Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Furahia Dunia Yetu Maridadi
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Februari 15
    • Furahia Dunia Yetu Maridadi

      WATAALAMU WA NYOTA wameona kwamba makao ya wanadamu ni doa dogo tu katika ulimwengu mkubwa sana. Uhai haujapatikana mahali pengine popote katika ulimwengu. Dunia ndiyo sayari ya pekee ambayo ina hali zinazofaa kabisa kwa ajili ya uhai.

      Zaidi ya hayo, tunaweza kufurahia maisha katika sayari hii maridadi. Inafurahisha kama nini kufurahia joto la jua siku yenye baridi! Ni nani kati yetu asiyevutiwa kuona rangi maridadi jua linapochomoza au kushuka? Bila shaka, jua letu linafanya mengi zaidi ya kutupendeza tu. Uhai wetu unategemea sana jua.

      Kwa mamilioni yasiyohesabika ya miaka, nguvu za uvutano za jua zimeshikilia dunia yetu na sayari nyingine katika mizunguko iliyo imara. Na kama wanafunzi wanavyojifunza shuleni, mfumo mzima wa jua unazunguka katikati ya kikundi chetu cha nyota kinachoitwa Kilimia. Lakini katika kikundi chetu cha nyota, jua ni moja tu kati ya nyota zaidi ya bilioni 100 zinazozunguka pamoja.

      Nguvu za uvutano zinashikilia kikundi chetu cha nyota pamoja na vikundi vingine 35 hivi vya nyota. Makundi makubwa zaidi ya nyota yana maelfu ya vikundi vya nyota. Inaelekea kwamba mfumo wetu wa jua haungekuwa imara sana ikiwa ungekuwa katika kundi kubwa zaidi lenye vikundi vingi sana vya nyota. Lakini, kama ilivyo, ni maeneo machache katika ulimwengu mzima “yanayofaa kwa ajili ya uhai tata kama wetu,” wanasema Guillermo Gonzalez na Jay W. Richards katika kitabu chao (The Privileged Planet).

      Je, uhai ulijitokeza wenyewe tu duniani kutokana na “mlipuko mkubwa” uliotukia kwa aksidenti? Au je, kuna kusudi muhimu zaidi la uhai katika Dunia hii maridadi?

      Watu wengi wamekata kauli kwamba dunia ambayo ni makao yetu ilibuniwa hasa ili kutegemeza uhai.a Karne nyingi zilizopita, mtungaji wa mashairi Mwebrania alizungumza kuhusu dunia na mbingu. Aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini?” (Zaburi 8:3, 4) Mtungaji huyo wa mashairi aliamini kwamba lazima kuna Muumba. Je, kauli hiyo inapatana na akili katika kizazi hiki cha kisayansi?

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona kitabu cha Zaburi, hasa Zaburi ya 8.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 3]

      “Kutoka mbali, Dunia inang’aa kama kito cha bluu katika anga lenye giza,” kinasema kitabu kimoja (The Illustrated Science Encyclopedia—Amazing Planet Earth).

      [Hisani]

      Globe: U.S. Fish & Wildlife Service, Washington, D.C./NASA

  • Mfumo Wetu wa Pekee wa Jua—Jinsi Ulivyotokea
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Februari 15
    • Mfumo Wetu wa Pekee wa Jua—Jinsi Ulivyotokea

      KUNA mambo mengi yanayofanya mfumo wetu wa jua uwe wa pekee katika ulimwengu mzima. Mfumo wetu wa jua uko kati ya mikono miwili inayozunguka ya kikundi chetu cha Kilimia katika eneo ambalo halina nyota nyingi sana likilinganishwa na maeneo mengine. Karibu nyota zote tunazoweza kuona usiku ziko mbali sana hivi kwamba zinapotazamwa kwa darubini kubwa zaidi, zinaonekana kama madoa madogo ya nuru. Je, mfumo wetu wa jua ulipaswa kuwa mahali ulipo?

      Ikiwa mfumo wetu wa jua ungekuwa karibu na sehemu ya katikati ya Kilimia, tungepata madhara kwa sababu ya kuwa katika eneo lenye msongamano mkubwa wa nyota. Kwa mfano, inaelekea kwamba mzunguko wa dunia ungevurugwa na hilo lingeathiri sana uhai wa wanadamu. Kama ilivyo, inaonekana kwamba mfumo wa jua upo mahali panapofaa kabisa katika kikundi chetu cha nyota ili kuepuka hatari hizo na nyinginezo. Hatari hizo zinatia ndani kuongezeka kwa joto mfumo wetu unapopita katika mawingu ya gesi na miale hatari inayotokana na nyota zinazolipuka.

      Jua ni nyota inayofaa mahitaji yetu. Jua linaendelea kutoa moto mkali, linadumu daima, si kubwa sana, na halina joto kali kupita kiasi. Nyota nyingi katika kikundi chetu ni ndogo sana kuliko jua letu na hazitoi mwangaza unaofaa wala kiasi kinachofaa cha joto ili kutegemeza uhai katika sayari kama dunia. Zaidi ya hilo, nguvu za uvutano zinaunganisha pamoja nyota moja au nyota nyingine nyingi ambazo zinazungukana. Tofauti na hilo, jua letu halitegemei nyota nyingine. Inaelekea kwamba mfumo wetu wa jua haungekuwa imara ikiwa ungeathiriwa na nguvu za uvutano za nyota mbili au zaidi zilizo kama jua.

      Kuna jambo lingine linalofanya mfumo wetu wa jua uwe wa pekee. Sayari kubwa zaidi nje ya mfumo wetu zenye mizunguko inayokaribia kuwa mviringo zipo pahali ambapo nguvu zake za uvutano haziwezi kuhatarisha sayari zilizo kama dunia.a Badala yake, sayari hizo zinafyonza na kuzuia vitu hatari. Wanasayansi Peter D. Ward na Donald Brownlee wanaeleza hivi katika kitabu chao (Rare Earth—Why Complex Life Is Uncommon in the Universe): “Mawe ya angani na nyotamkia zinaanguka kwenye mfumo wetu lakini si kwa wingi, kwa sababu tunakingwa na sayari kubwa za gesi kama vile Sumbula (Jupita) ambayo iko mbali nasi.” Mifumo mingine ya jua yenye sayari kubwa imegunduliwa. Lakini idadi kubwa ya sayari hizo zina mizunguko ambayo inaweza kuhatarisha sayari ndogo zaidi kama dunia.

      Kazi ya Mwezi

      Tangu zamani za kale, mwezi wetu umewashangaza wanadamu. Umewachochea watu kutunga mashairi na nyimbo. Kwa mfano, mtungaji wa zamani wa mashairi Mwebrania anasema kwamba mwezi ‘umefanywa imara mpaka wakati usio na kipimo, na kama vile shahidi mwaminifu angani.’—Zaburi 89:37.

      Njia moja muhimu ambayo mwezi unahusika katika kuendeleza uhai duniani ni kwamba nguvu zake za uvutano zinasababisha kujaa na kupwa kwa maji. Jambo hilo linadhaniwa kuwa muhimu kwa mawimbi ya bahari, ambayo ni ya maana sana kwa hali ya hewa duniani.

      Mwezi unatimiza kusudi lingine muhimu kwa sababu nguvu zake za uvutano zinaimarisha mhimili wa dunia wakati inapozunguka jua. Gazeti moja la kisayansi (Nature) linasema kwamba bila mwezi, mwinamo wa mhimili wa dunia ungebadilika-badilika kwa vipindi virefu kuanzia “karibu [digrii] 0 hadi [digrii] 85.” Wazia jinsi ingekuwa ikiwa mhimili wa dunia haungekuwa umeinama! Hatungekuwa na majira yenye kupendeza yanayobadilika-badilika na hatungepata mvua. Pia, kuinama kwa mhimili wa dunia kunazuia kusiwe na joto jingi sana au baridi kali sana ili kutegemeza uhai wetu. Mtaalamu wa nyota, Jacques Laskar, anakata kauli hii: “Hali yetu ya hewa ni imara kwa sababu ya jambo fulani la pekee: kuwapo kwa Mwezi.” Ili kuimarisha hali yetu ya hewa, mwezi wetu ni mkubwa ukilinganishwa na miezi mingine ya zile sayari kubwa.

      Hata hivyo, kazi nyingine ya mwezi ambayo inatajwa na mwandishi wa kitabu cha Biblia cha Mwanzo kilichoandikwa zamani ni kwamba mwezi unatoa mwangaza usiku.—Mwanzo 1:16.

      Hali Hizo Zilitokea Zenyewe au Zilitokezwa?

      Hali hizo zote zinazotukia kwa pamoja na ambazo zinategemeza uhai duniani na kufanya maisha yapendeze zilitokea jinsi gani? Inaonekana kwamba zilitokana na moja kati ya mambo haya mawili. Jambo la kwanza ni kwamba hali hizo zote zilitokea zenyewe tu bila kusudi lolote. La pili ni kwamba kuna mtu mwenye akili aliyezitokeza.

      Maelfu ya miaka iliyopita, Maandiko Mtakatifu yalisema kwamba ulimwengu ulibuniwa na kufanyizwa na Muumba, Mungu Mweza-Yote. Ikiwa hilo ni kweli, inamaanisha kwamba hali zilizo katika mfumo wetu wa jua hazikutokea tu zenyewe lakini zilibuniwa. Muumba alitupa masimulizi yaliyoandikwa ya hatua alizochukua ili kuwe na uhai duniani. Huenda ukashangaa kujua kwamba hata ingawa masimulizi hayo yaliandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita, matukio katika historia ya ulimwengu yanayoelezwa katika masimulizi hayo yanapatana na yale ambayo wanasayansi wanaamini. Masimulizi hayo yako katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo. Chunguza yale kinachosema.

      Masimulizi ya Mwanzo Kuhusu Uumbaji

      “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1) Maneno ya utangulizi ya Biblia yanazungumzia uumbaji wa mfumo wetu wa jua, kutia ndani sayari yetu, na pia uumbaji wa nyota zilizo katika mabilioni ya vikundi vya nyota vilivyo katika ulimwengu mzima. Kulingana na Biblia, wakati mmoja dunia ilikuwa “bila umbo, na ukiwa.” Hakukuwa na mabara wala nchi inayozaa. Lakini maneno yanayofuata yanakazia kile ambacho wanasayansi wanasema ni takwa muhimu zaidi ili sayari itegemeze uhai, yaani, maji mengi sana. Roho ya Mungu ilikuwa ‘ikienda huku na huku juu ya uso wa maji.’—Mwanzo 1:2.

      Ili maji yaliyo kwenye uso wa sayari yabaki yakiwa majimaji, ni lazima sayari hiyo iwe umbali unaofaa kabisa kutoka kwenye jua lake. “Sayari ya Mihiri ina baridi kali sana, Zuhura ina joto kali sana, Dunia ina hali zinazofaa kabisa,”anaeleza mtaalamu wa sayansi ya sayari, Andrew Ingersoll. Vivyo hivyo, ili mimea ikue ni lazima kuwe na mwangaza wa kutosha. Na kwa kweli, masimulizi ya Biblia yanasema kwamba katika kipindi cha mapema cha uumbaji, Mungu alifanya nuru ya jua ipenye mawingu meusi ya mvuke wa maji ambao ulifunika bahari kama ‘utepe wa kumfungia’ mtoto.—Ayubu 38:4, 9; Mwanzo 1:3-5.

      Katika mistari inayofuata ya kitabu cha Mwanzo, tunasoma kwamba Muumba alitokeza kile ambacho Biblia inaita “anga.” (Mwanzo 1:6-8) Anga hilo limejaa gesi zinazofanyiza angahewa ya dunia.

      Kisha, Biblia inaeleza kwamba Mungu alibadili uso wa dunia usiokuwa na umbo ili kufanya nchi kavu. (Mwanzo 1:9, 10) Inaelekea kwamba alibana uso wa dunia. Huenda hilo lilitokeza mabonde yenye kina na mabara yaliyoinuka kutoka baharini.—Zaburi 104:6-8.

      Wakati fulani usiojulikana katika historia ya dunia, Mungu aliumba viumbe wadogo wanaoitwa mwani katika bahari. Wakitumia nguvu za jua, viumbe hao wenye chembe moja wanaozaana bila kutegemea viumbe wengine wa jamii yao, walianza kubadili gesi ya kaboni dioksidi kuwa chakula na kuongeza oksijeni katika angahewa. Utaratibu huo wa ajabu uliboreshwa katika kipindi cha tatu cha uumbaji wakati mimea ilipoumbwa ambayo mwishowe ilifunika nchi. Hivyo, kiasi cha oksijeni katika angahewa kiliongezeka, jambo ambalo lingewezesha wanadamu na wanyama kuendeleza uhai wao kwa kupumua.—Mwanzo 1:11, 12.

      Ili kufanya nchi izae, Muumba alitokeza viumbe mbalimbali wadogo sana waishi ndani ya udongo. (Yeremia 51:15) Viumbe hao wadogo wanavunja-vunja vitu vilivyokufa, na kutokeza upya virutubishi ambavyo mimea inahitaji ili kukua. Bakteria fulani za pekee zilizo katika udongo zinafyonza nitrojeni kutoka katika hewa na kutengeneza virutubishi hivyo muhimu ili kuwezesha mimea kukua. Inastaajabisha kwamba kiasi kidogo cha udongo wenye rutuba kinaweza kuwa na viumbe wadogo bilioni sita!

      Andiko la Mwanzo 1:14-19 linaeleza kuhusu kuumbwa kwa jua, mwezi, na nyota katika kipindi cha nne cha uumbaji. Mwanzoni, huenda ikaonekana kwamba andiko hilo linapingana na maelezo ya Maandiko yaliyotangulia. Hata hivyo, kumbuka kwamba Musa, mwandikaji wa kitabu cha Mwanzo, aliandika masimulizi ya uumbaji kama mtazamaji aliye duniani. Inaelekea, jua, mwezi, na nyota zilianza kuonekana kupitia angahewa ya dunia katika kipindi cha nne cha uumbaji.

      Masimulizi ya Mwanzo yanaonyesha kwamba viumbe wa baharini walianza kuonekana katika kipindi cha tano cha uumbaji na viumbe wa nchi kavu na wanadamu wakatokea katika kipindi cha sita.—Mwanzo 1:20-31.

      Mungu Alitaka Wanadamu Wafurahie Maisha Duniani

      Je, huoni kwamba uhai duniani, ambao ulitokea kama ilivyoelezwa katika masimulizi ya kitabu cha Mwanzo, ulikusudiwa ufurahiwe? Je, umewahi kuamka asubuhi yenye jua, ukavuta hewa safi, na kufurahi kuwa hai? Labda ulitembea katika bustani na kufurahia umaridadi na harufu nzuri ya maua. Au huenda ulitembea katika shamba lenye miti ya matunda na kuchuma tunda tamu. Hungeweza kufurahia mambo hayo ikiwa: (1) dunia haingekuwa na maji mengi, (2) haingekuwa na joto na mwangaza wa kutosha wa jua, (3) ikiwa angahewa yetu haingekuwa na mchanganyiko unaofaa kabisa wa gesi mbalimbali, na (4) ikiwa hakungekuwa na nchi yenye rutuba.

      Hali hizo ambazo hazipatikani katika sayari ya Mihiri, Zuhura, na sayari nyingine jirani, hazikutokea zenyewe tu. Zilitokezwa kwa njia inayofaa kabisa ili maisha yapendeze duniani. Kama itakavyoonyeshwa katika habari inayofuata, Biblia inasema kwamba Muumba alibuni sayari yetu maridadi ili idumu milele.

      [Maelezo ya Chini]

      a Sayari nne zilizo ndani zaidi ya mfumo wetu wa jua, yaani, Zebaki, Zuhura, Dunia, na Mihiri, zinawekwa katika kikundi kimoja kwa sababu zina miamba. Sayari kubwa zilizo nje, yaani, Sumbula, Sarateni, Zohali, na Kausi, zimefanyizwa hasa kwa gesi.

      [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      “Endapo mimi nikiwa mtaalamu wa jiolojia ningeombwa niwaelezee kwa ufupi wachungaji wasio na elimu, kama yale makabila ambayo yalipewa Kitabu cha Mwanzo, maoni yetu ya leo kuhusu mwanzo wa dunia na kusitawi kwa uhai duniani, ningefuata kwa ukaribu sana lugha inayotumiwa katika sura ya kwanza ya kitabu cha Mwanzo.”—Mtaalamu wa jiolojia Wallace Pratt.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

      Ipo Mahali Panapofaa Kabisa Ili Kuuchunguza Ulimwengu

      Ikiwa jua lingekuwa kwingineko katika kikundi chetu cha nyota, hatungeweza kuona nyota vizuri. Kitabu kimoja (The Privileged Planet) kinaeleza kwamba “Mfumo wetu wa Jua uko . . . mbali na sehemu zenye vumbi, zilizo na mwangaza mwingi sana, hivi kwamba tunaweza kuona vizuri sana nyota zilizo karibu na zilizo mbali sana.”

      Zaidi ya hayo, ukubwa na umbali wa mwezi kutoka kwenye dunia unafaa kabisa ili mwezi ufunike jua wakati wa kupatwa kwa jua. Matukio hayo yasiyo ya kawaida na yenye kustaajabisha yamewawezesha wataalamu wa nyota kuchunguza jua. Uchunguzi wao umewawezesha kujua mambo mengi ambayo hayakuwa yamejulikana kuhusu kung’aa kwa nyota.

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Mwezi una uzito na ukubwa wa kutosha kuimarisha mhimili wa dunia

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Ni nini kinachowezesha kuwe na uhai duniani? Ni maji mengi sana, kiasi kinachofaa kabisa cha mwangaza na joto, nchi yenye rutuba, na angahewa

      [Hisani]

      Globe: Based on NASA Photo; wheat: Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

  • Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba
    Mnara wa Mlinzi—2007 | Februari 15
    • Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba

      JE, HUSHANGAI kwamba hali ambazo wanasayansi wanaamini kuwa ni muhimu kwa uhai katika sayari yoyote ile zinatajwa au kuzungumziwa moja kwa moja katika sura ya kwanza ya Biblia? Ni hali gani hizo?

      Ili uhai usitawi, lazima kuwe na maji mengi sana kama inavyotajwa katika Mwanzo 1:2. Lazima kuwe na kiwango kinachofaa kabisa cha joto kwenye sayari hiyo ili maji yaendelee kuwa majimaji. Ili kuwe na kiwango hicho cha joto, ni lazima sayari hiyo iwe umbali unaofaa kabisa kutoka kwenye jua lake. Masimulizi ya Mwanzo yanataja tena na tena jua na jinsi linavyoisaidia dunia.

      Ili sayari ikaliwe na watu, inapaswa kuwa na angahewa iliyo na mchanganyiko hususa wa gesi mbalimbali. Hali hiyo muhimu inatajwa katika Mwanzo 1:6-8. Kukua kwa mimea inayotajwa katika Mwanzo 1:11, 12, kunasaidia kutokeza kiasi kikubwa cha oksijeni. Sayari ambamo wanyama wa aina mbalimbali wanaweza kuishi inapaswa kuwa na mabara ya nchi kavu inayozaa kama ile inayotajwa katika Mwanzo 1:9-12. Mwishowe, ili kuwe na hali ya hewa inayofaa, lazima sayari iiname kwenye pembe inayofaa kabisa na ibaki papo hapo. Dunia imekaa hivyo kwa sababu ya nguvu za uvutano za mwezi wetu. Hali hiyo na baadhi ya faida zake zinatajwa katika Mwanzo 1:14, 16.

      Musa, mwandikaji wa zamani, ambaye hakuwa na elimu ya kisasa ya sayansi angeweza kujua mambo hayo namna gani? Je, alikuwa na uwezo usio wa kawaida wa kuelewa umuhimu wa mambo hayo, uwezo ambao watu wa siku zake hawakuwa nao? Alieleza mambo hayo kwa sababu aliongozwa na roho ya Muumba wa mbingu na dunia. Hilo ni jambo muhimu hasa tunapofikiria usahihi wa masimulizi ya Mwanzo.

      Biblia inaonyesha waziwazi kwamba maajabu ya ulimwengu unaotuzunguka yana kusudi fulani. “Mbingu ni mbingu za Yehova,” inasema Zaburi 115:16, “Bali dunia amewapa wana wa binadamu.” Zaburi nyingine inasema: “Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Ikiwa ulimwengu na dunia yetu maridadi ilibuniwa na kutokezwa na Muumba, bila shaka si vigumu kuamini kwamba yeye ana uwezo wa kutegemeza ulimwengu na dunia. Hilo linamaanisha kwamba unaweza kutarajia kwa uhakika kutimizwa kwa ahadi hii nzuri sana: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Kwa kweli, Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu” lakini “aliiumba ili ikaliwe” milele na wanadamu wanaothamini na kuheshimu kazi zake.—Isaya 45:18.

      Kulingana na Maandiko, Yesu alikuja duniani ili kutufundisha kumhusu Mungu na kusudi Lake la kuwapa wanadamu watiifu uzima wa milele. (Yohana 3:16) Tunahakikishiwa kwamba hivi karibuni Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ nao watu wanaopenda amani kutoka mataifa yote na ambao wanakubali maandalizi yake ya wokovu wataokoka. (Ufunuo 7:9, 14; 11:18) Maisha yatakuwa yenye kufurahisha kama nini kadiri wanadamu watakavyoendelea milele kugundua na kupendezwa na maajabu ya uumbaji wa Mungu!—Mhubiri 3:11; Waroma 8:21.

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

      NASA photo

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki