudu na huenda yakatokeza kifo au madhara mabaya.
“[Ku]cheza Dansi Ukingoni mwa Kaburi”
Kwa sababu ya mapambano ya kisiasa yasiyo koma, pupa, uchokozi, na uhasama wa kijamii na kikabila ulio na msingi imara, “jamii yote ya kibinadamu,” kama vile Gwynne Dyer alivyosema, “inacheza dansi ukingoni mwa kaburi.” Ulimwenguni kote, vikundi vya wachache wenye kuazimia—vikundi-vishawishi, wapigania-uhuru, magenge ya wahalifu, maharamia wa kimataifa, na wengineo—hufuatia mipango yake ya ubinafsi na huonekana kuwa na uwezo wa kuangamiza uwezekano wowote wa amani ulimwenguni vikitaka. Vikiwa kama wapangaji wenye mvurugo, vyaweza kufanya maisha ya wengine wote yawe yenye taabu.
Hata hivyo, kulingana na wafafanuzi wengi, vikundi vya upinzani au watu mmoja-mmoja wasiotawalika hawako peke yao katika kuzuia muungano wa ulimwengu. Lile taifa lenye kujitawala ndilo kizuizi kikubwa. Mataifa huru, asema mwandishi wa shughuli za vita, S. B. Payne, Jr., huwako katika “hali ya mchafuko wa kimataifa.” Hayo hufanya lolote lile ambalo hufaa zaidi masilahi yake ya kitaifa, kwa kujali kidogo au kutojali kabisa wengine. Tokeo ni kwamba, katika historia yote “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”—Mhubiri 8:9, chapa ya 1952.
Ni kweli, serikali fulani za kitaifa zimefaulu kwa kiasi fulani kupigana na ukosefu wa haki na uonevu, ndani ya mipaka ya maeneo yake na, kwa kiasi fulani, katika kiwango cha kimataifa. Pindi kwa pindi zimeanzisha kadiri fulani ya muungano wa kimataifa. Lakini hata wakati ambapo mataifa fulani yameungana ili kutenda dhidi ya taifa lenye uchokozi, mara nyingi shaka kwamba walitenda kutokana na kujipendeza wala si kutokana na kujali kikweli hali-njema ya wengine huendelea kuwako. Uhalisi ni kwamba serikali za kibinadamu hazina suluhisho kamili na lenye kudumu kwa ukosefu wa muungano ulimwenguni. Gwynne Dyer aeleza hivi: “Dhana ya kwamba mataifa yote ya ulimwengu yataungana pamoja ili kuzuia au kuadhibu uchokozi wa taifa-pinzani ni kanuni nzuri, lakini ni taifa au mataifa gani ambayo huamua taifa lenye uchokozi, na nani hulipia gharama za fedha na uhai ambazo huenda zikahitajiwa ili kulifanya hilo taifa-pinzani lenye uchokozi liuache?”
Bila shaka, uchokozi wa taifa lolote dhidi ya jingine wawezekana tu wakati ambapo raia walio wengi wa taifa hilo chokozi hawapingi uchokozi huo. Historia huonyesha tena na tena kwamba si katika “taifa-pinzani” fulani tu kwamba raia wametegemeza viongozi wao, wawe sawa au wasiwe sawa. Kwa hakika, wapangaji wa dunia walio wengi wamefanya hivyo. Wamefuata “uwongo, fitina na propaganda, bila kufikiri,” kama gazeti Time lilivyoeleza, zitokazo kwa viongozi wengi wa kisiasa na wa kidini.
Utukuzo wa taifa umewasha harara za watu ambao vinginevyo wangekuwa wenye kusababu na wenye huruma na umewasababisha kufanya uhalifu wa kinyama dhidi ya wanaume, wanawake, na watoto wa taifa jingine. Kwa kielelezo, kwa kurejezea Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mwanahistoria J. M. Roberts aeleza hivi: “Mojawapo ya mambo tata ya mwaka wa 1914 ni kwamba katika kila nchi idadi kubwa ya watu, wa vyama vyote, imani na ukoo, kwa kushangaza, waonekana kuwa wameenda vitani kwa kupenda na kwa furaha.” Je, watu wamejifunza somo tangu wakati huo? La! Uovu wa “kutukuza taifa bila kufikiri,” kama vile mwandishi wa habari Rod Usher alivyouita, waendelea kuharibu nafasi yoyote ile ya kuwa na muungano wa ulimwengu.
Kani Kutoka Nje Zafanya Kazi
Hata hivyo, kuna kizuizi kikubwa zaidi kwa muungano wa ulimwengu. Biblia hufunua kwamba kani kutoka nje zafanya kazi. Kani hizo zatambulishwa kuwa Shetani Ibilisi na vibaraka wake, roho waovu. Kulingana na Biblia, Shetani ni “mungu wa huu mfumo wa mambo [ambaye] amepofusha akili za wasioamini,” ili “habari njema yenye utukufu juu ya Kristo” isiwavutie.—2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 12:9.
Bila shaka, jambo hilo haliwaweki watu mmoja-mmoja huru na daraka la vitendo vyao wenyewe. Lakini laeleza ni kwa nini serikali za kibinadamu haziwezi kamwe kuanzisha ulimwengu wenye muungano kikweli. Maadamu Shetani Ibilisi aendelea kuwako, atawaathiri wanaume na wanawake wakuze zile ambazo Biblia huziita “kazi za mwili,” kutia na ‘uadui, zogo, magomvi na migawanyiko.’—Wagalatia 5:19-21.
Serikali ya Ulimwengu
Basi, suluhisho ni nini? Miaka ipatayo mia saba iliyopita, yule mshairi na mwanafalsafa Mwitalia aliyejulikana sana, Dante alionyesha jibu. Alitoa hoja kwamba serikali ya ulimwengu pekee ndio ingeweza kuhakikisha amani na muungano wa wanadamu. Kwa watu wengi tumaini la kuwa na serikali ya ulimwengu ya namna yoyote ni udanganyo tu, si jambo wawezalo kuwa na uhakika halisi nalo. “Serikali ya ulimwengu,” amalizia mtungaji, Payne, aliyetangulia kutajwa, “haiwezi kupatikana katika pindi hii ya historia.” Kwa nini? Kwa sababu ingeibidi serikali yoyote ya ulimwengu yenye kufaulu itoe uhakikisho kamili wa mambo mawili ambayo yaonekana kupita kabisa uwezo wa mwanadamu, yaani “serikali ya ulimwengu itakomesha vita na kwamba serikali ya ulimwengu haitakuwa mamlaka ya tufeni pote yenye kuonea.”
Ni jambo la hakika kwamba hakuna serikali ya kibinadamu itakayofanya hivyo wakati wowote. Hata hivyo, Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo waweza na utaondoa vita vyote. (Zaburi 46:9, 10; Mathayo 6:10) Kwa kweli, utaondoa wachochezi wa vita. Nabii Danieli huonyesha kwamba mwishoni mwa wakati uliowekwa na Mungu wa utawala wa kibinadamu juu ya dunia, utawala wa kibinadamu “[unge]kuwa ufalme uliogawanyika” kama “chuma [ambacho] kimechanganyika na udongo wa matope.” (Danieli 2:41-43) Hilo lingetokeza kuvunjika-vunjika kisiasa na mapambano yasiyoepukika. Na bado, Danieli asema kwamba Ufalme wa Mungu “utavunja falme [au serikali] hizi zote [zenye kufuatia utukuzo wa taifa na zisizo na muungano] vipande vipande,” ukisimamisha mahali pa hizo Ufalme wake mikononi mwa Yesu Kristo ambao umengojewa kwa muda mrefu.—Danieli 2:44.
-