Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kusumbuliwa Kingono—Tatizo la Duniani Pote
    Amkeni!—1996 | Mei 22
    • Kusumbuliwa Kingono—Tatizo la Duniani Pote

      KAZI ilikuwa imekuwa ogofyo kwa karani mmoja mchanga aitwaye Rena Weeks. Ni kweli kwamba kampuni ya sheria iliyomwajiri ilikuwa mashuhuri nayo ilikuwa na ofisi katika zaidi ya nchi dazani mbili. Lakini, yeye alimfanyia kazi mwanamume mmoja ambaye, kulingana na dai lake, hangeweza kuacha kumkamata-kamata na kumshika-shika. Hayo mashambulizi yenye kumwaibisha yaliandamana na usemi mchafu wenye kudokeza ngono.

      Miaka mingi iliyopita, wanawake waliokuwa katika hali kama hii hawakuwa na namna—ila tu labda waache kazi. ‘Neno [la mwanamke] dhidi ya [mwanamume]’ halingekuwa kesi. Na hata wale walioelekea kuamini yale ambayo mwanamke alisema labda wangepuuza tu tatizo hilo kwa kusema, ‘Si jambo kubwa.’ Lakini nyakati zimebadilika. Rena Weeks alifanya zaidi ya kukasirika tu na kuacha kazi. Yeye alishtaki.

      Baraza la mahakama la Marekani liliamuru apewe ridhaa ya dola 50,000 kwa sababu ya kufadhaika kihisia-moyo, pamoja na dola 225,000 za ziada ili kuadhibu yule aliyekuwa mkubwa wake wa kazi. Kisha katika hatua iliyonasa uangalifu wa makampuni ya biashara na ya sheria ulimwenguni pote, hilo baraza la mahakama liliamuru kampuni hiyo ilipe kiasi kikubwa sana cha pesa cha dola milioni 6.9 za ziada kikiwa adhabu ya kukosa kurekebisha hilo tatizo!

      Bila shaka kesi ya Weeks si kisa cha pekee cha aina hiyo. Shtaka jingine la majuzi lilihusu kampuni moja ya kitaifa (Marekani) yenye maduka mengi ya kuuza bidhaa kwa bei iliyopunguzwa. Mwajiriwa mmoja aitwaye Peggy Kimzey alidai kwamba msimamizi wake wa kazi alikuwa amemwambia maneno machafu mengi ya kingono. Katika 1993, Peggy Kimzey alijiuzulu kazi yake na kushtaki. Iliamriwa alipwe dola 35,000 kwa sababu ya kuaibishwa na masumbufu ya kiakili pamoja na dola 1 ya mfano kwa kupoteza mshahara. Baraza la mahakama liliamua pia kwamba aliyekuwa mwajiri wake alikuwa amefanyiza mazingira mabaya ya kazi kwa kuachilia kusumbuliwa kwake. Adhabu ikawa nini? Alitozwa Dola milioni 50!

      Gazeti Men’s Health lasema: “Kesi za kusumbuliwa kingono zimekuwa zikiongezeka sana. Katika 1990, EEOC [Tume ya Fursa Sawa ya Kuajiriwa] ilishughulikia malalamiko kama hayo 6,127; kufikia mwaka uliopita [1993] jumla ya mwaka mzima ilikuwa karibu maradufu kufikia 11,908.”

      Kutumia Mamlaka Vibaya

      Huku amri za mabaraza ya mahakama zikiwa habari kuu za vyombo vya habari, ukweli ni kwamba ni visa vichache tu ambavyo hupelekwa mahakamani. Wengi wanaosumbuliwa huugua kimya-kimya—wakiwa wadhulumiwa wa tendo baya la kutumia vibaya mamlaka na matisho linalofanywa katika ofisi, barabarani, katika basi, kwenye kaunta za chakula cha mchana, na katika viwanda. Nyakati nyingine, kuna ushurutisho wa kufanya ngono. Ingawa hivyo, mara nyingi udhia huwa matendo ya hila, yenye kuchokoza yasiyo na aibu: miguso isiyotakikana au isiyofaa, maneno machafu, na kutazamwa kwa tamaa ya kingono.

      Ni kweli kwamba wengine hukataa kutaja kwamba tabia hiyo ni kusumbuliwa, wakibisha kwamba ni jaribio tu la kijinga kwa upande wa wanaume fulani kuvutia uangalifu wa watu wa jinsia tofauti. Lakini wengi, kama mwandikaji Martha Langelan, hukataa majaribio kama hayo ya kutolea udhuru tabia mbaya. Yeye aandika: “Hiyo si kutafuta uchumba kijinga, au kutafuta uchumba kusiko na adabu, au kutafuta uchumba kimzaha, au kutafuta uchumba ‘kunakoeleweka vibaya.’ Haikusudiwi ivutie wanawake; hiyo ni tabia yenye kusudi jingine kabisa. Kama kulala kinguvu, kusumbua kingono kumekusudiwa kushurutisha wanawake, si kuwavutia. . . . [Huko] ni wonyesho wa mamlaka.” Ndiyo, mara nyingi kutendwa vibaya kwa njia hiyo ni njia nyingine tu iliyo katili ambayo “mutu ana uwezo juu ya mwenzake kwa kumwumiza.”—Muhubiri 8:9, Zaire Swahili Bible; linganisha Mhubiri 4:1.

      Mara nyingi wanawake hawafurahii kusumbuliwa kingono nao huitikia wakiwa na hisia kama machukizo na hasira hadi kushuka moyo na kuaibishwa. Mmoja aliyedhulumiwa akumbuka: “Hiyo hali ilinimaliza kabisa. Nilipoteza utumainifu wangu, uhakika wangu, kujistahi kwangu, na tamaa zangu za kazi-maisha. Utu wangu ukabadilika mara moja. Nilikuwa mtu mwenye furaha maishani. Nikawa mwenye uchungu, mpweke, na mwenye aibu.” Na wakati mdhulumu ni mwajiri au mtu mwingine mwenye mamlaka, kusumbuliwa hasa huwa kubaya hata zaidi.

      Basi, si ajabu kwamba mahakama zimeanza kuadhibu wakosaji na kuamuru wadhulumiwa walipwe ridhaa. Tangu Mahakama Kuu ya Marekani ifafanue kutendwa vibaya kwa njia hiyo kuwa ukiukaji wa haki za raia, waajiri wamezidi kuwa na daraka la kisheria la kudumisha mazingira ya kazi ambayo si “mabaya au yenye kuudhi.”

      Makampuni yaachiliayo kusumbuliwa kingono yaweza kupatwa na hali ya wafanyakazi kukosa motisha ya kazi, wengi kukosa-kosa kufika kazini, matokeo ya chini, na kuajiriwa kwa wafanyakazi wengi wanaochukua mahali pa wengine wanaoacha—bila kutaja hasara za kifedha wadhulumiwa wakiamua kushtaki.

      Kumeenea Kiasi Gani?

      Kusumbuliwa kingono kumeenea kwa kiasi gani hasa? Uchunguzi mbalimbali waonyesha kwamba zaidi ya nusu ya wanawake wanaofanya kazi Marekani wamesumbuliwa kingono. Hivyo kitabu kimoja chadai: “Kusumbuliwa kingono ni tatizo lililoenea sana. Hupata wanawake katika kila aina ya kazi tokea wahudumu wa hoteli hadi wakuu wa mashirika. Hutukia katika kila ngazi ya usimamizi wa mashirika na katika kila aina ya biashara na viwanda.” Hata hivyo, tatizo hilo haliko Marekani pekee. Kitabu Shockwaves: The Global Impact of Sexual Harassment, cha Susan L. Webb, chataja takwimu zifuatazo:a

      KANADA: “Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba wanawake 4 kati ya 10 waliripoti kuwa walisumbuliwa kingono wakiwa kazini.”

      JAPANI: “Uchunguzi wa Agosti 1991 ulionyesha kwamba asilimia 70 ya wanawake waliokubali kuhojiwa walisumbuliwa” kazini. “Asilimia 90 walisema kwamba walisumbuliwa kingono wakati wa kwenda na kutoka kazini.”

      AUSTRIA: “Uchunguzi wa 1986 ulionyesha kwamba karibu asilimia 31 ya wanawake waliripoti visa vibaya vya kusumbuliwa.”

      UFARANSA: “Katika 1991 uchunguzi mmoja . . . uligundua kwamba asilimia 21 ya wanawake 1,300 waliohojiwa walisema kwamba wao binafsi walikuwa wamepata kusumbuliwa kingono.”

      UHOLANZI: Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba “asilimia 58 ya wanawake waliokubali [kuhojiwa] walisema kwamba wao binafsi walipata kusumbuliwa kingono.”

      Ishara ya Nyakati

      Bila shaka, kuudhiwa na kusumbuliwa kazini si mambo mapya. Wanawake—na nyakati nyingine wanaume—walitendwa vibaya kwa njia hiyo hata huko nyuma katika nyakati za Biblia. (Mwanzo 39:7, 8; Ruthu 2:8, 9, 15) Lakini tabia hiyo mbaya yaonekana imeenea hasa leo. Kwa nini?

      Jambo moja ni kwamba katika miaka ya majuzi wanawake wengi sana wameanza kufanya kazi. Basi, wanawake wengi wamejipata katika hali ambazo wanaweza kutendwa vibaya. Hata hivyo, la muhimu hata zaidi ni unabii wa Biblia uliotabiriwa zamani sana: “Kumbuka hili! Kutakuwa na nyakati zilizo ngumu katika siku za mwisho. Watu watakuwa wenye ubinafsi, wenye pupa, wenye kujisifu, na hila; watakuwa wenye kutukana . . . ; watakuwa wasio na fadhili, wasio na huruma, wachongezi, wenye jeuri, na wakali.” (2 Timotheo 3:1-3, Today’s English Version) Kuenea kwa kusumbuliwa kingono ni mojawapo tu uthibitisho wenye kutokeza kwamba maneno hayo yanatimizwa leo. Kwa kupendeza, makala moja katika gazeti Men’s Health yasema kwamba “ongezeko la madai ya kusumbuliwa kingono limeandamana na kupunguka sana kwa adabu kwa ujumla. Tabia mbaya zipo kila mahali.”

      Kuenea kwa kusumbuliwa kingono pia kwaonyesha ile “adili mpya,” ambayo ilienea sana katika ulimwengu wakati wa miaka ya 1960. Kuvunjwa kwa maadili ya kidesturi kumeandamana na hali ya kushangaza sana ya kutojali haki na hisia za wengine. Hata chanzo kiwe nini, kusumbuliwa kingono ni jambo la kuogofya litokealo kazini. Wanaume na wanawake wanaweza kufanya nini ili kujilinda? Je, kutapata kuwa na wakati ambapo mahali pa kazi hapatakuwa na kusumbuliwa?

      [Maelezo ya Chini]

      a Takwimu huelekea kutofautiana, kwa kuwa watafiti hutumia njia na ufafanuzi tofauti-tofauti wa kusumbuliwa kingono.

      [Sanduku katika ukurasa wa4]

      Kusumbuliwa Kingono—Ngano Dhidi ya Mambo ya Hakika

      Ngano: Kusumbuliwa kingono huripotiwa kupita kiasi sana. Ni jambo jingine tu la kupita, tokeo la kutiliwa chumvi na kichaa la vyombo vya habari.

      Hakika: Sanasana, mwanamke hupata hasara sana kuliko faida kwa kuripoti juu ya kudhulumiwa. Kwa kweli, ni wanawake wachache tu (asilimia 22 kulingana na uchunguzi mmoja) ambao hupata kuambia mtu yeyote kwamba wamesumbuliwa. Hofu, haya, kujilaumu, kuvurugika akili, kutojua haki zao za kisheria hufanya wanawake wengi wanyamaze. Hivyo, wastadi wengi huamini kwamba tatizo hilo sanasana haliripotiwi!

      Ngano: Wanawake wengi hufurahia kuelekezewa fikira. Wale ambao hudai kwamba wamesumbuliwa ni wenye kuitikia mambo kupita kiasi.

      Hakika: Uchunguzi mbalimbali waonyesha kwa kudumu kwamba wanawake huudhikia kutendwa kwa njia isiyo ya adabu kama hiyo. Katika uchunguzi mmoja, “zaidi ya wanawake wawili kati ya kila watano walisema waliudhika sana na karibu thuluthi moja wakasema walikasirika.” Wengine waliripoti walihisi wasiwasi, kuumizwa, na kushuka moyo.

      Ngano: Wanaume husumbuliwa sawa tu na wanawake.

        Hakika: Watafiti wa Shirika la Kitaifa la Wanawake Wafanyao Kazi (Marekani) waripoti kwamba “visa vipatavyo asilimia 90 vya kusumbuliwa huhusu wanaume ambao wamesumbua wanawake, asilimia 9 ni visa vya watu wa jinsia moja . . . , na asilimia 1 huhusu wanawake ambao wamesumbua wanaume.”

  • Kusumbuliwa Kingono—Jinsi Unavyoweza Kujikinga
    Amkeni!—1996 | Mei 22
    • Kusumbuliwa Kingono—Jinsi Unavyoweza Kujikinga

      “HAKUNA mwanamke apaswaye kusumbuliwa kingono kila siku,” asema mhariri wa gazeti aitwaye Gretchen Morgenson, “wala si kusababu kuzuri kwa wanawake kutarajia mazingira safi kazini yasiyo na tabia ya kukosa adabu.” Jambo la kupongezwa ni kwamba jitihada za waajiri na za mahakama za kufanya kazini kuwa mahali salama zaidi zimepata matokeo kadhaa mazuri. Kwa kielelezo, hatari ya kushtakiwa imefanya waajiri na waajiriwa ulimwenguni pote wajaribu kuboresha mazingira ya kazi. Makampuni mengi yameanzisha taratibu zao yenyewe za kushughulikia kuudhiwa kazini. Mikutano na semina hufanywa ili kufunza waajiriwa tabia ifaayo kazini.

      Bila shaka, ni jambo la kupatana na akili kujua na kufuata sera za kampuni na sheria za hapo. (Warumi 13:1; Tito 2:9) Wakristo pia wamepata manufaa kwa kutumia kanuni za Biblia. Kufuata miongozo hiyo iliyopuliziwa katika shughuli zako na wafanyakazi wenzako kwaweza kukusaidia sana kuepuka kusumbuliwa kingono—au kusumbua wengine kingono.

      Mwenendo Uwafaao Wanaume

      Fikiria jinsi wanaume wanavyopaswa kuwatendea wanawake. Wastadi wengi hutahadharisha dhidi ya kugusa watu wa jinsia tofauti. Wao huonya kwamba kupiga mtu mgongoni kirafiki kwaweza kueleweka vibaya. “Mabaraza ya mahakama huchukua mguso kwa uzito sana,” asema wakili Frank Harty. Yeye anadokeza nini? “Kama ni zaidi ya kusalimiana kwa mkono, usikubali.” Kweli, Biblia haitoi sheria ya ujumla juu ya jambo hili.a Lakini kwa kufikiria hali ya sasa ya kisheria na kiadili, yafaa kujihadhari—hasa kwa wale ambao wana mwelekeo wa kugusa-gusa bila kutambua wanapoongea na wengine.

      Ni kweli kwamba si rahisi sikuzote kufuata shauri kama hilo. Kwa mfano, Glen amelelewa katika utamaduni wa Kihispania. “Nitokako,” yeye asema, “watu huelekea zaidi kukukumbatia kuliko hapa Marekani. Katika familia yetu mara nyingi sisi husalimia marafiki kwa busu, lakini hapa tulitahadharishwa tusiwe wepesi kufanya hivyo.” Hata hivyo, kanuni za Biblia huthibitika kuwa zenye msaada kwa habari hii. Mtume Paulo alimwambia kijana Timotheo: “Watendee wanaume wachanga kama ndugu, wanawake wazee kama mama, na wanawake wachanga kama dada, kwa utakato kamili.” (1 Timotheo 5:1, 2, New International Version) Je, hilo halingeondosha kabisa mguso wa kingono, wa kutongoza, au usiotakikana?

      Kanuni iyo hiyo yaweza kutumika pia kwa usemi. Kwa kufaa, Biblia husema: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wa kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi.” (Waefeso 5:3, 4) Wakili wa masuala ya kusumbuliwa kingono Kathy Chinoy adokeza kwamba kabla ya kusema jambo fikiria swali moja: “Je, ungetaka mama yako, dada yako, au binti yako asikie usemi huo?” Usemi mchafu wenye kudokeza ngono hushusha hadhi ya msemaji na ya msikiaji vilevile.

      Kuzuia Kusumbuliwa

      Mtu aweza kujaribuje kuepuka kusumbuliwa? Shauri ambalo Yesu aliwapa wanafunzi wake alipowatuma kwenye mgawo wao wa kwanza wa kuhubiri labda laweza kutumika katika muktadha huu: “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua.” (Mathayo 10:16) Vyovyote vile, Mkristo ana msaada. Biblia hutuhakikishia hivi: ‘Hekima iingiapo moyoni mwako, busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.’ (Mithali 2:10, 11) Basi, ebu tuchunguze baadhi ya kanuni za Biblia ziwezazo kukusaidia kujilinda.

      1. Chunga mwenendo wako pamoja na wafanyakazi wenzako. Hili halimaanishi kuwa baridi au mkali, kwa kuwa Biblia hutuhimiza ‘tujitahidi kuishi kwa amani na watu wote.’ (Waebrania 12:14, Habari Njema kwa Watu Wote; Warumi 12:18) Lakini kwa kuwa Biblia hutahadharisha Wakristo ‘waenende kwa hekima mbele yao walio nje,’ basi lapatana na akili kudumisha tabia ya uzito, hasa unaposhughulika na watu wa jinsia tofauti. (Wakolosai 4:5) Kitabu Talking Back to Sexual Pressure, cha Elizabeth Powell, huhimiza wafanyakazi “wajifunze tofauti iliyo kati ya mtazamo wenye kufurahisha unaofaa hali yao na aina ya urafiki ambayo yaweza kudokeza kwamba unakubali mambo ya kingono.”

      2. Vaa kwa kiasi. Unachovaa huwapa wengine ujumbe. Huko nyuma katika nyakati za Biblia, kuvaa mitindo fulani ya mavazi kulionyesha ikiwa mtu alikuwa mkosa-adili au mfanya ngono ovyo-ovyo. (Mithali 7:10) Na mara nyingi ndivyo ilivyo leo; mavazi yenye kubana, ya madoido, au yenye kuonyesha uchi yaweza kuvutia uangalifu usiofaa. Ni kweli kwamba wengine waweza kuhisi wana haki ya kuvaa chochote watakacho. Lakini kama mwandikaji Elizabeth Powell anavyosema, “ukifanya kazi miongoni mwa watu ambao wanaamini si kosa kuiba pesa, ningekuambia usiweke kibeti chako cha pesa katika mfuko wako wa nyuma. . . . Ni lazima utambue udhaifu wa . . . mitazamo ya jamii na kujaribu kujilinda usidhulumiwe nayo.” Hivyo, shauri la Biblia ni la kisasa. Hilo huonya wanawake kwa upole “wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi.” (1 Timotheo 2:9) Vaa kwa kiasi, na huenda usielekezewe sana usemi au matendo machafu.

      3. Chunga mashirika yako! Biblia hutuambia juu ya mwanamke mchanga aitwaye Dina aliyeshambuliwa kingono. Yaonekana alivutia uangalifu wa mshambulizi wake kwa sababu kwa ukawaida ‘alikuwa akitoka kuwaona binti za nchi’ ya Kanaani—wanawake waliojulikana kufanya ngono ovyo-ovyo! (Mwanzo 34:1, 2) Leo vilevile, ukiwa na mazoea ya kuzungumza na—au kuwasikiliza—wafanyakazi wenzako ambao hujulikana kuongea juu ya habari zenye kuamsha tamaa, basi wengine huenda wakaamua kwamba unaweza kukubali madokezo ya kingono.

      Hili halimaanishi kwamba ni lazima uepuke wafanyakazi wenzako. Lakini mazungumzo yakija kuwa machafu, mbona usiondoke? Kwa kupendeza, wengi wa Mashahidi wa Yehova wamepata kwamba kuwa na viwango vya juu vya kiadili huwalinda kutokana na kusumbuliwa.—1 Petro 2:12.

      4. Epuka hali zinazoweza kukufanya uridhiane. Biblia hueleza jinsi mwanamume kijana aitwaye Amnoni alivyofanya hila abaki peke yake na mwanamke mchanga aitwaye Tamari ili amtumie vibaya kingono. (2 Samweli 13:1-14) Leo vilevile wasumbuaji wanaweza kutenda kwa njia hiyo, labda kwa kualika mfanyakazi wa cheo cha chini kushiriki kunywa kileo au kubaki kazini baada ya saa za kawaida za kufunga kazi bila sababu yoyote nzuri. Jihadhari na mialiko kama hiyo! Biblia husema: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha.”—Mithali 22:3.

      Ukisumbuliwa

      Bila shaka wanaume fulani watafanya madokezo yasiyofaa hata kama mwanamke anajiendesha vizuri. Unapaswa kutendaje ukifanyiwa madokezo hayo? Wengine wamependekeza kushughulikia jambo hilo bila kukasirika! ‘Mambo ya kingono ofisini ni kichangamshi cha maisha!’ asema mwanamke mmoja. Hata hivyo, badala ya kuona uangalifu kama huo usiofaa kuwa wenye kuchekesha au wa kusifusifu, Wakristo wa kweli huchukizwa nao. Wao ‘huchukia lililo ovu’ na kutambua kwamba kusudi la miendo hiyo mara nyingi ni kumshawishi mtu aingie katika ukosefu wa adili kingono. (Warumi 12:9; linganisha 2 Timotheo 3:6.) Huo mwenendo mchafu huvunja adhama yao ya Kikristo. (Linganisha 1 Wathesalonike 4:7, 8.) Unaweza kushughulikiaje hali hizo?

      1. Chukua msimamo! Biblia hutuambia jinsi mtu mmoja mwenye kumhofu Mungu aitwaye Yosefu alivyoitikia mapendekezo yasiyo ya adili: “Ikawa baada ya mambo hayo, mke wa bwana wake akamtamani Yusufu, akamwambia, Lala nami.” Je, Yosefu alipuuza tu mapendekezo yake, akitumaini kwamba tatizo hilo lingeisha lenyewe tu? Tofauti kabisa! Biblia husema kwamba alikataa kijasiri mwendo wake, akisema: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?”—Mwanzo 39:7-9.

      Hatua alizochukua Yosefu hutuwekea kielelezo kizuri sisi sote wanaume na wanawake. Kupuuza—au jambo baya zaidi, kutishwa na—usemi wenye kudokeza ngono au tabia ya kutumia nguvu ni nadra sana iondoe tatizo; badala ya hivyo, hofu au kusitasita yaweza kufanya hali izidi kuwa mbaya! Mshauri wa jinsi ya kuepuka kulalwa kinguvu Martha Langelan atahadharisha kwamba watu ambao hulala wengine kinguvu mara nyingi hutumia kusumbua wengine kingono kuwa “njia ya kupima uwezekano wa mwanamke kujitetea akishambuliwa; ikiwa yeye ni mpole na mwoga anaposumbuliwa, wao hudhani kwamba mwanamke huyo atakuwa mpole na kuhofishwa ashambuliwapo.” Basi ni jambo muhimu uchukue msimamo mara moja unaposumbuliwa. Kulingana na mwandikaji mmoja, “kukataa mara moja na kwa njia ya wazi mara nyingi hutosha kumfanya msumbuaji aache tabia yake mbaya.”

      2. La yako na iwe la! Yesu alisema hilo katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:37) Taarifa yake hufaa katika pindi hizi, kwa kuwa mara nyingi wasumbuaji hawakomi. Unahitaji kuwa thabiti kwa kadiri gani? Hilo hutegemea hali na itikio la msumbuaji. Tumia kadiri yoyote ile ya uthabiti inayotakikana ili kudhihirisha msimamo wako. Katika visa fulani, taarifa sahili ya moja kwa moja kwa sauti tulivu itatosha. Mtazame kwa macho. Wastadi hudokeza yafuatayo: (a) Taja jinsi unavyohisi. (“Sipendi kamwe . . .”) (b) Taja kihususa tabia hiyo inayoudhi. (“. . . unapotumia usemi mbaya, mchafu . . . ”) (c) Umwambie wazi unalotaka afanye. (“Nataka ukome kunizungumzia kwa njia hiyo!”)

      “Hata hivyo,” Langelan atahadharisha, “mkabiliano usipite kiasi kamwe hata kufikia hatua ya kuwa mkali. Kuwa mkali pia (kutukana, kutisha, na kutumia maneno yenye kuumiza, kurusha ngumi, kumtemea mate msumbuaji) hakuna matokeo. Jeuri ya mdomo ni hatari, na hakuna haja ya kutumia nguvu ila tu kama umeshambuliwa kihalisi na unahitaji kujikinga.” Shauri kama hilo lenye kutumika hupatana na maneno ya Biblia kwenye Warumi 12:17: “Msimlipe mtu ovu kwa ovu.”

      Vipi ikiwa kusumbuliwa kwaendelea japo jitihada zako zote kukukomesha? Makampuni fulani yameanzisha taratibu za kushughulikia kusumbuliwa kingono. Mara nyingi tisho tu la kupeleka malalamiko kwa kampuni litafanya msumbuaji wako akome. Na tena huenda asikome. Kwa kusikitisha, kupata msimamizi wa kazi mwenye kusikiliza si rahisi sikuzote kwa wanawake au kwa wanaume. Glen, adaiye alisumbuliwa na mfanyakazi wa kike, alijaribu kulalamika. Yeye akumbuka: “Nilipomwambia mkubwa wa kazi kuhusu tatizo hilo, hakunisaidia hata kidogo. Kwa kweli yeye aliona hilo kuwa jambo la kuchekesha sana. Nililazimika tu kuchunga mwanamke huyo na kumwepa.”

      Wengine wamejaribu kushtaki kisheria. Lakini zile hukumu kubwa-kubwa unazosoma katika vyombo vya habari si kawaida hata kidogo. Isitoshe, kitabu Talking Back to Sexual Pressure huonya: “Utatuzi wa kisheria dhidi ya kusumbuliwa huhitaji nguvu nyingi sana za kihisia-moyo na wakati; huo hutokeza mkazo wa kimwili na kiakili.” Basi, kwa sababu nzuri Biblia huonya: “Usiharakishe kufanya mashtaka ya kisheria.” (Mithali 25:8, New World Translation) Baada ya kuhesabu gharama za kihisia-moyo na kiroho ya hatua ya kisheria, wengine wameonelea watafute kazi nyingine.

      Mwisho wa Kusumbuliwa

      Kusumbuliwa kingono si jambo jipya. Kumeenea ulimwenguni pote kama moyo wa kibinadamu usiokamilika, wenye pupa na hila. Tume za uchunguzi na kesi za mahakama hazitapata kamwe kuondolea jamii hali ya kusumbuliwa kingono. Kuondoa hali ya kusumbuliwa kingono huhitaji badiliko kubwa la moyo katika watu.

      Leo, Neno la Mungu na roho yake hutokeza badiliko hilo katika watu ulimwenguni pote. Ni kana kwamba mbwa-mwitu na simba wanajifunza kutenda kama wana-kondoo na ndama, kama ilivyotabiriwa na nabii Isaya. (Isaya 11:6-9) Kwa kujifunza Biblia pamoja na watu, kila mwaka Mashahidi wa Yehova husaidia maelfu mengi ya wale ambao zamani walikuwa “mbwa-mwitu” kufanya mabadiliko ya utu ya kudumu na ya kina sana. Watu hao hutii amri ya Kimaandiko ya ‘kuvua kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani’ na kuubadili na “utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”—Waefeso 4:22-24.

      Siku moja dunia itajawa na wanaume na wanawake ambao hushikilia viwango vya Biblia. Watu wenye kumhofu Mungu hungoja kwa tamaa siku hiyo, ambapo aina zote za kutendwa vibaya hazitakuwapo. Mpaka wakati huo, wao hukabiliana kwa kadiri wawezavyo na matendo mabaya ya leo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Tahadhari ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:1 ya ‘kutomgusa mwanamke’ yaonekana yarejezea kugusa kingono, bali si mguso wa kawaida. (Linganisha Mithali 6:29.) Katika huo muktadha, Paulo anahimiza useja na kuonya dhidi ya kujiingiza katika ukosefu wa adili kingono.—Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1973, la Kiingereza.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki